Riwaya-duka la roho

DUKA LA ROHO





SEHEMU YA 1.
SAA 2:50 ASUBUHI.
JIJINI DAR ES SALAAM, MAENEO YA SINZA AFRICA SANA.
Wanaonekana watu wawili wakiwa wanafukuzana huku mfukuzaji akiwa kakamata bastola aina ya Baleta ikiwa imefungwa kiwambo cha kuzuia sauti.
Baadhi ya wananchi walikuwa wamesimama wima wakitizama uwezo wa wale watu wawili kukimbia na kuruka baadhi ya magari ambayo yalikuwa yanakuja mbele yao kwa kasi.
Licha ya wananchi hao kuwa makini na kufuatilia mtanange ule kwa ukaribu zaidi, hawakujua ni nini sababu ya wanaume wale wa shoka kukimbizana tena kimya kimya. Wakashindwa kumsaidia mfukuzaji kwa sababu ugomvi hawakuujua. Kilichobaki kwa hawa wananchi ni kuendelea kujitazamia ufanisi mzima wa wale watu.
"Kimenuka huko. Boya lazima atakuwa kafumwa anakula mzigo wa watu pale Rombo Green View." Alisikika kijana mmoja ambaye alionekana kama muhuni muhuni kwa jinsi alivyo na hata lugha anayoitumia.
"Mmmh! Matepa. Rombo hadi huku Sana bado hawajachoka tu kufukuzana? Halafu yule kaka wa nyuma ana bastola, we unadhani ni kufumaniwa au yule wa mbele kakwapua cha watu kwenye gari. Maana huu wizi kwenye magari umekuwa mkubwa sana." Dada mmoja ambaye naye alikuwa kasimama kando ya barabara sawia na yule muhuni, alichangia maongezi kwa kumpinga yule muhuni.
"Aah! Sister Angel, mwizi gani kapiga suti matata kama ile. Suti ya laki saba ile. Angalia viatu na hata muonekano wa lile jembe. Yule kafumwa tu anakula manzi wa mkuu, acha afundishwe adabu leo." Yule muhuni aliyejulikana kwa jina moja la Matepa, alitetea pointi yake kwa vigezo vichache ambavyo kila mmoja alikubaliana navyo kasoro Angel.
" Mmmh! Matepa, siku hizi, mwenye suti ndio mwizi na mwenye muoneokano kama wako, ndio msamaria mwema. Hawa wezi wa siku hizi wajinga sana lakini wana akili kama nchwa." Yule dada ambaye naye alijulikana kwa jina moja la Angel, aliongea huku akianza kuondoka eneo lile maana watu aliokuwa anawafatilia walishatitia kutoka eneo lile.
" Umeona Sister Angel eeeh, hawa wavaa suti ndio washenzi sana. Lakini wakishavaa hivyo, wanaficha hata macho ya jeshi letu na kufanya sisi wavaa majinzi au kaptula kwa tisheti, kuonekana ndio waharifu. Hapo dada yangu umebonga." Matapa aliunga mkono kauli ya Angel ambaye badala ya kuchangia chochote, alipunga mkono wake hewani na safari ya kupotea eneo lile ikazidi kushika hatamu.
Wale majogoo wawili ambao walikuwa wanafukuzana, hakuna ambaye alisimama na kusaliti amri kwa mwenzake. Kasi ilikuwa inaongezeka kila dakika ambayo walikuwa wanakimbia kuifata barabara ya kwenda Makumbusho.
Yule mwanaume wa mbele ambaye alikuwa kavaa suti ya gharama, rangi ya kijivu. Chini viatu vya damu ya mzee, navyo vikionekana ni vya gharama. Ndiye alikuwa kivutio cha macho ya watu wengi waliokuwa wamesimama kando ya barabara. Aliweza kuruka baadhi ya magari kwa sarakasi mwanana zilizochanganyika na mbwembwe nyingi kama nyimbo za kibantu.
Kuna muda aliruka sarakasi na kutua juu ya gari lililokuwa kasi, kisha anajiachia kama mwenye kujitupa ndani ya maji kumbe anajitupa kwenye rami. Anapofika chini ya rami hiyo, hujiviringa kiustadi na kisha huinuka haraka na kuzidi 'kuchanja mbuga'. Manjonjo yote hayo, yalikuwa yanamkosesha raha yule wa nyuma kwani shabaha zake kumrenga mtuhumiwa wake, zilikuwa haziendi ipasavyo.
"Mkuu, mpo wapi? Huyu mtu si mtu asee, muda si mrefu tunampoteza." Yule jamaa wa nyuma alishika sikio lake ambapo kama utamwangalia kwa makini zaidi, utagundua kuwa kavaa 'earphones' ambazo huvaa wapelelezi au walinzi wakubwa duniani hasa katika kusaidia mawasiliano baina yake na kundi husika.
Na hapo yule jamaa alikuwa anawasiliana na kundi lake kuona kama atapata msaada juu ya mtu yule anayemfukuza.
"Okay. Basi mtegeni hapohapo maana naona wazi anakuja eneo hilo." Sauti ya yule mkimbizaji ilisikika tena ikijibu maelezo ya upande wa pili.
Baada ya hapo, aliachia kisikizio kile na kuzidisha mbio ili kumkaribia yule jamaa wa mbele yake.
Wakiwa katika kasi ya hatari, ghafla mbele ya yule jamaa wa mbele, inatokea gari aina ya Noah na kupiga msele mkali ambao uliifanya ile gari iseleleke tairi za nyuma lakini ni kama ilikuwa imepangwa itokee hivyo. Kwani baada ya mseleleko huo, ule ubavu wa nyuma wa ile gari, ulimpiga kikumbo kikali yule jamaa aliyekuwa anafukuzwa. Kikumbo hicho kikamfanya arushwe hatua kama nane kwenda nyuma, na wakati huohuo, yule jamaa wa nyuma naye hakuwa mbali na tukio lile.
Jamaa aliyepigwa kikumbo, akajikuta anarushwa bila kutegemea. Na katika kujiokoa ili asitulie viungo vya mwili ambavyo ni rahisi kuvunjika, akajikuta kasimama mbele ya jamaa mwenye mwili wa wastani na unaonekana kukumbana na mazoezi ya kutosha kila kukicha. Tabasamu likajitokeza kwenye uso wa kijana yule aliyerushiwa mtuhumiwa.
"Gotcha (Nimekupata)." Sauti ya ushindi ilisikika kwa jamaa yule na kutaka kumkamata mtu aliyekuwa anamfukuza kwa karibu saa moja na robo.
Lakini kabla hajamkamata, alishtukia akipigwa ngumi kali mbili za maeneo ya mabegani na kufanya bastola na pingu zake kudondoka. Kabla hajakaa sawa, mtuhumiwa wake tayari alikuwa kamsogelea na kumgonga kochwa kizito cha pua kilichomfanya yule mfukuzaji kuyumba kidogo na kusimama tena lakini hapohapo mtuhumiwa wake alikuwa kisharuka angani kidogo na kumsindikiza na teke la kifua ambapo safari hii alishindwa kijizua bali kukubali kwenda chini na kusalimia rami iliyopo maeneo yale.
Ni kama jamaa yule hakukumbwa na gari kwa jinsi alivyokuwa anajimudu kwenye kurusha mateke na kuruka sarakasi ambazo zilikuwa chachu tosha katika kumuadabisha mpinzani wake ambaye alishindwa kujibu mapigo na hivyo kugaa-gaa pale kwenye rami kama swala aliyechomwa upinde wenye sumu.
Yule kidume ambaye alikuwa amekwishamiliki mchezo mzima, sasa akawa anajiandaa kummaliza mpinzani wake kwa pigo ambalo yule jamaa aliyekuwa anamfukuza alipoliona, alikumbuka ni jinsi gani lilivyobeba uhai wa watu wengi akiwemo Mkuu wa Upepelezi kanda ya kati, Mzee Ismail Ambazeki. Askari muadilifu kupata kutokea katika nchi ya Tanzania.
Wakati Mzee Suma Ambazeki anapigwa pigo hilo, huyu kijana ambaye anajiandaa kupokea pigo hilo, alikuwa askari mdogo sana kicheo. Cheo chake kikamfanya awe dereva wa Mzee Suma au Ismail. Na siku wakati mtuhumiwa wake anampa pigo bosi wake, yeye alikuwa ndani ya gari akitetemeka hasa baada ya kuona mapigo 'konde' ya jamaa yule.
Akafumba macho yake ili asione jinsi lile pigo litakavyokita mwilini wake. Yule jamaa ambaye alikuwa anafukuzwa, tayari alishajitutumua na kujifua ipasavyo kwa ajili ya kumdondoshea pigo au tufani, yule kijana wa watu.
Akaruka juu huku sauti ya juu ya kikomando ikisikika tayari kwa kumwingizia pigo takatifu yule mfukuzaji.
Ni kama wote wawili walikuwa ndotoni. Hapa nawazungumzia yule aliyekuwa anapigwa na anayepiga. Mpigwaji, aliona kama Malaika mwokovu kamtokea na kumsaidia, lakini mtuhumiwa wake alijiona kama Malaika mtoa roho kamtembelea kwa wakati ule.
Akiwa juu huku akitoa sauti yake ya kikomandoo, alijikuta akipigwa teke zito la ubavu lililokata hadi sauti yake hiyo mbaya. Kabla hajaelewa wala kujiweka sawa kuangalia ni nini kilichompata, akapokea teke lingine la kijizungusha (round kick) ambalo lilimkuta kidevuni na kuzidi kumrudisha chini badala ya kumsimamisha.
Dhoruba ikazidi kumuandama yule mbabe wa mwanzo kwani safari hii alijikuta akikaliwa kifuani na kuanza kupigwa ngumi mfululizo kana kwamba mwili wake uligeuka kuwa begi la kupigia ngumi hizo.
Ndani ya dakika zisizozidi mbili, tayari yule mbabe alikuwa hoi huku uso wake ukiwa umelowa damu zilizochagizwa na kupasuka usoni.
"Hey. Mubarak, fanya kazi yako." Ni sauti iliyomuamuru yule aliyepewa kichapo na mtuhumiwa wake. Sauti ilienda sambamba na kurushiwa pingu ambazo aliziokota baada ya mbabe mmoja kuzifanya zitoke kwenye mikono ya mwanausalama Mubarak.
"Yes Madame (sawa mama)." Mubarak au Mubah kama alivozoeleka kuitwa na wenzake, alinyanyuka na kuziweka pingu alizorushiwa vema na kumwendea mtuhumiwa wake.
Japo yule mtuhumiwa alishasaliti amri, lakini Mubah ni kama alikuwa hajui hilo. Akaanza kumshushia mateke mazito tumboni yule mtuhumiwa.
"Hey Mubah, mfunge pingu, acha ujinga." Sauti ileile ya kike ilimfokea na Mubarak hapohapo amri akaifuata kwa kumfunga pingu yule mtuhumiwa wao na kumnyanyua, tayari kwa kumpeleka kwenye ile Noah iliyompa kikumbo.
Baada ya dakika moja, Mubah alikuwa tayari amekwishamaliza kumfunga pingu mtuhumiwa wake na kumuingiza kwenye ile Noah. Ndani ya Noah kulikuwa na wanaume wengine watatu, mmoja akiwa dereva na wengine wawili wakiwa wanacheza na mitambo zikiwemo kompyuta ndani ya gari ile.
Yule mwanamke, alikaa upande wa kushoto wa siti ya nyuma ya dereva, na Mubah akakaa upande wa kulia wakati huo mtuhumiwa wao akikaa katikati yao.
" Lisa Lindsay. Mwanamke niliyekupenda kwa moyo wangu wote. Upo mke wangu?" Sauti ya kukeresha ilimuuliza yule mwanamke huku muulizaji mwenyewe akiwa kajiinamisha kichwa chake bila kumuangalia usoni amuulizaye.
"Kwa nini umeamua kufanya kazi kama hii? Umekosa kabisa hata kazi ya kuuza vitumbua na sasa unajiweka katika kazi za utumwa kama hii? Kazi za kuhatarisha maisha yako na ya uwapendao." Jamaa alizidi kuongea lakini hakuna aliyemjibu.
"Ooh! Naona maongezi yangu hayawaingii vichwani mwenu. Ngoja nijaribu maongezi haya." Safari mtuhumiwa alinyanyua uso wake na kumuangalia Lisa. "Frank yupo wapi?" Swali likamtoka mtuhumiwa na kumfanya Lisa amwangalie usoni kwa mshtuko. "Nimegusa penyewe hapo. Anapenda kujiita Man'Sai. Mwanaume aliyetikisa dunia kwa kuiba "UKURASA WA HAMSINI" (Hii ni hadithi nyingine ambayo inaanza pale riwaya ya JINA itakapoishia). Mwanaume ambaye tulikuwa hatulali baada ya kugundua Lisa Lindsay anatoka naye kimapenzi. Yupo wapi sasa hivi. Yale maneno matamu ya nakupenda na porojo nyingi, vimeishia wapi? Hayupo tena nawe, kwisha habari yako." Yule jamaa aliongea na kumalizia kwa cheko ndefu iliyokera kila mtu mle kwenye gari. Lakini hakuna aliyethubutu kuongeza neno wala kufanya kitendo chochote cha ajabu.
"Martina Gunner Bokwa. Jina la mtoto wako." Yule mtuhumiwa akaongea maneno mengine yaliyovuta hisia za Lisa na kubaki mdomo wazi. "Kwa nini ulimuita mtoto majina ambayo si yake?" Jamaa akazidi kumshangaza Lisa kwa maneno ambayo yaligusa undani wa Lisa.
Akiwa kafungwa pingu na mikono yake ikiwa mbele, jamaa yule aliingiza mkono kwenye mfuko wa koti ulio maeneo ya kifuani kwake na kutoa picha ambayo ilimuonesha mtoto wa kike mwenye umri kati ya miaka miwili hadi mitatu.
Kwa mshangao na kwa kushtukiza, Lisa akampora ile picha yule jamaa huku uso wake ukijawa na hamaniko la haja.
"Umetoa wapi hii picha we mpumbavu?" Lisa alimuuliza yule jamaa huku akiwa tayari kamvamia na kumkaba shingoni.
Ni Mubarak ndiye akiyemuondoa kwenye mwili wa mtuhumiwa na kumpunguza hasira ambazo tayari zilikuwa zimemkamata kooni Lisa.
Wakati huo gari lao, lilikuwa linazidi kuacha maeneo kadhaa ya jiji la Dar es Salaam, na kuna sehemu Noah ile ilisimama kwa muda mrefu sababu ya foleni kubwa inayoendelea kutesa katikati ya jiji lile.
"Koho kohoo." Yule mtuhumiwa alijikohoza baada ya roba ya Lisa huku akijitengeneza na kukaa sawa kwenye kiti cha gari ile.
"Mubah. Hii ni picha ya Martina, nilimpiga mwenyewe na nilikuwa nimeiweka kwenye mkoba wangu. Sasa huyu kaipataje na mkoba huo nauficha kwani una vitu vingi vya siri." Lisa aliongea kwa sauti iliyojaa machungu huku ikichagizwa na hali ya kutaka kulia.
"Navijua vitu vyote vya siri. Ukaamua kuolewa na Gunner ili kuficha aibu. Hujui chochote kilicho nyuma ya .....
.." Jamaa yule hakumaliza sentensi yake, tayari Mubah alikuwa kamtandika ngumi nzito ya shavu hadi damu kiasi zikamrukia Lisa.
"Ooooh! Ni Prince Mubarak." Jamaa yule aliongea baada ya kujifuta damu zilizokuwa zinamchuruzika. "Na swali.moja tu kwako, na usipolijibu, nitakupa onyo tu." Jamaa alimtazama Mubah kabla hajauliza swali lake.
"Kwa nini umeamua kuweka dukani roho za uwapendao?" Jamaa alimuuliza Mubah lakini badala ya Mubah kujibu, yeye akachukua gundi aina ya 'sole tape' na kuizungusha mdomoni mwa mtuhumiwa yule mwenye mdomo wa kero na kukereketa.
"Thats will help, I think. (Hiyo itasaidia nadhani)" Lisa aliongea akikubaliana na kitendo kilichofanywa na Mubah.
****
Safari yao ilikomea eneo moja la ufukwe wa bahari ya hindi. Na baada ya hapo, Lisa alitoa simu yake ya mkononi na kuipiga.
Maongezi yalichukua dakika chache na simu ikakatwa.
Baada ya dakika zisizozidi kumi za kukata simu ile, kwa mbali, kwa kutumia darubini yake, Lisa aliona Nyambizi ikiibuka toka chini ya bahari na baadae ikafunguka kwa juu na boti ndogo saba zikatoka ndani yake. Boti hizo ni zile ziwezazo kubeba watu wawili kila boti moja.
Waendeshaji walikuwa wamevalia mavazi ya kuogolea na bunduki aina M16 zikiwa migongoni mwao.
Lisa akashushia darubini yake kifuani na kuwapa ishara wenzake ya kujiandaa hasa kutoka mle garini.
Boti saba zikasimama mbele ya wakubwa wa kazi, na kitendo bila kuchelewa, kundi linaloongozwa na Lisa likiwa na mtuhumiwa wao, wakakwea nyuma ya boti hizo ndogo na safari fupi ya kwenda kwenye Nyambizi moja ndogo kiasi, ikaanza.
Boti tano zikiwa mbele na nyingine mbili nyuma zikilinda usalama ili yule mtuhumiwa asitoroke, zikazidi kukata maji kuelekea kwenye nyambizi.
Wakiwa katika umbali fulani, Lisa alimuamuru dereva wa boti yake asimame. Naye baada ya kusimama, Lisa aligeuka nyuma na kuangalia kule alipotoka.
Kulikuwa hakuna watu wanaozunguka eneo lile, hiyo ikawa nafasi pekee ya Lisa kufanya alichokusudia.
Akatoa rimoti ndogo ambayo alibofya kitufe kimoja kilichokuwepo katikati. Na hapohapo, mlipuko mkubwa uliikumba ardhi ambayo gari aina ya Noah ilikuwa imeweka makao kwa muda.
Ni ile gari ambayo walikuwa wanaitumia Lisa na kundi lake. Baada ya kumalizia kazi ambayo waliipanga, sasa waliiteketeza na kuacha Jiji dogo la Dar Es Salaam kutetemeka kwa huo mlipuko. Wafanyakazi wa maeneo yale walikimbia huku na huko wakihisi jiji limevamiwa na magaidi hatari. Hakuna aliyekumbuka kugeuka nyuma, wote walikuwa wakinusuru roho zao. Hakika ilikuwa ni mshike mshike maeneo yale.
Baada ya kulidhika na kazi yake, Lisa akamgonga bega kumruhusu dereva wake aondoke, naye akatii amri na kwenda sehemu ambayo walipanga waende.
****
Ndani ya nyambizi ile, kulikuwa kuna pilika za hapa na pale hasa wale mafundi mitambo wanaongoza chombo kile maalumu kwa ajili ya kazi za kijeshi au kiusalama.
Naam, baada ya Lisa na kundi lake wakiwa sambamba na mtuhumiwa wao kuingia kwenye chombo kile, waliongozwa kwenye chumba maalumu na kuoneshwa nafasi zao za kukaa.
Baada ya kukaa, alitokea daktari mmoja akiongozana na kijana aliyebeba sinia dogo lililokuwa na sindano uwezazo kuzikamata kama bastola. Sindano hizo zenye dawa kiasi, kila mmoja alichomwa begani na baada ya dakika chache, macho ya hawa watu yakaanza kuwa mazito.
"Kazi za utumwa hizi. Hamtakiwi kujua hata ni wapi mnafanyia kazi na ndio maana mnapigwa sindano za usingizi ili msione mnapoenda. Stupid peoples." Sauti nzito iliyochanganyanyika na ulevi, ilimtoka yule mtuhumiwa aliyekuwa huru kuongea baada ya kutolewa ile gundi aliyozungushiwa na Mubah.
ITAENDELEA

DUKA LA ROHO





SEHEMU YA PILI
Ndani ya nyambizi ile, kulikuwa kuna pilika za hapa na pale hasa wale mafundi mitambo wanaongoza chombo kile maalumu kwa ajili ya kazi za kijeshi au kiusalama.
Naam, baada ya Lisa na kundi lake wakiwa sambamba na mtuhumiwa wao kuingia kwenye chombo kile, waliongozwa kwenye chumba maalumu na kuoneshwa nafasi zao za kukaa.
Baada ya kukaa, alitokea daktari mmoja akiongozana na kijana aliyebeba sinia dogo lililokuwa na sindano uwezazo kuzikamata kama bastola. Sindano hizo zenye dawa kiasi, kila mmoja alichomwa begani na baada ya dakika chache, macho ya hawa watu yakaanza kuwa mazito.
"Kazi za utumwa hizi. Hamtakiwi kujua hata ni wapi mnafanyia kazi na ndio maana mnapigwa sindano za usingizi ili msione mnapoenda. Stupid peoples." Sauti nzito iliyochanganyanyika na ulevi, ilimtoka yule mtuhumiwa aliyekuwa huru kuongea baada ya kutolewa ile gundi aliyozungushiwa na Mubah.
Hakuna aliyemjibu na badala yake, kila mmoja alibebwa na usingizi mzito.
****
FISSA (Federal Intelligence Secret Service Agencies)
Mlango mmoja mkubwa uliandikwa maandishi hayo ambapo ndipo hasa Lisa na Mubah wanafanya kazi zao. Ule usingizi mrefu ulikuwa umewapaa na sasa walikuwa wanatembea wenyewe huku wakimkwida vema mtuhumiwa wao ili asiwaponyoke.
"Kazi nzuri Agent Lisa. Mmefanya vizuri na kikosi chako." Sauti ya mtu mmoja mrefu kiasi na mweusi, ilisikika ikiwa kwenye jukwaa dogo ambalo mbele yake kulikuwa na watu wanachakalika na kompyuta zao huku skrini moja kubwa ikionesha kazi nzima wafanyazo wale wafanyakazi.
"Asante mkuu." Lisa alishukuru huku akiinama kidogo kuonesha heshima kwa mkuu wake wa kazi.
Mkuu yule akashuka toka kwenye lile jukwaa na moja kwa moja akamfuata yule mtuhumiwa na kumuangalia kwa macho makali kabla hajaanza kuongea.
"John Lobo. Nilishangaa sana nilipoambiwa kuwa u mzima. Nilikuua kwa mikono yangu, lakini leo ni kama nakutana na mzimu." Sauti ya yule bwana ilipenyeza kwenye masikio ya kila mmoja aliyesikia vema maongezi yale. "Sina kesi na wewe. Nilishakuua kipindi kile, hapa naanza na kesi nyingine." Alimaliza Mkuu wa FISSA na kugeuka nyuma kurudi kwenye lile jukwaa dogo.
"Malocha Malingumu." Sauti ya John Lobo, mtuhumiwa aliyekamatwa na kundi la Lisa, ilimuita yule mkuu wa kitengo cha siri cha huduma za kipelelezi nchini Tanzania. Bwana Malocha akasimama kumsikiliza kimtokacho John Lobo.
"Siyo kosa langu kuua familia yako. Nilinunua roho zao kwa kuamrishwa na shetani langu. Usilalamike sana. Hahahahahaaa." Lobo alimaliza kwa cheko lake la kukera kushinda hata la katuni au fisi.
"Mpelekeni Hell in Hell." Malocha akaamuru na kila mmoja alishituka baada ya kusikia amri hiyo.
