Riwaya: Banguzi

Riwaya: Banguzi

RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


________SEHEMU YA KUMI NA MOJA_________


"Ni ngumu mno ujue"

"Kama unampenda basi uwe tayari kutimiza hilo", Doreen aliposema hayo simu ya mkononi iliita. Aliinuka kutoka hapo kitini alipoketi akiongea na mdogo wake, akaenda kupokea simu hiyo.



_______________TIRIRIKA NAYO


Kwake ni wimbo ambao hakuhitaji kuusikia masikioni mwake, ni sauti ambaye aliiona ni sehemu ya utani kwa kuambiwa vile. Haikuwahi kujitokeza hata siku moja dada yake akawa ni sehemu ya kikwazo kwenye maisha yake, ila hiyo ikawa ni mara ya kwanza kwa kufanyiwa hivyo. Aliona wazi kuna namna yote ni mapenzi juu ya Jamal, yalielekea kumpofua. Hakujali hilo alichojali ni kuweza kumpata kijana yule, hakuelewa kabisa imekuwaje hadi aambiwe vile ilihali si mwenye nia mbaya naye. Yaani ajibiwe kama vile ni adui yake wakati haikuwa hivyo, ni maajabu kabisa.

Upande mwingine Doreen aliona ni amelimaliza suala lile, kwa jinsi alivyokuwa akiheshimiwa na mdogo wake. Hakutaraji kama angeweza kwenda kinyume na maneno yale, hakuwahi kufanyiwa hivyo na wala hakuwa na shaka ya hilo. mkubwa ni wa kusikilizwa na haki yake sharti apatiwe na mdogo, na hiyo ndiyo kaipata kutoka kwa ndugu yake huyo wa damu.

Hayo ni mawazo ya afisa huyu wa jeshi lakini huweza kuwa si sahihi, mwanadamu si mwenye kuwaza usahihi kwa kila kitu. Kutokana na kutojua ya mbeleni, huu ni udhaifu ambao anao kila kitu. Pia kutojua lililopo kifuani mwa mtu ni sehemu ya upungufu mwingine, hivyo haiwezi kufikiriwa usahihi wa mawazo yake.

Pamoja na hayo, waswahili huwa na msemo mmoja maridadi mno miongoni mwa misemo mingi waliyowahi kuitunga kuenda na hali halisi ya jamii. Husema ya kwamba, ukimkataza mtu basi ndiyo utakuwa umempa hamasa ya kujua kile ulichomkataza kina nini ndani yake. Makatazo pasipo kutoa sababu, ni sawa na kumwambia mtu afanye kile ulichomzuia. Hili hakulijua kabisa Doreen, alichojali yeye ni kusikilizwa tu. Laiti angelifikiria, basi angemfuatilia kwa karibu mno Alice.

_____________

Kundi la wengi ambao asili yao si ujasiri, haimaanishi kuwa hakutotatokea ambaye ni jasiri. Itakuja kuzaliwa kiumbe mpya ambaye atakuja kuwa tofauti na wale wa mwanzo, au kutokea ambaye atabadilika na kuweza kushangaza wengine katika eneo fulani ambalo watu huwa pamoja.

Kitendo cha Jamal kuwa kipenzi cha waliyo wengi shuleni Tambaza, ilipelekea akawa ni mwenye kuhitajika kimapenzi. Ila hulka ya kike na kushindwa kuongea, ndiyo ikawa ni kikwazo kikubwa cha kuweza kufanikiwa walau mmojawapo kutoa la moyoni. Walijaribu hata kuonesha ishara ila kutokana na jinsi ambavyo wengi wao hutaniwa mno wakawa wanaonekana ni sehemu ya utani kwake. Kukosekana kwa jasiri mmoja, mwenye kuweza kujitoa mhanga. Haikuwa chanzo cha wote kuwa hivyo, hapo ndipo akaibuka binti mmoja.

Hadija, binti wa kimakonde mwenye rangi ng'avu kwenye ngozi yake. Mwembamba akiwa na umbile lililojitenga kiurembo kiasi kwamba hata nguo ya shule ndefu na nusu kanzu aivaayo sambamba na shungi lake. Kushindwa kuuficha mtindo wa mwili wake ambao Muumba alimjalia. Binti huyu ndiye uvumilivu ulimshinda na kuja, alitafuta muda akamkuta kijana yule akiwa ni mwenyewe na kuamua kukaa akiomba kuzungumza naye. Hapo ndipo alipopasua jipu ili lisiweze kufikia hatua ya utambazi.

Maneno yaliyojaa hisia kali, alimfunulia kijana huyu ambaye ni mwingi wa masihara mno kiasi kwamba hajawahi kuoneka akiwa amekunja sura hata kwa sekunde moja tu. Binti aliamua kupangilia maneno na kuelezea hisia zake huku machozi yakimlenga, alitaka kuonesha ni kiasi gani mno amefika kwake. Matamko ambayo hata Jamal yalimfanya amtazame kwa huruma na akaingiwa na moyo wa imani, ila kitu kilichopo nafsini mwake kikamzuia kuweza kumtoa binti huyo kwenye mateso makali ambayo yupo ndani yake.
"Hadija........msichana mrembo, mwembamba mwenye urefu wa wastani na mwenye kila sifa ya kuhitajika kuwa na mvulana mzuri zaidi yangu, nafikiria haswa naona hukupaswa kabisa kunitamkia mimi nisiyestahiki kuwa na binti mrembo kama wewe", Jamal alisema baada ya kusikiliza maneno ya mtimni kwa binti huyo.

"Hapana Jamal usiseme hivyo, wewe kila msichana shuleni hapa anatamani haswa kuweza kuwa nawe hujiulizi wewe ni wa hadhi gani hadi kila mmoja atamani hilo. Wewe ni wa hadhi ya juu hata kuweza kuweza kumteka mlimbwende mwenye umaarufu duniani kimapenzi, ndiyo maana tunakupenda. Naomba sana usijishushe hadhi ni kuzidi kuniumiza mimi tu kwani wewe pendezo la moyo wangu, haikufaa nisikie unajitaja namna hiyo. Nipe mwamvuli wa huba, nondokane na jua kali mno la kusaka tulizo", Hadija aliongea akiwa ameweka kando kabisa aibu ya kike. Waswahili husema mficha uchi hazai, sasa kaona ni bora kuanika.

"Unajua ninakupenda mno na sipendi kabisa kukuumiza, nakupenda kama ninavyowapenda kila mwanadamu ndani ya dunia hii. Nimeumbwa na moyo wa kupenda na sijaumbwa na moyo wa kuchukia. Sipo radhi kabisa binadamu mwenzangu aweze kunyong'onea na kuungua moyo kwa ajili yangu. Hata wewe kukupa jibu lenye kuumiza sipo tayari kabisa, ila Hadija nitafanyaje unafikiri"

"No Jamal usiseme hivyo, nionee huruma mimi hadi machozi yanafikia kunitoka ili tu niweze kuweza hisia zangu kwako. Nateseka"

"Naelewa hilo, tatizo moyo wangu ni sawa na gari ya mashindano kwenye barabara ndefu ya huba. Yenye uwezo wa kubeba abiria mmoja tu wa pembeni, ambaye naweza kumwita ni msoma ramani wangu huku mimi nikiwa dereva kwenye njia hiyo ya kushindana kuweza kushinda vikwazo mbalimbali vya kimaisha. Vipi nitaweza kuongeza wa pili, nafasi iko wapi Hadija. Huoni naweza kukuweka juu ya paa ya gari hilo, tena nipo kwenye mwendokasi wa kushinda majaribu ya kimaisha. Ukianguka na kuumia mimi nitakuwa ni binadamu mwenye hatia, pia kumbuka nimekueleza moyo wangu ni wa kupenda tu na si kuumiza. Ili kuepuka hatia hiyo, sitokuwa na budi Hadija"

"Jamal please(huku akipiga magoti lakini Jamal anawahi kumzuia, ili asiweze kuwapa hisia mbaya watu)"

"Hadija hivi kukuumiza, na kukuacha bila ya maumivu kipi ni afadhali?"

"Ni bora kutoniumiza, ila si kuniacha Jamal"

"Sasa nitaweza vipi hayo, nafikiri lugha hiyo niliyoitumia kwako imekuwa ujumbe mzuri kabisa. Nimependwa na wa kwanza ambaye ameweza kuwahi wengine wote, na kuipata nafasi pekee ya kwenye moyo wangu kwanini kwanini nikudanganye"

"I don't care Jamal, nachohitaji ni kukupata wewe tu na si kingine"

"Ujue.....(Jamal alisita kuongea baada ya kuonekana kundi la wasichana wakifika mahali hapo)

Ujio wao mahali hapo, binti aliyekuwa akihitaji tulizo. Aliulaani kwa nguvu zote kwani waliingia na kuanza kucheka, kutokana na kumzoea kijana huyo ni mwingi mno wa kuchekesha. Jamal aliamua kufanya vituko na hata kumfanya Hadija naye acheke, alidumu namna hiyo kwa muda mfupi kisha akainuka na kuwaaaga anaelekea msalani. Alielekea moja kwa moja kwenye vyoo vya wavulana, kawaida vyoo vya shule hii vipo upande wa chini kabisa kwenye pembe ya jengo. Kutoka pale alipokuwa hadi chooni alitumia umbali kidogo hadi akafika, akaingia kwenye ukumbi wa mlangoni. Halafu akaufuata eneo ambalo hutumiwa na watu wa vituo vifupi, hapo hakukuta mtu.

Jamal kufika hapo aliamua kutazama kila upande na akahakikisha yupo mwenyewe, kilichofuata baada ya hapo alivuta pumzi kwa nguvu mno na kisha akaiachia kwa ghafla. Kitendo hicho kiliambatana na machozi kumtoka, mikono aliiweka kiunoni huku kichwa akiwa ameinamisha chini. Alivuta tena hewa na kuachia kwa mara nyingine na kupelekea machozi yamtoke zaidi, aliamua kuinua uso juu kutazama kwenye sehemu ya zege ambayo imewekwa ili kuhimili ghorofa ya juu ya jengo hilo.

Huku akinyoosha kidole cha shahada juu alisema, "na..najua ni vibaya kusemea humu ila sina pa kulalamikia wacha nilalamikie humu. Umenipa upendo kiasi kwamba sichukii mtu zaidi ya kuwapa furaha, pia umenifanya nisiweze kukosea mtu ndiyo maana sichukiwi. Nimekuwa ni mtendaji wa wema kwa kila mtu, lakini mbona unanipa mateso ya namna hii. Sistahiki kupenda mimi, kiumbe gani mwenye huruma anayemwona mwingine akiumia yupo radhi asimsaidie".

Alipoweka kituo cha maneno yake alifuta machozi yanayomtoka, kisha akavuta kamasi ambazo tayari zilianza kumnyemelea kutokana na kilio chake cha kimyakimya. Sauti aliyokuwa anaitoa haikuwa ya nguvu kiasi cha kuweza kusikika na wa nje, ila moyoni aliamini anayemlalamikia ni mwenye kumsikia.

"Maisha yangu ni bahati nasibu, sijui hata hatima yangu itakuwa ni lini. Pamoja na hayo lakini sikustahiki haya mimi, mateso juu ya mateso. Nawapa watu furaha lakini bado inabidi niwaumize, kutokana na hili ulilonijaalia. Kama lipo nililokukosea basi naomba nipatie adhabu nyingiine ila si hii kabisa, sipendi wengine waumie kwa ajili yangu ukumbuke", Jamal alizidi kulalamika huku akitoa kilio cha chini kwa chini, muda huo kukasikika sauti za viatu kuashiria kuna mtu ni mwenye kuja mahala hapo.

Aliamua kujifuta machozi kwa haraka, halafu akafungua suruali yake ya shule na kuzuga ni mwenye kuchomekea. Akifanya hivyo alimwona mvulana mmoja wa kidato cha sita akifika mahali hapo, huyo alipomwona aliachia tabasamu.

"Ayaaa! Sukari ya warembo mwenyewe Jay, usiye na makeke ya kutupia viwalo ila wananata tu juu yako", Kijana huyo alisema na kumfanya Jamal atabasamu huku akitikisa kichwa chake.

"Yaani nilivyo ni chumvi yao si unajua kituko tu muda wote ndiyo kinachekwa, sasa fikiri kipendawacho kitachekwaje na wanaokipenda na uelewe mimi ni kituko tu"

"Acha zako wewe, tembezea toto hizo zimeelewa ramani jamaa. Ngoja nipunguze oil hafu kidogo mara moja", Kijana huyo alipomalzia kuongea hayo alianza kujisaidia haja ndogo, muda huo Jamal akamwaga na kuondoka mahali hapo.

______________

_Jioni_
Alisikia akitikiswa kwa nguvu huku jina lake likiitwa, muda huo ambao ni mwenye kujilaza kutokana na uhovu wa kutwa nzima na usiku alihitaji mno kuamka akasome. Aliona ni karaha kwa jinsi alivyokuwa bado analihitaji godoro kwa usingizi wa majira ya jioni, ambao husindikizwa na kiubaridi kwa mbali kilichotokana na feni lililopo kwenye chumba hicho. Kevi alijikuta akiamka akiwa hana budi, alikutana uso kwa uso na rafiki yake ambaye wanaishi naye chumba kimoja katika hosteli zao.
"Jofu kuna nini jamaa huoni mida ya kulala hii mtu wangu, jioni ni kupiga msuli jamaa", Aliongea kichovu kwa kutoa lawama kwa rafiki yake.

"Mtu wangu kuna shori yupo nje hapo anakuulizia wewe, man sikujua kama yule demu ni kisu vile. Dadeki", Jofu alisema.

"We fala na ulivyo fisi ushamezea mate tayari, kwanza ni nani huyo?"

"Si Gina huyo, mtoto kala umini huo. Yaani mguu ni chopsi kabisa:"

"Ma**e huyo mtoto shida yake ni upini tu, utaupata. Ngoja nikamcheki kwanza, safisha rungu ile", Kevi alisema huku akiinuka kitandani.

Alitoka nje akiwa amevaa bukta, alijongea hadi kwenye henga na kuchukua suruali akaivaa kisha akatoka nje. Akiwa na mwendo wa kichovu alipofika eneo ambalo kuna mpira wa gurudumu la nje la gari ulichimbiwa ardhini, alijikuta akitoa macho kwa kutoamini kile alichokiona. Gin akiwa amevaa gauni fupi jeupe, amekaa kwenye mpira huo huku akibana miguu kutokana na urefu wa nguvu aliyovaa kutomsitiri vyema.

Kevi alijikuta akiachia tabasamu la haraka kisha akaliondoa kuepusha binti hivyo asizidi kumtupia jicho usoni. Kwani alipotokeza aliona ni mwenye uso wenye shauku ya kusubiria jambo, aliamua atoe tabasamu kisha auavae umakini juu yake.
"Hi Kevi"

"Hi Gina, upo poa mrembo?'

"Hofu kwako tu, nipo poa mie"

"Mimi mzima wa afya, naona si kawaida"

"Kawaida tu jamani, au kuja huku ndiyo unaona hivyo"

"Yap naona hivyo, niambie"

"(Akiuma midomo yake huku akilegeza macho kidogo) Kuna kitu nahitaji unielekeze hope utanisaidia maana unakielewa vizuri"

"Ni fizo au kemia?"

"Pure"

"Mh! Mbona huo ni uwanja wa Jay huo, mimi huko si mjuzi sana"

"Jamaniii si ulimwelekeza Fidawa mchana mimi nilikuwa na ishu nyingine ndiyo maana sikuwajoin"

"Ohooo! Kama ni hiyo basi nitakushukia tu usihofu mrembo, jinsi ulivyokuja namna hii unafikiri atachomoa nani. Hata kama hajui atajifanya kushika daftari tu"

"(Akicheka kiaibu) Stop please Kevi"

"Ok, saa ngapi"

"Nafikiri muda wa kujisomea usiku itakuwa poa zaidi, we unasomea wapi"

Kevi aliposikia hivyo, akabaki akifikiria juu ya hilo. Kwa jinsi alivyo mpenda mabinti, aliona hiyo ni nafasi pekee haswa baada ya kuliona umbile la Gina. Alimtamani, na binti ndiyo alizidi kuweka mikogo mbalimbali kuzidi kumchanganya kabisa.

"Pindi na dawa huyu ngoja nivutie machinjioni kabisa" Aljisema moyoni kisha akasema, "Mimi leo ninasomea geto humu maana sitoki kwenda Azania wala Muhimbili kusoma. Vipi unaweza kuwepo".

Maneno hayo yalimfanya Gina ajifikiria kwa sekunde kadhaa huku akipeleka mboni yake ya jicho pembeni, Kevi aliganda ni mwenye shauku kubwa mno ya kutaka kujua kama atakubali jambo hilo.

"Mh!", Gina aliguna.

"Mh! What Gina, hautokuwa na nafasi muda huo. Basi tufanye muda mwingine au?'

"Nop siyo hivyo, Iam ready nitakuja muda huo"

"Good girl, same as your beauty"

"Mmmmmh! Jamani"

*MMMH! HUYU KELVIN HUYU

*GINA KUBAGUA WA KUMFUNDISHA NAYE

*JAMAL NI MWENYE VITA KUBWA YA KINAFSI, JE ATAISHINDA?

*VIPI HADIJA ATAWEZA KUKUBALIANA NA HALI HALISI KAMA ALIVYOELEZWA NA JAMAL?






ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


________SEHEMU YA KUMI NA MBILI_________




"Nop siyo hivyo, Iam ready nitakuja muda huo"

"Good girl, same as your beauty"

"Mmmmmh! Jamani"



__________________TIRIRIKA NAYO

Kevi alishajiona ni mshindi kuweza kumpata Gina hadi muda huo, mtoto wa kike kuweza kutoka hadi chumbani kwa mvulana asiye ndugu yake. Tena usiku hata kama ni kwa miadi ya kusoma, haikufaa kujiamini namna hiyo. Ila kwa Gina ilikuwa ni ajabu kwa kuamua kukubaliana na kila kitu. Kijana chotara alijipa asilimia mia moja. Binti huyo asingeweza kutoka salama akiingia kwenye himaya yake. Toka lini Mamba akaacha windo lililojileta lenyewe kwenye milki yake, ni jambo gumu mno kutokea, ni sawa na Mbwa mwenye njaa achunge mnofu wa nyama uliyopo mdomoni mwake kwa amri ya anayemfuga.

_____________

Upande mwingine majira hayo, alionekana kijana mwembamba na mwenyemrefu wa wastani akifika kwenye lango la zahanati ya magonjwa ya moyo iliyopo maeneo ya Kigogo jijini Dar es salaam. Ni katika muda ambao dakatari bingwa wa eneo hilo huwepo baada ya kutoka kwenye hospitli kubwa.

Kijana huyo mwenye nguo nadhifu mno, alifika mahali hapo akiwa na mkoba wa begani. Alipoingia ndani ya zahanati hiyo alikumbana na mapokezi ambapo alimkuta muuguzi mwenye zamu akiwa yupo kazini kama ilivyo ada. Alijongea hadi kwenye kioo cha mapokezi na kupelekea binti mwenye jukumu la kupokea wageni amuwekee uso wa bashasha kwa ujio wake.

"Karibu", Alikaribishwa.

"Asante dada, habari yako", Aliitikia ukirimu huo kisha akatoa salamu.

"Salama tu za wewe?"

"Salama,. dokta nimemkuta"

"Ndiyo yupo sijui ulikuwa na miadi naye?'

"Hapana sikuwa na miadi naye ila ni muhimu niweze kuonana naye"

"kaka yangu kwa hilo nikuweke wazi siwezi kukusaidia, kuingia hapa hadi uweze kuonana na daktari sharti uwe na miadi naye na si vinginevyo"

"Dada yangu ni muhimu mno"

"Hata kama ulitakiwa uje hapa ujipatie namba upangiwe siku ya kuja. Kwa leo yupo ofisini kwake anamsubiri mgonjwa wake ambaye ni huyohuyo na ahitaji mwingine kutokana na muda atakaochukua kumshughulikia"

Kijana huyo aliposikia kauli hiyo, alifumba macho kwa sekunde kadhaa kisha akaimanisha uso chini. Aliganda hapo akionekana ni mwenye tafakuri kuu, hatimaye alionesha ishara ya kukata tamaa kwani dada yule hakuonesha kujali kwa hali aliyomwonesha baada ya kusikia hayo. Alichojali ni kuchunga masharti anayopewa na mwajiri wake, ili asiweze kutia kitumbua chake mchanga.
"Ok", Alipotamka hivyo aliingiza mkono kwenye mkoba, alipoutoa ukawa umeshika bastola yenye sailensa

Alichezesha macho kwenye kila pande kwa mara nyingine, na kuona yupo mwenyewe kisha akaielekeza kwa binti yule, ambaye muda huo hakuwa na habari. Macho yote aliyaelekeza kwenye simutamba yake, hata kasiba ilipoelekea usawa wa paji lake la uso hakujua hilo. Loh! Ama kweli simujanja hizi hupumbaza watu, banati huyo alimaizi kijana huyo alishatokomea baada ya kumweleza utaratibu wa hapo.

"Mlango wa Dokta Yunus ni upi?", Kijana aliuliza na kumfanya amtazame. Alipoiona silaha ya moto alijikuta akishtuka ila aliwahiwa kutulizwa kwa kidole ha shahada tu kilichowekwa mdomoni. Kisha akaawambiwa, "sihitaji kusikia sauti yeyote ikitoka kwenye koo lake, naomba unitajie mlango wa Dokta Yunus upo wapi. Si sina miadi, hii ndiyo yenye miadi sasa".

Binti alivaa suruali yenye rangi ya kijani iliyopuka, ambayo ni sare za wauguzi. Kitendo cha kuelekezewa silaha namna hiyo, alijikuta akiachia haja ndogo mwenye bila ya kupenda huku akitetemeka. Alitaja uelekeo wa chumbani kwa daktari aliyetajwa jina, hata hivyo hakukuweza kumwacha salama. Bastola ile ilikohoa kwa sauti ya chini, paji lake la uso lilitobolewa hapo hapo.

"Pata safari ya kuzimu bila miadi", Kijana alisema kwa sauti ya chini kisha akarejea upesi hadi ulipo mlango wa kutokea zahanatini. Alifunga kwa ndani kisha akabadili kibao kilichopo mlangoni hapo ambacho kina maandishi 'close' na 'open'. Alikigeuza nyuma na kusomeka 'close' ikimaanisha kituo hicho cha afya kimefungwa majira hayo.

Alipotimiza hayo, moja kwa moja alipiga hatua kuelekea ndani mahali ambapo aliuona mlango unaingia kwenye korido ya jengo hilo, alipovuka kizngiti alitembea hatua takribani kumi akafikia mlango uliyoandikwa 'Doctor'. Hapo bila ya kuwa na hofu yeyote aliusukuma na kuingia ndani, ambapo alikutana na mandhari ya chumba cha Tabibu chenye samani za kisasa.

Bado hakuwa ameificha bastola yake, jambo ambalo lilimfanya mwenye chumba hicho ashtuke baada ya kumwona akimjia namna hiyo. Mwenyeji alipotaka kutoa sauti kwa kuona kifaa kisichopaswa kuwekwa hadharani, aliashiriwa akae kimya na aketi kwenye kiti chake.

"Dokta Yunus leo ni zamu yako", Kijana alinena kisha akaingiza mkono kwa mara nyingine kwenye mkoba wake. Alitoa mafaili kadhaa ambayo aliyarusha mezani kisha akasema, "soma hayo mafaili, uniambie tatizo hilo unaweza kulitibu?"

Alitumia dakika takribani mbili kupitia faili hiyo, kisha akalisogeza mbele huku jasho likimtoka kwa kihoro. Alibaki akimkodolea macho mtu yule ambaye hakutia neno jingine, akibaki ni mwenye kusubiri kwa hamu aweze kupatiwa jibu juu ya kile alichokiamuru.

Alipoona kimya kimezidi pasipokupewa jibu lolote ilimbidi atumie namna ya ukali huku jicho akilipeleka kwa daktari yule,"Hey! Usiniwekee usiku hapa, nimekwambia nini?"

"Hilo tatizo hilo lililopo huko ni very serious, siwezi kulitibu kabisa. Hata duniani kote hakuna aliyewahi kuugua na akabaki salama", Dokta alisema.

"Hilo ndiyo jibu umefeli, hujiulizi ni wangapi wanalia huku duniani kutokana na kukosekana tiba kwenye tatizo hilo. Yaani kusoma kote na kujinasibisha wewe ni bingwa wa kwenye maeneo hayo umefeli kutibu hilo. Ngoja ndugu waonje kile ambacho wengine wanakionja kwa kufeli kwako huko", Kijana huyo alisema kwa uchungu, alipomaliza alifumua paji la uso la Tabibu aliyemkuta kwa silaha yake kisha akachukua faili lake na kutoka ndani humo.

_________

Baada ya Gina kuondoka, Kevi aliingia ndani moja kwa moja na kumweleza mwenzake juu ya walichoafikiana. Jofu ambaye ni mwenye tabia kama za rafiki yake, alimsihi mno hiyo ni nafasi pekee ya kutoichezea kwani mnyange kajileta mwenyewe kwenye machinjio yao. Kijana hawa ni wenye kusoma uwezo wa haraka wa tabia za kina dada mbalimbali kuendana na mazingira ambayo hufika. Hivyo walishajua namna ya kuweza kushughulika na mabinti wa namna hiyo, akili kwa haraka ziliangukia kwenye majira ya kipindi hicho.

Eneo la Upanga ambalo ndiyo wanaishi walijua wazi majira ya jioni kulikuwa na kuna upepo mno haswa maeneo ya nje. Yote ni kutokana na kuwa karibu na bahari ya Hindi ingawa haiwezi kuonekana, kutoka hapo hadi daraja la Salenda si mbali mno. Hivyo chanzo kikubwa cha maji hakipo mbali, upepo wake lazima waupate, Hivyo hali hiyo walijua lazima binti yule ajae na nguo yenye kufunika mwili wake kwa kiasi kikubwa, jambo hilo itakuwa ngumu kwa Kevi kujaribu kutimiza azma yake.

Walichekecha bongo zao hima mno, hatimaye wakapata suluhu ya hayo. Ndani walijua lazima wafunge mlango kutokana na kuhofia mbu, na maeneo hayo kusipokuwa na feni basi joto litakuwepo tu. Kibaya zaidi chumba chao hakikuwa na feni la juu wanatumia la kuchomekwa kwenye soketi. Hapo ndipo wakaona ni namna nzuri ya kuweza kumfanya binti huyo apunguze mavazi yake, waliamua kuliondoa feni lao na kulipelekea chumba cha jirani ili akija kusiwepo na namna ya kupunguza joto umo ndani.

Baada ya kumaliza hayo Jofu alisema, "Sasa hapo mwana kuku lazima aende kibla mwenyewee"

"Na joto la humu dadeki lazima avue kama ana sweta la kumkinga na baridi. Sasa hapo ndiyo atakuwa kaisha mwenyeweee", Kevi alisema.

"Mchinjaji na ngawira yake...."

"Makali ndiyo huongea tu"

"Maliza kazi Kevi, kaja mwenyeweee"

________

Wakati walafi wa wakiandaa mazingira ya kupata chakula chao, Shehoza yu ndani ya kilabu kimoja cha kunywa vileo akiwa na Doreen. Muda huo tayari giza lilishaingia na watu wengi hupenda kujiliwaza kidogo kabla hawajafika majumbani mwao kwa ajili ya kupumzika. Ndipo matabibu hawa walikutana kwa pamoja, ukaribu baina yao ukiwa umezidi tangu wafahamiane kupitia Jamal.

Muda huo ni Doreen ndiye aliyehitaji kuonana naye kwa haraka, la si hivyo Shehoza angelikuwa yupo nyumbani kwake na mpwa wake asiyeisha vituko. Aliitikia wito kwa haraka kuweza kusikia kilichofanya Afisa yule wa jeshi kumuhitaji majira ya usiku. Wakati huo wapo kwenye meza ambayo imejitenga kidogo na wengine ikiwa jirani na kisiki cha mti ambacho kinaonekana wazi kilifyekwa kupisha ujenzi wa kilabu hicho.

"Afande wangu usiyeweza kunipa amri kwenye sekta yangu niambie, si kawaida katikati ya wiki hii", Shehoza alisema huku akitabasamu, na kumfanya binti yule achanue uso wake.

"Habibu wangu niseme kipi kingine zaidi ya kukumbuka na kuhitaji haswa kukutana na wewe maana kuna zito zaidi", Doreen alisema huku akipapasa kiganja cha Shehoza.

"Nuru ya moyo wangu, nipo kwa ajili yako hata kama ungeniambia nikakuwakilishe uwanja wa vita pia nipo tayari. Nimetega sikio kuweza kusikiliza wito wako na si vinginevyo mahabuba"

"Tunatakiwa tuzuie hili lisitokee kwa usalama zaidi mpenzi"

"Bado umeniacha kwenye barabara yenye njia panda nyingi mno, hujaniweka wazi kabisa nini haswa"

"Alice anampenda Jamal , kwa jinsi nimuonavyomuona inabidi tufanye kitu upesi mno. Nimemkanya juu ya hilo lakini akikutana naye huko mbele tusipokuwepo ataweza kuzuia hisi zake kweli. Hata kama ananisikiliza, mchana wa leo hili limeniletea wasiwasi", Shehoza aliposikia maneno hayo aliweka kiganja kwenye uso wake kama anapangusa kitu kisha akamtazama Doreen.

"Jamal ni mwenye kujielewa mno hawezi kufikia huko ila inabidi tu tuwaepushe wasiwe karibu"

"Shehoza kumbuka mwanaume mtego wake mkubwa ni mwanamke, je unamwandaa vipi kwa kujipa imani hiyo. Hata uwepo wetu kati yao si kila muda, unajua wazi Jamal hahitajiki kubughudhiwa kwa namna yeyote ile"

"Ok, nafikiri tumuhamishe shule ya mbali na hapa Alice itakuwa ni suluhu, awe anakuja likizo tu na akiwepo Jamal atakuwa kwa dada jijini Tanga hakuna namna nyingine. Namuhitaji mno kwa namna yeyote Jamal, sitohitaji apatwe na tatizo"

"Nalitambua hilo ndiyo maana nikakupa taarifa mapema, nadhani apelekwe Bagamoyo kusoma namtafutia uhamisho upesi sana, akirudi likizo wewe fanya kama ulivyoamua itakuwa ni namna bora zaidi"

"Ok, hilo limepita. Ila na mimi kuniita hapa kuna jingine limenijia kichwani mwangu sasa hivi"

"Niambie"

"Leo tunalala wote"

"Mmh! Mpenzi kesho kumbuka kesho ni kazini jamani, huoni nitachelewa na ninaingia asubuhi"

"Sote wa asubuhi kesho ya nini tuchelewe, hapo ni kubeba vazi tu na kufikia kwangu tu"

"Ok mshindi wewe, naona leo umeamua niende nikacheke tu huko kama mwendawazimu. Wacha Jamal akaniue mbavu tu"

"Leo unaenda kupata tiba ya gonjwa la kununa kama unalo, hutokunja sura hadi unatoka nyumbani kwangu. Utacheka kidogo tu, ila ndani utacheka zaidi"

"(Akiangalia kando)Bwanaaa"

__________________

Gina akiwa amevaa suruali ya mazoezi, na koti lake kwa juu. Alifika kwenye makazi ya Kevi ambaye muda huo alikuwa yupo peke yake, majira hayo alimkuta kijana huyo akiwa yupo nje akiperuzi mtandaoni kwa kutumia simutamba yake. Kitendo cha yeye kuwasili mahali hapo, alimfanya asitishe kutumia kifaa cha kiganjani na kumkaribisha yeye kwa bashasha.

Binti aliketi jirani na kijana kisha akaisifia simu nzuri ya kiganjanji aliyonayo, kwa kipindi hicho ambapo simu za namna hiyo hazikuwa zimeshika kasi. Tendo hilo likawa ni mwanzo wa kukaribisha maongezi baina yao, ambayo yalidumu kwa muda mrefu. Yangeendelea kutawala kama si Kevi kumuuliza kuhusu kusoma, binti alishajisahau kabisa lengo lililomleta hapo ni lipo zaidi ya kuendelea kuongea tu.

Ndipo alipouliza eneo ambalo wangetumia kwa ajili ya kujisomea, Kevi alimuweka wazi hakukuwa na kingine ila meza na viti viwili ambavyo vipo chumbani mwake. Gina hakuwa na jinsi zaidi ya kukubaliana kuingia ndani kuweza kuelekezwa somo kama alivyoomba.

Alikaribishwa kwenye chumba hicho chenye vitanda viwili vilivyobebana na kukiwa na meza ya kujisomea, binti kuingia ndani aliyataalii mandhari hadi pale aliponeshwa mahali pa kukaa ndipo akaacha.

"Gina samahani nahitaji niufunge mlango huu, maana humu mbu wanaingia na mimi si mtumiaji wa neti usiku. Huwa inanipa tabu mno", Kevi alisema na kumpelekea binti amtazame kwa sekunde kadhaa.

"Its ok, hata mimi ninaona utapata tabu usiku. Kuwa huru tu hapa ni ndani kwako", Gina alisema. Kevi hakupoteza muda alienda kuufunga mlnago wa chumba hicho kisha akasogea mezani muda ambao banati alishaanza kutoa kitabu cha hesabu.

*MMMH! GINA!

*SHEHOZA NA DOREEN NAO WANA YAO, JE MPANGO WAO UTAFANIIWA?

*MUUAJI NI NANI? NA KWANINI ANAUA?





ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

______SEHEMU YA KUMI NA TATU________



"Nop siyo hivyo, Iam ready nitakuja muda huo"

"Good girl, same as your beauty"

"Mmmmmh! Jamani"


______________TIRIRIKA NAYO

Ingawa binti huyu ni mwenye kuwaamBia marafiki zake jinsi anavyompenda kijana huyu, ila hakujua kama huo ni sehemu ya mtego aliyowekewa na yeye kaingia kwenye mstari uleule. Kama ni njiwa basi ameingiza miguu yake mwenyewe kwenye kitanzi kilichotengenezwa na uzi mgumu, kinachofuata hapo ni mtegaji tu kuvUta uzi huo na kumfunga miguu yote miwili au mmoja kama akiwahi kwenda juu tangu afyatue.

