Riwaya: Banguzi

Riwaya: Banguzi

Hassan Mambosasa

JF-Expert Member
Joined
Aug 2, 2014
Posts
3,387
Reaction score
4,609
Mojawapo ya kazi zangu, zinazotarajiwa kutiririka hapa jukwaani hadi kufikia mwisho wake, kwa siku zitatoka sehemu mbili hadi inafikia tamati humu ndani. Karibuni
 

Attachments

  • Banguzi.jpg
    Banguzi.jpg
    58.9 KB · Views: 186

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA KWANZA_____


Jicho lisilo kavu wala kuwa na unyevu sana ndani yake, analo hata kwenye hali hiyo bado halikuweza kupotea. Mboni za rangi ya nyeusi zililipamba, ambalo lilizungukwa na kope ndefu ziso na matunzo tofuati na ilivyozoelekea na watu wa umri aliyo nao. Uso wake mwembamba mrefu wa wastani, wenye pua isiyochongoka sana pamoja na midomo midogo ambayo ilionekana kuanza kumpauka. Haikuacha kudhihirisha kwamba huyu aliwahi kuwa mnyange, tena angeweka vikolombwezo usoni mwake angebaki mrembo daima.

Mabinti wengi wa rika hilo hupenda kuendelea kuonekana ni wapo kwenye 'fomu' ila kwa huyu haikuwa hivyo. Nywele zilibaki kutibuka tu ingawa zilioneshwa zinapewa matunzo ya kila siku ndani ya maisha yake. Alipo amevaa nguo nadhifu, akiwa ameketi kitako kitandani, macho ameyakodoa kuelekeza mbele pasipo kupepesa. Haikuchukua muda basi chozi humtoka, laiti ungelimwona ungalisema ya kwamba ni analia. Ila haikuwa hivyo, mtu mwenye kufikia hali hii hawezi kuwa na simanzi ya namna hiyo labda arejewe kidogo na jambo lililomfanya akawa namna hiyo ndiyo anaweza kuangusha chozi.

Mwanadamu daima akikodoa jicho muda mrefu pasipo kupepesa, basi chozi humnyemelea. Ndiyo ilivyo kwa binti huyo, hakuchezesha macho yake ndiyo maana ikawa namna hiyo. Hata waliyopo mbele yake wanaomtazama tu anavyotokwa na chozi, walihisi yu ndani ya huzuni kali ila haikuwa hivyo.
Mwanamke mtu mzima aliyejipara haswa, pamoja na mabinti wawili waliyovuka umri wa kupevuka wakikimbilia mvuko wa umri wendawazimu walibaki wakimtazama Msichana huyo ambaye sura yake imelandana na zao. Walimwonea huruma kwa hali aliyo nayo, kiasi cha kushindwa kusema kile kimsibucho hadi kufikia awe namna hiyo.

"Mama hivi Dada atapona kweli, miaka miwili sasa yupo hivi?", Mmoja kati ya Mabinti hao aliuliza swali.

"Na wewe Spora maswali gani hayo ya kuniuliza, atapona kweli unamaanisha nini? Huamini kama atapona, yaani unakosa imani kwenye jaribio dogo kama hili", Mama huyo alimkaripia Bintiye.

"Si hivyo Mama ninaumia mno kumwona dada yangu yupo kwenye hali hii, natamani sana arejee kama mwanzo. Nampenda sana dada yangu" Spora aliyekemewa hapo awali kwa kutoa kauli ya kukatisha tamaa, alisema kisha akaenda kuketi jirani na Dada yake.

Alimshika kichwa chake na kukilaza begani mwake, Binti kama yeye aliyemzidi umri naye anatii amri na kujiegemeza akiwa yu kimya tu haongei chochote. Msichana aliyesalia baada ya kuliona hilo chozi lilimdondoka, anajifuta huku akimtazama Dada yake kwa simanzi kuu. Hali hiyo ilipelekea Mama yake kumwambia, "Eliza usilie mwanangu dada yako bado mzima huyu, atapona tu tuombe Mungu tu ingawa tumehangaika naye". Eliza aliposikia hivyo alisema, "Ila Mama inauma sana naamini Mama Jeta kafanya ushirikina tu si bure kisa anamchukia Dada yetu".

"Elizaaa! Hebu kuwa wa kisasa mwanangu, bado na wewe upo kwenye imani za kishirikina. Ingekuwa ni imani hizo maombi yote aliyofanyiwa si angekuwa mzima hivi sasa. Amini huo ni mtihani wa Mungu, msitake kuniliza na mimi hapa kwa maneno hayo. Siamini mama kama yule anaweza kufanya haya haswa akijua jinsi mwanae nilivyokuwa nikimwona kama mwanangu, kama kumchukia binti yangu ni haki yake kuwa hivyo, mwacheni awe vile Gina dada yenu alikosea sana. Ila hawezi kufikiaa hatua ya kufanya vile," Mama huyo alisema huku akifikicha macho yake ambayo yalianza kulengwa na machozi.

Alipoweka kituo tu kwenye maneno yake, alitoka humo chumbani, akiwaacha mabinti zake pekee. Muda huo kitendo cha kuondoka, Binti mkubwa asiyeongea wala kufanya chochote, alishuka kitandani na kusimama wima ghafla. Eliza na Spora wakabaki wanatazama tu kwani hawakutaraji suala kama hilo, aliganda namna hiyo huku akipeleka macho kwenye kioo cha kujipamba kilichopo kwenye kabati meza ya vipodozi. Alikishangaa haswaa kionesha taswira hicho, hadi mdogo wake mmojawapo akashindwa kustahimili akamwita.

"Dada Gina", Spora aliita ila hakupokea mrejesho wowote ule kutoka kwa Binti huyo.
Mrembo huyu asiye na matunzo alipokitazama kioo hicho, ghafla alijiwa na kumbukumbu ya ajabu kichwani mwake. Muziki wa kizazi kipya anaanza kuusikia masikioni mwake, hajakaa sawa anasikia mayowe ya wasichana ambao waliashiria wazi kupagawishwa na mwenendo wa ala maalum pamoja na sauti zitokazo kwenye spika maalum. Anajikuta akizungusha shingo kutoka upande mmoja kwenda mwingine, akiwatafuta hao wanaocheza hivyo ni kina nani. Hakuweza kuona mtu yeyote, anajiona yu ndani ya kuta nyeupe tupu tu huku sauti hizo zikizidi kuvuma masikioni mwake. Aliporejesha macho kwenye kioo ambacho kimezongwa na vidopozi, anajiona akiwa ameweka nywele kwa mtindo wa kupendeza. Uso wake ukiwa umepambwa vilivyo, kifuani akiwa na mkufu wa dhahabu.

Kitendo cha kuliona pambo hilo, lisilosimama wala kusimikwa. Aliweka mkono shingoni mwake ambapo muda huo hakukuwa na kitu, hali ilimfanya ajipapase mara kadhaa kwani hakuamini kama kioo kile kichomwonesha akiwa na mkufu kiwe kinamdanganya. Loh! Masikini ya Mungu, Gina hakuwa akijitambua wala kuweza kumaizi hiyo ni sehemu ya kumbukumbu zilizopita ambazo zimelundikana kichwani mwake. Akifanya hayo wadogo zake walishaanza kuhisi kitu, walipaza sauti kumwita mama yao. Yeye wala hakuwa na habari na wito wa nguvu kwa mzazi wake wa kike, alibaki kaduwaa vilevile tu huku hana habari na chochote kile.

Mama alifika hima baada ya kusikia kuitwa huko, alimkuta Gina bado akikidolea macho kioo hicho. Akijitazama, hakuwa na furaha usoni mwake ila kwenye kioo anajiona ni mwenye furaha huku akiyumba kwa madaha kuendana na dundo wa muziki unaosikika masikioni mwake. Hajakaa sawa kupitia kioo anamwona banati mwingine aliyependeza haswa akiwa amevaa gauni jekundu akija kumkumbatia hapo kwenye kioo huku akipiga yowe kwa kunogewa na muziki. Kitendo hiko kinamfanya ajawe na tabasamu haswa, mara ghafla muziki ukazimika ghafla masikioni mwake. Yowe zito la Binti akiomba msaada linafuatia, hali hiyo inamfanya kwa haraka ashtuke na kurudi nyuma kwa ghafla huku akipiga kelele kisha kilio kinafuatia.

"Gina! Gina!", Mama yake anaitwa huku akihangika kumtuliza kutokana na kilio hicho alichokianzisha, ila inakuwa haina msaada wowote ule. Mama huyo alipoona hali ni tete aliagiza, "Wewe Eliza hebu funika hicho kioo na kanga, Spora leta vidonge vyake pale kwenye kabati tumpe alale".

Mabinti kwa pamoja walikimbia kwenda huko walipotumwa, kila mmoja anatimiza agizo lake kwa wakati husika. Gina anapewa dawa ambayo inamfanya atulie, analala papo hapo na kuwaacha jamaa zao wakimtazama kwa masikitiko makuu.

****

Siku iliyofuata asubuhi eneo jingine kabisa lenye mchanganyiko wa watu, alionekana mwanamke aliyevaa suti za kisasa za kike zenye mfumo wa suruali. Akipishana na watu kwa tabu, huyo aliingia upande ambao una mabanda mengi yaliyobanana ambayo huuzwa vitu mbalimbali za vyumbani. Alitembea huku akipita mabao kadhaa yenye vitunguu, nyanya na baadhi ya viungo hadi akafika kwenye eneo lenye kuuza njegere pamoja na maharage mabichi. Hapo ndipo aliweka kituo, akapeleka macho kumtazama Mchuuzi.

"Karibu Dada", Alilakiwa.

"Asante Kaka yangu, njegere mnauzaje?"

"Njegere kipimo kidogo ni shilingi 1000 na kikubwa ni shilingi 3000"

"Nipatie kipimo kikubwa viwili" Mwanamke huyo alisema hivyo anahisi kuguswa begani mwake, anapogeuka anaishia kusema, "Waaaoh! Spora mdogo wangu". Anakumbatiana na msichana ambaye alimgusa bega.

"Haya za masiku we mtoto, yaani mmekuwa adimu nyinyi", Alianza kuongea na Spora.

"Nzuri tu, Dada tupo si unajua da Gina hali ndiyo ileile ndiyo maana hatuonekana muda wote tupo naye"

"Mungu wangu namhurumia sana shosti wangu Gina, Mama nimemwambia hali ile ilianza vipi na nikamshauri cha kufanya ila naona amekikatia tamaa ndiyo hali inakuwa vile"

"Da Heriety kwani uliongea naye vipi mama"

"(Akipokea njegere zilizopo kwenye mfuko laini, huku akimpatia Muuzaji pesa yake) Wadogo zangu unajua bila ya maneno ya Jeta na kile alichokisababisha ndiyo chanzo cha yote yale, msamaha wa yule mama ndiyo kila kitu. Gina alikosea tena sana, ndiyo kosa lake linalomfanya awe vile. Najua nyote hamkuwahi kusikia yote kiupana, ila mimi niliyesoma naye na kukaa naye chumba kimoja hosteli shuleni hadi chuoni ndiyo ninajua hilo. Anahitaji msamaha sana wa Mama Jeta kwa niaba ya Jeta"

"Mh! Hebu da Heriety hebu subiri ninunue vitu maramoja hapahapa, unieleze", Spora aliagiza kwa haraka kile kilichomleta sokoni huko, alipomaliza akamtazama Heriety aliyekuwa akimsubiri kama alivyopenda. Alisogea naye hadi mbali na eneo lenye watu kisha akamwambia, "Dada najua wewe ndiyo unayejua mengi sana kuhusu dada yangu kipindi yupo chuo kuliko hata mama yetu. Maana wewe umesoma naye toka Kidato cha tano hadi chuo, niambie kipi kimemsibu hadi akawa vile. Sikupata kukisikia kisa kile chote"

"Ni kweli Spora mimi ndiye niliyesoma naye Gina, ninayajua mengi ambayo mengi sikuyaweza kuyazungumza kwa mama yako kwani yanatuhusu sisi mabinti tu. Hata kama mama naye ni mwanamke ila mengine, ilinibidi niyaache tu ili kumsitiri shoga yangu. Spora mdogo wangu, mwanzo wa histori haya yalianza tukiwa 'form five' ambapo watu watatu ndiyo chanzo cha Gina kuwa vile. Kevi, Jeta na Allice. Laiti kama isingekuwa uwepo wa hao basi hii leo Gina angekuwa na maisha mazuri kama sisi"

"Kwani ilikuwaje?"

"Ni hadithi ndefu sana, ila ukae ukijua mwanzo wa yote yalianza kupikika tukiwa kidato cha tano. Yakaja kuharibika siku ya 'graduation' yetu usiku ule yaani keshatunukiwa cheti chake cha Degree ndiyo yanamkumba hayo. Yamepelekea kidonda kisichoponda, yaani dondandugu kila kukicha linakuwa. Kama manvyomuona pale alipofikia, mwanzo alikuwa mkaaji kimya tu na si mwongeaji na mambo mengine akifanya ila leo hii hafanyi chochote".

"Dada unanieleza juu juu tu wala huniambii ilikuwaje"

"Spora mdogo wangu, inahitaji muda mwingi sana wa kutulia maana ni kisa kirefu hichi si kama unavyofikiri tukikaa hapa na kukianza sidhani kama tutakimaliza. Yaani hapa tutatumia muda wetu ila hakitoisha, nafikiri leo ni ijumaa na kesho ni jumamosi siku ya mapumziko. Siku ya kesho hiyo ninawaalika kwangu kupata chakula cha jioni, naamini tutapata muda mzuri wa kuzungumza kwani mume wangu amesafiri hivi sasa. Kwa hapa haitowezekana, tuombe uzima hiyo kesho mjue kila kitu kuhusu dada yenu"

"Sawa dada, ngoja nikuache mimi niwahi nyumbani. Kesho nitakuja na Eliza huko"

"Karibuni wadogo zangu, mtanikuta"

****


Kuagana kwa Heriety na Spora haukuwa mwisho wa mazungunzo kwa wanadamu wote, bali ni kwao tu. Upande mwingine ndani ya dunia hii, nchi hiyohiyo waliyopo. Mwanamke mmoja alikuwa amesimama nje ya nyumba kuukuu, akiwa anatazama mkabala na mwanamama mwingine ambaye amevaa vilivyo kuliko yeye. Upande mwingine wa nyumba hiyo kulionekana turubai kubwa, kukiwa wanaume kadhaa waliyopo hapo wakiwa wametulia huku minong'ono ikiwa inasikika kwa mbali. Umbali uliyopo kutoka hapo walipo, hadi ambapo wanaume wamekaa. Hakukuwazuia kuweza kufanya mazungumzo yao, waliamua kuwa huru nayo.

"Shoga mimi ndiyo ninaingia hivi sasa tangu siku nilivyoondoka niambie kunani hivi sasa hapa?", Mwanamke aliyefana kimavazi alisaili.

"Yaani shoga mara moja hii ushasahau, hujui kama siku kama ya leo ndiyo ambayo Jamal alitutoka (machozi yakimlenga). Mwaka wa pili huu bila mwanangu, Mungu ndiyo anajua kwanini amenitenganisha naye. Alimpa maradhi hadi akaja kumchukua Jamal wangu"

"Nimeshasahau mwenzangu, ila pole kwa hilo. Kazi ya Mola haina makosa. Wajua wote duniani tumezaliwa na siku moja tutatoweka, shukuru Mungu kwa kila hali shoga kidonda cha miaka miwili iliyopita usikitoneshe tena mwenzangu"

"Sawa, niambie za huko utokapo?"

"Kwema tu Shoga, nimepita hapa nikwambie mzigo unaenda vizuri huko. Kariakoo wateja ni wengi siku hizi yaani mambo ni safi. Mgao wako ni huu hapa" Mwanamke yule aliposema hivyo, alitoa burungutu la pesa na kumpatia mwenzake ambaye alilifunga kwa haraka kwenye pindo la nguo.

"Mwenzangu safari tuongeze mzigo na twende wote, tusaidane maana naona siku hizi mambo ni supa kama kabisa. Wateja wengi hadi mzigo wote umeisha haraka hivyo"

"Fanya hivyo Fatuma, kazi iishe haraka maana tukiwa wawili mambo yatakuwa rahisi tu"

"Haya shoga, wacha mimi nikaendelee na mengine huko ndani si unajua kuna ugeni leo"
"Haya mimi nawahi nyumbani"

Wanawake hao waliagana, mmoja alirejea ndani na mwingine akashika njia yake. Eneo hilo haikupita muda mrefu kulianza kunukia harufu ya ubani huku dua zikisomwa. Muda huo Kiongozi wa dini wa eneo hilo aliitwa kuongoza dua hiyo, yeye bila ya kusita aliisoma hapo huku akisaidiwa na baadhi ya wasaidizi wake. Hakukuwa na uchangamfu wowote ule, shughuli yenyewe ni kumbukumbu kwa marehemu haikuhitajika kuwekwa kikolombwezo chochote. Dua na ulaji wa chakula ndiyo ulifanyika, majira ya mchana kila kitu kilitimia. Wenyeji walitoa shukrani za dhati kwa wote waliyowasaidia hadi kukamilika kwa kumbukumbu hiyo, baada ya hapo wageni walitawanyika wakabaki wenye nyumba hiyo tu.

****

"You know what? I'm so happy today, sikutegemea kama ningeweza kufika na kukipata hiki nilichonacho hivi sasa. Mungu ndiyo muweza wa yote" Sauti ya Kijana mmoja ilisikika ikiwaambia wenzake waliyovaa majoho ambao wapo kwenye viti vya plastiki vilivyozunguka meza
"Jeta si wewe tu hadi hapa wote tuna furaha ya hayo hebu muulize hapo Bibie Lui, uone kama hana furaha", Msichana mwingine alisema huku akicheka na kupelekea Jeta na Binti mwenye kujulikana kwa jina la Lui watazamane kwa bashasha kisha wakapigana mabusu mbele ya wenzao wote. Makofi yalifuatia huku wengine wakishangilia hali hiyo.

*JETA NI NANI?
*LUI NI NANI?
*GINA NI NANI? KWANINI AWE VILE?
*HERIETY ANA HABARI GANI NYINGINE JUU YA GINA?


ITAENDELEA!!
 

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA




_____SEHEMU YA PILI________


"Jeta si wewe tu hadi hapa wote tuna furaha ya hayo hebu muulize hapo Bibie Lui, uone kama hana furaha", Msichana mwingine alisema huku akicheka na kupelekea Jeta na Binti mwenye kujulikana kwa jina la Lui watazamane kwa bashasha kisha wakapigana mabusu mbele ya wenzao wote. Makofi yalifuatia huku wengine wakishangilia hali hiyo.


______________TIRIRIKA NAYO

Wapenzi hao walionesha mapenzi ya dhati kwao, pamoja na furaha kuu waliyo nayo kwenye siku muhimu katika maisha yao. Majoho waliyoyavaa ambayo yalisheheni mataji mbalimbali yaliashiria ni namna gani walivyo na furaha katika maisha yao. Kwa pamoja waliinua bilauri za vinywaji vyao na kuzigonganisha, mlio wa mgongano huo unapelekea kusikika mvumo wa ving'ora vya gari la wagonjwa pamoja na sauti ya mwanamke akilia kwa uchungu. Hii inamfanya Gina agutuke kwa nguvu kutoka mahali ambapo anaziona bilauri za vinywaji za nyumbani, alirudi nyuma kwa mshtuko na kuanza kuhema huku machozi yakimtoka hata ashindwe kuongea chochote kile. Majira hayo alikaa kwenye kochi sebuleni, aliinuka na kukimbia chumbani kwake kwa uoga huku akiwaacha wadogo na mama yake wasielewe nini kinachoendelea.

"Hebu Eliza kimbia haraka kamwangalie dada yake asije kujidhuru bure", Mama yao alisema na binti yake akatii, alipoondoka aliweka mikono kichwani huku akisema, "Mungu wee! Sijui mwanangu anakumbuka nini au anaona kitu gani kila akiona vitu hivyo. Picha zake zote tumezificha, sasa mara kioo kinamfanya awe kivingine mara glass hizi nazo dah!"

"Mama cool down, everything will be okay", Spora alisema.

"Okay, ila haya anayoyafanya yananishangaza sana yaani nafikiri hata kwenda kwa Sangoma nikidhani ni jambo la giza linamtesa"

"Mama tusifikie huko, hebu tusubiri baada ya jumamosi ndiyo tutajua nini cha kufanya. Nampenda sana dada yangu nipo radhi arejee kwenye hali ya kawaida, ila si kwa imani hizo ambazo hapo awali ulizipinga kwani nyumba ya ibada alishaingia na kufanyiwa maombezi ila hakukuwa na nafuu yeyote"

****


_FIJI_
Mlio wa feni uliendelea kusumbua ingawa ulitoa vitu viwili kwa wakati, navyo ni faraja pamoja na kero kutoka ukuukuu wake na kuendelea kufanya kazi pasipo kufanyiwa marekebisho. Ufariji wake ulimfanya Mtumiaji asiweze kuhisi kama ni karaha zaidi ya kuendelea kufanya kazi zake kwa muda mrefu, liliendelea kufanya kazi yake huku aliyepo kwenye ofisi yenye samani za kisasa pamoja na kiyoyozi ambacho kilizimwa kutokana na hali ya hewa ilivyo kiasi cha kuruhusu madirisha kuwa wazi. Ofisi hii ilipambwa na kuta zenye rangi nyeupe, huku aliyepo hapo ndani akiwa na suti pamoja na koti jeupe likiwa limezungushwa nyuma ya kiti. Haikuhitaji elimu ya ziada kuweza kung'amua kuwa hapo ni hospitali, na huyo aliyepo ni Tabibu.

Daktari huyo akiwa na kifaa chake cha kufanya kazi shingoni alionekana akiandika faili fulani, mara akasikia mlango ukifunguliwa kisha akaingia Muuguzi mwenye asili ya kihindi akiwa na faili mkononi mwake. Huyu alimfanya aachie tabasamu kumwona kwake, naye alipokea bashasha kutoka kwa nesi huyu.