"Hamjanisikia?" Malocha aliuliza baada ya kuona hakuna kinachotendeka baada ya amri.
"Lakini Mkuu huyu tutampoteza kule. Kumbuka CIA na FBi wanamtaka mzima." Lisa akiongea kumuelewesha mkuu wake.
"Kwa hiyo unashauri apelekwe wapi?" Malocha akauliza tena swali.
"Nadhani twende naye 123K." Alitoa wazo Lisa.
"Kwa hiyo akakae tu! Kaja kukaa hapa au kusema ukweli?" Malocha alimtupia swali Lisa.
"Lakini si kumpeleka Hell in Hell. Atasema nini kule?" Lisa alijitetea.
"Hivi mmenileta huku nije kusema kitu au nije kupiga story na 'school mate' wenzangu?" Lobo alifungua kinywa chake na kuwauliza wale wanaoshauriana wapi wampeleke.
"Kama mnataka mnijue au niseme chochote, hilo mmekosea. Hapa hampati kitu wajinga nyie." Lobo akamaliza na hapohapo ngumi nzito ya tumbo ilitua. Alikuwa ni Mubah aliyemuadabisha.
"Utalipa hii dogo." Lobo alimwambia Mubah na Mubah badala ya kutilia maanani yale maneno, alimuongeza konde lingine zito la tumboni.
"Big Mistake(Kosa kubwa) Lakini bado unanafasi ya kulisawazisha." Lobo alimwambia tena Mubah baada ya kuinuka alipokuwa kainama kwa sababu ya kupigwa ngumi ile.
"Mpelekeni 123F6."Malocha aliamuru tena. Na kitendo bila kuchelewa, Lisa na Mubarak walimkamata kushoto na kulia na kuanza kumkokota kwenda chumba walichokiita 123F6.
HELL IN HELL
Hichi ni chumba kipana kilichopo ndani ya FISSA. Ndani ya chumba hiki kuna kiti cha umeme ambacho hutumika kuwasulubu watuhumiwa nguri na saa nyingine kuwaua.
Pia kuna tank kubwa ambalo limejengwa kwa vioo, na tank hilo ndani yake kuna maji. Pia hutumika kusulubisha watuhumiwa kwa kuwazamisha humo au wakiona haongei, hufungulia umeme uliyoungwa ndani ya tank hilo na kuanza kumpiga shoti mtuhumiwa. Hizo ni silaha chache zilizopo katika chumba kiitwacho Hell In Hell. Mbali na hayo, kuna vifaa vya kunyongea na kuchania ngozi.
Ni chumba ambacho kinaogopwa hata na wafanyakazi wenyewe. Kinatisha kwa matendo yanayofanyika huko.
123K
Hiki pia ni chumba kilichopo hukohuko FISSA. Chumba hiki pia ni kipana na kina meza moja kubwa pamoja na kioo ambacho ukiwa ndani huwezi kumuona wa nje lakini wa nje anamuona wa ndani.
Chumba hichi ni kwa ajili ya kumuhoji mtuhumiwa kwa mdomo bila kumsulubisha. Na hata kama watataka.kufanya hivyo, basi hutumia viungo vyao kama ngumi na mateke.
123F6
Hiki ni chumba kipana pia kwa ajili ya mahojiano na watuhumiwa. Ndani ya chumba hiki, mahojiano huwa ni ya kulazimisha uongee ukweli kwa kubanwa na silaha mbalimbali pamoja kuchomwa na vitu vyenye ncha kali lakini lengo likiwa utoke mzima.
Na mara nyingi kama mtuhumiwa ni mgumu, basi hupigwa sindano yenye dawa kali ambayo hufanya ubongo na akili ya mtuhumiwa iwaze kusema ukweli tu.
Humo ndimo ambamo John Lobo kapelekwa. Nyuso mbili ambazo hazina utani zilikuwa zimesimama pembeni ya chumba hicho huku wakijaribu jaribu vifaa vyao. Mzee mmoja ambaye alikuwa anapuliza gesi yenye moto juu, aligeuka haraka baada ya kusikia mlango wa chumba kile ukifunguliwa.
"Ooh! Lisa. Umefanikiwa kumkamata Lobo. Kazi nzuri sana binti." Mzee yule aliongea kumpongeza Lisa.
"Asante Babu Pujini, hakuleta shida wakati wa kumkamata." Lisa alimjibu Mzee Pujini ambaye alikuwa ana asili fulani ya Kihindi lakini ni Muafrika halisi kutoka Tanzania.
"Good Lisa. Ndio umemleta kwenye shughuli eeh." Mzee Pujini aliongea huku akianza kuchezea tena ile gesi kwenye kibubu maalumu kinachotengeneza moto huo wa gesi.
"Ndio babu. Fanya yako." Lisa alijibu na wakati huo Mubah alikuwa anafungua pingu alizokuwa kamfunga John Lobo.
Licha ya Lisa na Mzee Pujini kuongea mengi yanayomhusu John Lobo, lakini Lobo mwenyewe hakuwepo kwenye dunia yao bali macho yake yalikuwa yakipepesa huku na huko, chini na juu ya chumba kile.
"Huyu hapa Mzee." Sauti ya Mubarak ilisikika huku ikifuatiwa na kumsukuma Lobo kwa mzee yule bingwa wa kutoa adhabu kwa watuhumiwa mbalimbali.
"Beda. Muondoe misuti yake huyu bwana." Mzee Pujini alimsukumia Lobo kwa Beda, jamaa fulani wa makamo na kwenye mwili mkubwa kutokana na kunyanyua vitu vizito.
Naye Beda bila kuchelewa, akaanza kumwondoa nguo John Lobo na wakati huo Lisa na Mubah walishatoka katika chumba kile na Mzee Pujini alishakifunga.
****
"Lobo. Nia yako na washirika wako ni nini?" Sauti ya kiume ilisikika katika chumba kiitwacho 123F6.
Ilikuwa ni sauti ya Malocha ikitoka kwenye spika zilizopo kwenye chumba kile.
Lobo alikuwa akivuja damu nyingi kifuani na maeneo ya usoni. Alikuwa kalegea kwa mateso makali ambayo yalitoka mikononi mwa Beda na Mzee Pujini.
"Kazi yangu ni kuuza au kununua roho tu! Sina kazi nyingine. Sina nia na wala sijui washirika wangu ni wakina nani." Lobo alijibu swali la Malocha na baada ya jibu hilo, Malocha alitoa ruhusa ya mateso kuendelea.
Mzee Pujini akachukua kile kibubu chenye gesi na kuwasha gesi ile. Baada ya kuweka moto fulani kwenye kibubu kile cha gesi, akamfata Lobo na kuanza kumpitishia machoni bila kumdhuru bali kumsikilizisha joto litokalo mle kwenye kibubu.
"Joto hili linaenda kwenye maungo yako ya uzazi." Mzee Pujini akiwa kavalia kama Daktari, akaongea huku taratibu akianza kushusha moto ule kwenye maeneo ambayo kayataja.
Licha ya hayo yote kutukia, uso wa John Lobo ulikuwa si wenye mashaka wala uoga. Ni kama alishazoea yale mateso, lakini yote ni sababu alikuwa mkomavu katika nyanja kama zile.
Mzee Pujini akafika maeneo ya uzazi ya John Lobo, na bila kusita akapulizia gesi ya moto maeneo yale na kumfanya John Lobo atoe sauti kali iliyochanganyika na maumivu. Hakika mkomavu na kamanda wa mateso, alikuwa anaumia.
"You fu**n, motherfu***r you're hurting me. (We mpumbavu, (tusi). Unaniumiza)." Sauti ya maumivu makali ilisikika kutoka kwenye kinywa cha Lobo ikifuatana na matusi mazito ya wazazi kumuelekea Mzee Pujini.
"Sema ukweli tuache hili zoezi." Mzee Pujini aliacha kuchoka maeneo nyeti ya Lobo na kumuomba aseme ukweli.
"Pale nitakapofanikiwa kusimama kwenye hiki kiti, wewe ndio utakuwa wa kwanza kufa." John Lobo alimwambia Mzee Pujini maneno ambayo yule mzee alitabasamu kwa dharau kisha akaangalia kile kioo ambacho wa ndani hamuoni wa nje ikiwa ni ishara ya kuwaambia waulize swali lingine.
"Lobo. Hatupo hapa kukuumiza. Ni rahisi tu! Unashirikiana na nani na nini nia yako kwa ufanyayo." Swali lilelile lilitoka kwenye kinywa cha Malocha.
"Hahahaaa. Malocha, mbona unajiumiza sana. Nimekwisha kwambia, sina nia zaidi ya kuuza na kununua roho za watu. Au unataka nikwambie duka la roho lilipo?" Lobo aliuliza huku uso wake ukielekea kwenye kile kioo kana kwamba anawaona wale wanaomtupia maswali kwa kunong'onezana.
"Lobo. Hatupo katika utani. Umemuua Kamanda wa Kikosi cha Upepelezi kanda ya kati. Umewatishia amani mawaziri mbalimbali na kauli yako ya kununua roho zao. Ukawaua baadhi ya viongozi hao. Ukaona haitoshi, ukaanza kuwaondoa mabalozi mbalimbali wa nchi hii kwa kuwaua. Sasa umegusa pabaya zaidi. Marekani.
Umegusa nchi ambayo hatuiwezi kwa kitu chochote....." Sauti ya Malocha ilikuwa ikielezea baadhi ya maovu ya John Lobo lakini kabla hajamaliza maongezi yake, sauti yenye hasira kupindukia, ilimkata kauli.
"Eti hatuiwezi kwa chochote. Ni ujinga gani ambao umekujaa kichwani we' mpumbavu? Marekani anachotuweza ni nini? Au ndio kasumba zenu za uoga bado zimewatawala kichwani mwenu?
Huyu Frank anapambana na kutafutwa kwa udi na uvumba na watu gani? Si ni hawahawa Wamarekani? Mbona hawampati? Mbona hata wakimpata wanamshindwa? Kaua makomando wangapi Wakimarekani. Usiwe mjinga Malocha. Umiza kichwa fala wewe." Kauli chafu zilitiririka toka kinywani mwa Lobo na hakuna aliyethubutu kumkatiza hadi alipomaliza mwenyewe.
"Sound like it's true. But none of it is real. (Sauti kama ya ukweli. Lakini hakuna kati hivyo chenye uhalisia)." Malocha aliongea kwa kutumia lugha ya ughaibuni.
"Frank, never killed any commander from America. He just killed the terrorists, and bad guys. (Frank hakuua kamanda yeyote wa Kimarekani. Aliua wavamizi na watu wabaya pekee)." Sauti ya Lisa iliunga maelezo ambayo Malocha aliyaacha kati.
"Inaonekana hamjui lolote la kwa nini Frank anatafutwa na kwa nini kajificha. Na mbaya zaidi, hao anaowaua ndio mimi na baadhi yenu nyie wapelelezi mnawasujudia. Mtakufa kama panya kwenye sumu kwa mkono wangu." Lobo aliongea kwa hasira huku akijaribu kuchomoa mikono yake toka kwenye kiti alichokuwa kafungwa barabara na wazee wa kazi wa chumba 123F6.
Hali ya kujikakamua ili atoke pale kwenye kiti, ilifanya mwili wake ututumke na kusambaa misuli kama ananyanyua vitu vizito.
"Mzee Pujini. Fanya yako." Malocha aliongea kumruhusu tena Mzee Pujini aendeleze adhabu zake.
Mzee Pujini naye bila kusita, akajaribu moto wake angani kabla hajaanza kazi ya kuchoma ngozi nyeusi ya John Lobo.
****
"Hahahahahaa. Kuna muda hamna haja ya kulia bali kucheka kwa sababu maumivu uyapatayo, ni sawa na kukutekenya tu." Sauti ya John Lobo iliongea baada ya Mzee Pujini kumaliza kumchoma kwa gesi maeneo ya ndani ya mapaja na kifuani.
"Look like you are so tough. Lets see. (Unaonekana kama mgumu. Ngoja tuone)." Sauti ya Beda, mshirika au msaidizi wa Mzee Pujini ilisikika ikiongea hayo huku ye' mwenyewe akivaa grovu tayari kutimiza majukumu yake.
Beda akachukua visu fulani vidogo vilivyo kwenye mkoba maalumu kwa ajili ya kuvihifahidhia. Na baada ya kukamata visu hivyo viwili, akawa anavinoa kwa kuvisugulisha vyenyewe kwa vyenyewe huku akitembea mbele ya Lobo huku na huko.
Visu vilivyokuwa vinang'aa kama almasi lakini ni vya siliva, vilipita kifuani mwa Lobo haraka na kuacha alama kama ya X kifuani hapo, na kabla hata Lobo hajalia kwa sababu ya maumivu, akamwagiwa mafuta fulani spesheli ambayo yanauma si kawaida pale yawekwapo kwenye vidonda, lakini ni tiba tosha kwa ambaye anavuja damu.
"Fuc*** you FISSA. And fuc** you all and your mama."Lobo alitukana matusi mazito ya Kimarekani kwa sababu ya maumivu makali yaliyokuwa yanampata kwa wakati ule. Hakika alikuwa katika mateso, lakini bado hakuwa tayari kusema ukweli wowote.
"Lobo. Nia yako ni nini na washirika wako ni wakina nani?" Malocha aliuliza kwa sauti kali tena.
"Nia yangu ni kusafisha pasafi kwa kuweka uchafu. Washirika wangu ni uchafu, umenielewa?." Lobo alijibu kwa hasira kali zilizokuwa zimemjaa moyoni sababu ya kuchanjwa na kuteswa na FISSA.
"Mkuu, niachie mimi nikamuhoji mlemle." Mubarak alitoa ombi ambalo halikukataliwa kwa sababu majibu ya John Lobo yalikuwa hayana mashiko hata kidogo vichwani mwao.
"Ooh! Mubah. Umekuja kuchukua ujumbe wako." Lobo alitoa tabasamu pana baada ya kumuona Mubarak kaingia ndani ya chumba kile.
Mubah hakuongea chochote zaidi ya kuchukua chuma chenye ncha kali kwenye ule mkoba wa kuhifadhia vifaa hivyo vya mateso.
"Nauliza swali. Nataka jibu sahihi." Mubah alimwambia Lobo huku akikaa kwenye kiti ambacho alikivutia mbele ya Lobo.
Lobo badala ya kujibu, alitabasamu tena. Tabasamu la kukereketa hata ubongo wa kichaa.
ITAENDELEA

DUKA LA ROHO





SEHEMU YA TATU
"Mkuu, niachie mimi nikamuhoji mlemle." Mubarak alitoa ombi ambalo halikukataliwa kwa sababu majibu ya John Lobo yalikuwa hayana mashiko hata kidogo vichwani mwao.
"Ooh! Mubah. Umekuja kuchukua ujumbe wako." Lobo alitoa tabasamu pana baada ya kumuona Mubarak kaingia ndani ya chumba kile.
Mubah hakuongea chochote zaidi ya kuchukua chuma chenye ncha kali kwenye ule mkoba wa kuhifadhia vifaa hivyo vya mateso.
"Nauliza swali. Nataka jibu sahihi." Mubah alimwambia Lobo huku akikaa kwenye kiti ambacho alikivutia mbele ya Lobo.
Lobo badala ya kujibu, alitabasamu tena. Tabasamu la kukereketa hata ubongo wa kichaa.
"Mubah. There's two choices. Buy or Sell. (Mubah. Kuna machaguo mawili. Nunua au Uza)" Lobo alimwambia Mubah kwa sauti tulivu. Mubah hakuwa mwenye wasiwasi bali kumtaza John Lobo machoni."The rules of these choices are very simple. (Sheria za haya machaguo ni marahisi sana)" Sauti ya Lobo ilizidi kuchukua nafasi."Acha kazi yako au endelea na kazi yako. Ukiacha kazi, utakuwa umenunua roho za familia yako. Watanusurika na mikono yangu. Ukiendelea na kazi, utakuwa umeniuzia roho za uwapendao. Rahisi sana." Lobo alimaliza kauli yake na hapohapo kwa hasira, Mubah alikandamiza kile chuma chenye ncha kali kwenye paja la Lobo.
Kabla hata Lobo hajakaa sawa kusikilizia yale maumivu, akapokea konde zito la shavu la kushoto hadi damu zikaruka upande mwingine.
Tayari Mubah alikuwa kapandwa na hasira kali ambazo zilimpelekea kusimama na kuanza kumpa mateke mazito John Lobo.
Hata pale Malocha alipomuamuru aache anachokifanya, hakusikia lolote bali ngumi na mateke ndivyo aliona ni suluhu tosha kumpunguzia hasira.
Ni Beda na Mzee Pujini ndio walimkamata na kumsogeza pembeni asiendelee kufanya 'unyambirisi' aliokuwa anaufanya.
Kiti alichokuwa kakalishwa Lobo, kilikuwa kimechimbiwa chini hivyo wakati anapigwa alikuwa hadondoki wala kuyumba, hivyo kufanya maumivu kumwingia vilivyo.
"Fpuu." Lobo alitema damu pembeni baada ya Mubah kuwa anasukumwa pembeni.
"Mtoeni nje." Sauti ya kwenye spika ilisikika ikiamuru Mubah atolewe nje.
"Mubah." Lobo alimuita Mubah kabla hajatoka. Mubah akageuka kumuangalia yule mtu aliyemuita.
"Sijabadili maamuzi yangu. Anza kuhesabu sasa, unamasaa ishirini na nne kufanya nilichokwambia.
Angalia saa yako, au angalia ile pale." Lobo alimuonesha kwa macho saa iliyokuwa ukutani. Mubah akaiangalia kisha akarudisha macho yake kwa Lobo.
"Tick Tock." Lobo aliongea sauti ya mshale wa saa na kumfanya Mubah ajikurupue toka kwenye mikono ya Mzee Pujini na Beda kwa ajili ya.kwenda kumpa kisago tena Lobo. Lakini hakufanikiwa hilo kwa sababu tayari alikuwa kwenye mikono imara.
"Unafanya nini Mubah." Malocha alimuuliza kwa hasira Mubah baada ya kutolewa katika kile chumba.
"Ni hasira mkuu. Kaniambia maneno ya ajabu sana yule mjinga."
"Hasira za kijinga hizo. Unadhani wakina Beda wangekuwa wanaendekeza hasira kwa kutukanwa na kutishiwa, watuhimiwa wangekuwa wanapona?" Mubah akainamisha kichwa chini na kujiona amekosa mbele ya Mkuu wake.
"Embu twendeni ofisini." Malocha aliamrisha na hakuna aliyekataa kati ya Lisa na Mubah ambao walikuwa kwenye kile kioo wakifatilia mateso ayapatayo Lobo kwa makini na ukaribu.
BAADA YA NUSU SAA.
Ni king'ora kilichokuwepo ndani ya Shirika lile la siri, ndicho kilichowashtua Lisa, Malocha na Mubah waliokuwa ofisini wakijadili njia mbadala za kumfanya Lobo aongee.
Kabla hawajajua sababu ya king'ora hicho kulia, mara mlango wa kioo wa ofisi ya Malocha, aliingia mfanyakazi mmoja akiwa kavaa "headphones" masikioni zilizounganika na kipaza sauti moja kwa moja. Ukimuona ni kama mtangazaiji wa radio fulani, lakini sio.
"Mkuu. Lobo katoroka. Na kawaua Beda na Mzee Pujini." Taarifa hizo zikawakurupua wale vijana wa kazi kwa pamoja na kuanza kuelekea kule walipomuacha John Lobo.
Wakaingia moja kwa moja kwenye kile chumba ambacho walimuacha Lobo, lakini macho yao yalitua kwenye miili ya wachapa kazi wao ikiwa maiti, tena si maiti pekee, bali maiti za kutisha.
Mzee Pujini alikuwa kachomwa na kisu kirefu walichokuwa wanatumia kutesea watuhumiwa. Kisu hicho kiliingia kwenye jicho lake la kulia na kubaki kimenata hapohapo.
Haikuwa hivyo pekee, bali pia shingo yake ilikuwa imechinjwa na alama ya mkato huo wa kisu, ilijitokeza na kuonesha koromeo lake.
Picha nyingine ni ya Beda, msaidizi wa Mzee Pujini. Shingoni, upande wa kushoto kulikuwa na tobo refu kama liliingizwa msumari wa nchi kumi hadi kumi na mbili. Katika paji la uso, pia kulikuwa na kisu kimenatia hapo. Ilikuwa inatisha kuangalia mara mbili.
Walipoanza kutazama huko na huko ndani ya FISSA, waligundua pia kuwa wafanyakazi wao saba walikuwa wameuawa kwa njia kama ambazo Beda na Mzee Pujini walivyokufa. Ni visu na mikasi ndivyo vilivyohusika kuwamaliza wafanyakazi hao.
Na kuna maiti ilikutwa haina mavazi. Ni wazi John Lobo alivaa mavazi ya maiti hiyo kabla hajaenda kwenye Jet P112, ndege ya kivita inayokimbia kuliko zote duniani (Nimeilezea kwenye simulizi ya Jina). Na kutoroka nayo.
"Nadhani alijikamatisha ili aje kuiba hii ndege." Malocha aliongea kwa huzuni baada ya ndege hiyo ghali kuibwa na Malocha.
Ni ndege ambayo Afrika zipo mbili tu! Tanzania na Afrika Kusini.
Wakati anaongea hayo, yeye na wafanyakazi wengine, walikuwa wanatazama mkanda wa jinsi Lobo alivyokuwa anatoroka.
Alionekana akivunja mkono wa kiti kwa kujitutumua, na baadaye akachomoa mkono wa kulia na kile kilichomshika mkono wakati yupo kwenye kiti, kilibaki kwenye mkono huo kikiwa na msumari mrefu uliokuwa umekamata kiti.
Mzee Pujini alipokuwa anataka kwenda kumshika Lobo, Lobo akawahi kisu kikali alichokirusha kiustadi na kwenda kumchoma kwenye jicho. Kabla ya Mzee yule hajakaa sawa wala kusikilizia yale maumivu, Lobo tayari alishadaka kisu kingine na kuruka sarakasi ya chinichini na kisha akamcharanga mzee yule shingo yake.
Wakati huo Beda alikuwa akihangaika kufungua mlango lakini alishindwa kwa sababu ya kutetemeka kwa woga.
Wakati yupo hapo mlangoni, alisikia sauti ya Lobo ikimwambia Mzee Pujini kuwa alimuahidi kuwa atamuua wa kwanza. Beda akafanya kosa kubwa kugeuka na kuangalia tukio la mwenzake kufa, kwani kile kisu kilichopita shingoni kwa Mzee Pujini, ndicho kilichorushwa na kutua sawia kwenye paji lake la uso wake. Kabla hajadondoka, Lobo alimuwahi na kuingiza shingoni ule msumari uliokuwa umeshika kile kishikio cha kiti. Na hapohapo akauchomoa kwa fujo huku ukimuacha Beda akidondoka kama mzigo wa gunia la maharage.
Na baada ya picha ile mbaya ya mauaji ya Beda na Mzee Pujini, Lobo alionekana akienda kwenye mlango wa chumba kile na kubonyeza namba maalumu ambazo hufungulia mlango ule, na baada ya kubofya, mlango ukafunguka.
"Inaonekana anajua mengi sana ndani ya FISSA. Hadi namba za siri za kufungulia ule mlango." Malocha alionesha wazi mshangao wake wakati video ile ukiendelea kucheza.
Lobo akatoka nje ya chumba kile lakini baada ya dakika kama moja akarudi tena na kisha akachukua visu kadhaa kwenye ule mkoba maalumu wa kuhifadhia visu hivyo.
