Riwaya: Banguzi

Riwaya: Banguzi

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

______SEHEMU YA KUMI NA TISA______



Wenzake wakicheka, aliona ni karaha mno sauti zao. Alitamani hata nao wapatwe na hali kama yake, ndiyo hivyo halikuwezekana. Hakika jinsia ya kike ikijua kuchukia, basi hilo ni balaa kubwa lisilo na kipimo. Jinsi anavyopewa kipaumbele na mhusika mwenye siku yake, na namna ambavyo watu wanavyokongwa nyoyo na vituko vyake ndiyo kulizidi kumfanya aungue nafsini mwake.



_________TIRIRIKA NAYO

Hali hii aliyo nayo Gina, laiti kama Jamal angeliitambua mapema basi asingeruhusu itokee kwake. Lakini ndiyo hivyo hakuwa na walau umaizi juu ya suala hilo, yeye aliona sehemu hiyo mambo yote yalikuwa yakienda sawa. Tabia yake ya kupuuzia mambo, ilimfanya wala asiwe na fikra juu ya binti zaidi ya kumwona ni asiyejitambua ingawa amefika kwenye ngazi kubwa ya elimu ya sekondari.

Hatimaye Jamal alishuka chini akiwa hana hili wala lile, akakumbatiana na Heriety kwa furaha. Alipoketi kitini tu, mabinti wengi walimfuata na kila mmoja akiwa anamwongelesha na kuhitaji ajibiwe. Wapo waliyotaka kupiga naye picha na wala hakuzuia hilo alikubali bila hiyana. Kijana aligeuka kuwa nyota wa sherehe hiyo kuliko hata mwenye kuhusika nayo, muda huo hata Heriety mwenye alikuja kuketi naye karibu kutokana na kumuhusudu mno.

Aliongea naye kwani ni faraja tosha kwake kutokea jambo kama hilo, binti alipenda kumwona kijana kila muda. Alihitaji haswa walau kuliona tabasamu lake kila saa, ni mwenye kutaka kusikia sauti yake yenye kumletea bashasha kila aitoapo. Hakika alifika mno kwake, ila hakuwahi kuonesha ishara yeyote ile kwake. Jamal hakuwahi kufikiri jambo kama hilo kama litakuwepo kwa Heriety, alimwona ni rafiki tu na wala hakuwahi kumwonesha ishara yeyote ya kumpenda.

Ndiyo maana hakuwa na shaka yeyote akiwa yupo karibu yake, laiti kama angelikuwa na tatizo naye basi asingeliweza kuwa naye namna hiyo. Gina aliitwa kujumuika nao mahala walipo ambapo walikuwa na baadhi ya marafiki wengine, hakuweza kupinga hilo ingawa moyoni alilaani mno jinsi utaratibu unayoenda hapo. Walikula kwa pmoja chakula huku Jamal akiendelea kuwafurahisha, hadi wanamaliza.

Hatimaye muda wa kucheza muziki ukafika, Heriety akaomba kuufungua muziki na kijana anayemhusudu. Shoga yake ndiyo akawa anaungua moyoni kabisa kwa kuona anapewa kipaumbele, alitaka kuona hata awe kafukuzwa kwenye sherehe hiyo lakini ndiyo jambo hilo halikuwezekana hata kidogo.
Muziki ulichezeka hadi ilipofika usiku mnene zaidi, ambapo watu walianza kupungua mmoja baada ya mwingine na kusoge eneo la jirani ambapo kuna mahema. Wachache walielekea zilipo hoteli eneo hilo wapumzike. Wengine waliendelea kuburudika hadi ilipokaribia alfajiri ndipo kila mmoja alikwenda kulala, muda huo Jamal aliongozana na watu wake aliyokuja nao hadi kwenye hoteli iliyopo jirani na hapo akaenda kupumzika.

______________

Watu wakiuchapa usingizi upande wa Bagamoyo, ndani ya jiji la Dar es salaam kwenye uwanja wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere. Watu maalum waliyovaa suti nyeusi walionekana wakiwa wamesimama eneo la kusubiri wageni. Hawa walijipanga vyema huku kukiwa na mtu mzima mwenye asili ya usomali akiwa amesimama mbele yao.

Haikuchukua muda mrefu wa kujipanga hivyo, aliingia mwanaume wa kisomali mwenye suti nyeupe akiwa na mikufu kadha ya rangi ya fedha shingoni ambayo kila mmoja ulikuwa na kidani chenye kung'aa. Huyu alipoonekana mbele ya mwanaume wa kisomali alionesha tabasamu usoni mwake, halafu akamkumbatia kwa nguvu mno huku akionekana ni mwenye kumkumbuka mno.
"JD ni miaka sasa hujarejea nchini, nimekukumbuka mno mdogo wangu", Mwanaume mpokezi alisema.

"Anko Husa kazi kwa Fernando ni nyingi mno, yaani sasa hivi nimeamua kustaafu kabisa huko na kuja kuendesha miradi yangu. Vipi mwanangu hajambo? Katibiwa?"

"Hajambo ila mambo ni yaleyale hakuna jipya, ila nikupe pongezi kwa kuwa na mtoto mwanafalsafa namna ile", Husa alisema kisha akamwongoza JD hadi nje ambapo kulikuwa na magari kadhaa ya kifahari yenye kuwasubiri. Aliingia gari moja naye, huku mizigo yake ikiwekwa nyuma na safari ya kuondoka mahala hapo ikaanza msafara ukiwa mrefu.

"Hebu nipe mpya yote yaliyojiri kipindi chote ambacho mimi sipo, nitahitaji muhtasari tu lakini mkanda mzima tukifika nyumbani uniambie"

"Ni mengi mno yaliyojiri ila kikubwa ni kwamba, Mwanahawa ni kanuna mno kwa kutorejea kwako miaka zaidi ya kumi hadi mtoto kawa mkubwa. Yaani anamlea yeye na mimi nikitoa msaada ila anaona kama umemtelekeza"

"Nitaanzaje kuitelekeza damu yangu mimi, kwanza yupo wapi huyo mwanamke hivi sasa? Nahitaji sana kumwona kijana wangu Kimweri"

"Karejea kwao sasa hivi, ila Kimweri yupo ukimwona nadhani utamsahau kabisa"

"Huyo sihitaji nionane naye sasa hivi, najua kwa jinsi mama yake alivyokasirika basi kwake hakutokuwa na afadhali. Ngoja niweke mambo sawa kwa Mwanahawa"

______________


"Jus JD yule kaingia mjini leo hii, kwanza nahitaji kuonana naye anaweza kuwa msaada kwangu", Jus alisema akiwa ameketi ndani ya gari akimwona JD akitoka na wafuasi wake, pembeni yake aliketi Avi.

"Utaanzia wapi au hujui yule jamaa ni kibaraka wa Fernando kwanza unajua yupo kwa kazi gani huku nchini, kama kaja kukuua wewe je?", Avi alimwambia

"Ukiona nimeachiwa hadi nikakimbia ujue hana shida na mimi, tena yeye ndiye aliyenishauri nitoroke Fernando hana nia nzuri ila sikumsikiliza hata hadi yananikuta haya. Nahitaji niongee naye kama kuna ufumbuzi mwingine zaidi juu ya jambo hili, nimechoka kuwa mtumwa wa dawa"

"Kumbe hadi jamaa alikupa ushauri wa kutoroka usiwe mtumwa wa Fernando. Mzee yule huwa hana muda wa kumlipa fadhila mtu mwenye asili ya weusi moja kwa moja. JD asili si yako yule ndiyo maana kadumu"

"Najuta haswa, ok hebu washa gari twondoke naona msafara wake unapotea ule"

Muda huo wakijadili hayo, walimwona msomali yule akipita na kundi kubwa na wafuasi wake sambamba na Mjomba wake. Msafara ulipoanza kutoweka kwa kasi ndipo nao wakaanza kuufuatilia kwa kisiri mno huku wakihakikisha hawawezi kugunduliwa. Walifika hadi maeneo ya Ilala ambapo magari hayo kwa pamoja yaliingia eneo ambalo kuna nyumba ya kifahari yenye ghorofa mbili.

Vijana hao waliipita nyumba hiyo na kuja kusimama baada ya kuivuka mitaa mwili hivi, hapo ndipo kwa pamoja walitazamana baada ya kujua eneo ambalo mtu wao waliyokuwa wakitamtafuta ndiyoalifikia.

Walifika eneo ambalo kuna makutano ya barabara na wakahitaji kugeuka na kurejea kule walipotoka. Hapo ilimbidi Avi akanyage breki akiwa hana hili wala lile, kitendo cha kufanya hivyo kilisikika kishindo cha ajabu kisha wakaona gari lao likipelekwa upande wa pili wa barabara huku vioo vikiruka. Haikuhitaji elimu ya ziada kuweza kubaini kuwa wamegomgwa sehemu ya ubavuni jirani kabisa na magurudumu ya nyuma.

Kujiri tukio hilo hakuna ambaye alitaka kulaza damu humo garini, Avi alifungua mkanda upesi na akajirusha nje. Jus naye akafuatia ambapo waliangukia pande tofauti. Mmoja akiwa kulia na mwingine kushoto, upande wa kulia ndipo lilionekana lori lenye mtungi wa kuchanganya zege likiwa limeegeshwa.

Upande huo ndiyo alipoangukia Jus, na kitendo cha kutua chini tu. Alibimbirika kiufundi kisha akasimama wima kwa mara nyingine, akiwa namna hiyo alihisi mvumo ukimjia upande wa shavu la kushoto. Alibonyea chini kwa haraka baada ya kubaini hiyo ilikuwa ni ngumi, akiwa huko kabla hajainuka alitupa konde zito la tumboni ambalo lilimpata sawia mrushaji ngumi aliyekuwepo gizani. Aliinuka na ngumi nyingine ya kidevu na kumfanya mtu huyo aende chini, hukohuko alimuwahi kwa kumkanyaga kifuani mara mbili na kumfanya ateme damu mdomoni.

Upande wa Avi ulikuwa na afadhali hakukutana na kikwazo chochote ila aliona kile kilichokuwa kikimkumba Jus. Mwenzake alipoweza kumwangusha yule mvamizi, alishuhudia akijiwa na mwingine katika muda ambao anamshambulia kwa kukanyaga yule aliyejaribu kumdhibiti. Avi hakutaka yamkute makubwa , alitoka kwa kasi upande huo aliyokuwepo.

Alipokanyaga barabarani alikimbia kwa hatua mbili kubwa kisha akajirusha juu, alipokuja kutua alitua mabegani kwa yule mwingine aliyekuwa nyuma ya Jus. Hata mwenzake alipogeuka nyuma hakujishughulisha alijua tayari kamalizwa. Mhindi huyu bila ya kuchelewa akiwa ameketi mabegani kwa adui, alimpiga viwiko kadhaa vya utosi . Alihakikisha hadi anayumba na kuelekea chini, ndipo akajifanya kama vile anatoka mabegani mwake. Ila yule mtu alipofika chini, miguu ya Avi ilimbana shingoni na huku akawa anauvuta mkono mmoja. Mtu yule alijaribu kujinasua ila hakuweza hata, alibaki akizungusha miguu kutoka upande mmoja kuelekea mwingine.

"Kakutuma nani?', Jus aliuliza huku akimtazama adui yao aliyepigwa kabari. "Husemi siyo, Avi ongeza nguvu hizo hadi ataje mwenyewe".

"Mkuu Husa ndiyo katuagiza bada ya kupewa taarifa na vibaraka wake waliyopo kwenye maegesho kuwa mnawafuatilia", Hatimaye alisema mwenyewe na hapo Jus alijikuta akitoa tusi zito la nguoni kisha akamtukania Husa mama yake.

"Yule msomali sijui ana dawa, yaani pamoja na mbinu zote zile kumwingia na kuufuata msafara wake bado katushtukia", Jus alisema kisha akamwambia Avi, "Oyaa mzimishe huyo usimuue tu ukifanya hivyo jua JD atajua sisi tunataka vita na yeye". Alipotoa mari hiyo aligeuza uso kwa yule adui akamweleza, "Mwambie Husa J.Stone anahitaji kuonana na JD, hatuhitaji uadui wowote naye"

Ulipotolewa ujumbe huo kwa haraka Avi alibana yule mtu hadi alipoona kaishiwa nguvu ndiyo akamwachia, wote kwa pamoja waliingia kwenye gari lao ambalo limharibika upande wa nyuma. Avi akiwa ni dereva walitokomea eneo hilo kuelekea upande wa kusini wa eneo hilo, hawakutaka wakutwe eneo hilo ambalo halikuwa mbali sana kutoka yalipo makazi ya JD.

___________________

Muda mchache baadaye vijana wengine wa JD walidhani kuwa kazi waliyoenda kuifanya wenzao imekamilika. Walikubaliana waje baada ya dakika kumi na tano tangu wagonge gari hiyo ili wasafishe na ktuoacha ushahidi, walipofika muda mwafaka waliwakuta wenzao wakiwa wamelala chini hawajiwezi na ile gari iliyolengwa haikuwepo. Walichokifanya kwa haraka ni kuwachukua kisha wakarejea hadi yalipo makao yao, walifikishwa hadi mbele ya JD na Husa ambao walipowaona tu ilijulikana wazi huo ni ujumbe ndiyo maana hawakuawa.

Walipewa huduma ya kwanza hadi walipopata nafuu, JD aliamuru waletwe hadi eneo ambalo yupo na mjomba wake wakiongea. Amri ilitimziwa na walifikishwa wakawekwa chini huku wakiwa na hali ileile, walipoinua macho walitazamana na sura ya wakubwa zao wasiyo na mzaha hata kidogo.

"Mmeachiwa mmeambiwa mtuletee ujumbe mnaweza kutupatia", JD alisema na hapo hao vijana wakaeleza kila kitu juu ya walichoachiwa.

"Huyo mtu ni nani huyu", Husa aliuliza.

"Jus kum*****e kumbe yupo nchini, aisee basi hapa nahisi kuna vifo vya madaktari vimetokea jamaa kuua kwake ni kama mchezo tu", JD alisema.

"Ni kweli na hadi sasa hivi kuna madaktari wawili wa moyo wameuawa hapa nchini"

"ni huyu aliyewapa kichapo hiki, ni muuaji hatari mno ila kuwaacha wazima hawa maana yake hana vita na mimi zaidi ya mazungumzo tu. Anko bora ulivyoweka vibaraka kule airport"

"Una uhakika hana hatari yeyote ile huyu mtu?"

"Nakuhakikishia asilimia mia moja, ila hawa vijana waache yule mtu si kiwango chao ndiyo maana wapo hivi. Ulikosea kutuma mtu wa kumdhibiti, hawafai adhabu"

"Hilo halina shaka, ila huyu mtu imekuwaje hadi akajua unafika leo?'

"Akija ndiyo tutajua yote, nafikiri namba zangu za simu anazo hadi kufikia awe anajua ratiba yangu ya leo. Tusubiri simu yake tu"

_____________________

Mapambazuko ya siku mpya yalimkuta Jamal akiwa yu usingizini kutokana na uchovu wa usiku uliyopita. Majira ya saa nne asubuhi ndipo alipoweza kuamka, alishuka kitandani akiwa na uchovu mkubwa na alielekea moja kwa moja hadi maliwatoni ambapo alisafisha meno pamoja na mwili wake ndipo akarejeana kuvaa nguo nyingine.

Kifungua kinywa nacho aliletewa humo ndani muda mrefu, aliamua kupata ndipo alipotaka nje na kutazama kule ambapo baadhi ya watu walilala kwenye mahema. Aliona baadhi ya vijumba hivyo vya nguo ngumu vikiwepo huku vingine vikikunjwa, alikaa eneo la mbele ya hotelini hapo huku akitazama mandhari nzuri ya ufukwe wa bahari ambapo jana tu ametoka kukutana na kioja cha mwaka. Alijiuta akitabasamu kila akikumbuka kile alichojionea jana, hakununa hata ingawa alikiri hapo awali ameingiwa na chuki moyoni mwake.

Majira ya saa tano akiwa mahali hapo, simu yake ya mkononi iliita. Alipotazama mpigaji aliona ni Heriety, aliipokea kwa uchangamfu na kuongea maneno machache kisha akaonekana akikubaliana naye kitu halafu akaanza kushuka kwenye ngazi za hotelini.

"Dogo unaenda wapi bila kutupa sisi taarifa, unajua upo ugenini huku", Sauti ya Paki ilisikika na kumfanya ageuke nyuma na kumtazama kisha akasema, "nashuka kule beach mwenye party kanishtua sasa hivi kuna beach party imeanza ndiyo naelekea"

"Sasa sikia dogo, inabidi tuongozane na wewe ila tutakuwa nyuma yako zaidi ya kuwepo karibu muda wote ni ugenini huku", Oze ambaye alikuwepo karibu alisema, Jamal hakuwa na hiyana na alifuatana na watu hao kuelekea huko.

Walitembea mwendo wa dakika mbili wakatokea upande mwingine wa ufukwe huu ambao ulikuwa umesheheni watu wakiwa na mavazi ya kuogelea. Madanga kwa mabanti wote waliweka sehemu kubwa ya miili yao nje eneo hili, hata kina Paki walijikuta wakipiga uruzi kuonesha wamepagawa mno kuwaona mabinti namna hiyo. Jamal aliposikia alijikuta akiwatania na hapo wakacheka wote kwa pamoja, walifika hadi katikati ya kundi la watu ambapo Paki alisimama upande mwingine tofauti na Oze huku Jamal akasogea eneo alilopo Heriety ambayo mwili wake upo kwenye vazi la kuogelea jambo ambalo lilimfanya Jamal aduwae hata pale alipokumbatiwa alitumia sekunde kadhaa ndipo akapokea kumbatio hilo kwa kumfumbatana na mikono.


*VIPI CHUKI YA GINA ITAMWACHA SALAMA?

*VIPI CHUKI YA JAMAL ATAINGIWA NA MAWAZO YA KULIPA UBAYA?







ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_______SEHEMU YA ISHIRINI__________

...............Madanga kwa mabanti wote waliweka sehemu kubwa ya miili yao nje eneo hili, hata kina Paki walijikuta wakipiga uruzi kuonesha wamepagawa mno kuwaona mabinti namna hiyo. Jamal aliposikia alijikuta akiwatania na hapo wakacheka wote kwa pamoja, walifika hadi katikati ya kundi la watu ambapo Paki alisimama upande mwingine tofauti na Oze huku Jamal akasogea eneo alilopo Heriety ambayo mwili wake upo kwenye vazi la kuogelea jambo ambalo lilimfanya Jamal aduwae hata pale alipokumbatiwa alitumia sekunde kadhaa ndipo akapokea kumbatio hilo kwa kumfumbatana na mikono.


_______________TIRIRIKA NAYO


Kuonekana kwake hata mabinti wengine walijisogeza, sura yake bado ilikuwa machoni mwao ingawa waliiona kwa mara ya kwanza usiku kwenye taa za mwanga usiyo mkali. Jamal akiwa na mwenyeji wake walienda hadi eneo lenye vitanda maalum kwa ajili ya kupumzika watu wanaoogelea wakalala hapo. Walinzi wake ambao wapo kwa ajili ya kuhakikisha hakumbwi na chochote wakawa hawachezi mbali, walijifanya ni wenye kujichanganya ila macho yote yalikuwa kwake tu.

Wengi hawakujua kma kijana huyo ni mwenye kulindwa, zaidi ya kuona watu wale ni wapo eneo hilo tu kwa ajili ya kutuliza vichwa vyao. Mandhari ya hapo haikuwa imekodiwa yote hadi isemwe kuwa mwenye kualikwa ndiyo huruhusiwa, bali ni watu kuingia kama sehemu ya kujiliwaza tu ila malipo yalifanywa na mwenye siku yake kwa ajili yao.

Muziki ulipigwa eneo la jirani na hapo, huku kukiwa na jukwaa dogo ambalo kuna mabango yenye picha ya Heriety. Kuendana na mdundo wa ala zenye mpangilio maalum. Wengi walionekana wakicheza kwa furaha huku wakiwa na mavazi hayo, wengine walijiachia kwenye maji huku wakisherekea kwa furaha. Hakika ni shughuli iliyoandaliwa kiaina yake.

Ujio wa Jamal eneo hilo ulimfanya mwenye shughuli kuketi chini na kuzungumza naye, mabinti wengine waliungana naye jambo ambalo Heriety hakulipenda ila hakuwa na jinsi zaidi ya kukubaliana na hali halisi. Hakuzoea ukorofi wala kisirani labda mahali inapobidi, hivyo hakutaka kujiwekea sifa mbaya kwenye siku yake muhimu.

______________

Yakijiri hayo upande wa majini, Gina alikuwa amesimama kwenye eneo ambalo maji yalimfika shingoni akiwa anatazama kule ambapo Jamal yupo. Alishamwona tangu anaingia hadi anafika pale na kuzungukwa na warembo wengi. Siku hii aliianza kwa furaha kubwa na ujio wa mbaya wake mahali hapo, kulimfanya ahisi bashasha imetumbukia nyongo.
Alikereka haswa na kutamani hata awe ni mwenye shughuli ili aweze kuchukua uamuzi wowote ule. Ila haikuwezekana hilo suala, tena rafiki yake ndiyo anamhusudu kupitiliza. Angeanzia wapi hadharani kufanya mambo kama hayo si ingekuwa mwanzo wa kujipalia makaa. Bashasha la kule ufukweni lilipozidi, aliamua kutoa mlio mithili ya mtu mwenye kubusu na wanaume wanne walisogea jirani naye ambao walionesha ni wahuni kupitiliza.

"Mnakumbuka makubaliano ya jana?", Aliwauliza.

"Tutasahau vipi wakati suala lenye mchongo wa pesa", Mmojawapo alisema.

"Mtu wenu ni yule aliyezungukwa na watu wengi, hakikisheni mnamtia adabu tu kila kitu tutamalizana"

"Kumbe yule ni kazi ndogo hii, ngoja twende sasa hivi hakuna wa kututisha Bagamoyo hii ilimradi tutimize mishe yetu"

"No! Siyo hapa nyinyi, yule ana walinzi nahisi na pia watu wanaona mmeongea na mimi huoni mtaniweka mimi pabaya"

"Ok, ngoja tutoke tukamchora jinsi alivyo halafu tutarejea hapa kukwambia"

Vijana hao walipoanza kutoka nje ya maji, baadhi ya mabinti ambao walikuja hapo si sherehe hiyo walipowaona tu waliwapisha wakiwa na hofu kuu. Hii ilionesha ni namna gani hawa watu si wageni eneo hilo, labada kwa hawa wakazi wa nje ya mji ndiyo hawakuweza kuwafahamu.
Watu hawa walikutana na Gina kutokana na msaaada wa kijana mmoja mwenye kusoma shule ya Tambaza. Huyo naye hakuwa akimpenda Jamal, na mwenye kumpenda mno Heriety ila hakuwahi kufua dafu hata alipojaribu kuchombeza. Kitendo cha kumwona naye siku nzima kwenye shughuli ile alihisi binti yule amemwalika makusudi aje kumuumiza. Kumbe alichukuliwa ni kama rafiki ingawa hakupewa bahati ya kuwa fuadi wa bibie, huyo ndiye alihadaiwa na Gina tena kibaya zaidi ni mwenyeji wa huko Bagamoyo. Huyu ndiye alifanya mpango na wahuni wale hadi wakaonana na Gina, ili waje kumfanyia kitu kibaya Jamal.

Wahuni hawa walianza kusogelea kwenye vitanda vile ambavyo kina Jamal wapo, hawakuwa wakijua tayari eneo hilo kina Oze wapo. Walipokarbia tu walimwona mtu mwenye bukta iliyofika ugokoni, juu akiwa na fulana ambalo lilifunikwa na shati kwa upana kwa asilimi kubwa. Huyu aliwakalia mbele yao, na hakuwa mwingine ila ni Oze mwenyewe, wakiwa hawajachukua uamuzi wowote Paki naye aliongezeka akiwa na suti ya mikono mifupi kama ilivyo kawaida yake. Waliziba njia ya wahuni hawa, na kupelekea watazamwe kwa macho ya chuki.
"Usalama wenu ni kurejea kule mlipotoka kwa yule malaya aliyewatuma. Nafikiri mnanijua mimi ni nani na ninafanya kazi kwa nani, sasa epusheni usalama wenu kuingia hatarini", Oze alisema.

"Oze tunakupata vyema, ila seme nini na sisi tupo kwenye mishe yetu. Tupisheni tukasome ramani ipo vipi?", Mmoja wa wale watukutu alisema.

"Ninachowaambia ni hivi, huyo mnayetaka kumfuata ndiyo tupo hapa kumlinda si yule dogo mwenye nguo nyeupe pale", Paki alisema huku mkono wake ukiwa umeshika kiunoni.

"Sikia huu ni msala ambao haufai hata kidogo mnauingilia, aliyetupa hii kazi ni bosi wetu nafikiri mnamjua vyema nyinyi. Msijiingize kwenye msala msiyoweza kuutuliza kisa chuki za yule mtoto, yaani toka mnachonga mpango kwenye maji sisi tunawachora tu mnafikiri mishe hizo hatujapitia sisi kabla ya kufika huku", Oze alisema.

Watukutu wale waligeuza wenyewe na kuanza kurejea kule walipotoka, huku akiwa wamejua ni wanacheza na moto mkubwa kiasi gani. Walishukuru kwa kukuta ahueni kabla ya kuingia kwenye ligi yenyewe, walifika hadi kwenye maji na kuanza kuogelea hadi upande aliyopo Gina. Ambaye hakuwa na habari na kile kilichokuwa kikiendelea, kwani walizuiwa eneo ambalo kulikuwa na watu wengi hakuona chochote.

"Sikia we dogo, kazi uliyotupa hatuwezi kukufanyia hata kama utatupa milioni mia. Maisha yetu ni muhimu", Mmojawapo aliongea.

"Mbona siwaelewi jamani, kuna nini mlichokiona huko?", Gina aliposema hivyo mmojawapo aligeuka na kumwonesha upande aliyopo Paki, na sehemu aliyosimama Oze huku akimwambia, "Unawaona wale wahuni, ndiyo wanalinda huyu kama uliwahi kuwaona kabla basi tambua ni wale watu ni zaidi ya majambazi na sisi ni wahuni tu wa mitaani. Aliyewatuma kumlinda yule dogo ambaye anapendwa na kila mtu basi tambua ni tishio kwa wahuni hata majmbazi, hatuwezi kuweka maisha yetu hatarini".

"He! Yamekuwa hayo, na nyinyi mnawaogopa wale?"