"Naam Ladhika, karibu", Alimlaki.

"Asante Dokta Aesop naona unaendelea kuwajibika, tangu uje huku Fiji sijakuona walau ukiwa ni mwenye kutembea tu zaidi ya kufanya kazi tu na kutulia nyumbani kwako ukiendelea na majukumu ya kitabibu"

"Nimejifunga kwenye kifungo cha kuokoa maisha ya wanadamu wenye matatizo ya aina hii, wacha nitumie muda wangu mwingi katika kutafuta mbinu mbalimbali za kusaidia wanadamu. Wengi ni wenye kuhitaji msaada kila kukicha, nimezunguka nchi kadhaa nikisaidia watu wa namna hii na nakutana na matatizo ya aina tofauti hivyo lazima nitumie muda wangu mwingi kuwasaidia" Dokta Aesop akisema hayo Ladhika aliweka faili mezani kwake kisha akaanza kutalii mandhari ya humo ndani kama ndiyo anayaona, alizungusha macho kutoka pande moja hadi nyingine. Hatimaye akaja kuyatuliza kwenye picha mbili ziliyopo ukutani humo ndani, alizitazama kisha akarejesha macho kwa Tabibu.

"Dokta umekuwa mwingi wa kazi na wala hukuwahi kuniambia watu wale waliyopo pale ukutani ni kina nani. Nakutambua wazi wewe ni Mgiriki na umezaliwa nchini Ugiriki, na familia yako ipo Ugiriki. Nitazamapo watu weusi kama wale ambao unasema ni muhimu kubaki na kumbukumbu zao kichwani mwako, huwa hunifafanulii"

"Ladhika, nina kila umuhimu kwa mmojawapo kati ya wale wawili. Huku nikibaki kujivunia sikuwahi kumwona mtu jasiri kama yeye. Wingi wangu wa kazi ndiyo unanifanya nishindwe hata walau kukosa nafasi ya kukueleza hilo, ila naamini siku ya jumapili asubuhi ndiyo wasaa mzuri wa kuweza kukufunulia kila kitu. Ukajua kwanini nimependa kuongozana na picha za vijana hawa wawili, ninawahusudu sana"

"Sawa utunze ahadi yako tu Dokta..... faili la mgonjwa ulilolihitaji hilo hapo mezani wacha nikaendelea na kazi zangu nyingine"

"Majira hayo napenda sana kufanya mazoezi angalau ya kukimbia, huwa sina ratiba ya kikazi labda itokee kuna mgonjwa wa dharura. Vinginevyo nitakuwa ninaendelea na kuuweka mwili wangu sawa. Nashukuru kwa kuniletea faili hilo, nahitaji nipange cha kufanya juu yake huyu kijana"

"Sawa Dokta, hata siku hiyo nipo mapumziko nafikiri itakuwa muda mzuri haswa kujua kuhusu hilo. Nikuache ufanye kazi kwa hivi sasa"

Ladhika alitoka na kumwacha Dokta Aesop akiendelea kufanya kazi yake, kwa jinsi alivyojitolea maisha yake kwa ajili ya kushughulikia maradhi ya watu wengine. Kwa jina kamili anaitwa Dokta Achillios Aesop, tabibu mwenye shahada ya uzamivu kuhusu masuala ya moyo wa mwanadamu. Ametumia muda wake mwingi kusema taaluma hiyo pamoja na kufanyia kazi kwenye nchi mbalimbali. Ni mwenye familia na alishawahi kuoa ila walitofautiana na mke wake hivyo walitalikiana, ana watoto wakubwa na wote ni matabibu wakubwa nchini Ugiriki.

Daktari huyu hupenda haswa kufanya tafiti na kujua kila tatizo jipya ambalo linahusu taaluma yake na kuweza kulitatua. Hili lilipelekea agundue aina mpya ya matibabu ya maradhi kadhaa ya moyo ambayo yalishindikana. Ilimpelekea kutunukiwa uprofessa ila hapendi kutumia zaidi ya kubaki kujiita Dokta, nchini kwao tu ndiyo wanamtambua kama Professa Achillios Aesop. Huyu bwana kwa kubobea zaidi kwenye taaluma hii, suala la maslahi katika matibabu mara nyingi huliweka kando. Zipo mara nyingi alizoweza kufanya kazi kwa kujitolea kwa nchi mbalimbali, ili aweze kuokoa maisha ya watu ambao hawana kipato cha kukidhi matibabu hayo. Hupenda sana kusafiri na kikosi chake cha matibabu kutoka nchi moja hadi nyingine, kutafuta mahali ambapo kuna wenye shida. Wale waliyo na kipato walitozwa pesa, ila wasiyo na uwezo walisaidiwa na gharama zake alizibeba yeye mwenyewe ikiwemo kuwalipa watu wake.

Alipendwa sana kila nchi anayofika kutokana na moyo wake wa kujitolea kwa watu wasiyojiweza, alizunguka mabara kadhaa na hatimaye akaingia barani Afrika. Huko ndipo alitembelea nchi zote akishughulika na tatizo hilo, hatimaye akaja Tanzania ikawa nchi ya mwisho kupita akiwa na matabibu wake. Nchi hiyo aliipenda mno kiasi cha cha kuweka makazi kwa mdua mrefu, huku akiwalipa madaktari wake wasaidizi gharama nyingine baada ya kumaliza kutibu warejee nchini Ugiriki. Yeye akawa mkazi wa nchini humo, hata watoto wake wakawa wanafika kumwona na kurejea. Huko ndipo alipoweza kuweka historia ya kipekee na kujionea mengi akiwa huko. Hadi pale alipofikiria ni muda mwafaka wa kuhama na kwenda kuishi sehemu nyingine za duniani na kupelekea aangukie nchi ya mashariki ya mbali iitwayo Fiji.

****

Toka aingie ndani kutokana na kumbukumbu zile zilizomnga kwa ghafla na kisha kupotea, hakula chochote na hata alipohimizwa kula ikawa kazi bure. Usiku ulimkuta namna hiyo na hata akapitiwa na usingizi pasipo kutia kitu tumboni mwake. Asubuhi ya siku ya jumamosi ndipo alipoamka, aliogeshwa na kusafishwa kinywa kisha akawekwa kitandani. Siku hii hakuleta mgomo wa kutia chakula, alilishwa na kutii amri hadi alipomaliza akaachwa apumzike.

Ikawa ni ahueni kwa ndugu zake, alitulia na utulivu ambao kidogo uliwafanya wawe na amani. Pamoja na kuchanganyikiwa kwake, Gina hakuwa na fujo kuu kama ilivyo wengine, labda akumbuke kitu halafu kimtoke kichwani na kuanza kumvuruga akili yake ndiyo angefanya mambo ya ajabu. Vinginevyo utulivu ndiyo kawaida yake daima, hadi majira hayo yakawa ni hayohayo akiwa ni mkimya kupitiliza na wala hakuongea lolote lile. Si Bubu ila msongo wa mawazo ndiyo umemfanya awe namna hiyo, ndugu wamehangaika mno kwa madaktari wa kawaida ambao wamewashauri kutumia vindonge tu vya kuweza kutuliza hali hiyo. Ndiyo wanafuata ushauri huo, ikawa akionekana kuleta jambo jingine geni kabisa basi hufanya hivyo na aendelee kukaa kwenye hali ya utulivu. Dawa zikiisha Tabibu aliyekuwa akimpatia tiba, ndiye aliyewashauri wafike na kuchukua zingine na si kuzitafuta madukani.

Watu wengi husema sana kuwa maisha ya dawa si mazuri, ila kwa familia hii ni bora wangeendelee na dawa kama walivyoshauriwa na daktari ambaye huwa anamtibu mara nyingi. Kanuni ile ya kufuata ushauri wa mganga wa kisasa waliiona ni ahueni, ingawa hadi kufikia majira hayo hawakuwa wameona tumaini lolote ile.

****

Siku hii ya jumamosi ni siku mapumziko, ambapo sehemu zingine wafanyakazi huwa hawafiki kabisa. Huku wengine wakifanya kazi hadi saa sita mchana kisha hurejea makwao kupata mapumziko. Mmoja wa watu wasiyogusa ofisi zao siku za mapumziko, alionekana akiwa ameketi eneo la nje la nyumba ya kifahari huku akibarizi upepo mwana utokao ufukwe wa bahari ambao haukuwa mbali kutoka hapo alipo.

Pembeni yake alisimama kijana aliyevaa fulana nyeusi pamoja na suruali aina ya 'jeans' akiwa mtulivu tu. Mtu huyo alionesha ni namna gani mwenye kupenda ukwasi, alivaa madini ya gharama kubwa shingoni akiwa na ameketi eneo ambalo jirani kuna chupa ya mvinyo wa bei ghali. Pembezoni ilionekana bilauri imejazwa kimiminika chekundu.

"Leo hivi huu mpango wa kuendelea kuwepo nchini Tanzania utauendeleza hadi lini?", Kijana aliyevaa nguo nyeusi aliuliza.

"Hadi nisikie Kaka yangu amefariki dunia ndiyo nitaondoka mahali hapa, hii kwa dunia nzima iweze kuishi. Nimefoji taaluma kwa ili tu niweze kuwaokoa wanadamu", Leo alijibu.

"Naelewa hilo, ila vipi Jus akijua kama upo huku, unafikiri itakuwaje wakati anajua kabisa ulimpiga vita muda mrefu tangu upo nchini kwetu kule. Unafikiri hawezi kuhisi kuna mkono wako katika hili"

"Ndiyo maana sitaki anione katika hili, nimechagua nijifanye mwenye taaluma hii makusudi ili nisiweze kukutana naye tena mara nyingi kazi zangu nafanya kwa usiri mkubwa. Najua siku zake zitahesabika, niko radhi kuondoka na kurejea nchini kwangu hadi pale tu nitakaposhuhudia kifo chake na si vinginevyo"

"Vizuri kwa kusimamia maisha ya wengi, ila aliyemfanya vile hana huruma hata thumni nakwambia"

"Ukimfanyia kazi ukatili jua, ukikosea kufanya kazi yake lazima akufanyie ukatili. Leo ratiba vipi mbali na mapumziko?"

"Supervisor kashauri tupumzike ndani tu tusitoke si unajua huyo jamaa yako anayekaribia kuanza kutumia Kitimaguru anazunguka jijini sana siku hizi"

"Ok hakuna shaka ilimradi kazi isiweze kuharibika"

****

_JUMAPILI_,
_ SAA KUMI NA MBILI_,
_FIJI_

Tofauti ya masaa nchini Tanzania na jamhuri ya Fiji, ni masaa tisa, ambapo nchi ya bara la Afrika ipo nyuma kimasaa. Majira hayo ni saa tatu usiku, kule ni saa kumi na mbili asubuhi. Muda huo Dokta Aesop alionekana akikimbia taratibu akikatisha mitaa kadhaa ya eneo analoishi nchini humo. Akiwa pembezoni mwa barabara alikimbia huku akipishana na magari machache tu asubuhi, jasho likimvuja aliendelea kukatiza mitaa hadi akafika eneo ambalo kuna kituo cha mabasi ya kukusanya abiria nchini humo. Hapo akamkuta Ladhika akiwa amevaa nguo za mazoezi ameketi, akiwa bado mwili una moto alisimama huku akirusha miguu akihema kwa kutoa pumzi puani.

"Dokta ndiyo maana umri umeenda sana ila bado unaonekana ni mwenye miaka hamsini tu", Ladhika alisema huku akitabasamu.

"Mazoezi ndiyo kila kitu ndani ya dunia hii, sitaki nije kutembelea fimbo mapema yote hii. Hata kama nimegusa miaka sabini", Dokta Aesop alisema huku akihema kwa kuchangamsha mwili kwa muda mrefu.

"Hongera, naona leo umetunza ahadi yako ile. Karibia hapa subira yangu mahali hapa ni kwa ajili ya kusikia tu kuhusu hao"

Dokta Aesop aliposikia hivyo aliketi jirani na Ladhika halafu akasema, "Kwakuwa umeonesha nia ya kutaka kutambua kwanini ninatembea na picha za watu weusi wale, sina budi kukueleza. Ila unapaswa utambue kuna sababu kuu mbili, ya kwanza ni upendo na nyingine ni ujasiri na kujitoa kwa lolote"

"Ndiyo Dokta"

Tabibu wa siku nyingi akaanza kusimulia, "niliwahi kuzunguka nchi mbalimbali duniani, ila Tanzania nakumbuka ni ardhi iliyonivutia. Ni nchi isiyokuwa na maendeleo makubwa sana, ila aina ya watu wake wanaoishi huko ndiyo walinivutia haswa na kutamani kuendelea kukaa hapo. Niliwasili na jopo la madaktari wasaidizi wapatao kumi na tano nchini humo, ambapo tuliweka kambi yetu ya kwanza eneo la mnazi mmoja na baadaye tukahamishia hospitali ya taifa ya nchi ile. Tulihudumia watanzania wengi kwa kujitolea tu huku nikipoteza kiasi kikubwa kwangu kuona wanadamu wengine wanasalia kuishi duniani. Kusikika kwetu kulipelekea watu mbalimbali kuanza kumiminika jijini Dar wakidhani ni sehemu moja tu tungefikia, siku za kuwepo jijini humo zilipokatika tuliondoka moja na kusogea mkoa wa Pwani. Tukaweka kambi hospitali iitwayo Tumbi, huko tuliendelea na tiba yetu vilevile. Tulimaliza huko kote na hatimaye tukafika mikoa mingine, hadi tukaja kuangukia mkoa ule ambao umenifanya niweze kubaki na picha ya bini uliyeiona kule ofisini kwangu.

*DOKTA AESOP ANA NINI YA KUSIMULIA?
*JUS NI NANI KWANINI ANAFUATILIWA MNO N LEO?



ITAENDELEA
 

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



__________SEHEMU YA TATU_________

.........Kusikika kwetu kulipelekea watu mbalimbali kuanza kumiminika jijini Dar wakidhani ni sehemu moja tu tungefikia, siku za kuwepo jijini humo zilipokatika tuliondoka moja na kusogea mkoa wa Pwani. Tukaweka kambi hospitali iitwayo Tumbi, huko tuliendelea na tiba yetu vilevile. Tulimaliza huko kote na hatimaye tukafika mikoa mingine, hadi tukaja kuangukia mkoa ule ambao umenifanya niweze kubaki na picha ya bini uliyeiona kule ofisini kwangu.

____________TIRIRIKA NAYO
Harakati zetu na matibabu, hatimaye tukahamia mkoani Tanga. Huko tulisaidia wengi mno kama ilivyo mikoa mingine. Pia niliweza kuwa rafiki wa moja ya familia ambayo niliisaidia mimi mwenyewe katika kuokoa maisha ya moyo wa familia ile. Kichwa wake yaani baba wa nyumba, akatokea kwa rafiki yangu mkubwa. Nilipokuwa nipo mapumzikoni yeye pekee ndiye niliyekaa naye kuongea mambo mbalimbali, mtu huyo niliyemfahamu kwa jina la Bosco. Alikuwa ni mfanyakazi wa bandari Tanga, huyu nilielewana naye vyema kutokana na uelewa wake kwenye kingereza.

Enzi zile watu waliyokuwa wakijua lugha hii ni wachache sana, kwa nchi ile ambayo wasomi hawakuwa wengi zaidi ya kuwepo wachache. Tena hao wamejijaza maeneo ya mjini tu na mahali pengine, mkoani Tanga kipindi hicho wasomi ni wa kuhesabika kutokana na kukimbilia jijini Dar ambapo ndiyo waliona kunafaa haswa kuendesha maisha yao. Nani angependa kukaa mkoani sehemu zingine wakati mjini ndiyo kuliaminika kuna ufahari wanaoutafuta.

Ladhika napenda nadhani umesikia haswa kuhusu kutoendelea kwa nchi za barani Afrika, basi napenda utambue kunachangiwa na wasomi wenyewe wa bara lile. Yaani wanashindwa kujua kuwa wakikimbilia sehemu ambazo hazijaendelea, hudum za kijamiii zitawafuata wao na kisha maeneo hayo kujikwamua kutoka kwenye giza nene. Wao wanajua kukimbilia wanapopaona kuzuri, yaani wale wanashindwa kujua hata uzuri huo haukujileta wenyewe bali uliletwa na watu kama wao. Ndiyo maana huko Tanga wasomi ni wachache mno, wapo wanao uelewa wa lugha hii lakini bado wana hofu kubwa ya kukaa na mimi mzungu. Yaani kipindi kile ngozi hii ilikuwa ikionekana ni kama miungu, wao walihofu kuisogelea. Ndiyo maana nilipata rafiki huyo nikiwa mkoani kule, tena huo ukiwa ni mkoa wangu wa mwisho kikazi.

Bwana Bosco kuendelea kuishi naye kwa muda mrefu kama rafiki, nilipata bahati ya kujua kuwa naye ingawa ni msomi bado anatawaliwa na fikra za kizamani. Imani za kishirikina zipo kichwani mwake kama ilivyo wengine ambao wanaamini baadhi ya mambo kwenye maisha yake yanatokana na mikosi ya wanadamu wenzake. Kwakuwa mimi sikuwa na imani nayo hayo mambo, ilinibidi nianze kumbadili kutoka kwenye uelekeo huko na kumpelekea mwingine. Huyu bwana alidai yeye kila mtoto anayezaa, hima afe akizaliwa, au aishi juma moja tu basi kwake ni kifo. Nakumbuka enzi zile huko Tanga imani hizo zilitawala kupitiliza, watu wana hofu kubwa kuhusu uchawi. Mtu mwenye itikadi za namna hii, iliniwia vigumu kuanza kumtoa hadi kumrejesha kwenye mstari mwingine na kuamua kufanya jambo kwenye maisha yake. Niliamua nitumie uzoefu wangu kidogo kwenye masuala hayo, ingawa si sehemu ya utaalamu niliyobeba. Kumweleza na kumuweka wazi, angalau macho yake yafumbuke aone mengine hayapo hivyo.

Hata alipoanza kunielewa bado hakuwa amehamisha akili yake moja kwa moja kutoka kwenye imani potofu. Kila tulipokuwa tukikatiza mitaa barabara kadhaa za Tanga, akikutana na nazi imevunjwa au hirizi basi kwake alirejea kulekule. Rafiki huyu ambaye kiumri alilingana na mwanangu, aliweza kuondokana na masuala hayo. Hatimaye mkewe akashika ujauzito, huo ndiyo ukaanza kuwa mwanzo wa majaribu kwa Mwanamke yule aliyekuwa akiniheshimu kama mzazi wake. Mimba ikiwa na miezi minne, bwana Bosco alipooza ghafla viungo vyote. Mwili mzima ukawa haufanyi chochote zaidi ya kichwa tu. Aliendelea na hali hiyo, mimi ndiyo nikawa nahakikisha anapata matunzo safi na mkewe anapata kila hitaji la mjamzito. Nakumbuka zikiwa zimebaki siku chache mwanamke yule ajifungue, Bosco alitengemaa.

Usiku wa kuamkia mei 20 mwaka 1985 ndipo alipoweza kujifungua salama mtoto wa kike. Kutokana na heshima yangu na jinsi nilivyohangika hadi siku anayojifungua, Bwana na Bibi Bosco walinipa heshima ya kumpa jina binti yao huyo. Awali niliikataa kongoweo yao hiyo lakini niliposhinikizwa na wote wawili. Niliiridhia kwa mikono miwili, nikaamua kumwita Luigina ambalo ni jina la kwetu Ugiriki lenye maana ya aliyezaliwa vizuri. Jina hilo walilipokea vyema, na mtoto huyo hakufariki kama nilivyosikia kwa wengine na hadi anafikisha miaka mitano yaani 1990 niliendelea kumwona ni mwenye afya njema. Majira hayo nilishachukua uraia wa nchi hii, na hata wale wasaidizi wangu walishaondoka nchini baada ya kukamilisha kazi yao. Walirejea nchini Ugiriki wakiniacha nikiendelea kuishi Tanzania nilipopapenda. Makazi yakawa Amboni huku nikifanya kazi hospitali kwa kujitolea vilevile kwa wasiyojiweza, na kuwalipisha pesa wale wote wenye uwezo wa kumudu matibabu yangu.

Mnamo mwaka 1992, Bosco na mkewe walipata mtoto wa pili. Huyo ni binti alivyokuwa wa awali. baada ya uzao huo ndiyo ukaja kuwa mwanzo wa kuishi mpweke. rafiki ambaye nilizoeana naye kwa muda mrefu, alihamishwa kikazi na akahama yeye na familia yake jijini Dar es salaam. Huko baadaye mwaka 1995 walipata binti mwingine ambaye nilifika kumwona na kuwapongeza kisha nikarejea Tanga kuendelea na kazi zangu. Maisha yalisonga mbele huku mimi nikiwa ni mwenye kuwasiliana mara kwa mara kwa kutumia barua na rafiki yangu, nakumbuka mwaka 1999 familia ile iliiingiwa na simanzi na hata mimi nikawa kwenye hali hiyo. Bosco ambaye kiumri nilimpita miaka ishirini, alifariki dunia kwa ajali ya gari. Kipindi ambacho familia ile haina muhimili mwingine zaidi yake, ilipitia wakati mgumu na hapo mimi nikabeba jukumu la kuwaongoza. Nilihakikisha yule Mama anasoma masomo ya muda mfupi, akapata ajira kulekule kazini kwa mumewe mimi ndiyo nikarejea Tanga,

Luigina kwangu nitaendelea kubaki na picha yake tu daima, binti huyu alinipenda na hata kuniita babu. Alikuja kunitembelea na kuishi nyumbani kwangu kwa siku kadhaa na kisha hurejea nyumbani kwao, upendo wake kwangu ulinifanya nibakie na picha hiyo na ndiyo maana ninatembea nayo kila mahali. Katu sitoiacha, mtu ambaye hukuwahi kuwa na nasaba naye kunipa nafasi ya kumpa jina mtoto, tena akaliridhia kwa mikono miwili jina la kigiriki ambalo wala hakulielewa maana yake hapo awali. Na hata nilipowaeleza hakutilia shaka yeyote na kuniamini, hivyo kubeba picha ya binti yake ni faraja tosha kwangu kwani nilipenda kumwona na hata nikiwa mbali huku nitahitaji kuiona sura yake. Naamini picha zile ndiyo faraja tosha kwangu nikiwa huku ugenini"

"Sasa Dokta nimeelewa kwanini una picha ya yule binti pale ofisini kwako, mimi ni mhindi kabisa jambo kama lile akilifanya mtu wa kwetu ni dharaua kubwa kwa jinsi watu weusi wanavyochukiwa kwetu. Lakini kwa hiyo sababu yako hata mimi ninaweza kuiweka pale sitohofu lolote lile", Ladhika alisema.