Hakuishia hapo, pia akaenda kwenye mkono wa kushoto wa Mzee Pujini na kumvua saa yake. Akaangalia kama inaenda sawa na ya ukutani, na aliporidhika, akaenda karibu na kamera iliyokuwa inachukua ule mkanda wanaouangalia wakina Malocha muda ule. Kisha akatoa ishara kwa kutembeza kidole kama ufanyavyo mshale wa saa, na mdomoni kwake alionekana akitaja maneno yasemakayo TICK TOCK, hiyo ni sauti ya mshale wa saa.
Baada ya kitendo hicho, uso wa Mubah ukabadilika na kujawa hofu zaidi kwani Lobo ujumbe ule alikuwa anamuelekezea yeye. Mubah akawa hana raha hata kidogo hasa baada ya kuona mauaji ya hatari anayoendelea kuyafanya Lobo.
Visu alivyovichukua mle 123F6 vilikuwa vinarushwa kiustadi na kuwakuta baadhi ya wafanyakazi ambapo mmojawapo alivuliwa nguo, na nguo hizo, Lobo akazieweka mwilini mwake kabla hajakwea ndege aina ya Jet P112 na kuiondoa kwa kasi toka kwenye shirika lile la siri la kipepelezi.
****
"Kuna kitu kinaendelea nchini kwetu kikubwa sana. Haiwezekani huyu Lobo akawa anajua ramani nzima ya jengo letu. Lazima kuna mtu toka humu au nje, anatoa siri za FISSA. Tunatakiwa kumjua na kumkamata mara moja." Malocha aliongea kwa hasira na kugonga meza moja kubwa ambayo ipo katika chumba maalumu cha mikutano ndani ya FISSA. Mkutano huo uliitishwa na Malocha baada ya kumaliza mkanda mzima aliokuwa anaufanya Lobo.
Wafanyakazi wapatao ishirini, ambao wote ni wakuu katika idara fulani, waliitwa kujadili suala ambalo limetokea saa moja lililopita.
Hakuna aliyejaribu kuchangia mjadala ule wakati Malocha akishindwa kuzuia hasira zake na kuanza kuiadhibu meza.
"Mkuu." Sauti moja iliita toka mlangoni. Ni yuleyule aliyekuja kuwapa taarifa kuwa Lobo katoroka. Na sasa alifungua mlango wa chumba kile kutoa taarifa nyingine.
"Mr. President anakuhitaji kwenye simu." Jamaa alitoa taarifa na kufunga mlango ule na kwenda eneo husika kwa ajili ya kuendelea na kazi yake.Kwa kuwa simu ya mezani ilikuwa mlemle kwenye kile chumba, Malocha aliipokea na kuweka sauti ya juu ili kila mmoja asikie.
"Heshima yako mkuu." Malocha alisalimia baada ya kuipokea simu ile.
"Ni nzuri. Nasikia Lobo kaondoka na Jet P112." Sauti ya Rais iliitikia salamu na kuunganisha na swali.
"Ndio, lakini tutaipata tu Mkuu." Malocha akuongea kwa sauti ya kukata kata.
"Mnajua ndege hiyo wanaenda kufanyia kazi gani? Mbona mmefanya uzembe wa hali ya juu nyie washenzi" Rais alifoka kwa sauti kali.
"Mnajua azimio la kuchukua ndege hiyo. Vipi wakienda kulipua nchi za watu huko!? Mnadhani Tanzania tutapona? Sasa nasema hivi, ndani ya wiki moja, ndege hiyo iwepo humo. Vinginevyo, watu mtakuwa hamna ajira na maisha yenu yataishia jela. Fanya nachokwambia Malocha." Rais akakata simu ile bila hata kusikiliza upande wa pili.
"Nadhani mmesikia. Sasa ni kazi tu." Malocha aliongea kwa unyonge huku akitembea kuelekea mlango wa kutokea, lakini kabla hajafanikiwa kutoka, yule mtoa taarifa akaingia tena na taarifa mpya.
"Prince Mubarak. Simu yako. Kuna mtu anashida na wewe." Baada ya taarifa hiyo, jamaa akaondoka na Mubah bila kuchelewa akaenda kwenye ileile simu na kufanya kama Malocha alivyofanya.
Malocha akiwa anaelekea kutoka, alijikuta akisimama mlangoni baada ya kusikia sauti itokayo kwenye simu ile.
"Haloo Mubah. John Lobo hapa." Lobo alijitambulisha na kumfanya Malocha ageuke na kusimama wima akimwangalia Mubah.
"Nipo kwako hapa. Na mchumba wako ananitibu majeraha mliyonipa huko. Oooh! Ana nywele laini sana, na zinanukia pia." Lobo aliongea kwa sauti ya chini huku pua zake zikisikika zikinusa kitu.
Baada ya kunusa huko, sauti ya kike ya mtoto ilisikika ikiwa na furaha kwa kulitaja jina la Uncle Mubah.
"Usijali Mubah. Mama, Mchumba wako, dada na wajomba zako wapo salama. Huyu mjomba mwenye mwaka mmoja, ni mzuri sana Mubah. Fanya chaguzi sahihi, uza au nunua roho zao.
Acha kazi yako au endelea na kazi yako, chagua ni lako Mubah. Yamebaki masaa ishirini. Tick Tock." Baada ya maneno hayo toka kwa Lobo, simu ikakatwa.
"Nifanye nini?" Swali la kwanza kuliuliza Mubah baada ya simu ile kukatwa. Alikuwa kama hajielewi pale alipouliza swali lile.
"Hiyo ndio nafasi pekee ya kumkamata huyu mbwa na kumfikisha mahakama za uharifu duniani." Malocha aliongea hayo huku akirudi katika sehemu yake aliyokuwapo mwanzo.
"Tutaweka ulinzi wa kutosha katika nyumba yako, hakuna ambaye ataingia ndani wala kusogelea eneo lile. Snipers na walinzi wenye mbwa wawezao kunusa kilometa kadhaa, watazagaa kila eneo la mtaa wako. Hakuna atakayeumia siku hiyo. Usijali kuhusu hilo." Malocha aliongezea kuhusu mkakati wake na kumtoa hofu Mubah ambaye alikuwa akihisi kama anataka kufa.
"Hapana mkuu. Familia yangu ndio kila kitu kwangu. Kazi si kitu, naomba niache kazi hii mara moja kuikoa familia yangu. Huyu si mtu wa maskhara hata kidogo, ni hatari kama moto. Naomba niachane na hii kazi, naombeni sana." Mubarak alijikuta akiomba kuacha kazi sababu ya ule mkwara mzito.
"Utakuwa mjinga kama ukiacha kazi ka sababu ya mtu mmoja kama Lobo. Sikiliza Mubah, tunakuhakikisha usalama wa familia yako. Pale walipo, tunawatoa kisiri siri na kuwapeleka nyumba nyingine zenye usalama zaidi ya pale. Na hapo kwako ndipo tutaweka watu wenye sura kama za familia yako lakini wenye uwezo wa kupambana. Usiogope kuhusu maisha ya familia yako, watakuwa salama." Mubah akashusha pumzi ndefu kama ahueni ya maneno yale toka kwa Malocha, mkuu wake wa kazi.
"Asante mkuu." Mubah akashukuru na baada ya hapo,mkakati kabambe ukaanza kupangwa na wanamkutano ule.
****
"Lakini Mkuu, mkumbuke huyu Lobo si mtu wa kuchezea. Na mbaya zaidi tunahisi humu ndani kuna vibaraka wanaosaidiana naye. Huoni kama tutakuwa tunaiuza familia ya Mubah kwa bei rahisi kabisa." Lisa alikuwa ofisini kwa mkuu wake baada ya kutoka kwenye ule mkutano mfupi.
Alienda katika ofisi ile ili kumpa ushauri kama huo Bwana Malocha.
ITAENDELEA
DUKA LA ROHO




SEHEMU YA NNE
"Utakuwa mjinga kama ukiacha kazi ka sababu ya mtu mmoja kama Lobo. Sikiliza Mubah, tunakuhakikisha usalama wa familia yako. Pale walipo, tunawatoa kisiri siri na kuwapeleka nyumba nyingine zenye usalama zaidi ya pale. Na hapo kwako ndipo tutaweka watu wenye sura kama za familia yako lakini wenye uwezo wa kupambana. Usiogope kuhusu maisha ya familia yako, watakuwa salama." Mubah akashusha pumzi ndefu kama ahueni ya maneno yale toka kwa Malocha, mkuu wake wa kazi.
"Asante mkuu." Mubah akashukuru na baada ya hapo,mkakati kabambe ukaanza kupangwa na wanamkutano ule.
****
"Lakini Mkuu, mkumbuke huyu Lobo si mtu wa kuchezea. Na mbaya zaidi tunahisi humu ndani kuna vibaraka wanaosaidiana naye. Huoni kama tutakuwa tunaiuza familia ya Mubah kwa bei rahisi kabisa." Lisa alikuwa ofisini kwa mkuu wake baada ya kutoka kwenye ule mkutano mfupi.
Alienda katika ofisi ile ili kumpa ushauri kama huo Bwana Malocha.
"Usijali Lisa. Hilo pia nimelifikiria kwa kina na ndio maana pale mkutanoni, nimesema sehemu ambayo tutaificha familia ya Mubah. Lakini kiukweli, sipo huko ambapo tutawapeleka. Wataenda sehemu nyingine kabisa." Malocha alimtoa wasiwasi Lisa huku akimpa vipande baadhi ambavyo walivifanya katika ule mkutano wao.
"Okay. Hapo sawa. Na kingine tukumbuke kuwa yule pia ni Sniper, nadhani unakumbuka sana alichokifanya nyuma. Tuwe makini zaidi tukiwa maeneo ya mtaa ule. Kila baada ya kilometa mbili, kuwe na mlinzi juu na chini. Hiyo itasaidia sana."
"Usijali Lisa, nimekuelewa na nitafanyia kazi hilo." Malocha alionesha shukurani zake kwa Lisa ambaye baada ya kutoa ushauri huo, alitoka ofisini mle na kuelekea kwa Mubah ambapo napo alikuwa anamtia moyo na kumueleza mikakati waliyoipanga.
****
Saa tatu asubuhi, yakiwa yamebakia masaa kuna na matano ili ahadi aliyotoa Lobo itumie, gari moja nyeusi ilisimama nje ya nyumba moja kubwa kiasi na baada ya sekunde kadhaa, alishuka kijana Mubah na kuelekea katika nyumba hiyo.
Katika shirika la siri la kipelelezi, sehemu ambayo Mubah anafanyia kazi, si ruhusa kwa mfanyakazi yeyote kutoka ndani ya shirika hilo mida mibaya hasa usiku. Na ndio maana hata Mubah alipopokea simu ya matatizo ya familia yake, hakuondoka hadi asubuhi hiyo ambayo kwake ilikuwa kama mwaka kuifikia.
"Oooh! Mubah. Ulikuwa wapi mwanangu." Mama yake Mubah ambaye alionekana wazi uzee umemchukua, alimkimbilia kwa shida mwana wake kabla ya familia nzima nayo haijafanya hivyo.
"Usijali mama. Nipo salama kabisa na nimekuja kwa ajili yenu." Mubah aliwapa moyo ndugu na familia yake.
"Jana alikuja mtu anaumwa, akamuomba wifi amsaidie kutibu majeraha. Sisi tulikuwa tunamwogopa, ila akasema anafahamiana na wewe. Na hata baadae alipopiga simu, tukasikia sauti yako. Sema akaenda kuongelea nje na baada ya kurudi alimuomba wifi afanye alichokiomba mwanzo. Yaani amtibu yale majeraha." Dada wa Mubah alitoa taarifa ambazo kwa Mubah alibaki akiwa kakodoa macho tu. Ye' alidhani Lobo alikuja na kuitishia amani familia yake, na kumbe alikuja kwa njia za kiutu.
Akakuna kichwa chake kijana huyu huku akishindwa afanye nini kwa wakati ule.
"Pia alipoanza kuondoka aliacha ujumbe ule pale." Dada wa Mubah alisonta kidole chake ukutani na kuonesha ujumbe aliouacha John Lobo.
Alisogea karibu maana ni kama alikuwa hauoni japo ulikuwa na maandishi makubwa meusi kwenye karatasi nyeupe iliyochomwa kwa kisu kwenye ukuta huo wa nyumba iishiyo familia ya Mubah.
Ujumbe ulisomeka "TICK TOCK" na kwa juu yake saa ya ukutani ya Mubah ilikuwa ikienda taratibu kwa mlio huo wa tick tock. Mubah akahisi kuchanganyikiwa.
"Anko. Anko yule mwingine kanipa hii hapa na ......" Kabla ya yule mtoto wa dada yake, mtoto mwenye umri wa miaka saba hadi nane hajamaliza kauli yake, Mubah tayari alimpora kile kitu ambacho alikuwa kakishika yule mjomba wake.
Kilikuwa ni kibanio kizuri cha nywele kilichonakishiwa na madini ghali ya dhahabu.
Mjomba yule wa Mubah alikuwa anafuraha kila alipokiangalia, lakini kitendo cha Mubah kumpora na kuanza kukikanyaga kanyaga, kikafanya yule mtoto asiseme kitu kingine ambacho kapewa. Alikuwa kavaa pambo zuri katika nkono wake, pambo hilo pia alipewa na John Lobo.
Mjomba wa Mubah akakimbilia chumbani kwa mama yake na huko safari ya kilio ikachukua nafasi yake. Aliona kama Mjomba wake kamkatili sana nafsi yake kwa kile kitendo. Watoto bwana.
"Naomba mjiandae. Leo saa mbili usiku tutaondoka katika nyumba hii. Tupo katika hatari kubwa sana. Na ninaomba, jirani au mtu yeyote asijue ni wapi au muda gani tunatatoka hapa. Tupo katika hatari." Mubah akiongea huku uso wake ukiwa na mashaka makubwa sana hali iliyofanya familia yake kuzingatia maneno yake. Familia nzima ilimjua Mubah kama askari wa Tanzania. Hivyo aliposema maneno hayo, kila mmoja akaamini kuna kitu cha hatari hasa pale walipovuta sura ya yule mtu aliyekuja usiku wa jana yake.
"Usiwe na wasiwasi dear. Mambo yote tutayafata." Ilikuwa ni sauti ya Zakia Bin Ashib ikimfariji mpenzi wake walipokuwa chumbani wakipanga baadhi ya vitu vyao kwa ajili ya kuondoka usiku huo.
Maneno hayo ya faraja, yalikuja pale Mubah alipomueleza mkasa mzima uliomsibu siku ya jana yake tangu alipoanza kukimbizana na Lobo hadi unyama alioufanya kule FISSA.
Ndani ya maongezi hayo, Mubah hakuthubutu kuongea kuhusu ndege iliyoibiwa au mahali ambapo anafanyia kazi.
Zakia Bin Ashib, kila kukicha alikuwa anamuomba mpenzi wake amueleze ni wapi anafanyia kazi zake, lakini Mubah alikuwa anakataa kusema ukweli kwa sababu ya masharti ya shirika lake.
****
Saa mbili usiku, kwa kutumia handaki dogo lililo katika sebule la Mubah, familia yote iliingia huko na kutokezea katika zizi la ng'ombe, kilometa kadhaa kutoka kwenye nyumba ya Mubah. Hakuna aliyewahi kufikiria kuwa nyumba ya Mubah inahandaki hilo. Awe mama yake au mchumba wake. Hivyo kitendo cha wao kuingizwa huko na kutokea kwenye zizi la ng'ombe, likawa ni hadithi nyingine ya kusisimua ambayo Mubah alipaswa kuilezea.
Baada ya kuibukia zizini huko, gari moja ya kimarekani, ilifunguka milango yake na watu idadi ya familia ya Mubah, walijitojeza. Macho ya familia ya Mubah ikazidi kushangazwa hasa wale watu wanavofanana nao.
Watu wale, wakaipita familia ya Mubah na kuingia katika handaki lile lile ambalo walitokea familia ile.
Familia ya Mubah, ikapanda na gari ile na safari ya kwenda pasipojulikana ikachukua nafasi yake wakati huo Mubah alirudi nyumbani kwake na kuanza kutoa maelezo yote yanayofaa.
Huko nje ulinzi ulikuwa ni wa hali juu kuliko hata ule ambao huwekwa rais wa nchi fulani akifika nchini.
Wapelelezi walikuwa wakipita katika mtaa huo kama wapita njia na hakuna ambaye alihisi kuwa wale ni wapelelezi. Wadunguaji (Snipers) walikuwa kila upande katika eneo lile wakiwa na bunduki zao maalumu kwa ajili ya kudungulia mtuhumiwa wao.
Huko FISSA, Lisa na Malocha walikuwa wanawapa taarifa watu wao wa kazi hasa kwa picha ambazo zilikuwa zinatumwa kwa satellite. Kila mtu tofauti waliyemtilia mashaka akipita, FISSA walitoa taarifa kwa kikosi kazi chao kilichoongozwa na Mubah.
Hatimaye zikabaki dakika kumi na tano za ahadi ya Lobo kutimia. Kila mtu moyo ukawa unamdunda kwa sababu mtu wanayemtega si mtu mdogo. Ni eidha wamkamate hai au akiwa maiti. Lakini je!? Uhakika wa kumkamata upo? Swali hilo ndio likafanya mioyo ya wachapakazi wale kutokuwa na amani.
Mbwa wasiojua kubweka bali kufanya kazi yao, nao wakawa wananusa kila sehemu walipopitishwa. Ulinzi ulikuwa mkubwa haswa. Mtaa mzima anaoishi Mubah ulitapakaa ulinzi wa hali ya juu.
Zikiwa zimebaki dakika saba za jambo alilopanga Lobo kutimia, simu ya Mubah ilianza kuita mbele ya familia yake ile mpya. Namba ya mpigaji haikuonekana bali kuandika neno 'private call'.
Mubah akawapa ishara wale watu waanze kutimiza maadhimio waliyoyapanga.
Bila kuchelewa, meza kubwa ya mle ndani ikafunuliwa na watu wote wakasogea pale mezani na kutazama mahanjumati na mapochopocho kadhalika yaliyoandaliwa kiufundi na wafanyakazi wa FISSA. Wakaanza kusali kwa sauti na ndipo Mubah akasogea pembeni kidogo na kupokea simu ile.
"Hallow." Mubah akaita baada ya kupokea simu.
"Heloo Mubah. Niambie kamanda wangu." Sauti ya Lobo iliitikia upande wa pili na wakati huo wale waliondaliwa kupambana na Lobo, walizidi kupamba moto kuombea chakula.
"Stupid Lobo." Mubah akatoa tusi dogo.
"Mmmh! Siku hizi mmeokoka Mubah. Mnasalia chakula kwa kukemea kwa jina la Yesu. Muislamu halisi kama wewe!?" Lobo aliongea na kucheka sana na hapohapo wale washirika wa Mubah walikatisha sala zao na kugundua kuwa walikuwa wanasali Kikristo wakati familia ya Mubah ni Waislam.
Japo Mubah alikuwa mbali nao, lakini wao pia waliyasikia yale maongezi kwa kutumia vinasa sauti vilivyokuwa masikioni mwao kama vishikizo.
"Okay. Ondoa shaka Kamanda, siwezi kuingilia maisha uliyoyaanza na familia yako ya kujibambika.
Nipo hapa kukukumbusha kuwa zimebaki dakika tano na sekunde kadhaa ili ahadi yetu itimie. Huku ulipoileta familia yako, nadhani panafaa sana kufanya kazi yetu. Na kingine, kabla sijafanya chochote kwa huo ugeni ulioniletea kwako, naomba utoke nje na ushuhudie mara ya mwisho mtaa wako. Toka, waweza kuniona navyoua vimbwa vyenu." Lobo akamaliza kuongea lakini hakukuta simu.
Mubah akawa kama kachanganyikiwa, akatoka nje kasi na kuanza kuangaza huko na huko, akasogea hadi barabarani na kuzidi kushangaa. Aliweza kuwaona wapelelezi wenzake na wakamuoneshea ishara ya kumuuliza vipi? Lakini Mubah ni kama alikuwa kapandwa na kichaa na wakati huo simu ikiwa sikioni kwake.
"Ha ha hahahaaa. Mubah, Mubah, Mubah. Bado dakika mbili. Embu ongea kwanza na mjomba wako." Lobo alisikika tena kwenye simu ile aliyoipiga.
"Ankoo tusaidie tumefungwa kamba na jambaziii." Mjomba wa Mubah alipiga kelele kwa nguvu na kumfanya Mubah ahisi kama anamabawa lakini hawezi kupaa kwenda kutoa msaada. Akabaki katikati ya barabara na simu ikiwa sikioni kwake.
"Ooh! Nasikia pia ulikanyaga-kanyaga kibanio changu. Zawadi nzuri kabisa kutoka Malyasia. Nimemletea anko wako lakini umekiharibu. Ila hamna tatizo, bali tatizo litakuwepo kama pale chini ulipokikanyagia kitabaki palepale. Najua kipo palepale, embu nenda kakiangalie." Mubah akatoka mbio tena na kuingia tena nyumbani kwake. Hapo alichokishuhudia, hakika hakuwahi kukifikiria katika kichwa chake.
Miili minne, akiwepo na yule mtoto ambaye walimfanya kama mjomba wa Mubah ilikuwa imelala kifudifudi kwenye viti walivyokalia huku moshi mdogo ukiwatoka midomoni mwao. Nyuso zao zilijikunyata na kuwa kama za wazee wa miaka mia moja. Damu ilikaushwa katika miili yao kwa kutumia sumu kali inayosambaa kwa hewa.
Mubah alipoangalia sehemu alipokanyagia kile kibanio, alikuta kuna majivu machache ambayo yalitokana na kile kibanio kuungua.
"Nadhani umeona. Sikutaka kukuua wewe. Na hata hicho kimdoli mlichokifanya ni kitoto kidogo, nacho kingekuwa na uhai, ningeua tu! Na nitakiua hichi nilochonacho huku baada ya dakika tatu kupita." Lobo aliongea kwa sauti iliyojaa chuki.
"Hiyo sumu inatoka kwenye madini ya yellowstone. Madini yafananayo na almasi sema yenyewe ni ya njano na yanayeyuka. Husambaa kwa sekunde thelathini baada ya kuchomwa moto na hupotea kwa sekunde kumi na tano baada ya kusambaa. Kibanio hicho nilieweka jiwe dogo sana la madini hayo. Na nilitega kifyatulio ambacho kikifyatuka, hutengeneza moto. Nimefanikiwa hilo Mubah, asante kwa kuniletea wateja hao. Bado dakika mbili." Lobo akamaliza kuongea na kuacha simu hewani ili asikie upande wa pili.
"Nooooooo. Don't do that Lobo. Please." Mubah alijikuta akipiga kelele ya nguvu huku akijaribu kuomba msamaha.
Kelele hizo zikawafikia walinzi wa nje nao wakakimbilia ndani wote, hata wale wadunguaji nao ikabidi kushuka kule juu haraka na kwenda ndani kutazama kile kinachoendelea. Walichokikuta ndani, hakika kiliwatoa machozi na kuwaacha katika mshangao. Sasa hivi miili ile ilikuwa ikipukutika kama majivu ya karatasi na mwisho wake yakabaki mafuvu yamekaa kwenye viti.
"Sasa naweza kukusikiliza Mubah, unadakika moja. Toka nje na mtu yeyote asikuone kama umetoka. Nataka nikuoneshe kitu." Sauti ya Lobo ilisikika ikimuongelesha Mubah kwenye simu.