Somo lenyewe ambalo hujulikana kama ugonjwa wa taifa, lilianza kuelekezwa na kijana huyo ambaye hakuwa mjuvi mno ila ilibidi abebe dhima ambayo aliikubali hapo awali kuitimiza. Kaweka ahadi hakuwa tayari kuivunja kwa mnyange huyu. Aliuvaa ualimu na akatuliza akili mno, kuhakikisha aelekezwaye ni mwenye kunyaka kitu ndani ya ubongo wake baada ya kuisha muda wa kuelekezwa na si atoke mtupu.

Kipindi kisichohitaji ubao wala chaki kikiendelea, hali ya jijini naye ilianza kuleta bughudha yake. Ilijua haswa kumkera binti huyu, ambaye kutokana na uwepo wa wao wawili aliendelea kustahimili akiona anaweza kuvumilia. Hakujua malezi ya kulelewa kwa kupulizwa muda wote akiwa yu ndani ya eneo lenye halijoto, yangeweza kuleta makuruhu kwake. Aliendelea kustahimilia kipindi hicho, kutokana na vazi alilolivaa ndani hakutaka kabisa kufungua walau zipu ya koti lake lililolandana rangi na suruali ya chini aliyovaa.

Asiyezoea tangu lini shida akavumiliana shida? Ingekuwa ni maajabu mno ambaye hakukulia kwenye tabu kidogo kuweza kustahimili kero hiyo. Gina mwenyewe alishusha zipu ya jaketi chini hadi usawa wa kifua kuruhusu hewa iweze kuingia. Muda huo uso unang'aa mno kwa jasho lililoanza kumnyemelea kwa matundu ya kutolea takamwili hiyo yaliyopo usoni mwake. Nguo laini nyeupe iliyokatiza kifuani mwake ambaye ilitaka kufanana na brazia, ilidhihirika. Yeye hakujalia hilo alimua kuweka macho kwenye dafarti ambalo Kevi anaendelea kukokotoa.

Napo haikuwa ni afadhali, aliifunika mikono na mabega yake, aliamua kufungua zipu yote na kupelekea nguo ya ndani yenye mikanda kuanzia kifuani ionekane. Mabega yaliyojaa na ngozi isiyo na doa hata moja ilionekana kwa kijana huyu ambaye alijifanya kipofu. Kumbe moyoni anashangilia ushindi uu karibuni, aliendelea kujivika ualimu kama vile haoni. Gina aliweka macho hapo huku akilikinja koti na kuanza kujipepepea, Kevi akiwa anaendelea kufundisha alijifanya kukatisha baada ya kuhisi ubaridi ambao alijua ni kutokana na kujipepea kwa binti huyo.

"Anhaaa1 Nilijua umekuja na feni humu ndani kumbe ni jaketi lako", Alisema huku akionesha kushangzwa na badiliko ya hali ya hewa ya ghafla.

"(Akitabasamu) Nawe huilo feni nilitolee wapi, humu ndani kuna joto jamani sijui hata mnaishi wewe na mwenzako"

"Humu tupo kisela zaidi sema karibu tutanunua feni la juu si unajua hii hali haivumiliki. Nakuonea huruma, naona kama nina hatia mno kukupa tabu namna hii"

"Ooooh! Kevi usijali wala nini"

"Ok, tuendeleee"

Kuongea maneno machache, tayari Kevi alishakitupia macho kifua cha Gina. Walafi wa sketi daima hawashangai tu bila kutia neno, kufanya hivyo ni kumfanya binti ahisi ushamtamani. Majira hayo somo likiendelea akawa ni mithili ya Mamba mwenye kupanga namna ya kumshambulia Nyumbu aliyepo ukingoni mwa mto. Aliendelea kushuka kipindi huku akipiga soga mbili tatu na si kama ilivyokuwa hapo awali. Muda mchache baadaye alipelekea hadi binti akaanza kufanya masihara mwenyewe mbele ya kijana huyo, jamaa hakuonesha ni mtu wa utani mno ila mambo yalivyozidi kwenda naye akaanza kumfanya mzaha.

Gina aliona ni sehemu ya kutaniana tu, kwake ilikuwa ni faraja mno kumbe bwana mkubwa hapo ameshaanza kummezea mate baadaya kuona tungi moli za hupa ya chai ya vikombe viwili. Msichana huyu hakujua kwanini wahenga walisema mzaha mzaha hutumbua usaha, yeye aliendelea na kile alichokiona ni sehemu ya kudumisha ukaribu wake na Kevi kwa kupitia kutaniana.

Alipoanza kutekenywa alichukulia ni jambo la kawaida mno, alipokuja kutahamaki ni baada ya kuhisi wadudu wa mtembeo washavamia mwili wake. Hakujiweza na akawa ni mwenye kuishiwa nguvu, kijana naye alizidisha upagawishi kwenye maungo ya binti huyo. Akawa hadi hajitambui muda ambao alitolewa suruali yake aliyovaa ya chini, na hata kinguo cha juu kilichopo ndani ya jaketi ya traki.

Akasalia na mfuniko stara pekee, huo ndiyo aliweza kuleta pingamizi ulipotaka kutolewa. Ila kutokana na utaalamu wa kijana huyu aliweza kuondolewa napo. Akakaribisha kiingine, mlafi mwenye njaa akawa amepata chakula. Huo ndiyo ukawa mwanzo wa Gina kumpatia tunda Kevi, daftari wala hakulikumbuka kama alikuja kufundisha zaidi ya kuhamia kwenye kitanda pamoja naye. Ulimwengu wakahamia mwingine pasipo kutumia chombo chochote cha kisayansi chenye kuweza kuwatoa ndani ya dunia hii, ashiki tu ndiyo zilipelekea huko.
____________

__Mapambazuko__
Asubuhi na mapema, taarifa ya kifo cha Dokta Yunus mmoja wa madaktari bingwa wa moyo kutoka hospitali ya Taifa. Zilimfikia Shehoza akiwa anavalishwa nguo na Doreen ambaye alilala naye kwa pamoja usiku mzima. Mshtuko aliyoupata uligunduliwa hata na mpenzi wake mwenyewe ambaye alihoji juu ya hali hiyo, mwanaume aliamua kumuweka wazi mwandani kwae juu ya kilichotokea.
"Mungu wangu, kapigwa risasi?!", Doreen aliuliza kwa mshangao

"Ndiyo habari niliyoipata amekutwa kwenye ofisi yake kwenye dispensary yake ile ya Kigogo", Shehoza alisema.

"Sasa usalama unaelekea kuwa mdogo mno, kwani alikuwa na ugomvi na mtu huyu?"

"Wala hakuwahi kuwa na ugomvi na mtu, halafu unajua huyu ni dakarti wa pili wa moyo kukutwa amepigwa risasi. Unamkumbuka Mashishanga wa Bukoba yule, mwezi uliyopita tumemzika kwa tatizo hilohilo"

"Halafu unajua ninaanza kuwa na shaka kwanini wawe ni taaluma moja tu wanamalizwa namna hiyo na si wengine wowote. kuna kitu"

"Afande wangu mwamrisha mtima wangu tusijiwekee imani hiyo kabla uchunguzi haujafanyijka, maana hawa madaktari tuliyowapoteza walikuwa ni marafiki wakubwa mno. Usikute kuna jingine kabisa"

"Haya Dokta wangu, mtibu huba langu. Ngoja nivae vazi tuwahi kazini si unajua tena zamu ya asubuhi hii, Afande akizama hospitali na sipo zamu si itakuwa ni balaa hilo"

"Unamhofia Jenerali Kulika sana, yule afande kauzu hadi kwenu nyinyi warembo"

"Bora Kulika anaweza kukuelewa, mkute kaingia huko Afande Belinda au Afande Marwa"

"Haya vaa mama"

Wandani hawa walifanya hima kwa pamoja ili kila mmoja aweze kuwahi kibaruani mwake, Doreen alivaa gwanda lake nadhifu na akaweka kofia kichwani mwake. Kukamilika kwa nguo hiyo ya kiofisa, ilifanya Shehoza ampe saluti ya kiutani ingawa hakuwa akijua chochote kuhusu protokali za jeshi. Kicheko baina yao kilifuata baada ya yeye kufanya hivyo, haikuchukua muda mrefu walitoka kwa pamoja wakiwa wameongozana na Jamal.

Wakitumia usafiri mmoja, walitoka nyumbani wanapoishi hadi wakafika Upanga jirani na kambi ya Ngome. Hapo Doreen na Jamal waliteremeka na akabaki mjomba mtu ambaye alinyoosha moja kwa moja hadi kazini kwake. Afisa aliingia ofisini huku mwanafunzi akiingia shuleni.

__________

Heriety mwenye kuishi chumba kimoja na Gina, alishangazwa kumwona rafiki yake huyo akiingia asubuhi hiyo tena akiwa na uchovu mkubwa kupitiliza. Usiku uliyopita alimwaga kuwa anaenda kujisomea ila hakumtaarifu kuwa atapitilzia hadi kunakucha, tena kibaya zaidi alimwambia anaenda kwa Kevi.

Uingiaji wake na hata jinsi harufu ya jasho inayotoka ilimpa ishara nyingine mno, uchovu wake haukuhitaji elimu ya darasani kwa binti huyu kushindwa kutambua kile kilichokuwa kimetokea huko alipotoka. Ule usemi wa kwamba ukipatikana mkia wa Ng'ombe aliyekuwa akitafutwe kwa muda mrefu ukiwa pembezoni mwa mto, basi ameshatafunwa. Ulitosha wazi kumjulisha Heriety kuwa tunda lilishamegwa, kwani Gina alipoingia ndani tu kitu cha kwanza ikawa ni kukimbilia kuoga na si kingine.

Alibaki akisikitika jinsi mwenzake huyo alivyojitoa kwa kijana yule, mwenye kujua alama za ndani za mwanmke mithili ya dereva ajuavyo vibao vya barabarani akiwa safarini. Hakutaka kutia lolote juu ya hilo, kwani alishawaeleza kabisa hajali chochote kuhusu tabia yake, anachokiangalia ni yeye kuweza kumpata kijana mwenye mvuto kama yule. Kumpa risala ni sawa na kulitolea adhana sikio lililokufa, ukitegemea wito huo wa ibada utaweza kusikika na kutimizwa.

Ukimya muda mwingine wafaa sana, na ndiyo msichana huyu aliamua kuuchukua muda huo akimalizia kuvaa nguo ajiandae kwenda shuleni kwa ajili ya vipindi. Alipomalzia Gina alishaingia ndani lakini hakuonesha ni mwenye kutaka kuingia darasani kwa siku hiyo, Heriety alisubiri lakini ndiyo kwanza anamwona mwenzake akijilaza.

"Gina vipi mama, nakusubiri wewe si unajua muda wa mstarini unakaribia", Heriety alisema.

"Aaah! Wewe nenda tu nimechoka hatari, leo napumzika nitaingia drasani kesho" Gina alinena na muda huohuo mlango wa chumbani mwao ulifunguliwa akaingia Grace akiwa tayari ameshavaa sare kwa ajili ya kuingia darani.

Hali ya Gina kutokuwa tayari kuingia darasani, aliwasabahi na kisha akayaelekeza macho kwa mwenzao ambaye alikuwa na kanga tu akiwa amejilaza kitadani akioneakana ni mwenye kunyemelewa na usingizi majira hayo ingawa ametoka kuoga.

"Hee! Wewe Lui vipi mbona hivyo jamani si muda wa darasani unaelekea huu, mbona mwenzetu ndiyo kwanza unaonekana una usingizi?", Grace aliuliza.

"Nimechoka hatari acheni tu, hapa inabidi nilale hakuna namna. Heryn ukitoka niagizie msosi kwa Mama Juma hapo, atume mtu aniletee huku", Gina alisema.

"Umechoka na nini wewe?", Grace alihoji.

"Achoke wapi kachoshwa huyu, kapiga kwata jeshi la msomali", Heriety aliongea kimasihara na kumfanya Grae acheke kwani alishajua anamaanisha nini. Gina aliinuka kwa haraka mno huku mkono ukiwa kifuani kwa kushikilia kanga maana ilianza kumwanguka na mlango ukiwa haujafungwa vizuri, aliachia kofi la nguvu ambalo halikumpata Heriety aliyekimbilia nje huku akicheka kama kichaa.

Grace ndiyo kabisa alibaki akishindwa hata kusimama na akawa amekaa kitako, aliendelea kucheka kwa nguvu mno huku akimtazama Gina ambaye hakuelewa alipata wapi nguvu za kuinuka hivyo na kujaribu kufanya yote hayo. Muda mchache baadaye Heriety alirejea huku akicheka tena, na kufanya kicheko kisimame baina ya watu hao wawili wakimtazama mwenzao.

"Nyau nyie mshaniona kituko kwahiyo"

"Jamaa kajua kakumua vile kama koligeti hadi hujiwezi, ama kweli gari lilipata dereva kalipelekesha awezavyo", Heriety aliendelea kuropoka huku akicheka.

"Heryn utaniua mwenzio mbavu zinauma", Grace alisema hku akicheka kwa nguvu hadi machozi yakawa yanamtoka, Gina ilimbidi atulie kimya tu kwani siku hiyo alipatikana haswa, hakuwa na ujanja mwingine wala mbinu ya kuweza kuendana na utani wao.

"Jipu lilipata mkamuaji jamani, kutoka kujihisi mwepesi hadi kujihisi mzito kama meli ya makontena. Jamaa kakuhamishia uzito wake wote", Heriety aliendelea kuleta masiahra kwa mwenzake, Grace ndiyo aliendelea kucheka huku sauti ikawa haitoki vizuri ya kicheko chake.

"Manyang'au nyinyi mkimaliza ndiyo mtajijua kama mmechelewa kuingia shuleni. Mkafagie na kudeki korido zote leo, endeleeni kunicheka"

"Halafu kweli umeongea mama mkamuo, tumechelewa. Grace twende bwana huyo, kahimili gunia mwache apumzike", Heriety aliendelea kutania huku akitokea nje, mwenzake naye alifuata huku akiendelea kucheka kwa nguvu mno.

_______________

Jofu alimpongeza rafiki yake kwa kuweza kutimiza dhamira yake, ya kuujua mwili wa binti yule ambao aliusifu ni mlaini kupitiliza. Wavulana hawa mmoja akiwa amepata walau bahati ya kuingia na binti, basi mwingine yupo radhi hata akalale kwenye darasa ambalo wanapenda kusomea au hata kwa jirani ilimradi mwenzake aweze kumaliza mchezo mzima. Muda ambao Kevi yupo akivunja katazo la Muumba, mwenzake hakuwa mbali. Ni chumba cha jirani tu akiendelea kusikia kile kilichokuwa kikitendeka humo ndani, hata ilipofika binti akalala yeye alishapokea ujumbe wa kumweleza kazi huku ilifanikiwa.

Wenyewe walichukulia msichana yule ni wa kumfungua miguu na kumalizana nao kama walivyo wengine, hakuna hata mmoja aliyemshauri mwenzake na kumweleza kuwa amepata mwenza wa baadaye. Kwao walimwona ni kipoozeo tu cha hali zao, tena hawakufikiria binti aliyetoka humo ndani atakuwa ana fikra gani kwao.

Majira hayo kwa pamoja walikaa meza za nyuma darasani kusubiri mwalimu aweze kuingia, Kevi hakuwa kama Gina ambaye alichoka mno kwa shughuli nzito iliyofanyika usiku uliyopita, kwake kucheza gwaride zito kama lile ilikuwa ni kawaida mno. Siku zote mwanajeshi hawezi kuiona tabu ya kwata, ilihali tayari alishaiva kwa mafunzo mbalimbali ya ukomavu. Kwake ni suala la kawaida mno, ndivyo ilivyokuwa kwa kijana huyu. Ingawa alimaizi mapema, binti asingeweza kuingia darasani kwa shughuli nzito namna ile.

Yatakiwa kuhurumiwa mno kwa binti yule, kuamua kujitoa kwa kijana kama huyu mwenye kutumia utanashati wake kama silaha. Ameangusha wengi kwa kutumia namna ambayo amemjaalia Muumba, banati kama yule hakufaa kuingia mikono ya haramia wa kimapenzi kama huyu tena akiwa anamjua vilivyo. Ni sawa na kuingia mto wenye Mamba wakali, huku ukiwa unatambua fika hapo ulipotia mguu ni mahali kwenye viumbe wa aina fulani. Hakika ni wa kuonesa huruma mno, kwa kutozingatia.

*LOH! GINA KAAMUA KUJITOA KWA KELVIN

*JE TENDO LILE LITAZAA UHUSIANO?

*TABIBU WAWILI KUUAWA, NINI CHANZO?







ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_______SEHEMU YA KUMI NA NNE_______



Yatakiwa kuhurumiwa mno kwa binti yule, kuamua kujitoa kwa kijana kama huyu mwenye kutumia utanashati wake kama silaha. Ameangusha wengi kwa kutumia namna ambayo amemjaalia Muumba, banati kama yule hakufaa kuingia mikono ya haramia wa kimapenzi kama huyu tena akiwa anamjua vilivyo. Ni sawa na kuingia mto wenye Mamba wakali, huku ukiwa unatambua fika hapo ulipotia mguu ni mahali kwenye viumbe wa aina fulani. Hakika ni wa kuonesa huruma mno, kwa kutozingatia.