"Ubaguzi dhidi ya watu weusi haupo huko kwenu tu, hata nchini kwetu upo na sehemu nyingi za barani Ulaya. Ingawa wapo wazaliwa wa Ulaya wenye ngozi nyeusi, napenda niseme bado ubaguzi hautoisha. Niliaminishwa watu weusi ni wana mambo ya ajabu wenye roho mbaya na waliyolaanika, ndiyo maana weupe wakawa wanawachukia. Ila nilipofika barani kwao na kujionea hali halisi, Waafrika ni watu bora ndani ya dunia hii nakiri hilo, maana pamoja na yote kuwafanyia miaka iliyopita hawajawahi kutufanyia ubaya sisi. Babu zetu ndiyo walivamia Afrika, wakaweka tawala kule kinguvu, wakaua baadhi ya jamaa zao, wakawachukua kinguvu wengine na kuwasambaza mabara mengine kama watumwa. Bado walipopata uhuru wakaendelea kunyanyasika ardhi ya ugenini, wao waliyopo nyumbani wanalijua hilo. Ila tunapokuja barani kwao wanatupokea kikarimu, hadi tunajihisi tupo nyumbani na si ugenini", Dokta Aesop alisema.

"Kumbe"

"Ndiyo hali halisi hiyo, pamoja na baadhi ya wazungu wenzangu kuendelea kuharibu vizazi hadi vizazi vya kiafrika ili tu wasiendelee kwa kutumia teknolojia. Bado wanatupokea kwa moyo mkunjufu. Kuibuka kwa vikundi vya mapigano kule, basi kama si Amerika ni Ulaya wao ndiyo chanzo. Kuvurugika kisiasa kwa baadhi ya nchi, ni roho mbaya za baadhi ya watu weupe. Lakini yote hayo wanatupokea kwa bashasha, niambie kuna kiumbe wa aina hii duniani"

"Dokta hadi hapo napenda kukiri Watu weusi wana mioyo ya ajabu sana, yaani hayo yote ingekuwa ni nchi yetu basi ni chuki za kiuhasama. India hadi sasa kuna familia zina visasi kisa ubaya uliyofanywa na babu wa zama hizo wa familia fulani. Yaani ubaguzi umepewa kipaumbele, tunabaguana sisi wenyewe kwa wenyewe"

"Tatizo la kumpa nafasi mdudu anayeitwa Chuki atawale maisha yenu ndiyo hilo. Chuki amewekwa na imani, na kumgeuza mwenye kuamini ni bora hata ukageuze jabali la baharini peke yako"

"Ni kweli Dokta, enhee! Vipi kuhusu yule kijana niliyemwona kwenye picha uliyoiweka ukutani. Mwenye sura nzuri akiwa na tabasamu pana usoni mwake", Ladhika aliponena hayo, Dokta Aesop alitokwa na chozi hadi akamshngaza binti huyo. Alihoji, "Dokta vipi imekuwaje?".

Dokta Aesop alijibu, "Shujaa wa moyo wake, nikimkumbuka lazima chozi lilinitiririke ndiyo niweze kusimulia haya. Maana kama kuna kiumbe aliyepewa moyo wenye matatizo ila umebeba misimamo ya ajabu tena mwenye kumfanya kiumbe mwingine asihisi mwenye huzuni dunia hii. Basi yule ndiyo wa kwanza, hakujijali alivyo bali alijali nini mtima wake unataka hata kama ni hatari".

****

Upande wa nchini Tanzania majira ya saa tatu usiku, muda huu ni tayari kina Eliza washamaliza kula chakula walichoandaliwa na mwenyeji wao Heriety. Ambaye aliahidi kuja kuwapa kisa kizima kilichofanya hadi dada yao akawa ni mwenye kuchanganyikiwa namna ile. Walifika mapema na walikuwa na shauku na kutaka kukisikia muda mrefu, ila waliambiwa wawe na subira, hadi ulipotimu muda huo ambao wapo wenyewe kwenye sebule ya kisasa. Macho waliyaelekeza alipo mwanamke aliyewazidi umri, waliyemheshimu kutokana na urafiki uliyopo kati yake na mzaliwa wa kwanza wa familia yao.
"Sasa wadogo zangu inabidi niwaeleze kisa hiki, maana mpo kwenye umri ambao sisi tuliupitia. Mjifunze na nyinyi, eneo ambalo kulikuwa kuna Nyoka msije mkakanyaga pia. Siwezi kuwaacha njia panda kwenye hili", Heriety alisema.
"Ndiyo dada", Eliza akaitikia.
"Yaani nilikuwa nasubiri hilo kwa hamu dada yangu, ndiyo maana nipo hapa. Hata ukikesha kueleza, nipo kusikiliza tu hakuna namna nyingine hapa", Spora alisema na kupelekea Heriety atabasamu kisha akajiandaaa kuwasimulia kisa hiko.

****


_MIAKA NANE ILIYOPITA___


Ukali wa jua bado haujadhirika, isipokuwa nuru yake ndiyo imeweza kubainika. Asubuhi njema aliyojalia Muweza, iliyosubiriwa kwa hamu kuu na viumbe waliyopo duniani. Ni zaidi ya siku kwa waliyopo subirani, wote waliyo na hamu ya siku hii walijawa na bashasha kuu. Wakiwa wamo ndani ya uzio wa wavu pamoja na lango la enzi, katika moja ya shule maarufu na ya siku nyingi Dar es salaam. Wavulana kwa wasichana, walisimama nje ya jengo kuu la shule hii ambalo lina maandishi yakitangaza jina lake.

Waliyokuwa wageni wa hapo walipata wasaa wa kutazama upande mwingine wa eneo hilo, ambapo kuna shule ya kimataifa ya Tanganyika pamoja na jengo la TAKUKURU ambalo ndiyo makao yake makubwa nchini. Ndani ya mwezi aprili, siku ambayo wanafunzi wengi wa kidato cha tano huripori kwenye shule walizopangiwa baada ya kufaulu mtihani wa kidato cha nne. Hapo ni ndani ya uzio wa shule ya sekondari Tambaza, ambayo ni ya miaka mingi mno na imesifika haswa kwa kutoa wasomi kadhaa na watu maarufu.

Ndiyo vijana hao walidhirika wakiwa na mavazi ambayo asilimia kubwa yalitoka shule ambazo walimalizia na si sare za shule hiyo ambazo ni nadra sana kuzipata madukani kutokana na upekee wa rangi yake. Wachache waliyofika mapema mno kwenye shule hiyo ndiyo waliweza kupata marafiki papo kwa kuonana asubuhi hiyo. Huku wengine wamejitenga kutoka na kukutana na watu wageni, na pia kutokuwa na mazeoa ya kuchangamkia watu.

Majira haya alidhirika binti mwenye mwili wa wastani, rangi ya ngozi ikiwa ni ng'avu. Mwenye nywele ndefu ambazo alizisuka mistari, fumbatio jembamba pamoja na unono kuanzia kiunoni kushuka hadi miguuni. Ujio wake mahala hapo ulipelekea wengi watupe macho, haswa wavulana kutokana na kuona kiumbe mwenye sifa kadhaa za kuonesha Muumba hakosei katika kuumba mwili wa mwanadamu.

Binti huyu kila alipopita na kukuta kikundi cha watu, basi aliacha salamu na kusogea hivyohivyo. Hakuonesha ria ile kuwapita kimya pasipo kuacha sabahi, hali hiyo ilifanya wengi wamwone ni msichana wa kipekee haswa. Hadi alipofika kwenye kundi la mabinti wenzake na kuwapa salamu, bado aliacha shingo za watu zikiwa zimeweka mgomo wa kugeuka. Hapo napo alionesha uchangamfu, alipokewa namna hiyohiyo kwa wapya wenzake wanaoripoti shuleni kwa mara ya kwanza.

Wavulana wengi wapo waliyotaka walau kulifahamu jina la msichana yule, ila haikutokea bahati hiyo. Wengi hawakupata ujasiri wa kuinua miguu, kusogea pale kwenye kundi la mabinti. Ulafi ndiyo kitu ambacho wangedhaniwa wanacho. Kuwasili kwa mgandisha shingo zao kukiwa bado kupo vichwani mwao, mara aliingia mganduaji wa shingo hizo na kuelekea upande mwingine.

Huyu hakuwa na sifa tofauti na yule aliyewanasisha, isipokuwa kipimo cha mwili tu. Huyu aliongezeka kidogo mwili, na kumfanya awe mzuri zaidi kuliko hata yule aliyetangulia hapo awali. Wa kwanza kumwona walipelekea macho tangu yupo mbali na kuanza kuambizana mmoja baada ya mwingine, hatimaye wakapeleka macho huko wakiamtazama msichama anayekuja kama vile hataki. Laiti kama ingelikuwa ni mara ya kwanza kumwona, basi kila mtu angeweza kusema kalazimishwa kuja shule kwa jinsi anavyotembea, hiyo ikawa ni hulka yake ya utembeaji jinsi ilivyo. Walitamani walau akifika afungue kinywa kuwapa sabahi ili waweze kusikia sauti, lakini haikuwa hivyo. Aliwapita kama vile ni majabali, hadi akafika pale kwenye kundi la mabinti wengine. Kitu hicho baadhi yao walikichukia mno, huku wengine wakiona ni jambo la kawaida tu kwani ndiyo mwanzo wa kuonana huo.

*MWANZO WA WANAFUNZI WAPYA SHULENI, JE UNA NINI HUO?
*DOKTA AESOP NA HERIETY WAMEAMUA KUFUNGUKA KUWAELEZA WENGINE, JE NI YAPI HAYO?





ITAENDELEA!!
 

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



________SEHEMU YA NNE____


.........Walitamani walau akifika afungue kinywa kuwapa sabahi ili waweze kusikia sauti, lakini haikuwa hivyo. Aliwapita kama vile ni majabali, hadi akafika pale kwenye kundi la mabinti wengine. Kitu hicho baadhi yao walikichukia mno, huku wengine wakiona ni jambo la kawaida tu kwani ndiyo mwanzo wa kuonana huo.



________TIRIRIKA NAYO

Hatimaye majira ya saa mbili asubuhi ndipo walimu walipoanza kupokea wanafunzi hao wapya, majira hayo ndipo ikajulikana waliagizwa kuleta vifaa kuendana na mchepuo wanausoma. Asilimia kubwa ya wasomaji walivificha sehemu ya kuingia getini, ilipofika majira hayo kila mmoja alishika cha kwake mkononi kwenda ofisi ya taaluma. Mkononi kila mmoja akiwa na fomu ya kujiunga shule hiyo pamoja na viambatanisho vingine muhimu. Zoezi la kupokea wanafunzi lilianza, huku wakipangiwa sehemu za kwenda baada ya kutoka ofisini humo.

Wanafunzi wa kidato cha tano baada ya muda walijuana wale wanaosoma darasa moja, majira hayo ndipo wale mabinti ambao walizinasa shingo za watu walipoweza kukutana wakiwa mchepuo mmoja. Huko baadhi ya wavulana waliyopangiwa nao usomi mmoja walikuwepo, haikuwa jambo rahisi kubaini tu wale warembo ni wa kusoma kombi ya sayansi. Tena ile yenye kuhusisha masomo ya hesabu, fizikia na kemia, yaani PCM. Hawa walipangiwa sehemu ya juu ya jengo la shule hiyo yenye ghorofa moja ambapo hujulikana na kuwepo wanafunzi wa michepuo hiyo.

Siku hii haikuweza kuwa ya masomo kutokana na ukaribisho wa wanafunzi wapya ndani ya shule hiyo. Waliyoweza kuendelea na vipindi vyao hawakuwa wengine, ila ni kdiato cha sita tu wenyeji wa shule hiyo. Wageni ikawa ni sehemu ya kupiga domo kusogeza muda mbele, kwani upokeaji bado haukuwa umemalizika. Majira haya vikundi kwa vikundi walikaa kuendana na jinsia zao, wachache ndiyo walichanganyika. Darasa la PCM soga likiwa limetawala, aliingia mwanafunzi mmoja ambaye kimavazi alivaa suruali duni chini huku juu akiwa na shati jipya. Viatu vyake havikuwa vikitangaza upendezaji, zaidi ya kuakisi hali duni kwa kijana huyo. Ambaye usoni sura haikuwa haba, alijaalia uzuri wa kiume ila haukudhihirika kutokana na uduni aliyokuwa nao.

Ingelikuwa ni vijana wa rika hili, basi wangeweza kumwita 'handsome' asiye na matunzo. Alipofika usawa wa mbele ya darasa, alitupiwa macho na baadhi ya watu. Hilo lilimfanya atabasamu na kisha akasabahi, wachache waliyoweza kuitikia huku wengi wao wakiwa ni wakimya kuonesha ria juu yake. Hilo hakulijali, yeye alipitliza moja kwa hadi hadi kwenye kiti kimojawapo klichokuwa kitupu. Hicho alikibeba na kuja kukiweka eneo ambalo kuna wavulana wenzake wakiongea.

"Niaje majamaa", Aliwasabahi huku akiwapa mkono mmoja baada ya mwingine. Upande huo alichangamkiwa, watoto wa kiume daima si wenye kupenda kuonesha majivuno isipokuwa wachache tu. Hao walimpa ushirikiano, alipoketi chini ni kila mmoja kuanza kumuuliza maswali kadhaa. Aliyajibu halafu akatulia soga alilolikuta hapo yaendelee. Maongezi yalivyokuwa yakiendelea ndipo yule kijana alipoweza kufahamika jina lake, aliitwa Jamal Mdoe. Ilibainika hilo baada ya kujitambulisha hapo mbele ya wenzake.

Wavulana waliyokaa naye muda mchache huyo kijana mwenzao, waliweza kubaini ni mtu ambaye ni mpenda kuongea na mchangamfu kupitiliza. Asilimia kubwa ya maongezi yake yakawa ni kuchekesha kupitiliza, kitambo kifupi akapelekea kuwa liwazo la kupoteza muda kwa wenzake. Hakuisha vituko, kila neno aliloliongea liliashiria kituko. Kicheko kikawapanda na hata wakajikuta wakipaza sauti, watoto wa kike wa humo ndani wala hawakuweza kujua ni kitu gani kinachoendelea.

________________

Mabinti wawili warembo walitawala mazungumzo ya upande wa wasichana waliyojitenga mita kadhaa kutoka walipo wavulana. Mmoja alikuwa ni mchangamfu na mwingine ni mwenye kufuatisha kile kinachosemwa hapo. Hawa vicheko vilipozidi upande wa pili waligeuza shingo na kutazama ila wasijue kinachoendela, kawaida ya mabinti ni wenye kupenda kila kitu hata mengine wasiyohusika nayo. Ndiyo hawa nao wakataka kumaizi haswa kile kiwafanyacho wenzao hadi wakafurahi namna ile, hawakuweza kwani maneno hayakuwa yakisikika ila mwongeaji aliyeonekana kutawala mjadala akawa ni kijana yule mgeni ambaye muda mchache uliyopita wametoka kumnyamazia salamu yake.

"Hii huyu anaongea yaani, si ametoka kuingia mdua mfupi uliyopita tu. Kawa mwenyeji hivi sasa", Binti aliyenasa shingo za watu kule getini, ambaye alisalimia kila kitu ndiye aliyesema hayo.
"Heryn umeonaeh! Anaonekana ni mpenda sifa sana na watu wa namna hiyo wala siwapendi ", Binti aliyeingia pale mlangoni na kuonesha ni mwenye majivuno alisema.

"Hapana Lui, huwezi jua jamani kuongea vile isiwe tabu. Ukumbuke kila mtu huzaliwa na tabia yake, kuongea haitoshi kumtuhumu mtu ni mwenye sifa", Mwanafunzi mwingine alisema.

"Enhee! Ni kweli Grace, unajua mimi nilichoweza kujua kuhusu mtazamo wa kila binadamu kwa wengine. Mimi nilipoingia pale getini na kuanza kusalimia kila mmoja, wapo ambao wameniona ni mwenye uchangamfu na wengine ninajipendekeza. Vilevile wewe Lui pale ulipopita na kuwanyamazia wapo waliyokuona ni wenye dharau. Jamani muonacho si kile mkidhaniacho", Heryn alisema.

"Aaargh! I don't care about that, salamu yangu si ya kila mtu waache wafikire hivyo. I will not die wakinidhani hivyo, they will waste their time tu", Lui alisema.

"No Lui, thats not right. Maelewano na kila mmoja ni nguzo muhimu kwenye maisha, kesho yako huijui", Mwenzao mmoja alishauri.

"No way, jamani lets cut this. Ninaremain na msimamo wangu huu huu always, tuongee mengine lakini si kuhusu hao", Lui aliongea kidharau.

Alipomaliza kuongea hayo, muda huo huo aliingia mvulana mwenye sare za shule hiyo ambazo hakueleweka alizipata wapi wakati wengine bado hawana. Huyu alikuwa mweupe na nadhifu kupiliza, akiwa amependeza mno hadi wengine waliyomo humo ndani wakaanza kumtazama yeye. Alisalimia wote aliyowakuta kisha akaenda kukaa upande ambao kuna wavulana wengine, hapo shingo za wasichana wote ziliwageuka kwake. Naye hakuonesha kujali zaidi ya kugongesha mikono na wenzake, asilimia kubwa waligandisha shingo kasoro tu Heryn ndiye hakuduwazwa namna hiyo.

"Girls mnajisahau sasa hivi, vipi huyo smart boy kawanasa akili zenu?", Heryn aliuliza.

"Exacty, he is so hot" Grace alisema na kupelekea Lui amkate jicho kali kwa ghafla.

"Lui whats wrong? Feeling jealous?", Msichana mwingine aliuliza na kupelekea wengine waanze kucheka.

"She is fall on him", Heryn alidakia na wote wakacheka huku wakimtazama yeye tu.

"pals stop that but wacha niseme ukweli. Sikutarajia kukutana na that kind of boy"

__________________


"Haya sukari ya warembo, sumaku ya kina dada. Naona uliwahi kuripoti kuliko sisi, hadi sare umepata", Jamal alimwambia yule kijana mtanashati.

"Nop Mazee, nimepata sample na kuongea na fundi wa shule hii nikashona ya kwangu maana nimesikia fundi wa hapa anachukua kipimo vya kiuno tu na urefu wa nguo. Si mwanzo wa kuvaa vituko huko", Kijana yule alijibu.

"(Akiweka mikono kichwani) Tobaa! Pick up itavesha turubai la scania sasa", Jamal akaropoka na wengine wakaanza kucheka.

"Mnajua huyu si mzima kabisa, waya umekatika", Kijana yule alisema huku akicheka kwa nguvu.

"Kwahiyo ushaniona mimi fyuzi boksi au, kwanza ujajitambulisha usije ukawa na sura ya sumaku tu ila jina ni sewage system ya Kariakoo. Tukujue jamaa"

"Okay naitwa Kelvin Donald ukipenda niite Kevi, ila jamaa nahisi huna bandama kabisa. Unayaongea hayakuchekeshi ila kwa wengine hawawezi", Kevi alisema.

"Okay ngoja niwe serious, unajua nini wanadamu ni watu ambao tunapenda sana kuishi marefu na tunajiona tunaishi maisha marefu. Lakini haipo hivyo ni mafupi tu haya, wacha nifanye kile moyo unapenda nisije nikaja kuondoka nikiwa sijatimiza kile kinachopenda moyo wangu. Napenda sana wanadamu wengine wawe na matabasamu kwenye nyuso, sipendi kiumbe anune. Ndiyo maana huwa ninapenda kuchekesha tangu nipo mdogo"

"Jamal ndiyo unapenda kuchekesha kachaa, ila wewe ni mtu usiyeonekana kucheka hata kidogo mbona upo hivyo na nimekugundua wewe ukicheka basi ni pale unapolenga wengine wacheke na si vinginevvyo", Mmojawapo alisema.

"Hujakosea Rama, ukweli ndani ya dunia hii sijaona chochote kile cha kunifurahisha hadi niweze kucheka. Vyote nivionavyo naamini ipo siku moja nitavikacha nitafurahiaje jambo la mpito majamaa. Najua kwenu nyinyi ni ngumu mno, ila mkae mkijua wote tunaishi kwa bahati nasibu ndiyo maana siwezi kufurahia life hii ila napenda wengine mfurahie"

"Una moyo wa ajabu, hujijali wewe unajali wengine. Muda wote nimekaa nikakusikiliza nikakuona ni mtu fulani hivi ambaye umeshikwa sana na imani. Ndiyo maana una hofu ya kifo muda wowote ule, wachache wapo kama wewe. You are special Jamal", Mmoja kati ya wavulana ambaye alikaa muda mrefu sana aliongea.

"But, bado siamini Jamal kama hilo tu ndiyo sababu ya wewe kutopenda kucheka, nadhani kuna jingine la ziada", Kevi alisema.

"Ni hilo tu hakuna jingine jamani, ila naomba mumshukuruni Mungu sana hajawapa mioyo ya kujihisi nyinyi ni wenye kufa siku yeyote maana mna amani. Ila kwangu haipo hivyo, ninajijua nimezaliwa ili nife na nitaendelea kubaki na imani hiyo tu", Pamoja na kuongea maneno hayo bado alionesha tabasamu kwa mbali kama vile ni mwenye kutania kile akiongeacho.

"Jamal nikuulize kitu kama hutojali", Mwingine alidakia.