Mubah akafanya kama alivyoambiwa.
"Sogea mbali na nyumba yako. Na itazame kwa macho ya umakini, utaona kitu cha kukupendesha. Zimebaki sekunde kumi na tano muda wetu uishe." Lobo alitoa ombi ambalo Mubah alilifanya haraka na kukazia macho yake kwenye nyumba yake ambayo ndani yake kulikuwa na wafanyakazi wenye uhai wapatao kumi na moja.
"Tano, Nne, Tatu." Lobo akaanza kuhesabu sekunde zilizobaki hadi akafikia moja, kisha sifuri.
Macho ya Mubah yakajawa na taharuki ya ajabu. Hakuwahi kufikiria katika maisha yake kuwa kuna siku atashuhudia kile anachokishuhudia kwenye nyumba yake. Alishazoea ni kwenye filamu za kivita tu! Ndio awezapo kuona yale mambo.
Lakini sasa anajionea kwa macho yake yale ambayo alikuwa anayaona kwenye filamu.
Nyumba yake ililipuka yote na kuteketea kama vile uonavyo kwenye filamu ndege au meli inapopigwa bomu. Nyumba ikazidi kuteketea na kuteketea hadi vile vilivyomo ndani.
Mubah akapiga magoti na kulia kwa sauti huku akipiga chini ngumi kadhaa lakini bado hakukuta simu bali kusikiliza kilichokuwa kinataka kujiri.
"Woooou. I like that sound of boom, yoo. (Waau. Nimeipenda hiyo sauti ya buum, yoo)" Lobo alisikika akiongea hayo kwenye simu baada ya ule mlipuko mkubwa kutokea kwenye nyumba ya Mubah.
"Please Lobo, naomba uiache familia yangu. Nakuomba Lobo, nitaacha kazi kama utakavyo." Mubah akikuwa anaomba msamaha huku kapiga magoti katikati ya barabara ya lami iliyokuwa inapitwa watu huku na huko kukimbia ule mshikemshike wa bomu.
"Too late Mubah. Umechelewa mwenyewe kufanya chaguo lililo sahihi na mimi huwa sikwepeshi kauli yangu." Lobo aliongea hayo na hapohapo sauti ya 'kitoto kichanga' ikaanza kulia.
ITAENDELEA

DUKA LA ROHO




SEHEMU YA TANO
Mubah akapiga magoti na kulia kwa sauti huku akipiga chini ngumi kadhaa lakini bado hakukuta simu bali kusikiliza kilichokuwa kinataka kujiri.
"Woooou. I like that sound of boom, yoo. (Waau. Nimeipenda hiyo sauti ya buum, yoo)" Lobo alisikika akiongea hayo kwenye simu baada ya ule mlipuko mkubwa kutokea kwenye nyumba ya Mubah.
"Please Lobo, naomba uiache familia yangu. Nakuomba Lobo, nitaacha kazi kama utakavyo." Mubah akikuwa anaomba msamaha huku kapiga magoti katikati ya barabara ya lami iliyokuwa inapitwa watu huku na huko kukimbia ule mshikemshike wa bomu.
"Too late Mubah. Umechelewa mwenyewe kufanya chaguo lililo sahihi na mimi huwa sikwepeshi kauli yangu." Lobo aliongea hayo na hapohapo sauti ya 'kitoto kichanga' ikaanza kulia.
"Muache mwanangu we kafiri. Na kwambia muache." Sauti ya dada wa Mubah ilisikika na kupenya kwenye ngoma za Mubah. Wakati huo sauti ya.kichanga iliendelea kulia na mara ikakata ghafla baada ya mlio mkali wa bastola kutoka.
"Nooo." Sauti ya dada wa Mubah ilisikika mara moja na baada ya hapo haikusikika tena.
Lobo akiwa anachalaza mluzi usioeleweka ni wa wimbo gani, akaongea kwenye simu ambayo Mubah alikuwa bado hajaikata.
"Dada yako kazimia baada kuona mwanaye mdogo nikitoboa kichwa chake kwa risasi yangu. Hahahahaaa. Nasikitika hutoona maiti zao kwa macho yako bali utaona picha za maiti yao. Naua na kupiga picha." Lobo alimpa taarifa Mubah ambayo ilimzidishia maumivu moyoni.
"Lobo tafadhali, nisamehe. Kuwa na utu we' mtu. Naomba uniachie familia yangu." Mubah aliongea kwa sauti ya kitetemeshi iliyojaa kilio.
"Ankoo tuokee." Sauti ya mjomba kipenzi wa Mubah ilisikika.
Mubah akahisi mwenye kutaka kufa lakini hakufa bali alizidi kushikilia simu yake sikioni.
"Anko kwa heri. Labda tutakuja kuonana tena. Nakupenda sana ank....." Yule mjomba wa Mubah hakumaliza kuongea kitu akamezwa na mlio wa bastola ya John Lobo na hapohapo hakusikika tena.
Mubah alilia kwa sauti ya juu ambayo ilimfanya adondoke kwenye lami alipokuwa kapiga magoti na wakati anadondoka, akaliona gari moja jeusi likipita karibu yake na mtu aliyekuwamo mle ndani, alimuangalia kisha akatabasamu kwa tabasamu pana kabla hajafunga kioo cha upande wake kilichokuwa cheusi.
Sura ile ya kiume haikuwa ngeni kwake, lakini alisahau kaiona wapi. Na wakati huo alikuwa hana nguvu zozote za kuinuka pale alipo ili akimbize lile gari. Badala yake, alilala pale chini taratibu huku akianza kuona giza likitanda usoni pake.
"Huyu nimeingiza bastola mdomoni na kufumua ubongo wa nyuma kwa bastola yangu. Ha ha haaa raha sana kuua." Hiyo ndiyo sauti ya mwisho ya kutoka kwa Lobo ambayo Mubah aliisikia.
Fahamu zikapotea kwa sababu ya machungu tele yaliyojengeka moyoni mwake.
****
Ilichukua karibu saa moja kwa Mubah kuamka na kushtuka tena baada ya kukumbuka yale ya nyuma. Tayari alikuwa yupo ndani ya FISSA baada ya wafanyakazi wenzake kuja kumuokota pale chini alipokuwa kazimia.
"Husna, Husna, Husna, Husnaaa. Kweli umeenda uncle wangu niliyekupenda kuliko wote nyumbani? Nitacheka na nani tena, nani atanifurahisha pale niwapo na machungu. Ooh! Mungu wangu nisaidie." Mubah alikuwa akilia kwa uchungu mbele ya wafanyakazi wengine ndani ya FISSA.
"Nyamaza Mubah. Pole sana. Hakuna ambaye hana hayo machungu. Tuliizoea familia yako na tuliwazoea wafanyakazi wetu, lakini wote hatunao tena. Inatuuma sana." Dada mmoja mrefu na mweusi lakini mwenye mvuto wa aina yake, alijaribu kumbembeleza Mubah aliyekuwa akilia kama mtoto mdogo.
"Atalipa tu huyu mbwa. Nitamuua kwa risasi zangu. Nitamuua Lobo na washirika wake wote. Nishamuona mmoja, nitamsaka na kumuadhibu pumbavu yule." Mubah aliongea kwa hasira huku akinyanyuka katika kitanda cha dispensari iliyopo mlemle ndani ya FISSA.
Akashika kitasa cha mlango wa kituo kile cha afya na kutoka humo kituoni na kuanza kuelekea ofisi za kipepelezi hasa kule zinapokaa kamera maalumu za kufatilia mienendo yote ya kazi za FISSA.
"Niwekee mkanda wenye tukio zima la pale nyumbani." Mubah aliongea mbele ya mwanakaka mmoja aliyekuwa anacheza na kompyuta za mle.
Yule jamaa hakuwa na kipingamizi hasa kwa kuwa ule mkanda unamgusa sana aliyemuamuru auweke. Akauweka na kisha ukaanza kucheza matukio yote yaliyokuwa yanaendelea siku hiyo kabla Mubah hajazimia.
Mkanda huo ukaenda hadi mahali ambapo nyumba ya Mubah ilipolipuliwa.
"Rudisha hapo kidogo." Mubah akamwambia maneno yale yule opareta. Jamaa bila ubishi akarudisha sehemu ambayo inaonesha nyumba ya Mubah ndio inataka kulipuka.
"Umeona hapo?" Mubah akaonesha kwa kidole sehemu husika anayotaka yule opareta aione.
Opareta akatazama kwa makini, alipoona kama hapaoni, akapavuta kwa ukaribu kisha akatoa mawimbi ambayo yanasababisha picha isionekane vema.
"Okay. Hili ni bomu toka kwenye RPG hili." Opareta akaongea baada ya kugundua hilo jambo.
"Sasa kumbe John Lobo hayupo peke yake. Wakati nyumba hii inalipuka, mimi nilikuwa naongea naye na alikuwa na familia yangu mbali na pale nyumbani. Lazima tuwasake hawa washenzi." Mubah aliongea kwa hasira na kukita ngumi nzito kwenye meza iloyomo mle ndani.
Kwa hasira akageuka nyuma na kutaka kuanza kutoka lakini baada ya kugeuka, akakutana na sura ya Malocha.
"Mubah. Unatakiwa kupumzika kwa miezi miwili. Hii kesi tuachie sisi, tutaimaliza tu!" Malocha alimwambia Mubah ambaye alimtazama kwa jicho kali na la ghasia.
"Huu ushauri ungenipa kabla familia yangu haijaondoka duniani. Ungeniambia niache kazi kabisa ili familia yangu ipone, lakini siyo sasa hivi. Nitapigana kufa na kupona ili huyu mbwa nimkamate. Nimeshajua hayupo peke yake, nitamsaka tu!" Mubah alimueleza Malocha na kumpita pale aliposimama kwa kutaka kutoka ndani ya ofisi ile. Lakini Malocha akamkamata mkono na kumrudisha mbele ya upeo wa macho yake.
"Nilipoteza familia yangu kwa mkono wa huyuhuyu Lobo. Kwa risasi tano alizopewa, hakumkosa yeyote katika familia yangu. Nilijawa na jazba kama wewe hivyo, nikapania kumuua na nilifanikiwa kukamatiwa huyu mtu, nikawa naye uso kwa uso akicheka kwa dharau. Nilikata shingo yake, kisha nikamvunja miguu kwa risasi mbili na tatu nikamchapa nazo kifuani (MKASA HUU UPO KWENYE RIWAYA YA JINA). Nikadhani amekufa, lakini leo hii tunapambana naye tena. Naona ni kama mzimu au shetani ambaye hafi, au jini. Lobo huwezi kupambana naye peke yako na ukashinda vita yake. Utapotea Mubah." Malocha aliongea kwa makini na kwa upole huku machozi yakiwa yanataka kumtoka kwa mbali.
"Baada ya kupoteza familia yako, ukamsaka na kumpata kisha ukamuua. Niachie na mimi, nimepoteza familia yangu, nimsake nimpate kisha nitakuletea kiwiliwili chake." Sauti ya kujiamini toka kwa Mubah ilipenya masikioni mwa wale wanaofatilia yale maongezi, akiwemo Malocha.
"Nimekwisha kwambia, acha hiyo kesi. Ni amri siyo ombi. Nakupa miezi miwili ya kupumzika, utake usitake, utaenda mapumziko." Malocha ikabidi atumie nguvu za uongozi wake kuwasilisha hisia zake. Mubah akatulia kwa muda kabla hajarudi kwa yule opareta na kuchukua ule mkanda wenye tukio zima la siku hiyo.
"Familia yangu ipo?" Mubah alimuuliza Malocha kabla hajachukua hatua nyingine kutoka mle ofisini.
"Nyumba na walinzi wakiwa na familia yako, vyote vilipigwa kiberiti. Hakuna ambacho kimesalia, labda majivu." Malocha alimjibu Mubah huku uso wake akiutazamisha mbele na chozi la kiume likamtiririka jasiri huyu upande wake wa kulia.
"We will be fine boss. Don't cry sir (Tutakuwa sawa mkuu. Usilie)" Mubah akamwambia mkuu wake huku akimgonga gonga bega lake kumfariji.
Baada ya hapo, akatoka nje ya ofisi ile na kuelekea kwa Lisa ambaye baada ya kumuona Mubah, alimkimbilia na kumkumbatia.
"Upo sawa Mubah." Lisa alimuuliza baada ya kumuachia.
"Nipo sawa Lisa. Lakini bado sijajua ni vipi Lobo alijua kuwa familia yangu ipo kule." Mubah alimuuliza Lisa.
"Nadhani kuna kitu alikiacha katika mwili wa mwanafamilia wako, hicho ndio kilikuwa na GPS ambayo inaonesha popote waendapo." Lisa akamjibu Mubah na hapo Mubah akakumbuka kile kibanio kilichokuwa kina sumu hatari kutoka kwenye Yellowstone. Lakini pia akakumbuka maneno ya mjomba wake kuwa alipewa kibanio na kitu kingine ambacho yule mjomba hakumalizia kukisema baada ya Mubah kumpora kile kibanio.
"Nadhani itakuwa hivyo maana kuna sumu waliivuta wale wenzangu wengine, ilitoka kwenye banio ambalo mimi nilimpora Husna, mjomba wangu. Lakini pia Husna alipewa kitu kingine na Lobo, nadhani kiliambatana na hiyo GPS. Ila hamna tatizo, naenda likizo ya miezi miwili, lakini sitalala. Nitakutumia sana kukupa taarifa za kila upelelezi wangu." Mubah alimwambia Lisa na kisha wakaongea maneno machache ya kufarijiana kabla Mubah hajachukua jukumu la kwenda chumba cha mapumziko kilichomo FISSA.
****
"Bado sijaipata mkuu. Na familia yote ya Prince Mubarak imeteketea." Ni sauti ya Malocha ikiwa inaongea kwenye simu ambayo ilipigwa usiku ule wa saa tano. Alikuwa rais wa nchi akiulizia ndege kama imepatikana.
"Nasemaje. Mi' sijali hayo mambo yenu ya kijinga kwenda kukamata mtu mmoja kwa kutumia watu mia badala ya kufata maelezo ya mtu anachokitaka. Nachotaka mimi hapo ni hiyo ndege tu! Jumamosi ijayo Rais wa Cuba anakuja, unadhani kuna nini kitatokea kama hiyo ndege haijapatikana? Naitaka hiyo ndege kabla ya Jumamosi." Rais akakata simu na kumuacha Malocha akiwa katika wakati mgumu kuliko nyakati zote ambazo kawahi kuzipitia kimaongezi.
Akiwa na hasira za kuweza kufanya jambo lolote bila kujizuia, akatoka nje ya ofisi yake na kisha akaita wafanyakazi wote wa lile shirika.
"Ondokeni wote usiku huu. Sitaki mtu humu." Malocha aliongea kwa hasira baada ya mjumuiko wa wafanyakazi wake kuja eneo husika.
"Lakini mkuu, si ruhusa kuondoka usiku." Mfanyakazi mmoja alikumbusha sheria ya shirika lao.
"Ninekwishasema. Lawama zote nitabeba mimi, na si yeyote humu. Poteeni haraka kabla sijafanya kitu cha ajabu humu." Walimjua Malocha vilivyo, hivyo baada ya kauli ile, wakazima vitendea kazi vyao na kwenda kwenye usafiri maalumu kwa ajili ya kuwatoa nje ya shirika lile.
Sasa shirika lote la kipelelezi likawa limebaki patupu. Hakuna mtu zaidi ya Malocha aliyekuwa analanda huku na huko akijaribu kutafakari hili na lile kuhusu John Lobo.
"Kanishinda huyu mbwa. Sina jinsi, inabidi nimtafute tu! Nadhani nitafanikiwa." Yalikuwa maneno ya Malocha akiongea peke yake.
Baada ya maneno hayo, akaenda moja kwa moja ofisini kwake na kutwaa simu ya mezani, kisha akaifungua na kuweka kitu fulani ambacho kilisaidia watu wasinase maongezi ambayo watakuwa wanayaongea kupitia simu hiyo.
"Halo kaka." Malocha aliitika baada ya simu kupokelewa.
"Vipi Malocha." Jamaa wa upande wa pili alisalimia.
"John Lobo karudi." Malocha alimwambia yule jamaa wa pili.
"Mkamateni sasa." Jamaa akajibu kifupi na kukata simu.
Malocha akapagawa kwa kitendo kile cha jamaa. Hakujua atafanya nini ili kumshawishi yule jamaa amsikilize.
Akatulia kwenye kiti chake akitafakari njia za kumvuta mtu wake amsikilize. Baada ya dakika kadhaa, akapata wazo la cha kufanya. Akatwaa simu yake tena na kupiga namba zilezile.
"Usinipigie tena Malocha." Jamaa alisikika akilalamika kwenye simu.
"Lisa yupo katika hatari ya kuuawa na Lobo." Malocha akaongea kwa kifupi na kisha akakata simu.
*****
NYUMBANI KWA LISA.
Alifika mida ya usiku sana na kukuta aishio nao wamekwishalala. Akafungua mlango wa nyumba yake kwa funguo ambazo anazo na kisha akaingia chumbani kwake ambapo alivua mavazi yake ya kazi na kuyaweka pembeni. Akavaa mavazi ya kwenda kuogea na baada ya hapo akaelekea bafuni kujisafi.
Dakika saba za kujisafi zikatimia, ndipo akatoka akijipukuta na kuelekea katika kitanda ambacho analala na mume wake Bwana Gunner, jamaa mwenye asili ya Kameruni na Kirusi.
Lisa akavuta kipande cha shuka alichojifunika mumewe na yeye akajifunika tayari kwa kuutafuta usingizi.
"Kazi zako vipi. Na leo mbona usiku?" Gunner alimuuliza mkewe Lisa.
"Kuna matatizo makubwa ofisini." Lisa alijibu kimkato na kutulia kabla ya kushtuliwa na mkono wa Gunner uliopita kiunoni kwake na kumgeuzia upande wake. Wakawa wanabadilishana pumzi kwa sababu sasa walitazamana.
"Kumetokea nini?" Gunner akamuuliza Lisa swali ambalo Lisa alilijibu pia kwa kifupi lakini lilieleza kila kitu ambacho kilitokea.
Baada ya maelezo hayo, Gunner alimbusu Lisa mdomoni na Lisa naye hakuwa nyuma bali kumpa ulimi kabisa bwana yule mweusi na aliyejengeka mwili sababu ya mazoezi ayafanyayo.
ITAENDELEA
 
inakuwaje mtu unaquote hadithi nzima? tuache kukatana stimu bhanaa!.......mtoa hadithi mekulove buree bila hata chenchii!....tafadhali endelea maana haya ni zaid ya mahaba kwa hadith zako tam
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA MBILI
Sitakuwa tayari kumpoteza Martina kama nilivyompoteza Mjomba wangu. Nitakuwa nawe Lisa." Mubah aliongea kwa sauti ya hamasa na kuonekana mwenye utayari kwa lolote lile.
"Sijawahi kuingia mapambanoni. Huu ndio muda wangu wa kufanya hivyo. Nitakuwa nyuma yako Lisa." Opareta wa mitambo wa Malocha alisimama na kuungana na wakina Lisa waliokuwa wanafarijiana.
"Mimi pia. Naingia katika mpambano." Jamaa mwingine akakamilisha kundi la watu watano ambao waliweka mikono yao katika umoja na kisha kwa pamoja wakatamka. "Kwa Martina na Lisa." Sauti hizo zikawapa amsha katika mioyo yao na mpango kabambe wa kumuokoa Martina ukaanza papo hapo.
****
TURIN, ITALIA.
Pirlo baada ya kutoroka salama kule Vatican, alichukua ndege binafsi na kwenda moja kwa moja katika Jiji lingine la marah, Jiji la Turin. Si kama alienda huko kwa ajili ya raha, bali alienda kwa ajili ya taarifa maalumu ya alichokipata usiku wa kuamkia siku hiyo.
Akaingia katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro lililopo hapo Turin na kisha akakaa kwenye viti vya kanisa hivyo na kupiga ishara ya msalaba kwa kutazama sanamu ya Bikira la Maria iliyokuwa imembeba mtoto mdogo na shingo yake ikiwa imepindia kushoto kuonesha huruma ya Mama huyo.
Ndani ya kanisa kulikuwepo na watu sita pekee wakionekana wenye kufanya sala za toba baada ya maungamo yao. Pirlo alikuwa katika sala fupi za kujiandaa kabla hajaenda kwenye maungamo.
Ilikuwa ni kawaida yake kufanya maungamo kila Alhamisi, na alikuwa anafanya maungamo hayo katika kanisa moja tu! Ambalo alikuwepo muda huo. Japo pia alikuwa anafanya maungamo hayo katika kanisa hilo, pia alikuwa anafanyia kwenye kijumba kilekile kila akienda. Na muda wa saa saba ndio ulikuwa muda wake wa kufanya maungamo hayo.
Ilipotimu saa saba kamili, akaenda kwenye kijumba hicho maalumu na kupiga magoti tayari kwa maungamo.
"Father. I need to go back in Tanzania. (Baba. Nahitaji kurudi Tanzania)" Pirlo aliongea hayo baada ya kupiga ishara ya msalaba.
"Why? (Kwa nini?)" Yule Padri akamuuliza swali Pirlo. Pirlo akaanza kumuhadithia kila kitu alichokisikia na kukiona.
Wakati yupo kwenye ndege binafsi akielekea Turin, Pirlo alitoa kompyuta yake mpakato na kisha akavua saa yake ambayo ilikuwa inagonga kengere usiku wa jana yake. Kwenye saa hiyo, akachomoa kitu kidogo kama memori kadi lakini hakikuwa memori kadi kwa sababu chenyewe waweza kukiwasha na kukizima.
Akakiwasha na kisha akakichoneka katika kifaa maalumu ambacho hutumika kuchomekea memori kadi. Akaingiza kifaa hicho kwenye kompyuta yake mpakato na kuperuzi kila kitu kilichoonekana mle kwenye kile kifaa alichokitoa kwenye saa. Hapo akaanza kuona tukio zima ambalo limefanyika nchini Tanzania hasa baada ya ule mtambo wa SGT kufunguka. Akaona eneo zima ambapo mtambo ule ulikuwepo na akaona ni nani anamiliki mtambo huo.
Pia akaona kazi uliyoifanya ya kutafuta namba fulani ambayo ni za Malocha na kisha baada ya kuipata, mtambo ule ulifungwa.
Pirlo hakuishia hapo, katika kile kifaa, pia akafanikiwa kudaka maongezi yaliyofanyika katika namba ile iliyochukuliwa na SGT. Pirlo akapumua pumzi ndefu na akawa hana raha baada ya kugundua nia ya wale watu.
Akafunga kompyuta yake mpakato na kutulia. Kisha akili yake akaihamishia China alipowahi kusomea Sayansi.
SHANGHAI, CHINA.
Kulikuwa kuna jopo la wanafunzi wapatao kumi katika chumba kimoja cha kufanya majaribio ya Kisayansi. Katika wanafunzi hao kumi ambao walionekana akili yao wameegemeza kwenye kutengeneza kitu fulani, kulikuwa kuna mweusi mmoja tu!
Mweusi huyo alijiita Hyung Sheing. Wenzake walijuwa historia yake kuwa alikuwa anaasili mbili, ya Kichina na Kimarekani. Hyung aliwaambia kuwa baba yake ni Mchina lakini Mama yake ni Mmarekani mweusi ambaye alifariki pindi anamleta yeye duniani. Pia akawaambia wenzake kuwa baba yake aliondoka duniani wakati yeye anamiaka kumi tu! Aliishi katika uyatima hadi alipopata mfadhili akiwa na miaka kumi na mitano, na ndiye anayemsomesha hadi muda huo akiwa na miaka ishirini na saba.