"Sikia wewe sisi tumeliona jua kabla yako, tunajua kila kitu juu ya magenge ya wahuni. Zile namba ni nyingine kabisa yaani ukiwaona wale kwa pamoja jua kuna range tatu zimekuja nao nazo zina wahuni kupitiliza"

"Ok nimewaelewa ila nashindwa kuelewa yule ni nani haswa hadi alindwe vile wakati tunamjua anatoka maisha duni mno", Gina alihitaji kujua kila kitu kuhusu Jamal.

"Yule dogo nahisi tu bosi wao kampenda maana anaonekana ni mwenye nyota ya kupendwa mno, sasa kutoka kuja huenda kapewa ulinzi tu maana sijawahi kuiona sura yake kwenye himaya yao niseme ni mtoto wa yule Mzee"

"Ok nimewaelewa"

____________

_____Tanga____

Majira haya ya asubuhi ikikimbilia mchana, msafara wa magari ulionekana ukiingia eneo ambalo ni uswahili tena ukidhihirisha umebeba matajiri haswa. Watoto wa mtaani walibaki njiani wakiushangaa kwani haikuwa kawaida kuweza kufika kwa magari ya watu wenye nazo tena mengi.

Wengi walidhani kuna kiongozi anafika hapo lakini kwa wenye uelewa na magari ya serikali walipingana na hayo, haswa baada ya kuona vibao vya namba za usajili zenye majina na si namba za serikali au usajili maalum kwa gari. Magari hayo yalitembea kwa kasi kubwa mno hadi yakafika eneo ambalo kuna nyumba kubwa ya matofali ikiwa imeezekwa kwa makuti juu ambayo ilijengwa na vyumba vya nje kadhaa.

Hapo yaliweka kituo na yakasimama pembeni ya njia kwa pamoja, watu wenye fulana nyueusi pamoja na suruali aina ya jeansi huku chini wakiwa na viatu vizito. Walishuka kwa haraka na wakajipanga mstari, muda huohuo mlango wa gari mojawapo ulifunguliwa na hao wenye kuonekana wazi ni Wapambe.

Mguu mrefu ulitangulia kutokeza kisha mwye umiliki wake akaonekana akiwa na miwani nyeusi mwake, JD ndiyo alidhihirika hapo akiwa na miwani ya jua usoni mwake. Nyuma yake alifuata Husa ambaye alimwongoza huku wakifuatana na baadhi ya walinzi. Walifika mlango wa mbele wa nyumba hiyo ambapo walikutana na mzee mmoja akiwa ameketi kwenye kiti, JD alipomwona alimsogelea kiutiiifu kisha akampatia mkono akionekana ni mwenye unyenyekevu mkubwa mno kwake.

"Jamshid", Mzee huyo aliita huku akiinuka kwa tabu huku akionekana kutoamini.

"Baba, shikamoo", JD aliitikia

"Marhabaa! Yaani umekaa miaka kumi nje ya nchi hadi binti yangu kakata tamaa kabisa ya kurejea kwako ndiyo maana kaja kijijini kuliko kutumia mali zako"

"Nilitoa ahadi ningerejea na nimeitimiza, yuko wapi huyo Mwanahawa na pia nahitaji nionane na Kimweri"

"Baba pita tu ndani kwake ni palepale alipokuwa akilala, utamkuta"

JD hakutia neno lolote, aliwaamuru aliyofika nao wasubiri hapo nje huku Husa akikaribia jamvini na kuongea na mzee mwenyeji.

Aliingia kwenye ukumbi usiyo na sakafu na moja kwa moja akafka kwenye chumba chenye mlango kuukuu. Aligonga mara moja na kusubiri afunguliwe,kulipopita ukimya aligongwa kwa mara mbili mfululizo kisha akasubiri. Mlango ulifunguliwa na alijitokeza mwanamke mtu mzima ambaye alionesha kutopata matunzo, ila bado urembo haujamtupa.

JD alipomwona alijikuta akishtuka na hata mwanamama naye hali hiyo ilimkumba, akiwa anamshangaa mnyange yule wa zamani kwa haraka alijaribu kufunga kufunga mlango huku uso wake ukionesha kuchukia. JD aliwahi kwa kuweka mkono kisha akaweka kitatu chake cha thamani ili ashindwe kufunga, alikutana na nguvu ya mwanamke mwenye kutotaka kushindwa dhidi ya nguvu zake zilizozuia tendo hilo.
"Mwanahawa si unisikilize kwanza ndo mambo gani hayo jamani, si nilikwambia ninaenda kusoma na ikabidi nifanye kazi huko kwa muda ndiyo nirejee nchini", JD alisema.

"Jamshid unawez kunidanganya mmi na unaendelea kunidanganya", Mwanahawa alisema kijaribu kuzuia kwa nguvu ila alizidiwa na JD akamsukuma kwa ndani halafu akaingia na kuufunga mlango.

"Jamshid toka sihitaji kukuona kabisa, umeniweka umri wote hadi sasa sijaolewa kwa ajili yako tu"

"Sasa ningefanyaje jamani wakati kazi ni muhimu, sikuruhusiwa kurudi ningeanzia wapi kutoroka wakati nilikula kiapo kwa marehemu baba niitimize hiyo"

"Mwongo wewe, unafikiri sijui kinachoendelea JD hadi uniambie hivyo. Unajua wazi baba yako ni nani na wewe umekuwa nani, ndiyo maana sikuhitaji chochote kutoka kwako nikaja kuishi huku kuliko kuishi kwenye mali za mtu wa aina hiyo na hata kutambulika nimezaa na mtu wa aina yako"

"Siyo hivyo nisikilize basi"

"Hapana! Hapana! Uliniambia ni miaka minne tu unarejea na sasa ni miaka kumi ndiyo unarudi Jamshid kweli, hujui hata mwanao anafanana vipi hujui ana hali ganmi na ulijua tunahangaika naye kwa tatizo lipi. Baba wa aina gani wewe, bora hata nilivyofanya kuliko aendelee kujitukuza kuwa ana mzazi kama wewe. Mwenye magenge ya uhalifu, hapana kwa kweli siwezi kukusikiliza, ahadi uliyonipa unafikiri nitaanzaje kukutilia maanani ilihali hukuitimiza"

"Hujui ni mangapi yamenikuta mimi hadi nikafikia kutoonekana kwa miaka hiyo, nikamwacha mwanangu"

"(huku akikitwaa kisu) Jamshid ondoka tafadhali, unajua kabisa nikishika hivi kinachofuata ni nini. Sioni hasara kabisa"

"No! No! Usifikie huko ngoja nitoke nje", JD hakuwa na neno, pamoja na kumiliki kundi kubwa la watu wenye roho za paka, bado kwa mwanamke huyu alikuwa ni mwenye kujishusha. Kitendo cha kushika kisu yule bibie, alielewa vyema kinachofuata ni kipi, aliamua kutoka nje mwenyewe huku akiwa maumivu moyoni mwake kwa kushindwa kuweka mambo sawa.

____________


Majira ya mchana waalikwa wote walipata chakula cha mchana kwenye shsrehe hiyo ya ufukweni, bado muda wa kuendelea kuwa pamoja ulikuwepo kwani siku yenye kukumbukwa kuzaliwa kwa mwenzao haikuwa imeisha Walikula kwa pamoja huku wakifurahi, walipomaliza kula kwa pamoja Heriety aliwatangazia watu juu ya kinahofuata ambacho wengi walikishangilia.

Siku hiyo walitakiwa kuimaliza kwa pamoja kwenye hifadhi ya taifa iliyopo mpakani kwa Bagamoyo na Tanga, yaani Saadani mbuga iliyopo jirani na bahari ya Hindi. Wote walipewa muda wa kujiandaa na magari mawili ya abiria yakawa yamewasili mahali hapo kuwachukua wote, muda mchache baadaye walipakiwa kwenye gari huku Jamal akitumia usafiri aliyokuja nao tena akimwomba Heriety wapande naye. Binti huyo hakufanya ajizi, alikubalia ombi hilo na safari ikaanza huku msafara wa range rover ukiwa mbele.

Gari alilopo Jamal liliwekwa kati na walinzi wakawa mbele na nyma, magari hayo yaliongozana kwa kasi kubwa huku yakimaliza kilomita kuweza kuwasilia Saadani. Wakiwa ndani ya gari hilo walipiga domo kupoteza muda huku, kwani safari haikuwa fupi. Heriety ilikuwa ni mara yake ya kwanza kufika huko akawa ni mwenye kushangaa mno hadi wanakaribia kufika eneo stahiki baada ya kuanza kulikaribia daraja la wami kwa upande huo ambalo lilifanya binti huyo aanze kuingiwa na uoga.

Hakuwahi kuona daraja lenye mbao katikati na hiyo ndiyo ikawa ni mara ya kwanza, hakika lilimtia hofu mno akajikuta akimganda Jamal mwilini huku akificha uso wake kuhofia kuvuka hapo.
"Jamal tutapita kweli hapa juu ya mbao huoni ni hatari, nimesikia huu mto una mamba", Alisema kwa uoga.


*SHEREHE INAHAMIA SAADAN, KIPI KITAKACHOJIRI?

*JD AMEJIKUTA AKISHINDWA KUWEKA MAMBO SAWA, JE ATACHUKUA HATUA GANI?






ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA_______


Hakuwahi kuona daraja lenye mbao katikati na hiyo ndiyo ikawa ni mara ya kwanza, hakika lilimtia hofu mno akajikuta akimganda Jamal mwilini huku akificha uso wake kuhofia kuvuka hapo.

"Jamal tutapita kweli hapa juu ya mbao huoni ni hatari, nimesikia huu mto una mamba", Alisema kwa uoga.


____________TIRIRIKA NAYO

"Relax dogo, hapa yanapita mgari madogo karibu ya kila aina hata yale ya kubeba mizigo midogo", Paki alisema huku akimtazama Heriety aliyeingiwa na uoga baada ya kuona daraja wanaloelekea kulivuka.

"Sasa wewe unavyona tungekuwa hatupiti tungeleta gari huku?", Jamal naye akauliza kimasihara.

Binti akiwa na hofu alishuhudia gari likipita eneo hilo, hadi linamalizika hawakupatwa na tatizo lilote. Hapo ndiyo akajua ni daraja imara tofauti na vile linavyoonekana. Hofu yake juu ya mto wami ambao hupita hapo kuelekea baharini kumwaga maji yake. Ilimwisha na kuona ni daraja madhubuti kama yalivyo mengine. Uoga wa sehemu hii hakuwa kwake tu, bali hata kwa wenzake waliyokuwa wapo kwenye gari la abiria wakielekea kuvuka hapo. Nao waliingiwa na hofu mno, ila ujasiri uliwafika baada ya kuona wanapita bila wasiwasi wowote ule.

Bada ya kitambo msafara wote uliwasili hifadhi ya taifa ambapo walipokewa na ugeni ambao hawakutaraji kuukuta mahala hapo. Upande walipoegesha magari yao, walimwona mzee wa makamo akiwa amesimama na mwanamke ambaye alilandana kila kitu na Heriety. Watu hao mwenye siku yake aliposhuka garini walimkumbatia kwa shangwe, kisha wakakaribisha wengine waliyofika hapo ili kumfanya mwenzao asiwe na huzuni siku hii kubwa.

Wenyeji wa hapo hawakuwa watu wengine ila Job Kabari na Angeline Kabari, wanandoa wa siku nyingi na moja ya watu wenye uwezo mkubwa wa kifedha nchini Tanzania. Hawa ni wafanyabiashara wakubwa mno nchini ambao ni nadra sana kuonekana sura zao, ila majina yao yalijulikana wazi kutokana na miradi mikubwa waliyokuwa nayo. Wengi hawakuwahi kuwaona ana kwa ana ila nyuso zao walizishuhudia mara kadhaa kwenye vyombo vya habari, hawa nao hawakujua kwanini walikuwepo mahala hapo.

Ila ukweli ambao ulijulikana na wachache miongoni mwa hao, ni kwamba hawa ndiyo wazazi wa Heriety. Ambaye alijulikana ni mwenye maisha ya kujiweza ila hakuwahi kuwaeleza kuwa yeye ni mtoto wa nani. Kuwaona mahala hapo, walikuja kumaizi hadi pale walipotambulishwa na binti mwenyewe na kisha utambulisho dhidi yao ukafuatia kwa mara nyingine. Hapo ndipo wengi wao wakajua kuwa wanasoma na mtoto wa mwenye nazo shuleni, walibaki mdomo wazi haswa hata Gina ambaye ni rafiki mkubwa hakuwa akijua hilo. Alielezwa kijuujuu juu ya wazazi wa mwenzie, alishangaa mno.

Kutoondoka kwa pamoja siku ile ya kufungwa shule kisa kukwaruzana kwao, ndiyo ikawa chanzo cha yeye kutojua hayo, laiti kama asingelikwazana naye. Basi angewefahamu mapema, ila ndiyo hivyo wasaa huo aliukosa hadi kuja kufikia siku hiyo.
__________________

Upande wa Alice, shule kwake ilikuwa ni mithili ya nyama iliyopasukiwa nyongo kinywani mwa mlaji. Alijikuta akiwa ni mpweke na hata wasichana wengine wa shule hiyo waliyojitahidi walau kuzoeana naye, ilikuwa ni ngumu kwake. Tangu afike hapo ni juma moja, siku zote amekuwa ni mtu wa kujitenga mno na si kujichanganya na wengine.

Shule hii ambayo ni mwaka wa pili kwa kipindi hiko tangu kuanza kuwa mchanganyiko, alijikuta akijiona yu ndani ya kifungo kwenye gereza lenye mateso makubwa. Jamal hamwoni, tabasamu lake halioni, habibu wa moyo wake yu mbali. Kwake ni zaidi hata ya kupigwa mijeledi, ilimuumiza mno na hata akafikia hatua ya kumlaani dada yake kwa hicho alimchomfanyia. Laiti angelijua ukweli, angemshukuru mno Doreen kwa kuamua kufanya hivyo. Lakini ndiyo hivyo, usilolijua ni sawa na usiku wa giza.

Wasichana tofauti na hata wavulana, walimfuata na kujaribu walau kuongea naye mawili matatu ila hakuwa mwongeaji zaidi ya kusikiliza tu. Mara nyingi alijionesha ni namna gani mwenye huzuni na hata kufikia hatua ya kutaka kukaa peke yake, aliweka wazi baadhi ya nyakati hajisikii kukaa na mtu zaidi ya kuwa mwenyewe.

Juma moja tu shuleni tayari alishaanza kujulikana kutokana na tabia yake hiyo, wengi walimwona ni mwenye majivuno na wachache walimfikiria ni mwenye huzni ndiyo maana akawa namna hiyo. Ila ukweli wa yote aliujua yeye mwenyewe, huku wachache washikao mpini wakijua tu kuhusu sumu waliyolishwa na Doreen.

_______________

Jijini Dar es salaam, siku hii ya mapumziko sehemu nyingi ni tulivu kutokana na kutokuwepo kwa pilika nyingi. Wengine walitumia siku hii kwa ajili ya kwenda kumuabudu Mungu, wengine walijipumzisha majumbani mwao. Katikati ya jiji kulibaki ni kutulivu haswa maeneo ya Posta ambayo hujulikana kwa kuwepo ofisi za makampuni mengi ambayo hutumia kama ni makao makuu yake. Magari kadhaa yalipita hata daladala za jijini siku hii hazikuonekana kujaza kupitiliza, misururu ya magari ndiyo haikuwepo kabisa kutokana na upungufu wa magari binafsi siku hiyo.

Pamoja na upweke wa siku hiyo, upande wa eneo ambalo hutumiwa kwa wasafiri wa kwenda visiwani. Upande wa kulia mwa Posta ya zamani, magari ya kifahari yalionekana yakiingia kwenye lango la magari eneo la bandari hiyo ndogo. Wapambe wengi walidhihirika baada ya kuingia msafara huo, jinsi uzito wa ujio ulivyo ingeweza kudhaniwa ni mtu mzito ameingia hapo. Ila namba za magari yale, ilitambulisha wazi aliyefika mahala hapo alikuwa ni nani hadi kufikia kuwekwe ulinzi mkali.

Upande wa ndani eneo la maegesho hapo bandarini, boti ndogo ya kisasa ilionekana ikiwa imeweka nanga. Kushoto mwake nchi kavu, kulionekana gari aina ya toyota landcruiser nyeusi na kulia kwake kulionekana gari ya range rover nyeusi zote zikiwa zimekaa sanjari. Magari yaliyopo mengi mlango ulifunguliwa wa mojawapo la katikati, JD akaonekana akishuka huku akiwa amevaa shati jeupe na suruali nyeupe hadi kiatu kilikuwa rangi hiyohiyo. Motokaa iliyopo pekee napo, milango miwili ilifunguliwa, akaonekana Jus na Avi wakiwa pamoja.

Hawa walijongea kwa taratibu kuelekea alipo JD, walipokaribia wote kwa pamoja walipekuliwa ndiyo wakaruhusiwa kumsogelea kibosile yule ambaye nyuma yake yupo Husa akiwa na mavazi sare naye. JD na Jus waligonganisha mikono yao kwa ishara ya kusalimiana kihuni kisha wakakumbatiana, Avi naye alisalimiana namna hiyohiyo naye.

"Iam so sorry kwa kilichokupata Jus", JD alisema.

"Its ok limepita, nafikiri ningefuata ushauri wako nadhani ningekuwa naishi kiamani hadi hivi sasa", Jus alisema.

"Napaswa nikulaumu sana kwa hilo ila unaonekana wazi bado upo imara, nikupongeze kwa hilo. Fernando si mtu mzuri hata, nililitambua hilo mapema mno ndiyo maana nikakupa ushauri ule. Mimi kilichoniweka muda mrefu ni asili yangu tu, hakuwa na mapenzi na mtu mweusi, shida yake ni kuwatumia tu kisha awaache"

"Ni kweli uyasemayo, (Jus alimwangalia Avi huku akiongea) nadhani unamkumbuka huyu naye hakuona umuhimu wa kubaki pale baada ya kusikia wahindi wenzake wameuawa kisa kufeli kazi. Ndiyo maana kakimbilia huku baada ya kuona anasakwa sana"

"Namkumbuka vyema huyu, moja wa madereva hatari kuwahi kutokea kuwa chini ya Fernando. Mwenye kujua kuchezea usukani wa gari haswa, pia ni mmoja wa mtu hatari katika mapigano. Ila Jus kwanini umegeuza kibao kwa watu wasiyo na hatia, ubaya ulifanyiwa kule ukumbuke"

"Kwa nilichofanyiwa wacha niamue vile, hili ni donda ndugu lipo moyoni mwangu na dawa yake ilishazikwa nitapona vipi"

"Unaweza kunieleza kiundani zaidi"

"Nafikiri tuchukue uelekeo wa eneo la kuzungumza nitakupa maelezo yote kiupana"

"Ok tuingie ndani ya boti"

___________

Majira haya wanafunzi pamoja na watu wengine waliyofika kuhudhuria sherehe ya Heriety, waliutumia muda huo wakitalii maeneo mbalimbali ya hifadhi hiyo wakiwa wapo kwenye gari maalum. Walijionea wanyama mbalimbali huku wakichukua picha za kumbukumbu, walipita kila mahali na hatimaye wakafika kwenye eneo ambalo ni jirani mno na mto Wami.

Kutokana na uwepo wa Mamba wengi na Viboko, ilibidi wasisogee jirani na mto huo zaidi ya kupiga picha kwa mbali kwa kujionea wanyama hao. Wengi walifurahia mno kwa kujionea viumbe ambao hawakuwahi kuwatia machoni, pamoja na kuiona delta ya mto Wami. Furaha ya kutaka kuburudika ilipelekea wachache kati yao kutaka kuingia kwenye boti iliyopo jirani na hapo ili wapite sehemu kadhaa wajioneee vizuri.

Hamu hiyo ilianza na mtu mmoja ambaye alitoa raia kwa wenzake, kisha ikafuata kwa wengine ambao waliliridhia kwa mikono miwili. Hapo ndipo ikabidi boti kadhaa ziletwe ili wote waweze kutosheleza. Safari ikaanza huku kina Jamal, Heriety, Gina pamoja na marafiki kadhaa wakiwa wamekaa kwenye chombo kimoja.

Wengi walichukua wasaa wa kupiga picha mikoko ambayo ilikuwa ikionekana upande wa Delta hiyo. Furaha ilitawala upande wa kila mmoja, hata Gina naye alionesha ni jinsi gani mwenye kufurahishwa. Aliweka tabasamu muda mwingi huku akiwa yupo upande wa kushoto wa Jamal na kulia kwake kukiwa na kijana yule ambaye alisuka mpango hadi wakapatikana wahuni wa kuja kumvamia Jamal.

Jamal upande wa kulia kwake ndani ya boti hiyo, aliketi Heriety ambaye ndiye aliyekuwa akiongea naye kwa muda mwingi huku wakitazama kando kushangaa upana wa mto huo unaoelekea baharni. Hatimaye mambo yakawanogea, wakasimama huku wakiwa wameshikilia chuma wasiangukie kwenye maji, waliendelea kupiga picha tena majira hayo wala hakuna aliyekuwa akihofia uwepo wa Ngwena eneo hilo la kina kirefu. Mambo yaliponoga zaidi Heriety alichukua kamera na kumrekodi Jamal, ambaye alikuwa akiongea kwa furaha huku akishangilia.

Wengi walicheka mno alipoanza kutamka maneno hayo, huku akiegemea chuma, alijiona yupo huru zaidi kwa kufanya hivyo na kupelekea hata wengine nao waanze kumrekodi vilevile. Yakijiri hayo, Gina na mtu wake walikuwa wakicheka na kutaniana kwa furaha huku wakiwa hawajali vituko vya Jamal. Hawakueleweka walikuwa wakiongea nini maana walikuwa wakiumana sikio huku kila mmoja akicheka, waliendelea na mtindo huohuo huku wakianza kitu kipya katika utani wao.

Walitekenyana huku wakicheka, mtindo huo aliaunza Gina mara kadhaa kwa kijana yule ila hakuweza kumfanya ashtuke. Muda ambao Jamal yupo katikati ya vituko vyake, binti alitekenywa kwa ghafla. Hapo alijikuta akimtamka, "Mamaa!". Kisha akashtuka hadi akamsukuma Jamal ambaye wala hakuwa na hili wala lile, kijana wa watu akaangukia mtoni kwa ghafla na kupelekea mayowe yaanze kutoka kwa mabinti kwa tukio hilo. Hata Gina mwenyewe alionesha kushtushwa na hilo, akaweka mikono kichwani huku akionekana kuanza kuchanganyikiwa.

___________________


JD, Husa, Jus na Avi kwa pamoja waliingia kwenye boti ya kifahari na wakafikia eneo la juu ya chombo hicho ambapo kuna viti vinne vilivyozunguka meza moja. Hapo ndipo walipoweka kituo muda ambao chombo hicho kiling'oa nanga na kuanza kuondoka bandarini hapo. Kila mmoja majira hayo alikuwa ameshika kinywaji, huku wakibarizi kwenye upepo wa bahari kipindi kichache baadaye hawakuona umuhimu wake baada ya kufika kwenye soko la samaki la Feri. Ilibidi Nahodha wa chombo hicho akiondoe kwa kasi eneo hilo, hadi wakafika mbali ndipo wakawa hawapatia harufu ya shombo ya eneo lile.

"Jus unaweza kusimulia kile kilichokukuta hadi ukafikia kuanza hayo", JD alisema.

"Bila shaka"

"Basi tupe habari, ila nimesahau kukupongeza kwa kuwapa kifinyo watu wangu hadi wakawa hawajiwezi", Husa alisema na kupelekea wengine wacheke.

Jus alianza kusimulia, "safari yangu ya kimaisha ilianza kuwa mbaya zaidi pale nilipofiwa na wazazi wangu wawili. Nikabaki nikiwa na ndugu yangu wa pekee tu Leo. Huyu naye hakuwa ni mwenye kuweza kujitegemea ikabidi nimpiganie yeye, nilianza kuishi kwa kuuza chupa za plastiki kwetu Haiti hadi nikaweza kumaliza elimu nikitegemea hayo tu kunisomesha. Muda niliyohitimu Leo alishaanza kujiweza naye, akawa anasoma kwa kutegemea kazi ileile. Milo yetu hakuwa yenye kuridhisha ilifika kipindi tukawa tunakosa mlo mmoja tu ilimradi tupate walau pesa ya kusoma. Pamoja na hayo Mungu hakunitupa, alikuwa upande wangu nilikacha kuendelea na chuo kwa kukosa pesa zaidi nikaamua kujitupa jeshini. Huko ndipo kuliponibadilisha hadi mkanijua nyinyi kama Jus the fire, niliingia kikosi ukomandoo nikapata mafunzo yote ya hatari na baadaye nikaja kuwa mmoja wa wanajeshi hatari na wa kuaminika ndani ya kikosi cha jeshi la Haiti.
Muda huo unafika napenda nikiri sikuwahi kuwa mzalendo ndani ya jeshi, nilikuwa naitafuta pesa haswa na tamaa juu ya yake iliniendesha haikuniacha. Nilifanya kazi kama mwanajeshi na pale ilipotokea pesa ya kuhitaji kuipata mtaani, basi nipo tayari nisaliti kiapo changu na kuweza kuipata. Mwenendo huu ndiyo ukawa mwanzo wa kukutana na Fernando, tajiri kutoka nchini Argentina ambaye ni kinara wa mtandao wa madawa nchini mule na pia mfanyabiashara mkubwa mno. Hapo ndipo wengi wetu tulijuana mule, nikawa sasa nina pesa mno kupitia kwake, nilifanya mauaji na pia kuhusika uharamia mkubwa nikijulikana kwa jina la Black ninja hakuna aliyewahi kufikiri kama yote yale yanafanywa na mwanajeshi wa kuaminika.

Mjuavyo dunia haina siri, siku moja mwanajeshi mwenzangu wa kikosi cha siri alikuja kukuta mavazi yangu ya kazi haramu nyumbani kwangu. Huyu nilijaribu kupambana naye ili siri isigundulike ila alinitoroka na kuja kutoa siri. Huo ndiyo ukawa mwanzo wa mimi kuishi maisha ya kuhamahama na hatimaye nikaamua kuhamia nchini Argentina kukwepa mkono wa sheria. Huko ndipo nilikuja kukutana na wewe JD pamoja na wewe Avi , na pia huko ndiyo nilipokuja kujuana na Juliana. Binti mwenye asili ya kimeksiko, anayesoma uchumi kwenye chuo kikuu.