"Upo huru"

"Jina lako linaonesha wazi ni Mwislamu, je wewe ni mtu uliyeingia sana ndani kwenye dini? Maana ninaamini wenye imani hizo ndiyo mara nyingi huwa namna hiyo", Aliulizwa.

"Tangu nipo kidato cha kwanza nimekuwa ni mtu mwenye kujitolea kusoma vitabu mbalimbali vya falsafa hivi ndivyo chanzo cha kunibadilisha kuwa hivi. Ninaishi kwa principal na ndiyo hizi na napenda kuona kila mtu akitabasamu. Tabasamu langu mimi kuliona si muhimu hata kidogo"

"Kumbe mfuasi wa kina Plato wewe", Kevi alisema.

"Haswaa ndiyo mwenyewe mimi", Jamal aliposema hivyo muda huohuo kengele ya hapo shuleni ilisikika, "Ohoo! Breki hii, tutokeni kama vipi tuanzeni kuzunguka mazingira ya huku nje"

Mwanzo wa wanafunzi wapya wa kidato cha tano, ukawa ni huo. Walizoeana na kuwa pamoja hawa wavulana kutokana na Jamal, huyu ndiye kiungo chao. Ilifika mahali darasa hilo wakawa ni wenye kuongozana pamoja kila mahali waendapo, walipenda kumsikiliza mchekeshaji wao kila alichokuwa akikisema. Huyu mara nyingi ni mtu mwenye kuwafurahisha watu ila hubeba maneno yenye ujumbe ndani yake. Kadri siku zilivyokuwa zikienda na hata kufikia muda wa masomo kuanza. Jamal alitokea kuwa kipenzi cha wengi mule darasani. Huyu mara nyingi alipenda kuona watu wana upendo kati ya wanafunzi wengine, hakutaka kuona mtu anamchukia mwingine na hata yeye kuwa anachukiwa.

Ilipotokea mmojawapo akikorofishana na mwingine, basi yeye ndiye huwa kiungo cha kupatanisha watu. Tabia yake ya kuchekesha hakuiacha na hata akiwa na mbele ya walimu ikawa ni hayohayo ingawa aliweza kuchunga staha tofauti na vile awavyo kwa wanafunzi wenzake. Hata mhula haukufika akatokea kuwa kipenzi cha walimu wengi hapo shuleni, pamoja na ucheshi wake alijawa na adabu kwa walimu hao. Upendo wake huo haukuishia darasani kwao tu, bali ulienda hata kwa wengine, Alipenda kumsaliamia na kuongea na yeyote yule, ila si kila mmoja aliyependa hilo.

Wanadamu tumejaaliwa mitazamo tofauti mno, fikra zetu daima haziwezi kuwa sawa lazima zingine zikinzane. Ndiyo ilivyokuwa kwa baadhi ya wanafunzi wengine, wapo waliyomuona ni mtu mwenye kupenda kujipendekeza. Wapo waliyomwona ni kero kwao kwa kufuatwa haswa na kina dada waliyopenda kufurahi kila wakiwa karibu naye. Huo ukawa ni mwanzo wa kuzaliwa ugomvi kwa baadhi ya wanafunzi waliyoweka mapenzi shuleni, wenye kutaka baadhi ya wasichana mahali hapo. Wapo wengine ambao ni mabanati kwa mtu mwenye mtazamo wa kawaida, angeweza kusema ni damu zao hazikuendana na Jamal. La! Haikuwa hivyo bali hawakupendezwa naye kutokana na mwonekano wake na kupenda mno kumwongelesha yeyote yule.

Hawa walitamani haswa itokee siku asiweze kufika shuleni hapo, au ahame kabisa kwa kutompenda. Pamoja na hayo bado Jamal akikutana aliwasalimia na hata wengine kumsonya, wapo waliyomwambia hawatakia habari hizo anazozifanya. Walimwambia awafanyie wengine ila kwao hapana, mmojawapo akiwa ni Lui. Binti aliyejawa ria, alitamka maneno hayo tena kwa kuonesha kuchukizwa naye. Jamal alipotafuta sababu ya binti huyo kuwa hivyo haikuipata. Kutokana na kutopenda mno kuwakwaza wengine, aliheshimu mawazo yao na hakuonekana akiwafanyia masihara ya namna hiyo.

Pamoja na hayo, bado alibaki kuwa kipenzi cha wengi shuleni hapo. Wala hawakuona chuki ndogodngo zilizokuwa juu yake. Karibu kila mtu alipenda haswa kuongea naye, mbali na kuchekesha alipobadilika huongea kwa busara na pia kuwa mshauri mzuri kwa watu. Siku zilivyoenda hapo shuleni, jina lake la Jamal watu waliamua kulifukia na likabaki ni kuandikika kwenye daftari au kwenye mtihani kumtambulisha yeye ni nani. Ila si kukaa vinywani mwa watu, Jay likawa ni jina jipya kutokana na herufi ya kwanza ya jina inayotamkwa. Akawa ni mwingine, hata ikafika kipindi akiuliziwa kwa jina halisi ikawa ni ngumu kumpata.

Muhula wa kwanza ukikaribia kuisha, mashindano ya kombe ndani ya shule hiyo yalianza, timu mbalimbali za madarasa zilichuana kuhakikisha zinapata kitita cha shilingi laki moja kwa mshindi wa kwanza.

*KEVI ADHIHIRIKA
*WANAFUNZI WAPYA NA VITU VIPYA
*NINI KITAKACHOJIRI?
*UPYA WAO UNA KIPI HASWA?





ITAENDELEA!!


 

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_______SEHEMU YA TANO_____

Muhula wa kwanza ukikaribia kuisha, mashindano ya kombe ndani ya shule hiyo yalianza, timu mbalimbali za madarasa zilichuana kuhakikisha zinapata kitita cha shilingi laki moja kwa mshindi wa kwanza.


________TIRIRIKA NAYO

Hapo ndipo wale wenye vipaji vya mpira wa miguu, walipopata wasaa wa kuonesha vipawa vyao mbele ya wengine. Ratiba ilitoka na kila baada ya mwisho wa vipindi basi timu mbili zilichuana kuweza kupata ushindi. Raundi ya kwanza ya mashidano, timu kadhaa zilifungwa huku zingine zikiwa zimeibuka kidedea. Miongoni mwao ni darasa la PCM liliweza kuibuka na ushindi na kujiwekea nafasi nzuri, mzunguko uliyofuata ikawa ni ya kupigania kusalia kwenye makundi maalum ambayo madarasa manne hupangwa na kutakiwa kusalia mawili tu waweze kuendelea mbele zaidi.

Hiyo ilijulikana kama mtoano, ambapo watakaopita daima huingia robo fainali. Majira haya Jamal yeye hakuwa mchezaji mpira bali alibaki kushangilia. Tena yeye ndiye aliyepelekea kikosi kizima kicheze kwa ari kutokana na uhamasishaji wake. Mzunguko huo wapo waliyochukia kutokana na ushangiliaji wake, ila ulipomalizika mpira basi yeye akawa ni mwenye kusuluhisha hilo kwa kuwaomba radhi kama walichukia. Mashindano yaliendelea na hatimaye ikaja kufika hatua ya nusu fainali, mzunguko ambao wengine hawatokuja kusahau uwepo wa Jamal kwenye darasa lao ndiyo huo uliwadia.

Shuleni Tambaza mwaka huo katika vikosi vyote vya madarasa, kimoja tu ndiyo kiliogopwa kwa kusheheni wachezaji wengi wenye ujuzi wa hali ya juu. Hawa ni wanafunzi wa kidato cha sita mchepuo wa biashara au ECA. Timu ilihofiwa haswa kwani wao ndiyo wanatetea ubingwa na bado ni kikosi ambacho hakijapta mpinzani.

Siku hii kabla ya kuanza mechi kama kawaida yake aliwapa ari wenzake na kuwaambia ushindi ni jambo muhimu kwao, aliwaasa kutojali kuwa wanapambana na kikosi kikubwa namna gani bali wao waangalie kushinda tu na si kushindwa.

Mpambano huo hadi unaanza ni wanafunzi wengi kutoka madarasa tofauti waliyokuwa na hamu ya kuwaona wanafunzi wa kidato cha tano kama watafua dafu kwenye hilo. Mchuano ulianza kwa kila mmoja kuonesha upinzani wa hali ya juu, mabingwa watetezi walidhihirisha kwa kutaka goli zaidi. Walitumia muda mwingi kwenye kushambulia na kutawala eneo la kati la kiungo, uchezaji wa namna hii awali timu ya PCM ilionekana kumudu ila kadri muda ulivyokuwa ukienda walishindwa kustahimilia wakaanza kushambuliwa. Golikipa wao akawa na kazi kubwa, aliokoa mashuti mengi na hata kutoa nje na kusababisha kona. Mpambano ulienda hivyo na hadi kufikia mapumziko, golini kwao zilishapigwa kona sita.

Muda ambao wachezaji wanapumzika Jamal aliutumia kwa kuwaasa, "Jamani tukazeni haswa hima tufunge au tufike matuta nao. Kufungwa ni mwiko, kushambulia kupata goli mkumbuke jamani".

Aliwakumbusha wenzake ambao majira hayo walikuwa wakiendelea kunywa maji, haikuchukua muda mrefu wakarejea uwanjani tena kuendelea kupambana kuendelea kuusaka ushindi kwa namna yeyote ile. Mpira ulianza kwa namna yake, walionesha kushambulia kutafuta goli ila ulinzi wa eneo lile ulikuwa ni dhabiti, mara chache waliweza kumzidi ujanja kiungo mkabali wa timu ya ECA ambaye ndiye aliyepoteza mawasiliano ya viungo wao uwanjani. Huyo alijua vyema kuvuruga mipango yao ya kusonga mbele kutafuta goli, baadhi ya pasi alizinasa mara nyingi na kuwaharibia.

Bado haikuwa sababu ya kushindwa kuendelea kupambana, walilisaka goli kwa nguvu na ilifika mahali hata baadhi ya walinzi wakawa wanapanda mbele. Hilo likawa ni kosa kubwa, ambalo hawakulitambua. Walishambulia namna hiyo mara mbili, ila kibao kilikuja kuwageukia dakika ya sitini ya mchezo, walipopanda mbele walishambuliwa kwa kushtukiza wakajikuta wakifungwa goli ambalo liliwavunja moyo hadi baadhi ya wachezaji. Jamal jambo hilo lilipotokea alijikuta akifika eneo ambalo husimama mpangaji kikosi wao na kuhimiza watu waendelee kucheza muda bado haujaisha. Majira haya ndipo walizidiwa na winga wao wa kulia tu ndiyo alionekana kuwa hatari kwa timu ile, naye hakudumu uwanjani aliumizwa na kushindwa kuendelea na mchezo.

Jambo hilo kwa haraka zaidi lilimfanya Jamal ainuke hadi eneo amblo kuna jezi za timu yao, alizitwaa zilizosalia na kukimbilia eneo la kujificha ambapo alizivaa. Alirejea kwa kasi ambapo watu walishangaa kumwona kazivaa nguo zile, yeye hakujali alifika aliomba viatu na soksi akapatiwa na wanafunzi wenzake. Alipomaliza akakimbia kwa haraka hadi usawa wa ukumbi mdogo wa shule hiyo, ambapo upo jirani na uwanja wa mpira.

"Jamal sijawahi kukuona ukicheza toka mashindano yanaanza", Anayepanga kikosi alimwambia.

"Oska sina muda wa kukueleza hilo, sabu fasta ongea na jamaa wa mezani huyo. Huoni hatuna wa akiba jamaa", Alisema.

Mpango wa kuingia uwanjani alifanyiwa na hatimaye akachukua nafasi ya winga aliyeumia, hajawahi kuonekana akicheza mpira ila hapo aliwashangaza wengi kwa kuamua kuingia ndani. Eneo aliloumizwa mchezaji aliyetoka lilikuwa ni mbali kutoka goli la timu pinzani. Hivyo waliuanza mpira kwa kukipigiana pasi za chini kwa chini wakiwa wanajihami haswa wasiweze kuongezwa goli. Usambazaji wa mipira haukufika mbali waliporwa na wachezaji wa ECA wakaanza kupandisha mashmbulizi kwa nguvu zote. Majira hayo kiungo mkabali wa PCM alifanikiwa kuingilia pasi zao na kisha akaanza moja kwa kumpigia kiungo wa kati, huyu wala hakutaka mbwembwe nyingi. Alitembea na mpira na akaona mbele wameweka ukuta mkubwa, aliamua kurejea nyuma.

Kitendo cha kurudi kuelekea lilipo goli lake, kilifanya baadhi ya wachezaji wa ECA wapande mbele. Kungo wa kati huyu alipoona hiyo ilikuwa ni nafasi njema aliutungua mpira pasi ya juu kuelekea upande wa winga ya kulia. Huko alifanikiwa kuulenga vyema ambalo ulimkuta Jamal aliyetuliza kifuani kisha akaushusha chini na kuanza kukimbia kwa kasi akiingia ndani. Mchezaji wa kwanza wa ECA kusogea mbele yake alivutwa upande wa kushoto, alipojaa Jamal akapita kulia ambapo alikutana na mwingine aliyetanua miguu kumuwekea kizuizi. Huyu alimpiga tobo la kiufundi akiruka miguu yake akazidi kuchanja mbuga, aliyesalia mbele majira hayo ni golikipa tu. Naye hakusubiri asogee langoni zaidi alitoka kumfuata kwa kasi, alidhamiria kumzuia na alimvamia na matokeo yake ni kujikuta akilambwa chenga mbaya na lango likabaki wazi. Hapohapo Jamal akasawazisha bao hilo na kusababisha shangwe zilipuke, faraja zilizopotea hapo awali kwa kufungwa zikarejea.

Hatimaye mpira ukawekwa kati, ikiwa ni dakika ya sabini na tano. ECA waliuanza pira kwa kupiga pasi za kasi zaidi na kuelekea mbele. Mpira waliporwa na beki wa kulia wa PCM ambaye aliulenga moja kwa moja kwa Jamal, huko haukuweza kufika tena kutokana na ulinzi wa wapinzani kujua hatari yake. Walimkaba vilivyo na kuutoa nje, mpira ukawa ni wa shambulia nikushambulie hadi inafika dakika ya themanini na tano. Muda huo PCM hawakuwa na imani ya kuweza kushinda na walichokifanya ni kulinda wasiweze kufungwa jingine, timu karibia yote ikarejea nyuma huku wachezaji wachache tu wakisalia mbele akiwemo strika.

Zikiwa zimebaki dakika mbili tu mpira kumalizika, mpira ulikuwa ukichezeka katikati ya uwanja na majira hayo ni PCM waliyokuwa wanaumiliki. Walipiga pasi kutoka upande mmoja hadi mwingine, majira haya Jamal alishahama namba kutoka winga ya kulia akasogea ya kushoto. Kiungo wa kati alimwona vyema mahali alipokuwepo, aliupeleka mpira kwake. Huu ulikuja wa usawa wa kiuno na ukamlazimu kuunyanyua mguu mmoja kuuliza mpira, alipouweka chini tayari mabeki wanne walishamfuata kumkaba. Jamal alipowaona aliamua kufanya kama vile anarejea eneo la kati ya uwanja. Hawa walipunguza kasi ya kumfuata watatu wakarejea nyuma kuweza kuhakikisha hakuna mpinzani atakayepenya. Kitendo hicho hawakujua kama wamefanya kosa kubwa, majira ambayo kipa wao kasogea mbele kidogo.

Walipokuja kutahamaki, Jamal hakufika kati badala yake aligeuka na shuti la nguvu la juu. Golikipa wao alishindwa hata afanye nini zaidi ya kuutazama mpira ukitua wavuni, mwamuzi alionesha ishara ya kuweka mpira kati kwa kukubali hilo ni goli. Yakifanyika hayo muda huo wachezai wenzake wanamkimbilia mfungaji, Jamal alianza kujihisi ndivyo sivyo aliyumba mara moja kurudi nyuma na alipokaa sawa akaangukia kifua chini. Waliyokimbia kwa kasi walifika karibu yake na kusimama kwa mshangao, hata kushangilia kwao kulikatika papo hapo. Jamal alipoanguka hivyo aliinua kichwa mara moja wakajua ni aina ya ushangiliaji wakaendelea kupiga kelele, ila alipokilaza tena ikawa ndiyo basi hakuamka. Washangiliaji safari hii hawakujua kitu, muda wa kutoa mashabiki na kuanzisha mpira ndipo walipokuja kubaini mwenzao hajitambui.

Ilibidi atolewe kwa haraka na mpira uendelea kwani hakukuwa na muda wa kutosha, Jamal alienda kupatiwa huduma ya kwanza na hali ilipokuwa haijakaa sawa alikimbizwa haraka hospitali ya taifa(Muhimbili) ambayo haipo mbali kutoka hapo shuleni. Mpira uliendelea na hadi kipenga cha mwisho kikapulizwa, mabingwa watetezi wakwa wametolewa kwenye mchuano huo na PCM wamefika fainali tayari.

______________________

Kufumbua macho kwake alianza kuusikia mlio wa mashine ya mapigo ya moyo, alishazoea kujikuta yupo ndani ya chumba chake kila anapoamka ila siku hii akajikuta yupo mahali kwingine. Ambapo si pageni kwake, aliamka na kutaka kukaa kitako ila akazuiwa na kuambiwa ajilaze. Alipotazama macho mbele alikutana na sura ya Tabibu, asiye mgeni machoni mwake. Jamal alimshangaa kwa sekunde kadhaa Daktari yule, ambaye anamtazama kwa umakini mkubwa mno.

"Jamal", Aliitwa.

"Imekuwaje?", Aliuliza.

"tulia kwanza", Alipoambiwa neno hilo ndipo akaanza kukumbuka kile ambacho kilimkuta, hadi mara ya mwisho macho yake yanafunga. Alipoelewa sababu ya kuwa hapo aliuliza, "Sasa hivi saa ngapi?".

"Saa nane mchana, ulipoteza fahamu tangu jana jioni", Dokta alimjibu kisha akaendelea, "najua una kipaji cha mpira Jamal ila kwa usalama wako nilikwambia usicheze, kwanini umecheza?"

"Daima ninapenda sana darasa langu liwe na furaha, lilipoingiwa na simanzi ndiyo nikafanya hilo"

"Unawapenda sana wanadamu lakini jiangalie wewe pia, wewe ni mgonjwa Jamal hilo unalijua. Kuwa makini sana, kama ukipenda wengine pia mpende na mama yako pia. Usimtese hivi, jana kashinda kwenye benchi aking'atwa na mbu hadi sasa hivi"

"Sawa nimekuelewa"

"naomba umwite Mama, mwambia mwanae nipo salama"

Hatimaye Mama Jamal aliitwa, aliingia ndani na kujionea hali ya mwanae na hapo akajiwa na faraja. Jamal alishindwa hospitalini siku hiyo ya Alhamisi, ijumaa aliruhusiwa na kurejea nyumbani kwao ambapo alipumzika hadi jumapili. Siku ya jumatatu ambapo alitakiwa shuleni kuendelea na mitihani alifika kama kawaida, siku hii alipokewa kwa shangwe kubwa na wanafunzi wenzake wa PCM hata wa madarasa mengine walifika na kumpa pole kwa hali iliyomfika. Muda wa kukaa mstarini ilibidi aitwe mbele kuongea machache, kutokana na jinsi suala hilo lilivyogusa shule nzima. Aliposhuka ndipo Mwalimu wa zamu akaamua kuliongelea na yeye, ndipo hapo Jamal alipotambua kuwa wanafunzi wenzake na walimu walifika kumjulia hali ila hakuwa amerejewa na fahamu majira hayo.

Muda wa kuingia darasani kuendelea na mitihani ya mwisho wa mhula ulifika, siku hiyo ilipita na hatimaye siku ya jumatano ambayo shule nzima ilimaliza mtihani ilifuata. Siku hiyo majira ya jioni kulichezwa mechi ya kugombania mshindi wa tatu, kumalizika mchezo huo ECA wakashinda na kuwa na uhakika wa kujishingia shilingi 25000. Siku ya alhamisi ambayo ni ya kufunga shule, pia ikiwa imepangwa kuchezeka fainali ya michuano ya mpira wa miguu shuleni hapo. PCM na EGM wakawa wametinga fainali, mpambano ulisubiriwa kwa muda mrefu kuweza kutimia. Siku hii ya michezo ambayo ilipangwa pia kukaribisha wanafunzi wa kidato cha tano, muziki wa kukodishwa uliwekwa hapo.

Mashindano ya utangulizi yalianza na hatimaye mechi yenyewe ikaja baadaye, waamuzi maalum walikodiwa na waliichezesha hadi mchezo ukaisha bila majibu na kupelekea wafikie kupiga penalti. Upande huu wa bahati Mungu akawa upande wa PCM ambapo walishinda kombe hilo kwa mikwaju minne kwa miwili.

Furaha ikawa kwa timu nzima ila siku hii aliyebebwa juu juu akawa ni Jamal, bado mchango wake kwenye mchezo mgumu haukuwa umesahaulika kwani bila yeye wasingelifika hapo. Siku hii ndipo kijana wa watu akamwona Liu kwa mara ya kwanza akija kumkumbatia huku akifurahia, alijiona wa pekee kijana huyu hata akasahau yale asiyopaswa kuyawaza.

Hatimaye walijinyakulia zawadi yao huku jina lake likiimbwa tu, hadi anabebwa juu majira ambayo muziki unaondolewa uwanjani na kupelekwa kwenye ukumbi mkubwa. Huko ndipo Jamal alipokuja kuona mambo ni ndivyo sivyo, kawaida huwa wanaanza kushindanisha wenye vipaji mbalimbali na hata bila kuchunuana humo ndani watu walipewa nafasi ya kutoa burudani. Huku ndipo kipaza sauti kikamwangukia Jamal, akaanza kufanya ucheshi wake ambao alichekesha wengi mno. Katikati ya fujo zake za kufurahisha watu alijikuta akitaja jina la Lui, hapo wengi wakaanza kumtazama binti huyo.