Historia hiyo ikawafanya wenzake na wanafunzi wote kumuona wa kipekee na kuwa naye bega kwa bega ili atimize ndoto zake za kuwa mwanasayansi mkubwa duniani.
Na ndoto hiyo ndiyo alikuwa anaifanyia kazi siku hiyo ambapo jopo la wanafunzi wenzake lilikuwa likitengeneza mtambo uliyoitwa Satellite GPS Traces (SGT). Baada ya kuumaliza mtambo huo, waliujaribu na kuona unafaa sana kwa ajili ya kufanya kazi za kipelelezi na nyingine nyingi zenye manufaa na zisizo na manufaa.
Lakini japo pia walifanikiwa kuutengeneza mtambo ule, Hyung akatoa wazo kuwa watengeneze kitu ambacho kitaweza kuufatilia mtambo huo kwa chochote utakachofanya. Wengi walikataa wazo hilo kwa sababu kazi waliyopewa na shirika la kipelelezi la China, walikwisha imaliza. Lakini hawakumkatisha tamaa, wakampa formula zote ambazo wameutengenezea mtambo ule, kisha wakamuacha peke yake katika maabara ile.
Hyung akaanza kuunda kitu ambacho kitaufatilia mtambo ule. Tangu saa sita mchana hadi saa nane za usiku, Hyung alikuwa bado anatengeneza kifaa hicho ambacho hakutaka kiwe kikubwa sana. Ndipo mida ya saa kumi usiku, akafanikiwa kumaliza kazi yake na kuijaribu. Kweli kifaa chake kikakubali punde tu, mtambo wa SGT ulipofunguliwa. Akaenda mbali zaidi kwa kuchunguza mambo mbalimbali ya duniani na kwa kile kifaa alichokitengene
za, kikadaka yote hayo. Na ndiyo hiyo saa ambayo sasa anaimiliki Pirlo aliyekuwapo Italia.
Ni kwa nini saa anayo Pirlo? Hili ndilo jibu.
Baada ya kuumaliza ule mtambo na wanafunzi waliofanikisha suala hilo kutunukiwa vyeti maalumu kabisa akiwemo Hyung, mtambo huo ukachukuliwa na kuanza kupelekwa katika shirika la kipelelezi huku Hyung akiwa hajawaambia wenzake wala mtu yeyote kuwa kafanikiwa kutengeneza kifaa kitakachoufatilia mtambo ule.
Kukiwa na ulinzi hafifu wakati mtambo huo mkubwa unapelekwa kwenye idara ya upelelezi China, mbele ya gari lililoubeba mtambo huo, ilitokea gari nyingine kubwa zaidi na kuanza kuishambulia gari yenye mtambo. Haikupita muda, gari hilo likawa kimya na walinzi wote wakiwa maiti.
Kundi la watu wasiojulikana, wakashuka toka garini na kufungua gari lile kubwa lililobeba mtambo. Walipohakiki kuwa kuna mali yao, wakaita helkopta waliyoiandaa na kushusha sumaku kubwa ambayo ilinasa kwenye mtambo ule wenye ukubwa wa duara lile la katikati kwenye uwanja wa mpira lakini kwenda juu mtambo ule ni mrefu zaidi. Helkopta ikauchukua mtambo huo na kutitia nao pasipojulikana.
Baada ya patashika hiyo, ndipo kundi hilohilo, likapewa amri nyingine ya kwenda kuwaangamiza wanafunzi wote walioshiriki kuutengeneza mtambo ule. Wanafunzi karibu wote walipoteza maisha yao kasoro Hyung ambaye alichezwa na chale mapema na kuamua kukimbilia Italia ambapo huko alibadili jina na kujiita Pirlo.
****
"Kwa hiyo unaondoka lini." Padri alimuuliza Pirlo baada ya kusikiliza yote yaliyotokea.
"Leoleo. Natakiwa kufika kule kabla ya saa nne." Pirlo akajibu na yule Padri akamwambia aende chumba fulani kwa ajili ya kukutana naye uso kwa uso na kujadili suala hilo. Pirlo akapiga ishara ya msalaba na kwenda kwenye viti ambapo alitumia dakika kama tano kujifanya anasali. Akatoka hapo na kuelekea nje kwenye chumba alichoelekezwa na yule Padri.
Huko akakutana na Mzee mmoja mwenye mvi nyingi kichwani kwake na walipoonana wakakumbatiana na mzee yule akampeleka kwenye chumba kingine cha siri zaidi.
Chumba kilijaa vifaa vingi vya mapigano hadi kijana Pirlo alikuwa haamini kama huko nje kuna kanisa. Mapanga ya kininja, bunduki na silaha zote aliziona hapo.
"Huku ndipo kwenye nyanja yetu ya upelelezi Pirlo." Mzee yule alimwambia Pirlo huku akicheka na macho ya Pirlo yalikuwa yanalanda huku na huko akishangaa wafanyakazi wenye mavazi ya Kitawa wanavyochalaza kiparaza cha kompyuta. "Ulichagua jina zuri sana kijana. Eti Pirlo, ukajidai yule mchezaji wetu wa Italia. Kwa nini usingejiita Balloteli, Muafrika mwenzako?" Mzee yule alikuwa akiongea kwa utani na kuchechemea kutokana na uzee wake.
Akafika sehemu moja ambayo ndio ilikuwa mwisho wa safari yake. Akagota na kumuita jamaa mmoja aliyekuwa anahusika na sehemu ile.
"Alejandro." Mzee yule aliita kwa sauti kutokana na mtu aliyekuwa anamuita kutokuwepo. Mara akiwa anamtafuta huku na huko, akashangaa kitu kinapita mbele yake kwa kasi halafu kikasimama mbele yake na kuanza kuongea.
"Hellow Mr. Alexander." Kitu hicho kilikuwa kimevaa suti lakini baada ya sauti hiyo, hali fulani ya umeme ikatokea kwenye suti hiyo na sura ya Muitaliano ikaonekana ikiwa inatabasamu.
"Alejandro. Kila wakati we' ni mtu wa kubuni ujinga tu!" Mzee Alexander alilalamika huku akimuangalia yule mtaalamu.
"Hii ni suti ambayo unaweza ukakimbia kwa kasi yoyote bila kuonekana. Na pia haingizi risasi hata kidogo. Mbali na hapo, ukivaa suti hii, na hii saa unaweza kuwa unatoa umeme mwilini mwako." Yule bwana aliyefahamika kwa jina Alejandro alitoa sifa baadhi ya vazi alilovaa na kumfanya Pirlo kuitamani suti ile.
"Achana na mambo yako. Huyu ni yule kijana wetu wa SGT, anasema mtambo umefunguliwa huko na anataka akauteketeze. Nimemleta kwako ili umpe vifaa maalumu." Mzee Alexander alieleza yote kuhusu Pirlo.
"Oooh! Mr. Hyung. Hii suti nakupa wewe Kamanda. Nenda nayo." Alejandro akiongea huku akiivua ile suti na yeye kubaki na boxer. Sekunde kadhaa akachukua rimoti fulani akaibonyeza vitufe fulani na ghafla likasogea begi fulani na kufunguka. Baada ya kufunguka, zikatokea nguo nyingine na mara zikaanza kujivalisha zenyewe mwilini.
"Haya twende." Alejandro alimwambia Pirlo baada mbwembwe nyingi. Pirlo akacheka na kisha akamfuata kijana yule mtukutu sehemu anayotaka waende.
Huko Alejandro akamtengenezea kitambulisho kingine atakachoingilia Tanzania na kisha akampa vifaa maalumu kwa ajili ya mapambano.
Pirlo akalidhika na kazi ya Mzee Alexander na Alejandro.
Akaaga na kuelekea uwanja wa ndege ambapo alikuta ndege maalumu kwa ajili ya kumpeleka Dar es Salaam, Tanzania.
****
Saa mbili usiku, yakiwa yamebaki masaa manne ya Lobo kutimiza adhma yake, Lisa alikuwa kwenye chumba cha mawasiliano akisubiri simu maalumu kutoka kwa Gunner.
Hali ya mawingu ilikuwa imetanda nje na Dar es Salaam nzima. Ilionesha wazi muda wowote mvua itakunya katika Jiji lile.
Saa tatu, simu ya Malocha iliita na hapohapo ikaungwa na mtaalamu wao na maongezi yao yakaanza kusikika bila chenga.
"Haloo FISSA. Lisa kabakiza masaa matatu. Naomba mfuate haya maelezo machache ambayo nitawapa. Mtoto yupo sehemu nyingine ambapo ni huko Gongo La Mboto kwa mbele na Lisa naomba aje huku Kibaha. Najua ndani ya masaa mawili atakuwa amefika. Hamna foleni usiku huu. Kama mnampenda Martina, naomba Lisa aje peke yake. Sitaki mchezo kuhusu hilo. Nawatazama kwa ukaribu, mkijaribu kuleta ukanjanja wowote, Martina mtaletewa mzoga hapo kesho. Zingatieni hilo, nawaoneni. Umebakiza masaa matatu, Lisa. Fanya maamuzi.TICK TOCK." Sauti ya Lobo ilisikika na wala hakuwa na muda wa kusikiliza upande wa pili, akakata simu.
"Mambo yatakuwa magumu hapa. Kama wamefanikiwa kujua mawasiliano yangu, nauhakika wanajua pia kuwa tupo wapi." Malocha aliongea kwa kukata tamaa mbele ya wafanyakazi wake.
"Usijali Malocha, mmefanya kazi kubwa sana hadi hapa. Naomba mwanangu mnilelee vizuri. Mkimpata Frank, muonesheni mwanaye, msimfiche na mwambieni nampenda sana." Lisa alimaliza kuongea maneno machache na kisha akatoka nje tayari kwa safari ya kibaha.
Hakusahau simu ambayo atakuwa anawasiliana na wakina Lobo kama hatowaona. Akawaacha wakina Malocha wakiwa katika masikitiko makubwa mioyoni mwao.
"Hamna jinsi. Tunakupenda Lisa." Malocha alinong'ona maneno ambayo Lisa hakuyasikia. Mtoto wa kike akakwea gari tayari kwa kwenda alipoelekezwa.
****
"Oooh! Lisa. Karibu tena katika mikono yangu." Ni sauti ya Gunner ambayo iliongea baada ya Lisa kusimamishwa kwenye barabara ya rami iliyopo eneo la Kibaha na kutoka nje ya gari lake.
"Muachie mwanangu Gunner." Lisa akafoka kwa hasira.
"Usijali. Tayari nimekwishawaambia mbwa wako mwanao alipo. Wapo njiani wanaelekea huko." Gunner akaongea na wakati huo mvua ya manyunyu ilikuwa imeanza kushika namba eneo hilo. "Zimebaki dakika kumi za Lobo kichukua roho yako. Umefanya maamuzi sahihi sana kwa kununua roho ya Martina." Lobo akazidi kutiririka.
"Fanyeni haraka. Sina muda wa kukaa na hii roho, ni yenu." Lisa akafoka tena.
"Hapana mke wangu, sheria zinasema masaa ishirini na nne. Bado dakika saba tu, utakuwa kuzimu. Lobo yumo mle, anasubiri kazi yake." Gunner alipoonesha sehemu Lobo alipo, taa za gari zikawashwa mara moja na kuzimwa.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA TATU
"Usijali. Tayari nimekwishawaambia mbwa wako mwanao alipo. Wapo njiani wanaelekea huko." Gunner akaongea na wakati huo mvua ya manyunyu ilikuwa imeanza kushika namba eneo hilo. "Zimebaki dakika kumi za Lobo kichukua roho yako. Umefanya maamuzi sahihi sana kwa kununua roho ya Martina." Lobo akazidi kutiririka.
"Fanyeni haraka. Sina muda wa kukaa na hii roho, ni yenu." Lisa akafoka tena.
"Hapana mke wangu, sheria zinasema masaa ishirini na nne. Bado dakika saba tu, utakuwa kuzimu. Lobo yumo mle, anasubiri kazi yake." Gunner alipoonesha sehemu Lobo alipo, taa za gari zikawashwa mara moja na kuzimwa.
"Mi' si mke wako pia." Lisa aliongea kwa kujiamini mbele ya Gunner ambaye alimpiga kofi zito lililompeleka Lisa chini ya rami. Mara baada ya kofi hilo, akaanza kumpiga mateke mazito binti yule kana kwamba hamjui.
"Mjinga wewe. Nitakuua mimi." Gunner aliongea kwa hasira huku akimtemea maji ya mvua Lisa. Radi nazo zilikuwa zinawaka huku na huko na kuonesha vazi la suti nyeusi aliyovaa Gunner. "Muda wa Lobo umewadia, kwa heri Lisa." Gunner alimuaga mkewe na kwenda kwenye gari alilopo Lobo. Wakati anaingia, John Lobo akawa anatoka upande mwingine.
Koti lake jeusi na refu linalochagizwa na kung'aa kama la majambazi, lilimfanya kumchora Lobo kama katili la hatari sana. Kila radi zilivyocharaza anga, uso wa Lobo ulionekana na mkononi kwake akiwa kakamata bastola iliyofungwa kiwambo cha sauti.
"Muda wa kufa Lisa. Imebaki dakika moja." Alipoongea hayo, radi ikapiga tena na uso wake mweupe kiasi huku kichwani akiwa hana nywele, zikamfanya Lisa aamini kuwa muda wake kweli umeisha.
Akanyanyuka pale alipokuwa kalala baada ya kupigwa na Gunner, akapiga magoti tayari kwa kukipokea kifo chake.
"Kumi, Tisa, Nane, Saba, Sita, Tano ......" Lobo akawa anahesabu sekunde ambazo zilikuwa zimebaki. Lisa akafumba macho yake baada ya sekunde kufikia nne.
Akiwa kajiandaa kufa mtoto wa kike, na wakati huo kifyatulio cha risasi kikiwa tayari kufyatuliwa na Lobo, muujiza wa ajabu ukatokea. Hakika ulikuwa muujiza wa aina yake.
Lobo akiwa anaanza kufyatua kifyatulio cha bastola yake, mara mkono wake wa kushoto ukachomwa na vitu kama nyota zenye ncha kali. Maumivu aliyoyapata dakika hiyo, yalikuwa hayaelezeki. Akiwa katika hali hiyo akajikuta akidondosha bastola yake na kuanza kutazama ni wapi vitu vile vimetokea. Wakati anatazama huku na huko, radi ikapiga na hapo akaona kitu mfano wa mtu aliyevaa nguo nyeusi anakuja kwa kasi ya popo mbele yake. Nasema ni mfano wa mtu kwa sababu kilikuwa kina kasi ambayo mtu wa kawaida hana hata kidogo lakini umbile hilo la mtu lilikuwa limetunukiwa kasi hiyo.
Kuja kutahamaki, kitu hicho kikampiga mateke mawili mazito John Lobo. La kwanza lilimkuta kifuani, kitu hicho kikiwa bado kipo angani, kikammalizia teke la pili la hatari shingoni. Lobo akapaishwa hadi kwenye boneti ya gari walilokuja nalo.
Radi nyingine ikapiga, hapo kile kitu kikaonekana kimesimama wima kwa mtindo wa kupigana. Lobo akagonga boneti la gari ile, na Gunner akawasha taa. Sasa alionekana mtu ambaye kafunikwa sura lakini kavaa suti ya gharama.
Kwa kasi, Lobo akashuka toka kwenye boneti na kumfuata yule mtu asiye na sura na kuanza kupambana naye wakati huo Lisa maswali kibao yaliendelea kutiririka katika kichwa chake asijue kile ni kitu gani au ni mtu gani na kaja sehemu ile kufanya nini.
Lobo akarusha teke, lakini cha kushangaza mtu yule alilidaka teke hilo kwa mguu wake wa kushoto na kulibana nyuma ya goti. Lobo akawa hana ujanja wa kutumia miguu yake. Akaanza kurusha ngumi ambapo yule mtu asiye na sura alikuwa akizitoa nje bila hata kurusha zake.
Ngumi ambayo Lobo aliivuta kwa nguvu zake zote, mtu yule aliidaka na sasa akawa kakamata mkono na mguu wa Lobo. Lobo akawa kakamatika hana la kufanya. Mara yule mtu alirudisha kichwa chake nyuma na kukipeleka mbele kwa kasi, kikatua kwenye pua ya Lobo. Damu zikamchuruzika Lobo lakini hakuenda popote kwa sababu alikuwa kabanwa ipasavyo na mtu yule.
Wakati damu zinaendelea kumtoka, Lobo akajikuta akipokea kichwa kingine palepale alipopigwa mwanzo. Maumivu yaliyompata, hakusita kupiga kelele na nadhani angesimulia hadi kwa wajukuu zake.
Hapo yule mtu alimuachia mkono na kisha akaanza kutandaza ngumi zisizo na idadi kwenye kifua cha Lobo. Ngumi ya mwisho ilitua tena kwenye pua, na hapohapo mtu yule akamuachia Lobo mguu wake na kuruka teke zito la kuzunguka. Lobo akapaa juu na kisha akatua chini kama mzigo akiwa kachafuka kwa damu na hali yake ikiwa wazi ni mbaya.
Yule bwana akawa bado kasimama palepale akiwa kakunja ngumi na sura yake iliyofungwa na sijui nini, ikiwa imeinama kwa kusubiri jambo lingine.
Mvua sasa ilikuwa hainyeshi tena bali kubaki miungurumo ya hapa na pale. Gunner akafungua mlango wa gari yake na kwa madaha akachomoka toka mle ndani na kisha akaenda kwa Lobo na kumuingiza ndani ya gari.
"Safi sana. Yaonekana una uwezo mkubwa wa kupigana. Haijalishi, lakini sasa unapambana na mzimu." Gunner aliongea na muda huohuo akachomoka kwa kasi na alipofika mbele ya yule mtu, alisimama ghafla na kuanza kurusha ngumi nyingi zisizo na idadi. Zilikuwa zinarushwa kuelekea kichwani, kifuani na kila mahali ambapo Gunner aliona patamsaidia kumnyamazisha mpinzani wake aliyekuwa anakazi ya kuzitoa na kuzikwepa.
Kuna ngumi moja ya hatari Gunner aliirusha na jamaa yule aliikwepa kwa kuinama kidogo, lakini kwa bahati mbaya alipoinama, Gunner akaachia ngumi ya mkono mwingine ambayo ilimkuta jamaa yule kidevuni na kumrusha hadi alipo Lisa. Alipotua chini, tayari Gunner alikwishafika, akamkalia kwa juu na kuanza kumtwanga ngumi za usoni.
Ilikuwa ni 'kimuhemuhe' au patashika kwa shimo kuchimbika. Mtu yule ambaye alikuwa kazibwa na mask, ni wazi alikuwa taabani hasa pale mwanaume wa shoka Gunner aliposhika ile mask iliyoungana na suti yake na kutaka kuiondoa.
Alipoishika, ndipo alipogundua inaseli za umeme ambazo ni hadi ubonyeze kitu fulani ndizo nazo zijifungue. Gunner akajaribu kuzamisha vidole vyake kwenye ile mask kwa kutaka kuirarua lakini kwa bahati mbaya alipokea pigo hafifu toka kwa Lisa lililopigwa kwa teke baada ya Lisa kuona mtu anayemsaidia kuzidiwa maarifa. Ni pigo hafifu kwa sababu si lile ambalo ungepigwa nalo na Lisa wakati yu mzima.
Gunner akajikuta akimuachia yule mtu na kumfuata Lisa ambaye alikuwa kasimama pembeni kidogo na pale. Kwa hasira nyingi, Gunner alimpiga kofi zito Lisa na lile kofi yule mtu aliyechini aliliona na likamshtua vilivyo. Mwanamke kupigwa kama mwanaume, yule mtu alistaajabu ya Filauni sasa baada ya kuyashuhudia ya Mussa.
Gunner hakuishia kwenye kofi pekee, Lisa alipoyumba baada ya kofi lile, Gunner akaruka teke la kutanguliza mguu mbele na likakita nyuma ya kiuno cha Lisa. Lisa masikini ya MUNGU akadondoka chini na kugaa gaa kwa maumivu.
Gunner akazidi kuonesha ukatili wake dhidi ya wanawake. Na hakika alikuwa katili. Mateke mazito kwenda tumboni, kifuani na saa nyingine kumkanyaga Lisa kichwani kama mwenye kuua nyoka kwa kumkanyaga na kiatu, usingeweza kusema huyu jamaa ana roho ya utu hata kidogo.
"Heeeey." Sauti kali ilisikika nyuma ya Gunner aliyekuwa anamsulubu Lisa. Akiwa anapumua haraka, Gunner akageuka nyuma kumuangalia anayemuita huku bado mguu wake upo juu ya mwili wa Lisa.
Akamtazama Lisa aliyekuwa anagaragara kwa maumivu, kisha Gunner akampiga teke dogo kama anatoa pasi ya mpira. Akamuacha na taratibu akaanza kwenda alipo yule mtu aliyekuwa kasimama na kuweka mguu mmoja mbele kama wafanyavyo wacheza mapigano ya miguu na mikono (karate).
"Hivyo ndivyo mama yako alivyokufundisha kucheza na mwanamke?" Yule bwana kwa mara ya kwanza aliongea baada ya kufoka.
"Oooh! Mama? Namchukia mama yangu kwa sababu alinitelekeza nilipozaliwa tu. Nampenda sana baba." Gunner alijibu huku akivaa vizuri groves zake nyeusi.
"Kwa hiyo baba yako ndio kakufundisha kuwapiga wanawake? Eti we' tasa." Yule jamaa aliongea maneno ya kukarahisha na Gunner yakamuuma.
"Usiniite hivyo."
"Tayari nimekwisha kuita sasa." Jamaa yule safari hii alikuwa anaongea huku akizunguka kwa hatua ndogondogo akimtazama Gunner kwa makini. "We' ni mgumba tu, hahahaaa." Jamaa akacheka kwa dharau.
"Mmmh! Yaonekana mswahili sana kijana. Lakini mbona hauvui hicho kiuchafu kichwani? Unaogopa nini?" Gunner aliuliza na wakati huo Lobo alikuwa ndani ya gari akifatilia ule mpambano kwa makini japo alikuwa katika maumivu makali ya kuvunjwa mfupa wa pua.
"Ooooh! Nimesahau kuwa ulikuwa unataka kuvua hii sura. Usijali Mgumba, ngoja nitimize." Jamaa yule aliongea na kufunua koti lake la suti sehemu ya mkononi, akaanza kuiobonyeza saa yake na sekunde kadhaa, ile mask ikaanza kutoa sauti za shoti ya umeme na baadaye ikapotea kabisa na kubaki sura ya yule bwana akiwa katika suti mwanana na ya kumpendeza pia.
Ni yuleyule Pirlo wa Italia na Hyung wa China, ndiye sasa alioneokana vema kwenye uso wa Gunner aliyebaki katabasamu tu bila kusema chochote.
"A coward's back. (Muoga karudi)" Gunner aliongea huku bado katabasamu.
"Karudi kuangamiza zao la wagumba na matasa." Pirlo au Hyung akajibu.
"Huwezi kunisimamisha Man'Sai, tayari nina kila kitu." Gunner akaongea akilitaja jina la Man'Sai ambalo ni jina alilojipa Frank Masai. Lisa kusikia jina hilo, akajikuta akipata hata nguvu na kutazama kule Frank Masai alipo.
