Daniel Mjema, Moshi
HATIMAYE Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), imemburuza mahakamani mkurugenzi mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka mjini Moshi (MUWSA), Anthony Kasonta kwa tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka.
Kasonta alifikishwa kortini jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Kilimanjaro, Gabriel Shayo akiwa na mshtakiwa mwenzake, John Ndetiko ambaye wakati makosa hayo yakitendeka alikuwa Kaimu Meneja wa Fedha na Utawala wa MUWSA.
Waendesha mashtaka wa Takukuru, Maghela Ndimbo na Melkizedeck Gunda walidai mahakamani kuwa vigogo hao wawili walitumia vibaya madaraka yao kwa kuidhinisha malipo ya safari hewa za mafunzo kwa watumishi watano.
Ilidaiwa kuwa Julai 3, 2007 Kasonta na Ndetiko wakiwa waajiriwa wa MUWSA kwa makusudi waliidhinisha malipo ya safari hewa za mafunzo kwenda Dar es Salaam kwa watumishi Witness Shoo na Rehema Nelson waliolipwa Sh310,000 kila mmoja.
Katika shtaka la pili, inadaiwa kuwa Julai 4 mwaka huo huo, washtakiwa hao waliidhinisha malipo kwa safari hewa za mafunzo kwenda Dodoma kwa watumishi Samwel Millu, Siael Lyamuya waliolipwa Sh290,000 kila mmoja.
Mtumishi mwingine aliyetajwa katika hati ya mashtaka, Anna Maurice aliidhinishiwa malipo ya sh292,000 kwa ziara hiyo hewa ya mafunzo kwenda Dodoma .
Waendesha mashtaka hao wa Takukuru walidai kuwa kitendo kilichofanywa na watumishi hao wa MUWSA kilikuwa ni matumizi mabaya ya madaraka ambalo ni kosa chini ya sheria namba 11 ya kuzuia na kupambana na rushwa ya mwaka 2007.
Washtakiwa hao wanaotetewa na wakili wa kujitegemea wa mjini Moshi, Godwin Sandi walikanusha mashtaka hayo na kuachiwa kwa dhamana ya maandishi ya Sh1.5 milioni kila mmoja na kuwa na wadhamini wawili wenye mali isiyohamishika.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Machi 15 mwaka huu baada ya waendesha mashtaka wa Takukuru kuieleza Mahakama kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika.
Mwaka 2008, gazeti hili lilifichua taarifa za Takukuru kuwachunguza maofisa kadhaa wa MUWSA kuhusiana na matumizi mabaya ya fedha na madaraka, lakini mamlaka hiyo ikakanusha kwa nguvu kuwapo kwa tuhuma hizo.
Licha ya Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Kilimanjaro, Alexander Budigilla kuthibitisha maofisa hao kuhojiwa, bado uongozi wa MUWSA ulienda mbali na kununua kurasa katika magazeti mawili na kukanusha tuhuma hizo.
Budigilla alipohojiwa na Mwananchi jana alisema kufunguliwa kwa kesi hiyo ni mwanzo tu na kwamba zipo kesi nyingi nzito zaidi zinazotarajiwa kufunguliwa baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kuzitolea kibali.
"Tuna majalada mengine ya kesi kubwa dhidi ya maofisa wa MUWSA ambayo tunasubiri kibali cha DPP ili ziende mahakamaniâ¦huu ni mwanzo tu, tumpe muda DPP aweze kuyapitia majalada yote,"alisema Budigilla.
SOURCE:
http://www.mwananchi.co.tz/newsrids.asp?id=17893