"Najua wengi mshazoea kumwita Lui, alibatizwa kwa kuitwa Luigina. Leo nitapenda nimwite kwa jina la Gina hapahapa, mama wa vipodozi. Siku ukija kukosa hivyo vipodozi na una watoto wamekuzoea vile, nahisi watamuuliza Baba yao huyu mgeni kafika lini", Huo ulikuwa ni sehemu ya utani wake, ulichekesha wengi ila kwa Gina hakuonesha kufurahishwa nao zaidi ya kuinamisha sura chini alipotazamwa na wengi.

Jamal aliposhusha kipaza sauti, Gina alimfuata moja kwa moja hadi alipo na kumwomba kwenda kuongea naye nje ya ukumbi huo mara moja. Bila ya hiyana alitoka hadi nje ambako hakukuwa na mwanafunzi yeyote, kufika huko ndiyo binti akabadilika sura na kuonesha kuchukia.

"Jamal please sipendi kitu nikisema sipendi jua sipendi kweli, si nilikwambia. Kukumbatia kinyago wewe isiwe sababu ya haya yote. Naomba tusifike mbali, elewa siwapendi watu wa aina yako thats why sitaki hata kukusalimia. Usilazimishe mambo kituko wewe", Gina alimwaga maneno mfululizo, alipomaliza hapo aliingia ukumbini akimwacha kijana wa watu hana raha.

*NINI KIMEMKUTA JAMAL?
*GINA HATIMAYE AONEKANA, JE ANA TATIZO GANI NA JAMAL?
*MAMBO YANAZIDI KUJIFUNGUA




ITAENDELEA!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



____SEHEMU YA SITA______


"Jamal please sipendi kitu nikisema sipendi jua sipendi kweli, si nilikwambia. Kukumbatia kinyago wewe isiwe sababu ya haya yote. Naomba tusifike mbali, elewa siwapendi watu wa aina yako thats why sitaki hata kukusalimia. Usilazimishe mambo kituko wewe", Gina alimwaga maneno mfululizo, alipomaliza hapo aliingia ukumbini akimwacha kijana wa watu hana raha.



______________TIRIRIKA NAYO

Jamal wala hakutarajia kama angeweza kukutana na jambo kama hilo, yeye alizoea kufanya utani na alidhani tayari Gina na yeye maelewano yapo. Kumbe alimuwekea maigizo na hapo ndipo akamaizi hilo jambo, nafsini alijiuliza ni kitu gani ambacho kilimfanya binti yule awe vile. Hakuwahi kumkosea hata lakini amejikuta akiwa miongoni mwa wasiyoiva naye chungu moja bila hata kuwana sababu. Maneno aliyomwagiwa wala hayakusikika na mtu isipokuwa alikuwa peke yake tu aliyeweza kusikia yote yale hadi ikafikia muda ambao hali yake ilianza kubadilika ghafla.

Jamal alianza kuhema kwa hali ya kawaida, ghafla hali ikabadilika na akaanza kutoa pumzi kwa nguvu. Alipoona hali hiyo moja kwa moja alikimbilia kuketi kwenye kiti kilichopo pembezoni mwa ukuta wa ukumbi huo. Huko wala hakuna aliyejua kilichomtokea nje. Alijikuta akiishiwa nguvu tu na hatimaye akajigemeza kwenye mgongo wa kiti cha plastiki huku akiendelea kupumua kwa nguvu. Akiwa namna hiyo alianza kuhisi pua ni zenye kutekenya, kukiwa na maumviu kwa mbali kama vile ni mwenye kuingiwa na maji puani. Hali hiyo ilimfanya ainue uso juu kwa haraka, pua hazikuweza tena kumsaidia kupumua zaidi ya mdomo tu ambao aliuacha wazi kama vile haukuwa unaweza kufunga.

Aliendelea kuvuta pumzi kwa nguvu na hata mwili akauhisi umeanza kumpungua nguvu kuliko hata awali, safari hii hata mkono hakuweza kuunyanyua alilegea haswa. Hakutokea mtu yeyote yule majira hayo, wanafunzi wote ni wenye kuburudika na muziki. Walimu walishaondoka wengi wao kwani siku hiyo ni siku maalum ya kufunga shule, muda mchache hiyo nguvu ya kuinua shingo juu nayo ikakosekana. Akaipeleka pembeni na hapo ndipo kukaonekana jingine. Kile kitekenyecho pua hapo awali kilivuja safari hii, si nyingine bali ni damu ndiyo ilimtoka bila hata kuweza kuzuia.

"Mungu, Mungu nilifanya nini mimi hadi kustahiki haya. Sijawahi kumfanyia ubaya yeyote mtu hadi niadhibiwe namna hii", Aliongea kwa sauti hafifu na kupelekea atolee pumzi puani na hapo kupelekea damu zilizobakia puani ziweze kutoka zaidi.

Haikuchukua muda mrefu, Jamal aliona akipoteza nuru ya maho yake, na hatimaye akahisi giza likitanda mbele. Hakujua kile kinachoendelea tena hadi pale alipokuja kufumbua macho yake, akajikuta yupo mahali asipopatambua ambapo palifanana kiasi chake na kule ambapo alipojikuta baada ya kunaguka uwanjani. Si kwingine bali ni hospitali ndipo alipojikuta, ambayo wala hawakuhi kufika tangu azaliwe. Alipoangaza upande wa kushoto kwake aliona mrija wa dirpu ukiwa umechomekwa mkononi mwake, aliporejesha macho upande wa kulia. Alikutana na meza pamoja na kiti vikiwa vipo mita kadhaa kutoka hapo alipo.

Hakujua ni wapi hapo alipofikishwa majira ahyo, eneo ambalo madirisha yake ni yenye vioo vya kusukuma. Pageni kwake na kumejaa ugeni kwa kila kitu, akiwa namna hiyo alijitazama mavazi yale aliyoyavaa. Ndipo alipotambua ni mwenye 'vesti' tu kwa juu, alishangaaa. Alipojaribu kufungua shuka chini kwa nguvu hafifu, suruali yake ya shule ndiyo aliishuhudia. Swali lililobaki kichwani mwake ni juu ya kufika kwake mahala hapo, napo hakupata jibu ndipo akaanza kukumbuka kwa mara ya mwisho alipokuwapo.

Kumbukumbu nazo hazikumnyima ushirikiano juu ya hilo, aliweza kung'amua juu ya kukereka kwa Gina na kumtolea maneno machafu. Pia kujia na hali mbaya, alipofikiria hilo alitabasamu tu na si kuhuzunika. Jamal alijionesha ni mtu wa ajabu namna gani, kwa yote aliyofanyiwa bado alipokumbuka aliishia kuonesha bashasha tu, ingelikuwa mwingine ni wa kuumia tu ila huyu aliishia kufanya hivyo.

Akiwa namna hiyo, haikuchukua hata muda mrefu. Mlango ulifunguliwa, alijikuta akitupa macho huko kwa hima kuona huyo aliyeingia. Ndipo alipoweza kumshuhudia Mwanamke aliyevaa gwanda za kijeshi zenye mabaka pasipo kuwa na kofia, juu akiwa amelifunika vazi lake na koti la kitabibu na shingoni akiwa amebeba kipima mapigo ya moyo. Haikuhitaji elimu ya ziada kuweza kumtambua huyo ni tabibu, ila kuvaa gwanda namna ile alibaki akijiuliza ni wa kutoka wapi. Hakuwahi kufika hospitalini na kukuta daktari wa kijeshi, hii ndiyo mara ya kwanza baada ya kuamka hapo kitandani. Mwanamke yule alijongea hadi akafika mita chache tu kutoka kilipo kitanda, alibaki akimtazama kwa tabasamu hafifu.
"Jamal, pole sana", Alisema.

"Hapa ni wapi, na nimefikaje?", Aliuliza.

"Jana majira ya kuelekea alasiri ulipoteza fahamu ukiwa shuleni, ndipo wenzako wakakuleta hapa"
"Jana?! Inamaana imepita siku moja nipo kitandani? Ok niambie ni wapi?"

"Humu ni ndani ya kambi ya Ngome, makao makuu ya JWTZ nchini. Hii ni hospitali ya jeshi, nadhani umeshaelewa ukaribu wa kutoka shuleni kwneu hadi hapa na umbali wa kutoka pale hadi Muhimbili ni mkubwa ndiyo maana upo hapa"

"Sawa nashukuru, nilijua nimetaifishiwa uhuru wangu kwa muda kuona hilo gwanda nasubiriwa niamke tu nipewe kibano"

"(Akicheka) Wala hakuna kitu kama hicho, ila Jamal nilichokigundua kwako nadhani si kigeni unakijua fika maana inaonekana si mara ya kwanza kukutwa na kitu kama hicho. Hili la jana ni kukerwa na kitu, naomba usiwe kwenye hali kama hiyo"

"Tabasamu ndiyo huficha hisia za mimi kuwa na hali fulani isiyopendeza kama vile kukasirika au kufaidhika. Lakini ukumbuke mchele humeza maji, lakini si kila kiwnago. Itafikia kingine wala hakitaweza kumezwa, unajua nini namaanisha Dokta"

"Niite tu Doreen ukipenda au dada Doreen si mbaya, sijaelewa"

"Ok, ni hivi hali ilizidi kiwango ndiyo maana nikawa vile. Maji yalizidi unga dada Doreen"

"Kwa ulichokisema sikulaumu mdogo wangu, ninahokushauri epuka vile vinavyokufanya uwe hivyo. Ndiyo njia nzuri tu ya kuweza kuishi hapa duniani kwa muda uliyobaki lakini si kuendelea kuweza vitu kama hivyo kichwani. Matokea ni kuwa na msongo wa mawazo, Ndiyo unaweza kuugua, tuachane na hayo. Nilipojairbu kuuliza kuhusu uwepo wa ndugu zako hakuna mwanafunzi mwenzako aliyeweza kujibu, ila kuna mmoja tu ndiyo aliahidi kuja leo naye alishirikiana na wengine kukuleta"

"Classmate wako Jamal, anayeonesha kukujali kuliko wote. Au una wangapi wanayofanya hivyo?"

"Nina idadi kubwa ya watu wanaonipenda shuleni, ingawa moyo wangu umewekwa kufuli kwa wavaa sketi, naweza kumjua jina"

"(Akitabasamu) Heriety ndiyo jina aliloniachia pamoja na namba yake ya simu, atarejea tu ameenda hosteli kwao"

"Heriety Job itakuwa"

"Hilo ni juu yako Jamal mimi siwezi kufahamu, ila unabidi uwataarifu jamaa zako kutokana na hali yako hiyo mdogo wangu"

"jamaa niliyenaye hivi sasa hapa jijini ni mjomba wangu sina mwingine na huyo nadhani hivi sasa yupo kwenye harakati za kunitafuta mimi. Mama ameshaondoka kurudi Tanga"

__________________

Upande wa ndani ya hosteli za wasichana zilizopo nje ya shule ya Tambaza, siku hii wasichana wengine walikuwa ni wenye kupakia mzigo yao waweze kuondoka kurejea makwao. Ni muda wa likizo ndiyo huo umewadia, hawawezi tena kusalia, nyumbani walihitaji sana kupumzika kwa muda ili waweze kurejea tena na kuendelea na masomo yao. Majira hayo hadi Gina alikuwa ni mwenye kuweka mizigo yake vizuri aweze kurejea nyumbani, Heriety pekee ndiyo hakuwa amefanya hivyo. Alivaa vizuri tu kwa kutoka lakini hakuwa amejiandaa kwenda nyumbani kwao. Hakupanga hata nguo moja kwenye begi lake, hali ambayo ilimfanya hata hata Gina rafiki yake ashangae

"Heryn una mpango gani jamani? Mbona upo hivyo, unajua mama atafika muda si mrefu hapa na umenipromise tunakueskoti hadi kwenu", Gina alisema.

"Hapana nimebadili msimamo Gina, siwezi kuondoka hadi Jamal nihakikishe anawasiliana na ndugu zake. Mimi ndiye niliyeacha namba yangu, sina budi kulibeba hili", Heriety alijibu na kumfanya Gina amtazame kwa macho makali.
"Jamal anakuhusu nini wewe? Humjui alipotoka zaidi ya kujuana naye class. Leave his matter, hana umuhimu in your life"

"He! Gina kuondoka na wewe isiwe iwe namna hiyo, hata wewe umenijua shule tu na si vinginevyo mbona hujiulizi mimi nakuhusu nini hadi utake kunibeba kwenye gari la kwenu. Just go, ushanitibua kabisa. Be my friend haimeans unipangie maamuzi"

"He! Yamekuwa hayo Heryn"

"Thats all, sina majadala unaweza kwenda kama unajiona ni mwenye kuishi bila shida maisha yako yote. Kesho yangu mimi siijui, yako unaijua? Unajua nani atakuwa msaada wako. Even Jamal ni wa kukutana naye miezi hata sita haijafika, bado siwezi kuacha katu kumsaidia. You may go"

Heriety alipomaliza kuongea maneno hayo, alichukua simu yake tu na kutoka ndani ya chumba hicho wanachoishi. Alimwacha mwenzake akiwa amesimama tu, katika siku ambayo aliudhiwa na Gina. Basi hiyo ni mojawapo, alijuta haswa kuweka urafiki naye. Mtu ambaye wala hakuwa na huruma na wengine, kiasi cha kutaka kumwacha asiye na hali atelekezwe hospitali tu. Alifahamu hilo na wala hakumaizi kama chanzo cha kijana yule kulazwa ni huyohuyo, laiti angelikuja kubaini hilo kama si kuvunja urafiki basi wangeweza kuweka kuweka ugomvi kwa jinsi kila mmoja alivyokuwa akishikilia upande wake.

Gina alipoachwa peke yake chumbani aliishia kusonya kisha akasema, "kalogwa huyu, yule karagosi ana kitu gani cha kuweza kumfanya ahangaike namna hiyo. Mtoto wa kishua unajileta kwa kile kijitu, loh! Siwezi kuwa na rafiki kama huyu hata".

Alipoyaongea hayo alijibwaga kitandani, huku akionekana ni mwenye kusubiri jambo kuliko muhimu kuweza kujiri. Binti huyu ni mwenye moyo wa ajabu mno, hakuwahi kuudhiwa na kijana yule ila alionesha chuki za wazi kwake. Kiasi cha kuweza kutokuwa na huruma naye, chuki isiyo na chanzo kabisa ndiyo ipo moyoni mwake.

_____________________

Heriety alifanikiwa kufika hospitalini, alimkuta tayari Jamal ni mwenye siha ya ahueni ingawa nguvu hazikuwepo mwilini mwake. Uhakika wa yule aliyeweza kutoa msaada kwake ndiyo aliweza kuuona mahala hapo baada ya kumwona binti yule ambaye aliambiwa na Tabibu yule kuwa ndiyo kamsaidia hadi kufikia akawa hapo. Hali aliyokuwa nayo kijana yule ikawa ni ya kuridhisha, kilichobaki ikawa ni kumtafuta mjomba wake huyo ambaye aliambiwa yu ndani ya jiji la Dar es salaam.

Hilo nalo halikuweza kuwa tabu, iliweza kujulikana mjomba wa Jamal ni daktari mkubwa wa hospitali ya taifa ya Muhimbili. Huyu alipigiwa simu na kuelezwa hali halisi aliyo nayo Jamal, ilimchukua muda wa dakika kadhaa kuweza kufika hapo ndipo akamwona mpwa wake akiwa na yule binti aliyejitolea kumsaidia hadi kuweza kutaaarifiwa ndugu yake. Hapo ndipo pia Madaktari wawili kutoka sehemu tofauti waliweza kukutana. Dokta Doreen aliweza kumwona mwenzake mwenye taaaluma kama hiyo ndani ya jiji. Ukawa ni mwanzo mwingine wa kujuana kwao, huku Jamal akiwa chachu ya hayo kutokana na tabia yake ya ucheshi aliyoidumisha humo.

"Jamani niwashukuruni haswa kwa kuweza kumpa msaada mpwa wangu", Mjomba wa Jamal alishukuru.

"Usijali Dokta, ni jukumu letu kuweza kutoa msaada kwa yeyote mwenye tatizo. Wa kumshukuru ni huyu binti aliyeweza kuhakikisha huyu hadhuriki kwa lolote", Dokta Doreen ambaye majira hayo wala hakuwa na koti la kitabibu alisema, tena akimwashiria Heriety ambaye alitoa msaada kwa Jamal.

Mjomba wake Jamal alimgeukia Heriety na kumwambia, "Binti, nasema asante sana ila kusema hilo naona kama vile haitotosheleza. Umenisaidia sana, huyu kwa sasa ndiyye ndugu pekee ninayeishi naye hapa jijini sina mwingine. Kutoonekana kwake nyumbani kwa siku ya jana, kumenifanya nihangaike haswa. Jioni hakuonekana nikaja shuleni napo ikawa hakuna yeyote yule zaidi ya kukuta lango limefungwa na mnaanza likizo". Alipomaliza hayo alimgeukia Jamal na kumwambia, "jamaa na wewe unajua staili yao unayopenda kuishi inatatiza, umekataa kuongoanza na Paki. Je nisingejua?"
"Anko haina haja ya kufuatana na Paki, kikubwa tushukuru Mungu mimi ni mzima. Sijawa mtoto wa kuchungwa kila muda, napenda nifurahishe wengine nifurahi. Hivyo kuwa na mtu najihisi sipo huru kufanya hayo", Jamal alisema.

"Ila Jamal anachosema mjomba wako ni sawa tu, unatakiwa uwe na mtu kwa hali hiyo", Dokta Doreen alisema.

"Jamani kwani Jamal anaugua nini? Mnajua sijajua", Heriety alisema na kupelekea mjomba mtu na Dokta Doreen watazamane.

"Hali ileile kama iliyomkuta siku ile alipomaliza kucheza mpira, ila jana tu alikuwa na stress ndiyo akawa vile. Huyu hatakiwi hata kukasirika", Dokta Doreen alisema.

"Inamaana huyu naye ana presha?", Heriety aliropoka kutokana na uelewa wake juu ya alichokisikia.

"Binti unajua nini, kila binadamu ndani ya dunia hii ana blood pressure. Hata wewe mwenyewe unayo, ila unahitajika haswa kuwa nayo makini. Haitakiwi kuwa juu sana wala kuwa chini sana, iwe normal. Ikizidi ni matatizo. Sasa huyu mwenzako ilimzidi, najua utashangaa sana kutokana na huu mwili wake na hilo tatizo analoumwa", Mjomba wake Jamal alieleza.
"Nilizoea ni tatizo lenye kuwakumba watu wanene tu ila nashangaa hata huyu, ila nasikia ukifanya mazoezi unaipunguza na kuwa ya kawaida"
"Ni kweli, ila kwa huyu ni hapana hatakiwi kufanya hivyo. Ndiyo maana siku ile aliyopelekwa Muhimbili alikuwa vile ingawa ni sehemu ya mazoezi", Mjomba alifafanua.


*KUNA YAPI YAMEFICHIKANA JUU YA AFYA YA JAMAL?
*GINA NA TABIA YAKE, KESHO ANAIJUA KWELI?
*PONGEZI KWA HERIETY KWA KUONESHA UBINADAMU NA HURUMA


ITAENDELEA!!!
 

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



______SEHEMU YA SABA______-


"Nilizoea ni tatizo lenye kuwakumba watu wanene tu ila nashangaa hata huyu, ila nasikia ukifanya mazoezi unaipunguza na kuwa ya kawaida"
"Ni kweli, ila kwa huyu ni hapana hatakiwi kufanya hivyo. Ndiyo maana siku ile aliyopelekwa Muhimbili alikuwa vile ingawa ni sehemu ya mazoezi", Mjomba alifafanua.



____________TIRIRIKA NAYO

Matabibu wawili, mmoja mwenye cheo ndani ya jeshi la ulinzi nchini. Mwingine akiwa nitumishi wa kawaida wa nchi pasipo kuwa na wadhifa mwingine wowote, walitosha kumfanya Heriety akose swali la kuuliza. Alirdhika nayo kutokana na taaluma ya watu hao wawili. Mjomba wa Jamal na pia Dokta Doreen, alisalia humo ndani kwa muda mfupi tu, akaaga na kuondoka ili aweze kurejea hosteli ambapo alihitaji haswa kuondoka na kurejea nyumbani.

Aliwaacha watatu tu ambao ni wenye kujua mengine zaidi. Muda wa kutoka kwake ndipo Mjomba akaeuza shingo kwa Jamal na kusema, "napendelea sana ufanye kile unachokitaka mjomba lakini inapofika muda ambao usalama wako ni wa muhimu. Basi walau ruhusu maamuzi yangu, walau unisikilize hata mimi".

Jamal aliposikia hayo alitabasamu kisha akasema, "Anko mimi nakusikiliza haswaa tatizo ni the way nataka mimi niishi. Wewe ni mkubwa kwangu, nitakusikiliza na pia sitoacha kukusikiliza. Nyumbani kule ninaishi na watu wa aina fulani, ila nikitoka na kuja shule huku ninakutana na wengine wa tofauti kabisa. Napenda nijue wengine wana experience gani kwenye maisha haya, thats all"

"Shehoza, huyu mpwa anko wako ana maisha ya maajabu sana. Maneno yake yamenvutia mno. Binadamu wa kipekee sana", Dokta Doreen alisema.

"Unajua Kapteni huyu mtoto muda mwingine najihisi hata nipo na mtu mzima mwezangu. Ni mwenye maneno na pia maamzi ya kipekee, ndiyo maana namchunga sana sitaki hata kumpoteza", Shehoza alisema kisha akamgeukia Jamal na kumwambia, "Jamal you are my everything anko, ndiyo maana nataka nihakikishe kuwa upo salama kila siku"

"Anko najua hilo ila napenda niwe na furaha, nadhani fuiraha yangu pia ni ya kwako. Staili yangu ndiyo inanifanya niwe na furaha, je hutaki kuona nikiwa hivyo?"

"Napenda mno, kwa hilo siwezi kukuzuia ila naomba uchunge haswa jicho langu lisije kuwa jekundu kwa ajili yako Jamal", Shehoza alisema.

"Hiyo hali ni haipepukiki anko, ila tusiende mbele sana. Najivunia sana uwepo wako".

_____________

SIKU KADHAA BAADAYE

__Uwanja wa Majani mapana, Tanga_

Ndege binafsi ya kukodi, ilidhihirika ikishuka kwa kasi kwenye njia ya kurukia za uwanja mdogo wa ndani. Hatimaye iligusa ardhi ya uwanja huo na kuanza kwenda mbio, mwishowe ilisimama eneo la maegesho. Haikuchukua muda mashine ilizimwa, halafu mlango ulifunguliwa. Alionekana kijana anayelekea utuzima akishuka, nyuma yake kukifuatiwa na kijana mdogo aliyependeza haswa akiwa amebeba mkoba mdogo mno huku machoni akiwa amevaa miwani ya giza.

Kitendo cha wao kukanyaga ardhi ya uwanja huo, walianza kujongea kuelekea eneo la kutokea nje. Ambapo kwa mbele yao alionekana kijana aliyevalia sare za wafanyakazi wa uwanjani hapo akisogea, huyu alimfikia mkadala kabisa mkubwa aliyeshuka mule ndegeni. Alimpa mkono huku akitabasamu, hatimaye wakasalimiana salamu ya vijana kuonesha hawakuwa wameuacha umri wa damujoto.

"Ismail ni adimu wewe kuonekana huku", Mwenye sare za uwanja huo alisema.

"Tony acha tu yaani kazi nyingi kupitiliza, yaani leo unavyoona nimeomba ruhusa mara moja nimlete mdogo wangu nyumbani kuna ishu ndogo ya kufanya", Mkubwa mwenyewe ambaye aliitwa Ismail, ndiyo alizungumza.

Hakukawia sana kubadilishana maneno na mtu hyo aliyeonesha wazi kujuana naye kabla, aliondoka na kutoka hadi nje ya uwanja huo. Hapo alikuta gari binafsi ikiwa inamsubiri, kutokeza kwao kwa nje. Alionekana Mzee wa makamo ambaye aliwasalimia kwa pamoja, kisha akawaongoza hadi ndani yake.

"Karibuni sana Tanga, mwongozo unaanza wapi Ismail?, Mzee aliwakaribisha kisha akauliza.

"Kwanza tupeleke kwa kliniki ya Mgiriki, halafu tukitoka hapo ni moja kwa moja nyumbani. Nina muda mrefu sijatia mguu huko", Ismail alieleza.

Safari ya kutoka mahali hapo ilichukua nafasi yake, waliondoka moja kwa moja hadi wakafika katikati ya jiji la Tanga. Walichukua uelekeo wa raskazone, huko walifika mahali husika. Baada ya kuvuka hospitali ya Bombo walisimama mahali ambapo kuna jengo la ghorofa moja, hapo Ismail na yule mdogo walishuka na kuingia ndani. Mzee alibaki kuwasubiri mahali hapo.

____________

Majira ambayo Ismail yupo jijini Tanga, upande wa Dar es salaam eneo lenye mabwawa ya kuogelea kadhaa. Kukiwa na vibanda kadhaa vya makuti huku ambavyo vilitamalaki idadi ya watu wakiwa na vinywaji wakifurahi. Ilidhihirisha ni eneo ambalo wengi hupenda kuja kufurahia, kwa jinsi walivyokuwa wakinywa na kuburudika huku wengine wakipiga mbizi kwenye maji yaliyopo hapo.

Upande wa ukingo wa sehemu moja ya kuogelea, mvulana na msichana ambao walikaa kimahaba huku miili yao ikichuruzika maji. Walidhihirika wakiongea kwa sauti ya chini tena kwa furaha, huku wakiegemeana kimzaha na kucheka.

Kila maneno yaliyokuwa yakitoka kinywani kwa mmojawapo ingawa hayakusikika, yalimfanya mwingine aachie tabasamu. Walifikia hatua ya kupigana mabusu mashavuni mwao, hii ikiendelea na ni wachache waliyowatzama ila asilimia kubwa ya wengi walikuwa wakiendelea na mambo yao.

Haikuwa jambo la jabu kuona wandani wapo namna hiyo, ila upendezwaji wao kuwa namna ile ulifanya wachache watamani kuwa mmojawapo pale. Iwe wa kiume alitamani walau kuwa na banati kama yule, wa kike naye hamu ya kukaa na kijana yule iliwajaa. Wachache waliyovutwa na mahaba hayo kutokana na utamani wa macho, ndiyo waliweka mawazo hayo.

Miongoni mwao hao, binti mmoja mwenye umbo matata akiwa amekaa na wadogo zake wawili. Naye alishikwa na hisi hizohizo, haswaa akitazama umbile maridadi la kijana yule aliyevaa kaptura fupi. Mwili wenye rangi mchanganyiko, pamoja na nywele ziso asili barani Afrika, huyu alijikuta akikaa kabisa kwenye ukingo ambao yupo mkabala na wandani wale wenye kujua kujiachia vilivyo. Mbele yake kukiwa na mabinti wadogo wakiwa wanaogelea, ambao hawakuwa na muda wa kumtazama jinsi alivyohamisha macho mahali kule ambapo kuna wa umri wake wakiendelea kufurahia.

Hata alipoitwa na wasichana wale waliyopo mbele wala hakuwa akisikia, alipokuja kuguswa ndipo akagutuka na kutambua ni mwenye kuhitajika na wasichana wale. Kitendo cha kutolewa ndani ya mawazo, kilipelekea aingiwe na mshtuko na kuwafanya wale wadogo watazame kule alipokuwa akiangalia. Walipokiona hiko, walijikuta wakicheka na kisha wakamtolea macho yeye, watoto hawa ingawa bado ni wadogo wa kustahiki kukaa na wazazi wao. Walishaanza kujua jema na baya, asali na tango na hata nyumba na chumba.

Hiyo haikuwa swala gumu kwao kuweza kumaizi binti yule alitekwa mno na wale waliyopo mbele yao, waliishia kucheka tu kwa jinsi alivyo. Hata mkubwa wao huyo aliingiwa na soni, kuona amebainiwa kuwa alipumbazwa na vipendezesha macho. Wasichana wale hata kile ambacho walitaka kumwambia, walighairi papo hapo. Wakajikuta wakirejea kuogelea, kitendo hicho kilimfanya banati yule awaone ni jipu karaha kwa kumvuruga mawazo yake.

"Mlikuwa mnaniitia nini?", Aliwauliza ila alipokea kicheko huku akiwashuhudia wakiendelea kuogelea kama kawaida.

Aliamua kuwapuuzia na kisha akarejesha macho kule walipo wandani, loh! Hakuwaona tena wakiwa namna ile, safari hii aliwashuhudia wakiwa wapo ndani ya maji kwenye ukingo wa mbali kutoka alipo. Hii ilimfanya alaani haswa, alikosa burudani ya kutosha kuweza kuwashuhudia wapenzi wale. Kuwaona wakiogelea kwake haikuwa kivutio tena, alihitaji haswa kuendelea kuufaidi ule ukaribu wao wa mwanzo lakini ndiyo hivyo mambo yalibadilika.

"Hawa watoto shenzi kabisa", Alijisemea kwa sauti ya chini akiwalaani wale waliyomshtua kutoka kwenye burudani ya kipekee.

Binti huyu mwenye kustahiki kuitwa mrembo, alijikuta akisimama juu na kudhihirisha umbile lake matata lenye unene ule uliyojijenga kiupekee. Kudhihirisha uundi wa Muweza kuweza kusani umbo hilo, vazi la kuogelea ndiyo kabisa likaendelea kuweka kila kitu wazi. Kiasi kwamba laiti kama angelikuwepo fukwe zile ambazo zimejaa waswahili kupitiliza, basi angelikuwa chakula cha jumuiya kwa kilazima kwa jinsi watu walivyochafukwa na akili wakiona miili ya namna hiyo.

Kukaa kwake wima, hakuchukua muda, alijitumbukiza ndani ya maji kwa mtindo maarufu kama 'kupiga mchomo'. Alianza kuyakata maji kwa ufundi kuelekea kule ambapo wadogo wale waliyomshtua wapo, wao walipomwona walibadili uelekeo huku wakiendelea kucheka. Kitendo hiko hakukifurahia ila aliamua kuacha tu lipite, maana hapo hakukuwa mahali stahiki kuzozana nao.

__________________

"Ismail huyu mdogo wako hali yake ni serius kabisa. Unatakiwa kuwa makini naye, kama ulivyoelezwa hapo awali kwa situation yake hakuna tiba tena. Bali kumchunga ndiyo kitu pekee kinachoweza kumfanya akaishi muda mrefu", Daktari mwenye asili ya kizungu alisema huku akiwatazama watu wawili wenye asili ya kiafrika.

"Kwahiyo Dokta hakuna njia nyingine zaidi, maana hili swala wewe ndiyo mtalamu pekee uliyobaki hapa nchini", Ismail alisema huku akimtazama kijana aliyepo pembeni yake kimasikitiko mno.

"Nafikiri umeweza kujua kwamba anasumbuliwa na mengi mno, hayo mengine hayatibiki na ndiyo yanapelekea tatizo hilo. Nitamwandikia dawa tu awe anazitumia kila siku ya maisha yake mara moja tu asubuhi, naamini hizi ndiyo zitaweza kumsaidia. Kuwa naye makini sana",

"Sawa Dokta hakuna shaka juu ya hilo", Ismail alijibu.

"Kimweri hakuna kiumbe awezaye kuishi bila changamoto katika maisha haya, unavyoona hapa kila mmoja anazo ila tu tunajitahidi kuzificha. Hali yako pia ione ni sehemu ya changamoto, huwezi jua Mungu amekupa nini mbeleni kuwa na jambo kama hilo. Kuwa imara na mchangamfu kama ulivyo hivi sasa, niliwahi kusikia uwepo wa kijana wa aina hii huko Muhimbili. Hajapona ila hadi sasa hivi yupo na anaendelea na kazi zake mjini, na ana familia" Dokta alieleza.

"Natambua hilo Dokta, hadi hivi sasa. Hili si kitu kwangu, ilimradi bado ninaendelea kupumua kama kawaida". Kimweri alijibu.

"Ninachoweza kukushauri hivi sasa ni uwe makini na masomo yako, mapenzi ya ujana ni hatari sana kwako. Kaa nayo mbali kabisa, uje kuchukua mwenza wa ukweli wa maisha yako"

"Sijawahi kufikiri kuhusu mapenzi na sitokuja kufikiria juu ya suala hilo, muda huu ambao ninahitaji nijijenge kimaisha"

"Vyema sana kijana, Ismail naamini wewe unaweza kumtunza na kumwepusha. Hii ni mboni yako ilinde isiingie pabaya. Niwatakie maisha mema"

"Tunashukuru Dokta", Walitoa shukrani wote kwa pamoja, haikuchukua mdua waliamua kuagana.

Ismail pamoja na mdogo wake kama alivyomtambulisha waliondoka mahali hapo, wakimwacha Dakari akiendelea na shughuli zingine. Wageni hawa walifika kumwona mbobezi huyu aliyelowea nchini Tanzania kwa muda mrefu, huo ukawa ni mwanzo wa mengine kwenye maisha yao wote watatu waliyokuwa hapo.

____________


_Siku mbili baadaye___
Mabadiliko ya hali ya hewa ya ghafla ambayo wala hayakutarajiwa na wakazi wa jijini Dar es salaam. Yalipekea kuanza kuongezeka kwa mji kwenye mito inayokatiza jijini, haikueleweka suala hilo lilitokana na nini katika kipindi ambacho hakikutegemewa kunyesha mvua kubwa. Wingu zito lilitanda majira hayo ya saa nne asubuhi, kufanya hali ilbadilike na kuonekana ni jioni kumbe ndiyo kwanza mwanzoni mwa siku mpya. Yakiendelea hayo maeneo ya barabara ya Morogoro ipitayo jirani na viwanja vya jangwani, watu waliichukulia hali hiyo ni ya kawaida.

Kuanza kuongezeka kwa maji kwenye mto Msimbazi, wao walipaona ni jambo la ada. Muda huo yakiendelea kujaa, walikuja kugutuka wakati ambao yameanza kufika kwenye kingo za mwisho za madaraja ya hapo. Kipindi ambacho kuna foleni kubwa iliyopo makutano ya 'Fire', ambayo yalitokana na kusimama Askari wa barabarani badala ya taa za kuongozea magari.

Muda huo wachache waliyokuwa na wasiwasi mkubwa walishaanza kupiga honi kwa nguvu mno kusihi huko mbele magari yaruhusiwe, Askari wa barabarani aliyejawa na kiburi wala hakuonekana kujali hilo. Aliendelea kuyaacha magari yakiwa namna hiyo, aliporuhusu pia hayakwenda yote isipokuwa ni machache tu na asilimia kubwa yakabaki. Wakiendelea kuhimmiza hivyo maji yalizidi kuingia darajani, awali yalipita kama mfejeji uliyoziba juu ya barabara. Lakini yalipozidi wingi ndipo walipozidi kiwango, magari yaliyopo karibu na madaraja yalianza kuyumbishwa. Yalipelekwa kushoto na kunapoelekea maji, gari dogo aina 'toyota saloon' iliyopo darajani ndiyo ilikumbwa na masaibu mazito.

Ilivutwa hadi ikafika kwenye kingo za machuma mafupi mno, muda huo hakuna ambaye alithubutu kusoge jirani na maji yenye nguvu. Waliishia kuona tu mikono ya mtu ikiwa inagonga kioo cha gari, kwa kushindwa kufungua upande huo mwingine kutokana na nguvu ya maji ilivyo. Gari ilipofika ukingoni mwa vyuma na kuzuiwa, bado hakuna ambaye aliyejaribu kusogea. Wingi wa maji ulipozidi kwa mara nyingine, walishuhudia ikianza kuinuliwa magurumu ya upande wa kulia taratibu. Likitokea hilo, raia walimshuhudia kijana mmoja akijitumbukiza kwenye maji kwa ghafla. Hapo ndipo wanadamu walibaki mdomo wazi, wakiwa wanaliwaza jambo lile haikupita muda kijana yule alirejea kwenye ukingo wa mkondo huo mkubwa wa maji ambapo umati wa watu upo.

"Nisaidieni chuma jamani haraka sana, kabla gari haijapinduliwa mtoni. Atakufa yule", Alihimiza.

"Wee kijana usijifanye unajua sana kuokoa watu utakufa", Mzee mmoja alipaza sauti na kupuuzia alichosema.

"We Mzee kwani utaishi milele ndani ya dunia hii, kila mtu kaandikiwa kifo chake na wewe huwezi jua utakuja namna gani. Labda hapo uliposimama ardhi itaporomoka na kuingia ndani, unategemea nani atakuwa msaada wako kama huhitaji kusaidia wengine", Kijana huyo alimpazia sauti huyo mzee, alipoona watu wamekaa kimya na hakuna anayetoa msaada aliamua kuokota kipande kigumu cha jiwe na kurejea tena majini.

*ISMAIL NA KIMWERI WADHIHIRIKA NDANI YA RIWAYA, WANA YAPI?

*BINTI AZAMA KWENYE PENZI LA KUTAZAMA, NINI KITAKACHOFUATA?

*KIJANA ANAJITOLEA AJITOLEA KUMSAIDIA ASIYEMJUA, NI NANI HUYU?


ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA




___________SEHEMU YA NANE__________


"We Mzee kwani utaishi milele ndani ya dunia hii, kila mtu kaandikiwa kifo chake na wewe huwezi jua utakuja namna gani. Labda hapo uliposimama ardhi itaporomoka na kuingia ndani, unategemea nani atakuwa msaada wako kama huhitaji kusaidia wengine", Kijana huyo alimpazia sauti huyo mzee, alipoona watu wamekaa kimya na hakuna anayetoa msaada aliamua kuokota kipande kigumu cha jiwe na kurejea tena majini.



________TIRIRIKA NAYO

Wengi walistajaabu sana ujasiri wa kijana yule hata kufikia hatua ya kucheza 'sebene' na maji yale yenye nguvu. Ujasiri wa wengine katu hawakuthubutu kufanya vile ilihali wanajua nguvu ya maji, alipoingia kwenye mvutano ule . Ukimya ulifuata, kila mmoja akisema lake moyoni juu ya kijana jasiri namna ile. Hata wale kinamama ambao hapo awali walimwona ni mwenye kujitafutia balaa, waliweka mikono yao ishara ya kuomba aweze kurejea salama salimini.

Macho yao wakiwa wameyaelekeza pale alipo kijana yule akicheza pata potea na kimiminika chenye nguvu kubwa mno hata ya kuweza kuondoa uhai wa mtu. Kwa uwezo wa Muweza hatimaye alifanikiwa kumtoa Mwanamke aliyekuwa ndani ya gari ile kwa tabu mno. Hadi akafika naye sehemu yenye maji yasiyo na nguvu, ndipo watu waliyokuwa mwanzo wakimwona anajitafutia matatizo waliposogea karibu na kujaribu kumsaidia mkubeba mwanamke yule.

Ujaji wako mahali hapo ulimfanya kijana hata abaki anawashangaa, utayari wao wa kutaka kumnyanyua mwanamama yule. Ulimpelekea awakwepe na kuwatazama kwa macho makali, jambo hilo liliwafanya wale watu wapenda kujitafutia sifa kwa tukio rahisi. Wabaki wakimlaumu mno kwa kutotaka kusaidiwa, kwake aliwaona wanafiki kwani hata ushirikiano wa kuweza kumletea chuma tu cha kuvunja kioo aweze kumnusuru hawakuwa nao. Ndiyo waje kuonesha kujali kumsaidia, wakati ambao ameshakamilisha kazi yake.

"Hata aibu hamna wanaume watu wazima kabisa, uje unisaidie nini hivi sasa wakati hapo mwanzo mligoma", Ndiyo maneno aliyowapa kwa lawama zao.

"Halafu wewe dogo sana ujue hebu kuwa na adabu", Mmojawapo miongoni mwa kundi la walalamikaji, aliongea na huyo ndiye aliyeonesha kuwa ni mwongeaji mwingi.

Kufikia hapo kauli yake hiyo, hata raia wengine walianza kumlaumu yeye. Haswa kwa kuwa mstari wa mbele zaidi kulalamika ilihali hakutoa msaada. Wakiendelea kutupiana maneno, yule kijana kwa haraka zaidi alitoka mahala hapo akiwa amembeba mwanamke ambaye alionesha wazi kumzidi uzito. Alienda naye hadi upande wa barabara ya Morogoro unaoelekea Magomeni, akiwa anakaribia kufika huko. Gari ya kisasa aina ya Landcruiser ilisogea jirani zaidi. Ilpofika usawa wake ilisita kuendelea na mwendo, hapo mlango wa dereva ukafunguliwa na akashuka mtu mwenye nguo nyeupe pamoja na kofia mithili ya Askari.
Mtu yule aliyeshuka garini alimpokea hima huku akisema,"dogo ni majanga haya sasa unayaleta".
"Jamaa hatuna muda wa kujadili hili, tuwahi haraka sana hospitali tumpeleke huyu mama. Mimi pia niwahi hukohuko", Alisema.

"Hii ni hatari kwako lazima niseme ujue, Bosi akijua huoni kama nitakuwa hatarini mimi"

"(Akihema kwa nguvu na kuyumba akionekana kukosa muhimili) Tunaenda au hatuendi, halafu jamaa hayo maguo yako kama mkata nyama ukiongozana na mimi usiyavae. Unanifanya nionekane mtoto wa kigogo kumbe nina tabu tupu"

"Poa ingia garini haraka sana, tuwahi"

Hawakuweka wakati sana, kwa pamoja waliingia garini na kuondoka mahala hapo. Wakiaacha raia wa eneo hilo wakiwa na fikra nyingine kabisa juu ya kijana yule, walijiuliza sana juu ya hadhi ni nani. Hadi aje kuchukuliwa na gari la kifahari kama lile, ilihali mavazi yake hayakuonesha ni mwenye chembe za ukwasi. Hawakupata jibu ya hilo, kwani alikuwa ni mgeni kwao. Vilevile, mwenye kustahiki kutoa ufafanuzi ni yeye pekee. Ndiyo maana wakabaki bila ya kuwa na lolote juu yake.
________________

Tangu alipomwona yule kijana mwenye mwandani wake majini, bado mawazo lukuki yalikuwa juu yake. Majira hayo ni tayari ameshaondoka yule mwenye kumpeleka mbali kimawazo, akabaki pekee akiyatazama mazingira yale ambayo waliketi wawili wale. Wadogo ambao hapo awali walikuwa wakichangamkia kuogelea, majira hayo wala hawakuwa na hamu tena ya kufanya hivyo. Hata yeye mwenyewe ilimbidi tu asiwe namna hiyo kutokana na mvua ya ghafla iliyoanza kunyemelea mahala hapo.

Aliamua kuinuka na kusogea eneo la kujikinga akiwa yupo na wadogo zake wale. Mvua hii ndiyo ile ambayo ilileta dhoruba maeneo ya jangwani na kupelekea kujaa kwa mto. Haikuwahi kutokea kubadilika kwa majira kwa ghafla namna hiyo. Ilipozidi kuwa kubwa ndipo banati hawa walishindwa kabisa kuendelea kusalia mahala hapo. Kila mmoja aliongoza eneo ambalo hutumiwa kubadilisha nguo kwa ajili ya kureja nyumbani. Hamu ya kuendelea kustarehe tayari ilishatibuliwa na hali ya hewa.

Muda mchache baadaye wote kwa pamoja walikuwa wapo ndani ya gari waliyofikia, ukimya ukiwa umetawala kati yao huku kila mmoja akiwa amepitisha hali ya kunyamaza akiwaza lake. Binti huyu kila fikra yake ilikuwa ipo kwa kijana yule, mtanashati wa mavazi na hadi kuvutia kinamna nyingine kabisa. Safari iliendelea huku akiwa yu mkimya mwingi, na hata wadogo zake walipoanza kuongea yeye wala hakuwa karibu nao. Hadi pale alipokuja kutingishwa ndipo alipomaizi ya kuwa ni mwenye kusemeshwa, na wala hakusikia kile alichoambiwa hata alipozinduliwa huko.
"Dada unawaza nini mbona hivyo?', Aliulizwa.