Tabasamu la shida likamtoka mwanamke yule alipothibitisha sura ya Frank Masai.
"Oooh! Kumbe wanijua eeh. Sasa ndio nimerudi hivyo. Naanza na SGT kisha namalizia na Jet P112. Zote naziharibu." Frank aliongea kwa utulivu na sasa alikuwa kasimama akimuangalia adui yake.
"Hahahaaa. Wameshindwa makundi kama FBI, we bwege utaweza." Gunner akaongea kwa dharau.
"Hizo ni akili za Wagumba wengi wa dunia hii. Wanadhani kufanya kazi katika makundi ndio kufanikiwa. Njia ya kufanikiwa ni kuwa peke yako na kufanya kila kitu peke yako. Sihitaji msaada kutimiza nilichokitaka. Msaada wangu ni MUNGU tu." Masai aliongea kwa utulivu na Gunner akacheka tena.
"Okay Man'Sai. Lisa huyo hapo, nimekulindia sana. Ni mtamu mnooo, hahahaaa." Gunner akajidai anatoa maneno ya kejeli.
"Hahahaa. Usemayo ni ya kweli, ila unapewa utamu unashindwa kuleta matunda ya utamu huo. Mwanaume suruali wewe. Hahahaaa." Masai akakejeli naye jambo lililomfanya Gunner apandwe na hasira na kujikuta akikimbia kwa haraka kwenda kwa Masai ambaye safari hii alimuonesha huyu bwana kwa nini anatafutwa kwa udi na uvumba kwenye hii dunia na hapatikani.
Gunner akiwa katika kasi hiyo, akamfikia Frank Masai na kuanza kurusha ngumi nzito kama kawaida yake, lakini ubaya alimkuta hata Masai akiwa katika hasira za kumuona akimpiga Lisa kama mwanaume mwenzake.
Ngumi nyingi alizorusha Gunner, Masai alizipangua na yeye akawa anarusha zake kwa chati, yaani kwa kumendea. Gunner akajichanganya kidogo kwenye kurusha ngumi hizo, Masai akapangua na kutupa yake ambayo ilimkuta jamaa kwenye pua. Gunner akashika pua yake na kujisahau kuwa yupo mpambanoni. Frank akatupa ngumi nyingine ambayo hiyo ikatua kwenye shavu la kushoto na kumfanya Gunner aegemee upande wa kulia. Kosa kubwa kwa Gunner kwani wakati anaegemea upande huo, tayari Man'Sai alikuwa katupa ngumi nyingine nzito zaidi na kupiga shavu la kulia ambapo alikuwa anaegemea Gunner.
Damu kiasi zikamtoka Gunner lakini haikumaanisha ndio mpambano umeisha. Man'Sai akaruka teke zito lililompeleka Gunner hadi kwenye gari la Lisa.
Frank akiwa katika ubora wake wa kwenye riwaya ya Jina na Ukurasa wa Hamsini, akamuonesha Gunner kuwa yeye si wale aliowategemea katika maisha yake, bali yeye ni yule ambaye hakupaswa hata kumuota ujio wake.
Gunner alisikia sauti ya maji na sauti kama ya karatasi inayopepea ikija nyuma yake. Alipogeuka, kwa msaada wa taa za gari alizoziwasha wakati Lobo anasulubishwa, aliona viatu vya gharama alivyovaa Frank vikichapua katikati ya maji ya mvua iliyokata muda mchache uliopita. Maji hayo kila Frank alipotua mguu wake huku akikimbia, basi yaliruka kwa pembeni kuonesha kuwa zile mbio zilikuwa ni nzito. Sauti kama karatasi inayopepea, ilikuwa ni suti mwanana aliyotinga Man'Sai, ilikuwa inatoa sauti hiyo wakati anakimbia kwa hatua ndogondogo kumfuata Gunner aliyekaribu na gari la Lisa.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA TANO
"You son of the bitch Man'Sai." Malocha alisikika akitukana huku akiwa kachanua tabasamu la haja usoni kwake. Akamfuata Masai na kumkumbatia kwa nguvu huku akicheka kwa furaha.
"Nimerudi sasa. Nimekuja kununua roho." Masai aliongea baada ya kuachiana na Malocha ambaye alikuwa haamini kama mtu aliyedhani hatotokea, atatokea.
"Karibu Jambazi langu. Nilikusubiri kwa muda mrefu sana. Hadi nikaamua kuingia kazini mwenyewe." Malocha alitamka hayo huku akimuangalia Frank usoni.
"Usijali. Subira yavuta heri." Naye akampa msemo wa Kihenga rafiki yake kipenzi Malocha.
"Jamani. Mlikuwa mkisikia nikiongea kuhusu Frank Masai au Man'Sai kila mara. Huyu ndiye yeye sasa." Malocha.alimtambulisha Masai mbele ya kikundi kazi chake cha watu watatu.
"Nilikuwa natamani sana kukuona. Hatimaye leo nimekutana na 'legend' wa nchi hii." Mubah aliongea hayo huku akimpa Masai mkono. "Naitwa Prince Mubarak au Mubah." Akajitambulisha Mubah.
"Nakufahamu Mubah. Pole sana kwa yaliyokukuta." Maneno hayo yalienda sambamba na mkono mwingine wa Masai kuogonga gonga begani Mubah.
Baada ya maneno machache na kutambuana, moja kwa moja hadithi mbalimbali zikapamba moto baina ya wale watu.
"Kwa hiyo mlipo mkamata Lobo, alisema anatumwa na nani na kwa nini?" Masai aliwauliza wale wapelelezi swali hilo.
"Aaagh. Boya tu yule. Hakujibu jibu sahihi bali kusema kuwa katumwa na uchafu kuja kusafisha pasafi kwa kuweka uchafu." Malocha alijibu kwa sauti ya kukereka.
"Kwa hiyo hilo jibu nyie hamkulifanyia kazi?" Masai akauliza tena na kuwafanya wale wana FISSA kengere ya kitu kugongwa vichwani mwao.
"Hapana. Hatukufanyia kazi chochote. Kwani kuna jambo hapo kati Man'Sai?" Malocha alijibu na kuuliza akiwa na shahuku ya kujua alichong'amua Masai.
"Ndio. Lipo jambo ambalo mlipaswa kulifanya. Kusafisha pasafi kwa kuweka uchafu. Kauli hii haiwagongi vichwani hata kidogo?" Wote wakanyanyua vichwa juu kama wenye kufikiria jambo lakini wasipate mawazo sahihi.
"Mmmh! Masai, haya mambo mengine yapaswa kuwa na watu kama wewe, wenye kutambua jambo mapema kwa mara moja pale walisikiapo tu." Ni sauti ya Lisa ilichombeza katika mjadala ule.
"Kweli kabisa Man'Sai. Lisa yupo sahihi." Malocha akashabikia huku akisogeza mgongo wake kwenda mbele kusikiliza maneno ya Masai atakayoyaongea.
"Kuna viongozi wangapi ambao John Lobo kawaua?" Masai akauliza huku akimuangalia Malocha usoni. Malocha akatulia na kufanya hesabu za watu ambao Lobo alifanikiwa kuwaua.
"Saba. Nakumbuka wakuu saba Lobo aliwamaliza. Akiwemo waziri wa Wanawake na watoto." Malocha akajibu.
"Baada ya kuwaua, ni wakina nani waliowekwa madarakani?" Masai akatupa swali lingine.
"Damn you Man'Sai. You're crazy son of the bitch."Malocha akarudisha mgongo wake kwenye kochi huku kachanua tabasamu baada ya kupata maana ya maneno ya John Lobo.
"Nadhani umekwishanielewa nachomaanisha na alichojaribu kuwaambia Lobo." Masai akaingia kwenye vichwa vya wale watu.
"Kusafisha pasafi kwa kuweka uchafu. Yaani kuondoa watu wasafi sehemu fulani kwa kuwaweka wachafu. Kwa hiyo njia aliyokuwa anaitumia ni kwa kuua au kuwalazimisha waachie madaraka." Malocha aliongea peke yake na kuwafungua hata wale ambao hawakuelewa. "Upo sahihi Man' Sai. Natazama watu waliowekwa hizo nafasi, ni wazi hawana usafi bali uchafu tu. Tazama baada ya kifo cha Kamanda wa Polisi kanda ya kati, limewekwa lile pumbavu, mikoa imezidi kuongezeka maovu." Malocha alizidi kutiririka anachokijua.
"Upo sahihi kabisa Man'Sai. Hata uongozi uliowekwa FISSA baada ya sisi kuondolewa, ni wa ajabu." Mubah akachangia.
"Nadhani sasa tumekwishajua nini kipo katikati ya haya mambo kwa kutumia kauli ya Lobo. Sasa kama tumejua, tuangalie chanzo chake. Nani anayewateua hawa?" Masai akauliza tena.
"Ni Rais yule kidomo domo." Mubah akadakia hata bila kujiuliza mara kadhaa.
"Ni kweli, Rais wa nchi anahusika sana na haya mambo, lakini na yeye roho yake ipo dukani na ndio maana anafanya haya yote." Malocha akajibu na kuwashangaza wote waliokuwepo katika mjadala ule kasoro Masai.
"Nani yupo katikati ya haya mambo sasa?" Masai akamuuliza Malocha.
"Chris Shadow au The Shadow ndiye kila kitu." Jibu hilo likamnyong'onyeza kabisa Frank Masai. Hakutegemea kabisa jibu lile kwa wakati ule.
"Kwa hiyo wote wanafanya kazi chini ya The Shadow. Nitamtafuta huyu mbwa kwa gharama yoyote ile, na nitamuua." Frank alijikuta akijiapiza.
"The Shadow ndiye nani jamani." Mubah aliomba kutolewa gizani kuhusu mtu aitwaye The Shadow.
"Alipojiita The Shadow, hakukosea hata kidogo. Jamaa ni kama kivuli. Hutembea kutokana na kubadilika kwa majira. Hukufuata popote uendapo kama akiamua kufanya hivyo. Na mbaya zaidi, hata wafanyakazi wake hawajawahi kumuona. Hao wakina Gunner, wanasikiaga sauti ya mgurumo tu wakati wanaambiwa waongee na bosi wao. Huyo ndiye aliyewaunda wale watoto wa mauaji miaka ishirini iliyopita, wale watoto waliojiita Panya Roads, na mimi nilikuwepo. Aliua wazazi wangu wote kabla ya kuniunganisha kwenye lile kundi la wachafu. Na ndiye aliyepachika viongozi kwenye kila nchi akiwatumia viongozi hao kunyonya wananchi. Namsaka kwa mwaka wa saba sasa. Kwenye ile ishu ya Jina, alihusika kwa asilimia tisini. Kwenye ukurasa wa hamsini, jina lake lilikuwa la mwisho, lakini nilimkosa. Ni mtu hatari, usiombe aweke mkono wake kwenye ukifanyacho, utajuta." Masai akamaliza kumuelezea The Shadow kwa kifupi.
Sura za wapelelezi zilikuwa kimya zikichambua neno hadi neno kutoka kinywani mwa Masai. Kimya kikatanda huku sura ya kila mmoja aliyekuwamo mle ndani zikitafakari jambo lake.
"Mamaa." Sauti ya Martina ilisikika na kila mmoja aligeuka kumtazama. Alikuwa katoka katika usingizi mzito wakati anamuita mama yake.
Akaanza kusogea taratibu kwenda kwa mama yake huku akifikicha macho yake. Lakini alipomuona Masai, akasita kidogo na kurudi nyuma kwa uoga.
"Martina. Njoo umsalimu baba eeh." Lisa liongea huku akiinuka pale kochini alipokuwa amekaa na Frank.
"Huyo ni adui. Baba aliniambia." Martina aliongea hayo huku akizidi kurudi nyuma kwa uoga.
"Hapana Martina. Huyu ndiye baba yako, siyo adui." Lisa alijaribu kumuelekeza mwanaye ambaye hakusikia ushauri huo na badala yake alikimbilia chumbani alipotoka huku mama yake akimfuata kwa nyuma.
"Unakazi hapo baba mtu. Na sura lako la kijambazi hilo. Hahahaaa, mtoto lazima azogoe." Malocha alimtania Frank ambaye macho yake yalikuwa kule walipokimbilia familia yake.
"Nakwambia. Hapo ni tatizo. Noma na soo kilo kumi. Sijui kama ataelewa." Frank aliongea huku akitabasamu kana kwamba hajashtuka sana kwa kilichotokea. Lakini kiundani, alikuwa kaumia sana hasa alipogundua mtoto wake anafundishwa ugaidi.
"Na wewe umezidi. Hata kuja kumtembelea shem ukawa unaona tatizo. Kujificha gani huko. Acha mtoto akuoneshe." Malocha alizidi kumkandamiza Masai.
"Aaaagh. Sasa unadhani nisipojificha nitaishije. Mi ni kama embe, naonekana msimu hadi msimu. Kama hapa ni msimu wa kazi, na mimi ndio naibuka toka chimbo na 'full materials'." Wale jamaa ambao walikuwa hawamjui Frank Masai, walikuwa ni wa kutabasamu tu wakati wawili wale wakitaniana.
Hakuna aliyeamini na atakayeamini pale atakapokutana na Masai na kuambiwa huyu ndiye yeye. Kijana mtukutu na mjanja mdomoni. Anajua lugha zipatazo tano, tena zote zinatumika Kimataifa. Lakini ni kama muhuni wa jijini asiye na faida yoyote.
"Hahahaaa. Kwa hiyo sasa hivi ni msimu wa maembe." Malocha akauliza na kuzidi kucheka.
"Haaa! Huyu kiongozi wenu vipi? Hajui maembe yapo sokoni sasa hivi yanauza roho zao. Hapa nimepewa hela na Lisa, naenda kununua roho ya embe liitwalo Gunner. Na wewe Mubah, nipe changu mapema nikununulie embe Lobo." Masai akaongea na kuwaacha wale jamaa kutabasamu wasijue cha kujibu. "Huyu jambazi, nilimnunulia roho ya Lobo, lakini upimbi wake akamkwangua na kisu, matokeo yake, leo anapasua watu vichwa hadimu kama hivi." Wakazidi kutaniana wale watu hadi Lisa aliporudi.
"Kakataa katakata kuja kukusalimia." Lisa akamwambia Masai.
"Hamna tatizo, punde atanielewa tu." Frank hakutaka kumkatisha tamaa Lisa wala nafsi yake.
"Okay. Hamna tatizo. Naona kalala tena." Lisa aliongeza maneno.
"Okay. Nasikia kesho Rais wa Urusi anakuja. Mnajua mikakati ya hawa jamaa?" Frank aliwauliza wale wapelelezi.
"Aagh. Sisi hatuhusiki tena. Kazi ya FISSA hiyo." Malocha akajibu kwa kukereka.
"Hapana Malocha. Wajua kuwa wamechukua ndege ya P.112 toka kwako? Halafu pia wanamtambo wa kuzima satellites zote uzijuazo. Mtambo huo waliuiba China. Na mimi nilishiriki kuutengeneza na ni mimi pekee ndiye mwenye kifaa cha kuufatilia. Hata mawasiliano yenu niliyanasa kupitia kifaa changu hicho.
Namba zako walizipata kwa kutumia huo mtambo. Wajua nia yao?" Masai akaacha swali likielea angani na hakuna aliyelijibu. "Basi ipo hivi, ndege waliyoichukua, kumbuka ni mali ya Marekani na Urusi hawajui kuwa Tanzania kapewa ndege hiyo. Kitakachofanyika hiyo kesho wakati Rais wa Urusi anakuja, ni kushambulia ndege yake kwa kutumia Jet P.112 na hali hiyo itafanya Urusi kuamini kuwa Wamarekani wamewaulia Rais wao. Unajua Urus anashirikiana na nani?" Swali lingine likabaki linaelea hewani na Frank hakutaka kuwakosesha majibu. "China, Cuba, Korea Kaskazini na Japan ambao hawa Wajapan, pia wapo pamoja na Ujerumani, Italia na Bulgaria.
Hawa Wamarekani, mabest wao ni Ufaransa, Uingereza, Hispania, America yote ile, Poland na nchi nyingi za 'Capitalism'. Sasa nini kitakachotokea baada ya mauaji ya Rais wa Urusi?" Masai akauliza tena.
"World War Three ( Vita ya Tatu ya Dunia)" Mubah akajibu swali hilo.
"Exactly Mubah (Upo sawa Mubah). Dunia itaingia vitani na wakati sisi weusi tukibebwa na kupelekwa kupigana vita vyao. Ndicho mkitakacho?" Wote wakatikisa vichwa vyao kushoto kulia kuonesha kuwa hawataki. " Sasa The Shadow, anataka iwe hivyo. Ili kumdhibiti isitokee, yapasa kuzuia huu ujinga. Tukizuia hii, roho ya Lobo na mwenzake, ni yetu." Masai akamaliza huku akiwapa hamasa wenzake walioukubali ukweli kwa kila neno.
"Sasa tunafanyaje kuwazuia hawa washenzi?" Malocha akauliza swali ambalo Frank alilipokea kwa tabasamu pana.
"So easy my friend. Nimekuja kusimamisha kila ujinga hapa. Niachieni mimi haya mambo. Mtaona wenyewe mabadiliko. Lakini wakati mimi najiandaa kuzima ujinga wa hawa watu, nyie nendeni mkamchukue yule mkuu wa polisi kanda ya kati, atatusaidia sana." Masai akatoa maelekezo mengine ambayo yaliitikiwa kwa ari ya hali ya juu. " Na huyu Rais wenu anapelekwapelekwa tu, kesho naye anauawa ili kisingizio kiwe kikubwa. Sasa hapo ndipo patakuwa pabaya. Tunatakiwa kufahamu sisi ni wakina nani? Nchi yetu inamarafiki wangapi? Hawa wanaotengenezwa kuwa maadui, wote tuna urafiki nao. Sasa nini kitatokea baada ya kundi la Gunner kufanya upuuzi wake? Jibu nawaachia vichwani mwenu. Mubah na jamaa hapo, kamleteni Kamanda Kondo, yupo Dar hapahapa kwa ajili ya shughuli ya kesho. Mimi naelekea mahala kuchukua vifaa vyangu, baada ya saa moja, nitakuwepo hapa. Naomba na nyie muwepo." Frank akamaliza kikao kile na kila mmoja akaenda kwenye majukumu yake.
****
IJUMAA SAA SABA MCHANA.
Wakati Masai na Lisa wakiitaabisha miili yao kabla hawajaenda kwa Malocha, kundi zima linaloongozwa na Gunner Samuel Bokwa lilikuwa linajadili mambo yatakayofanyika kesho yake, yaani katika ujio wa Rais wa Urusi. Waliona wazi kuwa vita vya tatu vya dunia vilikuwa vimewadia, ama la! Basi lazima kutatokea vita kubwa baina ya mataifa yale makubwa duniani.
"Kesho ndiyo kesho jamani. Kama ni siku ya kuzaliwa, basi ni krisimasi, Yesu anazaliwa. Lakini si Krisimasi bali 'Armageddon' ." Gunner aliongea huku akienda huko na huku kwa tambo na mbwembwe akijaribu kufananisha siku ya kesho na siku kuzaliwa Yesu au mwisho wa dunia. (Armageddon)
"Kweli boss. Na tayari dereva maalumu wa kuendesha Jet P.112 amekwishapatikana. Hiyo ni fursa pekee ya sisi kuitawala dunia. Vita wapigane wao, sisi tuwe watu wa kuuza silaha tu! Mwisho wa siku vita vikiisha, tunachukua uongozi wa kidunia kwa ubabe." Yule Mrusi mmoja anayeendesha mitambo ya mle ndani aliongea kuunga mkono kauli ya mkuu wake, Gunner.
"Upo sahihi Boyka. Na kwa ushindi huo, hata The Shadow atatutunuku nishani ya pekee." Gunner alizidi kutamba.
"Lakini mkuu." Sauti nzito iliita. Gunner akamuangalia yule aliyemuita. Alikuwa kabandikwa bandeji puani na kwenye paji lake la uso. Alikuwa ni John Lobo.
"Sema Lobo." Gunner akampa nafasi ya kuongea mshirika wake.
"Kuna mtu katika maongezi haya tunamsahau wakati tunafikiria kusheherekea." Akameza mate kidogo kisha akasongesha maongezi yake. " Frank Masai. Atakuwa tatizo kubwa sana katika mpango wetu. Unamjua yule alivyoking'ang'anizi." Akatulia kusikia upande wa pili utajibu nini.
"Masai ni kama sisimizi ambaye hana miguu. Hana teknolojia ya kutuzuia sisi hata kidogo. Yule ni kama samaki ndani ya maji ya moto, humo haogelei bali kupikwa." Gunner akatamba kwa maneno bila kujua ni nini akizungumziacho.
"Gunner. Masai si hivyo umdhaniavyo. Yule ni kikwazo kuliko kikwazo chenyewe. Embu fikiria ni vipi kajua kuwa tupo Kibaha na Lisa? Fikiria katumia muda gani kuwauwa wale walinzi tuliowapa Martina halafu katokea tena Kibaha. Unadhani ni mtu wa aina gani yule?" Lobo akaonesha wasiwasi wake wazi kabisa.
"Hahahaa. Lobo my friend. Hilo lisikuumize kichwa hata chembe. Yule ni sisimizi, as I told you. Don't worry man, hana madhara yule." Gunner akajihakikishia kuwa yupo salama bila kujua upande wa shilingi wa sisimizi huyo ambaye hana miguu. Yawezekana ndiye mfalme wa sisimizi wote duniani, hakujua hilo.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA SITA
"Gunner. Masai si hivyo umdhaniavyo. Yule ni kikwazo kuliko kikwazo chenyewe. Embu fikiria ni vipi kajua kuwa tupo Kibaha na Lisa? Fikiria katumia muda gani kuwauwa wale walinzi tuliowapa Martina halafu katokea tena Kibaha. Unadhani ni mtu wa aina gani yule?" Lobo akaonesha wasiwasi wake wazi kabisa.
"Hahahaa. Lobo my friend. Hilo lisikuumize kichwa hata chembe. Yule ni sisimizi, as I told you. Don't worry man, hana madhara yule." Gunner akajihakikishia kuwa yupo salama bila kujua upande wa shilingi wa sisimizi huyo ambaye hana miguu. Yawezekana ndiye mfalme wa sisimizi wote duniani, hakujua hilo.
"Tatizo lako Gunner hujui na hutaki kuumiza kichwa chako kujua. Sasa mimi nakufungua kichwa chako. Subiri hapo." Lobo akanyanyuka na kuwaacha wenzake pale katika chumba cha mkutano na kwenda chumba fulani ambapo alitoka na bahasha fulani kuu kuu. " Angalia kilichomo humo." Lobo akamkabidhi Gunner bahasha ile.
"Hizi ni picha za wale waliotengeneza mtambo wa SGT." Gunner akaongea baada ya kutoa kilichomo ndani ya bahasha.
"Hujang'amua chochote kwenye hiyo picha?" Lobo akatupa swali kwa kiongozi wake.
"Nachojua hawa jamaa walikuwa ni hatari katika sayansi hasa kwenye mitambo itumiayo kompyuta, lakini wote tuliwaua." Gunner akajibu alichokijua kwenye ile picha.
"Hahahahaaaa. Ndio maana nilikwambia hutaki kushughulisha akili yako kufikiria. Embu muangalie huyo Muafrika aliyevaa miwani ya macho." Gunner akasogeza ile picha karibu zaidi na macho yake. Akaona haitoshi, akaanza kuangalia picha hadi picha kwa sababu ya yule Muafrika.
