NomaaaaaaaaaaaaaaaCABO-DELGADO-PART 37
Komandoo "JS" akauliza, "Kachero Manu mmemuacha wapi? toeni jibu nyinyi makhabithi la sivyo na nyie naondosha roho zenu sasa hivi". Hapo hapo Kachero Manu akatambua huyu yupo upande wake kwa sababu kama angekuwa upande wa adui angekuwa anajua kila kitu kinachoendelea na asingemteka rubani yule. Akaibia Kachero Manu kumtazama kwa jicho pembe, akaona ni mtu aliyefuga masharafa mashavuni mwake yenye mvi nyeupe, akakumbuka Komandoo "JS" anafuga masharafa kutokana na picha aliyopewa ofisini Dar es salaam na Bosi wake.
Alichofanya Kachero Manu ni kujitambulisha kwa lugha ya siri (SPY-CODE) aliyopewa ya kuwasiliana na Komandoo "JS" pindi alipojitambulisha ujio wake na uhitaji wa gari na nyumba ya kukodi. Akasema kwa sauti ya juu "wewe ni CUT-OUT?" akimaanisha anamuuliza Komandoo "JS" ni kiunganishi kati ya ofisi ya Makachero wa Tanzania nchini Msumbiji?.
Makachero wazoefu wana lugha zao ambazo wanazitumia kuwasiliana ambazo ni ngumu kwa asiyemhusika kuzifahamu. Mfano ukiskia msemo, "EARS ONLY" maana yake ni taarifa ya siri mno haitakiwi kuandikwa ila inafikishwa kwa maneno pekee, au ukiskia "DEAD DROP" maana yake ni mzigo ambao Kachero mmoja ataupeleka sehemu fulani atauacha kisha mwingine ataupitia kuuchukua mzigo huo bila Makachero wawili hao kuonana uso kwa uso.
Hivyo kitendo cha kutumia neno "CUT OUT" hapo hapo wakatambuana, Komandoo "JS" akashusha bastola zake chini, na Kachero Manu akachomoa bastola yake na kumuweka chini ya ulinzi yule dereva wa Bob Chinanga na kumpa amri ya kumfungua kamba rubani wa helikopta.
Baada ya pilikapilika hizo za dakika chake safari ikaanza muda wa kama saa 3:05 usiku. Hawakuwa na muda wa kupoteza huku rubani akipewa tahadhari ya kutoleta ujanja wowote wa sungura utakaogharimu maisha yake. Wakati wakiwa juu angani wameanza kupaa meta chache tu ikasikika milipuko mikubwa ya mabomu huko chini kambini, 'Gorongosa Camp' inateketea kwa moto.
Dr.Anabella na Kachero Manu wakatazamana huku kila mmoja akitabasamu, alikuwa Kachero Manu amelipua mabomu aliyoyatega pale kambini kwa kutumia kitendambali (rimoti) ya mkononi mwake aliyovaa kama saa mkononi. Kiwingu kizito cha moto mwekundu kilitanda kuizunguka kambi ya Gorongosa usiku huo utasema siku ya kiama ndio imetoka. Kambi hiyo iliteketezwa kabisa bila kusaza kitu chochote.
SURA YA KUMI NA NANE
Mwisho wao Mafioso wa Cabo-Delgado umewadia
Soko la Baraca maana yake ni soko la vitu vya bei rahisi. Hili soko lipo katikati ya Mji wa Pemba kilometa takribani kama 2 tu kutokea barabara ya pwani (Coastal Road). Ni soko ambalo wakati wote limefurika limefurika Wafanyabiashara na wateja wao. Sokoni hapo ni maarufu pia kwa bidhaa za vinyago vya Kimakonde vya kila sampuli ikiwemo na bidhaa za baharini. Ni soko ambalo aghalabu utakutana na watalii wa kutoka nchi za ng'ambo kama China, Japani, Marekani na mataifa mengineyo ya kigeni wakiwa wametingwa kujitafutia zawadi za bidhaa asilia za kurejea nazo nchini kwao.
Waswahili wanasema kila kwenye msafara wa mamba na kenge nao hawakosekani, kwani katika harakati hizi za soko la Baraca za watu kujitafutia riziki zao za halali za kujiendeshea maisha kwa ajili yao na familia zao, kampuni ya "Monte Branco Ltd" nao walijichomeka katika eneo hili kwa kuwekeza kiwanda cha daraja la kati cha kusindika korosho, lakini ndani yake ilikuwa ni ofisi yao kuu ya kupanga mipango haramu yote ya kuhujumu nchi ya Msumbiji. Chini ya kiwanda inasemekana kulikuwa na ofisi za wapanga madili na wizi wa kila aina ambao walikuwa wanalipwa mishahara minono na mmiliki wa kampuni Bwana Alfredo.
Dr.Anabella ameshawahi kupelekwa huko chini ya kiwanda zaidi ya mara moja na mchumba wake Inspekta Jenerali Mark enzi mapenzi yao yamepamba moto. Mark katika kutaka kujionyesha kuwa ni mtu muhimu sana mbele ya Bwana Alfredo, siku ya kwanza alimchukua Dr.Anabella usiku wa manane siku ambayo Dr.Anabella alikuwa na zamu ya usiku katika hospitali ya kiwandani hapo akampeleka huko kwenye mahandaki chini ya kiwanda kumtembeza. Yalikuwa ni mahandaki yenye maofisi na chumba zenye starehe zote na mahitaji yote muhimu yanapatikana. Milango yake ilikuwa ni ya kufunguka kwa rimoti inayofunguliwa na namba za siri maalumu. Inspekta Mark alimdanganya Dr.Anabella kuwa anazitumia ofisi hizo za siri kupangia baadhi ya operesheni dhidi ya wahalifu.
Kiwandani hapo ndio palipangwa kufanyika mkutano wa Mwisho ambao utahitimisha uhai wa Kachero Manu, na kutoa onyo kali kwa wote wenye kufuatilia nyendo za Bwana Alfredo katika biashara zake za rubi na nyinginezo.
Mkutano ulipangwa uanze saa 4:00 kamili usiku, huku ukumbi ulikuwa umepambwa vikorombwezo vyote muhimu kwa mahitaji ya mkutano huo muhimu. Na washirika wote wa Bwana Alfredo, Mafioso wenzake kutoka Ureno na Afrika ya kusini walikuwa wameshawasili Pemba tayari kwa mkutano. Wengi walikuwa ni vigogo wana hisa wa kampuni na watendaji wakuu wa shughuli za kila siku za kampuni. Inspekta Jenerali Mark Noble alikuwa hatulii kama mbwa koko jike mwenye joto anayehitaji kupandwa. Alikuwa kama mtu mwenye mazonge yanayotokana kuelemewa na majukumu. Yeye kama akiwa Afisa Usalama Mkuu wa kampuni na kiongozi wa kikundi cha mateso cha "NACATANAS" alikuwa anahaha kuhakikisha mambo yanaenda kama yalivyopangwa bila kuharibiwa na mtu yoyote.
Lakini kilichokuwa kinamnyima raha ni kitendo cha helikopta kutokea Gorongosa kambini kuchelewa kufika Pemba. Alikuwa amempa maagizo Bob Chinanga ya kuhakikisha wanafika Pemba ifikapo saa 2:00 usiku. Sasa muda huo wa saa 3:15 usiku muda ukiwa unayoyoma haonekani Bob Chinanga wala wasaidizi wake. Mbaya zaidi ilikuwa mwanzoni anawasiliana na rubani na kule kambini lakini sasa alikuwa akipiga simu zote hazipatikani kabisa.
Kijasho chembamba kikaanza kumtiririka usoni na kwenye makwapa ya mikono yake jasho jekejeke likawa linamtiririka. Kengele ya hatari ikagonga kichwani mwake kuwa huenda Kachero kawazidi nguvu. Lakini kwa upande mwingine anajipa matumaini haiwezekani mtu mmoja aweze kuteketeza kikosi kizima cha zaidi ya watu elfu na ushee na kama akiweza basi itakuwa ni zaidi ya miujiza hashara ya Mtume Musa kwa Farao alipoenda kuwakomboa wana wa Israeli.
Inspekta Jenerali Mark Noble alikuwa ameshachoshwa na maisha haya ya mikiki mikiki. Aliweka nia na adhima ya kuacha kazi katika idara ya Polisi ya Msumbiji, kisha pia astaafu kazi kutoka "Monte Branco Ltd" kazi ambayo ilishakuwa hatarishi kwake. Ambapo suala la kupoteza uhai ilikuwa ni dakika sifuri. Alipanga achukue mafao yake kisha aondoke na mchumba wake Dr.Anabella kwenda kuishi kwenye visiwa vya Madagascar. Kwa mafao yake atakayopewa na Bwana Alfredo yalimpa jeuri na kiburi cha kuweza kuishi nchi yoyote ya Kiafrika bila kufanya kazi kwa muda hata wa miaka 50.
Inspekta Jenerali Mark akiwa amezama kwenye dimbwi la mawazo nje ya sehemu ya kuegeshea magari akiwa anawasubiri akina Bob Chinanga akasikia mlio wa simu yake unaita akaanza kupagawa. Akadhani anataka kuulizwa kuhusu ujio wa Kachero Manu. Ulikuwa ni mlio maalumu kwa ajili ya Bosi wake Bwana Alfredo, akajidhania kama yupo ndotoni maana hakutegemea kupokea simu ya Bwana Alfredo katika kipindi kigumu kama hiki. Alipoitoa simu yake akaipokea huku vidole vinatetemeka kama mlevi gongo.
"Habari za siku BIG BOSS" alisema Mark kwa sauti ya kujifaragua na kujilazimisha furaha. "Njoo ofisini mara moja kabla ya kikao nina mazungumzo nyeti na wewe...!" kisha kabla ya kujibu kitu chochote ikawa tayari simu imeshakatwa na Bwana Alfredo. Moyo wa Mark ukalipuka, na kuanza kwenda mbio kama mwanariadha anayeshindania medali ya dhahabu katika mbio za meta 100 moja. Akapiga moyo konde kuwa liwalo na liwe ngoja aende akamsikilize Bosi wake.
Akaanza kutembea kuelekea kwenye ofisi ya Bwana Alfredo iliyoko chini ya kiwanda kwenye handaki kwa kupitia kwenye maegesho ya magari, huku anajifanya kutikisa funguo za gari yake kupotezea hofu yake kuonyesha anajiamini. Lakini mawazoni alikuwa anajiambia leo kazi ipo kusuka au kunyoa.