_____________TIRIRIKA NAYO

Soga juu ya kujitoa mhanga kwa Gina ndiyo lilikuwa likiendelea majira hayo, ilifikia mahali wakawa wanacheka kwa nguvu kusimuliana jinsi ambavyo aliweza kumchosha binti wa watu. Wakati ambao ilitosha kwa wao kujisomea, ikageuka ni wa kuongea maneno ya uani tu.
___________

Upande wa Gina ilikuwa ni faraja mno kuweza kumpatia tunda kijana yule ampendaye, alijitahidi awezavyo akihakikisha atakolea kwenye mwili wake. Hadi muda huo alipitiwa usingizini lakini njozi iliyotawala ikawa ni juu ya Kevi. Hakika alishika mno hadi akilini, alijiona yu pamoja naye na tayari wamefungua ukurasa mpya. Alijigeuza kitandani huku na huko akisikia maneno matamu ya ndotoni kutoka kwa kijana huyo, mwishowe alijikuta akiongea kwa kuyajibu huku mikono akiwa ameifumbata.

Hakika akili yake ilikamatwa vilivyo hadi kufikia kumtaja akiwa yu usingizini, laiti kama kungelikuwepo na mtu humo ndani ingekuwa ni jambo jingine kabisa na angetoa faida kubwa kwa yule anayemsikiliza. Aliendelea kugaragara akijiona amekabidhiwa utawala wa ulimwengu mzima dnani ya siku moja tu.

Akiwa yu mbali kimawazo usingizini, mlango wa chumbani uligongwa kwa nguvu zaidi ya mara moja ila hakusikia. Mgongaji alijitahidi awezavyo kwani alijua wazi humo ndani kuna kiumbe akiwa amejipumzisha, aliendelea kutumia nundu za mkono wake katika kuuliza mlango.

Gina akiwa yu njozini kwa ghafla alijihisi kama vile yale aliyokuwa akiyafaidi ni kama sinema yenye kuburudisha. Ikiwa imefika kilele cha kumpa burudani karaha za kugongwa kwa mlango, alihisi ni sawa na ukatwaji wa umeme wakati akiwa yu kwenye hali ya juu ya kukonga moyo yake. Yale yote aliyokuwa akiyaona yanajiri, ghafla alihisi yakizimika na akajikuta akiamka akiwa na hasira kuu. Alitamani hata apenye kwenye ukuta afike nje, amkamate huyo anayegonga mlango na amtafune lakini hakuwa akiweza kufanya hilo.

Aliamua kuinuka tu akiwa ameshika kanga yake vizuri, aliposimama wima aliifunga kifuani kisha akaenda moja kwa moja kufungua mlango. Kizingitini alikutana na mwanamke mtu mzima akiwa ameshika chombo chenye stafustahi, hapo ndipo kumbukumbu yake ikamjia ya kwamba aliagiza hilo kwa rafiki wakati anatoka kwenda shule. Hasira ikampoa ingawa alilaani ujio wa mwanamke yule, aliyekatiza furaha yake ya kufikirika.

"Chakula hiki hapa", Aliambiwa huku akikabidhiwa, alipokea sahani hiyo. Halafu akasema, "asante".

Alikwenda kukiweka mezani, na alichukua pesa aliyohitajika kulipia kisha akaja kumpatia mwanamke yule mwenye kutafuta tonge la siku kupitia umamalishe. Aliagwa na akafunga mlango kisha akaanza kutembea kichovu kurejea katikati ya chumba hicho, alifikia kwenye kiti cha kusomea kisha akaketi mahala hapo. Kichwa alikiinua juu, akafumba macho kwa sekunde kadhaa. Akiwa namna hiyo aliachia tabsamu mwanana na kufanya uso wake uchanue zaidi ingawa ni mwenye mang'ang'amu ya usingizi. Alidhihirisha ni namna gani Muumba alivyompendelea, hakika ni mrembo mno ingeongezwa na vipodozi ingekuwa ni zaidi kabisa.

"I love you Kelvin, I love so much", Alisema huku akiwa bado hajafumbua macho yake, mikono akaileta kwa pamoja kifuani mwake.

Laiti kama angelitokea mtu na kumwona, basi angelimfananisha na mwendawazimu. Kwani anaongea mwenyewe tena kwa sauti isiyo ndogo, na pili ni mwenye kutabasamu bila ya sababu yeyote ile. Hakika alipagawa mno, kama ni kupenda alifikia kiwango cha kupitiliza kwa kijana yule.
_______________

Muda wa kumalizika kwa vipindi shuleni Tambaza, Alice alionekana akiingia ndani akiwa na vazi la shule ya Benjamin Mkapa. Urembo wake ulidhihirika wazi ingawa yupo ndani ya sare, ni binti msafi kupitiliza kuanzia mavazi hadi viatu vyake. Pamoja na vumbi la jijini aliweza kujichunga na kuonekana ni wa kung'aa muda wote, shati ndiyo lilikoza kwa weupe kiasi kwamba likimulikwa na jua basi linaumiza macho ya wengine. Viatu ndiyo kama hakuwa amekanyaga ardhi zaidi ya kutembea hewani, kumbe katembea baada ya kushuka kituoni. Nywele binti huyu alizisuka kwa mtindo maalum wa shuleni, zikionekani ni nyeusi na nyingi kupitiliza.

Alipofika eneo la jengo la darasa, wavulana waliyokuwa wakitoka shuleni walimtupia macho. Hakuonesha kujali, alijongea kwa mwendo wake wa kujivuta hadi akafika eneo ambalo lina duka ndani ya shule hiyo. Hapo ndipo alimkuta msichana aliamua kumuuliza jina la Jamal ambalo lilileta tabu kumpata ila alipotaja wasifu aliweza kujulikana, kutokana na umaarufu wa kijana yule aliambiwa asubiri tu huku akidadisiwa na nani wake.

Alitaja ni rafiki tu na akaambiwa aketi anaenda kuitiwa, haikuchukua muda Jamal alifika mahala hapo akamkuta mnyange huyo kwenye mwonekano tofauti na aliyouzoea.

Alice naye alishangaa kwani kijana yule alizoea kumwona na mavazi ya kisasa zaidi. Ila hapo alivaa kikawaida tofauti na wavulana wengine wanaopenda kuvaa mitindo ya kimawazi hata kuzishona suruali zao za shule kwa namna nyingine. Alipopewa tabasamu na Jamal aliamua kumkimbilia kwa haraka, akamkumbatia kwa sekunde kadhaa humo dukani.

"Ni wewe au mwingine?" Jamal aliuliza akiwa bado amegandwa mwilini.

"Ni mimi yule na si mwingine, I miss you Jamal. Huonekani", Alisema.

"Kwahiyo hapa unaona uniform tu na viatu tu?"

"Siyo hivyo bwana, umeadimika mno"

"Nimekuwa mpunga msimu wa kiangazi?"

"(Alimwachia na kumpiga kibao) ushaanza uswahili wako mwone"

Jamal akijibu hayo, msichana mwenye kuuza duka hilo alishaanza kucheka kwani alimzoea ni kawaida yake. Hata aliponyamaza na kutoendelea na majibu yake, yeye aliendelea kucheka tu, asilimia kubwa ya wasichana kila wakimwona hujikuta wakicheka tu na hivi ndivyo ilivyokuwa kwake.

"Dada asante sana kwa kunikaribishia mgeni wangu, kungekuwa na Jamal wengi basi ningekwachia mmoja kama zawadi ili akupe furaha ya maisha. Tatizo Mungu hakutoa kopi yake", Jamal alimwambia msichana huyo huku akitoka na Alice humo dukani.
_____________

Mtu akionekana na kile kitu ambacho hakuzoeleka nacho, basi huwa ni habari kubwa mno kama ni mwenye kukaa midomoni mwa watu. Wale wenye kupenda kufuailia ya wengine basi huweza hata kuambizana ili kila mmoja akajionee, au asikie juu ya kile cha ajabu. Jamal kujiwa na msichana mrembo namna ile shuleni, ilikuwa ni habari nyingine kwa mabinti wa hapo. Aliyeona wa kwanza na jinsi walivyokuwa wakifurahi pamoja aliwaambia wengine, huo ndiyo ukawa mwanzo wa kusambaa kwa habari hiyo.

Alipoenda kuketi naye kwenye mgawaha maarufu sana hapo kwa watu wenye kupenda kuonekana wapo juu. Basi wengi walipita hapo mara wamsabahi Jamal, au wakatishe tu ilimradi tu kila mmoja aone ni banati gani huyo aliyenyoosha miguu kuja kumfuata kipenzi cha watu.

Habari ikavuma mithili ya mbiu ya mgambo, hatimaye ikamfikia Hadija aliyekuwa yupo hosteli akiwa amejilaza. Huyu aliona ni sehemu ya utani, ilipozidi kuongelewa na kila mmoja alimua kutoka mwenye kuja kujionea. Je ni kweli mwanaume yule ametembelewa na binti mwingine. Fikirani aliweka huenda ni ndugu yake kama itakuwa ni kweli kapatwa na ugeni, hakuwa na wazo kama huyo ni mpenzi wake.

Akitembea mwendo wa shauku mithili ya mwenye kuwahi sanjari, alifika hadi jirani na ofisi ya mlezi wa kike wa shule. Hapo aliweka kituo kidogo na kupelekea macho huko huenda angekuwa anamwona, ila uzio wa mbao wa mgahawa ule ulimzuia na hapo akajikuta akikata shauri. Akaenda moja kwa moja, alifika na kuuvuka na hapo ndipo moyo wake ulipopiga kwa nguvu.

Kumwona mnyange tena alionesha wazi hakuwa na nasaba na Jamal, banati ambaye kifuani alionekana ni mwenye rozali. Hii ilionesha ni mwenye dini tofauti na kipenzi cha moyo wake, vipi anaweza kuwa ndugu yake. Hapo akaingiwa na wasiwasi haswa alipoona mwenye jinsi moja akimshika ukosi, ustahimilivu ulimshinda na alipitiliza moja kwa moja hadi usawa wa madarasani ili aonekana wazi ni mwenye kupita tu mahala hapo.

____________

Baada ya kumaliza zamu yake kazini, moja kwa moja aliamua kwenda shuleni kwa mdogo wake. Jambo ambalo alilipanga usiku uliyopita na mpenzi wake, aliazimia kulitimiza upesi iwezekanavyo. Akiwa na vazi lilelile la kazini, aliingia kwenye gari ya jeshi, huku akiendeshwa na dereva mwenye cheo kidogo.

Alifika Kariakoo na akavuka mzunguko kisha akachukua upande wa kulia, ambao unaelekea Ilala. Alifika hadi kwenye shule ya Benjamini Mkapta, ambapo aliingiza gari ndani. Alilipeleka hadi maegesho kwenye jengo kuu lenye ofisi ya mkuu wa shule, gari iliposimama tu hakusubiri afunguliwe mlango alishuka mwenyewe akiwa hana kofia kichwani mwake.

Urembo wake ulifanya awashangaze wengi kwa vazi lile alilokuwa nalo, hakujali aliingia ndani moja kwa moja.

Alifika muda ambao ni mwafaka, bado uongozi wa shule ulikuwepo ndani. Hivyo aliweza kuonana na Mkuu wa shule kuweza kutimiza kile kilichomleta, ilimbidi adanganye tu na si kusema sababu stahiki ambayo ilimfanya hadi aje kumwombea uhamisho mdogo wake. Akiongeza na kutotaka mdogo wake ajulishwe kama anatakiwa kuhamishwa shule, majibu aliyoyapata ni juma moja baadaye angeweza kupata uhamisho wake ila mdogo wake alihitajika kujaza fomu ya kuonesha kuwa hadaiwi chochote shuleni hapo.

Doreen aliona ugumu wa suala hilo, hapo Alice lazima ajue kile kinachoendelea na hakuwa tayari kuona hilo likitokea. Ilimbidi atumie akili ya kuzaliwa na kuomba ijazwe hapo shuleni bila ya yeye mwenyewe kujua na uhamisho huo atakuja kuuchukua. Ni suala ambalo ni gumu mno kwa Mkuu wa shule ila kutokana na ushawishi wa binti huyu, ambaye amewahi kushika uongozi kwenye kambi tofauti kabla hajaletwa makao makuu. Aliweza kufanikisha hilo, bila hata kutumia njia siiyo halali. Ule usemi wa penye uzia penyeza rupia haukufanya kazi, ila aliweza kutimiza kila kitu. Aliondoka akiwa na majibu stahiki na kusubiri kama mdogo wake alikuwa anadaiwa chochote, aweze kulipa ilimradi aondolewe shuleni hapo.

________________

Siku hiyo ilikuwa ni kuna mechi ya kirafiki kwenye uwanja wa shule, hii ilisababisha Jamal na Alice wahamie eneo la bwalo dogo ya shule hiyo lililopakana na uwanja. Yote ni kuweza kushuhudia uhondo wa mchuano huo hapo shuleni, walifika mpira ukiwa haujaanza na baadhi ya wanafunzi wakiwa wanachezea mpira kujifurahisha wakati vikosi vikiwa maeneo yao vikivaa jezi kwa ajili ya kipute hicho.

Alice alifikia kuketi kwenye meza za madarasa zilizowekwa hapo kwa watu kukalia, Jamal naye aliketi pembeni yake huku akielewa wazi ameacha gumzo ndani ya siku hiyo kwa kuja na mrembo huyo. Kupenda kwake mpira, haikuchukua muda aliamua kuingia katikati ya uwanja huku akimwacha binti akimpungia mkono tu.

Wanafunzi waliyokuwa wakichezea mpira walipomwona, walijua wazi na yeye mwenye kuhitaji kugusa mpira walau kidogo. Mmojawapo alimpigia pasi ya chini, Jamal alipelekea macho yake moja kwa moja upande ambao kipute kinakuja. Alitegesha sehemu ya pembeniya mguu na ulipofika aliuinua juu, ulipokuwa ukishuka chini aliutegeshea bega akaupiga ukarejea tena juu. Ambapo ulimfikia kichwani mwake, aliipiga danadana kadhaa za kichwani kisha akautuliza gambani, akaushusha gotini na hatimaye akaupelekea mguuni. Aliendelea na danadana na akaupiga tena juu, aliinama ukatua shingo mwake. Alijiinua kwa nguvu zaidi ukarudi tena juu, mara hii aliuachia hadi ulipofika usawa wa mguuni akaupiga kuwarejeshea wenzake waliyokuwa wanauchezea.

Alipomaliza kuonesha manjonjo yake hayo alijongea kwa taratibu kurejea pale alipo Alice, akiwa anatembea namna hiyo mpira ukapigwa tena kuelekea upande wake na hakuwa ameuona hadi pale Alice alipomwonesha kwa ishara. Kwa haraka kijana huyu mwenye kujua kuuchezea mguuni mwake, aliugonga na kisigino ukawa unakuja mbele yake mithili ya anajivika kanzu. Alikuja kuuweka gotini kisha akaushusha mguuni, alipiga danadana kadhaa huku akionesha uwezo wake wa kuuongoza. Ghafla alifanya kama vile ni anapiga mbele walipo wengine lakini haikuwa hivyo, aliupiga ukamvuka kichwani mwake na kurejea kule unapotoka.

"Wee Jamal ungenipiga ujue", Alice alisema kwa uoga na kumfanya kijana huyo atabasamu.

________________

Umbea ni kazi isiyo na malipo, na wafanyaji wala hawaoni uvivu wa kutumia nguvu zao za vinywa cha hata milango mingine ya fahamu kuweza kuutimiza. Ni ajabu jingine hilo, ila mtu akiambiwa kuhusu kazi nyingine yenye kuingiza kipato, basi huwa mgumu mno kufanya. Ila kupeleka taarifa ambayo haimuhusu, ni jambo rahisi mno kwake. Hakika wanadamu ni watu wa ajabu mno, vya faida huweza kuvitupilia mbali kabisa ila vingine ni vya muhimu hata kama havina manufaa yeyote yale.

Habari za kuonekana Jamal na msichana mrembo hata kina Heriety ambao wao nao wameshikwa mitimani. Waliambizana na kweli wakajionea, sasa ikawa ni kazi ya kurejea kule wanapoishi ambapo yupo Gina pekee na kumweleza kila kitu. Ama kweli mabinti acha tu waitwe mabinti, hawakujali hata kama rafiki yao mwenye kumdharau huyo kijana na hakuwa akitaka habari zake wakaamua kumweleza.

Tena jinsi ambavyo akili zao wanazijua wenyewe, hawakujali kama ni wenye kuumizwa na hilo wao waliliweka ni sehemu ya maongezi yao tu. Tena wakawa wanaongea hadi mbele ya kipofu wa mapenzi, hali iliyopelekea awashngae tu.
" Hee! Inamaana huyo Jamal leo kawa star wa shule kabisa, yaani yule kituko", Gina aliongea kidharau.

"Yaani shosti leo hii ungemwona mwenyewe ungebaki mdomo wazi, yaani naona kapanga kumkomesha mtu yule si bure", Grace aliongea.

"Kwani huyo girl ana nini hadi atuzidi sisi na nyinyi hadi mmeamua kumuweka ni topic. C ut it"

"Gina shosti usione tunapayuka tu nenda sasa hivi kuna mechi huko shuleni, boys wote wapo huko hadi Kevi ndiyo utajionea", Heriety alisema.

"Ngoja niende nikamwone Kevi tu, ili nikione hicho kituko chenu", Gina alisema huku akiinuka kitandani alipokuwa amejilaza.


*DOREEN SHULENI KWA AKINA ALICE KUCHUKUA UHAMISHO, JE ATAFANIKIWA KUMUHAMISHA?