Nilifanya kazi za kila aina na nikawa na maisha mazuri mno, niliendelea kuishi kiamani huku nikitumia namba tofauti kuwasiliana na mdogo wangu ambaye naye mawasiliano yalizorota. Kila nilipokuwa nikimpigia basi ni kunipa shutuma, huku akiwa amesahau kazi zangu ndiyo zimemsomesha hadi akafika kupata ajira. Niliachana naye na kuangalia maisha yangu.......


*KUTEKENYWA KWA GINA, KUNAPELEKEA MAAFA. ITAKUWAJE? NANI ATAMWELEWA?

*JAMAL ATUMBUKIA MTO WAMI JIRANI NA DELTA YAKE, JE ATATOKA SALAMA? ILIHALI KUNA VIBOKO NA HATA MAMBA HAWAPO MBALI KUTOKA HAPO ALIPOINGIA


*JUS ANA YAPI YA KUWAELEZA?







ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



____________SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI______

Nilifanya kazi za kila aina na nikawa na maisha mazuri mno, niliendelea kuishi kiamani huku nikitumia namba tofauti kuwasiliana na mdogo wangu ambaye naye mawasiliano yalizorota. Kila nilipokuwa nikimpigia basi ni kunipa shutuma, huku akiwa amesahau kazi zangu ndiyo zimemsomesha hadi akafika kupata ajira. Niliachana naye na kuangalia maisha yangu.......




______________TIRIRIKA NAYO
Ila iliniuuma mno kuweza kugeukwa na ndugu yangu kisa hiko, yaani alisahau kabisa wote tulikuwa ni watumwa wa pesa na ndiyo imepelekea hadi tukafikia huko"

"Sasa hadi hapo tumejua ni jinsi gani ulivyoweza kuingia kwenye kundi la Fernando, tueleze mengine yote", Husa alisema.

+++++++

__Miaka kumi nyuma___

_Buenos Aires, Argentina_

Gari ndogo ya kimichezo ambayo iliongozana na msururu wa pikipiki mbele na nyuma, ilipita kwa kasi kwenye barabara ya Av Brasil huku baadhi ya magari yakiwa kando baada ya kuiona ikikaribia. Ilienda moja kwa moja hadi ilipofika kwenye barabara Gral.Hamos hapo ilinyoosha ikafika njia kuu ya Au 9 de Julio, iliingia upande wa kushoto kuelekea zilipo njia za juu zinazounganisha barabara hiyo na Au 25 de Mayo.

Ulivuka makutano hayo na kuendelea na safari yake hadi ulipofika jirani na Mgahawa wa Mc Donald's. Hapo gari hilo liliegeshwa kisha akashuka kijana mwenye shuti nyeusi akiwa na kofia aina ya Pama kichwani mwake, huyu ni mwenye asili ya barani Afrika tofauti na wenyeji wa mji huo ambao wengi wao ni walatino wa kimrekani pamoja na wahindi wekundu.

Bwana huyu pamoja na kuonekana ni mwenye nazo, ilitarajiwa labda angeweza kushuka na ulinzi mkubwa lakini aliteremka mwenyewe na aliingia ndani akiwa pekee huku mkononi akiwa na mkoba wa namba. Ndani ya magahawa kulikuwa na watu tofauti majira hayo kila mmoja akiweka tumbo lake sawa, ujio wake hakuna aliyemtilia maanani miongoni mwa ngozi nyeupe nyingi.

Akiwa na mkoba wake aliangaza pande kadhaa humo ndani, hatimaye macho yakatua kwa Mhindi mwekundu aliyekaa pekee akiwa na suti nyeupe na mikufu kadhaa ya dhahabu shingoni mwake. Alimtazama machoni mhindi huyo na kupelekea macho yagongane, kukutana kwa nyuso zao alipewa ishara ambayo ilimfanya aachie bashasha na kisha akajongea hadi kwenye meza ambayo kuna mtu huyo.
"Vizuri kwa kuchunga wakati Stone", Aliambiwa.

"Daima wakati ndiyo kila kitu, napaswa niuchunge", Alisema huku akiketi kitini na Mhudumu alimjia muda huohuo, aliombwa kuagiza anachokiendelea naye akatii.

"Nadhani ni muda wa kufanya makubaliano yetu, mzigo unao?"

"Mzigo ni huu hapa mkononi mwangu, vipi bakshishi ipo?"

"(Akiweka mkoba mezani) Nadhani kila mmoja amekuja na kile kinachohitajika"

"Sheria namba moja, fungua mkoba niuone na mimi nitafungua wa kwangu chini ya miguu uuone"

"Sawa kama upendavyo"

Mhindi yule alifungua mkoba kwake kinamna ya usiri, Stone alijionea dola za kimarekani zikiwa zimepangwa kwa ustadi mkubwa. Alizipitisha macho yake kwa haraka, kisha akatia mkono ndani ya mkoba na kuzishika. Alijiridhisha mwenyewe hazikuwa batili na noti halisi, naye kwa haraka alifungua mzigo aliyokuja nao.

Mhindi alishuhudia dawa za kkulevya zikiwa zimepangwa kinamna ya upekee, naye alizigusa kisha akatingisha kichwa kuridhia. Kilichofuata hapo ilikuwa ni kubadilishana tu mizigo, Stone alichukua mkoba wa fedha na akauacha wa kwake pale chini. Kinywaji alichokiagiza majira hayo kilishafika na alikinywa kidogo tu, kufikiwa kwa makubaliano hakuona umuhimu wa kuendelea nacho zaidi ya kuinuka hapo kitini na kuondoka.

Hatimaye alifika garini na kuingia upesi, pembeni yake kwenye usukani alionekana Mhindi wa bara hindi akiwa ameshika usukani. Alifunga mkanda wa haraka kisha akapandisha kioo cha giza, alifungua mkoba wa pesa na kuanza kuzitazama vizuri fedha alizopewa kujiridhisha zaidi.

"Kitu chenyewe hiki", Alisema.

"Sasa kazi imeisha hii, vipi kuhusu mzigo wetu aliyobaki nao jamaa?' Mhindi aliuliza.

"Avi tulia, sisi twende watakuja kuuchukua vijana namna wajuavyo si unajua sisi ndiyo sisi"

Waliamua kutoka mahala hapo kwa kasi ya ajabu, huku msafara wa pikipiki ukiwa nyuma kama ilivyo ada. Walishamaliza biashara iliyowaleta hapo, walimwacha Mhindi mwekundu yule naye akiwa anazuga tu wakati usogee aondoke hapo kwani lililomleta lilishaisha.

Robo saa baadaye naye alibeba mkoba wenye mzigo akaamua kutoka nje ya mgahawa, alijongea kwa mwendo wa kujiamini akiwa hana hofu yeyote lakini alipofika nje ving'ora vya polisi vilisikika kutoka kila pande ya barabara ya Lima. Hakuwa na shaka nayo akaingia upande wa kulia wa njia hiyo akijua ni wana yao mengine maaskari wa jiji hilo.

Haikuwa hivyo, magari yote yalikuja kumzunguka na kumuweka kwenye ukuta. Muda huohuo walishuka polisi wakiwa na silaha za moto mikononi mwao na kumuelekezea. Walimwamuru aweke mzigo chini na kisha aweke mikono kichwani naye akatii, askari mmoja kwa hima alikuja kumfunga pingu kisha akampeleka kwenye gari mojawapo na kumwingiza ndani.

Tukio hilo lilipotokea waliliona wachache tu na ndani ya mdua mfupi kukawa hakuna gari lolote lililosalia, yalitokomea huku raia wengi wakijua aliyedakwa pale ni mhalifu tu hakuna jingine. Hawakujua kuna namna nyingine kabisa, waliyoijua ni wenye kuhusika nayo.

Msafara ule wa magari ya polisi ulikuja kusimama kwenye msitu huku ving'ora vikiwa vimezimwa tayari, kwa haraka Mhindi mwekundu alishushwa mahali hapo na kusukumwa akiwa chini ya ulinzi. Aliingizwa katikati ya pori na kuja kuwekwa chini huku akitazamana na watu wengine ambao hawakuwa maaskari. Hawa walibeba silaha za moto mikononi mwao, alipowaona hao tu ndiyo akajua amechezewa mchezo hatari.

"Mkienda kwa Stone mwambieni kum****e zake", Mhindi alifoka kwa hasira ingawa yupo chini ya ulinzi.

"Jamani mkuu kasemaje juu ya huyu?' Mmoja wa wale Askari polisi aliuliza.

"Kateni umeme tu hapo si unajua kazi ishaisha", Mmoja wa watu waliyokutwa porini humo alisema, kutoka kwa kauli hiyo Mhindi yule alipigwa risasi ya goti na kisha ikafuata ya kiuno. Hawakumkawiza, walimmalizia na risasi za kifua na moja ya kichwani ikawa ni mwisho wa habari yake.

"Nyinyi endeleeni na kazi iliyobaki ya kurudisha huo mzigo mahala pake, sisi tuachieni huu mzoga tujue pa kuuhifadhi si unajua ni mbolea hii kwa miti ya huku porini"

++++

Usiku wa siku hiyo ndani ya kilabu kimoja maarufu mjini Buenos Aires, kulikuwa na pilika nyingi huku wengi wao wakiwa wamekuja kujifurahisha. Muziki wa mahadhi ya nchi humo, ulirindima huku watu asilimia kubwa wakiwa wanausakata vilivyo, mwangaza wa ndani ya kilabu hiki ulikuwa ni rangi nyekundu inayofifia na kufanya watu wasiweza kuonana vizuri.

Wengine wakiburudika na muziki, wapo waliyokuwa wakicheza kamari upande mwingine wa meza ya kufanyia mchezo huo. Pia wapo waliyokuwa wanatazama madansi wa utupu kuburudisha macho yao, upande kwingine kulionekana makochi ambapo kulikuwa na wanaume wachache wakiwa wamezungukwa na maguberi ambao walikuja kuvuna pato lao la siku kupitia miili yao. Kiufupi ndani humo kulijaa kila aina ya ushenzi, na wale waliyoweka bango ya kukataza wasiyotimiza miaka kumi na nane kuingia humo hawakuwa wamekosea. Wapo sahihi, hakukuwafaa hata.

Mezani wanapocheza kamari, Stone akiwa na binti mwenye asili ya kilatino walikuja kwa pamoja kuja kutumia pato lao la siku na hata kuvuna jingine ndani ya mchezo huo. Kijana huyu mwenye ngozi nyeusi alijua haswa kuwamaliza wenzie, kila zilipochangwa karata kwa mara nyingine basi yeye ndiyo alikuwa ni mlaji. Alifurahia haswa huku akishangailia na kupigana mabusu na binti mrembo aliyekuja naye.

Kawaida ya mchezo hu asilimia kubwa wauchezao si watu wazuri, na kitendo cha kuliwa hupelekea kutaka kufanywa jambo lolote baya. Pesa za watu zilipoonekana kujaa kwa Stone ustahimilivu uliwaishia na wakajikuta wakimwelekeza bastola, binti aliyekuwa naye alishtuka mno na kumkumbatia kwa uoga ila kwake hakuona jambo la kumtisha alijikuta akitabasamu tu huku akiwatazama watu weupe hao waliyomuwekea silaha.

"Usijichekeshe wewe nakwambia inuka upesi, huwezi kuwa mlaji kila muda. Mchezeshaji mtazame huyu huenda kaficha karata", Mtu mmoja ambaye ni mtu mzima aliongea huku akielekeza bastola kwa Stone.

"Unafikiri kila mtu kakaa kiwizi, huu mchezo ni bahati ndiyo ushindi. Leo hii imeangukia kwangu", Stone alisema kwa kujiamini huku akitabasamu, mtu yule ndiyo kwanza alitoa usalama wa silaha yake kisha akamwonesha yupo tayari kufyatua.

"Jus inuka tafadhali atatuua huyu", Binti naye alishinikiza lakini wala hakufanya jambo hilo.

Yule mtu ndiyo akaingiwa na hasira kabisa, aliisogeza bastola jirani na uso wa Jus, hakujua hilo ni kosa kubwa kulifanya kwa kiumbe huyu. Kutahamki, alinyang'anywa kinamna ya ajabu na kisha akaelekezewa yeye, waliyokuwa hapo walishtushwa mno na tukio hilo ambalo halikutarajiwa. Hakuna ambaye alifikiri kama Jus ni mwenye kasi namna ile, kiasi cha kuweza kumpora mwenye silaha bila kufyatukiwa.

"Unachezaje na chombo usichojua kukichezea wewe, unafikiri nilivyokishika hivyo ninashindwa kukumaliza " Jus alisema na kisha akaishusha silaha chini halafu akamtazama mchezeshaji na kumwambia, "Unaweza kuja kunitazama kama kweli ninaiba kwenye mchezo".

Mwenye kuongoza mchezo alikuja kumkagua na akajiridhisha hakukuwa na udanganyifu aliyoufanya, hapo wanaocheza wakajua ni bahati kama ilivyo nyingine. Amani ilirejea na Jus alirejesha silaha kwa Mzungu yule, hakutaka kukaa tena hapo aliamua kuinuka na kuchukua pesa zake zote. Alishikana kimahaba na mrembo wake kisha akaondoka hapo, majira hayo tayari ilikuwa ni usiku mnene. Alitoka nje na kufika hadi garini akamwingiza mrembo ndani naye akawa anazunguka upande wa pili aendeshe, akiwa kwenye haraka hizo za kuelekea upande ulipo alijiwa na yule mzungu aliyemuwekea bastola kule ndani.

Ujio wake mahala hapo ulimfanya asite na kisha amtazame kwa umakini halafu akauliza, "Umekuja kuninyooshea bastola kwa mara nyingine". Swali hilo lilifanya mtu yule atoe tabasamu kisha akanyoosha mkono kumpatia huku akisema, "Alfonso"

"Stone", Jus naye akasema huku akipokea mkono ule.

"Nimependa uwezo wako na kasi yako, nadhani nitahitaji sana mawasiliano nawe"

"Nenda moja kwa moja kwenye mada"

"Nahitaji kufanya kazi nawewe, hii ni kadi yangu ya mawasiliano. Bakshishi ipo ni wewe tu kuamua ima uwe tayari au la"

"Asante, nikutakie usiku mwema", Jus alisema huku akingia upande wa dereva wa gari, aliwsha chombo chake na kukiondoa hpo huku akimwacha jamaa yule akimtazama.

++++

Asubuhi iliyofuata Jus na Alfonso walikutana pamoja kwenye hoteli ya nyota tano iliyopo jijini humo. Walifika hapo kupata kifungua kinywa kwenye mgahawa, miadi ya kuonana walikubaliana na majira hayo wapo pamoja. Kijana mweusi daima akisikia kuna suala la kupata pesa, basi huwa mstari wa mbele katika kuhakikisha linatimia. Ndiyo maana alifika kwa wakati hapo, akaonana na Alfonso.

Muda huo mpenzi aliyekuwa naye siku iliyopita hakuwepo, alifika mwenyewe kwani kwenye mipango kama hii mwanamke huwa hahusiki. Majira hayo mezani kulikuwa na kahawa, ambayo alipenda kuitumia kama kifungua kinywa. Naye Alfonso aliagiza hiyohiyo kuweza kuchangamsha mwili.

"Nimependa sana umakini wako, umeenda na wakati", Alfonso alisema

"Wakati ni mali zaidi ya shehena ya Almasi, lazima nienda nao sawa. Naam nipo hapa kuweza kukusikiliza"

"Ndiyo maana nikahitaji haswa kuweza kuonana nawe" Alfonso alisema huku akiingiza mkono mfukoni na kutoa picha ambayo alimpatia Jus.

"Luciana Gomez, mtoto wa waziri mkuu wa nchi hii"

"Haswa ndiyo mwenyewe huyu"

"Anasoma chuo kikuu cha Buenos Aires akiwa mwaka wa pili akichukua shahada ya sheria"

"Kabisa ndiyo yeye huyohuyo wala hujakosea, nahitaji unifanyie kazi"

"Nyoosha maelezo"

"Nahitaji atekwe na kuletwa kwenye himaya yangu leo hii, pesa yeyote ipo kwa ajili ya kutimiza lengo hilo"

"Dola laki tano kazi yako naikamilisha jua kabla halijazama, chini ya hapo nadhani hiyo pesa yako ukaliwe tu kamari siwezi kufanya kazi kwa pesa pungufu"

"Pesa ipo tayari kutokana na uzito wa kazi yenyewe, nachohitaji itimie kazi kuendana na muda huo uliyouweka"

"Kwanza nusu ya malipo ndiyo mengine yafuate nikija kukamilisha kazi yenyewe"

"Hakuna shida"

++++

Masaa machache baadaye kwenye eneo la chuo kikuu kikubwa nchini, kampusi ambayo huwa na wanafunzi wa sheria pekee. Lango kuu la kutokea kulionekana watu kadhaa wakitoka wengi wao wakiwa ni vijana waliyovaa mavazi ya kileo huku wachaceh wakiwa ni watu wazima. Hakukuonekana ngozi nyeusi yeyote miongoni mwao, zaidi ya kudhihirika ngozi nyeupe tupu zikiwa na asili tofauti tu.

Miongoni mwa wanafunzi hao binti wa waziri mkuu wa nchi, ni mmojawapo akiwa amevaa gauni fupi jeupe huku akiongozana na kundi kubwa la wasichana. Majira hayo ilikuwa ni muda wake wa kutoka na Jus alishajua hilo tangu mapema, yupo jirani na gari ambalo hutumia binti huyo urudi nyumbani kila atokapo chuoni. Kazi aliyotakiwa kuifanya aliitambua ilihitajika kutumia nguvu, isingewezekana ngozi nyeusi kama yeye kumsogelea binti yule na kukubaliwa kuzungumza naye. Alijiaanda kivingine kuweza kutimiza lengo lake, pesa ilimwendesha mno.


*KWANZA TUMJUE JUS, JE ANA KISA KIPI KILICHOMFANYA AWEPO JIJINI?

*YAPI YALIYOMPELEKEA AKAWA NI MUUAJI?

*JE NAYE ANA BANGUZI?

*TUTAREJEA KWA AKINA GINA





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


____SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU___


Miongoni mwa wanafunzi hao binti wa waziri mkuu wa nchi, ni mmojawapo akiwa amevaa gauni fupi jeupe huku akiongozana na kundi kubwa la wasichana. Majira hayo ilikuwa ni muda wake wa kutoka na Jus alishajua hilo tangu mapema, yupo jirani na gari ambalo hutumia binti huyo urudi nyumbani kila atokapo chuoni. Kazi aliyotakiwa kuifanya aliitambua ilihitajika kutumia nguvu, isingewezekana ngozi nyeusi kama yeye kumsogelea binti yule na kukubaliwa kuzungumza naye. Alijiaanda kivingine kuweza kutimiza lengo lake, pesa ilimwendesha mno.


___________TIRIRIKA NAYO

Binti Luciana alipofikia usawa wa kupanda gari la nyumbani kwao, ndipo chombo cha moto cha barabarani alichokipanda Jus kilipokuja kwa kasi na kusimama mbele ya gari ambalo binti huyo alijihitaji kuondoka nalo. Akiwa hajaelewa kinachoendelea mlango wa gari ndogo ya abiria ulifunguliwa, kwa kasi ya ajabu alivutwa na kuingizwa ndani kisha lango likafungwa kwa ghafla.

Dereva aliyekuwa akifanya kazi na Jus, alikanyaga akselereta kwa nguvu na kuondoka hapo kwa kasi ya ajabu. Aliacha Walinzi wa binti waliyopo garini mule wakipiga risasi kuelekea walipo ila hawakuweza kulifanya gari lisimame, kazi ambayo ilionekana ni nzito hapo awali Jus aliifanya kwa wepesi wa hali ya juu kiasi kwamba walinzi akili zao zilikuwa kama zimeganda vile.

Kutokana na mji huu kuwa na taa nyingi za kuongozea magari ambapo kila mahali hufungwa kamera. Kukimbia kuelekea mafichoni moja kwa moja ingekuwa ni jambo la hatari, kwani hadi kufikia majira hayo polisi walishapata fununu ya kila kitu juu ya ilichotokea. Pia kushuka na kubadili gari ingekuwa ni kujianika sura zao mbele ya kamera za CCTV(Closed circuit television) ambazo zimezagaa mitaa karibia kila mahali.

Watekaji hawa walichokifanya kwa haraka ni kukimbilia nje ya maji ambapo waliingia barabaraba zinazoenda porini. Walifanikiwa kufika ndani ya pori kabisa ambapo walisikia ving'ora vikilia kutoka njia kuu. Huko walipotelea ndani zaidi na wakaenda hadi eneo ambalo kuna kichaka ambapo kuna gari ndogo ya kifahari yenye vioo vya giza ikiwa imeegeshwa. Upesi walishuka na kumfunga yule binti mikono na miguu kisha wamuweka gundi mdomoni.

Walimwingiza kwenye mfuko mweusi na wakaenda kumuweka sehemu ya kuweka mizigo ya gari ile nyingine iliyopo huko porini. Walipomaliza hivyo waliondoa kila ushahidi kwenye gari ile ndogo kisha wakaitega bomu na kuingia kwenye motokaa nyingine wakaondoka kuelekea kule walipotoka.

Mwendo wa nusu kilomita tu njini walipishana na gari za polisi zikikimbia kwa kasi kuelekea kule walipotokea. waoa walijikuta wakitabasmau tu kwani walishawapiga chenga. Jus na mwenzake mwenye taaluma ya udereva walifanikiwa kufika hadi jijini ambapo walielekea moja kwa moja hadi mahali ambapo waliagana wakutane na Alfonso.

Walikutana na mzungu yule ndani ya ghala lenye kuhifadhiwa biadhaa za kiwandani, huko walikabidhi mzigo ambapo ulipofunguliwa kuhakikisha kama ni wenyewe kisha wakakabidhiwa kiasi chao cha pesa. Makubaliano yalienda kama ilivyokuwa, Jus aliondoka akiwa na fedha yake huku Alfonso akibaki na Luciana.

++++

Hali ilikuwa ni tete mno kwa Waziri mkuu wa Argentina, Gomez Martinez. Hakutarajia kama polisi wangeweza kushindwa kumtafuta binti yake hadi inafikia giza kuingia, alichachawa mno na akajikuta akiwakaripia kwa nguvu maaskari wenye kuhusika na usalama wa raia kwa kushindwa kutimiza kazi yao ipasavyo. Eti wameshindwa kuwakuta watuhumiwa ilihali gari lao wamelipua na kukimbia, ilikuwa ni methali ambayo asiyoeielewa maana yake.

Alihimiza kila namna na kutaka kuwepo na msako pori zima lile, kila upande uzungukwe kuhakikisha watekaji wanapatikana. Jambo hilo lilitimizwa kwa upesi huku akiwa hajui kama wahusika hawakuweka makazi humo. Wawindaji wa usiku na hata wengine waliyofika hapo porini kule kwa ajili ya shughuli zao, waliwekwa kitimoto na maaskari hao wakibanwa juu ya kuonekana watu wakishuka kwenye gari. waliyoonekana na sura za kijambazi ndiyo kabisa waliwekwa hatiani kuweza kuteswa wakihisiwa ni watekaji.

Wangefanyaje ilihali wakitoa taarifa ya kutoonekana kwa binti yule, hakuna aliyeeleweka mbele ya Mheshimiwa aliyechanganyikiwa kisa binti yake haonekani. Hakika isingeweza kueleweka, ndiyo ilikuwa kwa viongozi wakubwa pamoja na jambo likiwa gumu upande huhitaji wengine waelewe ugumu wanaoupata. Ila kwa wengine si waelewa hata, wanaona ni sehemu ya uzembe tu.

Hadi inafika saa sita usiku Gomez hakuwa amelala zaidi ya kushinda chumba cha mawasiliano akiongea na wanausalama waliyopo porini kule kufanikisha kazi hiyo. Mambo yalipozidi kuwa magumu ndipo alipoona dunia chungu, alijikuta akilia kama mtoto mdogo huku mkewe naye akiwa hajiwezi kwa kupotelewa na binti huyo. Akiwa kwenye simanzi kali usiku wa manane ndipo alipoweza kupokea simu, hii ilimweleza kuwa akimtaka binti yake basi ahakikisha anatoa kitita cha dola milioni mbili.

Alitajiwa namba ya akaunti ya benki ya kuweka pesa hizo ndipo angeweza kumpata banati wake, Gomez alipoelekezwa kuhusu hayo kutokana na hali ya kuchnganyikiwa alijikuta akimtukana tu aliyempa maelezo badala ya kutenda kile alichoambiwa. Alipomaliza kuongea hivyo alikata simu papo hapo kisha akashika kichwa chake na kuendelea kulia, aliinamisha kichwan akilia kama mtoto mdogo.

"Mheshimiwa simu iliyokupigia hivi sasa tumeipata eneo inapotokea", Mmoja wa vijana wa mawasiliano waliyopo nyumbani kwake alisema, Gomez alijikuta akikirupuka kutoka hapo alipojiinamia na kusema, "Eeeh! Unasema! Hakikisha kamera za eneo hilo zote zinamwonesha mpigaji simu hiyo.

"Tumempata ni huyu", Kijana mwingine mwenye utaalamu wa kuongoza kamera za ulinzi alisema, Gomez alijikuta akikurupuka kutoka kwenye kochi na kusogelea kioo cha tarakilishi kuweza kujionea.

Walimwona mzee akiwa ndiyo anaongea na simu ya kibandani katikati, ilipokatwa simu alionekana akipiga ngumi kwa nguvu kwenye kuta za kibanda hiko. uwezo wake wa kutupa mkono ulionesha ni namna asivyo mzee na ana nguvu za ziada mwilini mwake, hilo liliwashangaza vijana hao. Kwa upesi waliwasiliana na maaskari waliyopo kazini na kuwapa taarifa huyo mtu ashikwe mara moja, walibaki wakishuhudia huenda mtu yule angeweza kutiwa nguvuni pia wasiweza kumpoteza kujua ni wapi atakuwa ameelekea.

Walimshuhudia akitoa simu mfukoni mwake na kumpigia mtu, muda mchache baadaye kulisikika sauti ya bastola ikipigwa juu. Hawa hawakujua imetoka wapi, ilihali polisi waliyokuwa wakimuwahi bado hawajafika hapo. Mlio huo uliambatana kwa kusikika mayowe ya kundi kubwa la watu, hapo waliweza kuona umati mkubwa wa watu ukipita kukimbia upande kilipo kibanda hiko. Walikizonga na kupelekea hata kamera zikawa hazimwoneshi, kupita kwa watu hao kulipoisha mtu yule hawakumwona tena. Gomez alijikuta akiwa haelewi katorokaje, ila ukweli ulibaki kama ulivyo kuwa lile kundi la watu ndiyo limetumika kama njia ya kutoroka kwake.