"Shit. Ina maana Masai alikuwa mmoja wa hawa wanasayansi? Halafu hawakumuua wale wajinga licha ya kuwalipa mabilioni ya dollars." Macho ya Gunner ni wazi yalikumbwa na mshtuko baada ya kujua ni nini Lobo anajaribu kumuelekeza.
"Na japo walishindwa kumuua, huyo jamaa pia The Shadow alimuhitaji akiwa hai ili awe mfanyakazi wake. Huyo ndiye alikuwa tegemeo la Wanasayansi wote katika kile chuo ambacho ndicho chuo bora duniani kwa Sayansi. Sasa vuta picha hapa unapambana na nani." Lobo akamtazama usoni Gunner kabla hajaendelea. " Anajua Sayansi kuliko sisi, mjanja kuliko sisi. Kajificha miaka mitano bila kuonekana nchini kwake. Anapiga mkono kuliko sisi na mbaya zaidi, anawashirika makini kuliko sisi, kuna kichwa Gunner." Lobo akamaliza kwa tabasamu pana kutokana na maelezo yake.
"Hizo dharau sasa Lobo. Yule ni mbwa tu. Hana sifa uzitajazo." Gunner akawa kapandisha hasira kwa maneno kuntu ya Lobo.
"Huo ndio ukweli Gunner. Man'Sai ni mbwa haswa, tena mbwa wa mtaa. Anajua shida za mtaa wake na anajua njia zote za mtaani. We can't stop him by ourselves." Lobo akazidi kuropoka lakini maneno yake, yakachukuliwa tofauti na Gunner.
"Wewe ni muoga Lobo. Wewe ni kunguru mla sabuni ambaye muosha vyombo akija, huchapa mbawa zake kwa uoga wa kumwagiwa ukoko." Gunner aliongea shombo ambazo ziliwafanya wale washirika wengine waanze kucheka.
"Tatizo lako Gunner ni kichwa kokoto. Mgumu kuelewa nachomaanisha. Hapa mimi namaanisha, tuombe msaada zaidi kuhusu hili. Peke yetu hatuwezi nakwambia. Hatujui ni nini anacho Masai na hatujui atatumiaje alichonacho. Hivi kwa akili yako, unadhani nani anajua kuwa tuna mtambo wa SGT zaidi ya sisi wenyewe?" Lobo akauliza na kuwaangalia wenzake, alipoona hamna jibu, akatupa jiwe la msingi kwenye uelewesho wake. "Masai anajua kuwa tuna mtambo wa SGT. Kajuaje? Hilo nalo bado unataka kuelekezwa kuwa ni la hatari katika mpango wetu? Don't be stupid. Na nyie wote mnaochekacheka kama Malaya kaona pochi ya mwanaume inafunguliwa, acheni ujinga." Hasira tayari zilikuwa zimempanda Lobo.
"Okay Lobo. Nini unachoshauri sasa. Tugandishe mpango wetu? Huo ni ujinga kuliko ujinga wenyewe. Au tuongeze jeshi? Huo pia ni ujinga zaidi hata ya kusitisha mpango wetu. Tumeteketeza nusu ng'ombe, sembuse haka kamkia Masai?" Hali ya kujiamini ilikuwa katika mwili wa Gunner na kufanya asisikie la mtu wa.karibu katika kazi zake.
"Okay. Kwa kuwa wewe ndiye kiongozi kipofu unayeongoza baadhi ya vipofu, hamna tatizo kuhusu ulichoamua. Ila kwa kukupa taarifa tu! Kama mpango utabumba, basi ujue mkono wa The Shadow utatuchezea sana. Hatutosalimika hata kwa ukubwa wa punje moja ya mchanga. Katupa kila kitu tulichokihitaji tena kwa gharama kubwa, sasa ngoja mpango uende kinyume, na kauli zako chafu za kibishi, zitakutokea puani." Lobo akasimama na kukusanya picha zake na kuanza kuondoka mle ndani. Licha ya Gunner kuwa kiongozi mkuu wa mapambano yale, lakini anapofika kwa Lobo, huwa kama wanalingana na anashindwa kuonesha cheche zake za uongozi.
"A coward (Muoga)" Gunner alitamka hayo wakati Lobo anaelekea kwenye mlango wa kutokea mle ndani.
"We'll see what's next. (Tutaona kitakachofuata)"Lobo akatoka nje ya chumba kile baada ya maneno hayo.
"Mpango utakamilika tu. Msijali wandugu, maadam tuna kila kitu cha muhimu, hakuna kitakachotusimamisha." Gunner akawatoa hofu washirika waliobaki kabla na yeye hajatoka katika chumba kile.
****
Saa kumi na dakika kadhaa, kundi lililotumwa kwenda kumkamata Kamanda Kondo lilikuwa limerudi na Masai naye alikuwa katika chumba maalumu kwa ajili ya mahojiano ya mtu yule ambaye alipewa ukuu wa polisi kanda ya kati baada ya kifo cha kutatanisha cha Mzee Ismail Ambazeki ambaye alikuwa anaendeshwa kwenda na kurudi na askari mwenye cheo kidogo wa kipindi hicho, Bwana Prince Mubarak.
"Kwa nini ulimuua Mzee Ismail?" Sauti ya Mubah ilimuuliza Kondo.
"Hapana. Mimi mbona sijamuua? Mimi niponipo tu, wala sikumuua." Kamanda yule alijibu huku akitetemeka kama si polisi mkuu tena wa mikoa kama mitatu ya kati.
"Kwa hiyo nani alimuua." Mubah akamuuliza huku akiweka mikono yake miwili kwenye magoti ya yule mzee ambaye alizidi kuchanganyikiwa licha ya Mubah kuwa katika hali ya kawaida.
"Mimi niliwekwa na Rais. Lakini kuna mtu huwa naongea naye simjui anasema nikileta ujinga na mimi nitakufa kama Mzee Ismail. Hivyo kama kuna jambo la maovu linataka kufanyika kanda ya kati, wananipa taarifa nisilifatilie." Huku akitetemeka, yule mzee akawa anaropoka kila anachokijua hadi wakina Mubah wakalidhika.
"Sasa sisi tunakuachia, nenda kaendelee na majukumu yako ila fumba domo lako na kamwe usije ukasema kuwa umekutana na sisi. Kesho wanataka kumuua Rais wa Urusi, ni sisi pekee wa kuzuia jambo hili, lakini na wewe tunaomba uwe makini sana. Macho yako yawe yanatembea huku na huko kama nyuki yatima." Mubah aliongea maneno ambayo yaliitikiwa kwa kichwa na Mzee yule.
Akatolewa katika chumba kile na kupelekwa sebuleni kisha akavishwa mzula mweusi na kutolewa katika nyumba ile tayari kwa kupelekwa katika hoteli aliyofikia.
"Upo vizuri kijana. Nimependa sana unavyofanya kazi zako. Hongera." Frank akamsifia Mubah.
"Kawaida kaka. Kazi ya Lisa hii, ndiye ticha wangu." Mubah aliongea na wote wakacheka kwa maneno hayo. Wakati huo, mtoto Martina alikuwa anacheza uwani na jamaa ambaye alizoeana naye.
*****
JUMAMOSI, SIKU YA RAIS WA URUSI KUJA.
Gunner na kundi lake waliiita siku hii ni mwisho wa dunia. Lakini kundi la Malocha waliita siku hii ya ukombozi wa dunia. Sayansi na akili nyingi ndivyo ambavyo vilikuwa vinatawala siku hii ya aina yake. Mitambo kama SGT na ndege aina ya Jet P.112, ndivyo hasa viliwapa vichwa mtuno Gunner na wenzake.
Wakati huo Masai naye alikuwa anacheza na akili zao. Alishajua kila kitu kuhusu mpango wao. Alichofanya yeye ni kuunga mitambo kadhaa kwenye chumba cha mitambo ya Malocha.
Hakuna aliyejua anachokifanya Masai hadi pale waliposhuhudia kwenye skrini zao wanaiona Dar es Salaam nzima bila kokoro wala papara. Hapo ndipo walipoamini kuwa mtu waliyenaye siyo 'size' yao hata kidogo.
"Hapa ndipo kambi ya Gunner na wenzake ilipo." Masai alionesha kwa kidole sehemu ambayo alitaka wenzake waone.
"Ukifanya hivi, utaona kila kitu." Akavuta lile eneo na mara pakaoneka vizuri kabisa na kila kitu kinachoendelea eneo lile kilionekana safi.
"Mmmh! Kaka upo vizuri. Hapo tunafatilia kila kitu bila tatizo." Mubah alimpongeza Masai.
"Hichi nilichoweka humu, hata satellites zote zikizimwa na mtambo wao, sisi tutaendelea kuona mambo yote. Cha msingi ni sisi kuwa macho zaidi ya kila kitu. Picha ya kile tendo inakuja baada ya dakika moja. Na ndege yenu ipo mlee." Akaonesha tena kwa kidole Masai..
"Mmmmh! Aisee hawa jamaa ni hatari sana. Sasa wameichimbia au?" Mubah akauliza na wakati huo wenzake wote walikuwa kimya wakisubiri muda ufike wa kuanza kazi.
"Pale pana kitu kama handaki. Pakifunguka ujue ndio muda wa dege lile kutoka. Tupaangalie sana pale." Akaongeza jambo la muhimu Masai.
"Sasa mbona kuna miti? Wamewezaje kuchimba na wakati kuna miti mikubwa kama ile." Mubah aliuliza kwa mshangao.
"Mzungu anaakili ndogo sana ya kuteka hata akili ya kuku. Hapo ndipo katuzidi huyu mtu." Frank aliongea bila kujibu swali la Mubah. "Kwa hiyo tunawasimamishia tukiwa hapahapa?" Lisa akauliza.
"Hapana. Nyie mtaenda na hivi hapa vidude. Mi' nitabaki na huyu fundi hapa, rafiki wa Martina. Tutawasiliana na mtapata matokeo yote ya kinachoendelea. Mtaona tu wenyewe." Masai akamaliza maelezo mafupi aliyoyatoa na kila mmoja alikubaliana na mpango ule.
****
Wakati huku wengine wakipanga kuukaribisha mwisho wa dunia na wengine kuikomboa, kuna wale wananchi ambao walikuwa hawana A wala E. Hawa ndio wale waliokuwa wamejipanga kandokando ya barabara ambazo zilikuwa safi siku ile kuliko siku zote za maisha yao. Zilipigwa maji na kung'aa kama zimesafishwa kwa mafuta ya kupikia. Walishangilia na kutandika khanga zao kama vile sikukuu ya matawi, hakika walikuwa katika furaha.
Mbali na hao wa kujipanga barabarani, kule uwanja wa ndege kulikuwa na vikundi mbalimbali vya jadi. Waliimba na kucheza ngoma za jadi. Wakaonesha uwezo wao wa kuvaa mavazi ya asili na mbwembwe mbalimbali za kijadi, yote ilimradi kuionesha dunia kuwa Tanzania bado inadumisha mila na wakati teknolojia imevamia mila hizo na sasa utandawazi ndio neno linalochukua nafasi kubwa kuliko jadi.
Vifijo na nderemo viliendelea kuchukua nafasi yake na kila aliyebahatika kuona hali ile, hakusita kutabasamu kwa kutoa meno yake yote nje. Hakuna aliyejua kuwa mwisho wa dunia unaanzia pale. Hakuna aliyejua na kamwe wasingeweza kujua hilo.
Ndani ya ndege ya Rais wa Urusi, kulikuwa kuna marubani kadha wa kadha wakiingoza ndege ile kwa utaratibu na kwa heshima kubwa bila kuwa na papara kwa sababu wamembeba mtu mkubwa labda kushinda hata Rais wa Marekani, Warusi wote wanaamini hilo.
Rais wa Urusi, Bwana Ragio Pendrovic alikuwa akiangalia huku na huko wakati akipewa makaratasi kadhaa ya kupitia ambayo yangehusika katika kutoa hotuba afikapo nchini Tanzania. Hakuwa na wasiwasi hasa pale alipowaza kichwani mwake kuwa ndege yake inaulinzi wa kipekee ambao hakuna kitakachotokea kama ikivamiwa. Na wakati huohuo, moyo wake uliiamini Tanzania kama nchi ya amani hivyo hamna ambacho kitamdhulu pindi atakapokanyaga ardhi yenye utajiri kuliko ardhi yoyote Afrika lakini wananchi wake ni masikini labda kuliko nchi yoyote ukanda wa Afrika Kusini.
Hiyo ni kwa sababu viongozi wa nchi hiyo wanajali zaidi kujaza matumbo yao yasiyotosheka hata kwa sinia zima la pilau.
Viongozi hawa naweza kuwafananisha na fisi ambaye hata kama kashiba, bado atafatilia hata kile kidogo ambacho kimebebwa na kunguru mroho. Wapo tayari kuchukua chochote ambacho masikini kajitafutia au kajivumbulia na kukifanya kuwa chao.
Kamwe hawataifanya nchi hiyo kuwa na matajiri kama watajali matumbo yao yajae na wakati huo wanayaminya ya wengine chakula wakilacho, na wanaenda mbali zaidi kwa kuyatapisha chakula hicho wanachojitafutia.
Naweza sema ni upuuzi kwa mtu kusema nchi hiyo ni ya demokrasia. Demokrasia ipo wapi?
ITAENDELEA
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA SABA
Viongozi hawa naweza kuwafananisha na fisi ambaye hata kama kashiba, bado atafatilia hata kile kidogo ambacho kimebebwa na kunguru mroho. Wapo tayari kuchukua chochote ambacho masikini kajitafutia au kajivumbulia na kukifanya kuwa chao.
Kamwe hawataifanya nchi hiyo kuwa na matajiri kama watajali matumbo yao yajae na wakati huo wanayaminya ya wengine chakula wakilacho, na wanaenda mbali zaidi kwa kuyatapisha chakula hicho wanachojitafutia.
Naweza sema ni upuuzi kwa mtu kusema nchi hiyo ni ya demokrasia. Demokrasia ipo wapi?
Au labda sisi wananchi akili zetu zimeingiliwa na mafuta ya taa. Ila tukirudi nyuma miaka ya 1861 hadi 1865, kuna Rais mmoja wa Marekani anaitwa Abraham Lincoln, alikuwa ni Rais wa Kumi na Sita na ndiye aliyepigana zaidi kuondoa ubaguzi wa rangi Marekani. Yeye alisema kuwa "Democracy is a government "of the people, by the people, and for the people." (Demokrasia ni serikali ya watu, kwa watu na kwa ajili ya watu). Je, serikali yetu ipo hivyo, au ndio tunakunwa vichwa na wakati hata sisi tuna kucha? Ukisema sana wanakuzima, je hiyo ni demokrasia? Mimi sijui na sitaki kuongelea sana huko.
****
Wakati tendo la kumpokea Rais wa Urusi likizidi kuchukua nafasi yake katika ardhi ya Demokrasia ya Tanzania, Gunner Bokwa alikuwa anafatilia kila kitu kwa makini kwenye kamera kadhaa ambazo waliweza kuona eneo zima atakalopita Rais na mazingira yake.
"Pale ndipo tulipoweka bomu la masaa, na kule nyuma yapo mawili. Na pale ndipo Jet P.112 itakapoharibu mambo yote. Na wakati huo, sisi tutakuwa hapo kwenye huo mnara tunashuhudia tukio zima. Itakuwa sherehe leo." Gunner aliongea huku akiwaonesha wenzake kazi nzima waliyoifanya.
"Kwa hiyo hayo mabomu ya masaa yanalinalipuka saa ngapi?" Lobo akamuuliza Gunner.
"Ni dakika tano. Hapa nikibonyeza hii saa, mabomu yanaanza kijihesabu. Nataka huyo rais kabla hajatoka nje ya uwanja, kuwe tayari kuna mlipuko huko nje." Gunner alizidi kutabainisha alochokipanga.
"Okay. Sasa tungeenda maana kuna masaa mawili ili Rais afike. Tungeenda hilo eneo tulilolipanga." Lobo alitoa ushauri na Gunner akaanza kuwapa majukumu ya kufanya watu wake hasa yule mtaalamu wa TEHAMA.
"Nitakupigia simu baada ya kuona mambo yapo sawa. Hapo ndipo utawasha SGT ili kuwazingua wale wanaotufatilia. Baada ya hapo, ni tifu tu!" Gunner akampa muongozo yule bwana kwa jina la Boyka. Akakubali kila mpango na muda huohuo, Gunner akaenda kwenye Jet P.112 na kuwakuta madereva watatu wakijaribu hili na lile.
"Baada ya mlipuko, kazi itakuwa kwenu. Ni kuteketeza kila kitu hadi ndege yao wanayojidai nayo. Hamna kuacha na wakati huo sisi tutakuwa tunachukua video zetu za kuchonganisha." Muongozo ukazidi kitolewa toka kwenye kinywa cha Gunner.
"Usijali bosi." Wale jamaa wakajibu kwa lugha sijui ya wapi.
Gunner akatoka ndani ya ndege na kwenda lilipo gari lake ambapo alipanda na John Lobo na kijana mwingine machachari kwa muonekano tu.
****
"Bosi." Mtaalamu wa TEHAMA upande wa akina Malocha aliita. "Naona gari hili hapa la wakina Gunner linaondoka pale kwao." Akatoa taarifa mbele ya Malocha na Masai.
"Vema. Sasa Malocha, Lisa na Ndita rafiki wa Martina, mtaenda sehemu ambayo nitawaelekeza." Masai akagawa majukumu na hakuna aliyepinga hilo.
Kama walivyochaguliwa, wakatoka nje ya nyumba ile na kwenda kukwea gari lao ambalo nalo liliwashwa na kuondoka kuelekea uwanja wa ndege wa Dar es Salaam.
NUSU SAA KABLA YA RAIS WA URUSI HAJAFIKA.
Mioyo ya wengi ilikuwa inapwita kwa kihoro hasa kutokana na ujio ule wa Rais mkubwa katika dunia hii. Kila moyo ulidunda kwa njia yake. Lakini kuna mioyo ya makundi mawili, yenyewe ilikuwa inadunda kimapinduzi pekee.
"Naona kama muda hauendi kabisa." Gunner aliongea na Lobo akatabasamu na kutikisa kichwa chake kama kusikitika. Wote walikuwamo ndani ya gari lao aina ya VX8. Gunner akashusha punzi ndefu na kisha katwaa simu yake maalumu kwa ajili ya kuwasiliana na wataalamu wake kule nyumbani.
"Boyka. Anza kufungua mtambo wa SGT na waambie wale wa ndege nao wafanye yao kabisa. Waanze kuipasha moto hiyo ndege, muda wa mapinduzi umewadia." Gunner akatoa taarifa na kukata simu yake hiyo. "Lobo. Tunamaliza mchezo leo hii." Kwa furaha ya hali ya juu alimgeukia rafiki yake na kumshika mkono wa heri.
Kwa upande wa akina Malocha na Lisa, bado walikuwa wanafuata maelekezo ya Masai na gari lao lilikuwa limeegeshwa mbali kabisa na eneo la uwanja wa ndege. Waliwaona wapelelezi mbalimbali wakiwepo wale wa FISSA na binafsi. Wote walikuwa wanavifaa maalumu ambavyo waliweza kuwasiliana na kundi zima ambalo lilikuwa linalanda huku na huko katika kudumisha usalama wa eneo lile.
Zikiwa zimebaki dakika kumi, gari zipatazo kumi na mbili zote zikiwa zinafanana kwa rangi zake nyeusi, na aina ya Mercedes Benz zilifika pale uwanjani kwa msururu mrefu ambao uliwafanya wananchi kusogezwa pembeni na wengine kuamriwa waache kupita pale.
Naam baada ya vuguvugu hilo kutulia, Rais wa Nchi ya Tanzania alishuka toka katika gari ya pili akiwa na mkewe aliyevalia mavazi ya kitenge. Gari ya nyuma yake, alitoka waziri mkuu na mkewe pia aliyevaa vazi la badhee, vazi maarufu sana nchini Nigeria. Wanaume hawa wakubwa wa nchi, waliyaweka makoti yao ya suti nyeusi vema kabla hawajaanza kupiga hatua kwa hatua kuingia uwanja wa ndege wa Dar es Salaam.
Wakaingia uwanjani na moja kwa moja wakaenda kwenye sehemu fulani iliyoezekwa turubai ili jua lisiwapate. Wakawa wanaburudika na ngoma za asili.
****
"Muda umefika." Gunner aliongea na kutoa rimoti ndogo ambayo aliibonyeza na mara ikaanza kuhesabau dakika. Tayari alikuwa ameyafungulia mabomu matatu ambayo yalitegwa kuzunguka ule uwanja wa ndege.
Yalikuwa ni mabomu magumu kutambulika na wanausalama kwa sababu yalikuwa yameezekwa au kujengwa kwa plastiki kwenye lile kava lake la nje. Hakuna aliyejua kuwa yapo maeneo yale na yanaendeshwa kwa rimoti maalumu.
Wakati hayo yanaendelea huko nje, kwa mbali angani, ndege ya Rais wa Urusi ilionekana na kwa mbwembwe nyingi, Tanzania nao walirusha ndege tatu za kivita na kuikaribisha ndege ya rais huyo kwa kuisindikiza kwa nyuma. Baada ya ndege ya Rais wa Urusi kutua, zikiwa zimebaki dakika mbili mabomu kulipuka, ndege zile za jeshi zikapaa juu kwa pamoja na kisha zikapinda bawa moja mbele ya Rais wa nchi yao, hiyo ni ishara ya heshima kwa Kamanda wao wa Majeshi.
Dakika moja mbele, Rais wa Urusi alikuwa anashuka toka kwenye ndege yake na kama shamra shamra ndipo zilipozidi maradufu ya pale. Wacheza ngoma walizidi kukata viuno na wakati huo wanaume wakiruka sarakasi za hapa na pale kwa madaha na kwa kupendeza.
"Hey. Mawasiliano kwangu yamekatika." Jamaa mmoja ambaye ni mpelelezi, alimfuata mwenzake na kumpa taarifa hiyo.
"Hata mimi aisee." Jamaa mmoja alijibu.
"Kutakuwa na hatari, haraka twende kwa Rais kabla mambo hayajawa mambo." Jamaa yule aliyempa taarifa mwenzake na kisha wakaanza kukimbilia ndani ya uwanja wa ndege.
"Vipi. Mbona mambo hayajipi?" Lobo akamgeukia Gunner na kumuuliza. Gunner akawa anabonyeza kitufe cha rimoti yake lakini hakuna jipya. "Dakika ya saba hii. Hadi wanaanza kuimba wimbo wa taifa, naona kimya tu." Lobo akazidi kupambanisha maongezi yake.
"Shit. Wajinga wametegua nini mabomu?" Gunner akaongea huku kijasho chembamba kikimtiririka. Wakati hajui la kifanya, mara simu yake ikaita.
Akatazama kioo cha simu hiyo, hakuona hata namba ya mpigaji. Lakini haikuwa sababu ya yeye kutoipokea.
Baada ya kuipokea tu! Ndani ya gari alilopanda pakakumbwa na giza kiasi kisha kioo cha mbele cha gari yake, kikaanza kama kuchorwa chorwa na umeme mwekundu na hali hiyo ilipotulia, akaona sura ambayo kamwe hakuitegemea kwa wakati ule. Alikuwa ni Frank Masai akicheka kwa nyodo nyingi.