*HALI ALIYOIONA HADIJA, VIPI ATAFANIKIWA KUISTAHIMILI?

*GINA ANATAKA KWENDA KUMWONA BARAFU WA MOYO WAKE, ITAKUWAJE?








ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


________SEHEMU YA KUMI NA TANO_______



"Yaani shosti leo hii ungemwona mwenyewe ungebaki mdomo wazi, yaani naona kapanga kumkomesha mtu yule si bure", Grace aliongea.

"Kwani huyo girl ana nini hadi atuzidi sisi na nyinyi hadi mmeamua kumuweka ni topic. C ut it"


_______________TIRIRIKA NAYO

Hakuweka usiku tena, zaidi ya kubadili nguo tena akiongozana na wenzake ambao wala hawakumbuka kutulia chini. Walirejea shuleni eneo ambalo kuna mpira, huko walimkuta mrembo bado yu na Jamal, Gina mwenyewe akajionea wenzake wana haki yakumwita hivyo ingawa hakuwa mwenye mwili uliyojaza sana kama wao.

Baada ya kuona hilo aliamua apuuzie moja kwa moja na kuamua kumtafuta Kevi, aliangaza macho huku na huko na hatimaye akamwona akiwa yupo mwenyewe chini ya mwarobaini akitazama mpira unavyoenda. Bibie bila ajizi alikanyaga mguu kuelekea alipo kijana yule mwenye haiba, akipita pembezoni mwa uwanja hatimaye alifika upande wa pili na kumsogelea kijana huyo. Kufika na kufika alimgusa begani huku akitabsamu, alitegemea kupokea sura yenye bashasha lakini haikuwa zaidi ya kutazamwa kama vile ni mwenye kuonwa muda huo tu na si kabla ya hapo.
"Wewe vipi?", Kevi aliuliza.

"Jamani Kevi kwani hujui kinachoendelea, hadi tuka have a fun jana", Gin alisema.

"Ndiyo najua vyema jana ilikuwa vipi? Na leo imekuwaje?"

"Kevi mpenzi mbona sikuelewi?"

"Heee! Gina nimekuwa mpenzi wako kweli mimi, toka lini? Hebu nieleze"

"Unafikiri jana ilikuwaje?'

"Tuseme ni shetani tu alitupitia Gina, ila hatujakubalina kuwa wapenzi iweje leo uniite hivyo. Unajua kabisa mimi nina mpenzi"

"(Machozi yakimlenga) Kevi I can't believe ni wewe kweli?"

"Gina stop waste your time, haupo moyoni mwangu. Usitegemee kunipa mwili nitakuwa wako, forget about that"

"No I can't, nakupenda"

"Inaonekana huelewi wewe, chukua time yako wewe mimi sina muda na malaya"

Kevi alipoongea maneno hayo, aliamua kuondoka moja kwa moja hapo alipo na kuelekea upande mwingine wa uwanja. Alimwacha Gina akiwa amesimama hapohapo, mboni za macho yake zikianza kulowa taratibu. Hakutarajia kama yangekuwa hayo, alishaonywa mara nyingi kuhusu huyo kijana na watu wengi aliyowafanyia vibaya. Ila hakusikia hadi yamekuja kumkuta na yeye, laiti kama angeliwasikiliza hayo yasingemtokea.

Akimtazama kijana ambaye alijua tayari ameshafungua ukurasa mpaya, bado hakuwa akiamini kama ameachwa 'solemba'. Ndani ya muda mfupi tu tangu aweze kuwa naye kimwili, masikini Gina alipenda asipopendwa na hayo ndiyo yalimkuta. Laiti kama angelikuwa na utambuzi wala asingefikia huko, lakini ndiyo hivyo ameshapumbaa kwenye huba la Kevi.

Hakujua alifanya dhima ya muuza karanga, ya kuonjesha wateja karanga zake ili wajue utamu wake wanunue. Kwake yeye alisahau si kila mtu ni mnunuzi, wengine hupenda kujua tu karanga hizo zina joto gani au chumvi yake ikoje. Kama haikuwapendeza basi hawawezi kununua kamwe, laiti angeyatambua hayo basi asingetokewa na hayo yanayomkuta muda huo.

Alishasahau kabisa kuwa mnunua ndizi haonji na wala haangalii ndani ipo vipi, yeye huvutiwa na rangi ya ganda la nje na afya ya zao hilo. Yeye kaonjesha kabisa baada ya kuguswa tu, tena akiwa amejipeleka mwenyewee akijua hayo huweza kutokea yote. Hakika alipotea njia, kwa kujifanya anajua.

Mwishowe alilia akiwa yupo hapohapo, akimtazama Kevi ambaye ameshafika upande ambao kuna wanafunzi wengine wakiwa wapo makini wakiangalia mpira. Umbali tu kutoka walipo wengine ndiyo haukuweza kumtambulisha kuwa ni mwenye huzuni, ila kwa wenzake ilishajulikana hilo.

_________________

"Heryn nilijua tu kitamkuta kile, mwone Gina masikini", Grace alisema kwa sauti ya masikitiko akiwa wala hazingatii mtanange unaoendelea katikati ya uwanja.

"Tena nahisi kachangnyikiwa pale si bure, hebu twende kule", Heriety alisema na kisha akaanza kukimbia akizunguka pembeni ya uwanja kuelekea upande wa pili.

Grace naye akawa yupo nyuma yake kuwahi huko, walifika hadi alipo Gina ambapo walimwona uso wake ukiwa umelowa machozi. Mabinti hawa walijikuta wakisimama wenyewe na kubaki wakimshangaa mwenzao huyo, alitoka akiwa na hali sawa ila muda huo kabadilika kama vile kafiwa.

Waliduwaa kwa sekunde kadhaa ila walimsogelea na kumshika bega kila mmoja, Gina aliwahi kuwakumbatia kwa nguvu mno huku akiendelea kulia. Hakutarajia kabisa kufanyiwa vile na mtu ambaye alijitoa kwake. Hakika ni zaidi ya maumivu, wenzake hawa waliamua kumbembeleza hadi pale alipotulia. Walimfuta machozi na kuamua kutoka naye nje ya shule, hawakuona umuhimu wa kubaki mahali hapo. Walirejea kwenye hosteli za nje ambazo wanaishi, huku kila mmoja akisubiri aambiwe kile kilichojiri.

Gina alipofika wala hakuongea na mtu, alipanda tu kitandani na kujilaza. Unyonge mkubwa aliyokuwa nao hakuna ambaye alithubutu kumuuliza chochote walimwacha tu na kisha wakatoka nje.

"Yaani nahisi kimempata kama kile kilichomkuta Edna", Heriety alisema.

"Yaani unajua yule kaka na uzuri wake ameona ni sababu ya kuja kunyanyasa watu, mwanamke akimfungulia nguo tu basi kwake atamfanyia visa. Angejua nilivyo simpendi", Grace alisema kwa hasira.

"Ila Lui naye kayataka mwenyewe tulimwambia kabisa yule jamaa hafai, ona sasa kaenda kutumika na kaachwa"

"Shosti mimi siwezi kumlaumu mwenzetu, kupenda napo ni upofu. Anampenda haswa na si kutaka kudate tu. Its really love kwa mtu asiyejua thamani yake"

"Asiyependwa ndiyo hujua thamani ya pendo na mwenye kupendwa wala hajui thamani yake. Masikini Gina unajua mtu pekee wa kufaa kuwa na mwanamke yeyote ndani ya shule yetu naona ni Jamal tu. Laiti angelikuwa anampenda yule basi yasingemkuta hayo"

"Thats true, Jamal ni kipenzi cha watu na hakuwahi kuchukiwa na mtu yeyote kutokana na kumfanyia jambo lolote. Maana hajui ubaya na anajua kukaa na kila mtu, yaani Edna siku ile alivyolizwa alitulizwa na huyo jamaa, hadi leo naye kajikuta anampenda ila ndiyo hivyo that boy nahisi kawahiwa ndiyo anaheshimu sana hisia ya huyo aliyemuwahi"

"Heriety nisikufiche Iam in love with him badly zaidi hata vile ninavyokwambia but how can i start"

"Mimi pia pale nimekufa nimeoza ila sina jinsi, zaidi ya kuendelea kuishi naye jinsi alivyo. Boy ambaye kila mahali unapoenda basi watu ni mwenye maelewano mazuri naye, kule kambini tulipompeleka yaani nimekuja kurudi kawa rafiki wa Dokta. Yaani jinsi alivyo na anavyoelewana na watu, he kills me"

"(Akitabasamu) We are mad in love with funny guy"

"You are right"


________________


"Mwanangu wewe ni mbaya aisee, ushachenji gia angani. Mtoto alijua unatumia chombo chake cha huba, kumbe umedandia na umeshuka ulipofika safari yako", Jofu alimsifia mwenzake baada ya kuona kile chote kilichokuwa kikiendelea kule, muda huo kwa pamoja walikuwa wamekaa jirani na uzio wa seng'enge uliyopo nyuma ya goli la kusini mwa uwanja.

"Demu lofe kweli yule, alijua kuniachia ndiyo nitanasa hajui nina ulimi wa mwonjaji vyakula wa Presdaa wa nchi nishaonja kila aina ya chakula"

"Ha! Ha! Ha! Ha! Ha! Mwanangu wewe mafia kupitiliza, yaani aliingia cha kiume"

"Ndo hapo bwana akakuta masinki ya kukojoa wima, sasa katoka mwenyewe"

Muda huohuo kundi kubwa la wavulana wengine wakafika mahala hapo, ambao ni wenye urafiki nao mkubwa. Baada ya kupeana naye salamu ya ujana, kila mmoja aliyeona kile kilichokuwa kikiendelea kule alimpongeza.

Vijana hawa walimjua mwenzao vyema, kuona kitu kinatokea namna ile ni wazi tayari alishamaliza kazi. Haikuhitaji elimu ya ziada, kwani hakuwahi kuwa na mazoea na binti yule hadi kufikia kumefuata namna ile. Yaani kumchangamkia kijana yule, wakati aliishia kumtazama juu juu tu.

Vijana hawa pia walishafurahishwa na hilo, kwani binti yule kwao walimwona ni mwenye tabia ya ria. Wengine wote waliyowahi kufanyiwa vile walichukulia ni sehemu ya kujifurahisha lakini kwa Gina ilikuwa ni furaha kwao na walimwona hana jipya kwani tayari alishafunguliwa miguu.

Mambo haya kwa asilimia kubwa huwa yanawakuta kinadada, wakijiona ni wenye kufika mahala stahiki muda mwingie huwa wanakuwa wameingia pabaya haswa baada ya kujirahisha kwa wavulana. Hata kama anajua unampenda ila kwa vijana wa sasa akifanikiwa kukupata kirahisi basi kwake ataonekana ni mlupo. Hili jambo mabinti wengi ni wagumu kulielewa, hujiona wakishajitoa kwa kila kitu kwa kijana fulani basi ataona anampenda.

Muda mwingine yahitaji binti kuwa na msimamo walau kidogo, hata mvulana akija kumpata aelewe alimpata binti wa aina gani. Ajisifu kwa kuwa naye, na si kugusa tu amebogojoka mithili ya mbilimbi iliyoiva sana. Huku ni kuonekana binti mrahisi kupitiliza, wengi ndiyo huharibu. Kumpenda mtu haimaanishi kujirahisha kwake kwa mara ya kwanza tu mnakuwa pamoja, huku ni kujionesha ni namna gani ulivyo rahisi kufunguka mithili ya mlango wa choo cha umma.

__________________

Udaku shuleni uliendelea kama kawaida, hadi mechi inaisha na Jamal kuondoka na Alice. Wapo waliyoamua kumfuatilia kwa ukaribu, walipotoka nje ya geti na kuelekea upande wa kushoto wa barabara ya umoja wa mataifa. Waliyokosa kazi walikuwa pamoja nao, walipoifuata barabara na kuingia upande wa kushoto tena uelekeo ilipo shule ya kimataifa ya Tanganyika bado hawakujua kama wanafuatiliwa. Hakika kuna watu wanafaa haswa kuwa waandishi wa habari kwa jinsi wanavyojua kupekua ya watu.

Jamal pamoja na binti huyo waliingia ndani ya jengo hilo la shule ya kimatifa, walielekea moja kwa moja hadi eneo la maegesho. Hapo walikutana na dereva wa kina Jamal, ambaye walisalimiana naye na kisha kwa pamoja wakapanda ndani ya gari lile analolitumia. Mshika usukani alifanya kazi yake ya kuitoa motokaa ndani humo na kisha akaelekea uelekeo wa ofisi za TAKUKURU. Alipofika usawa wa njia ya Umoja wa mataifa, aliingia kushoto na kutokomea. Muda huo kuna mabinti walikuwa wakishuhudia kila kilichokuwa kikiendelea, walipoona wametoka ndipo wakatazamana kwa pamoja.
"Hivi yule mdada ni mtoto wa nani, maana sijawahi kumwona Jamal akiondoka na gari", Mmoja wa mabinti alinena.

"Mwenzangu hata mimi sijui, kumbe jamaa msimamo wake wote na kutooonekana na binti. Nyuma yupo yule" Mwingine akadakia.

"Jamani turudini shuleni haraka mje tumetoka mara moja tu, washaondoka wale" Mwingine aliwakumbusha huku akigeuka nyuma na kurejea kule alipotoka, wengine nao wakafuat kwa nyuma.

___________________

Yakijiri hayo kwenye chumba maalum cha uchunguzi, mwili wa Dokta Yunus ulikuwa umewekwa juu ya meza pana huku watu wawili wakiutazama kwa umakini wakiwa wamevaa mipira mikono. Mmoja akipiga picha na mwingine alikuwa akiendelea kuugeuza pande moja hadi nyingine, hawakuona jingine la ziada isipokuwa jeraha la risasi ambalo lilikuwa lipo kichwani tu.

"Leo hapa hakuna kingine zaidi, Jus kaamua kumaliza kwa kuacha alama nyingine kabisa", Yule aliyekuwa akipiga picha alinena.

"Muzu huyu mjinga inabidi apotezwe mara moja, tukiendelea kumlea ataleta maafa zaidi. Keshaua wawili, sisi tunakuwa tunakuja kuangalia kinyesi alichokiacha tu baada ya kunya. Sasa ni muda wa kumdaka kabla hajanya", Leo alisema.

"Hilo linahitaji mkakati haswa, unajua Jus ni very inteliigent na anajua nini anafanya"

"Hata kama, tutaendelea kuwaza wingi wa akili zake hadi lini. Kumbuka yupo Tanzania tu kumstop yule. Kaka yangu ni ana donda ndugu, dawa ilishazikwa. Hakuna namna nyingine zaidi ya kummaliza yeye, atamaliza wengi"

"Sawa ila tutoke humu ndani, hiyo dawa tuliyowalevya wasimamizi wa hicho chumba muda wowote wataamka"

Hawakupoteza muda, walitoka kwa haraka hadi nje ambapo eneo la kuingia humo ndani majira hayo wasimamizi wote walikuwa wamelala kwenye viti vyao. Waliwapita kama vile hawajui kile kinachoendelea na kisha wakaondoka eneo hilo, walionesha ni namna gani walivyo makini na kile wanachokifanya kwa jinsi walivyotumia ujuzi wa hali ya juu kuingia humu na hata kuondoka wakiwa wamewalaza wasimamizi.

________________

Jamal na dereva wake walifika nyumbani majira ya jioni giza likiwa limeanza kunyemelea. Walimkuta tayari Shehoza ameshaingia ndani. Mfanyakazi mwenye jukumu la kumwendesha, pamoja na kijana huyo waliingia hadi ndani wakasalimiana naye na kuongea naye mambo mawili matatu. Haikuchukua muda mrefu kila mmoja aliamua kushika lake, hapo ndipo Jamal akaingia hadi chumbani kwake.

Alifunga mlango na akaweka begi lake kitandani, muda huohuo alipotua mizigo hiyo aliweka mikono kiunoni kisha akainamisha kichwa chini. Alikaa namna hiyo kwa sekunde kadha na alipoinua uso, machozi tayari yalishajaa machoni mwake na taratibu yalianza kumtiririka. Macho aliyaelekeza juu kwenye taa ya umeme iliyopambwa mapambo ya gharama.

"Nimeamua kudanganya kihisia jambo ambalo si kawaida, nimeamua kuzifanya fikra za mtu zifikiri jambo siyo. Ona sasa amefikiri nina uhusiano na Alice, kwanini Mungu umenifanya hivi jamani. Sipendi kumuumiza mtu ila sasa hivi ninaanza kuwaumiza ili tu wakae mbali nami. Sifanyi haki kabisa", Jamal alisema huku machozi yakimtoka.


*GINA YAMEMKUTA, JE ATAWEZA KUSTAHIMILI?

*WAVULANA WENYE KUMCHUKIA GINA WAMEFURAHI KWA YALIYOMKUMBA, VIPI HESHIMA YA BINTI ITAKUWEPO?

*JAMAL NI MWENYE KULIA TU, SIKU GANI ATAFURAHI?






ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

______SEHEMU YA KUMI NA SITA_____


"Nimeamua kudanganya kihisia jambo ambalo si kawaida, nimeamua kuzifanya fikra za mtu zifikiri jambo siyo. Ona sasa amefikiri nina uhusiano na Alice, kwanini Mungu umenifanya hivi jamani. Sipendi kumuumiza mtu ila sasa hivi ninaanza kuwaumiza ili tu wakae mbali nami. Sifanyi haki kabisa", Jamal alisema huku machozi yakimtoka.