"Fuatilieni kamera zote za eneo hilo, chunguzeni makundi yote ya watu kwa umakini pia angalieni alivyotoka mule ndani", Gomez aliamuru akionekana kuchanganyikiwa.

"Kwanza ilikuwa vipi usiku kama ule kuonekana idadi kubwa ya watu namna ile wakikimbia, wanakimbia nini?", Alizidi kuuliza maswali.

"Mheshimiwa mlio ule wa bunduki ulitoka ndani ya Gosprezo, klabu maarufu ya usiku ndiyo watu waliyopo mule ndani wakakimbia kuokoa maisha yao", Kijana wa tarakilishi alisema.

Walifuatilia kila namna juu ya kutoroka kwa mtu yule, ila hawakubaini lolote wala kujua ni wapi alipoelekea. Haikuhitaji akili za ziada kuweza kutambua kuwa aliyepiga risasi na yule aliyekuwa akipiga simu. Ni watu wenye lengo moja, ilijulikana wazi nyendo yao ingekuwa inafuatilia, ndiyo maana wakaamua kufanya hila namna ile ili wampige chenga.

Askari polisi nao waliwasili eneo hilo, wakawa wanaonekana kwenye tarakilishi ila hawakuweza kubaini chochote zaidi ya kukuta mavazi ya yule mtu yakiwa chini. Pia walikuta kukiwa na wigi na ndevu za bandia vilevile. Gomez alipoelezwa hivyo ndiyo alizidi kuchachawa kabisa yaani wamemkosa mtu yule.

"Hebu ngoja", Alisema na kisha akawatazama vijana wake na kunena,"nyinyi endeleeni na kazi yenu nitarejea mara moja". Alipoongea hayo alitoka nje akiwaacha wataalamu wakiendelea na kazi yake, hakumsemesha yeyote ndani ya nyumba yake zaidi ya kuingia garini usiku huo akionekana ni mwenye kuwahi mahali fulani.

++++

Baada ya dakika takribani kumi na tano, msafara wa magari ulionekana ukiingia kwenye nyumba ya kifahari yenye kufanana na kasri la kifalme. Msururu huo ulipita moja kwa moja hadi ukaja kusimama kwenye eneo lenye mzunguko wa barabara ndani humo. Mahali hapo kulionekana walinzi wegi wakiwa wameshika silaha zao, kuingia kwa msururu huo kulipelekea mwenye milki hiyo kuweza kutoka ndani eneo la baraza kuu la jumba lake akiwa anatazama kule yaliposimamia.

Mlango wa motokaa mojawapo kati ya zile zilizofika mahali hapo, ulifunguliwa na kupelekea mwenye nyumba yule apige hatua kushuka kwenye ngazi za baraza akiwa amefuatana na walinzi kadhaa. Mtu huyu mwenye asili ya latino, alitoka ndani akiwa amevaa mavazi ya kulalia tu huku miguuni akiwa na viatu vya wazi. Alifika hadi mbele ya mgeni aliyefika mahali hapo, huku ujio wake ukionekana kuna jambo kubwa kupitiliza.

"Gomez vipi mbona usiku huu tena, si ungekuja asubuhi tu huoni kama ni muda wa kupumzika", Mwenyeji huo alisema.

"Fernado nitapumzika vipi wakati binti yangu katoka, au hujui hili", Gomez aliongea kwa papara.

"Tuliza papara kwanza, najua kuhusu hilo ila hukuwahi kunishirikisha kabisa nashangaa ujio wako mahala hapa"

"Nahitaji msaada wako Fernando, siku hii iliyoingia saa sita usiku isiishe binti awe amepatikana"

"Gomez, Gomez si una nguvu ya vyombo vya dola na unatambua wazi mimi nina njia gani naitumia. Ukasema huwezi kuwa mkono nami"

"Fernando, Fernando! Tunaweza kuongea"

"Ok tuingie ndani"

Kwa pamoja waliingia ndani na kutokea kwenye sebule ya kisasa, Gomez alikaribishwa kochini kisha akapewa kilevi. Kutokana na hali ilivyo hakuwa na jinsi zaidi Ya kupokea kileo hiko na kisha kukinywa kwa pupa, alipomaliza bilauri yake ilikuwa tupu na kuomba awekewe tena.

"Gomez taratibu hii pombe si ya mchezo hii, pia nahitaji urejee kwenye akili zako tujadili suala hili vizuri ndiyo utatoa maamuzi stahiki"

"Nimepoa hasira yangu iliyoachanganyika na huzuni sasa hivi, nachohitaji binti yangu arudi tu na si kingine"

"Fafanua"

"Mtekaji wa binti yangu kapiga simu na kutoa namba za benki anahitaji dola milioni mbili ndiyo aweze kumwachia. Sisi ni watu wenye kusaka pesa kwenye njia tofati, hili suala limetuweka tuwe ndani ya njia moja. Ipo dola milioni nne, mara mbili aliyoweka mtekaji. Nahitaji mwanangu arudi na niione maiti ya mtekaji"

"Kumbe kazi ndogo namna hiyo, kuna mtambo upo wa mauaji. Si ikiisha siku hii tu nadhani asubuhi haifiki mtoto wako anapatikana. Bakshishi kwanza, nimpe kazi hiyo aifanye", Gomez aliposikia maneno hayo, kwa haraka alimwita mmoja wa wapambe wake, huyo alikuja na kitabu cha cheki na kumpatia pamoja na kalamu. Waziri mkuu aliandika cheki kisha akampatia Fernando ambaye aliachia tabasamu hafifu baada ya kuitazama.

"Sasa subiri uone kazi itakavyokuwa", Fernando alisema kisha akagiza aletewe simu yake, alisubiri kwa dakikaa na ilipofika aliichukua na kubonyeza namba kadhaa kisha akaiweka sikioni na kusema, "Stone dola milioni moja ipo hapa, nahiaji Luciana Gomez apatikane kabla hakujakucha, urudi na maiti ya mtekaji" Alikata simu bila ya kusikiliza upande wa pili kama umekubali au la, alipomaliza alimtazama Gomez.

"Huyu niliyempatia kazi hii jua anajua kufanya lolote kukiwa na pesa tu. Sasa tusubiri hadi muda niliyompatia"

++++

Simu ya Fernando ilimfikia Jus akiwa yupo kwenye harakati za kwenda kulala usiku huo, aliposikia msamiati pesa usingizi wote ulimwisha na akajikuta akisitisha jambo hilo. Uzuri wa mahali alipowekwa Luciana anapajua, tena alipokwenda kufanya uhaini wala hakuwa ameweka sura yake wazi. Walipomuweka ndani ya mfuko ndiyo aliweza kuiacha sura wazi, hivyo hakuonekana.

Aliamua kusitisha mpango huo na kurejea kule ghalani alipohifadhiwa, safari hii hakuja kirafiki tena zaidi ya kuingia kishari. Mtu mwingine kupata dau la pesa, kwake yupo tayari kumgeuka yule ambaye walikubaliana naye kufanya naye mpango hapo awali. Hii ndiyo rangi halisi ya Jus ambayo Alfonso hakuijua wakati akimpatia mpango wa pesa. Harudishi kiasi chochote cha hela, ilimradi aweze kutimiza tu kile alichohitajika.

Alipofika eneo la nyuma la ghala ile, alitoa bastola mbili ambazo alizifunga sailensa kila moja kisha akaruka uzio wa jengo hilo. Alipotua chini aliangaza kila upande na kuhakikisha usalama upo halafu akaingia ndani, silaha zikiwa mikono yote alitembea kwa kujidai kama vile hakuwa ameingia kishari hapo. Alifika hadi eneo ambalo amefungwa Luciana ambapo alimkuta Alfonso akiwa amesimama na vijana wake wanne, ujio wake mahali hapo ulimshangaza hata rafiki yake wa muda mfupi aliyejua tayari wamejnga ukaribu kwa kumpatia kazi hiyo.

"Unafuata nini?", Alfonso aliuliza.

"Nimemfuata Luciana, ulitegemea nije kufuata nini hapa", Jus alipojibu hivyo, alielekeza bastola upande walipo watu wale, kwa haraka alizikoholesha na kuwangusha wote kwa pamoja huku binti waziri akiwa hajui kinachoendelea kutokana na kufungwa kitambaa usoni mwake. Aliachwa Alfonso tu ambaye alibaki akiwa na mshngao, wepesi wake aliujua vilivyo na alijua hadi hapo amekwisha tayari.

"Kwanini?", Alfonso aliuliza.

"Pesa tu, nimelipwa nije kumkomboa huyu na baba yake. Niwie radhi sana kwa hilo". Jus alipomaliza kuongea hivyo alimpiga risasi ya kichwa Alfonso, huo ndiyo ukawa mwisho wake wa kuweka makubaliano naye mtu asiyeaminika mwenye kufuata pesa tu.



*PESA TU NDIYO CHANZO CHA YOTE HAYA, JE ITAMFIKISHA WAPI?

*USALITI WA JUS KWA AJILI YA PESA, ATADUMU NAO?






ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

____SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE_____


"Pesa tu, nimelipwa nije kumkomboa huyu na baba yake. Niwie radhi sana kwa hilo". Jus alipomaliza kuongea hivyo alimpiga risasi ya kichwa Alfonso, huo ndiyo ukawa mwisho wake wa kuweka makubaliano naye mtu asiyeaminika mwenye kufuata pesa tu.



____________TIRIRIKA NAYO

Alipokamilisha kazi aliyotumwa aliamua kumfungua Luciana kisha akamtwaa, binti huyu aliposikia maneno aliyokuwa akiyasema wala hakuwa na shaka naye tena. Aliamua kuongozana hadi anabeba mwili wa Alfsono na kuutupa nje ya uzio. Alipofanya kitendo hicho alimchukua na kutoka naye had nje na kuzunguka hadi ambapo aliuchukua mwi;li ule na kuuweka sehemu ya mizigo ya gari alilokuja nalo.

Alimchukua yule binti na kuingia naye garini na kuondoka, safari yao ilikuja kuishia kwenye nyumba ya Fernando ambapo aliruhusiwa na kuingia na binti hadi ndani. Muda huu hata bado alfajiri haikuwa imefika, alienda sambamba na muda aliyokubali kufanya akzi.

Gomez aliletewa binti yake, alijikuta akichanganyikiwa na kumkumbatia kwa nguvu mno huku akitokwa na machozi ya furaha. Alipeleka Mack pia kwa kijana yule aliyefanikisha kazi hiyo, alijikuta akishukuru kwake kwa kuweza kutimiza kazi hiyo.

"Gomez nilikupa ahadi, huo mtambo mweusi hapo yaani kazi yake ni kuupa saa tu ya kutimiza kazi. Ukiona hajakwambia muda huo ni mdogo, basi jua anaweza kuitimiza kazi hiyo. Toka ninamtoa Haiti sijajuta hata kumtumia hadi leo hii", Fernando alisema.

"Hata mimi leo nimeiona kazi yake kuwa inafaa zaidi, tupo mkondo mmoja sasa hivi kaka yangu", Gomez alisema huku akimtazama mlatini mwenzake.

"Haina shaka", Fernando alisema kisha akamgeukia Jus na kumuuliza, "Umetimiza sharti jingine la kazi hii?"

"Hakika, mnaweza kwenda kujionea wenyewe"

Jus alitoka nje huku akifuatana na mabwana wakubwa wenye jina ndani ya nchi hiyo, aliwafikisha hadi kwenye gari lake kisha akawapeleka sehemu ya nyuma mabapo alifungua na kuwaacha waone. Kila mmoja alishuhudia yule aliyekuwa amemshikilia Luciana, akiwa ni mfu tayari.

"Kawaida ya mila ya familia yetu ni ipi?", Gomez alimuuliza Fernando.

"Mtu wa aina hii akishikwa kama ni mfu basi anaenda kutupwa bwala la Mamba aliloliunda Mzee Martinez. Nadhani mila zetu ulizitupa kwa muda mrefu sana", Fernando alisema.

"Sasa ni wakati wa kuirejea asili yangu, naona nikiwa kwenye namna nyingine wananichezea hadi ndevu zangu hawa watu. Roho ya kimartinez bado ipo mwilini mwangu"

"Napenda nikalishuhudie mwenyewe hilo tukio, basi sijaamini kama Gomez kama wewe umerejea"

Ilibidi Jus apewe kiasi cha pesa alichoahidiwa na Fernando ambacho kipo ndani ya nyumba hiyo, aliondoka hapo akiwaacha ndugu wawili waliyokuwa wapo pamoja kwa muda mrefu wakijadiliana kuhusu mwili wa Alfonso. Hakuthubutu kufungua mdomo wake kuwaeleza kuwa yeye nidye alihusika na utekaji ule, alimaizi wazi roho ya paka aliyo nayo tajiri wake angeweza kumfanya chochote haswa baada ya kubaini amehusika na utekwaji wa mpwa wake.

Fernando Martinez na Gomez Martinez hawa walatino walikaa kwa kipindi kirefu mno baada ya mmojawapo kuingia kwenye utumishi wa umma na kutupa shughuli zote ambazo mwenzake alirithi kutoka kwa baba yao. Wote kwa pamoja ni wana wa Martinez mmoja wa watu tishio kuwahi kutokea nchini bara la Amerika ya kusini ambaye naye alirithi kazi hiyo kutoka kwa baba yake mzazi. Mikoba ya uendeshwaji wa magenge ya kihuni iliangukia kwa Fernando na huo ndiyo ukawa mwanzo wa Gomez kuchukua njia nyingine ya kimaisha.

Hawakuwahi kuwa na maelewano mazuri na hadi wanakuja kukutana siku hiyo, Fernando ambaye ni mkubwa alijua mdogo wake kishari lakini aliposikia ni mwenye kuhitaji msaada alitanguliza pesa mbele. Kutokana na uhasama wao alifanya hivyo moja kwa moja, ingawa hapo awali alitamani kumwanzishia fujo alipoiona sura yake mahala hpo.

++++

Mfuko wa Jus ulituna haswa na kwa kuua ndege wawili kwa jiwe moja, kwanza alichukua dola laki mbili na nusu kwenye mgao wa dola laki tano zilizotolewa kutokana na utekaji wao kwa Luciana. Pia akaja kumalizia mara mbili ya mgao mzima aliyoupata kule. Alijiona ni mjanja mno kwa kulamba dume kwenye mchezo wa karata, wala hakuwaza kuwa alifanya dhuluma pia kwenye mchezo huo.

Alifanikiwa kufika nyumbani kwake salama, ambapo alihifadhi fedha haraka sana na kisha akapitiliza kulala moja kwa moja kutokana na kuukata usingizi wake kwa tamaa ya hela. Usingizi ulimjia kwa amani hadi pale kulipokucha hakuwa ameamka, alikuja kuamka majira ya adhuhuri baada ya kujiwa na rafiki yake mwenye kushughulikia naye kwenye kazi hizo haramu.

Avi ambaye mara nyingi huwa ni dereva wakiwa kwenye kazi yenye kuhitaji watu wawili au yenye kutumia gari. Ndiyo aliwasili na kumfanya akatishe usingizi wake na kuja kuungana naye katika kipindi hicho ambacho mpenzi wake hayupo.

Jus aliamua kumweleza kila kitu swahiba yake huyu kilivyokwenda hadi kufanikiwa kupata kiasi kile kikubwa cha pesa, alimpongeza mno kwa kuweza kucheza na akili za matajiri wale kiasi cha kuomba pesa hizo na asijulikane.

"Ila mtu wangu kama wale watu wapo pamoja basi kuwa makini mno kwenye madili yako, likikandamiza la mmoja basi jua ndiyo utakuwa mwanzo wa kuingia pabaya. Fernando ni mnyama, mdogo wake unafikiri atakuwa vipi naye",


"Yaani mtu wangu inabidi niwe hivyo tu maana nimesikia Gomez, anaenda kumtupa yule boya kwenye bwawa la Mamba"

"Ohoo! Kaka na mdogo wake akili zao sawa, yaani hawa walatino aisee ukikutana naye kwenye harakati kama hizi bora ukutane na mamba mtoni tu"

"Kikubwa ni kupiga pesa zao tu, wakihitaji tupoteze roho ya mtu. Kuna kitu gani dunia hii kianchosakswa zaidi ya pesa wacha tuzipate tu hakuna namna nyingine"

"Hapo umesema pesa ni muhimu mno"

++++

Wakati Jus akiwa anajua ni mwisho wa kazi ile na hataweza kukutana na kitu chenye kuhusika nayo, Luciana kwake ilikuwa ni mwanzo wa kitu kingine. Usiku yule aliyoweza kuwa na mwanaume yule mwenye nguvu ambaye amemkomboa, ndiyo uawa mwanzo wa kuwa na hisia nyingine juu yake.

Awali alipoondoka baada ya kukanidhiwa pesa zake, alihisi kutaka kumwona kila muda ila hakuwa na ubavu wa kuweza kumzuia asiweze kuondoka. Alimsindikiza kwa macho alipoweza kutoweka nyumbani kwa baba yake mkubwa, ila haikuwa ni sababu ya kaucha kumuweka fikirani mtu yule.

Mwanzo alijua ni mawazo ya kawaida tu, lakini alipokumbuka wakati anaiona misuli yake kipindi anaendesha gari alijikuta akikiri mwenyewe amemhusudu mtu mweusi yule. Asiyejua kuongea maneno mengi, hakujua angeweza kumpata wapi baada ya kuweza kumwona na kisha kumpoteza machoni mwake tu. Pia hakuelewa aanze vipi kutafuta makazi ya yule kijana, akisema amuulize Fernando angeweza kukaribisha mengine anamjua wazi mtu yule jinsi alivyo kutokana na kuzisikia habari zilivyo.

Nyumbani kwao alifikisha na kupokewa kwa furaha na mama yake na hata wadogo zake, lakini haikuwa sababu ya kuweza kumfanya amsahau Jus. Alimkaa moyoni mno kijana yule mwenye kujua kufanya kazi yake vilivyo, muda ule ambao baba yake mkubwa akimsifia kutimiza kazi kuendana na muda yeye ndiyo ilikuwa ni faraja mno. Loh! Ameingia mapenzini na muuaji, binti kaipenda roho ya paka.

++++

Majira ya mchana wa siku hiyo Fernando na Gomez walifika hadi kwenye kijiji kimoja kilichopo nje ya mji wanaoishi. Huko walifika kwenye nyumba ya kifahari mno iliyopo katikati ya mashamba makubwa ya mizabibu. Walifika hadi kwa mwanamke mmoja mzee ambaye alishangaa kuwaona pamoja na wala hakutarajia jambo hilo. Kufika hapo kulimfanya Ajuza huyo kwa haraka mno atwae bunduki yenye bomba mbili na kutoka kuelekea walipo, alipofika aliielekeza moja kwa moja kwa Gomez ambaye hakuonesha hofu yeyote kufanyiwa hivyo.

"Fernando huyu Panya mwoga umemtoa wapi?". Aliuliza.

"Si Panya wala Paka huyo, ni Simba amerejea kwenye mila zetu. Mkaribishe mwanao mama", Fernando alisema.

"Mtu kutoka kuacha desturi zetu kisa tu kuogopa kuchafuka kisiasa ni nani?", Mwanamke huyo alisema na alipomaliza alifyatua risasi ambayo ilipita juu ya kichwa cha Gomez, waziri mkuu huyu wa nchi wala hakutetereka ndiyo kwanza alisimama kikakamavu. Jambo hilo lilifanya Ajuza yule aaachie tabasamu kisha akaja kumkumbatia kwa nguvu, kitendo hicho kilipelekea walinzi wa eneo hilo wapige risasi hewani kuashiria ni tukio jipya.

Kama vile ambavyo Gomez aliahidi, mlatino huyo kwa jinsi asivyokuwa na roho ya huruma. Aliuburuza mwili wa Alfonso hadi jirani na bwawa lenye mamba, akiwa hapo aliagiza shoka kuanza kuukata vipande ule mwili kisha katupa bwawani. Ni ukatili aliyoufanya ila hapo kama vile ni tendo la furaha, kila mmoja alifurahi mno kwa hicho kitu na kufikia hatua ya kumkumbatia alipomaliza kazi hiyo. Walifarijika mno waliposhuhudia Ngwena wakigombania nyama za mwanadamu mwenzao, kwao haikuwa jambo lenye kusikitisha.

"Alikosa wa kuteka akaamua kumteka Luciana, hayo ndiyo malipo yangu. Tena asingemuua yule kunguru, ningefanya hivyo mwenyewe", Gomez alisema huku akitazama bwawani.

"Khaa! Kama ni wa kumteka mjukuu wangu bora mngemshika mzima na kumleta huku. Nilitaka aliwe na mamba huku anajiona ndiyo ingekuwa ni funzo tosha"

"Mtambo wa mauaji ulipewa maelekezo urudi na maiti na ndiyo ulivyofanya. Tungejua tungempa kazi ya kumleta hai", Fernando alisema.

"Kazi ya kunguru mweusi hii, ile rangi siipendi sana naona ulikosea ungempa mwingine si yeye"

"Hakuna mtambo wenye kufanya kazi kwa haraka kama ule, sikuwa na mwingine wa kumpatia", Fernando alisema kisha akaingiza mfukoni mwake na kutoa cheki ya pesa aliyopatiwa na mdogo wake, aliichana vipande huku akiona. Alipomaliza hilo alisema, "Kwakuwa umerudi kwenye mstari wetu haikuwa na haja ya kuchukua malipo yako, sisi ni ndugu"

++++

Mzazi wake akiwa yupo kijijini, Luciana aliamua kutumia watu anaowajua wenye kujua makundi ya kihalifu nchi nzima kuweza kumsaidia kumpata walau jina la kinana aliyemwokoa. Hakujua kama yule ndiye aliyemshika na kumtia shimoni, aliangalia walau kuweza kupata jina lake ndiyo ajue namna gani atampata. Alijaribu kwa wengi mno lakini hakuweza kujua jina lake, siku nzima alihangaika na hilo mwishowe akajikuta akikata tamaa.

Usiku mnene akiwa anajiandaa kulala ndipo alipojiwa na wazo jingine, aliamini akilifanya hilo angeweza kujua kila kitu kuhusu mtu yule mweusi. Aliamua kuuliza kwa mmoja wa vibaraka wa Fernando ndipo alipoweza kupata habari kumuhusu yule mtu. Alielezwa kuwa yule hakuwa na ajira rasmi kwa Mzee yule isipokuwa ni kufanya kuendana na makubaliano tu, yaani ni muuaji wa kimkataba tu ambaye anamtumia kwa ajili ya shughuli zake.

Luciana hata alipojua mtu aliyemuweka moyoni ni muuaji tena hatari, hakuwa tayari kurudisha nyuma moyo alitaka ampate tu. Alipouliza kuhusu mahali ambapo anaptikana, hapo ndiyo ikawa ni ngumu mno, hawakuwa wakijua anaishi wapi zaidi ya mtu wake wa karibu kikazi ndiyo mwenye kumaizi hayo. Ikawa ni ugumu mwingine kuweza kumpata Jus ambaye anajulikana haswa kwa jina la Stone kwa Fernando, ila binti huyu hakukata tamaa ilimradi amepata jina alihakikisha atampata kwa gharama yeyote ile.

++++

Luciana akiazimia hayo, Jus alikuwa yu karibu na mwandani wake ambaye ni mwanachuo nchini humo. Juliana Tores, binti kimeksiko mwenye kuishi humo kimasomo tu kutokana na kufadhiliwa na Jus. Siku hii kijana huyu mweusi aliitumia kufurahia naye mpenzi wake wa maisha, akiwa kwenye fukwe bahari wakitumia siku pamoja kwa furaha.

Wapenzi hawa walijumuika kucheza michezo mbalimbali na kula pamoja, pamoja na baadhi kuwashangaa jinsi walivyo na asilia tofauti, wao hawakulijali hilo zaidi ya kufuata kile moyo wao unapenda. Walikodi hadi boti na kuingia nayo majini kuzunguka eneo la rasi ndani ya mji huo, pesa ilitumika kwenye starehe hizo ila kwao haikuwa tatizo maana zilikuwa ni nyingi. Walizunguka sehemu kadhaa baharini, Jus akiwa ndiyo mshika usukani wa boti hilo na kuiongoza vyema. Walifika mahali na kusimamisha kisha wakaingia baharini kuogelea, yote ni kuweza kutimiza furaha yao.

Kila walichokuwa wakikifanya walirekodi kwenye kamera, huo ndiyo ulikuwa utaratibu wao wakifika maeneo ya starehe kama hayo ambayo ni ya wazi Walishazoea wanapopata muda wa kupumzika hujikumbusha kwa kutazama waliyoyafanya. Walipokinai starehe hiyo walirejea ufukweni, ambapo walipumzika huku wakaanzisha mazungumzo.
"Jus, ni mwaka wa mwisho nipo chuo. Nafikiri ni muda mwafaka wa kwenda kwa baba, ndoa ni muhimu", Juliana alisema

"Nalitambua hilo, nafikiri ni vyema zaidi nikikuona umeshatunukiwa kabisa shahada yako na mambo yako yapo sawa ndiyo twende au unaonaje? Nataka ajue ahadi ile niliyompa ya kuhakikisha maisha yako yanakuwa mazuri nimetimiza"

"Mimi sina neno juu ya hilo, nachotaka ni kuwa pamoja zaidi ya zaidi. Nakupenda sana Justus"

"Nadhani mimi ni zaidi ya unavyonipenda, kukuona wewe ndiyo furaha yangu duniani sina kingine cha kuweza kunifanya nitabasamu isipokuwa kukuweka wewe machoni mwangu nakupenda sana Juliana wangu"

Kutoka kwa kauli hiyo kuliambatana na kupigana mabusu kwa pamoja, kisha wakakumbatiana kwa pamoja. Jus pamoja na kuwa na roho ya kinyama bado kwa binti huyu ni mwenye kulainika mno, mithili ya mkate ugusapo chai. Hakuwa na ujanja, huo ndiyo udhaifu wake mkubwa ingawa hakuna aliyekuwa akijua hilo. Hakuwahi hata kuthubutu kumwambia rafiki yake juu ya kuwa mdhaifu kwa binti huyo, alibaki nalo moyoni tu.

*FERNANDO NA GOMEZ WAPO PAMOJA.

*JUS ALIWACHEZEA MCHEZOO BILA YA KUJUA, VIPI IKIJULIKANA?

*JE LUCIANA ATAFANIKIWA KUMPATA JUS?




ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO_____


Kutoka kwa kauli hiyo kuliambatana na kupigana mabusu kwa pamoja, kisha wakakumbatiana kwa pamoja. Jus pamoja na kuwa na roho ya kinyama bado kwa binti huyu ni mwenye kulainika mno, mithili ya mkate ugusapo chai. Hakuwa na ujanja, huo ndiyo udhaifu wake mkubwa ingawa hakuna aliyekuwa akijua hilo. Hakuwahi hata kuthubutu kumwambia rafiki yake juu ya kuwa mdhaifu kwa binti huyo, alibaki nalo moyoni tu.