"Tatizo lako Gunner huna akili. Mi nadhani unajua kabisa kuwa mimi ni mmoja wa walioshiriki kutengeneza SGT. Sasa kwa mawazo yako ya uozo, unadhani baada ya kutengeneza huo mtambo, hatukutengeneza ant-SGT?" Masai akakaa kimya kidogo na kuendelea. "Ant-SGT, ninayo mimi peke yangu. Wale wengine wametengeneza lakini hadi sasa bado hawajang'amua mtambo huu upo wapi." Masai akamaliza na Gunner ni wazi alikuwa hoi kwa kile akionacho.
"Okay. Sipo huko Gunner. Naona jinsi unavyohangaika na mabomu yako. Hayo ni sisi ndio tuliyabuni, tunajua njia zote za kuyategua hata bila kuyashika. Nilichofanya kikubwa ni kuyazima tu kwa kutumia kompyuta. Usihangaike kuyategua. Na ndege ambayo unaitegemea kama pigo la mwisho, bora uwaambie jamaa zako waache tu. Mambo yatakuwa magumu endapo watajitokeza." Frank akachimba mkwara wakati huo Lobo alikuwa kimya akifatilia kila neno la Masai.
"Hakisimami kitu Masai. Tutamaliza kila kitu hapahapa." Gunner akaleta upinzani wa maneno.
"Oooh! Na wewe nawe mbishi hivyo? Labda tufanye hivi." Masai alipoongea hayo, Gunner alihisi kitu kikali kikipita katika bega lake. Maumivu aliyoyapata, yalikuwa hayasimuliki, lakini pia alipomuangalia dereva wake, alikuwa tayari ni maiti kwa risasi ile kupita shingoni kwake.
"Hiyo risasi hatujakukosa bahati mbaya. Ilipangwa ipite hapohapo kwenye bega lako. Huyo bwege tumemuua makusudi tu." Sauti ya Masai ilisikika tena baada ya Gunner kushika bega lake kwa sababu ya maumivu. Gunner akatazama huku na huko kuona ile risasi imetokea wapi lakini hakuona dalili yoyote ya risasi hiyo ilipotokea. Vioo vya gari vilivyofungwa hadi juu, vilikuwa salama kabisa.
"Unataka nini Masai?" Gunner aliuliza kwa hasira.
"Nachotaka ni wewe kusimamisha mpango wako haraka kabla sijafanya chochote cha ajabu." Masai akajibu jibu ambalo Gunner alikataa katukatu kulitimiza.
"Bora nife Masai. Bora nife kuliko kupindua mpango wangu." Sauti kavu na yenye kujiamini ilijibu.
"Okay. Kama umechagua kufa, ngoja nikupeleke huko unapopataka." Masai akiwa na sauti ya umakini, alikubaliana na Gunner na mara gari la watu wale likawaka bila wao kuligusa. Wote wawili waliokuwamo mle ndani walishangaa mambo yaliyokuwa yanatukia. Wakadhani labda ni ndoto lakini ilikuwa kweli hiyo.
Wakajaribu kufungua milango ya gari lile, haikufunguka wala kuwa dalili ya.kufunguka.
"Gunner, chini ya kiti chako kuna zawadi yako maalumu, naomba uitazame."Sauti ya Masai iliwatoa mawazoni wale jamaa wawili na wakati huo gari lao lilikuwa linabadili gia. Gunner akapinda mgongo na kuingiza mkono chini ya kiti na kuvuta begi fulani lililokuwepo huko.
Akaliweka mapajani na kisha akalifungua zipu. Macho yakamtoka pima kama jusi lililobanwa na mlango.
"Mabomu yako hayo. Zilibaki dakika mbili ili yawalipukie, lakini nikagandisha yasifanye hivyo. Sasa chagua, kuuza au kununua roho zenu. Mkitaka kununua, waambie wajinga wenu wa ndege ambao naweza kuwasimamisha hata mimi, lakini nataka Gunner ndio asimamishe. Waambie hao wajinga, waachane na mpango huo. Au kama hautaki, mi sina tatizo. Nakuachia mabomu yako. Chaguo ni lako, TICK TOCK." Mara baada ya maneno hayo, mabomu yale yakaanza kuhesabau dakika zilizobaki na gari lao hawa mabwana, likazidi kutembea lenyewe toka pale lilipo kwa kwenda sehemu nyingine ambayo haina watu wengi.
Lobo alikuwa kimya akimuangalia mkuu wake alivyopagawa na wakati huo, kile kioo chenye picha ya Frank Masai kilikuwa kinaendelea kuonesha picha hiyo kwa kumuona Masai akipiga mluzi na kucheza kwa furaha.
"Umeshinda Masai. Nawaambia waache." Hata Lobo aliyepembeni alishusha pumzi ndefu baada ya maneno yale. Na hapo mabomu yake yakasimama zikiwa zikebaki sekunde tisa yalipuke.
"Wasiliana nao sasa hivi, ukileta ubwege, ngoma inasoma hadi sifuri hiyo." Masai akatoa onyo na simu yake akaikata lakini kwenye kioo cha gari ile bado alionekana akiwaangalia Lobo na Gunner wanachokifanya.
"Hallow Morgan. Abort the mission now. (Holoo Morgan. Achana na huo mpango sasa hivi)" Gunner alimwambia mmoja wa marubani wa ndege ile.
"Kwa nini Gunner?" Swali likatoka kwa mtu ambaye anawasiliana naye.
"Nimekwishasema. Fanya nilichokwambia." Baada ya maneno hayo ya hasira, Gunner akakata simu yake.
"Safi Gunner. Safi sana. We ni mwanaume sasa kwa kuwa umesikiliza mwanaume mwenzako anataka nini." Mbele ya kile kioo cha gari yao, sauti ilisikika na kumfanya Lobo atabasamu na kutokea kumpenda sana Masai kwa mambo anayoyafanya.
"Nikikukamata Masai. Utajuta." Gunner alifoka kwa hasira na wakati anafanya hayo, mara simu yake ikaita. Alipoangalia alikuta ni yule rubani aliyetoka kuwasiliana naye punde. Gunner akapokea ile simu.
"Tumeambiwa hakuna kuabort mission." Yule rubani aliongea kwa wahka.
"Nani kasema?" Gunner aliuliza kwa sauti yenye kitetemeshi na hasira juu yake.
"The Shadow." Rubani yule alijibu na kukata simu haraka. Gunner akabaki kinywa wazi asijue Masai atachukua maamuzi gani.
"Usiwe na wasiwasi Gunner. Nilijua haya yatatokea tu. Nimekuja kuteketeza matkenolojia yenu yote mliyopewa, sihitaji kuona haya mauchafu. Angalia ubishi wa huyo mbwa wenu mnayemuabudu." Frank Masai aliongea hayo na kisha akabonyeza vitu fulani fulani alipokuwa kasimama, na picha kwenye kile kioo cha gari la Gunner,ikabadilika na kuanza kuonesha ndege aina ya Jet P.112.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA KUMI NA NANE
"Tumeambiwa hakuna kuabort mission." Yule rubani aliongea kwa wahka.
"Nani kasema?" Gunner aliuliza kwa sauti yenye kitetemeshi na hasira juu yake.
"The Shadow." Rubani yule alijibu na kukata simu haraka. Gunner akabaki kinywa wazi asijue Masai atachukua maamuzi gani.
"Usiwe na wasiwasi Gunner. Nilijua haya yatatokea tu. Nimekuja kuteketeza matkenolojia yenu yote mliyopewa, sihitaji kuona haya mauchafu. Angalia ubishi wa huyo mbwa wenu mnayemuabudu." Frank Masai aliongea hayo na kisha akabonyeza vitu fulani fulani alipokuwa kasimama, na picha kwenye kile kioo cha gari la Gunner,ikabadilika na kuanza kuonesha ndege aina ya Jet P.112.
Ndege ilikuwa inatoka angani kwa kasi ya ajabu tayari kwa kudondoka uwanja wa ndege ambapo Rais wa Urusi na Tanzania tayari walishamaliza mambo mengi na sasa walikuwa wanasalimia wacheza ngoma za jadi.
Ndege ile ikiwa inashuka, mara ikaanza kukata kona kuelekea kushoto. Marubani wa mle ndani wakaanza kuhaha kuirudisha katika uelekeo wake lakini wakawa wanashindwa. Ikawa hali tete kwao hasa pale ndege ilipoacha muelekeo wa kwenda kudondoka uwanjani na kuanza kwenda kwa kasi eneo ilipo bahari ya Hindi.
P.112 ilipofika katikati ya bahari ya Hindi, ikiwa bado ipo juu, ikalipuka na mshindo mkubwa ukaikumba Dar es Salaam.
"Yuhuuuuu." Sauti ya Man'Sai ilisikika ikishangilia kama mchezaji aliyefunga goli. Wakati huo Gunner alikuwa katoa macho kama kaona maiti inayotembea.
"Man'Sai The Great." Lobo alijikuta akitamka maneno hayo na kumfanya Gunner amwangalie kwa jicho la hasira.
"Umeona hiyo Gunner?" Masai alimuuliza Gunner wakati vipande vya ndege ile vikidondokea baharini. "Bado SGT, hiyo rahisi tu. Sasa hivi FBI wamekwishajua upo wapi huo mtambo. Kabla hawajaufikia, nitakuwa nimekwisha umaliza." Masai alimaliza na mawasiliano kukata. Hali ya gari ikarudi palepale. Kioo kikawa safi na kuonesha ya nje kama mwanzo.
Gunner akatupa macho labda ataona risasi aliyopigwa ilipopita, hakuona chochote zaidi ya kumuona Lisa akimpigia saluti na kuingia kwenye gari fulani ambalo namba zake zilikuwa hazieleweki. Yaani zinabadilika kila dakika.
"Mmh! Ulisema Lobo. Katuzidi ujanja huyu bwege. Sasa ni muda wa kulipa kisasi, atatutambua huyu bwege." Gunner aliongea hayo kwa hasira huku akifungua vishikizo vya koti lake na kuangalia pale alipopigwa risasi na wakati huo, Lobo anamsukuma yule dereva mfu siti ya nyuma.
"Nilikwambia lakini. Namjua Masai kuliko unavyodhani. Ni msumbufu na ni mtu wa neno lake. Hukunielewa. Pale mpango ulipopanguka, kungekuwa na watu wengine wa kujitoa muhanga, wangemaliza yote haya. Wewe hukunielewa nilipokwambia tuongeze watu. Now what? Japo Masai hayupo upande wangu, lakini huyo jamaa mi namkubali kuliko wewe. Yaani angekuwa ndiye Gunner yule, sasa hivi tungekuwa tunatangaza vita vya dunia." Lobo aliongea huku akifoka.
"Sasa huko unanilaumu Lobo." Gunner aliongea kwa sauti ya kinyonge.
"Hapana. Ulipaswa kusikiliza pande zote na si kufanya maamuzi ya peke yako." Lobo alizidi kumpa maneno ya kweli patina wake.
"Okay Lobo, next tutapiga kazi kwa umoja." Gunner aliongea na kumruhusu Lobo kuwasha gari lake tayari kwa kuondoka eneo lile.
****
Masai baada ya kumaliza alichokifanya, akavaa suti aliyopewa ja Alejandro na kutoka nje ambapo alichukua usafiri wa pikipiki na kuanza kuelekea pori moja lililopo barabara ya kwenda Kibaha.
Kasi ya pikipiki aliyokuwa anaiendesha, kila mmoja pale Kivule alikuwa haamini kama ni mtu ndiye anaendesha. Pikipiki bora kabisa kupata kutokea duniani, ndiyo ambayo ilikuwa inatitia mtaa hadi mtaa hadi kufanikiwa kutoka Jiji la Dar es Salaam.
Alifika eneo analolitaka mapema kabisa na kukuta kupo kimya.
"Nenda kulia Masai." Alisikia sauti ikimuakuru kwenye kishikizo alichokibandika sikioni. Naye akaenda na kujificha pembezoni kidogo mwa ukuta mzito uliojengwa eneo lile.
Mara akatokea mlinzi mmoja ambaye alikuwa anakimbia na kama kangaroo, yaani akirukaruka. Akasimama mbele ya kichaka fulani na kupekua kwenye zipu yake. Akatoa sijui kinini na kuanza kujisaidia haja ndogo.
Kwa jinsi ilivyokuwa inatoka ile haja, mlinzi yule alijikuta akifumba macho yake na kuburudika ipasavyo na lile tendo.
Frank akiwa nyuma yake, akatoa nyota mbili na kuzirusha kiustadi kama ninja. Zikamkuta yule bwana shingoni upande wa nyuma. Akadondoka kama mzigo wa kuni. Umauti ukamkumba.
"Okay Masai. Hakuna kizuizi tena. Endelea." Mtaalamu aliyemuacha Kivule aliongea na Frank akapanda ukuta mkubwa uliokuwepo pale. Akajitoma ndani kwa kutulia miguu na kisha akaweka goti lake moja chini na kutazama huku na huko.
Akakimbia kwa kasi ya ajabu kutokana na suti aliyoivaa. Akafika eneo moja ambalo ndipo anaamini mtambo wa SGT upo.
"Fungua kidogo mtaalamu wangu." Masai aliongea huku kashika kishikizo chake kilichopo sikioni. Mara sehemu ile ilifunguka kwa ukimya mkubwa ambao si kawaida yake kuwa hivyo. Ukapatikana upenyo ambao Frank Masai atapita. Kijana wa watu akarusha kamba ambayo ilinasa mahala kwenye mti na kujikaza hapohapo.
Akiwa na begi lenye vifaa fulani humo, akarushia kamba iliyobaki ndani ya shimo lile na yeye akaanza kushuka hadi chini yake palipo mtambo wa SGT.
"Okay Mtaalamu. Nimeshakanyaga chini." Frank alimpa taarifa jamaa ambaye alikuwa anaendesha mitambo kule Kivule.
"Naona kila kitu Kamanda. Kazi nzuri sana." Mtaalamu akajibu kwa furaha. Frank akawasha taa ambayo aliigonga mkononi na kutoa mwanga wa buluu. Akaitupa taa ile sehemu fulani, na shimo lile refu likatapakaa ule mwanga. Sasa akaweza kuuona mtambo wa SGT ukiwa umetulia kando kando ya shimo lile.
Masai akasogea kwa uangalifu ili asilete kelele mle ndani. Akaufikia mtambo ule kisha akatoa vifaa fulani kwenye begi lake, na kwa taratibu, akaanza kufungua mfuniko uliokazwa vema kwa nati za China.
Kifaa alichotumia, kilikuwa kinatumia umeme hivyo ndani ya dakika mbili, mfuniko mdogo wa mtambo ule ulifunguka na Masai akaingiza mkono wake ndani ya mtambo na kushika kitu fulani ambacho kilikuwa kimeungwa na nyaya nyingi za mtambo ule.
Akazikata nyaya zile kwa uangalifu na pale alipomaliza, akaweka kile kitu kwenye begi lake.
Baada ya hapo. Akatoa bomu moja la kubandika ukutani na kufanya kama bomu linavyotaka. Baada ya kulibandika, akaliwasha liwe tayari kulipuka atakapo bonyeza rimoti yake. Akawa kamaliza kazi iliyompeleka.
Akashika kamba yake na kuanza kutoka nje. Dakika mbili mbele, akawa kashikilia uzio wa shimo lile na kichwa kimetoka nje. Akatoka kwa uangalifu mkubwa ili asidondokee ndani.
"Holoo." Masai akasikia sauti hiyo ikimshtua na alipotazama ni nani, akakutana na walinzi watatu huku wote wameshikilia mitutu yao ya bunduki.
"Ulipogusa mtambo, ukapeleka taarifa hadi ndani. Huku kwangu mawasiliano yalikatia." Masai alisikia sauti hiyo ikimuambia kwenye kile kishikizo chake cha sikioni.
"Karibu kwetu. Wewe ndiye Masai." Mlinzi mmoja aliuliza huku akicheka kwa dharau.
"Mbona chembamba halafu huna sura ya kutisha kama wanavyosema wakina Lobo." Mlinzi mwingine aliuliza huku akiwa hana mbavu kwa kicheko.
"Yaani hichi hata nikitupa bunduki... ." Mlinzi yule wa kwanza aliongea huku akitupa bunduki yake upande wa kushoto. "Hakinigusi hata ngumi moja." Akamaliza kwa kujigamba na kusogea mbele ya Masai.
"Yaani mimi hiki nikikipuliza tu! Kitayumba yumba kama kimelewa. Embu kione." Mlinzi wa tatu aliongea kwa mara ya kwanza huku anamsonda Masai kwa bunduki. Muda wote Masai alikuwa akiwatazama huku akihesabu pumzi zao kwa chati.
Katika hali ambayo hakuna mlinzi aliyetegemea, walijikuta hawana bunduki zao na wakati huo ile suti ya Masai ilishatengeneza maski usoni kwa kwake. Ilikuwa ni kasi ambayo hakuna aliyeidhania kwani wakati wao wakicheka hadi wanafumba macho yao, Masai alikuwa akibofya saa maalumu ya kuendesha suti yake.
"Haya sasa. Naanza na wewe ambaye hata bila binduki unanipiga." Masai akaongea huku akimfuata yule mlinzi aliyetupa bunduki pembeni. Ngumi mbili za kifua, na nne za tumboni kisha mbili za shingoni, zilotosha kumuondoa maisha yake yule mlinzi kwa sekunde kadhaa tu.
"Nakuja kwa wewe ambaye ukinipuliza naanguka. Haya nipulize." Yule mlinzi alikuwa akitetemeka kama vile kaona jini. Hawezi kufanya chochote na hapohapo haja ndogo ikawa inamchuruzika toka juu na kushukia kwenye mabuti aliyovaa. "Oooh! Hapo ndio unanipuliza?" Masai akauliza na wala hakupoteza muda wa kusikia jibu.
Akamshika yule bwana mkono wake na kwa nguvu akapiga ngumi mbili za kwapani zilizovunja mkono wa yule bwana. Kabla hajapiga kelele za maumivu, Masai akamalizia pigo la mwisho la kichwa cha mdomo. Jamaa alipopiga kelele, mdomo wake ulionekana wenye mapengo.
"Aaah! Nilitaka kukusahau. Umesema mimi sitishi? Na hapa je?" Baada ya maneno hayo, Masai akaitanua ile maski sehemu ya macho na kuonekana kama alien. Halafu kwa mdomo wake akapiga kelele zilizomfanya yule jamaa kuinama huku kaziba masikio yake kwa viganja vya mkono. Aliposimama, Masai akamtisha kama anamkimbiza. Jamaa akaona isiwe tabu, njia rahisi ni kukimbia tu. Jamaa akamuacha yule jamaa mwenye mapengo akiwa hana la kufanya.
"Siku nyingine muwe na heshima." Masai aliongea huku akimsukuma kichwa yule bwana na kumfanya ajigonge vibaya kwenye mti. Jamaa akazimia.
"Upo vizuri kaka." Sauti ya mtaalamu wa Malocha ilisikika ikimpongeza Masai kwenye mawasiliano aliyovaa sikioni kama kifungo cha shati.
"Usijali mtaalamu. Utajifunza mengi." Masai akajibu huku sura yake ikifunguka na muda huohuo, akarukia ukuta na kutokomea mbali na eneo lile.
****
" Boss. Masai alikuwepo hapa dakika kumi zilizopita na alionekana akigusa mtambo wa SGT ambao sasa haufanyi kazi." Boyka alimpa taarifa Gunner kwenye simu wakati jamaa yule akirudi na Lobo katika makao yao.
"Unasemaje Boyka?" Kwa mshangao Gunner akauliza.
"Na kaua walinzi wawili na mwingine yupo hapa hajitambui wala kuwa na meno." Boyka akazidi kumchanganya Gunner. Maongezi hayo Lobo alikuwa anayapata moja kwa moja wakati yanaendelea.
"Katega bomu kwenye SGT. Waambie hao jamaa waondoke haraka eneo hilo." Lobo akamwambia Gunner ambaye alitimiza suala hilo haraka.
"Boyka, ng'oa vitu vyote muhimu na kisha nenda kwenye ile nyumba yetu ya pili. Fanya haraka, kuna hatari hapo." Hakusubiri jibu Gunner, akakata simu na kuongeza kasi ya gari lake kupitia barabara ya Tazara kabla hajapindia Buguruni na kunyoosha kama anaelekea Ubungo.
****
"Wajinga naona wanakimbia nyumba." Mtaalamu wa mitambo upande wa Malocha aliongea baada ya kumuona Masai akiingia katika kile chumba chao cha kazi.
Tayari Lisa, Mubah na Malocha walisharudi na kuoneshwa kazi ambayo Masai kaifanya.
"Lazima wakimbie hapo. Kimbembe kitabaki kwa wale wajinga wanaojiita FBI. Lazma walie." Frank aliongea huku akivua koti la suti yake na kuliweka juu ya kiti kimoja mle ndani.
"Man'Sai nimeizimia hiyo suti yako." Malocha alimwambia Masai.
"Usijali Kamanda. Hii yako tu. Ngoja nimalize kazi yangu." Masai akajibu na kumfanya Malocha atabasamu kwani atakuwa kapata vazi ghali kuliko vazi lolote analolimiliki. Maongezi ya hapa na pale yaliendelea lakini yalikatishwa tena na mtaalamu.
"Hey. Naona kuna wazungu wamezunguka lile eneo la Gunner." Jamaa akatoa taarifa ambayo ilifanya kila mmoja kusogea karibu na skrini za mle ndani.
"Washenzi sana hawa. Sasa ngoja niwaoneshe kazi." Baada ya wapelelezi wale kulizunguka eneo zima la Gunner, wakaanza kuingia ndani mmoja mmoja na mwisho wake, wote walikuwa wamejaa ndani.
"Frank akabonyeza kitufe cha Enter kwenye kompyuta ambayo hakuna hata mmoja aliyewaza kuitumia. Mlipuko mkubwa ukaikumba ardhi ya pale na maeneo ya karibu. Ardhi ikatitia na kujifukia. FBI wote wakateketea palepale.
"Nawachukia sana hawa washenzi." Frank alitamka na kutoka katika kile chumba cha mitambo akiwaacha wakina Malocha wametumbua macho.
"Masai ni kichaa." Malocha aliongea huku akitikisa kichwa kushoto na kulia.
"Ila nampenda akifanyacho. Huwa hakosei, yupo sahihi." Mubah aliongea hayo na yule mtaalam alimpa 'tano' kuonesha kakubaliana na maneno yale ya Mubah.
*****
Katika kitongoji kilichopo nje kidogo mwa jiji la Dar es Salaam, wanapaita Mbezi Beach. John Lobo, Gunner na kundi lake la watu watatu waliobaki walikuwa wanajaribu kuunda mitambo yao tena kwa ajili ya mawasiliano.
Wakati hayo yakiendelea, simu ya Gunner iliita, na alipoiangalia aliona namba ngeni na 'code' namba yake si ya Tanzania. Kwa uoga na kujishuku, akaipokea na kuiweka sikioni.
"Nini kimetokea?" Swali la kwanza kulisikia Gunner baada ya simu ile kuipokea. Ilikuwa ni sauti nzito na inafanana na sauti ya redio iliyokwisha betri.
"Ni Masai." Gunner akajibu huku akitetema.
"Masai ndiye nani?" Sauti ile ikauliza kwa ukali na kumfanya Gunner kutojibu chochote. "Acha ujinga we mpumbavu. Nitakuua mimi. Umefanya ujinga ambao hutakiwi kusamehewa kosa lako." Ile sauti ilizidi kufoka.
"Hapana The Shadow. Tunaomba msamaha. Tupe nafasi nyingine tutafanya vema." Gunner alijitetea huku kijasho chembamba kikimtoka.
ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom