*NYUMA YAKO (MSIMU WA NNE) -- 03*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Basi Marshall akiwa hapo akasikia mtu akitapika. Akajikuta akipata hamu ya kujua, akasonga kutazama chumba kinachofuata, huko akamkuta Jack akiwa anatapikia kwenye mfuko. Tumbo lilimvuruga.
Kajasho chembamba kalikuwa kanamchuruza.
Marshall akiwa hapo anamtazama mwenzake, kabla hata hawajazungumza kitu, akastaajabu mwanga unammulika. Alipogeuza shingo yake kutazama, akaona boti kubwa umbali wa kama kilomita moja toka walipo.
Mara kidogo sauti toka kwenye kipaza sauti ikapaza kwanguvu,
"Mpo kwenye mpaka wa maji wa Morocco. Ninyi ni wakina nani?? Jitambulisheni na mtuonyeshe nyaraka zenu upesi!!"
Marshall akang'ata lips yake ya chini kisha akasema, "oh God! Mbona mapema hivi?"
ENDELEA
Marshall aliwaza cha kufanya na punde akaona ni vema akawataarifu wenzake kuhusu tukio hilo, lakini kabla hajafanya vivyo akabaini wenzake tayari wameshatoka ndani kutazama.
Watu hao walikuwa ni watatu kwa idadi: Kelly, Danielle na Jack. Wote walikuwa wametoa macho wakijaribu kuelewa kuna nini kinachoendelea. Kidogo Kelly akasafisha koo lake kama ishara alafu akasema,
“Acha niongee nao. I can handle this.”
“Sure?” Marshall akapata shaka kidogo. Alimtazama Kelly anavyosonga karibu naye.
“Yah! Si mara ya kwanza nafanya hivi,” akasema Kelly kwa kujiamini. Akasonga karibu kabisa na kushika kingo ya boti akitazama wale wageni wao. Muda si mrefu mwanamke huyo akakutana na hao wageni kwenye boti yao, boti ya serikali.
Ilikuwa ni boti kubwa yenye maafisa kama kumi na tano kwa idadi. Wawili walikuwa ni manahodha, wengine watatu wakiwa ni watu wanaohusika na ufundi na wengineo waliobaki wakiwa ni kama walinzi. Hao ndo walikuwa wamebebelea bunduki na wapo tenge kwa lolote litakalotokea!
Basi Kelly akiwa anatembea kwa madaha, akasonga mpaka kwa ‘captain’ wa boti na kumweleza kidogo kumhusu. Mwanamke huyo alijitambulisha kwa kusema kuwa yeye ni moja wa washiriki wa bwana Abdulaziz, mwana wa mfalme.
“Bila shaka mimi si mgeni machoni mwako,” alisema Kelly akimtazama captain kwa kurembua. Captain akatabasamu kidogo, akamtazama mwanamke huyo na kumwambia, “ngoja!” kisha mwanaume huyo akaenda zake ndani kufanya mawasiliano.
Kelly hakuwa na hofu. Haikuwa mara yake ya kwanza kukumbana na kadhia kama hiyo. Akiwa amerelax akangoja kwa kama dakika tatu kabla ya captain hajaja na kumwambia,
“Sijapata uhakiki wake.”
“Una maana gani hujapata uhakikiki wake?” Kelly akauliza upesi.
“Simu haijapokelewa kwahiyo hatuwezi kuwaruhusu,” akasema captain kisha akatoa ishara kwa watu wake wa usalama, wale waliobebelea bunduki, punde mabwana hao wakafuata wakina Marshall na kuwaweka chini ya ulinzi.
Wakawaamuru waende kwenye boti yao, nao walengwa wakatii.
“Hamuwezi kutufanyia hivi!” akasema Kelly akikunja sura. “Punde Abdulaziz atakapojua mlichofanya mtakuwa mahali pabaya.”
Hakuna aliyemsikiliza, wakasweka ndani ya chumba fulani na kufungiwa humo kwa komeo. Ndani kulikuwa ni kiza. Boti likawashwa na kutimka kuendelea na doria katika usiku huo.
“Sasa tunafanyaje?” akauliza Marshall. Alikuwa haonekani bali kusikika tu. Kwa mbali sauti ya mawimbi ilikuwa inasikika yakiwa yanakatwa na ncha ya boti.