________________TIRIRIKA NAYO

Siku nzima waliimaliza huko, jioni walirejea mahali wanapoishi huku kila mmoja akihitaji tulizo zaidi ya yale waliyokuwa wakiyafanya. Walianza starehe zingine wakiwa ndani jioni hiyo, haya ni mojawapo ya maisha ambayo Justus alipenda ayaone kila siku yakitokea kwenye kwake lakini ndiyo hivyo kilichopangwa hakiwezi kupangulika.

++++

Maisha ndani ya utawala wa Fernando akimtumia kwa makubaliano maalum aliyaona ni matamu mno. Hakuona ubaya wowote ingawa alishawahi kusikia juu ya tajiri yule kutotaka kabisa mtu mweusi, kupewa pesa kila alipokamilisha kazi kulimfanya aamini msemo huo haukuwa na ukweli wowote ndani yake. Aliendelea kumtumikia na kumwingizia faida kubwa, kwani hakukuwa na yeyote yule mwenye kufanya kazi kiufanisi kuliko yeye. Pia hakukuwahi kutokea kuharibibika kwa kazi iliyofika mikononi mwake.

Haikupita muda mrefu, wahindi waliyokuwa wapo kitengo cha kusafirisha mizigo kwa Mlatino yule walijikuta wakiingia kwenye hukumu mbaya baada ya ya kufanya na mzigo kuingia kwenye mikono ya dola. Watu hao waliuawa kiukatili mno na Fernando mwenyewe, tena kwa hasira zaidi aliamua kuua na wahindi waliyowashika kuwaleta hapo kwa kuona ngozi hiyo ndiyo yenye hatia na si wale wachache.

Tukio hilo kwa haraka liliamsha hisia nyingine kwa Avinansh Khanna maarufu kama Avi ambaye ni rafiki mkubwa wa Jus. Huyu aliona jinsi watu wa wakaribu na Fernando wakifanya kosa huweza kutouawa na kuachiwa au kupewa adhabu ngumu, ila taifa jingine huambatana na kupewa mateso makubwa mno yasiyostahiki kupewa kiumbe wa kawaida na kuishia kufa. Aliona kama pesa anazo nyingi mno na zinatosha kwenda kufungua mradi mwingine kwenye nchi za mbali na kuishi kiamani, kuliko kuendelea kumtumikia asiyetambua thamani hata wakifanya kosa la kibinadamu.

Aliamua kukutana na JD ambaye kipindi hicho alikuwa ni mhasibu mkuu wa Fernando, huku akiwa anahusishwa kwenye kazi mbalimbali za uhalifu. Huyu Jammshid msomali mwenye rangi ya ung'avu aliona kweli hakufaa kutumikia hapo, yeye alimwambia ni mwenye kizuizi kikubwa mno ndiyo maana yupo hapo na kama isingekuwa hivyo basi angeweza kuondoka hapo kurudi alipotoka. Alimshauri aondoke hapo na kuanza maisha mbali, jambo hili aliliafiki na kuamua kumshirikisha Jus juu ya hilo maana ni rafiki yake mkubwa mno.

Alitegemea angeweza kuungwa mkono kwenye suala hilo, lakini lililpokewa kwa namna ya kipekee. Jus alipinga kwa nguvu zote kuondoka hapo, na kumwambia bado alihitaji kkuzitafuta pesa nyingi zaidi kutoka kwa Fernando. Alimsihi juu ya kilichowapata wahindi wale kingeweza kuja kumkumba na yeye, hakumsikiliza. Avi aliamua kumuaga rafiki yake wa siku nyingi kuwa anaenda kuanzisha mapya barani Afrika kwa kuhofia kwenda India angeweza kusakwa na tajiri yule. Alimsihi tu kwa urafiki waliyokuwa nao amtunzie siri hiyo ya wapi alipoeleka, siku tatu baadaye Avi alitoa fedha zake zote kwenye kila akaunti ya kibenki yenye kujulikana. Alipomaliza hilo alifungua akaunti mpya zaidi ya moja kwenye benki za kimataifa na kuweka hela huko.

Alihofia mno Fernando angeweza kufunga akaunti zake zote za kibenki ili amkomoe, maana uwezo huo anao kutokana na ushawishi mkubwa wa kifedha. Alipokamilisha hilo ndipo alipotoroka kwa gari hadi nchini Uruguay, napo hakukaa alichukua ndege ambayo ilimfikisha Hispania. Napo hakuona kunafaa aliiishi kwa siku tatu tu na kisha akaondoka kwenda Morocco, alikaa siku chache kisha akaelekea Nigeria. Nchi zote hizo alisafiri kwa kutumia hati tofauti za kusafiri zikimwonesha ni raia wa nchi mbalimbali. Hatimaye mwishowe alifikia nchini Tanzani ambapo alifungua miradi, huko ndiyo kukawa makazi yake.

Justus aliendelea kusalia kwa Fernando, hata JD naye alimpa onyo juu ya kilichowakuta wale wahindi. Alimweleza yeye mzazi wake mmoja ni ana asili ya nchi ile, ndiyo maana mpaka muda huo ameendelea kuishi hapo. Huku naye akimsihi aondoke, Jus alikaidi angalizo hilo laiti angelijua ni bora hata angetoroka na mwenzake kuliko kuendelea kuwa mtumwa pesa. Siku zote mtoto akililia wembe we mpe, ndipo ataujua uzuri wake au ubaya wake. JD aliamua kumwacha Jus aendelee na kutumia fedha za Mlatino yule.

++++

Miezi miwili toka Avi aondoke, Luciana kwa mara ya kwanza alifanikiwa kumwona Jus akiwa anafanya manunuzi kwenye duka katikati ya jiji. Alifarijika mno na akajikuta akimpungia mkono kijana yule, ila hakupewa mrejesho wewote kutokana na mwenzake huyo ni wa kutoka familia ya aina gani. Binti alimsogelea na walinzi na kumwonesha bashasha, kijana ilimbidi tu amsabahi ila jambo hilo hakupenda litokee hata.

Alitamani kuondoka ila banati alihitaji kumwona anasalia mahala hapo, kukawa na mvutano mmoja akitumia ushawishi wa kumwongelesha kila muda na mwingine akitamani anayamaze amwage na kuondoka. Jus aliendelea kumsikiliza hadi pale alipotokea Juliana akamkumbatiana na kumbusu, ndipo Luciana aliingiwa na ukimya wa ghafla kwa kuona tukio hilo huku wivu ukimfurukuta rohoni mwake.

Jus alishukuru kwa jambo hilo na aliaga na kuondoka mahala hapo, Luciana hakuwa na ubavu tena wa kumzuia ila lilimuumiza hilo suala. Alitokea kumchukia Juliana binti ambaye hakuwa na hatia yeyote ile, kisa tu anampenda mwanaume ambaye kawahiwa naye. Alijiapiza atakuja kumfanyia kitu kibaya, kumuona binti mwenzake hata hamu ya kununua vitu ilimwisha na kuondoka na vichache tu ambavyo tayari alivipata.

++++

Mwezi mmoja baadaye Juliana alishika ujauzito, hapo ndipo Jus alipoanza kupunguza pilika ila hakuacha kwenda pale alipohitajika kwa tajiri yake. Akawa yu makini mno katika kumtunza mpenzi wake, chuoni akawa anamfuata na kumleta nyumbani pindi masomo yalipokuwa yakiisha. Jambo hili lilifanya chuki ya Luciana izidi maradufu, kwani mwenye kusoma chuo kimoja na Juliana.

Kipindi hicho ndipo kulipoanza visa, taarifa mbaya mbalimbali juu ya Jus zilienezwa hapo na kipindi kile binti na ujauzito kisirani kikawa kingi. Wakawa hawaishi kugombana kila muda ingawa hayo yalitulizwa, mwishoni Juliana alikuja kujua ni uongo na hapo ndiyo akaanza kuyapuuzia hayo maisha ya mahusiano yake yakawa imara.

Mambo yaliendelea kuwa mazuri lakini aliyekuwa akifanya visa hivyo yakawa ni yameoza kabisa, Justus naye baadaye alikuja kubaini chanzo cha yote ni Luciana. Maan dunia ahaina siri jambo hilo alikuja kudodosa hapo chuoni na kujua hilo, hasira ya kutokewa kwa jambo hilo alijikuta akienda kwa Fernando na kumwambia kuanzia siku hiyo hayupo tayari kuendelea na kazi hapo kutokana na hayo yanayomkumba. Tajiri huyu kutokana na kumuhitaji mno kwa kipindi hicho aliamua kumtuliza kwa kumwongezea malipo, lakini moyoni akabaki na lake.

Jus hakujua kumbe Mzee yule alishaandaa mpango wa kumtafuta mtu mwenye kuziba pengo lake. Kijana naye aliendelea kumtumikia lakini mwishowe aliamua kubwaga manyanga na kwa hasira akatangaza ataihama nchi. Hapo ndiyo alimtibua kabisa Fernando ambaye aliamua kumwita mtoto wa mdogo na kumbana vilivyo, Luciana akaeleza juu ya mahusiano ya Jus na Juliana.

Udhaifu ambao aliuficha kwa muda mrefu ukawa umedhihirika, kilichofua hapo ikawa ni Fernando kutumia uamuzi mgumu. Jus akiwa yupo mbali na mpenzi wake alikamatwa na kupelekwa mbele ya tajiri huyo, alipofikishwa hapo. Alichomwa sindano ya sumu ambayo hupoozesha na pia kuharibu moyo taratibu na hatimaye mtu kufa. Juliana aliachiwa na kuondoka mahala hapo. alipewa na ujumbe amfikishie Jus juu ya hali aliyokuwa nayo.

Justus ikawa ni pigo la pili kwenye maisha yake tangu awapoteze wazazi wake. Alihaha kila mahali kuhakikisha mpenzi anapona, lakini kote Ferndando alitembeza pesa na kuwaambia madaktari wote waseme hawezi kupona. Hatimaye alikata tamaa na kuanza kumuuguza Juliana ambaye hata chuo alishindwa kwenda, baada ya siku kadhaa akiwa anashughulika na mpenzi wake ndipo Fernando alipompigia simu na kumweleza akitaka mpenzi wake arejewe na nafuu basi aendelee kufanya kazi ndiyo atapewa dawa ya kumtuliza.

Hakuna na la kufanya zaidi ya kukubaliana na hilo, aliendelea kumtumikia huku akilipwa kama kawaida. Akifanya hizo kazi hakujua kama kuna kifaa kipya kimeagizwa kutoka mashariki ya mbali, alikuja kumaizi hilo baada ya kumshuhudia komandoo wa kirusi alipokuja kukaimu nafasi yake na yeye akaambiwa hana chake aondoke. Dawa hakupatiwa na aliendelea kumuuguza Juliana hadi alipokuja kufariki baada ya kujifungua mtoto na kiume.

Hasira zake baada ya tukio hilo, alianza kuzionesha kwa Fernando kwa kuharibu biashara mbalimbali. Jambo ambalo lilimkwaza tajiri yule akajikuta akimkamata na kumchoma sindano ya sumu ileile iliyompelekea madhara Juliana. Hiyo ndiyo ukawa mwanzo wa Justine kuua kila daktari aliyekuwa akimfuata na kumwambia kuhusu tatizo lake. Hali yake ilizidi kuwa mbaya kadri siku zilivyokuwa zikienda, hakuwa na msaada tena ingawa fedha zipo. Kipindi hicho ndiyo alijuta haswa kumfanyia kazi Mlatino yule.

Hali ilipokuwa tete ni JD ndiye aliyenunua kiasi kikubwa cha dawa za sumu ile ziweze kumsaidia. Ndipo akaweka kusimama tena imara na kufanya shughuli zingine, hasira zake alianza kuua kila daktari nchini humo. Vyombo vya dola vilipomwandama alianza kuishi kama digidigi huku mwanae akimwacha kwenye kituo cha kulelea watoto.

Maisha yake yalipokuwa ya namna hiyo Luciana alianza kujiona na hatia kwa kile alichokifanya lakini hakuwa na namna ya kumwomba msamaha. Alibaki na siri ya kuwa chanzo cha kufanya awe vile, ila hakujaribu kumwomba radhi kwa kuhofia maisha yake.

Jus alipoona mambo si mazuri mwaka mmoja baadaye alitoroka na mwanae, alienda hadi Meksiko napo alifanya hivyohivyo kwani akili ilishatibuka. Hakuwa akiwapenda madaktari, maana wao ndiyo chanzo cha kutotibiwa Juliana mapema kisa walipokea rushwa wasimtibu. Sumu aliyowekewa marehemu mpenziwe ni kiasi kidogo mno, ila kuchelewa kutibiwa kukawa ni chanzo cha kutopona. Aliyowekewa ikawa ni nyingi kuliko. Hii ndiyo ikawa sababu ya yeye kuua kila daktari, alifanya hivyo kwa nchi nyingi hata mdogo wake alipokuja kujua hivyo akaanza kumuwinda kila alipoenda na ukawa ndiyo mwanzo wa kungia Tanzania.

++++

"Jus nikupe pole sana kwa yaliyokupata, kiasi kile alichokudunga Fernando hakina dawa hata. Salama yako ni dozi hiyohiyo", JD alimweleza ukweli baadaye kusikiliza kisa chote cha Justus.

"Pole sana, vipi mwanao yupo wapi hivi sasa?", Husa naye alitoa pole na kumuuliza kuhusu mtoto wake.

"Mwanangu Paul kwa sasa yupo hapa hapa Tanzania, nimeamua nimuweke shule ya Bweni nikienda kumwona mara chache tu. Sasa fikirieni jamani, bila hongo za madaktari leo hii mama yake si angekuwepo. Ndiyo maana nawaua tu kwa kauli zao, maana maneno waliyokuwa wakimpa Juliana ni mabaya mno"

"Nafikiri umejua wazi Fernando si mtu mzuri, mimi unavyoona hivi hajui nina makazi sehemu gani na nimeamua kuaga tu naenda nyumbani kusalimia ndiyo hivi jumla. Anachojua kwetu ni kulekule, ndiyo maana nikarejea nchini niishi kwa amani", JD alisema.

"Yaani nisingewasikiliza nyinyi hivi sasa ningekuwa nipo mbali na familia yangu. Najuta haswa, ila sitokaa chini hadi nihakikishe hawa madaktari wanashika adabu. Luciana ni mfu, na pia Fernando nammaliza"

"Kwa sasa nikwambie tu huwezi kummaliza Fernando, watu wenye uwezo kama wewe amewaongeza ni wengi mno na ndiyo wanaomlinda. Fikiria jingine labda kumuua Gasper mtoto wake au Luciana chanzo cha matatizo. Tena sasa hivi baba yake ni mstaafu na yeye anaishi Fiji ni kazi rahisi mno" JD alishauri.

"Sawa, ila JD ilikuwaje hadi ukawa mtumwa wa yule mzee?"

"Nilizaliwa huku, ila kwa mama yangu ni upande mmoja wa familia yake ni wa kule. Nililetwa huku na kuja kuishi, ila mzazi wangu naye hawana tofauti na Fernando si nikajifunza mbinu mbaya za kivita. Nilipokwenda kule akaniwekea mtego na kuhitaji kufanya nami kazi kilazima. Kizuizi ni familia ya mama yangu, ilinibidi nijiunge naye wakati kule nilikuja kusoma tu na huku nimeacha mtoto tena mgonjwa na mwanamke anayenisubiri. Yaani Mzee yule hakujali hilo, familia ya mama yangu ilikuja kufariki yote kwa ajali ya meli, ila nliendelea kufanya kazi kwake hadi akawa anaamini siwezi kutoroka. Nilpoomba likizo nipumziko ndiyo jumla kama hivi, yule mzee hukutakiwa kumwambia kama unahitaji kujitoa ni kosa kubwa hilo", JD alieleza.

"Nafikiri mashetani ya kwetu yaliniamsha mapema nikakimbia, siwezi nikaakaa eneo nililoshuhudia wenzangu wakichinjwa na kuteswa kikatili", Avi alisema.

"Tena wewe ndiyo alikutafuta haswa, maana hajapata dereva kama wewe hadi leo hii ninavyoongea. Pengo lako lipo kule, wapo madereva lakini si wa kukufikia wewe", JD alisema.

________________


Wakina paki hatari hiyo walipooona iliwabidi wawahi, kwani pamoja na eneo hilo kutokuwa na mamba ila haikuwa ngumu kwa wao kutofika hapo waonapo kitoweo tu. Jamal hakuweza kuzama majini, kutokana na koti la kuelea alilolivaa. Aliendelea kuwa juu huku wengi wao wakipiga mayowe kwa hofu. Boti zilikuja kumzunguka kwa pamoja na kumuweka kati.

Oze kwa haraka alinyoosha mkono na kumwambia amshike, Jamal alitii na kumvuta hadi kwenye boti yao. Hofu waliyokuwa nayo watu hapo, hakuna aliyeweza kutaka kuendelea kufurahia. Maana Ngwena takribani sita walifika, ila waligeuza kurejea kule wanapokaa maana hawaishi kwenye kina kirefu cha maji kama hiko. Laiti kama wangelichelewa kidogo, basi ndiyo ingekuwa ni mwisho wa Jamal. Maana viumbe wale wala nyama wangemng'ata na kumzamisha kwenye maji tu, walivyo wengi wangemshambulia mno.


*HABARI YA JUS TUMEIMALIZA
*JAMAL AKOMBOLEWA, ATALITAFSIRI VIPI TUKIO HILO?





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA______

.............Maana Ngwena takribani sita walifika, ila waligeuza kurejea kule wanapokaa maana hawaishi kwenye kina kirefu cha maji kama hiko. Laiti kama wangelichelewa kidogo, basi ndiyo ingekuwa ni mwisho wa Jamal. Maana viumbe wale wala nyama wangemng'ata na kumzamisha kwenye maji tu, walivyo wengi wangemshambulia mno.


_________TIRIRIKA NAYO

Alipofika ufukweni alishuka pasipo kushushwa kwenye chombo kile huku nguo zake zikiwa zimelowa, kutokana na kutumbukia upande wenye kna kirefu tena Akiwa hana hili wale lile. Alijikuta akichachawa na kuanza kutembea hovyo pindi alipokanyaga ardhi. Oze na Paki walikuwa na kazi ya kumfuata huku wakiwa wameongozana na mmoja wa wasimamiz wa hifadhi.

Hali aliyoionesha Jamal ni wazi angeweza kufika eneo lenye wanyama wakali ndani ya mbuga hiyo. Walimfuata kwa nyuma huku kijana huyo akienda ndanI zadi ya pori, walIkaza mwendo kuweza kumfikia kwani kuokoka kwenye kifo haikuwa jamBo la mzaha hata kidogo. Kwa mtu wa kawaida akili akiendelea kuliwaza lile, basi kunaweza kumletea jambo jingine lolote lile.

Jamal alIkaza mwendo lakini Alifika mahali akaanza kutembea kivivu, hapo ndipo wale waliyopo nyuma yake wakamuwahi. Mwondoko mpya aliyoubadili nao hata haukudumu, akaanza kwenda kinamna nyingine. majira hayo alienda mithili ya mlevi na hakufika mbali alianguka chini akapoteza fahamu. Paki na Oze walifika upesi hapo na kuanza kumtingisha, ila hakuleta mrejesho wowote ule zaidi ya kutulia kama alivyo.

"Kwani ana nini?", Msimamizi wa hifadhi aliwauliza huku akiwapa ishara wenzake ambao wapo mbali.

"Kuokoka kule ndan ya maji si mchezo kabisa, lazma hali iwe namna hiii kwa huyu", Oze alijibu kisha akamtazama Paki na kumwambia, "Hebu mtoe hilo booya kifuani apate hewa fresh, we gemu fanya mpango wa gari haraka sana awahishwe kwa Dokta haraka mno"

Koti la kuzuia asizame walimwondoa, kisha wakaanza kumpepea kumpatia hewa nzuri. Hali ilipoanza kuwa si nzuri Paki alimbeba kwa haraka kuelekea kule ambapo gari lililotumika kuwachukua kuja jirani na mto lipo. Walifika eneo ambalo wanAfunzi wapo napo wao ndiyo walipobaki mdomo wazi, baada ya kumuona kijana yule akiwa na hali mbaya namna ile. Waliuliza maswali lakini hakuna aliyeweza kujibu, waliwahi kumpandisha kwenye gari.

Muda huohuo kukiwa na pilika na kutaka kuokoa maisha yake, gari la wagonjwa waliliwasili hapo na kulazimu ahamishiwe mule kwa uangalizi zaidi na si kuwekwa ndani ya gari la kawaida. Yakifanyika hayo, baadhi ya mabinti walianza kulia kabisa kwani muda mchache waliyokuwa naye walimwona akiwa ni yu mzima wa afya.
____________

Macho alikuja kuyafumbua baada ya takribani saa moja toka apatwe na giza, alijikuta kiwa yu ndani ya mandhari mpya. Aliangaza kila upande kuweza kung'amua kama aliwahi kufika hapo, ila hakuweza kupatwa na ufahamu wowote kuhusu uenyeji wa mazingira hayo.

Ndani ya wodi ya kawaida, ambayo wala hakuwahi kufika kabla. Jamal aliangaza vizuri ndani ya chumba hicho. Ndipo akamaizi kuwa pembeni ya kitanda kuna binti mrembo aliyelala huku ameficha uso wake na kuweka kichwa chake tu chenye nywele ndefu. Alimwangalia mno huku akivuta kumbukumbu ni wapi aliweza kumwona, sekunde kadhaa baadaye kichwa kilipoweza kuwa imara ndipo alipoweza kumtambua yule mtu ni nani.

Alijikuta akimshika nywele zake huku akitokwa na tabasamu hafifu, hali hiyo ilifanya binti huyo ainuke pale alipolala. Hakuwa mwingine ila ni Heriety ambaye alipeleka macho kwake, alijikuta akiingiwa na uso wa furaha.
"Nipo hapa kwa muda gani?", Aliuliza.

"Ni saa moja limepita tangu uwe hivi", Heriety alijibu na kupelekea kijana huyu alitazame dripu alilotundikiwa.

"Alhamdulillah, siku ya leo sitokuja kuisahau kwenye maisha yangu. Ningeweza kugeuka chakula cha viumbe wale wa kwenye maji. Kila nilipotoka kwenye maji nikawa ninawaza mno, nilikiona kifo kipo mbele yangu kabisa tena kibaya"

"Jamal shukuru Mungu tu upo sawa, Gina na Luka utani wao ndiyo umepelekea haya. Alishtuka akakugonga wewe ndiyo ukaingia kwenye maji"

"Ok tuliache hilo, naomba niitiwe Oze na Paki haraka sana", Jamal alisema na kupelekea Heriety atoke nje upesi, muda mchache baadaye aliyoagizwa waje waliwasili hapo wakiwa wanyonge mno na si wachangamfu. Alipowaona aliachia tabasamu tu wala hakujali hali waliyokuwa nayo, nao walionesha uhafifu wa bashasha nyuso mwao.

"Dogo unajua kile kichangu mnachosoma nacho kinahitaji kishikishwe adabu hakuna namna nyingine", Oze alisema.

"Ozee, potezea tu hakuna haja ya vitu hivyo hapa unajua sisi ni waalikwa tu fikiri itakuwaje kama kukijengeka picha mbaya kwa binti yule"

"True, anachosema dogo ni sawa. Tupotezee tu ila hakikisha Bosi hajui kuhusu hili, atatufanyia kitu kibaya kwa kutopanda nawe boti moja", Paki alisema.

"Hili litaishia hukuhuku halitofika"

_________


Habari ya kuamka kwa Jamal ililetwa kwa wazazi wa Heriety pamoja na mabinti wengine ambao walikuwa na shaka juu yake. Wengi hadi muda huo bado walikuwa wakimshukia Gina kutoka na kusababisha yote hayo, haswa baada ya kuendeleza mchezo wake na kijana Luka. Heriety ndiye aliyejaribu kutetea ili aonekane ni bahati mbaya lakini kuna baadhi hawakuwa wamemwelewa, kutokana na ushawishi wake ilibidi waache kumlaumu tu.

Binti Luigina kama kulia alilia mno kwa kusemwa na wengine ila haikuweza kubadilisha hali halisi. Alipoweza kusikia ameamka hakutaka kuweka giza alitaka kwenda kuongea naye kusisitiza zaidi ni kuhitaji kuonana na Jamal. Heriety alimsihi atulie kwanza apumzike, hakutaka kusikiliza na kusihi anataka kuonana naye ili asijihisi ni mwenye hatia.

Ilibidi mabinti hao waliyopo kwenye nyumba za kukodi ndani ya hifadhi, watoke hadi kwenye zahanati aliyolazwa Jamal ili wakamwone. Walifika wakakuta wazzi wa Heriety ndiyo wapo ndani, na waliambiwa wasubiri mahala hapo. Muda mchache baadaye Job Kabari na mke wake walitoka ndani ndipo nao wakaingia kumwona, walimkuta tayari dripu likiwa limeisha na yupo kwa ajili ya kupumzika tu. Waliongea maneno machache ndipo Gina naye akaomba kuongea naye, hilo halikupingwa na wote walitoka nje kumpisha akabaki na wapambe wa kijana yule.
"Una kipi cha kusema?", Jamal aliuliza akiwa hana uso wa furaha.

"Jay please naomba usinielewe vibaya ilikuwa ni bahati mbaya tu, utani wa Luka ndiyo umepelekea yale. Nisamehe", Gina alisema.

"Gina"

"I'm sorry Jamal"

"Naomba unisikilize, kile nilichokwambia usiku ule kariri ndiyo kipo moyoni wangu. Sijawahi kuchukia mtu kabla jua wewe ndiyo wa kwanza kutokea nikawa na chuki moyoni mwangu. Usifikiri hao majamaa waliyopo hapo ni watoto wadogo hadi wasielewe kile kinachoendelea. Nakuomba toka, sitaki niongee na wewe chochote"

"Jamal"

"Oze hebu mwoneshe ulichorekodi", Jamal alimwambia Ozee aliyekuwa yupo pembeni yake, mpambe yule bila kukawia alitoa kamera ndogo ya kurekodi picha za video na kumpatia Gina aitazame.

"Tazama na utujibu kama bahati mbaya ulikuwa ukiambizana nini na huyu Jamaa huku ukimtazama Jay kwa jicho la kuibia kutazama ni wapi alipokaa. Umepeleka jicho pembeni mara tatu wewe, ndipo ukaambizana naye akakutekenya tena umeruka kwa kuigiza kabisa", Paki alimwambia huku uso wake ukiwa hauna mzaha.

"Ulidhani kila mtu ni mwenye akili kama zako, nakuomba uondoke wewe. Unajaribu kuniua kabisa"

Gina kufikia hapo cha kuongea chenyewe hakuwa nacho, aliondoka huku uso akiwa ameuweka chini kiaibu. Siku hiyo ikawa ni mara ya kwanza kumsikia Jamal akiongea kihasira, jambo ambalo lilimwashiria alimaanisha kile anachokisema.

Binti huyu hakujua kama alipanga mpango ambao ni wa kufikirika mno, hata wenye akili ya kuchanganua matukio wangeuona ni wa kitoto mno na hauingii akilini hata. Yeye na Luka ndiyo watu waliyoamua yote hayo, shida yao wamsukume tu Jamal ndani ya maji eneo hilo. Walishafikia hatua ya kutaka kumuua tu kisa chuki zao, tena walitaka afie kwa kuliwa na mamba maana kufa maji isingewezekana kutokana na koti alilovaa.

Kupanda naye boti moja, ilikuwa ni sehemu ya hila yao. Ili tu walichokipanda kitimie. Hawa ndiyo chanzo cha kujaa nafasi kwenye chombo kile hadi Oze na Paki wakakosa nafasi ya kuwa naye karibu. Muda ambao wakiingia walipelekea msongamano mubwa mno na walinzi wakajikuta wakikosa nafasi wakaingia chombo kingine. Kufikia hatua hiyo walijiona wamefanikiwa mno kuweza kutimiza sehemu ya azma yao.

Hawakujua kama wanacheza na watu wenye akili zao, walidhani hawaonekani kutokana na umbali wa boti hizo uliyopo lakini kumbe Oze alichukua kamera akaivuta hadi eneo ambalo yupo Jamal akawa anatazama kila kinachoendelea. Mpambe yule aliamua kufanya hivyo kwani ingetokea lolote lile kubwa, basi awe na namna ya kujitetea kwa bosi juu ya hali hiyo. Siku zote watu husema ukizibiwa njia ya kutokea shimoni, basi toboa tundu jingine. Ndiyo alichokifanya mtu huyu, Gina na mwenzake hawakulijua hilo walidhani wameshafanikisha kila kitu.

Gina muda ule alianza kuongea na Luka na kupanga namna ya kuanza mpango wao, tayari walishafanikiwa hadi kukaa naye karibu. Hapo ndipo wakaanza kwa binti kumtekenya kijana, jambo ambalo watu waliona ni la kawaida kumbe una jingine lililokuwa limesukwa. Ilipofika muda wa kutekenywa kwa Gina ndipo walipokosea kwa kuatazama upande aliyopo Jamal ili waweze kuchukua hatua. Hapo ndipo Oze alipoweza kujua ulichezwa mchezo, tena kuondoka bila hata ya kujitetea ndiyo kabisa alionesha ni mwenye kuhusika na kila kitu.

______________

Sherehe ndani ya hifadhi iliisha salama, hakukujitokeza jambo la hatari jingine. Gina alishajua ulinzi wa namna gani uliyopo kwa kijana yule, aliambizana na mwenzake na kuamua kutulizana wasifanye lolote lile. Walirejea jijini kila mmoja siku ya jumatatu ambayo ni siku ya mapumziko, hakukuwa na vipindi shuleni.

Siku zilienda hatimaye mwaka wakawa wanaumaliza wa kiamsomo shuleni Tambaza, mahafali ya kidato cha sita yaliandaliwa shuleni hapo. Baada ya siku kadhaa yalisherekewa, mwezi mmoja baadaye kufanyika mtihani wa taifa huku wanafunzi wa kidato cha tano wakifanya wa kumaliza mwaka. Siku chache baadaye likizo ikachukua nafasi yake, huku wanafunzi wa kidato cha sita wakirejea makwao.

Kipindi hiki ndipo Alice alipoweza kurejea nyumbani baada ya upweke wa muda mrefu mno, napo alifika akitarajia angeweza kumkuta Jamal yupo jijini. ila haikuwa hivyo, kijana hakuwepo alikwenda mkoani kuimalizia likizo huko. Jambo hilo lilimuumiza mno akawa ni mwenye kuwasiliana naye tu kwa kutumia simu, pasipo kuipata nafasi ya kuonana naye.

Alice aliumia mno kutokana na hali hiyo, aliendelea kunung'unika kila siku kwenye maisha yake kwa kumkosa Jamal. Pamoja na hayo hakutaka kuendelea kukaa na kitu moyoni, aliamua kumweleza kila kitu kuhusu moyo wake ulipo kupitia simu. Alitarajia kuweza kupata jibu zuri, ila alichokutana nacho ni kilekile ambacho kiliwahi kumpata Hadija.

Eti Jamal ana mtu wake, wakati dada yake alimwambia hapaswi kuwa ndani ya uhusiano yule. Aliweka alama ya kuuliza mahala hapo, huku akihisi kuna mmojawapo ni mwenye kumdanganya. Kutokana na imani yake kubwa kwa kijana yule hakuhisi kama anaweza kufanya hivyo, akawa ameweka shaka kwa dada yake ambaye mara nyingi mno ni mwenye kutumia nguvu kuhusu suala hilo.

Binti akajiapiza ataenda alipo Jamal hata kwa gharama gani, alipanga mpango wa kwenda hukohuko na kumweleza kile alichoambiwa na anachomweleza yeye. Aliona hiyo ingeweza kuleta nafuu walau ya kuweza kupata tulizo. Kusafiri kutoka hapo jijini hadi mkoani, kungeweza kumfanya Jamal aone ni namna gani anapendwa.

Alifanya mipango ya chinichini ya safari yake, akijianda ili siku amchoropoke dada yake akiona liwalo na liwe. Ila hawezi kumkosa, alifanikiwa kuweka nguo zake muhimu na baadhi ya vitu hivyo kwa ajili ya safari muhimu. Pesa anazopatiwa nazo aliona zingemtosha kuweza kufanya safari kama hiyo, aliendelea kuwa msiri mno na mara nyingi akiwa amebadilika tabia kuliko hapo awali.

Hakujua kufanya hivyo ni kuanzisha wasiwasi mwingine kwa dada yake, ambaye alianza kuhisi hamwelewi tangu arejee likizo. Kutokana na hilo aliamua kuongea na mwanajeshi aliyopo chini yake ambaye aliwahi kumleta taarifa za kitu chochote kigeni anachokifanya mdogo wake. Alice hakujua kumhadaa mtu alitakiwa awe kama alivyokuwa hapo, akili yake iliwaza kuficha hilo na hakuelewa ni namna gani aliweke sirini. Hapo ndipo alikosea, nyendo zake Doreen akaanza kuzielewa.

Siku ya kwenda kukata tikiti kituo cha mabasi, kumbe alishaonekana na Pandikizi aliyowekwa. Alipotoka ofisi za basi la Raha leo Ubungo, mfuata nyendo aliingia kwenye ofisi na kujitambulisha na utaka kujua lichokuja kukifanya binti huyo ni kitu gani hapo. Alielezwa kila kitu, alipeleka taarifa moja kwa moja kwa Doreen ambaye majira hayo alikuwa yupo ofisini kwake. Alimwambiwa mtu yule aendelee kumfuaili hadi atakaporudi nymbani, kisha atoe taarifa, Doreen aliendelea kusubiri hadi pale alipopokea simu kutoka kwa askari jeshi yule.

Habari hiyo ilimfanya aingiwe na hasira mno, alijikuta akirudi nyumbani na kuacha kazi, kitu cha kwanza kukifikia ilikuwa ni kumpiga vibao mdogo visivyo na idadi.
"Dada nimefanya nini mbona unanionea?", Alice aliuliza huku akilia kwa uchungu.

"Wacha niendelea kukutandika utajua ulichokifanya ni kipi", Doreen alisema huku akizidi kumpiga vibao.

"Dadaaa! Si bora uniambie tu kosa langu ni lipi?"

"Mtu gani wewe usiyosikia, ahaya niambie ni tiketi uliyokata gari la Rahaleo unaenda wapi?"

*AARGH! GINA CHUKI GANI HIZO?
*VIPI GINA ATAISHIJE AKIMWONA JAMAL?
*ALICE KUPENDA NAPO KAGUNDULIKA, JE KIPI KITAMTOKEA?





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

_________SEHEMU YA ISHIRINI NA SABA______



"Dadaaa! Si bora uniambie tu kosa langu ni lipi?"

"Mtu gani wewe usiyosikia, ahaya niambie ni tiketi uliyokata gari la Rahaleo unaenda wapi?"


_____________TIRIRIKA NAYO

Swali hilo lilimfanya Alice abaki kimya asijue cha kujibu, alishaelewa wazi mpango wake umeviza. Hakujua imekuwa namna gani hadi kikawekwa wazi kila kitu, mwanzoni alijiona ni mwenye siri kumbe ndiyo kwanza anajianika.
"Si nakuuliza wew toka lini ukasafiri wewe kwenda mkoani, una ndugu gani huko? Hadi ufikie hatua ya kutoniaga, Jamal siyo ndiyo anakufanya ufanye haya yote!" Doreen aliongea kwa ukali.

"Dada ulitegemea nini sasa kama si mimi kufanya uamuzi huo, yaani umeamua kuniweka mbali naye na hata kumfanya aondoke mjini hapa"

"Alice wewe mtu gani usiyesikia wewe, nikwambie mara ngapi Jamal utamletea matatizo mbona huelewi. Mabinti nawajua nyinyi nimepitia umri kama huo, ukioneshwa unapenda wewe unafikiri itakuwaje kama si kuanza mengine"

"Matatizo yapi kwani Jamal hapendi? Yaani dada yangu wewe uliyenilea ndiyo umefanya yote hayo, haya yupo na mwanamke mwingine mmefurahi? Jamal sasa hivi anampenda mwingine, huyo ndiye hawezi kumletea matatizo?", Hilo lilikuwa ni suala jipya kwa Doreen, alijikuta ukali wake mwenye ukImwisha. Alimtazama mdogo wake kwa kutoamini hayo anayoambiwa, aliganda namna hiyo.

Alice kuzidi kuonesha kile anachokisema ni sahihi, alinyanyuka na wenda kuitwaa simu yaKe kisha akaileta hadi alipo Doreen na kumwonesha. Afisa huyu wa jeshi aliipokea simu na kuanza kusoma jumbe moja baadaya nyingine ambazo Alice na Jamal wamekuwa wakitumiana. AlijIkuta akikaa chini kabisa akiwa haamini kile anachokiona, yaani nguvu kubwa aliyoitumia kuzuia hilo na bado linatokea kwa mwingine. Tena maneno ya kijana yule alikuwa ameyapangilia haswa, kiasi cha kufanya yeyote yule aamini kile kisemawacho ni ukweli mtupu.

Alice aliinuka na kumtazama huku machozi yakiendelea kumtoka kwa uchungu, Doreen alijikuta akishindwa hata kumtazama mdogo wake usoni. Kumpiga kampiga kwa suala kama lile, mbaya zaidi alichokuwa akikihangaikia ni kazi bure tu.

"Ndiyo asiyetakiwa kupenda huyo?", Alice aliuliza huku akiendelea kulia.

"Yaani dada yangu mwenyewe ndiyo umekuja kunifanyia haya, siamini hata kidogo na sitokaa niamini. Sijawahi kuona ndugu wa damu mwenye kufanya jambo kama hili na leo ndiyo mara ya kwanza, I hate you", Alice aliendelea kulalamika, dada yake alikosa hata la kusema.

"Umenipeleka shule ya mbali, umenifanya niishi kifungoni. Hivi mimi sina haki ya kupenda dada? Mbona wewe ulipenda wakati ukiwa upo shuleni kabla hujakutana na mjomba wake Jamal. Utaanzaje kunizuia mimi kukatiza njia ambayo uliikatiza wewe na haikuharibu malengo yako? Kama si ubinafsi ni nini huo, tena kwa ndugu yako wa damu. Its shame to call you my sister", Alice alizidi kuongea kwa uchungu huku akilia, muda huohuo Doreen alijikuta akiinuka huku machozi yakimlenga kwa maneno aliyoambiwa. Alimsogelea ila ili amshike ila mdogo aliwahi kwa kumkwepa kama vile ni mwenye ukoma, tena alisogea kando hakujali macho ya huruma aliyokuwa akitazamwa na dada yake.

"Naomba usinisogelee kabisa", Alice alisema.

"Alice please", Doreen alihimiza.

Alipojaribu kumsogelea kwa mara nyingine, alimkwepa na kukimbia kulekea chumbani kwake. Doreen alimuwahi mdogo wake akiwa na lengo ya kuyaweka sawa, maneno aliyoambiwa hata yeye yalimuuma mno moyoni mwake.

Loh! Afisa huyu wa jeshi hakujua kama mwenye kupenda ni jura, aliamua kuchukua maamuzi vile anavyojua yeye. Hayo ni madhara yake ambayo yamemfanya aumie moyoni mwake, kuambiwa maneno mazito na ndugu ambaye anampenda kupitiliza ni kidonda kikubwa mno.

Uchungu wa matamshi yale, na kufungiwa mlango alijikuta akikaa chini mwenyewe bila ya kupenda mlangoni hapo huku akilia kwa uchungu. Pamoja na ujasiri wake wa kuhimili baadhi ya mafunzo linapokuja suala la hisia, halikuweza kumwacha salama. Kulia ndiyo kulimvaa kwa kufanya maamuzi hayo, alijuta haswa alitamani hata amweleze mdogo wake hali halisi hadi akafikia kuchukua hatua hiyo.

Akiwa kakaa eneo hilo haikupita muda mrefu alisikia kishindo kikitokea ndani ya chumba cha Alice. Kutokana na masikio shupavu aliyonayo afisa huyu, alijua wazi huyo ni mwanadamu ameanguka sakafuni. Ukiongezea na hali aliyoondoka nayo mdogo mahala hapo, hofu ilimzidi mno akiwa na vazi lake la kazini bado hajalivua alisimama wima kwa haraka.

Aliita jina la mdogo wake mara kadhaa ila hakupata mrejesho wowote zaidi ya kusikia ukimya tu. Moyo ulimwenda mbio mno na kujikuta akigonga mlango kwa nguvu, hakusikia chochote zaidi ya mkoromo kusikika. Doreen alijikuta akiwa na kiwewe zaidi ana akatazama kila upande eneo la koridoni alipo, hakuona cha maana
.
Alichezesha akili yake na hapo ndipo akajua yeye ni afisa wa kijeshi, anaweza kutumia sehemu ya nguvu zake kuingia humo. Bila ya kuchelewa alitazama buti alilovaa, kisha akautazama mlango. Aliruka teke moja la nguvu akaharibu kitasa, mlango ulitii amri ukafunguka ila kwa alichojione alijikuta akiweka mikono kichwani.

"Mungu wanguuu!", Alitamka kwa masikitiko huku machozi yakizidi kumtoka, mdogo amelala chini mahali kwenye dimbwi la damu huku akiwa hajitambui.

Doreen aliingia ndani kwa kasi, alichuchumaa chini na kuanza kumtingisha lakini hakusikia chochote kile. Alikiweka kichwa juu ya paja lake, hakujali damu inayomtoka ingeweza kumchafua. Alimkagua kwa haraka ndipo akaona kuna jeraha kwenye mshipa mkubwa wa shingoni. Alichukua nguo na kuliziba kisha akamwinua, upesi alimkimbiza hadi nje ambapo kulikuwa na Askari wa kike mwenye cheo kidogo aliyekuwa akimtumia kama dereva pindi anapotoka na gari la jeshini.
"Sitaki maswali zaidi, nataka uendeshe tuwahi dispensary ya karibu", Aliongea huku akifungua mlango na kuingia upande wa nyuma akiwa amembeba mdogo wake.

_________________

Robo saa baaadaye Shehoza akiwa bado yupo kazini, alipokea simu kutoka kwa Doreen akimweleza kila kitu juu ya kilichotokea hadi kukafikia kutokea jambo kama hilo. Suala hilo hata yeye mwenye lilimchanganya, hakutarajia kama itaweza kufikia huko. Lawama nyingi alizipokea kutoka kwa mpenzi wake juu ya hilo, huku haswa kwa tabia ya Jamal. Doreen alionesha wazi amemchukia mpwa wake, kwa jambo hilo lililotokea.

Shehoza hakuona umuhimu wa kuendelea kufanya kazi, hakujali kama kuna wagonjwa wangekuwa wanahitaji huduma yake. Alichoamua ni kukabidhi jukumu kwa daktari mwenzake, aliondoka Muhimbili hadi kwenye zahanati ambayo Alice amelazwa. Kutokana na mwendo kasi aliyokuwa akitumia hakukawia kufika, ripoti nzima aliipokea kuwa amepungikiwa damu muda huo ndiyo anawekewa.

"Shehoza ndiyo mambo gani haya? Jamali pamoja na kumwamini kote kule amekuwa mwongo hadi kufikia kufanya haya. Kama ana mpenzi kwanini asiseme tu tujue ili nimwambia huyu mdogo, hivi unajua huyu ni totally blind juu yake. Sasa ule mpango mdogo wangu mwenyewe ananichukia akiona mimi ndiyo chanzo hadi akawa amepata mwingine. Unajua ni hatari kiasi gani?", Doreen alisema huku machozi yakimtoka.

"Naomba unisikilize kwa umakini mpenzi, Jamal anapaswa kulaumiwa tena sana ila si kwa hilo unalosema wewe. Na sisi naweza kuona hadi hivi sasa tumekosea", Shehoza alisema.

"Unasemaje?!"

Shehoza aliwamua kuweka viganja vyake mashavuni mwa Doreen na akasema, "Kosa kubwa la Jamal ni kusema uongo tu, katumia uongo kuficha hali yake na sisi tukatumia mwingine kuficha hili suala litokee. Hapo ndipo tulipogongana, He is not in love hii ni hila yake na anaitumia mara nyingi mno. Tukiri tulichanganya mahesabu wote katika hili"

"Unafikiri tutafanyaje, mdogo wangu mwenyewe ananichukia mimi akiniona ni mbinafsi kwake. Unajua nimeamini hivi sasa huwezi kumkataza mtu kitu ambacho uliwahi kukifanya wewe hukupata madhara, nilitumia msemo wa fanya ninavyosema na si kama nilivyofanya"

"Cool down, kila kitu kitakuwa sawa. Mdogo wako atakupenda kama kawaida wa kuliua jambo hili likarudi kama kawaida ni mmoja tu ten anatakiwa aje kabla hajaamka", Shehoza aliweka kituo na akaendelea, "Jamal tu na si mwingine, yupo na kina Paki huko sasa inabidi arejee jijini upesi sana"

"Unajua wazi kusafiri kutoka Tanga hadi hapa ni masaa karibu matano. Unafikiri akiamka itakuwaje Shehoza?"

"huo ni usafiri wa kutumia gari tu, kwa ndege ni nusu saa tu atakuwa Airport"


Ilibidi kwa pamoja wapitishe uamuzi wa kumleta Jamal jijini, mpango ulipangwa kwa kuongea an walinzi wanaomlinda. Suala la nauli halikua tatizo na kwa pamoja walilifanikisha hilo, wakawa wanasubiri kwa hamu Jamal aweze kufika mjini.

____________

Ama kweli sikio la kufa, halisikii dawa. Pamoja na kufanyiwa yale na Kelvin, Gina hakuwa amekoma. Pale alipojiwa na kijana yule akiwa na shida kubwa ya jimai,kwake aliona ni wasaa huo umekuja. Hakuona hasara kumpatia mwili wake, alitumiwa kwa kupenda mwenyewe akiona ndiyo kupendwa huko na kila alipomaliza basi kijana huyo alikuwa ni mwenye kumwacha 'solemba'.

Akawa ni sawa na majani kwa Simba, umuhimu wake huonekana pale kukisomekana nyama tu. Ikipatikana hakuwa na tija tena zaidi ya kusahaulika, alijipa moyo huenda siku Kelvin atakuja kuelewa ni namna gani anampenda na jinsi anavyojitoa juu yake Kumbe mwenzake alimbatiza jina na kumwita kiporo, hukumbukwa tu panapokuwa hakuna chakula cha kupikwa siku mpya. Humwagwa kukiwa na kipya, hakika alipotoka mno na hakujijua.

Hakujua kuwa ukuumizao, ndiyo ukufunzao. Yeye alibaki na imani siku moja kijana huyo atarejea kwenye mstari. Ndiyo maana kila mara alipomwona akija kwake basi alijua ndiyo siku imetimia, kumbe mwenzake kaja kupungza karaha za mwili wake. Hadi kufikia siku hiyo, alishatumika mno na alikuwa anaona haya kuwaambia wenzake kutokana na kumuasa dhidi ya mvulana yule. Aliamua kufanya siri juu ya hilo, kutumiwa aliamua mwenyewe, jeraha la kujitakia halihitaji pole.

Kipindi cha mapumziko akawa ni mwenye kujitahidi mno kuweza kuwasiliana na Kevi, lakini mrejesho ikawa ni kitendawili kigumu kinachotegwa kila mara. Asipokuwepo mteguaji basi hubaki hivyohivyo, hakika aliiingia kwenye maisha ambayo yeye mwenyewe hakujua ni namna gani anaweza kutoka

Mvundika changa hula mbovu daima, hakukuwa na kumkomboa binti huyu kwa matumaini aliyo nao. Mwenye imani hageuki, ndiyo maana akaendelea kuwa namna hiyo ila ni mwenye kuingia kwenye shimo refu.

Vijana wale nao waliendelea kuambizana kila mara alipoenda kutumiwa, Kevi alijisifu mno na kusema amechakaza pale. Hakujali ni namna gani anapendwa na wala ni kwa kiasi kipi binti yule anaumia. Alishawafanyia hivo wasichana wengi mno, huyo akawa ni miongoni mwao. Toka lini aliyezoa kuona chozi la binti likimbelembeleza akawa na huruma kwa mwingine, katili huanza kwa kutoweka huruma kwa mmoja. Kijana huyu alishaota mizizi kila upande, ingawa naye kupo mahali ambapo alishikwa.

_______________


Jamal aliwasili uwanja wa ndege nusu saa baadaye tangu aondoke jijini Tanga, akiwa na kina Paki aliongozana nao kwa haraka hadi wakafika maegeshoni ambapo magari yalishafikisha mahali hapo ili tu aletwe. Msafara wao ulitoka hapo na baada ya dakika takribani ishirini walifika zahanati ile aliyolazwa Alice, akiwa na haraka kupitiliza alifika hadi eneo ambalo wapo kina Shehoza ambao waliona ni ahueni kwa kufika kwake mahala hapo.

"Vipi huko ndani?", Jamal akiwa na hofu kubwa.

"Ndiyo kaamka muda huu yaani amekuwa ni mwenye kukuulizia wewe tu muda wote", Shehoza alisema.

"Da Doreen naomba nisamehe sana, sikutumia namna nzuri ya kulificha hili jambo", Jamal aliposikia maneno ya mjomba wake hakushughulika nayo zaidi ya kuomba radhi kwa Doreen.

"(Huku akilengwa na machozi) Nitaachaje kutokusamehe wewe Jamal, wewe ndiyo mwenye kuweza kiungo kati ya mimi na mdogo wangu. Hata ukamua kumuweka wazi kila kitu siwezi kukulaumu, maana utakuwa umenisaidia pia", Doreen alisema.

"Hapana sitoweza kuweka wazi kila kitu, ila nakuahidi nikitoka kila kitu kitakuwa sawa. Niachie mimi"

"Haya mlango huo hapo"

Jamal alipooneshwa mlango wa wodi aliyolazwa Alice, aliwatazama kina Paki kisha akayarudisha macho kwa Shehoza na mpenziwe. Alishusha pumzi halafu akapiga hatua kuingia ndani ya wodi, muda huo alimkuta binti akiwa anatazama dari la chumba hicho huku machozi mengi yakimtoka mashavuni mwake. Alijikuta akiingiwa na huruma, ila alibaki akijiuliza angeamua kwenda na matakwa ya kila anayempenda. Angekuwa na wapenzi wangapi? Si ndiyo mwanzo wa kuonekana ni malaya, hakuhitaji ajijengee picha hiyo kwa jamii.

Alisogelea kitanda alicholazwa binti kwa karibu zaidi kisha akaita, "Alice".

Sauti yake iliposikika masikioni kwa binti yule, ikawa ni kama vile amekurupushwa. Msichana aliinuka kwa haraka kitandani, kiasi kwamba angejipa madhara na sindano ya dripu. Jamal alikaa kwa haraka kitandani na kumzuia. Binti alijikuta akimkumbatia kwa nguvu mno huku akianza kulia, ilimbidi achukue wasaa wa kumbembeleza hadi pale ahali yake ilipokuwa sawa.

"Alice kwanini lakini? Mbona umefanya haya? Hivi ndiyo suluhisho ya yote?", Jamal aliuliza kwa huzuni.

"Unategemea ningefanya unaponiambia una mpenzi wakati kipindi tukiwa wote kwa pamoja huku hukuonekana ni mwenye mtu. Maana yake mimi kupelekwa bweni kilazima ndiyo chanzo cha yote hayo, siamini dada yngu ndiyo anaweza kufanya hayo"

"Alice! Alice! Unasema nini wewe hivi toka lini dada yako akawa ni kukufanyia hivyo wewe. Mbona unaongea kitu ambacho hukijui? Hivi unajua kuhusu mimi kuwa na mpenzi hata kabla sijamaliza kidato cha nne ninaye, analijua hilo. Yeye ndiyo kaamua kutumia njia ya kukudanganya ili asikuumize wewe ungesikia hilo. Unafikiri kuna dada gani anayempenda mdogo wake angeweza kuona hilo likitokea?"

"Jamal!"

*GINA NI MTUMWA WA NGONO WA KEVI, NINI MWISHO WAKE?

*ALICE ALAZWA KWA TUKIO ALILOLIFANYA, JE ALISTAHIKI KUFANYA HIVYO?





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



_________SEHEMU YA ISHIRINI NA NANE_______




"Alice! Alice! Unasema nini wewe hivi toka lini dada yako akawa ni kukufanyia hivyo wewe. Mbona unaongea kitu ambacho hukijui? Hivi unajua kuhusu mimi kuwa na mpenzi hata kabla sijamaliza kidato cha nne ninaye, analijua hilo. Yeye ndiyo kaamua kutumia njia ya kukudanganya ili asikuumize wewe ungesikia hilo. Unafikiri kuna dada gani anayempenda mdogo wake angeweza kuona hilo likitokea?"
"Jamal!"