___________________TIRIRIKA NAYO

Hakuwa mwenye kupenda kuwaumiza wengine, ila ilifika muda akaona hakuna namna zaidi ya kuchukua uamuzi huo. Kwa manufaa yake na pia alivyojiamulia namna atakavyoishi, kiukweli hakuwahi kuwa na uhusiano na Alice. Ila aliamua kuonesha vile ili tu Hadija asiweze kuendelea kumfuata, atafute mwingine atakayemfaa na kumpenda ila si yeye.

Jamal alishajiharamishia kupenda, na hakuwa tayari kuona anafikia hatua ya kuazama mapenzini na binti yeyote yule. Daima ni mwenye kujiwekea maamuzi ambayo hapenda kabisa kuyavunja, hivyo hakuwa radhi kwenda kinyume na falsafa yake ile. Ingawa ni mwenye huruma kupitiliza bado haikumshawishi kuweza kwenda dhidi yaa utaratibu wake.
______________

Upande wa hosteli wanapoishi kina Gina, bado huzuni kwa mwenzao ilizidi kiwango. Walijitahidi wawezavyo katika kumtuliza ila haikuzaa matunda yeyote, waliishia kumwacha tu apumzike kwani hakuwa tayari kufanya lolote lile kisa kutendwa kimapenzi tu.

Mwishowe hata kula akawa na anagoma, walimlazimisha wawezavyo ili walau aweze kutia kitu mdomoni ila ikawa ni kutwanga maji kwenye kinu. Hakuweka chakula chochote hadi ilipofika siku ya pili mambo yakawa ni hayohayo, binti huyu mnadhifu wala hakuwa hata tayari kufanya usafi wowote ule pia. Asubuhi wenzake wanaenda shule hakuwa tayari kwenda nao, walipotoka kwenda kuoga hakuwa tayari kufanya hivyo. Kinywa pia hakuona umuhimu wa kukiweka safi.

Hakuona umuhimu wa kuweka mwili wake nadhifu, yule ambaye alipenda amwone ni binti wa aina gani mwenye kujipenda. Ndiyo huyo kaamua kumfanyia mabaya, sasa nani ambaye anaweza kumgeuza fikra na kujiona ana thamani. Wenzake wamejaribu wawezavyo lakini wala hakuna aliyeweza kufanikisha hilo, akabaki bila kuwa na usafi wowote.

Gina alimaliza siku hiyo akiwa hajaweka chochote mdomoni, hakutaka kufanya hivyo hata nguvu mwilini mwake ikapungua. Alichojua yeye ni kwenda haja tu, maji yenyewe hakuyaweka kinywani mwake, hali hiyo ilizidi kuwatisha wenzake na wakawa wanahaha mno kuhakikisha mwenzao anafanikiwa kula kitu chochote. Ila haikuwa hivyo, siku ya tatu iliwabidi waende kumtafutia mshauri. Hapo ndiyo afadhali ilipoonekana, Gina aliweza kukubali kula na hata kjisafisha na kurudia hali ya kawaida.

Furaha kwa wenzake ilirejea kwa kumwona akiwa rafiki yao yule waliyomzoea, walianza kumchangamsha kwa habari mbalimbali ila hawakuwa ni wenye kugusia kuhusu yule aliyemuumiza.

________________


_____Mwishoni mwa Juma___

Heriety majira haya aliamua kuyatumia kwenda kujiliwaza kwenye ufukwe wa bahari maeneo ya Msasani, siku hii alihitaji mno kuwa peke yake. hakufika eneo hili kwa lengo la kuogelea, ndiyo maana alifikia eneo ambalo kuna viti vya plastiki huku akiwa amekaa mwenyewe tu mahala hapo. Majira hayo akiwa yu mbali kimawazo, hakuwa na habari hata baada ya kiti kuvutwa. Macho yake aliyaelekeza ufukweni akiangalia mawimbi ya bahari yanavyokuja na kurudi, alipokuja kung'amua alipo kuna ugeni ni baadaya kugongwa meza.

Alipogeuza shingo alikutana na uso wa kijana ambaye si mgeni machoni mwake, aliyezoea kumwona karibu kila siku akiwepo shuleni. Huyu alimwachia bashasha pana na kuonesha haiba iliyopo usoni mwake, binti badala ya kuendana na jinsi alivyo alijikuta kibadilika na kuweka matuta mawili katikati ya nyusi zake. Hadi kijana yule akamshangaa, maana si ada hiyo ilihali hakuwahi kuwa na uhasama naye.

"Heryn upo poa?", Kijana huyo alimjulia hali.

"Kevi unafanya nini hapa?', Aliuliza kwa kumwona kijana aliyemuumiza rafiki yake.

"Kwani kuna ubaya jamani kwa mimi kukaa hapa, huoni itakuwa ni vizuri kuweza kupata mtu wa kupoteza naye muda . Wikiendi hii tunarefresh mind Heryn, kipi kibaya?"

"Waweze kutafuta mwingine wa kufanya hivyo, kwani mimi nahitaji kuwa peke yangu tu muda huu"

"No! No! Hata kiatu tu hakihitaji kuwa peke yake, muda wote kinatakiwa kiambatane na mwingine. Sasa utasemaje hivyo wakati wanadamu huwezi kuwa pekee yako"

"Kelvin! Hivi unaelewa kweli, nahitaji kuwa pekee yangu. Please leave me alone"

"Heryn"

"Usitake kuniudhi wewe, na sihitaji kumfokea mtu tafadhali ondoka"

"ok"

Kevi hakuwa na pingamizi, mwenyewe aliinuka kwenye kiti na kuondoka hapo. Alimwacha banati akiwa anatazama ufukweni, kijana mwenye kumchengua kila msichana kiakili. Siku hiyo aliona maajabu kwa kufanyiwa hivyo, kutokana na jinsi Heriety anavyopenda kuongea na kila mtu alijua ni itakuwa kwake hivyo, imekuwa mengine. Hakujua kile alichomfanyia Gina ndiyo sababu ya hayo, alijiona kaadhirishwa kuliko siku zote ndani ya maisha yake.

Heriety baada ya kuona amebaki mwenyewe, alijiona yu huru akiwa na ahueni ya kuondoka yule asiyempenda. Akiwa mahala hapo, kiti kilivutwa tena kwa mara ya pili. Kisha akahisi mtu akikaa, hakujali hilo yeye aliendelea kutupa macho kule alipokuwa. Akiwa namna hiyo alihisi kuguswa begani, jambo lililomfanya autoe mkono aliyefanya vile kwa hasira kisha akageuka kwa kasi kuweza kumkabili. Alipomwona aliyefanya vile hasira zenyewe zilipoa papo hapo, alikuwa mpole ghafla kisha akashusha pumzi kwa nguvu.

"Oooh! Jay, so sorry", Aliomba radhi baada ya kumwona Jamal waliyezoea kumwita jina jingine.

"Nini tatizo Heryn, unataka kunimaliza hapahapa", Jamal alisema.

"Forget about that Funny boy, kuna mtu kanichefua muda si mrefu nilijua karudi tena"

"Kakuchefua mbona hujatapika? Au umelamba ndimu"


"(akicheka) Jamal ushaanza yako sasa"

Ujio wa kijana huyo mahala hapo, ndipo ahueni na ile hasira ya kuondoka yule asiyempenda ilipoondoka. Alifurahi kumwona mvulana anayemhusudu akiwa amekuja kukaa naye, binti hakuhisi kujuta kuwa pamoja na Jamal. Alijihisi mwenye raha muda wote tena siku hiyo alijikuta akimpenda kupitiliza kutokana na mavazi aliyovaa. Hakuwahi kumwona akiwa amependeza namna hiyo, zaidi ya kumwona akiwa na sare za shule zisizompendeza kabisa.

________________

Yakiendelea hayo, Kevi akiwa na wenzake hawakuwa mbali kutoka hapo. Kitendo cha kuja pale mezani walishamwona akiwa mpweke, hadi jamaa anarejea walipo wenzake na kuwapa habari ilivyo bado hawakuwa wametoa macho kwake. Huku wakiwa hawaamini binti kama yule anaweza kumkatalia mtanashati, wakiwa hapo wakiona ni kioja mara walimwona Jamal akifika na kuketi jirani na Heryn. Watu hawa ndiyo waliingiwa na mstaajabu, hawakuwahi kumwona kijana yule akiwa amevaa nguo nzuri namna zaidi ya kumchukulia ni mmoja wa walalahoi tu.

"Oyaaa! Yule ni Jay au macho yangu yanaona vibaya?", Kevi aliuliza.

"Dah! Jamaa kumbe kwenye kutupia naye yumo, aisee nahisi kaazima", Jofu alisema.

"Nyie yule jamaa nahisi ni wa kishua tu anaamua kutuweka maigizo, nasikia siku ile alipokuwa uwanjani na ile pini ya Benja alichukuliwa na V8 la maana kuondoka kwao", Mwingine alidakia.

"Suma sikia, yule boya avitoe wapi kama hivyo. Labda yule gashi aliyetimba kumcheki, ndiyo wakishua ila siyo yeye", Kevi alipinga.

"Siyo hivyo jamaa, yule demu kaja na miguu na kashuka na daladala pale kituo cha Muhimbili. Wakati anashuka nilikuwa namng'aza tu, ule V8 ilitoka mule IST tena nasikia Jay ndiyo alikuwa akimpeleka huko siyo kupelekwa yeye"

"Suma wa wapi wewe, wakati analazwa yule boya kule Muhimbili maza kaja ni choka mbaya au haukuwepo wewe. Nakwambia jamaa ni mchovu tu, sema ule uchalechale wake ananasa wengi mno", Kevi alisema.

"Ndo hivyo, ila unajua nahisi huyu jamaa huyu mtoto kala. Maana anamwelewa vibaya, unakumbuka siku ya kufunga shule demu ndiyo kahangika naye huyu. Hata ule ukaaji wao pale kuna namna, cheki Heryn anamkumbatia kabisa", Jofu alisema huku akinyoosha kidole kwenda kule.

"Inamaana huyu Jay ndiyo alikuwa anasubiriwa hadi kanifanya nifukuzwe pale, man*na zake", Kevi alisema kwa kutopenda jambo lile.

"Jamaa mvungie tu, huoni kama umekula rafiki yake. Unafikiri wale magashi hawataambiana na wanalala room moja. Kaushie ile na jamaa naye ajidai, ila kapoa kwakweli", Suma alisema.

"Sumaa acha uchoko ujue, unajua wazi mimi nilitaka kuweka saini pale. Yule boya atanizidi vipi kete, lazima nimchimbe biti aachane na yule gashi"

"Weweee Kevi wa wapi wewe? Toka lini tukagombea demu sisi, vungia ile, wapo kibao hatujaonja kaushia ile na anatujua ni wazee wa baharini sisi. Tunakula kiumbe yeyote yule kasoro meli, unafikiri atakubali huyo", Jofu alishauri.

"Poa poa, ila jamaa akiamua kuanza kuwamega basi tutakuwa tumekosa. Magashi wanapenda ucheshi wake hadi namna anavyoliputa boli", Kevi alisema.

"Vunga, mademu wamejaa wengi tu Tambaza ni sehemu wapo wachache tu pale"

_________________


Gari aina ya toyota landruiser yenye mkonga ilionekana ikiwasili eneo la maegesho kwenye nyumba ya kifahari. Motokaa hiyo ilikuwa imejaa vumbi mno huku akiwa imebaba mizigo kadhaa juu ya gari hilo, lilisImama hapo huku likiendelea kunguruma pasipo kuzimwa.

Muda huohuo mlango wa dereva ulifunguliwa, Dokta Aesop alidhihirika akishukA ambapo alilakiwa na binti mwenye nguo maalum za wafanyakazi wa ndani. Huyu alikumbatiana naye akiwa na furaha kubwa, kisha akapokewa mkoba wake wa begani aliyoshuka nao. Haikuchukua muda mrefu, hatimaye alionekana mwanamke mtu mzima huyu alifika na kumkumbatia tabibu yule vilevile huku akiwa na furaha mno kupitiliza.

"Baba jamani hadi ukatusahau kama tupo jamani", Mwanamke huyo alisema huku akiwa na furaha.

"Nitaanza vipi kuwasahau nyinyi kama mpo, kwanza ni salama hapa?", Dokta Aesop aliuliza.

"Ni salama tu, za huko utokapo?"

"Huko ni kwema, wajukuu zangu wapo wapi naona nyumba ipo kimya mno"

"Gina yupo hosteli siku hizi anakaa hukohuko, Spora na wenzake ngoja utawaona muda si mrefu wametoka kidogo tu"

Dokta Aespo alisaidiana nao katika kushusha mizigo iliyopo humo garini, kisha kwa pamoja wakaingia ndani ya nyumba wakiwa na bashasha kuu kwa kukaa muda mrefu bila ya kuonana. Mama huyu alimheshimu sana tabibu kutokana na umri wake mkubwa na pia makubwa aliyowahi kuwafanyia kipindi cha nyuma.

Muda mchache baadaye aliweza kuwaona kina Spora ambao aliongea nao kwa muda mrefu, lakini hakutaka siku hiyo ipite pasipo kumuona Gina. Binti aliyempenda mno, na hata kumpatia jina ambalo analitumia. Wote kwa pamoja hapo ndipo walipotoka na kuelekea Upanga, kwenye makazi ya mjukuu wa hiyari wa daktari huyu.

______________

Yakijiri hayo, siku hii ikiwa na furaha kwa upande huo. Kwingine ikawa ni shubiri isiyofaa hata kuonjwa, hadi kufikia mtu aweze kuilaani ujio wake. Ndiyo wakati ambao Alice alijua dada yake amechukua uhamisho wa kumwondoa shule ya sekondari Benjamini na kumpeleka shule ya bweni Bagamoyo . Hakutarajia kabisa jambo kama hilo kuweza kutokea, alipoelezwa jambo hilo machozi yalianza kumlenga huku akimtazama dada yake kwa huzuni.

Moyoni aliumia mno kutenganishwa na Jamal, akiwa hajajua hata jinsi gani anavyompenda, aliona ni kama ametolewa kiungo muhimu kwenye mwili wake. Hatimaye machozi alishindwa kuyazuia na akajikuta akilia kwa uchungu, alijua nafasi ya kumpata Jamal ndiyo imepotea kwa jinsi alivyoonekana ni mwenye kutamaniwa na wengi. Ujio wake shuleni kule uliweza kumjulisha hilo, ingawa hawakuwa wakimsogelea mara kwa mara.

Moyoni alijikuta akilaani mno huo uamuzi wa dada yake aliyoufikia, kuamua jambo bila kumshirikisha hadi kufikia ameweza kuwafanya walimu wote wasaini kuonesha kuwa hadaiwi. Kibaya zaidi zilizopo hapo mbele yake ni fomu za kujiunga na shule ya Eagle(SHULE HII NI WAVULANA TU, IMETUMIKA KUONESHA NI YA MCHANGANYIKO. YOTE NI UBINIFU WA KIFASIHI TU)
Zikimuhitaji kutia sahihi tu kwani zilishajazwa hadi kuwekwa picha zake, ni jambo ambalo hakulitarajia kabisa kama litajiri. Alitakiwa aweke sahihi tu, ili ampatie dada yake ambaye angeziweka moja kwa moja kwenye bahasha ya kaki.

"Dada kwanini lakini? Yaani unanihamisha bila hata kunipa taarifa kama ulifuata uhamisho", Alice alilalalmika.

"Iam so sorry my young sis, sina budi kufanya hivi maana umeshindwa kabisa kutimiza kile nilichokwambia. Umeonesha ni jinsi ani hunisikilizi, sikupanga kukamilisha uhamisho huu mapema ila umenifanya niamue hivi", Doreen alisema.

"Dada nimefanya nini mimi hadi uamue haya?"

"Nilikwambia ukae mbali sana na Jamal kwa ajili ya usalama wake, ila hukutaka kunisikia. Kipi kilichokutoa ukaenda Tambaza siku ile ya mechi, hivi unadhani ukaribu uliyopo kutoka pale hadi kazini kwangu sitojua. Sikuwepo muda ule ila taarifa zote nimezipata. Alice husikii wewe na hunisikilizi"

"Dada siwezi kabisa kukaa mbali naye ndiyo maana nilikuja kumsalimia na kupiga stori naye"

"Si ulikubali kukaa mbali na yeye kwanini umeamua vile? Sasa ni hivi, kesho tunaenda mjini kununua vitu kwa ajili ya shule. Ukiniletea ujinga utajua kwanini nilipita jeshini, mabinti wa umri wenu nawatambua vizuri na kwa yule hatakiwi kupelekeshwa. Ndiyo maana nikakwambia stay away, ila ukajifanya unajua zaidi kuliko mimi"

"(Huku akilia) Dada please"


*ALICE ANAHITAJIKA KUWA MBALI NA JAMAL, JE ATAWEZA?

*DOREEN ANAMHAMISHA MDOGO WAKE KILAZIMA, JE NDIYO MWISHO WA TATIZO?







ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA

______SEHEMU YA KUMI NA SABA______


"Si ulikubali kukaa mbali na yeye kwanini umeamua vile? Sasa ni hivi, kesho tunaenda mjini kununua vitu kwa ajili ya shule. Ukiniletea ujinga utajua kwanini nilipita jeshini, mabinti wa umri wenu nawatambua vizuri na kwa yule hatakiwi kupelekeshwa. Ndiyo maana nikakwambia stay away, ila ukajifanya unajua zaidi kuliko mimi"

"(Huku akilia) Dada please"




____________TIRIRIKA NAYO


"Hukuweza kunisikiliza, sina mjadala Alice. Jiandae kwenda shule tu hakuna namna nyingine", Doreen alisema huku akimwonesha mdogo wake sehemu ya kuweka sahihi kwenye fomu.

Alice alibaki yu kalamu mkononi, asihindwe kufanya kile alichoagizwa. Machozi yakimtiririka mashavuni, akiwa haamini ndiyo mwanzo wa kukaa mbali na Jamal. Ni jambo lenye kuumiza, aliona ni mwenye kudhulumiwa haki yake ya msingi kwa kufanya hivyo. Kupenda kapenda, na kutenganishwa atenganishwe.

Badala ya kuweka sahihi alimtumbulia macho dada yake, ambaye ni mwenye kusubiri jambo hilo tu. Alidhani kuwa angeweza walau kubadili msimamo wake huo na kumwacha aendelee na masomo jijini, lakini katu hakufanya hivyo na hapo ndiyo alizidi kumwaga kimiminika kutoka machoni mwake. Huruma hakuiona toka kwa Afisa wa jeshi, ambaye ni mwenye kumpenda kupitiliza.
"Dada Doreen", Aliita kwa unyonge.

"nimekwambia saini hizo fomu Alice, sijakwambia uniite jina langu. Usinicheleweshe ujue"

"Dada please"

"Naona unataka nikubadilikie wewe, sasa subiri nirejee", Doreen alisema hayo huku akiwa amekunja uso haswa, aliinuka alipoketi na kuingia ndani.

Alice kusikia hayo, kwa haraka mno alitia saini fomu hizo sehemu zote alizohitajika. Alipomaliza aliziweka kwenye bahasha yake, muda mchache baadaye Doreen alirejea akiwa ameshika mkanda wa kijeshi mkononi huku uso wake ukiwa hauna mzaha. Alipofika aliitwaa bahasha kisha akazitoa fomu na kuzitazama, alipoona tayari ameshatia sahihi alishusha pumzi na kumtazama mdogo wake huku uso wake ukiwa hauna hasira kama ilivyokuwa hapo awali.

"Dada kwani hujawahi kupenda wewe hadi unifanyie hivi"

"Nimewahi na ninapenda hadi sasa, ila sikuwahi kuja kumtakia majanga kijana yeyote kisa moyo wangu. Nilikuonya wewe hukusikia hujui yule nimemjua vipi hadi nikaweza kuwa karibu naye, bila ya kumtibu nisingeweza kuwa jirani naye. Unakijua nilichomtibu wewe"

"Hata kama, ninampenda na sipo tayari kumkosa elewa hilo dada"

"Hivi unamtakia mema Jamal?"

"Ndiyo"

"Stay away from him, maliza masomo utafute kijana mwingine lakini si Jamal", Doreen alipoongea maneno hayo aliondoka mara moja akiwa na mkanda wake mkononi, alimwacha Alice bado ni mwenye kulia tu.

_________________

Siku hii pia ikawa ni ya faraja mno kwa Gina, aliweza kukutana na babu yake ambaye hakuonana naye kwa kipindi kirefu. Alijikuta akimganda mno tabibu huyo wa kigeni ambaye alifunga safari kutoka jijini Tanga, kuja tu kuwajulia hali. Hosteli napo hakukaa kwa jinsi alivyomkumbuka mzee huyo. Aliondoka kwa pamoja na familia kwenda nyumbani kwao ambapo walifurahi kwa pamoja, walijikuta wakisahau yote aliyoyapitia kwa kukutana na Dokta Aesop.

Yeye na wadogo zake kwa pamoja walimganda kwa kuongea naye, pamoja na kucheza naye kufurahia mambo mbalimbali. Mgiriki naye alifarijika mno, kwa kuona kama vile yupo na wajukuu wake wa damu na si wa hiyari. Alikaa nao hadi siku inaisha, usiku mnene ndiyo wote walienda kulala wakimwaga babu yao huyo.

Siku iliyofuata walishinda pamoja, kama vile hawakuwa wameongea naye kwa siku nzima. Dokta Aesop naye hakuona karaha kukaa nao, aliendelea na kubadilishana nao mawazo hadi pale ilipotimua majira ya machana ambapo alitaka kurejea Tanga ili aendelea na majukumu yake kwa siku inayofuata.

Kuaga kwake ikawa ni huzni kwa kina Gina, ila hawakuwa na jinsi zaidi ya kukubaliana na hali halisi. Walimsindikiza babu yao hadi alipokaribia kutoka nje ya mji, ndipo nao wakarejea kwa gari nyingine ya nyumbani kwao. Tabibu yule akaondoka akiwa na faraja mno, na wao pia ikawa ni hivyo ingawa walitamani haswa kukaa pamoja naye zaidi.

Majira ya jioni Gina naye hakuona umuhimu wa kuendelea kusalia nyumbani, alikusnaya vitu vidogo alivyokuja navyo kisha akaondoka kurejea hosteli. Alipelekwa kwa gari la hapo nyumbani kwao hadi Upanga, aliungana na marafiki zake ambao aliwakuta wakiwa wanabadilishana mawazo kwenye chumba chao.

___________________

Ujumbe mfupi wa maneno ulimfikia Jamal kutoka kwa binti ambaye alizoeana naye kutokana na ukaribu wake wa mkubwa wake. Hakutarajia kukutana na jambo kama hilo, lilimduwaza mno, kwani hapo awali walipokuwa wakiongea hakuwahi kugusiwa juu ya jambo ambalo alitaarifiwa. Hakujua undani wake na hata alipouliza sababu ya kutokea, napo hakuweza kupewa kiini cha kila kitu.

Majira haya ndipo alipoweza kujua kuwa Alice anahamishwa shule, siku inayofuta asubuhi alitakiwa kuripoti shuleni akiwa na vitu vyote muhimu kwa ajili ya maisha ya bweni. Muda huo anapewa taarifa ni tayari kila kitu kilishakamilika, na hakujua chanzo cha yote hayo kiasi cha kufichwa kila kitu juu ya kuhama kwa binti yule.

Ingawa hakutaka amuweke moyoni mwake, ukaribu wao aliona hakustahiki kushtukizwa hivyo alihitaji kuelezwa mapema mno. Jambo hilo lilifanya aongee na Doreen mwenyewe huenda angeweza kupata ufumbuzi wa kila kitu, huko napo aliambiwa jingine ambalo lilimshangaza zaidi juu ya Alice.

Doreen alitumia muda huo kumdanganya Jamal ili tu asijue sababu ya yeye kuweza kufanya hivyo, hata alipohitaji kumuaga rafiki yake napo kuliwekwa ugumu wa aina yake. Sababu ikiwa ni muda ambao wangeondoka kumpeleka shule, Jamal kusikia hayo wala hakutaka kuweka pingamizi jingine alikubaliana na hali ingawa hakuridhika na majibu ya dada mtu.
"Alice toka lini akakaribia kuingizwa kwenye makundi ya ajabu, anamhamisha kumuokoa toka lini mtu kama yule akafanywa hivyo. Si mtu mzima yule na akili zake", Jamal alibaki na kitendawili kisicho na jibu, ambacho alishindwa hata kumuuliza mhusika ampatie ufumbuzi kwa kuona namna hiyo ni kuharibu mambo kabisa.

Jambo hilo kama angelikuwa ni uongo basi ni mwanzo wa Alice kuja kumshukia dada yake, na hapo Doreen ataingia chuki na Jamal kwa kueleza lile ambalo alimwambia na kumwona hawezi kuweka siri. Kimya ndiyo alikipitisha kuweza kuepusha yote ambayo yangejitokeza kwa kutumia ulimi wake kudadisi.

______________

Asubuhi ya siku ya jumatatu ikisubiriwa Alice aweze kuondoka, upande mwingine kijana yule aliyemuua tabibu wa maradhi ya moyo alionekana akiinuka kitandani huku pumzi zake zikiwa zimeanza kukata. Aliinua huku akihemaa kwa nguvu na mwili ukimtetemeka. Napo kiuno kikashindwa kutoa ushirikiano kwa miguu na kuweza kumfanya asimame wima, hapo ndipo akajikuta akianguka baada ya kujaribu kusimama wima.

Mwili uliendelea kutetemeka, alijaribu kutambaa akiwa namna hiyo hadi akafika eneo ambalo lina kiti pamoja na meza yenye kioo cha kusimama wima mbele yake. Hapo ndipo alitumia mikono kwa nguvu akiijua na kuweza kukifikia kiti, kwa tabu alikaa huku akiendelea kuhema kwa nguvu akionesha anapumua kwa shida. Muda huohuo, alifungua saraka ya meza hiyo, alitoa kichupa kidogo cha dawa pamoja na bomba la sindano lililopo ndani ya pakiti.
Akiwa namna hiyo huku akionekana ni namna gani anaumia, aliitoa sindano kwenye pakiti kisha akaifunga kwenye bomba lake halafu akaichoma kwenye chupa ya dawa kwa juu. Alivuta dawa kwa kiasi chake kisha akachukua mpira uliyopo juu ya meza, alijifunga kwa shida halafu akaanza kujipiga mkononi hadi pale mishipa ilipojitokeza. Aliichoma sindano mahali hapo kwa taratibu, kisha akaisukuma dawa ndani hadi bomba likabaki tupu. Alipomaliza kufanya hivyo, alijikuta akikosa nguvu kabisa hadi kaanguka chini.

Giza lilitanda machoni mwake, hakuelewa chochote kilichoendelea hadi pale alipokuja kuhisi akipigwa shavuni mwake. Alikurupuka kwa upesi mno kisha akataka kuleta shambulizi kule alipohisi ndiyo upande ambao amesimama aliyempiga shavuni mwake.
"Hey Jus ni mimi hapa, hebu toa bomba la sindano hilo kwa haraka hapo mkononi litakutoboa ndani jinsi unavyokurupuka", Alikutana uso kwa uso na Mhindi mmoja ambaye ndiye alimwambia maneno hayo.

"Avi, uje vizuri muda mwingine si unajua wazi ninaishi kimachale halafu umenikuta nilikata jamaa yangu", Jus alisema.

"Jamaa yangu hii life ya kujidunga dawa kila siku asubuhi au jioni itaisha lini. Unajua upo kwenye mazingira ya tabu mno"

"Unafikiri nitaishije jamaa yangu, ndiyo matokeo ya kumfanyia kazi Fernando haya. Siwezi kupona kutokana na dawa hii na wala siwezi kukaa mbali na dawa, yaani leo miguu ilishaisha nguvu tayari nilijihisi nikianza kupooza. Kufika hapa mezani nimefika kwa mwendo wa nyoka, ningechelewa mikono nayo isingefanya kazi kabisa"

"Mtu wangu ila nilikupa onyo kabisa, kumfanyia kazi yule mzee ni nuksi sana. Mimi nimechoropoka, wewe ukaona pesa zake ni dili ona sasa unahangaika kila mahala ushaua madaktari wasiyoweza kukutibu, mpenzi wako umempoteza kwa yule Mafia. Na kila mahali utakapotia mguu basi jua mdogo wako anakufuata, kasoro hapa Tanzania tu ndiyo hajafika"

"Tusijipe uhakika kuwa Leo hajafika hapa, muhimu ni kuendelea kuwashikisha adabu madaktari. Hawajui ni namna gani watu huumia kwa kumtakia kuwa hawawezi kutibu ugonjwa fulani, bora umdanganye kwa kumpa maneno malaini. Nitaendelea kuwamaliza kila atakayetoa kauli mbovu. Ni muda wa kuwashikisha adabu hivi sasa"

"Ok sasa mpango wa leo upo vipi?"

"Leo ni kutulia kimya tu hadi polisi wasahau, ujue haujapita hata muda mrefu toka nimpoteze Dokta Yunus"

__________________


___Kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Heriety____

Mojawapo ya siku ambazo ziliandika kumbukumbuku muhimu kwenye maisha ya watu, basi hii ni mojawapo. Haitosahaulika siku hii ya mapumziko, ambapo wanafunzi wengi waliamua kuisherekea kwa pamoja kwenye hoteli maarufu iliyopo Bagamoyo. Kadhaa anasoma nao walialikwa, huku marafiki wa karibu wakiwemo pia.

Sherehe ilipangwa kufanyika majira ya usiku wa manane katika kuingia siku ya kuzaliwa kwa binti huyo, hivyo kila mmoja alijianda kutolala kwa ajili ya kuwa pamoja na wenzao. Majira ya jioni tayari eneo la tukio lilishawekwa kila kitu sawa, huku ndugu wa karibu wa binti huyo wakiwepo.

Upande ambao binti mwenye shughuli pamoja na wenzake walikaa pamoja, kulionekana napo kuandaliwa haswa na kila aliyefika aliingia huko ndani na kumpa salamu mwenzao ndiyo walitoka kwenda kujichanganya na wengine. Wavulana waliyoingia mahala hapo walijadiliwa na kuchambuliwa mmoja baada ya mwingine kila muda ambao walikuwa wakiwapa mgongo. Mabinti walijua haswa kuwasema wengine, huku wao wakiwa wamependeza mno hata ingekuwa ni ngumu kuweza kuwajua baadhi yao.

Ilipofika majira ya saa tatu usiku, kila mmoja ambaye alihitajika kufika kwa ajili ya shughuli hiyo, asilimia kubwa walionekana ila wachache tu ambao nao walidhihirika mmoja baada ya mwingine. kadri muda ulivyokuwa ukienda. Pamoja na hayo bado Heriety alionekana ni mwenye kukosa amani, ingawa wenzake walijitahidi mno kumfanya ajihisi na furaha. Hali ilipozidi ndipo baadhi yao walipoanza kuhisi mwenzao yupo tofauti na wengine, jambo hilo halikuvumilika Nasara alifanya udadisi upesi.
"Heryn mbona haupo sawa wakati muda ndiyo huo unakaribia nini tatizo?", Nasra aliuliza.

"Simwoni Jay hadi sasa hivi na aliniahidi kuwa atakuja", Alijibu.

"Relax, Jay si mtu wa kuvunja ahadi daima ni mwenye kutimiza kila anachokwambia usiwe na wasiwasi", Grace alisema.

"Mh! Hivi unafikiri atakuja hapa kwa usafiri gani, nyinyi acheni hizo mtu mwenyewe yule ni chokambaya si kuja kujitia aibu kwa simanzi zako Heryn", Gina aliongea kidharau.

"Gina please, kama utataka tukosane tena basi jaribu kumsema vibaya Jamal", Heriety alionesha kutopendezwa na maneno ya mwenzake.

"Okay sorry"

Subira yavuta heri, waliyosema hawa hawakukosea. Ikiwa imebaki saa moja tu sherehe iweze kuanza. Pazia la eneo ambalo mabinti wapo lilifunguliwa, wote kwa pamoja walipeleka macho huko. Ambapo walimshuhudia Jamal akiwa yu ndani ya mavazi ya kisasa na yenye kupendeza haswa, kiasi kwamba ambao hawakumzoea kumwona namna hiyo walibaki wakimshangaa haswa.

Alivaa fulana nyeupe ya mikono mirefu, chini akiwa na suruali ya 'jeans' yenye rangi nyeusi. Chini alivaa raba za kisasa zenye rangi nyeupe, mkono wa kushoto alivaa saa ya rangi ya fedha na juu kukiwa na mkufu wa dhahabu ambao aliuzungusha mkononi ingawa ulitosha kuvaliwa shingoni. Kidoleni alivaa pete yenye alama ya bawa la ndege, ambayo nayo ni rangi ya fedha huku mkono wa kulia ukiwa umeshikilia kofia nyeupe aina ya 'kapelo'. Mabinti walibaki kumkodolea macho, hata Gina mwenyewe akabaki kutoamini kama ni huyo aliyemzoea. Haswa baada ya kuona nywele zake ambazo zilichanwa kwa mtindo wenye kupendeza mno, tena zikionekana kama vile si za asili ya mzawa wa Tanzania.

"Woow! Jay!" Heriety alisema kwa sauti kubwa kisha kaachia yowe na kumkimbia akamkumbatia, wengine waliyosalia nao walifanya hivyo ikawa ni kumwachia huyu akumbatiane na huyu.

Gina ndiyo pekee alibaki alipoketi, hadi wenzake wanarudi yeye hakutoa hata salamu. Baada ya salamu ya kila mmoja, alianza kuwafurahisha kama ilivyo kawaida yake kisha akahitaji kuondoka hapo. Mabinti hao ilikuwa ngumu kumwachia pasipo kupiga naye picha, baada ya kutimiza kile wakitakacho alivaa kofia yake kichwani kisha akawaaga na kutoka ndnai humo.

"Gina halafu ile cheni aliyoivaa Jamal mkononi, kama niliwahi kuiona ukiwa nayo ndani kule hosteli", Nasra alisema na kumfanya Gina ashtuke.

"Hebu ngoja", Gina alisema huku akiinuka alipoketi.


*GINA ANAENDA KUHAKIKISHA, JE KWA CHUKI ZAKE ITAKUWAJE?

*JUS ANA TATIZO GANI HADI AWE VILE?

*JUS ALIFANYIWA NINI NA FERNDANDO?







ITAENDELEA!!!
 
RIWAYA: BANGUZI
NA: HASSAN O MAMBOSASA


_________SEHEMU YA KUMI NA NANE______


"Gina halafu ile cheni aliyoivaa Jamal mkononi, kama niliwahi kuiona ukiwa nayo ndani kule hosteli", Nasra alisema na kumfanya Gina ashtuke.

"Hebu ngoja", Gina alisema huku akiinuka alipoketi.



___________TIRIRIKA NAYO


Gina kusikia kauli hiyo, ukiongeza na jinsi alivyo na chuki kwa Jamal. Alijikuta akinyanyIka kwa kasi hata wenzake wakashangaa, alitoka nje kwa mwendo wa ajabu akimuwahi kijana ambaye ni chukizo la moyo wake. Alimwona akitembea kuelekea eneo la jirani na ufukwe akiwa mwenyewe tu huku, akiwa anatazama kioo cha simu ya mkononi ambayo aliishika.

Binti huyu hata bila ya kumsimamisha, aliwasha tochi ya simutamba na alikaza mwendo. Alipomsogelea aliutwaa mkono wa wa kushoto wa Jamal ambao ndiyo aliufunga mkufu ule. Kwa haraka aliuinua na kisha akaumulika kwa kurunzi ya simu, jambo hilo halikutarajiwa kabisa na mhusika na alibaki kumtazama tu asielewe kile alichomaanisha ni kipi hadi afikie namna hiyo. Tena kumfanyia kitu akionesha wazi ni mwenye kumdharau mno, kijana wa watu alibaki akimkodolea macho kwa mshngao asimwelewe.

"Hii cheni umeitoa wapi?", Alimuuliza kwa namna ya kishari.

"Kwani vipi? Mbona sikuelewi?",

"Hii cheni ni mali ya ukoo wa Aesop tu ambaye ni babu yangu, hii alikabidhiwa mama yangu tu"

"Basi kamuulize huyo anayeimiliki na si kuniuliza mimi, nafikiri sitokuwa na jibu la kukupa"

"Jamal unajua nakuuliza kistarabu tu, hii umeitoa wapi usitake tufike mbali"

"Na mimi nimekujibu kistarabu, sitaki kufika mbali na wewe na pia sihitaji kuweka mazungumzo ya muda mrefu na wewe kama ulivyotaka isiwe. Sina jibu jingine la kukupa, muulize huyo anayemiliki. Kuhusu mimi nilivyoipata sipo tayari kukwambia", Jibu la Jamal ambaye wala hakuonesha kukasirika usoni mwake, lilimfanya Gina aukamate mkono kwa nguvu mno.

Jamal alizidi kumshangaa, hakutumia nguvu yeyote ile kuutoa mkono wake zaidi ya kumtazama. Gina hakuishia hapo alianza kumtuhumu Jamal kwa tuhuma ambazo si zake, kuonekana na mkufu ule alianza kumsingizia kuhusika na wizi jambo ambalo hana uhakika nalo. Alipaza sauti akiendelea kuropoka, ila kwa kijana huyo wala hakutia neno lolote. Baadhi ya wanafunzi wanaosoma nao walijaa na kuwazunguka, huku kila mmoja akimtaka kijana ajibu ni wapi alipoutoa mkufu huo.

"Gina kwahiyo nishakuwa mwizi?", Aliuliza.

"Sihitaji maswali yako Jamal, naomba ujibu ni wapi umeitoa cheni ya mama yangu.

Mzozo ukiendelea wale mabinti waliyopo ndani wala hakuna hata mmoja aliyefika mahali hapo. Kutoka eneo walilopo ni mbali mno, wavulana kadhaa ndiyo waliweza kuwasili hapo wakiwa wameongozana na mabinti ambao waliyoalikwa ambao hawasomi shule ya Tambaza. Asilimia kubwa ni wageni kwao, na hao pia walishikilia bango kwa kitu ambacho wala hawakijui kimeanzia wapi.

Wakiendelea na mzozo muda huo waliwasili watu wawili mmoja akiwa amevaa suti ya kaunda ya mikono mifupi mwingine akiwa na mwili uliyojaa uku amevaa nguo nyeusi. Kitendo cha kuwaona watu hao moja kwa moja waliyopo mbele waliwapisha hadi wakasogea mbele ya kina Jamal. Gina bado hakuwa ameuachia mkono wake.

"Hey! Kuna nini?". Mwenye suti ya mikono mifupi aliuliza, mwenye mwili mkubwa alijaribu kusogea mbele ila yule mwenzake alimzuia. Gina alitumia muda huo kulalamika juu ya Jamal, huku akimtoa shutuma nyingine kutokana na vile anavyomjua kijana huyo.

"Binti una uhakika na unachokiongea?" Mwenye mwili mkubwa aliuliza kisha akawageuka waliyojikusanya hapo na kuwaambia, "nyinyi poteeni hapa mara moja, sihitaji kumwona hata moja"

Vijana hakuna aliyeleta ujuaji haswa baada ya kuona jitu la namna hiyo likiwapa mari, kila mmoja alishika njia yake wakasalia wanne tu hapo. Walipobaki hapo ndipo wale waliyoingia hapo mmojawapo akamwamuru Gina amwachie Jamal upesi, agizo hilo alibaki kushangaa lakini mara ya pili alipewa karipio na kutii mwenyewe.

"Sikia binti na usikilize sana, huyo unayemwona hapo na kumjua ni mwenye kuvaa nguo za kuchoka shuleni. Usikifikirie ana dhiki kupitilzia hadi afikie kuiba huo mkufu", Mwenye suti ya mikono kifupi aliongea.

"Paki potezea", Jamal alisema.

"Hapana dogo wacha nimpe ukweli, wewe dogo sikia na utusikilize kwa umakini mno. Huyu hana njaa ya kihivyo wala umasikini hadi aje aibe huo mkufu wa mama yako, pesa anapoishi ni sawa na maji ya kunywa tu. Unavyotuona hapa wote tupo hapa kumlinda yeye hadi hii sherehe inaisha, unajua tunalipwa kiasi gani ili awe sawa huyu", Paki alisema kwa ukali, alimfanya Gina abaki hana kauli. Binti akiwa hata kutia neno hajaweza alidakwa mkono na yule mwenye nguvu.

"Oze acheni basi majamaa, siyo namna hiyo"

"Dogo tulia leo tumwoneshe huyu unaishi maisha ya namna gani", Ozee aliposema hivyo alianza kumvuta Gina kwa nguvu akimpeleka eneo ambalo kuna magari yakiwa yameegeshwa.

Jamal aliambiwa afuate kwa nyuma naye akatii, watu wakiwa hawajui kinachoendelea binti alisogezwa hadi eneo la jirani ambapo kuna gari tatu za aina moja. Zote zikiwa range rover L322 za rangi nyeusi, hapo walikutana na vijana wengine waliyovaa nguo zinazofanana na za Oze. Gina alibaki akiwa ameingiwa na aibu ya mwaka, wala asijue cha kujitetea kutokana na hilo jambo lililomkuta. Kumsema mtu bila ya kuwa na uhakika yalimtokea, alibaki akimtazama Jamal kwa huruma ambaye wala hakuonekana ni mwenye huruma.

"Umeona hizi gari wewe, zimetolewa kwa ajili yake tu kuja kuletwa hapa", Oze alisema kwa hasira na kisha akamfuata Jamal, alimpekua mfukoni akaitoa simu ya bei mbaya ambayo aliisogeza usoni kwa Gina. Alimuuliza, "Una uwezo wa kununua simu kama hii?"

Binti alitingisha kichwa kuashiria hawezi, jambo hilo liliwafanya wale wote waliyopo hapo wasikitike mno. Walimwona ni msichana mjinga, kwani thamani ya kile anachodai kaibiwa hakifikii hata mara ya ishirini ya gharama ya simu hiyo. Jamal ndiyo kabisa alitazama chini akiwa na masikitiko makuu kwani hayo yote kayataka mwenyewe, kwa hatua waliyofikia walinzi hao hakuwa na uwezo wa kuingilia na ilionesha ni namna gani hao watu wapya ambao ndiyo anaonekana nao siku hiyo anawahofia mno.

"Sasa wewe kwa akili zako unafikiri alikosa kipi cha kununua hadi aje aibe cheni hiyo. Sikia tungeweza kukufanya kitu mbaya sana ila una bahati huyu jamaa uliyemkera hajuagi kulipa kisasi kwa ulichomfanyia. Kama ndiyo siku zote mlikuwa mnayasema maneno yale mkiwa naye shuleni, jua si wakati mwingine wa kuyaropoka. Potea nakwambia!", Oze alisema kwa kufoka na hasira juu, alipotoa amri ya kumfukuza Gina alijikuta akishtuka na kuondoka kwa kasi.

"Gina", Jamal alimwita na kumfanya asimame na kisha akamtazama usoni mwake. Aliamua kumweleza, "Sijawahi kuchukia mtu ndani ya dunia hii na wala sikuwa na natarajia nichukie mtu. Ila tambua wewe ndiyo wa kwanza kukuchukia, kuanzia muda huu hata nikiitazama sura yako najihisi hasira. Nenda na tutakutana huko kwenye sherehe, ila tambua kuanzia hii leo nakuchukia sana"

Gina aliondoa kichwa chini akiwa na aibu kuu, muda huo yakiendelea hayo baadhi ya watu wambea walishafika maeneo hayo na kujibana mahali wakiangalia kile kinachoendelea. Baada ya kutokomea Jamal alijishika kifuani na kuanza kuhema kwa nguvu, jambo lilifanya watu wenye sare kama za Oze takribnani wanne wamkimbilie. Walimshikilia vizuri huku Oze na Paki wakimtazama usoni kwa umakini, Jamal alionekana kianza kuhema kwa nguvu mno.

"Dogo vipi kweli utaweza kukesha kwenye sherehe hii au tuamshe popo muda huu huu. Kumbuka likikumba janga ni kesi kwetu", Paki alisema.

"Nitaweza kuendelea, nipeni dawa tu nijiweke sawa naingia huko muda si mrefu si unaona majira yamekaribia haya", Jamal alisema, mmojawapo alikimbia ndani ya gari na kurejea akiwa na kichupa kidogo cha dawa, alikifungua na kumpatia kidonge kimoja ambacho alikimeza bila ya maji.

Jamal aliganda akiwa amenamisha kwa dakika takribani moja, alipoinua alionekana ni mwenye tabasamu na nguvu ikarejea kwa mara nyingine. Aliomba aachiliwe anaweza kusimama mwenyewe, nao walitii mari na kumuweka ambapo alianza kumtazama mmoja baada ya mwingine.

"Nyie majamaa pale mngemtisha kumpiga kibao tu angejikolea haphapo, mmemuwekea uso wa mbuzi wa kumtoa mtu roho", Jamal alisema huku akicheka.

"(Akicheka) Dogo ushaanza zako, wahi huko party yenu inaanza muda si mrefu", Ozee alimwambia Jamal, ambaye aliagana nao kisha akarejea kule alipokuwa hapo mwanzoni.


_________________

Gina alifika kwa wenzake ambapo ndiyo walikuwa wakijiandaa kusogea eneo la tukio, aliungana ambapo wachache walianza kudadisi juu ya kile kinachomsibu lakini hakuongea lolote zaidi ya kuwaambia ni ya kwake. Alijivika uso wenye furaha lakini moyoni alibaki na jitimai kubwa kwa yaliyomkuta. Hakutarajia kama kuna siku atakuja kuaibika, na hiyo ikawa imebaki ni jeraha kubwa ndani ya moyo wake.

Furaha ambayo ilikuwepo tangu mwanzo wa sherehe, aliamua kuiweka ya maigizo na kujiunga na wenzake kwenye kupiga umbea hadi saa sita kasoro walikuwa tayari wapo eneo la tukio.

Ikiwa imebaki dakika moja kutimia kwa siku mpya, kwa pamoja walinyamaza kimya wakitazama saa iliyoletwa mahali hapo ikiwa iinonesha jinsi sekunde za dakika hiyo zikizidi kuyoyoma. Hatimaye saa sita kamili ikatimu na hapo wote kwa pamoja wakaanza kumwimbia mwenzao wakimtakia siku njema ya kuzaliwa, makofi yalinogesha wimbo huo huku wakisubiri kwa hamu aweza kuzima mishumaa.

Tendo hilo lilipotimia, ikafuata hatua ya kulishana keki na hapo ndipo Gina alipoumia kwa mara nyingine. Pamoja na kuwa ni rafiki wa karibu wa Heriety, ila wa kwanza kulishwa alikuwa ni Jamal ambaye alipewa sifa kedekede kipindi anaitwa. Wa pili ndiyo akaja yeye ila alihitaji mno apewe kipaumbele kwenye suala hilo, kutokana na ukaribu aliyo nao kwa mwenzake. Kidonda kingine kikawa ni hiko, alivumilia na kuivaa furaha lakini bado machungu hakuwa ameyasahau.

_________________

Sherehe ikiendelea simu ilipigwa kwa Shehoza ambaye majira hayo Yupo pamoja na Doreen wakiburudika nyumbani kwa Afisa huyo wa kijeshi aliyebaki mpweke baada ya kuondoka Alice kwenda bwenini. Muda huo wakiwa na furaha ghafla Shehoza alibadilika sura kwa ghafla, aliweka mikono shavuni akiwa anatazamwa tu na mpenzi jinsi alivyogeuka ghafla namna hiyo.

"Mpenzi vipi kuna nini?', Doreen aliuliza.

"Unaukumbuka ule mkufu ambao Jamal unapenda kumtania kumwambia ni wa kike?", Shehoza alirudisha swali na yeye

"Naukumbuka vyema ule, kwani imekuwaje?"

"Kuna kibinti huko kimemwona nao kimemtuhumu ni wa mama yake na kauiba"

"Huyo mtoto ana wazimu nini, Jamal ana nini cha kukosa mpaka afikie aibe ile cheni si kapewa yeye"

"Nasikia huko kina Paki wamemtia jambajamba tena Jamal aliishiwa nguvu alipomeza dawa akawa sawa. kacheka sana kawaambia wangezidisha mkwara kidogo angejikojolea"

"(Akicheka) Unajua mpwa wako naye muda mwingine simwelewi kabisa, muda huohuo kalipotezea hilo suala sijui ana moyo wa aina gani. Ila inabidi wawe makini naye sasa"

"Vijana wapo kazini wale, wakizembea tu wanajua kitakachowakuta ni kipi. Wala usihofu kuhusu hilo"

"Haya tuendelea na yetu", Doreen alisema huku akibusu midomo ya Shehoza.

___________________

Majira haya upande wa Bagamoyo, Jamal alikuwa ameshika kipaza sauti baada ya kuombwa kufanya hivyo. Bwana vituko kama kawaida yake hakutaka kubadili ada aliyo nayo. Alianza kuwavunja watu mbavu, kwa maneno tu huku akiwa hachezeshi mwili wake kuupeleka upande wowote ule. Vicheko vilijaa mahala hapo, kutokana na kipawa chake kilivyo.

Ilifika mahali akamwita Heriety mbele, hapo alianza kumfanyia vituko na kumfanya binti wa watu ashindwe hata kusimama kutokana na kuzidiwa na kucheka. Wengine ndiyo hawakuwa na afadhali, kwa jinsi kijana alivyojua kuitendea haki . Wakati akiyafanya yote hayo, ni Gina tu ndiyo hakuwa akicheka zaidi ya kumtazama huku akiwa amekunja sura mno.

Chuki ndiyo aliizidisha maradufu, akakumbuka yale ambayo yalimsibu muda uliyopita. Msababishaji akiwa ni huyohuyo, anageanza wapi kucheka wakati mdudu aitwae hasira anamtambaa kwenye moyo wake. Alitamani hata aache kuongea hayo maneno yake na kuondoka, pamoja na kupewa mikwara bado haikuweza kubadilia moyo wake. Ndiyo kwanza wametia moto mafuta ya petroli wakidhani watauzima, binti huyu ni mwenye moyo wa ajabu mno. Maya ilipozidi alijikuta akikunja uso zaidi huku akimtazama kijana yule, ambaye kamtamkia wazi hata yeye mwenye anamchukia baada ya kumvunjia heshima kwa kumpa tuhuma ambazo hahusiki nazo.

"Jamal naapa kwa baba yangu aliyepo kaburini, utajuta kunifahamu mimi Gina", Alijisemea moyo huku akiendelea kumkodolea macho, tena muda huu yalianza kuweka wekundu kuonesha ni namna gani kazidiwa na hasira.

Wenzake wakicheka, aliona ni karaha mno sauti zao. Alitamani hata nao wapatwe na hali kama yake, ndiyo hivyo halikuwezekana. Hakika jinsia ya kike ikijua kuchukia, basi hilo ni balaa kubwa lisilo na kipimo. Jinsi anavyopewa kipaumbele na mhusika mwenye siku yake, na namna ambavyo watu wanavyokongwa nyoyo na vituko vyake ndiyo kulizidi kumfanya aungue nafsini mwake.


*JAMAL NDANI YA CHUKI, GINA CHUKINI MARADUFU. JE CHUKI HIZI ITAACHA MTU SALAMA?

*SHEHOZA ANAJUA KITAKACHOWAPATA WALINZI NI KIPI IKIWA WATAZEMBEA, KAJUAJE?






ITAENDELEA!!!
 
Back
Top Bottom