“Tungoje kwanza,” akasema Kelly. “Nadhani hatuna haja ya kutumia nguvu hapa.”
“Tutangoja mpaka muda gani?” Danielle akauliza. “Endapo jua likichomoza itakuwa ni hatari zaidi kwetu.”
“Jua halitachomoza,” akasema Kelly kwa kujiamini. “Muda si mrefu Abdulaziz atapiga.”
“Lakini ulisema wewe haumfanyii kazi bwana Abdulaziz,” Jack akatia neno.
“Ndio, lakini bwana Abdulaziz hatambui hilo,” akasema Kelly. Basi wakangoja humo kwenye boti kwa kama robo saa, kimya. Wakaendelea kuvuta subra.
Ilipopita dakika ishirini na tano, sasa hata Kelly na yeye akaanza kupata wasiwasi na ukimya ule, akanyanyuka aende kugonga mlango asikizwe. Kabla hajafika, mara boti ikayumba na kumdondosha chini! Puh!
Boti ikayumba na kuyumba kwa muda kidogo kiasi kwamba akashindwa kabisa kusimama. Bahari haikuwa shwari.
Hawakukaa sana mara maji yakaanza kuzama humo ndani! Boti ilikuwa inayumba sana kwa sasa! Mawimbi yalikuwa makubwa na upepo nao ulichachamaa.
Boti ilipelekwa kushoto na kulia, juu na chini! Marshall pamoja na wenzake wakawa wanagongana na kuvamiana wakitupwa huku na kule.
“Inabidi tufanye jambo!” akasema Marshall. “La sivyo tutakufa humu!”
Ni wazi moja ya madirisha yaliyokuwa kwa chini humo chumbani yalikuwa yamepasuka. Maji yalikuwa yanazama ndani kila mara boti unavyoyumba!
Kidogokidogo yalikuwa yanaongezeka!
Punde kidogo mara king’ora kikaanza kulia. Boti ilikuwa imefungiwa mtambo wa kutambua hitilafu ya kuzamia kwa maji chomboni. Basi upesi wale mabwana wanaohusika na ufundi wakaanza kufanya namna kukabiliana na hatari hiyo.
Kidogo ndipo wakabaini tatizo. Ni chumba cha chini!
Basi upesi wakafungua mlango na kuanza kufanya marekebisho! Lakini haikuwa rahisi hata kidogo. Bado boti ilikuwa inayumbayumba kupelekeshwa na mawimbi. Utulivu ulikuwa ni mgumu kupatikana.
Kuna muda bwana mmoja akajikuta akitupwa na kwenda kujikita ukutani, akapoteza fahamu papo hapo! Mwingine naye almanusura kudondoka kama isingalikuwa kujishikiza na nguzo.
“Mmekamilisha?” akauliza captain. Akiwa amekaa karibu na usukani alikuwa amejishikza asiyumbe. Kulikuwa na sauti kubwa ya king’ora kwenye ‘system’ kumjulisha kwamba boti halipo salama.
Alama ya tone la maji lenye rangi nyekundu ilikuwa inamwekamweka chini ya usukani wake.
“Bado, hali si nzuri kabisa!” sauti ikamjibu toka kwenye ‘radio call’ ya boti. “hatupati utulivu wa kufanya kazi kabisa!”
“Fanyeni upesi!” captain akafoka. “Hatuna muda mrefu hapa. Mpaka chombo kiz--” wimbi kubwa likachapa kioo cha mbele kabisa ya boti na kufanya chombo hicho kisimame karibia na kubinukia huko nyuma!
Wimbi lilipopita, boti likarudi chini kwanguvu! Maji yakaruka juu na kuifunika boti hiyo kana kwamba mvua! Ni kheri boti ilisimama japo kwa mrama.
Upande wa kushoto wa uso wa Captain ulikuwa unavuja damu. Alikuwa amechoka. Bega lake pia la kulia lilikuwa linamvuta kwa maumivu makali. Akashika chombo cha mawasiliano na kuuliza,
“Mmekamilisha? --- mmekamilisha?”
Akatambua kifaa hicho hakikuwa kinafanya kazi tena. Maji yalikuwa yanachuruza toka ndani yake. Akatupia kifaa hicho chini na kujaribu kusonga aende kuangalia kinachoendelea.
Akamtaka mwenzake ashikilie usukani kurudisha chombo nchi kavu mara moja ingali yeye akitazama usalama.
Akafika kule chumbani, japo kwa shida, akakuta chumba kikiwa kimejawa na maji mengi! Akamulika na kurunzi asione mtu yoyote humo.
Akaita. Kimya.
Kidogo akatambua kuwa kuna sauti inatokea upande mwingine. Alipoenda kutazama, akakuta watu wake wakiwa chini, wanne kwa idadi! Na upande wa kushoto wa kile chumba kilichokuwa kimejaa maji, pia kulikuwa kunapenyeza maji kwa vingi vilevile!
Hajakaa muda mrefu pia akatambua kuwa boti haikuwa inakwenda kama vile alivyomuachia maagizo captain mwenzake! Kwa muda kidogo akashindwa kujua cha kufanya.
Tih!!! maji yakachapa tena boti! Mara hii yalipiga kwanguvu sana kiasi kwamba captain hakuweza kumudu kujizuia. Alitupiwa ukutani na akapoteza fahamu mara moja!
“Boti inazama! Narudia, boti inazama!” ilikuwa sauti ya captain aliyeachwa kwenye usukani. Hakuwa na kingine cha kufanya kuokoa chombo chao. Akiwa anaongozana na wenzake kadhaa wakanyofoa maboya na kujivika kisha wakatumbukia ndani ya maji.
Hata hawakuwakumbuka wenzao.
Walipookoa nafsi zao ndipo wakaanza kuulizana juu ya wengine.
“Watakuwa wamekufa!” mmoja akasema. Alikuwa ameshikilia boya na huku pia ameshika bunduki, bunduki iliyojawa na kushiba maji.
“Vipi tukaenda kuwatazama?” mmoja akauliza, lakini uso wake haukuwa unaonyesha kama kweli anamaanisha alichosema.
“Tutaendaje kwenye boti inayozama?” akauliza mwingine. Kabla ya yule aliyetoa wazo hajaongezea neno, akahisi jambo. Alibinyabinya boya lake kisha akawatazama wenzake kwa macho ya mshangao na kusema,
“Nahisi boya langu linapungua upepo!”
Wenzake nao walipotazama yao, wakagundua wote walikuwa kwenye mkondo mmoja. Hawajakaa sawa, wakafunikwa na wimbi kubwa lenye urefu wa nchi zisizopungua kumi na tano!
Bwaaaah!!
**
“Umefanya vema!” akasema Kelly akimgusa bega Marshall. Mwanamke huyo alikuwa ametoka kuchungulia kwenye vioo vya hadubini. “Hawataweza kudumu baharini. Watakufa kama wenzao!”
Marshall akamtazama Kelly, mwanamke huyo hakukaa nao sana akaelekea ndani ya chumba. “Sasa tunaweza kuendelea na safari yetu,” ikawa ndo kauli ya mwisho ya Kelly kabla hajaufunga mlango.
Kidogo kukawa kimya kwa mazungumzo. Danielle alimtazama Marshall kisha akamuuliza, “Una uhakika huyu ni mtu wa kumuamini?”
Wakati akiwa anauliza vivyo alikuwa anatazama mlango alimozama mwanamke huyo.
“Hatuna budi kuwa naye,” akasema Marshall. “Yeye ndo njia pekee ya kumpata Marietta, na hatimaye Raisi.”
Marshall aliposema hivyo akawaacha wenzake hapo na kwenda kule alimo Kelly. Alifungua mlango na kuangaza, akamkuta mwanamke huyo anatapikia kwenye mfuko.
“Nawe umeanza kutapika?” Marshall akauliza. “Nilidhani ni mzoefu!”
Kelly akauweka mfuko kando kisha akajifuta mdomo wake kwa mgongo wa kiganja. Akamtazama Marshall kisha akatazama chini na kuvuta hewa ndefu kwa pua yake nyembamba.
“Ni nini unataka Marshall?”
“Sikaribishwi?”