__________TIRIRIKA NAYO

"Huo ndiyo ukweli hujui ni kiasi gani umemuumiza dada yako kwa kumwambia yale. Hakutaka uumie na mimi nilikuwa sijui kama amekwambia uongo ili usiumie, uliponifunulia hisia zako nikiwa Tanga nikakujibu vile nikijua unaujua ukweli, mimi ndiyo niliyeharibu kila kitu ila hukupaswa kumtamkia maneno yale"

"(Huku akilia) Noooo!"

"Hapana usifikie hivyo, keshaelewa ulikuwa namna gani hadi kufikia kumwambia maneno kama yale. Alice ukae ukijua mimi napendwa na nimependwa na siwezi kupenda zaidi ya mmoja, nitakuwa sitendi haki. Ndiyo maana nikaamua kukuweka wazi, kama nisingekuwa na mtu basi tambua ningelikupenda wewe kwa jinsi ulivyoonesha ni namna gani ulivyo na mapenzi ya dhati", Aliposema maneno hayo Alice alionekana ni mwenye kulia mno, alichukua uamuzi wa kumbembeleza.

"Jamal ni ngumu sana kuukubali ukweli ila sina jinsi, nakupenda sana kuliko kitu chochote hadi nimefikia kumwambia maneno yale dada yangu niliyekuwa naye karibu kwa kipindi chote yote kisa wewe tu na si jingine. Nakupenda na nitaendelea kukupenda tu, naomba umwambie dada yangu anisamehe tu ni hasira zile"

"Dada yako kati ya watu waelewa dunia hii basi yeye ni namba moja, alishaelewa tangu mwanzo hata kabla hajakuleta huku. Ameshasamehe pia, ataweza vipi kukuchukia ndugu yake wa damu anayempenda kwa dhati"

Jamal alifanikiwa kulimaliza suala hilo kama ilivyopangwa, Alice hakuwa na chuki zaidi ya kuwa na majuto tu ambayo nayo yalizimwa kwa maneno ya faraja kutoka kwake. Alikaa naye hapo ndani akiongea naye kwa dakika kadhaa huku akivuta muda aweze kuerejea kule nje na kuwapa taarifa juu ya kilichotokea.

Kuongea namna hiyo Jamal aliinuka na kumwambia anaenda nje mara moja, binti hakuwa na pingamizi ila alimwambia amwitie dada yake aje kuongea naye. Aliridhia na kuelekea mlangoni kwa mwendo wa taratibu, alipouvuka na kuwa nje wote waliyopo hapo walikuwa wameketi na kitendo cha kumwona. Walisimama wima kwa haraka, huku wakimtazama kwa shauku.

Kumwangalia huo kulimfanya Jamal ainamishe kichwa chini kihuzuni, jambo hilo lilifanya wliyopo hapo nje wajue kuna habari mbaya inaandaliwa kutolewa. Aliweka uso chini kwa sekunde kadhaa, alipouinua alimtazama Doreen akiwa na huzuni kubwa.

"Jamal imekuwaje?', Doreen aliuliza huku akianza kungiwa na shaka.

"Doh", Alisema kinyonge kisha akawatazama wote halafu akarejesha macho kwa Doreen halafu akasema, "na uafande wako wote uso umekuchafuka kwa machozi, sikuwahi kudhani kama mjeda na nyota anadondosha chozi hivi..... Mambo ni mukidee Alice anakuita".

Alipotamka hayo Kina Paki walianza kucheka, Shehoza mwenyewe aliingiwa na kicheko . Wote walibana midomo yao wasitoe sauti, Doreen ndiyo alijikuta akimpiga kibao kisichoumiza Jamal, masihara yake aliyaweka kila mahali na hilo ndiyo jambo lililomfanya hadi akafikia hatua hiyo

Doreen alimgeukia Shehoza na kumwambia, "Unajua huyu mpwa wako muda mwingine zinamhama kabisa" Aliposema hivyo, alipiga hatua kuingia wodini moja kwa moja kwenda kuonana na mdogo wake.

_________________

JD kwa Mwanahawa alikuwa ni mwanaume asiyesikia wala kuambiwa chochote, yupo radhi hata asipende hadi mwisho wa maisha yake ikiwa atamkosa mwanamke yule. Alimhududu kupitiliza, kitendo cha kutokubali hata kusikilizwa kwake ilikuwa ni kidonda. Ingawa hakuwa mwenye kujionesha hadharani kuwa anateswa na suala hilo, liliendelea kumuunguza tu.

Mwanae hata machoni hajawahi kumuweka kisa kutokuwa na maelewano mazuri na mama yake, hadi kufikia siku hiyo alishatumia miezi kadhaa kuhimiza ila hakupata suluhu. Alimtumia hata baba mzazi wa mwanamke yule kuweza kumfikishia ujumbe, napo haikuzaa matunda. Hataki chochote kutoka kwake anachohitaji tu ni kutomwona kwenye maisha yake na si kingine. Hakuchoka aliendelea kumfuata na kumwambia, pamoja na kuwa mwenye hadhi kubwa alikuwa radhi hata akemewe mbele za watu ila si kuona anayempenda ana kinyongo.

Hadi kufikia siku ambayo Alice alilazwa, tayari aliweza kuweka maelewqano baina yao ila si kuweza kurudisha upendo. Walikutana na kuongea mambo mbalimbali, lakini alipogusia kuhusu kurudisha moyo nyuma. Alikutana na kipingamizi kutoka kwa mwanamke huyo wa kisambaa, aliivumilia hali hiyo huku akimsihi sana ahakikishe anakutana na mwanae.

Pamoja na kufanya makubwa mengi napo aliambulia patupu kutoka kwa mtoto wake, ndiyo kabisa hakuwa akitaka hata kumwona na kuongea naye. Jambo hilo lilimuumiza mno, mama hasikilizwi na mtoto akigusia kuhusu baba yake. Aliamua kupiga moyo konde na kusonga mbele huku akiamini ipo siku mtoto wake atakuja kurejea kwake, kufikia hapo akawa ni mwenye kutumia muda mwingi mkoani Tanga akiwa na Mwanahawa.

Pamoja na hayo hakuwahi kufunguka kueleza kisa cha yote, kwani alipotaka kugusia kuhusu huko alipokuwa ikawa ni kukatizwa tu. Mwanamke alimwona anajipanga kumdanganya, kutotimiza ahadi alimwona ni miongoni mwa waongo wakubwa mno. Hakika msomali kwa mwanamama huyu, hasikii hata la mwandhini.

__________________

Maelewano na mtu na dada yake yalirejea kama kawaida, Alice alitengemaaa hali yake na kuendelea kuitumia likizo. Jamal hakurejea tena Tanga aliendelea kuwa nao huku akimkumbusha kuwa ana mtu wake na yupo mbali na nchi.

Doreen naye hakuona ulazima wa mdogo wake kuendelea na shule ile ya bweni akiamini suala hilo lilishafika tamati, aliamua kumuweka mjini akimpeleka shule binafsi. Alice alianza kuwa mwanafunzi wa shule ya sekondari ya Shaaban Robert ambayo haikuwa mbali kutoka anaposoma Jamal. Ilisubiriwa kwa hamu shule iweze kufunguliwa ili kwa pamoja wayaanze masomo, Alice aliingiwa an furaha mno kwa kuweza kurejeshwa jijini

Hatimaye shule zikafunguliwa, wote kwa pamoja wakiwa ni kidato cha sita. Waliyaanza maisha mapya wakiwa pamoja kama marafiki huku Alice akiwa haoneshi namna yeyote ya kumtaka kimapenzi Jamal. Kuwa pamoja waliongeza nguvu kwenye kusoma, huku waksihirikiana na baadhi ya wanafunzi wa shule ya Tambaza. Hapo ndipo ukawa mwanzo wa Alice kuwa na urafiki na Heriert, kwani ilifika mahali naye akahamia hosteli za Upanga eneo ambalo kina Gina wanaishi.

Hapo awali wengi walijua ni mpenzi wa Jamal, lakini kuendeleza mazoea naye ndipo wakaja kubaini ni marafiki tu. Kuishi kwenye hosteli hizo ndiyo baadhi ya wanfunzi walishuhudia Jamal akiwa anafika hapo na akina Doreen. Alizoeana na wengi hapo ila chuki yake kwa Gina haikuwa imezikwa, majira hayo hata salamu wakawa hawapeani ilihali haijawahi kuzoeleka kwa kijana huyo kuwa namna hiyo. Siri ya chanzo cha yote kila mmoja alibaki nayo moyoni mwake hakuna aliyefungua na kuisema.

Jamal hakutaka Gina achukiwe, pia binti naye hakutaka aje kuonekana ni mbaya kwa wenzake alikaa na jambo hilo moyoni. Alipokuwa akichekesha Jamal basi anapotokea Gina lazima sura yake ibadilike, ila hujirudi kimaigizo ili asiwezs kujenga taswira nyingine kwa wenzao.

__________

Kumalizika kwa nusu muhula wa masomo kulifanyika tena michuano shuleni hapo, majira hayo Tambaza darasa la PCM kukiwa hakuna mpinzani kwenye suala la mpira. Waliweza kunyakua ubingwa kwa mara ya pili mfululizo na kuweka rekodi ya kuwa darasa ambalo limewahi kutetea ubingwa wake. Siku hiyo iliisha kwa kufanyka kwa sherehe ya kuwakaribisha kidato cha tano wapya, likizo iliingia kwa mara nyingine.

Kipindi hicho Alice na Heriety walifikia hatua ya kutembeleana hata majumbani mwao, urafiki ulikuwa ni mkubwa mno baina yao na wote wakawa wanajuana ni wenye kumpenda kijana mmoja. Pamoja na maelewano baina ya watu hawa wawili hakukuwahi kutokea walau kusalimiana kati ya Gina na Alice. Hawakuwahi kukwaruzana ila walijikuta wakiwa hawaongei kwa pamoja, Heriety alijiathidi awezavyo kuweza kuwafanya wapendane lakini haikuzaa matunda.

Wote kwa pamoja nyoyo zao hazikulandana, ndiyo ikawa hayo. Laiti kama wangelikuwa wanalandana wasingelifikia huko. Walishindwa kuelewana na binti akawa hana muda wa kuendelea kuwapatanisha, alibaki kuwa rafiki wa kila mmoja tu.

Likizo ilienda ikaisha na hatimaye nusu ya pili ya mhula ikafuata, vijana waliendelea kusoma kwa nguvu na hata wakawa wanakaribia kuhitimu. Mahafali ya kdiato cha sita shuleni hapo yaliandaliwa vilivyo, mazoezi ya kuburudisha waalikwa yalianza mara moja. Wenye vipaji na vipawa mbalimbali walichukua wasaa wa kujiandaa, makundi mbalimbali ya wanafunzi walikaa wakijifua ili kuweza kuifanya siku hiyo kuwa ya kihistoria.

Jamal ndipo alipojitolea kuingia sehemu mbili kwenye mahafali hayo, mojawapo ikiwa ni kwenye kugiza. Nyingine ikawa ni kwenye kufanya vichekesho jukwaani, mazoezi yalisimamiwa vyema na walimu hadi kuweza kufikia tamati na kuongoja siku ya siku ambayo ilipangwa kuwa alhamisi ya mwisho ya mwezi januari kabla ya kuingia februari ya kufanya mitihani.


SIKU YA MAHAFALI

Mapambo mengi yalidhihirika kwenye lango kuu la kuingia shuleni hapo, shule hii siku hiyo ilijulikana wazi kuna tukio kutokana na usafi uliyopitiliza na pia uingiaji wa wageni wengi . Majira ya saa mbili asubuhi tu ilifika eneo la maegesho likawa limejaa na ikabidi uwanja wa mpira utumike kama sehemu ya kuegesha magari.

Wanafunzi wa kdiato cha tano siku hii walikabidhiwa sehemu mbalimbali ili kuifanya siku isiwe mbaya kwa wahudhuriaji. Wapo waliyosimama eneo la kupokea, wengine wakawa wanaelekeza watu mahali pa kuketi kwenye ukumbi wa shule. Kila kitu kilienda kinachovyotakiwa kutokana na kuchukua mafunzo wa siku kadhaa ili wasije kuharibu chochote.

Eneo la nje ya jengo la shule kulionekana walinzi waliyovaa suti nyeusi wakiwa wamejipanga kiustadi, kila aliyewashuhudia alikiri humo ndani kuna mzito aliyefika kwa ajili tu ya kushuhudia sherehe nzima. Haikuwahi kutokea kitu kama hicho, hata waliyowahi kuuona msafara uliyoingia na watu hao walikiri kitu hicho.

Majira ya saa nne asubuhi ndipo ratiba nzima ya sherehe hiyo ilianza, watu wote walitulia kimya. Walianza kwa dua ya ufunguzi kisha ikafuata risala ya Rais wa serikali ya wanafunzi wa shule, baadaye ikaja risala ya Mkuu wa shule. Kulipomalizika hilo ndipo ikaja hotuba ya mgeni rasmi wa sherehe, vyote hivyo vilienda kwa kufuata taratibu maalum tena kwa kujali muda.

Wanafunzi wa shule hiyo wenye kuhitimu walipangwa ukamilifu maalum, kuendana na namba zao kwenye mtihani wa taifa. Tena walitulia haswa huku nguo zao nadhifu zikiwa zinawaonesha ni namna gani walivyopendeza, hata Jamal aliyezoeleka kuonekana ni mwenye mavazi duni siku alivaa tofauti na akiwa amechana kwa mtindo aliyozeoa akiwa nje ya shule. Nywele zake za asili ambazo alizoea kuzipaka dawa zibadilike, zilidhihirika wazi ambapo baadhi ya wanafunzi walimshangaa.

__________

Upande wa wageni waalikwa, Shehoza, Doreen na Alice walikuwepo wakiwa wamekaa viti vilivyo safu moja. Wote hao walitulia ila Shehoza hakuwa akionekana ni mwenye utulivu ndani ya sherehe hiyo, akawa ni mwenye kuangalia kila mara mbele mahali ambapo mpwa wake yupo. Aliporudisha macho aliyaelekeza upande wa nyuma, hali ilifanya Doreen moja kwa moja aingiwe na shaka kuna kitu amabcho si cha kawaida kwa mpenzi wake.

"Shehoza kuna nini?', Doreen aliuliza.

"Nina hofu Jamal akaongozwa na hisi kuliko kujali siku hii", Shehoza alisema.

"Kivipi?", Doreen alipouliza hivyo Shehoza aliamua kumuuma sikio ili kuepusha Alice asijue kile kinachoendelea.

"He! Nachokushauri mtumie SMS sasa hivi maana simu yake anayo ataiona", Doreen alisema.

"Hilo ndiyo la muhimu", Shehoza alikubaliana naye akafanya kama alivyomwambia, ujumbe mfupi wa maneno aliutuma kwa mpwa wake ambaye baada ya muda aliujibu.

"Ndiyo maana nampenda sana Jamal, ni mwelewa huyu", Shehoza alisema huku akimwonesha ujumbe mpenzi wake.

"Ni muda wa kujiunga naye kwenye furaha yake sasa"

____________

Muda wa kuitwa majina wanafunzi wale waliyofaulu vizuri uliwadia, majira haya wazazi walijiandaa kwa zawadi ya kuwatunza watoto wao. Upande wa masomo ya sayansi ndiyo ulipewa kipaumbele kwani huo huanzwa daima hata kwenye upangaji namba hapo shuleni, wote walitulia kimya kusikiliza mwenye kuitwa ni nani.

"mwanafunzi aliyefaulu vizuri kwenye somo la fizikia si mwingine ni Jamal Mdoe", Mshereheshaji aliposema hivyo wengi walipiga makofi, muda huo Jamal aliinuka kwa haraka na kwenda kupokea zawadi yake, alipokuwa akirudi tayari kina Shehoza walishafika hapo na kumvalisha mataji.

Zawadi ya kufaulu vizuri somo la hesabu, aliitwa tena akaichukua zawadi aiporejea kwa maajabu Dokta Aesop, Mama Gina na wazazi wa Heriety walinyanyuka na kumvalisha matajia na kumpa zawadi nyingine. Kutokea kwa hilo hata Gina mwenyewe alishangaa, alijikuta akibaki mdomo wazi baada ya kumwona babu yake naye aiinuka kuungana na mzazi wake.

Zawadi ya somo la kemia napo ilichukuliwa na yuleyule, kufanya vizuri kwenye masomo ya mchepuo wake. Akiwa anaelekea kukaa ndipo ukumbi mzima uligeuza macho nyuma, walinzi wenye suti nyeusi walisogea zaidi mbele alipo na kumfanya kijana huyo asimame ghafla.

Watu kwa macho yao walimshuhudia kibosile akija mbele huku akitembea kwa haraka, alipofika alimvalisha taji kisha akampatia kasha lenye zawadi. Baada ya hapo alikumbatiana naye, yakitokea hayo hata Mshereheshaji mwenyewe alinyamza kimya huku akitazama.

"Mr Jamshid!" Jamal aliita huku akionekana si mchangamfu.

"Una haki hta ya kuniita JD, its ok", Hakuwa mwingine ila ni JD aliyasem hayo huku akikumbatiana naye, alipomwachia alirejea alipoketi.


*JAMALI NA JD, KULIKONI?
*GINA ADUWAZWA NA MAMA YAKE PAMOJA NA BABU YAKE, KULIKONI?








ITAENDELEA!!!
 
Kaka Hassan aliyekuteka akuachie jamani tunakuhitaji huku
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA ISHIRINI NA TISA______




"Mr Jamshid!" Jamal aliita huku akionekana si mchangamfu.

"Una haki hta ya kuniita JD, its ok", Hakuwa mwingine ila ni JD aliyasem hayo huku akikumbatiana naye, alipomwachia alirejea alipoketi.



_________TIRIRIKA NAYO

Zawadi zingine ziliendelea kupokewa huku wengi wakiwa wamebaki na ujio wa JD eneo hilo, hadi afikie ampe zawadi Jamal. Hakuna aliyeweza kuwapata jibu la maswali isipokuwa mhusika mwenyewe, vilevile hakuna aliyetuhubutu kumsogelea msomali yule na kumuuliza kuhusu hilo. Wengi wanamhofu kutokana na jinsi anavyotembea na ulinzi mkubwa, hata anavyojulikana kutokana na familia aliyotokea.

_____________

Dokta Aesop na Mama Gina waliporejea kitini kila mmoja alikuwa naswali la kumuuliza juu mwenzake. Hakuna asiyetaka kujua sababu iliyompelekea hadi akafikia hatua ya kwenda kutoa zawadi kwa Jamal, walipoketi kitini kila mmoja alimtazama mwenzake huku nyuso zao zikiwa na mishangao.

"Baba na wewe unafahamu huyu?", Mama Gina alisema.

"Haswa namjua vilivyo kijana huyu, nitakueleza kwa kituo jinsi nilivyomjua", Dokta Aesop alisema huku akipeleka macho mbele ili asiweze kupitwa na kinachoendelea.

Ilimbidi Mama Gina atulie kimya ila alitaka kujua haswa, ukimya uliendelea kati yao na kila mmoja akawa yupo mbele kushuhudia kinachojiri. Ugawaji wa zawadi uliendelea kama kawaida, hadi ilipoisha suala hilo. Kisha ikaingia kutunukiwa vyeti wahitimu, wazazi mbalimbali walijumuika katika kuwapa zawadi vijana wao hadi kuliposiaha hilo ndipo ratiba nyingine ikafuata.

Waliingia wachezaji ngoma wao walionesha ujuzi wao hadi pale muda wao ulipoisha, baada ya hapo ndipo walipoingia waigizaji huku Jamal akiwa ni mmoja wao. Muda huo amebadili nguo za kuvaa zingine, alionesha uwezo wa hali ya juu kwenye fani hiyo kiasi cha kuwakosha wengi. Kutokana na jina lake kuwa kubwa ilipelekea wengi awape umakini, kwa jinsi nafasi aliyoicheza ndani ya sehemu hiyo ndipo akajikuta akibadilishwa jina siku hii.

Kijana huyu aliigiza akitumia jina la Jeta, hata baada ya igizo kuisha aliposhuka baadhi ya wanafunzi walianza kumwita hivyo. Mwenyewe aliona ni sehemu ya mzaha, aliruhusu liendelee kuitwa vilevile.

Jukwaani walipanda waimba mashairi ambao walifanya kazi yao vilivyo, na kupongezwa vilivyo. Baada ya kuteremka wao Mshereshaji alishika kipaza sauti na kusema, "Wageni waalikwa, nadhani ni muda mwafaka ambao ulikuwa ukisubiriwa kwa hamu na wanafunzi wa shule hii. Tunafunga dimba la burudani na stand up comedy, kwa mujiu wa ratiba yetu ili turuhusu mambo mengine yachukue wasaa. Wanafunzi hii zamu ni ya naniiii?!"

"Jetaaaa", Wanafunzi walilitamka jina la Jamal alilotumia kwenye igizo.

"Sauti bado ni ndogo hizo, anayemaliza ni naniii!"

"Jetaaaaaaa!"

"Tayari mshambatiza jina jipya haya mabibi na mabwana napenda nimkaribishe kwenu huyu mtu kama vile wanfunzi wenzake wanavyomwita. Namleta kwenu Jetaaaa", Msheheshaji alipomaliza kutamka hayo Jamal aliingia tena ukumbini kwa kutumia mlango wa mbele akiwa amevaa suti nadhaifu. Alikabidhiwa kipaza huku mbinja nyingi zikisikika kutoka pande tofauti, aliwapungia mkono na kisha akasogeza maikrofoni mdomoni mwake.

Siku ambayo wageni hawatokuja kuisahau tangu waanze kuingia shuleni hapo, wengi waliyofika hawakujua kwanini alishangiliwa mno alivyofika mbele ya umati huo wa watu. Alipoanza makeke yake pasipo kuchezesha mwili ndipo walikiri wanafunzi walikuwa na haki ya kupigiwa mbinja, Jeta kama wengine walivyomwita alijua kuchekesha watu hadi ikawa utulivu unakosekana kisa yeye.

Akifanya hiyo hakukuonekana hata tabasamu usoni mwake, ila hadhira ikawa haijiwezi kwa kicheko. Alifanya makeke yake kwa kutoka upande mmoja kwenda mwingine wa hapo mbele, alipohitimisha ratiba yake alipigiwa makofi na kila mmoja. Hata kitendo cha kutoka nje ya ukumbi wapo baadhi waliinuka kukimbilia huko, utulivu ulikosekana kwa dakika kadhaa kisa yeye na ulipokuja kupatikana hakuna kilichobaki isipkuwa kufunga sherehe hiyo kwa dua.


BAADA YA SAA MOJA
Tangu kuisha kwa mahafali na kuwa ni zamu ya wanafunzi kujumuika na wazazi wao, siku hii familia ya kina Heriety, Gina, Jamal na marafiki wengine wa kina Gina walikuwa pamoja kwa mwaliko maalum wa mzazi wa Heriety. Mara nyingine tena aliweza kushuhudia JD akiwa nao pamoja na kupelekea darasa waliloingia kuwa na ulinzi mkubwa.

Wengi walibaki na maswali juu na ujio wake tajiri yule mahala hapo, walijumuika naye kwa kufurahia pamoja. Keki ya pamoja ililetwa ambapo walilishwa wanafunzi wote na kisha ikafuata muda wa kutambulishana hapo ndani miongoni mwa familia hiyo zilizokutana pamoja.

Alianza Heriety kusimama na kuitambulisha familia yake, akafuatia Gina, na wengine wote waliyofika hapo wakafanya hivyo akabaki Jamal tu ambaye alikuwa akisuasua kufanya hivyo. Kusita kwake kulipozidi Shehoza alimwambia afanye hivyo kwani hakuwa na jinsi. Aliridhia kishindo upande huku akijivika tabasamu usoni, baada ya hapo alisimama akafika hadi mbele ya darasa.
"Niwashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuwatambulisha watu wa karibu yangu waliyoweza kufika kwenye sherehe hii muhimu ya kuihitimu kidato cha sita. Bila kupoteza muda ningependa nianze kutambulisha", Alipofikia hapo alimwashiria JD aje mbele naye bila kusita alifanya hivyo. Baada ya kufika alimshika bega akisema, "Huyu kwa jina anaitwa Jamshid Daud Dolan au J.D, ndiyo baba yangu mzazi". Alipoweka kituo hapo wengi walibaki mdomo wazi, hakuna aliyefikiri kuwa kijana huyu ni mwana wa tajiri mkubwa na pia mtu wa kuogopeka nchini.

Watu walipiga makofi naye alikumbatiana na JD, kisha msomali yule alirejea kukaa kwenye kiti. Shehoza naye aliitwa mbele na kutambulishwa, kisha akafuata Doreen na hatimaye akaingia Alice. Alipomaliza hilo suala aliketi chini, huku wahudhuriaji wakimpigia makofi.

____________

Kipindi Jamal akimtambulisha JD, Gina aliingiwa na hofu kubwa ambayo hakuwahi kuipata tangu afahamiane na kijana yule. Alimjua vyema mtu yule alikuwa ni nani ingawa muda mrefu hakuwa yupo nchini, sura yake haikubadilika aliwahi kuiona kwenye vyombo vya habari baada ya kwenda kufanyiwa mahojiano mahali alipokuwa akiishi. Hapo ndipo akajua alikuwa akicheza na hatari, aliyekumbuka maneno ya wale wahuni kuwa wanaomlinda Jamal ni majambazi hatari.

Aliamua kumtumia ujumbe Luka ambaye majira hayo yupo kwenye mgahawa wa shule hiyo kwani hakuna mzazi wake aliyefika siku hiyo. Kijana huyu alikaa na wenzake ambaye ujumbe huo ulimshtua mno, alijikuta akiingiwa na uoga pia kwa kucheza na mtoto wa mtu hatari jijini. Wenzake aliyokaa nao wakiongea waliona mabadiliko ya sura yake baada ya kuitazama simu yake, nao walijawa na shauku ya kutaka kumaizi kile kilichomfanya akawa namna ile.

"Luka vipi mbona hivyo?", Rafiki yake mmojawapo aliuliza.

"Mnakumbuka nilipowaambia tunamfanyia mpango Jay kwa kuzingua dili langu"

"Nakumbuka vizri si ukashirikiana na yule gashi, ulinipa mkanda mzima jamaa sijasahau", Mwingine akadakia.

"Sasa mtu wangu yule gashi ananitumia sms kuniambia kumbe JD ni baba mzazi wa Jay na yupo hapa kwa ajili ya mwanae. Unajua huyu ndiyo kaniingiza kwenye dili lile"

"Dah! Mwana nakushauri kama jamaa hakutoa maelezo kwa mshua wewe temana na dili hilo, ila kama katoa jiandae. Si unajua jamaa hakuwepo bongo ila wafuasi wake kazi zao unazijua, jiandae kwa mengine", Aliambiwa.