"Mh! Hamna", Alisema ingawa alidhirisha wazi ni mwenye kuficha kitu.

"Hamna nini wakati tunakusemesha mara ya nne wala husikii chochote hadi Spora kakuzindua"

"Eliza try to understand, siwazi chochote", Alisema akionesha hataki tena kubughudhiwa na maswali yao.

"Tantalalaaaaa!", Eliza aliropoka na kupelekea mwenzake acheke huku wakimtazama Dada yao.

"Lalalaaa Tantalalaaa!", Mwenzake naye aliropoka vilevile.

"Eliza na Spora msinitafute mjue"

Siku zote ukiwa na kitu ambacho wengine hutaki wakifahamu, basi ukiwekwa ishara yeyote ile lazima uhisi unasemwa wewe. Ndiyo iliyotokea kwa binti huyu, baada ya wadogo zake kuanza kuwasiliana kwa namna wanayojuana wao wenyewe. Hadi kupelekelea achukie, kutokana na kujishuku tu.

_____________

"Jamal mambo gani hayo Anko, huoni kama ungeishia kulazwa leo. Yaani na afya yako hiyo unaenda kumbeba mtu mzima kama huyo", Shehoza alilalamika huku mbele yake akimtazama Jamal aliyelala kwenye kitanda huku mkono mmoja ukiwa na dripu.

"Anko wasiwasi wa nini, nipo hai na sina tatizo. Ila sikuwa na la kufanya mbele ya watu wale waoga wasiyojua hata kumsadia aliyekuwa akielekea kufa", Jamal alijitetea.

"Hata kama Jamal, ukumbuke wewe ndiyo kila kitu kwangu. Bora hata ungemwita dereva aje kukusadia kumbeba kuliko kufanya vile. Hutakiwi kubeba uzito mkubwa wewe ni kwa usalama wako"

"Najua sana ila mwenye afadhali ni bora amsaidie asiye na fadhali itakuwa ni jambo jema zaidi. Anko uhai si kitu maana hata wa kesho yetu hatuijui, kutenda wema ndiyo kitu. Mimi nimefanya sehemu ya kutenda wema na wala sitohitaji nilipwe kwa nilichokifanya, ilimradi tu binadamau mwenzangu kawa salama na mimi nipo vizuri vilevile"

"Ok, mshindi ni wewe. Sasa sikia, yule mama tayari kesharejewa na fahamu na anakuhitaji akuone wewe uliyemsaidia hadi akaondokwa kwenye dhoruba ile ya ajabu. Dripu ikiisha kama una nguvu nitakueskoti hadi wodini kwake, ukaonane naye"

"Unaweza kunibebea dripu yangu yangu hii twende hukohuko nikamwone sasa hivi, niwie radhi wewe ni mkubwa wangu kwa kukupa dhima hii"

"Maliza kwanza hiyo dripu ndiyo mengine yafuate Jamal"

"Nikifa je?"

"Unajua wazi hayo maneno yako siyapendi ya kuzungumzwa kifo tu, unanitia simanzi Anko"

"(Akitabasamu) Nikifa moyo namaanisha maana hospitali hii ina manesi hao nikiwaona tu moyo unapiga hadi ukaribie kuchomoka, nikifa kwa ajili yao je nisitoke humu ndani tu kisa moyo upo kwao"

Shehoza alicheka wka nguvu aliposikia maneno hayo, kutokana na iinsi alivyozoeana naye. Matamshi hayo ilikuwa ni sehemu ya kawaida kutokana na wote kuwa itikadi ambazo zinaendana kwa kiasi chake. Ilimbidi aibebe ile dripu na kumpeleka kule ambapo alikuwa akihitaji kufika, waliongozana kwa pamoja huku njiani ikiwa ni vicheko tu kwa kila muuguzi watakayepishana naye.

Hata Jamal asipoamua kuweka kituko wao tu waliishia kucheka, maana kila mmoja alimjua vilivyo kutokana na kufika hospitalini hapo mara kwa mara. Ucheshi wake haukuwa jambo geni na alibakia kuwa kipenzi cha watu kwa jinsi alivyojiweka namna ya kipekee kwao.

Waliweza kuvuka vyumba kadhaa na hatimaye wakafika kwenye wodi moja ya kisasa ambayo hulazwa mtu mmoja tu, Jamal alipoiona hiyo hakushangazwa kabisa. Alishabaini yule mama ni mwenye kujiweza hadi akafikia kulazwa huko, aliongozwa kuingia ndani ambapo alikutana na mwanamke wa makamo. Jamal aliweza kumwona kwa mara nyingine akiwa ni mwenye kufumbua macho na si kufumba kama alivyomtoa ndani ya gari.
"Haya Bi Agatha nimekuletea shujaa wako huyu hapa, alikuwa akimalizia huduma ya kwanza na yeye" Shehoza alisema na kupelekea BI Agatha atabasamu.

"Oooh! Pole kumbe na wewe ni alikumbwa na balaa", Bi Agatha alisema alisema huku akimtazama Jamal.

"Usijali sana Mama, nipo safi kabisa, nikupe pole wewe kwa yaliyokufika. Wajionaje na hali?"

"Namshukuru Mungu mwanangu, kama asingekuleta wewe mahali pale ningekuwa mfu hivi sasa maana nisingetoka ndani ya gari mule"

"Usijali, ubnadamu ni kusaidiana na nisingekupa msaada wewe nisingekwa nimefanya haki kabisa"

"Haya Jamal nakutundikia dripu yako hapo pembeni", Shehoza alisema.

"Tundika tu mimi nishafika huku sirudi kule ng'oo"

"(akitabasamu) Haya mshindi wewe, Mama ngoja nikwachie mtu wako huyu. Ila mbavu zako hakikisha utafute spea kabisa, maana huyu mtu atazivunja"

"Akatafutie spea wapi wakati yupo ndani ya gereji ya binadamu hii, wote tunafanyiwa matengenezo" Jamal aliropoka na kumfanya Shehoza acheke kwa nguvu mno, hadi Bi Agatha naye hakusalia bila ya kucheka.

______________


_MAJUMA MAWILI BAADAYE___

Siku hii majira ya jioni, Jamal na Shehoza wapo ndani ya sebule ya kisasa yenye kuakisi ukwasi wa mmiliki wake. Wote wawili walivaa mavazi ya kupendeza huku wakiwa ni wenye kusubiria jambo kwa haraka, ukimya ulitawala na kila mmoja macho yakawa yapo kwenye kioo cha televisheni bapa iliyopo sebuleni hapo. Mchuano wa mpira wa miguu ulionekana ambao uliwafanya wasijaribu hata kufungua vinywa vyao, Wakiendelea kuangalia runinga, haikupita muda mrefu aliingia dereva yule ambaye aliongozana na Jamal kule Jangwani kumwokoa Bi Agatha.
"Ulikuwa unatuweka jamaa yangu, yaani tumekaa tunakusubiri wewe hapa", Shehoza alisema.

"Nisameheni jamani, nilipitia kujaza upepo tairi lilinizungua nikabadili njiani", Dreva alijitetea.

"Hakuna noma, Jamal twondoke zetu"

Wote kwa pamoja walitoka ndani ya sebule hiyo, waliiacha runinga ikiendelea kuwaka vilevile. Waliongozana hadi walipofika kwenye maegesho ya nyumbani ambapo kulikuwa na gari aina Range rover sport ikiwa imewekwa tayari kwa safari. Pasipo kukawia waliingia na mwongoza usukani akafanya kazi yake.
Iliwachukua dakika takribani ishirni kuweza kufika kwenye nyumba moja ya kifahari ambayo mbele ilikuwa na lango la rangi nyeusi. Geti hilo lilifunguliwa na waliingia ndani hadi wakfikia eneo la maegeshoni ambapo walikutana na warembo wawili waliyopishana umri. Kuwasili hapo walilakiwa kwa pamoja huku Jamal akionekana ni mwenye kushangaa zaidi, hadi Shehoza akawa hamwelewi mpwa wake.
"Jamal vipi?" Shehoza aliuliza.

"Anko kumbe Da Doreen akivua gwanda lake anapendeza hivi, siku ile alikuwa akinitisha tu buti lake lile" Jamal aliropoka.

"Doreen unamsikia huyu", Shehoza alisema huku akimtazama Binti mkubwa miongoni mwa wale wawili.

"Yaani huyo akili zake zinamtosha mwenyewe, achana naye"

"Kweli zinanitosha mimi maana nikikupa wewe zitakubana kabisa", Jamal akadakia na kuwafanya wote wacheke.

"Jamani karibu kwangu, Jamal, Shehoza kutana na Alice ni mdogo wangu huyu anasoma form five Benjamin", Wageni walipena mikono na binti huyu na kisha kwa pamoja wakaingia ndani ya nyumba.

Huu ulikuwa ni mwaliko wa chakula cha jioni, tangu pale walipojuana kwa mara ya kwanza baada ya kukutana hospitalini. Siku ambayo inasadikika iliandika kitu kingine kwenye historia ya kimaisha ya watu hao, hakuna aliyekuwa akijua kama mkutaniko huo ungeweza kuzua sababu nyingine kabisa. Wote ni wanadamu na hakuna ajuae ya mbeleni, laiti kama wangelijua hilo wangeliweza kubadili kutaniko hilo.

Hatimaye waliketi sebuleni na kuanza kuongea kwa pamoja, huku Jamal akiwa ametawala sehemu kubwa ya mazungunmzo hayo. Kila muda wote waliishia kucheka kwa jinsi alivyo na vituko, hata Alice akajikuta akiketi jirani naye kabisa huku akifurahi zaidi.
Siku zote binti hupenda haswa kuwa karibu na yule ambaye atamfanya ni mwenye furaha sana. Usogeaji wake hakuna aliyeutilia maanani zaidi ya kuona ni sehemu ya furaha tu, binti huyu alitamani hata Jamal asisite kuendelea na kuchekesha watu hapo.

Haikuchukua muda mrefu kwa pamoja walisogea eneo lenye chakula, walituliza matumbo yao kwa pamoja na walipotoka tu hapo walijigawa. Shehoza aliondoka sebuleni hapo, huku akimwacha mpwa wake yupo na Alice. Kubaki wawili, ikawa ni mwanzo wa mengine.

*JAMAL NA ALICE, MNA NINI?

*SHEHOZA NA DOREEN, KWANINI WAWAACHE WENYEWE?

*MUNGU AMJAALIZE MOYO WA KUJITOLEA ZAIDI JAMAL



ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_____SEHEMU YA TISA________


Haikuchukua muda mrefu kwa pamoja walisogea eneo lenye chakula, walituliza matumbo yao kwa pamoja na walipotoka tu hapo walijigawa. Shehoza aliondoka sebuleni hapo, huku akimwacha mpwa wake yupo na Alice. Kubaki wawili, ikawa ni mwanzo wa mengine.



_________TIRIRIKA NAYO

Historia mpya iliandikika kwa wote kuwa karibu muda huo, Jamal uongeaji wake hakujua ni mwanzo wa kujengeka kitu kingine ambacho hakuhitaji kuona kinatokea. Falsafa kubwa iliyotawala maisha yake ambayo ni kufurahisha wengine ili awe kipenzi cha kila mmoja duniani, ndiyo iliyokuja kufanya avute kile ambacho hakuhitaji kisogee.

Hakuwaza jingine mbele ya binti huyo ambaye ni mara ya kwanza kuonana naye, yeye alichoangalia na kumfurahisha tu na kuongea naye mambo mbalimbali akitumia masihara asilimia kubwa ya mazungumzo yake. Hata alipoanza kusifiwa juu ya ucheshi wake kwake aliona ni jambo la kawaida, alishasifiwa sana juu ya hilo na hiyo kwake haikuwa geni sana. Loh! Laiti angelijua hizo sifa asingezikubali hata kimoyoni, ila ndiyo hivyo hakuwa na mwenye kujua ya mbeleni.

Mara chache sana alimpatia nafasi Alice aweze kutawala mazungumzo, ila yeye alibakia kuchukua wasaa mkubwa ya maongezi hayo. Kukaa namna hiyo haikupita hata muda mrefu, walibadilishana namba za simu kila mmoja.
"Jamal wewe ni mcheshi sana", Alice alisema baada ya kunogewa na mazungmzo.

"Kawaida nipo, mbona wewe mchekaji sana", Jamal anaye akasema.

"Sasa jamani unataka ninune, nikifanya hivyo nitakuwa na matatizo si bure kabisa"

"Wapo wanaonuna kila nikichekesha sijui hao utawaweka kundi gani?"

"Hawana bandama labda, si kwa vituko vyako aisee. Na imani huyo wifi hajuti kuwa karibu na wewe"

"Kwanza atoke wapi? Maisha yenyewe mafupi nije kukonda siku si zangu"

"Kijana mzuri na mcheshi kama wewe utakosaje?'

"Wengine tuna damu za mbu, tukimsogelea mtu atatamani kutupiga kibao"

"Usiseme hivyo Jamal"

"Lazima niseme Alice nikichungulia mboga tu muda huu asubuhi haifiki mchana inachacha, ndiyo sembuse nijitokeze mbele za watu"

"(Akicheka) Sasa unapata dhambi huko unapoelekea, you are so handsome Jamal", Alice alipoongea maneno hayo alipunguza ukubwa macho yakawa ni usawa wa nusu mwezi, huku akipeleka jicho kwa mvulana aliyetokea kumfanya asahau kama kuna kununa dunia hii.

Haiba yake aliyotunukiwa ilionekana usoni mwake, jinsi alivyoweka mlango huo wa fahamu ulitosha hata kumfanya mwanaume mkware atoe kitita chochote cha pesa hata kama hakuombwa. Ni sawa na silaha ya moto kuelekezewa mtu, hata bila kuamriwa aweke mikono ataweka tu mwenyewe.

Mdogo huyu wa Afisa wa kijeshi, alibarikiwa kwa vingi ingawa hakuweza kupewa vyote kama ilivyo wanadamu wengine. Usoni alipatiwa wembamba, wenye macho makubwa ya wastani, pua iliyochongoka na midomo midogo mithili ya mtoto tena yenye rangi yake halisia kabla hajapaka chochote. Mwili ulikuwa ni mwembamba ila ule uliyojitenga vyemba, akiwa na miguu ya unene wa wastani kuendana na jinsi alivyo. Hakika alitosha kuitwa mrembo, bila hata kujiita mwenyewe. Usiku huo aliyovaa gauni fupi lililomkaa mwilini hadi kufanya mapaja yaonekane dhahiri akiketi, kuliweza kumshawishi mwanaume yeyote rijali.

Jamal naye moyoni alikiri amekaa na mnyange haswa, ingawa mtima wake haukuwa umempa nafasi ya kumfikiria zaidi ya kumwona ni banati kama walivyo wengine tu. Hata kushushiwa huko nusu mwezi, kwake aliona ni jambo la kawaida kwani alishawhi kufanyiwa hivyo mara nyingi mno. Uada wa kutazamwa namna hiyo haukuchukua hata muda mrefu ulianza kumtoka akilini, akajikuta akiishiwa maneno na kubaki akimwangalia tu. Kijana huyu hakujua hali hiyo ilianza kumkumba lini hadi afikie kuwa namna hiyo, ni ghafla mno kumkuta hakujielewa kabisa.
"Jamal", Alice aliita kwa sauti ya puani zaidi huku akijisogeza karibu zaidi.

Loh! Masikini kijana wa watu wala hakuwa na habari kama kaitwa kwa jinsi alivyopumbaa. Jambo hilo lilimshangaza Alice naye, hakujua kama Jamal muda huo mapigo ya moyo yalianza kumwenda mbio akiwa kama amegandishwa asijue lolote la kufanya. Binti huyu alikuja kumzindua kijana huyo kwa kumpiga kibao cha uchokozi ambacho kilimfanya ashtuke mno.
"What's wrong Jamal?", Aliuliza.

"Nothing", Alijibiwa

"Nothing what? Wakati nimekaa nakuona umeduwaa ghafla mno hadi uchangamfu umepotea ghafla hivyo, are you Ok?"

"Anyway forget about that", Jamal aliposema hivyo aliinuka haraka kochini hapo na kuelekea ulipo mlango mkubwa wa kutoka ndani hapo.

"Jamal, unaenda wapi?"

"Nahitaji kubadilisha hali ya hewa"

Jamal alitoka nje na kumfanya binti huyu ajihisi huenda kuna mahali amemkwaza, ana kasoro fulani ambayo haikumpendeza. Jambo hilo lilimfanya ajitazame mwilini mwake ila hakuona lolote lile. Alikummbuka maneno aliyokuwa akiyaongea, napo hakudhani kama kuna lenye kukwaza danga yule.

Hakutaka tena kusalia kochini, aliinuka juu na kupelekea gauni lake fupi kuwa juu kuliko kawaida. Jambo hilo lilimfanya alivute chini mara moja, lilikaa usawa wa juu kidogo ya magoti hapo ndipo akaona lipo kawaida. Alice aliongoza njia moja kwa moja kwenda nje kumfuata Jamal.

______________

"Big bro kwani nani huyo gashi ambaye haishi kukupigia simu muda huu?", Kijana mmoja mwenye asili ya ushombe alimuuliza mwenzake wakiwa wapo chumbani kwenye vitanda viwili tofauti vilivyo sambamba.

"Dogo ni gashi mmoja hivi wa skonga, yaani huyo tumevaana huko juu kwa juu nikiwa na Radhia ndiyo imekuwa kunipigia hadi majira haya", Kijana mwigine mwenye asili ya mchanganyiko kama ilivyo mwenzake alijibu.

"Sasa wewe nakujua ukiwa na yule manzi utakuwa umemlia mbuyu ndiyo maana kaamua kukutafuta"

"Fred unategemea nifanyeje mdogo wangu, unajua kabisa Radhia ni wivu na mkorofi. Ni kuvunga tu aisee"

"Ila mcheki huenda ana ishu huyo"

"Aaah! Wapi unadhani ana la maana basi huyu gashi, yaani nimeshapokea simu mara kibao yeye ni haoneshi kama ana la maana. Mpotezee tu"

"Mtu wangu shtua damu tu hapo upoteze, atakuona kuku mtamu"

"Hapo mwanangu umelonga, akijileta najipigia halafu najikataa. Akizungua namfanya kiporo tu maana mtoto wezere lipolipo na mwili umejaa kinamna fulani hivi"

"Unaona sasa ulivyo fala sasa bro, yaani unataka kuipotezea hiyo. Kula hiyo"
"Sasa Fred nishakuwa fala tena, dogo unazingua sasa adabu inashuka"

"Sorry Bro Kevi, ila hiyo usipoteze kabisa wewe tafuna"

"Hapo hakuna noma, simwachi"

Hawa ni vijana wenye kukaribiana kiumri, wenye itikadi moja kwenye mambo mbalimbali yahusuyo maisha yao. Ndiyo maana hawakuwa wakiisha kuongea kwa pamoja, hata kuambizana kwa baadhi ya mambo, wao ilikuwa ni jambo la kawaida kuweza kushirikishana. Mkubwa ni mwenye kuitwa Kelvin ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha tano shule ya sekondari Tambaza, mdogo ni Fredrick au 'Fred' kama alizoea kuitwa. Huyu ni mwanafunzi wa kidato cha tatu, akiwa amepishana miaka miwili kielimu na kaka yake.
___________

Alice alifika hadi alipo Jamal ambapo alimkuta akiwa yupo barazani, mikono ameshika kwenye sehemu ya vyuma huku akitazama yalipo maegesho ya mgari. Aliungana naye mahali hapo akisimama upande wa kushoto kwake, kisha akatupa macho usoni mwa kijana huyo ambaye ni mtanashati mno.
"Mawazo mengi yamekuzonga Jamal", Aliongea na kufanya atazamwe na mhusika.

"Oooh! Kumbe umefika hapa?"

"Sasa ulitegemea mimi nifanyeje Jamal, umeniacha hapo sebuleni nikiwa bored, nimekufuata wewe ila sikuoni ukiwa mchangamfua kama ilivyokuwa mwanzo"

"Hamna kitu, mabadiliko ya hali ya hewa huwa ya ghafla ndiyo sembuse mimi mwanadamu kubadilika ghafla"

"Ila kila kitu kina cause yake"

"Ila si kila cause inapaswa kuelezewa, mengine ya kuacha yapite Alice"

"Why?"

"Elewa hilo, ila sasa hivi nipo Ok. Ila angalia nisipigwe mabuti na mjeda huko ndani"
"(Akitabasamu) Wala Sis hayupo hivyo mbona ni mtu peace sana huyo"

"Sema hivyohivyo tu nije kurushwa kichurachura na kufulisha gwanda lile, nitakumeza wewe"

"( Akicheka) Sasa ukinimeza mimi si ndiyo utanitapika, dada yangu anavyonipenda unafikiri atakuacha. Atakupiga risasi"

"(Akishtuka kimaigizo kisha akaweka mikono tumboni) wee! Utanifanya nibanwe na tumbo la kuhara la fasta, risasi ni kama kipindupindu tu au ndoto ya kukojoa. Ukizubaa umeaibika kwenye nguo zako"

"(Akitabasamu) Ukinimeza as you said, ndiyo ataikoki akunyooshe kabisa"

"Huo uoga wake nikiwa ndani ya pipa, nitajikojolea lijae hadi limwagike. Isikie tu hiyo kitu"

"haaaaaa! Wewe mwoga sasa"

"Bora nibaki hivyohivyo tu aisee"

Hali ya kawaida ya Jamal ilirejea kama hapo awali, hakujisikia ganzi joto yeyote katikati ya miguu yake. Pia kukaa hapo alipapendelea akiwa na malengo mawili tofauti, moja ni kumfanya awe huru na vituko vya Alice. Jingine ni kumfanya binti aliyekuwa akimpa mtihani pasipo kalamu ashindwe walau kuendelea kufanya namna ile, Mita chache kutoka hapo maegeshoni alionekana mlinzi akiwa ni mwenye kutazama huko walipo. Pia dereva wao ambaye aliamua kutoka nje kupunga hewa alidhihirika.