Marshall akasonga karibu na mwanamke huyo. Akamtazama kidogo na kumuuliza, “Kwanini Abdulaziz alitoa amri uuawe?”
Kelly akabinua mdomo wake. Akajifuta tena na mgongo wa kiganja chake na kutulia.
“Kuna tatizo lolote? Tujuze. Unajua tupo pamoja kwenye hili.”
Mara boti ikayumba kwanguvu! Ni kheri walikuwa wamejishikiza. Angalu boti ilivyotuliatulia, Kelly akamtazama Marshall na kumwambia kwa sauti ya chini,
“Sijui ni nini kinatokea. Huenda Abdulaziz akawa ameshamshtukia Marietta.”
“Kivipi? - ulisema yeye hajui kama unamtumikia?”
“Sijui, Marshall! Nami nipo njia panda kama wewe. Tutakapofika nchi kavu nitawasiliana na Marietta nipate kujua.”
Kukawa kimya.
“ … Pengine Captain alimwambia tupo zaidi ya idadi,” Kelly akaongezea maneno. Mara hii Marshall akawa kimya kumtazama Kelly kwa umakini. Mwanamke huyo alikuwa anaonekana hayuko sawa. Uso wake ulikuwa kielelezo.
“Kelly, kuna shida yoyote?”
Kimya.
“Kelly, unaweza uka-share nasi. Tupo kwenye boti moja.”
Kelly akamtazama Marshall usoni. Macho yake yalikuwa yamelegea kiasi. Mdomo wake ulikuwa wazi akihema.
“Nataka tu kuwa mwenyewe, Marshall. Hilo tu.”
Marshall akanyanyuka.
“Tutaonana baadae!”
**
Saa kumi na moja asubuhi …
“Nasemaje! --” Abdulaziz akafoka. “Sitaki kusikia mtu yeyote amegusa nchi kavutokea huko baharini isipokuwa kwa bandari pekee!” mate yalikuwa yanamruka toka kinywani. Macho yalikuwa yamemtoka.
“Ongezeni walinz bandarini na pwani yote!” aliposema hayo akapachika simu mezani. Akang’ata meno yake na kunyanyua tena simu kumpigia Jamal.
“Bado!!” alifoka haswa. “Jamal, Jamal, kama hao watu hawatapatikana kwa siku ya leo. Utafute mahali pa kujifichia. La sivyo ni----” simu ikakata -- tiii-tiiii!
“Pumbavu!” akatusi. Akaweka namba tena na kupiga. Namna alivyokuwa anabonyeza namba hizo ni kana kwamba anataka kutoboa simu.
Simu ikaita pasipo kupokelewa. Akatusi na kutusi kupita kiasi.
**
“Jamal, anachosema Mahmoud kina ukwel wowote?”
Kwenye sebule hii ya kifahari walikuwapo watu wanne: wa kwanza alikuwa ni Aziz, crown prince, pili bwana Mahmoud, tatu Jamal na nne mpambe wa Aziz, bwana Ramadan.
Aziz, mwana wa mfalme anayeandaliwa kupokea madaraka, alikuwa amevalia kanzu yenye darizi za dhahabu. Mkono wake wa kushoto ulikuwa na saa aghali mno. Miguuni alikuwa amevaa sendozi zilizosanifiwa kwa ngozi ya simba.
Kitendo cha bwana Mahmoud kuwapo hapa, kulikuwa ni kumaanisha kuwa mpango wa ule wa bwana Aziz waliokuwa wameuadhimia ulikuwa umetimia.
Mahmoud alifanikiwa kuonana na bwana Ramadan na kumpa kila ‘sumu’. naye bwana Ramadan, akitaka kuonekana mtu mtenda kazi, akafikisha habari upesi kwa ulimi wake. Sasa alikuwa hapa akitazama kwa macho yake makubwa namna mambo yanavyoenda.
“Ni kweli kabisa,” akasema Jamal. “Abdulaziz anataka madaraka yako kwa njia yoyote ile. Na hapa tuongeapo, anamshikilia bwana yule wa Marekani akilenga kumtumia kama ushawishi kwenye kikao cha hadhara.”
Basi bwana Aziz kusikia hayo, akaamuru Abdulaziz akamatwe mara moja na aletwe mbele yake upesi!
**