"Dah! Kweli shori kanitia janga tu, kama vipi ngoja nisikilizie hali ikiwa shwari navunga tu"

______________


Muda huo Luka akijilaumu, upande wa darasani kulipo na mkusanyiko wa familia. Mama Gina alisimama mbele ya wazazi wenzake pamoja na wanafunzi na alisema, "Wazazi wenzangu pamoja na wanangu nyote, napenda siku ya leo niseme neno ambalo nilikaa muda mrefu pasipo kulitoa.......Nakumbuka mnamo mwaka juzi nikiwa ninaelekea kazini, nilikumbwa na mafuriko siku hiyo mimi Agatha nilijua ndiyo mwisho wa maisha yangu maana hakuna aliyejitolea kunisaidia. Nilikuwa pale daraja la mto Msimbazi na gari yangu ilianza kusombwa na maji muda ambao foleni ni kubwa mno chanzo ni trafiki pale faya. Mungu akamleta mwokozi ambaye hakuwa vizuri kiafya ila aliweza kunitoa kule ndani ya gari na kunifikisha hospitali nikiwa sijitambui. Nilipokuja kupatwa na fahamu ndipo nilikuja kukutana na sura ya kijana mcheshi na mwenye maneno yenye busara. Hakuhitaji chochote kutoka kwangu kwa kuweza kunikomboa, hili ilinifanya nimpe zawadi ya cheni yangu ambayo nilithamini niliyopokea kutoka kwa Baba yangu Aesop. Natamani sana ningeweza kuzaa mtoto kama huyo aliyeweza kuniita mama na kuniona kama mama yake.... Siku hii ya leo nilipokuja hapa shuleni kuhudhuria mahafali ya mwanangu Luigina, nimeweza kukutana naye kwa mara nyingine ingawa hakuwa akipenda kuonana wala kuja kwangu. Nimefanikiwa kumvisha taji na kumpa zawadi na naamini hapo alipo bado ana zawadi yangu niliyompatia. Na mimi ninayo ya kwake ni hii, naomba asimame tafadhali sina haja ya kumtaja jina".

Mama Gina au Bi Agatha alipomaliza kuongea, Jamal alisimama wima na kupelekea wazazi wapige makofi kwake. Aliashiriwa aje mbele naye akasogea, alifika hadi alipo ambapo alikumbatiana naye, kisha akasimama jirani naye huku akitazama ndugu wote wa wanafunzi waliyofika mahala hapo.

"Huyu ndiye shujaa wangu, bila yeye ningekuwa si hai leo. Natamani sana kuwa na mtoto kama yeye na hakuna mzazi humu miongoni mwenu asiyetamani suala hilo. Bwana JD nikupongeze kwa kuleta uzao wa malaika huyu, aliyejua kusaidia wengine huku akiwa hajali yeye ni mgonjwa pia hata alipofika hospitali alifikia kulazwa", Mama Gina aliongeza.

Alipofikia hapo, Gina alibaki ameinamisha uso chini hata kutazama mbele kwenye alishindwa. Hakuamini kama mvulana aliyemfanyia mabaya mengi ndiye huyo, aliyeweza kuokoa maisha ya mama yake mzazi ambaye walimkuta hospitalini akipewa tiba. Machozi yalimlenga ila alijitahidi kuficha hisi zake asionekane ni mwenye kulia, Akiwa bado anafikiria kuhusu hilo, babu yake wa hiyari naye akasogea mbele akiomba nafasi ya kuzungumza. Alifika na kumshika Jamal bega huku akiachia tabasamu, kijana alimpa ishara tabibu yule ambayo aliiafiki kisha akawatazama wahudhuriaji wote.

"Na mimi nahitaji niseme machache kuhusu huyu kijana ninayemtambua kwa jina la Kimweri na sikuwahi kuwaza kama ana jina jingine kabla ya siku hii. Niliwahi kudhani ni mdogo wa Dokta Ismail Shehoza na leo nimeweza kutambua ni mpwa wake. Mara ya kwanza kukutana ilikuwa ni Korogwe vijijini nikiwa nimeharibikiwa na gari, nilihitaji msaada mno kwani gari inachemsha na pia ina pancha. Huyu alijitokeza na kunisaidia kubadili tairi akiwa ni mtoto wa miaka nane tu, tena alinisaidia hadi kutafuta maji kuweka kwenye rejeta ya gari. Kufanya hayo yote nilizoea kumlipa aliyefanya ila kwa huyu akiwa ni mdogo hakuhitaji malipo yeyote, moyo wake huu ukawa ni chanzo cha mimi kujuana na familia yake ya Bwana Shehoza Mdoe wa kule Korogwe. Ndiyo maana sikusita kumpatia taji na zawadi ", Dokta Aesop naye alisema kisha akakumbatiana na Jamal.

Wazazi kadhaa walisogea mbele kumpongeza kwa moyo aliyouonesha kwa Mgiriki yule, kila mmoja akisema anatamani kuwa na mtoto kama yeye. Wapo waliyothubutu kutamka nyumbani mwao anakaribishwa na kujumuika kama mwanafamilia wao, siku hii Jamal alijisikia faraja mno na hata JD mwenyewe alitokwa na machozi ya furaha kwa kusikia moyo mzuri ambao mwanae wa kumzaa anao.

Siku ilimaliziwa kwa sherehe iliyofanyika nyumbani kwa Baba Heriety, ukaribu wa familia hizo ulizidi zaidi kwa kuchochewa na Jamal. Waliendelea kuishia kama ndugu huku Gina tu ndiyo akiwa hana amani moyoni mwake, bado yale aliyowahi kumfanyia Jamal yakawa yanamwandama nafsini mwake.

Hakufungua mdomo wake kuomba radhi aliendelea kuwa namna hiyo, hadi wanafanya mitihani ya mwisho kwake ikawa ni hiyohiyo. Alimaliza vizuri kila kitu ila bado hatia yake kwa Jeta ikawa inaishi moyoni mwake, alitafuta walau wa kumweleza aweze kumsaidia juu ya hilo ila hakukuwepo kwani kila mmoja ni mwenye mapenzi makubwa kwa Jamal. Alihofia kuweza kumuwekea uhasama baada ya kuwaleza kosa alke alilolifanya.

Pamoja na hayo bado hakuwa ni mwenye kumsahau Kelvin, kipindi alijaribu kumtafuta lakini ikawa ni nadra mno kumpata. Alipoonana naye ima atukanwe au atumiwe na kuachwa, alibaki ni mhanga wa penzi tu ila hakutaka kubadilika ndiyo kwanza aliendelea kumfuata kijana yule ambaye hana muda naye zaidi ya kumpotezea wakati.

_____________

Muda huu JD aliamua kuchukua hatua ya kuwaita Mama na mwana jijini ambapo walifikia kwake, ingawa hawakuwa wenye kuhitaji kuja ila shinikizo la Shehoza kwa pamoja waliingia kwenye himaya ya wasomali yenye kulindwa kupitiliza. Walikaribishwa na kula pamoja chakula cha mchana kwenye siku hiyo, ambapo mwenyeji alionesha kufurahisha na ujio wao ila wageni haikuwa hivyo.

Baada ya chakula ndipo Msomali huyu alipochukua wasaa wa kuwaeleza lengo la kuwata hapo, alipoanza kueleza Mwanahawa alionesha kutotaka kusikiliza lakini kwa ushawishi wa mdogo wake akakubali asikilize. JD alisimulia kila kitu kilichomkuta alipokuwa nje ya nchi na namna familia ya mama yake iliwekwa mtegoni kisa tu alitaka kurudi nyumbani baada ya kufanya kazi kwa Bwana Fernando. Hakuficha chochote aliamua kuwaweka wazi, alipomaliza aliinuka kutoka pale alipokaa na kusogea mbele yao kisha akapiga magoti.

"Nadhani mmenisikia na mkanisikiliza pia, hayo ndiyo yalikuwa maisha yangu huko Argentina kabla sijarejea hapa kwa kutoroka. Mliniona nina kosa na pia mkosefu kutokana na hili, pamoja na kujaribu kutimiza majukumu hata nikiwa mbali hamkunielewa. Kama ni hili ndiyo kosa napiga magoti hapa mbele yenu mnisamehe, kama hamuwezi mnaweza kunipa adhabu yeyote ilimradi msiwe na kinyongo nami", JD alisema huku akilengwa na machozi.



*GINA AJUE MEINGI MAZURI KUHUSU JAMAL, JE ATAOMBA MSAMAHA?
*AMESITA KUMUELEZA MTU KUHUSU HATIA YAKE, VIPI ATAWEZA KULIFICHA MIAKA YOTE?




ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



_____SEHEMU YA THELATHINI______


"Nadhani mmenisikia na mkanisikiliza pia, hayo ndiyo yalikuwa maisha yangu huko Argentina kabla sijarejea hapa kwa kutoroka. Mliniona nina kosa na pia mkosefu kutokana na hili, pamoja na kujaribu kutimiza majukumu hata nikiwa mbali hamkunielewa. Kama ni hili ndiyo kosa napiga magoti hapa mbele yenu mnisamehe, kama hamuwezi mnaweza kunipa adhabu yeyote ilimradi msiwe na kinyongo nami", JD alisema huku akilengwa na machozi.




____________TIRIRIKA NAYO

Mwanahawa alidondosha chozi, la huruma kwa JD. Hakufikiri kama angekuwa amewaza vibaya dhidi ya mpenzi wake ambaye alitoweka kwa miaka mingi. Ingawa alIombwa msamaha, ila moyoni alijiona ni mwenye hatia wa kutomsikiliza walau kujua kilichotokea. Asili ya familia yake alihisi huko atakuwa amepatiwa kibarua kipya na jamaa zake, ili asiweze kurejea nchini kuungana naye.

Huzuni aliinuka kitini na kwa haraka alimkimbilia JD na kumkumbatia akiwa amepiga magoti vilevile. Alilia sambamba naye huku Jamal akiwa ameinamisha kichwa chini asijue cha kufanya. Aliganda namna hiyo akiwatazama wazazi wake kwa kuibia, baba yake aliamua kumwita naye aje hapo aungane naye. Kutokana na huruma ya mama yake, naye hakuwa na ugumu moyoni mwake alijikuta akijongea na kumkumbatia mzazi wake.

Hasira ile iliyokuwepo hapo awali kwa JD, ikawa imetoweka. WakAwa ni sehemu ya familia moja, msomali huyo alimshukuru mno Shehoza kwa kuweza kumrejeshea furaha aliyoikosa kwa muda mrefu.

___________________

Siku zote mtu atakuwa na imani juu ya mtu fulani, hata asikie la kuambiwa juu yake hawezi kubadili msimamo katu. Ataendelea kuushikilia tu na kuwa nao, maana wanadamu wengine atawaona ni wenye hila kwenye penzi lake na wanataka kuvuruga akaangukie mikono asiyostahiki kuwepo.

Tabia mbovu za Kevi alizisikia ila hakuwahi kumwona akiwa na mwanamke mwingine, zaidi ya kupata fununu tu katembea na fulani. Hii ndiyo ilimpa matumaini na kuamini kijana yule mengine anawekewa chuku wala hayana ukweli wowote.

Kipindi hiko akisubiri majibu nyumbani na kutoka kwenda sehemu mbalimbali, alimwona kwa mara ya kwanza akiwa na binti mwingine. Hilo alilivumilia hakutaka kulisema, siku nyingine akamkuta akiwa na banati tofauti napo alikaa kimya hivyohivyo. Alipozidi kufumania Gina akaona sasa inatosha, akanyoosha mikono juu na kukubali kijana yule alipotea njia kuwa naye.

Ilikuwa ni jambo gumu mno kuamini hivyo, lakini kila alipofikiria wasichana hao wanaotembea na kijana yule. Nao wana watu wao wa kando, ambao pia wapo kimahusiano na mabinti wengine tofauti. Hii inajenga mtandao wa ngono mkubwa, laiti mmojawapo akaupata ugonjwa wa kisasa basi hakuna atakayepona miongoni mwao wote hapo.

Kwake ni heri kukimbia uwanja wa vita ili usipate jeraha, kuliko kuendelea kuipigania vita ambayo mwisho hakuujua. Aliamua kumsahau kijana huyo, kama kumtesa ilikuwa ni zaidi na alihitaji kuwa huru. Gina kwa mara ya kwanza akaanza kufuta mawasiliano ya Kevi na pia kumbukumbu yeyote ile inayoweza kukumbuka upendo wake.

Ni suala gumu mno ila hakuwa na jinsi, aliamua kulikabili huku siku za mwanzoni akionekana kuanza kulishindwa. Hatimaye baadaye vita hiyo alianza kuishinda, huku akijiona ni mtu huru zaidi baada ya kutoka ndani ya kifungo cha moyo. Mwanzoni aliamini ni kitu kigumu mno, baada ya kukiacha aliona wazi alikuwa akijipa tabu isiyokuwa na ulazima. Maisha bila Kevi, yawezekana.

_____________________

"Jamal, tiba ndiyo hii mwanangu kwanini usiikubali ili uwe huru kwenye tatizo lako?", JD alimsihi Jamal akiwa yupo naye nyumbani kwake.

"Naamini niliumbwa nikiwa hivi, baba katika kitu ambacho sipo radhi kwenye maisha yangu kufanyiwa basi ni upasuaji. Nimefanyiwa lakini sikuwahi kuona mafanikio yeyote. Bora Dokta Aesop aliyewahi kuniweka wazi hakuna njia ya tiba zaidi ya kutumua dawa nikihisi tatizo", Jamal alisema.

"Inamaana haiwezekani kwa wewe kupona?", Husa aliuliza.

"Ndiyo Babu haiwezekani na haitowezekana, kikubwa nipo hai na nina nguvu zangu ninaendelea vyema na maisha yangu. Naomba tuliache hili suala, sipo tayari kupasuliwa tena"

"Ok siwezi kukupinga kufikia umri wako ni mtu mzima, ninakuachia ufanye maamuzi mwenyewe. Ila sitokuwa tayari kukupoteza mwanangu, nipo radhi nikose kila kitu ila si wewe hata nitoe mali yangu yote kukuokoa nipo radhi. Sitarajii kupata mtoto mwingine kwenye umri aliyonao mama yako, na wala sina mpango wa kwenda nje nipate mtoto tena. Wewe ndiyo kila kitu, napenda utambue jinsi ulivyo na moyo wa ajabu umenifanya nibadilike na kuwa wa kipekee. Hata wale waliyokuwa wakifanya maovu naanza kuwasihi wabadilike, yote kutokana na wewe kunibadilisha", JD alisema

"Jamal unapaswa utambue, upo wewe kwa baba yako na pia upo wewe kwa mama yako hakuna mwingine. Maadamu umechukua uamuzi huo naomba ujichunge sana, tumewaweka kina Oze na Paki kwa ajili ya usalama wako tu na si vinginevyo", Husa aliongezea.

"Baba na Babu nimewasikia vyema, naahidi sitowaaacha na huzuni nitaendelea na mfumo huu huu wa maisha kwa ajili yenu nyinyi"


Pamoja na kuelewana na mzazi bado hakuwa akiishia hapo, alipendelea kuwa na Shehoza kule nyumbani kwake. Ulinzi wa vijana wa JD uliendelea kama kawaida, alipenda kuja kumtembelea na kumsalimia baba yake na kuongea naye au mzazi kuja kumwona.

Siku hiyo alifika baada ya kupokea wito kwake, kutokana na tatizo linalomsumbua. Mzazi huyo alipata ufumbuzi wa tatizo, aliamua kuja kuongea naye amsikilize ataamua vipi. Hakujua kama kufanyiwa upasuaji ilishawahi kutokea miaka ya nyuma kipindi teknolojia si kubwa, ila kitu walichokikuta ndani ya mwili wake ilijulikana wazi ni jambo kubwa linalomsibu. Ndiyo maana akagoma ufanyiwa, alijua yatakuwa ni yaleyale ya awali.

________________

Hatimaye matokeo ya kidato cha sita yalitoka, Jamal akawa amefaulu kwa daraja la kwanza na aliongoza mchepuo anaosoma kama kawaida. Wengine waliyosalia walipata madaraja ya pili, Gina na Heriety walifaulu vizuri mno na hata kufanikiwa kuchaguliwa chuo kikuu cha Dar es salaam ambapo waliingia sambamba na Jamal ila kwa kozi tofauti. Wao walichagua sayansi ya tarakilishi, yeye akiwa anasomea uhandisi wa umeme.

Alice naye alifaulu vyema masomo yake, akachagua kozi moja na rafiki yake Heriety. Urafiki ulishamiri mno hakutaka kuwa mbali naye, ndiyo maana akachukua uamuzi huo akiamini ndiyo njia stahiki ya kuendelea kuwa pamoja. Alice na binti huyu walishibana mno, ingawa hakuweza kuwa na maelewano na Gina.

Mwaka wa masomo waliuanza vizuri mwezi septemba, hadi kkufikia muda huo Gina hakuwa amenyanyua mdomo wake kumwomba radhi Jamal. Ingawa alifika nyumbani kwao na kuongea na wadogo zake kwa pamoja, huku naye akijitahidi kumwongelesha. Wakiwa na watu kwa pamoja walifikia hatua ya kuongea wenyewe, lakini wakibaki peke yao basi ukimya ulifuatia na Jeta huwa wa kwanza kuinuka na kumwacha binti pekee mahali alipokaa.

Waliishi namna hiyo kwa kipindi chote, hakuna aliywahi kujua kama watu hao kuna ugomvi kati yao uliwahi kuibuka kipindi cha nyuma. Ilibaki ni siri yao wawili, Gin alianza kubadilika baada ya kuanza masomo akawa ni mwenye kutamani kumwona kijana huyo hata kwa mbali tu.
Chuoni kila ifikapo asubuhi, basi hujipitisha darasa ambalo ana kipindi kijana huyo kuweza walau kumtia machoni. Hakujua alianzwa vipi na hali hiyo, alijikuta tu akiwa ni mtumwa nayo na aliifanya kuwa ni siri. Alipohofia kuwa anaweza kuhisiwa vibaya, aliunda urafiki na binti mmojawapo wa kozi ya unandisi wa umeme ilimradi atu aweze kuingia mule kumsalimia na kumwona Jeta.

___________________


"Sikuwahi kuwa na hisi kama hizi kabla ya hapo, sikuwahi kuwaza kama nilikuwa nipo kwenye upendo ambao ulianza mithili ya chuki ila baadaye ulikuja kuchepua kwa namna nyingine kabisa. Napenda nikiri pasipo kupepesa macho nakupenda, hata kama unanichukia mno kwa yale niliyowahi kukufanyia ila sitoacha kukutamkia wazi ni jinsi gani ninavyokupenda. Jeta nakupenda", Gina aliongea akiwa amesimama chini ya mti akimtamza Jamal aliyeegemea mti akiwa na nguo za nyeupe.

"Gina, Gina, Gina, binti uliyewahi kunichukia, binti uliyewahi kunifanya mambo yenye udhia, nisiyewahi kukukosea hadi ukanichukia, ukanipelekea na mimi niingiwe kwenye chuki wakati haikuwa kutokea. Leo imekuwaje?", Jamal aliuliza akiwa hana uso wenye mzaha.

"Nadhani kila jambo hutokea na sababu, chuki yangu and all juu yangu kuhusu wewe. Nafikiri ulikuwa ni upendo tu sikuwa najiweza, haiwezekani nichukie mtu bila ya kuwa sababu maalum. Nipende kumwangalia tu ili so wangu ujawe na chuki kipindi nikiwa shuleni, ushawahi kujiuliza ni namna gani unaweza kupenda kumtazama unayemchukia? Hapo ndipo nikajua ule ni upendo tu uliyoanza kwa namna ya chuki, ulikuwa ukitafuta reason ya kuonekana tu kwako na si kingine. Wema wako kwa mzazi wangu ukanifanya niondokane na chuki ile, kuanza kukaa nawe na kuona jinsi ulivyo kipenzi cha kila mtu ndiyo ikawa sababu ya kurejesha upendo wangu sehemu yake. Nakiri kwingine kote nilikosea njia ila kwako ndiyo njia sahihi",

Jamal huyu aliyezoeleka kuwa na uso wa tabasamu muda wote, hakuwa yule. Ni binadamu ambaye majira haya uso wenye umakini, alimtazama Gina wa jicho la kipekee ambalo lilianza kumpa jibu binti huyu maneno aliyokuwa akimwambia yamemwingia hadi mtimani mwake.

Gina aliamua kujisogeza karibu yake kabisa kwa mwendo wa kujivuta na hatimaye akafika hadi umbali mfupi mno nyuso zao zikiwa zinatazamana. Kijana alipeleka macho usoni mwake na kupelekea binti aanze kuingiwa na aibu akakwepesha uso ingawa alitamka maneno yale akiwa na ujasiri mkubwa. Alishindwa tu kustahimili macho ya mvulana, akiwa namna hiyo alibaki akisubiri walau aweze kupata jibu kutoka kwa Jamal napo ulipita ukimya pasipo kutokea.

Hali hiyo ilimpa uhakika kijana huyo hakuwa na la kusema, na kwa mara moja alichukua uamuzi wa kumtazama kwa jicho la kuibia. Akamwona katazama tu akionesha kaduwaa, namna hiyo binti alijikuta akitazama midomo ya jamaa. Tamaa ya kuzivaa papi zile ikamjia, akajikuta kwa kasi kubwa akisogeza uso wake jirani naye.

Alipokaribia kugusisha mdomo huku akiwa amefumba macho, alijikuta akigusa midomo mipana kuliko alivyotarajia kukuta ni midogo ya kijana yule mwenye asili mchanganyiko kwa mbali. Akiwa bado kagusisha alijikuta akifumbua macho kwa ghafla kuangalia mabadiliko hayo, afanalek! Alijikuta kishtuka kwa nguvu na kurejea nyuma akiwa haamini kwa kile alichokiona.

"Kelvin!", Aliita kwa nguvu akajikuta akimsukuma kijana yule aliyemwona.

Kitendo cha kusukuma vile alihisi amekuwa mwepesi kupitiliza, hadi kumsukuma kwa mkono mmoja tu akawa amesogea kando. Hakumwona tena na alianzaakujilaumu mno kwa kumbusu mdomo, akiwa namna hiyo ghafla alijihisi akiwa ananing'inia kwenye nyavu kama vile ni kiumbe ni aliyeingia mtegoni.

Alijitingisha na kujiona yupo palepale, hali iliyompelekea ajikute yupo kwenye kwenye chandarua kwa pembeni akiwa ametoka nje ya godoro. Ugumu wa kinga hiyo dhidi ya mbu ndiyo ulimfanya asiweze kuanguka chini, kumbe alikuwa amelala kwenye kitanda chake hosteli majira hayo. Aliyokuwa akiyashuhudia yote ni ndoto na si hali halisi, alibimbirika kurejea katikati ya kitanda kisha akakaa kitako huku akihema kwa nguvu kwa yale aliyoyashuhudia njozini.

"How come?, Alijiuliza na akatazama kitanda alicholala mwenzake wa humo chumbani ila hakuwepo, hapo alishusha pumzi ya ahueni kwa kuona yupo mwenyewe tu humo ndani.

"Sijui Heryn angekuwepo humu ndani ingekuwaje maana namna vizuri yule", Alijisemea huku akiondoa chandarua halafu akatoa miguu nje na kuiweka chini.

Kutokana na uchovu wa usingizi aliganda hapo kwa muda mfupi, kisha akachukua simu yake mkononi kutazaam ni saa ngapi hiyo hadi aingie usingizini na mwenzake awe hayupo. Alipowasha kioo cha simu, alikuta ni saa saba usiku. Hapo alijikuta akishtuka na kutazama huenda atakuwa ameenda msalani, lakini kitanda cha mwenzake kilikuwa kimetandikwa vilevile hakikuonesha kama ni mwenye kutoka nje mara moja tu usiku huo.

"Huyu nyau kaenda wapi? Yaani anachomoka usiku kimyakimya wala haniambii, hebu ngoja", Alijisemea kisha akatafuta namba za rafiki yake ampigie ila hazikuwa zikipatikana, alijikuta akimlaumu mno kwa kutoka bila kumwambia wakati urafiki wako hawakuwa wakifanya hivyo hata siku moja.

Usingizi wenyewe ulimwisha mara moja, akiwa namna hiyo umeme ndani ya chumba unazimika ghafla hali inayomshtua akidhani umeme umekatika ila alipotazama nje kupitia dirishani alibaini taa za baadhi ya vyumba zinawaka. Hiyo lilikuwa ni ajabu nyingine, yaani hosteli za jengo moja taa za sehemu zingine ziwake. Alibaki akiwa haelewi, alichukua simu yake na kuwasha tochi kisha akamulika kuelekea mlangoni
.
Gina kabla hata hajaufikia mlango, alisikia milio ya Paka ikitokea dirishani wakipigana. Jambo hilo lilimfanya apige mayowe kwa uoga, akiwa namna hiyo haikupita muda mrefu alisikia mingurumo ikitokea mlangoni. Binti alijikuta akirudi nyuma kwa kasi hadi akaparamia kiti nusura aanguke, akiwa hajakaa sawa mara akasikia sauti ya mtu akicheka kwa nguvu. Loh! Aliangaza upande wa dirishani akijua walau anaweza kumwona anayefanya hivyo kutokana na nje kuwepo mwangaza, ila hakuwaona.

Mwishoni aliamua kujivika tu ujasiri aende kulekule mlangoni, alimulika kurunzi ya simu huku akijongea kwa taratibu. Alipokaribia kufika taa ziliwaka kwa ghafla humo ndani, hapo alishusha pumzi za ahueni na akataka akutoka nje tu na si kubaki . Aliamua kuufikia mlango na alifanikiwa hilo, alishika kitasa akanyonga nacho kikatii amri. Aliufungua akiwa hajiamini, na hapo ndipo akajikuta akishtuka hadi akakaa chini kitako bila ya kupenda akiwa na fulana yake na kaptula ya kulalia.

"Sapraaaiziiiiiiii! Happy birthday", Sauti za mabinti wengi zilisikika wakiwa wapo mlangoni huku wameshika sahani yenye keki ndogo yiliyobeba mshumaa unaowaka.

*HII MICHEZO MINGINE HII.
*HIVI ILE NDOTO YA GINA INAKUAJE ILE, INA NINI?
*KINA NANI WALITOMFANYIA MCHEZO MBOVU GINA?






ITAENDELEA!!!
 
Back
Top Bottom