Alice asingeweza kufanya hivyo, ikiwa ni msichana mwenye kujiheshimu. Hata kama angekuwa ni mwenye kutokuwa na aibu bado ingekuwa ni ngumu, dalili za wazi za kuingiwa na kitu kipya moyoni mwake zimeshaonekana. Sasa angeamua kujiweka kama vile alivyokuwa ndani, basi ingekuwa ni fedheha kwake. Jamal angemwona ni guberi, hivyo angemkosa moja kwa moja. Hii ndiyo akili aliyoamua kuifanya kijana huyu, maana dalli zote alishaziona.
________________


SIKU HIYO IKAPITA
Siku kadhaa mbele Heriety na Gina walifanikiwa kuonana ufukweni maeneo ya Kigamboni, wasichana hawa ambapo awali walifarakana kisa tu kutokuwa huruma kwa mmojawapo. Walikutana wakiwa na kundi la wasichana wengine wanaosoma nao, huo ndiyo ukawa mwanzo wa wao kuanza kuongea kwa pamoja. Hawakuona sababu ya kuendelea kununiana kwa jambo ambalo lilishapita, walikaa sehemu huku wakizungumza na kukumbushiana mambo mbalimbali.

Heriety alichukua muda huo kuwaeleza baada ya Jamal kufikishwa zahanati ya kijeshi. Alipoeleza alijiwa na kumbukumbu ya maneno ambayo kijana yule aliyeamua kumsadia alimweleza, akaamua kuficha baadhi ya vitu kutokana na kuhimizwa asieleze. Hakujua kwanini aliombwa hivyo, hata kutaja ndugu aliyekuja kumchukua ni nani pia alikatazwa. Aliamua kueleza tu ugonjwa tu aliyoambiwa ambao kwa asilimia kubwa alifichwa chanzo halisi kilikuwa ni kitu gani, walisikitika mno hao wenzake kasoro tu Gina alichukulia ni jambo la kawaida.
"Inamaana Jamal kumbe ana BP, masikini na jinsi alivyo na kipenzi cha watu yaani namwonea huruma", Grace aliyekuwa miongoni mwao alieleza.

"Ndiyo hivyo jamani, ndiyo maana huwa hapendi kuchukia kabisa. Kama kuna aliyewahi kumwona akiwa amenuna aniambie, ni kiumbe wa ajabu sana yule", Heriety alisema.

"Huko kununa wapi, mimi sijawahi kuona hata mkunjo kwenye sura yake. Na kingine nilichokijua kuhusu yeye ni hapendi hata mtu amchukie na akijua hilo atamzoea ilimradi tu asiwe na chuki ya mtu", Mwingine alisema.

"Exactly Gilo, he is the man of people", Heriety alisema.

"Halafu kingine nilichokijua ni kwamba, ni mzuri mno yule ila anaishi maisha si mazuri ndiyo maana ana mavazi duni mno. Angekuwa kama Kelvin haki mule shuleni wangepigana watu ngumi", Mmojawapo aliyekaa kimya kipindi wenzake wanaongea alisema.

"Yap Nasra na wewe umeliona hilo, uzuri wa Jamal niliuona siku ile ambayo alibebwa akiwa anakimbizwa Muhimbili baada ya kufunga goli la ushindi kwenye mechi", Grace alisema na kupelekea wengine wacheke tu, muda huo Gina hakuwa ametia neno alibaki kimya tu.

"Heeeee! Inamaana Grace akija hapo na kukupa ya moyoni, utaingia line kabisa?", Heriety aliuliza.

"Sasa je! Nani ambaye hataki kuwa na boy mwenye kumpa furaha kila muda, asiyejua nini maana ya kuchukia. Mwenye matendo yenye kuvutia, nafikiri atakayekataa atakuwa na matatizo au chuki binafsi tu kwake", Grace alisema.

"Yaani yule angekuwa ni cheche, hivi wangetoka wangapi pale shule?",Nasra alisema na kupelekea wote waanze kutazamana kila mmoja.

"Eti Gina wewe ungepona kweli?" Gilo aliuliza swali ambalo Gina hakulipenda ila hakuwa na namna zaidi ya kulijibu tu.

"Jamal ni mcheshi na mwenye kuongea na kila mtu, but he is not my cup of tea. Yaani hanivutii kwenu ni mmekufa kwake nyote, but kwangu kuna mmoja huyo nikimwona tu nahisi kusisimkwa tu", Gina alisema.

"Heee! Makubwa haya, nani huyo?" Grace aliuliza.

"Its Kelvin, that boy is so handsome and smart"

"Hapo hatukulaumu kabisa, ila yule tatizo ni tabia hajatulia hata kidogo. Yaani mwaka Tambaza hana, keshatembea na girls kumi ninaowajua wa five na six", Nasra alisema.

"I don't care even ametoka na shule nzima, kwangu tabaki ni mwenye kuvutia tu. I love him" Gina alionesha kutojali anayoambiwa.


*WASICHANA NAO WAKIWA PAMOJA, WANA MENGI YA KWAO

*JAMAL AAMUE KUMKWEPA ALICE, KWANINI?

*JE MABINTI HAO WANAOMPENDA JAMAL, MMOJAWAPO AKIMPATA KUNA MWENYE UWEZO WA KUVUMILIA NA KUMWONA KAMA SHEMEJI?





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA



_____SEHEMU YA KUMI_________


"I don't care even ametoka na shule nzima, kwangu tabaki ni mwenye kuvutia tu. I love him" Gina alionesha kutojali anayoambiwa.



TIRIRIKA NAYO____________

"Mh! Makubwa haya, kwahiyo mwenzetu upo tayari kwa lolote lile ambalo litakukuta hata kama Kelvin akiwa na tatizo", Heriety alisema.

"Loce is blind , nimekuwa mpofu na sioni hata shimo lililopo mbele yangu juu yake girls. Toka nilipomwona akiwa yupo kwenye swimming na hot body yake, basi sijiwezi kabisa. That is boy is so hot", Gina alieleza.

"Sote hapa tunajua Gina hilo, ila kwakuwa umependa hatuna jinsi juu ya hilo. Kama ungekuwa ni kukupa ushauri, ningekwambia tafuta mvulana mwingine mzuri ila si Kelvin. Kwa sasa sina cha kukushauri, its up to you, maadam unajua ni mwenye tabia gani", Grace alisema.

Mvulana mtanashati ambaye hakufichika haiba yake hata akiwa ndani ya maji, yule aliyeonekana na Gina akiwa na wadogo zake. Ndiyo huyo Kelvin, alitokea haswa kuuteka moyo wake na akawa ni mwenye kutojiweza juu yake. Ingawa alijua wazi kijana yule chotara si mwenye tabia nzuri na mwenye idadi kubwa ya wasichana kule shuleni kwao na hata nje ya eneo la kituo chao cha kujipatia elimu. Hakuwa tayari kumkosa danga yule, ambaye hakuwa hata akijali upendo wake juu yake.

Waliyosema mapenzi ni upofu wala hawakuwa wamekosea, Luigina amepofuka haswa baada ya kumwona kwa mara nyingine akiwa yu wazi sehemu kubwa ya mwili wake. Hakujali hata kama aliyekuwa naye siku ile, alikuwa ni mpenzi wa kijana yule na tayari ilidhihirika ni mwenye nafasi kubwa kwenye moyo wake. Alichokiweka mbele ni kuweza kumpata, alibaki kuwa tayari hata kuchangia penzi hilo ndiyo maana akasema hajali kama ana mwanamke au hana.

Soga baina yao hao marafiki lilipamba moto na hatimaye hapo baadaye wakaagana na kila mmoja kuondoka.

________________

___Kufunguliwa shule____

Muhula mpya wa masomo ulianza, ndani ya shule ya Tambaza. Wale ambao hawakuwa wameweza kuwa pamoja kipindi cha mwezi mmoja, walirejea tena kuunganika katika kipindi hiki huku kila mmoja akiwa na hamu mno ya kuongea mwenzake. Siku hiyo ya kwanza masomo hayawakuwa yakienda sawa darasani, wanafunzi wengi walijawa na shauku ya kutaka kusimuliana mambo yenye kuhusu likizo.

Alipotoka mwalimu darasani tu, ikawa ni mwanzo wa wao kukaa vikundi na kuanza kuongea ya likizo. Majira haya yule mwenye uheshi kuliko wote, aliweza kuyatawala mazungumzo katika kikundi ambacho alikuwa nacho yupo karibu. Hadi akapelekea wasichana ambao hupenda mno kukaa na mvulana mwenye kufurahisha. Wasogee jirani naye na kucheka mno kwa kila alihokuwa akikitamka, Jamal alishageuka kuwa mchekeshaji mzuri kwani hata akama aliongea jambo lisilofurahisha na kutoa tabasamu basi wao waliishia kucheka tu.

Haikuchukua mrua mrefu, wanafunzi kadhaa walianza kuhamia kwenye kundi hilo. Walivutiwa mno na uongeaji wake, jambo hilo lilifanya Gina na aliyokuwa akiongea nao wabaki wachache mno lakini yeye hakuwa tayari kunyanyua mguu kusogea hapo. Ukweli ni kwamba alimchukia mno Jamal, ingawa hakuwahi kumkosea jambo ambalo lingefanya awe hivyo. Tangu mara ya kwanza alipomwona machoni kwake, hakuonesha kufurahishwa naye. Hakuwa na sababu maalum iliyompelekea kuwa hivuo, ila aliamua tu kuwa namna hiyo, laiti kama angelipewa madaraka makubwa hapo shuleni Tambaza. Yenye uwezo hata wa kumfukuza mwanafunzi, basi kijana yule asingekuwepo hapo shuleni kwa jinsi asivyopenda hata kumwona. Ni chuki bila ya sababu.

Upande wa kundi ambalo Jamal yupo aliendelea kutawala mazungumzo, ilipita kitambo mirefu hakukuwa na mwalimu aliyeingia darasani na hapo ndiyo akawa amepata wasaa wa kuendelea kuwa nyota ya maongezi hayo. Hadi mapumziko yanafika watu hawakutoka nje kisa kuendelea kumsikiliza kijana yule, hadi pale yeye mwenyewe alipowaambia kuhusu kuelekea huko. Baadhi hawakuwa tayari kwa hilo, kisa kupiga domo tu.
"Guys ni muda breki jamani, tutarudi baadaye sasa hivi twendeni huko. Matumbo yenu wengine yameanza fujo humo ndani, ni bora tuwahi kuliko ije kutokea vita ndani ya kuta za tumbo. Aftermath yake ya vita hivyo, itakuwa ni vidonda vya tumbo. Jalini afya zenu jamani twende breki", Jamal alisema huku akisimama, vicheko vilifuatia.

"Oyaa Jay umenogesha mtu wangu yaani hapa stimu za kwenda huko hamna, ila kwakuwa unaenda mwana twende sawa tunaenda pamoja huko", Mwanafunzi mmoja wa kiume alisema.

"Njaa na kuta za tumbo ni maadui wakubwa mno, chakula ndiyo diplomasia kati yao kuweza kuwafanya wasiweze kupigana hawa. Diplomasia hiyo itawafanya wawe kwenye vita baridi tu, nafikiri ukiwauliza watu wa HKL form six watakwambia ni nini maana ya vita hivyo. Sasa tuepusheni vita joto twendeni huko jamani, ila ni mpango wa kwenda Manzese leo tukamalize chapati zile", Aliwasihi na wote wakakubali kuelekea huko kantini.

________________

Haikuwa siku ya kwenda kazini kwake, aliishia kuwepo nyumbani tu, alibaki poekee ni mtumishi wa ndani. Siku hii aliipitisha kwa kutazama runinga tu, hakuwa na jmbo jingine la kufanya. Bi Agatha mwanamama yule ambaye alisaidiwa na Jamal, alibaki akiwa ameketi kwenye kochi la kisasa na macho yakiwa ameyaelekeza kwenye kioo bapa chenye kuleta picha. Huo ndiyo ikawa liwazo lake na macho yaliganda hapo tu, na alipoyarejesha chini basi yalifikia bilauri ya mvinyo. Ambayo aliinua na kuipelekea mdomoni kisha akapiga mafunda kadhaa, alifanya hivyo kwa mara kadhaa lakini ilipofika wakati fulani aliporejesha macho chini alijikuta anashindwa kuyainua tena kutazama kule runingani.
Mkono wake wa kushoto aliuona mkufu wa fedha ambao ulizungushwa vema na kuweza kuvalika. Huu ndiyo ulimfanya hata hamu ya kuendelea kutazama kioo kile imuishe hapohapo, aliyatuliza macho mahali hapo. Alijikuta akiuinua juu na kisha kuuangalia vyema kama vile hakuwa ameuona kabla. Aliushika kwa kiganja ha mkono mwinmgine huku akiendelea kutabasamu vyema kwa kuona fahari kuweza kuuvaa mkononi mwake.
"Wewe ni kama mama yangu, hata kama hukuweza kusababisha uzao wangu ila unastahiki kuitwa mama. Nilikuokoa nikiwa nina uchungu kwani mwenye kukuita wewe mama angeweza kuwa na uchungu kama angekupoteza, jambo ambalo limngeliweza kunikuta mimi ikiwa ningempoteza mama yangu. Hivyo wewe ni mama yangu tu, sina budi kukuita hivyo. Asante sana kwa zawadi yako ya cheni hii, nakuahidi nitaitunza vyema kwani umeweza kutambua umuhimu wangu kwa muda mfupi tu. Ila pamoja na hayo ningependa na wewe walau nikupatia mkufu huu ambao hutosha kabisa kuvaa shingoni, ila nitahitaji uuweke mkononi mwako. Naamini ukiuona basi utakumbuka kuwa kuna kijana mwenye kukupenda kama umemzaaa, kubali thamani hii niliyokupa kwa kupokea zawadi hii ndogo mno", Yalikuwa ni maneno ya Jamal yakiwa yanajirudia kichwani mwake, kila alipotazama zawadi ile aliyopewa.

Kweli kabisa aliweza kumkumbuka kila autazamapo mkufu ule, kama alivyoelezwa hapo awali. Bi Agath alibaki akishangaa na kudhani huenda alishushiwa Malaika kutoka mbinguni kuja kumwokoa na kumpa zawadi kama ile, kwani maneno aliyokuwa akitamka yule kijana kijana yalionesha ni mwenye moyo usiyo wa kawaida kabisa. Upendo kwa wandamu wenzake ulikithiri haswa, alijikuta akiwa na fahari haswa kuitwa mama na kijana yule ambaye hakuwahi kupelekea uzao wake.
"Laiti angelikuwa ni mwanangu wa kumzaa mwenyewe, basi dunia hii ningejiona ni mwanamke mwenye bahati ya kupata kijana mzuri kama yule. Sijawahi kumwona akiwa ni mfuasi wa dini, wala haoneshi kuwa ni mtu wa ibada. Ila huyu ninasema ni mtakatifu. Sijawahi kuona mwanadamu mwenye moyo wa hivi", Alijikuta akiongea maneno hayo ambayo muda huo, mtumishi wake wa ndani alikuwa yu karibu akimsikiliza.

Hakuwa na habari ya uwepo wake, ila kutokana na ukaribu aliyonao kwa binti anayemsaidia kazi za hapo ndani. Haikuwa jambo gumu kusogelewa na hata kuguswa na kutolewa ndani ya mawazo hayo yenye kumfanya hata asahau kuburudika kwa kupitia kioo cha runinga. Hapo ndipo Bi Agatha alipogutuka kutoka mawazoni, akageuka pembeni na kumtazama msaidizi wake wa kazi mwenye kuduwaa kwa jinsi alivyo.
"Mama tangu ulipotoka hospitali umekuwa ni mwenye kuuvaa huo mkufu muda wote na hata kwenda kuoga basi unao", Msaidizi wa kazi alisema.

"Anna mwanangu, siri ya mtungi aijuaye kata. Katu huwezi jua thamani ya mkufu huu ila ya kujua thamani ya mtu aliyenipa. Kwa macho unaonekana si wa gharama kubwa hata binti yangu amesema hivyohivyo, ila kutokana na mtu aliyenipatia basi huu ndiyo mkufu wa gharama kuliko yote niliyowahi kupatiwa hapa duniani"

"Kivipi?"

"Nitakueleza, kwanza umemaliza kazi huko isije ukakaa kunisikiliza huku ukichelewa kutimiza wajibu wako mwanangu"

"Nimemaliza kazi zote mama, naomba uniambie tu nijue ni wa nani"

"Nilikuwa nife kwenye mafuriko yale ya ghafla yaliyojitokeza pale mtoni, ila kutokana na kijana aliyeweza kuniokoa pale tena akiwa ni mgonjwa wala hakujali kuhusu kuumwa kwake. Ndiyo maana ninatembea na mkufu huu muda wote, kijana mwenye kuishi maisha ya kujiweza na mwenye adabu kupitiliza. Ni stahiki haswa niendelee kuwa na mkufu huu wake kama ishara ya kumkumbuka, Anna mwanangu ushawahi kusikia mwanamke kutamani angekuwa na kijana mwenye adabu kama kijana fulani?"

"Ndiyo Mama nishawahi kusikia kuhusu hilo"

"Basi mimi ndiyo nimetamani haswa laiti ningeweza kuwa na mtoto kama yule, au awe kaka wa mabinti zangu. Hakika hii nyumba ingebarikiwa kila kitu, ila ndiyo hivyo mwanamke mwenzangu ameweza kupewa baraka ya kuzaa mwana mwema namna ile. Mwenye kujawa na busara nyingi pamoja na ucheshi ilimradi hawezi kukukwaza moyoni mwako, yaani naapa hakuna ambaye aliwahi kukerwa na kijana yule. Na kama yupo mwenye chuki naye, basi ni chuki binaasi ila si kutokana na kuwahi kuudhiwa naye"

"Mama nimekuwa nikiongea nawe kuhusu mambo mbalimbali, na pia nimekuwa nikikupa ushauri kuhusu mambo mbalimbali. Nikiri tu hukuwahi kuwa namna hii kwa mtu ambaye hukuwahi kumzaa, hivi huyo kijana yupoje?"

"Maneno tu hayapaswi kuweza kumkchambua na kumwelezea kila kitu, naweza kuongea ila sitomaliza kueleza sifa yake. Nafikiri ikitokea siku akapata wasaa wa kuja kuniona hapa, nafikiri itakuwa ni jambo jema kabisa uje kushuhudia sifa za kijana huyo"

"Sawa Mama"

________________

Tangu alipoonana kwa mara ya kwanza na Jamal hakuwa akiisha maswali kwa dada yake juu ya kijana yule. Hata pale walipokuwa wakiongea kuhusu mambo ya kawaida basi hakusita kutaja jina la mvulana yule na kutolea mfano, jambo hilo hapo awali Doreen aliliona ni kawaida lakini lilivyozidi kushamiri akawa na shaka kuna zaidi ya jambo. Anamjua vyema mdogo wake hakuwa kuwa namna hiyo, mabadiliko hayo huenda kuna jipya ambalo halijui.

Ilifika kipindi akawa anamhoji kuwa namna ile ila hawakuwahi kupata jibu stahiki juu ya jambo lile. Siku hiyo baada ya mdogo wake kurejea akitokea shuleni, aliongea naye kama kawaida kwani alikuwa yupo mapumziko. Ila mambo yakawa ni yaleyale lazima Jamal atajwe kwa jambo fulani, ikawa ni kama jina pekee hilo mdomoni mwa Alice.
"Alice mimi ni dada yako naomba usinifiche lolote, niambie ukweli tu", Doreen alisema.

"Yes sis"

"Do you love Jamal?", swali hilo likawa ni zito mno kwake kwani alichelewa kutoa jibu. Aliinamisha uso chini, dada yake alisubiri jibu ila hakuwa akiona ujio wake.

"Alice mimi ni dada yako usinifiche chochote kile, maana imekuwa ni muda mrefu ukimtaja Jamal yaani haipiti muda basi kwako imekuwa ni namna hiyo"

"Dada unafikiri naweza kukujibu vipi hukusu suala lile, unanisomesha na kunilipia ada yangu, nahisi kutoa jibu naweza kuwa karaha kwako. Ila hakuna girl atakayeweza kustahimili kukaa na kijana yule asimpende, he is so special na mwenye kujiheshimu ingawa ni mcheshi kupitiliza hajawahi kuvunja heshima ya mtu kupitia kuchekesha kwake"

"(Akishusha pumzi) Pole sana mdogo wangu. moyo wako ulipo huko nahisi hata Shehoza mwenyewe akisikia hatoweza kukubali litokee hilo"

"Dadaaa kwaniniiii? I don't want to lose him"

"Alice, ni mapema mno kukueleza ishu ya Jamal ila kutokana nilivyomsikiliza Shehoza juu ya mpwa wake. Ni ngumu mno kuwa naye, hadi sasa naamini wapo wengi mno wanaompenda ila hilo suala ndiyo imekuwa tabu tu wasiweze kuwa naye kijana mtanashati na mcheshi kama yule"

"(Akitokwa na machozi) Siwezi kuacha kumpenda Jamal dada, nafikiri unajua wazi sijawahi kumpenda mwanaume namna hii na hiyo ndiyo mara ya kwanza. Siwezi kabisa".

"Stop crying Alice, ninayokwambia ni hali halisi mdogo wangu. Je unampenda kupitiliza?"

"Ndiyo Dada"

"Basi kama unampenda naomba usimuweke sehemu ya mapenzi. Ukimuweka huko utakuwa humpendi kijana yule"

"sijakuelewa"

"Ndiyo maana nikakwambia ni mapema mno kukwambia kuhusu suala hili, ila kariri hilo kwanza nililokwambia"

"Ni ngumu mno ujue"

"Kama unampenda basi uwe tayari kutimiza hilo", Doreen aliposema hayo simu ya mkononi iliita. Aliinuka kutoka hapo kitini alipoketi akiongea na mdogo wake, akaenda kupokea simu hiyo.


*MWANAMKE KUHITAJI MTOTO WA MWENZIE ANGEKUWA WAKE

*JAMAL ANA NINI?

*KWANINI ALICE AKATAZWE KUWA NAYE KARIBU KIMOYO?









ITAENDELEA!!!
 
Back
Top Bottom