Nyuma yako (Riwaya ya S. Mollel)

Nyuma yako (Riwaya ya S. Mollel)

Mkuu Stevemoleli habari za siku bwana! ,, nilikuwa mabali sana ila nashukuru nipo hapa karibu sasa hongera sana Kwa kazi nzuri na pia ahsante Kwa kiburudisho hiki!!
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 09 & 10*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Kwasababu mazungumzo yao ni faragha, akatoka ndani ya chumba cha daktari apate kuwa huru.

“Vipi Harold?”

“Tumezingirwa!” Harold akabwatuka. “Tumezungukwa nje ya jengo na watu waliobebelea silaha!”

“Serious?”

“Ndio! Wamekuja muda si mrefu. Ni sita kwa idadi!”

“Nakuja! Nakuja!”

Inspekta akaweka simu mfukoni kisha akanza kukimbia kama mwehu akielekea nje ya hospitali.

ENDELEA

Alijipaki kwenye gari yake nga kuendesha kwa kasi sana. Lakini kama haitoshi akawataarifu na polisi wengine waliopo karibu juu ya swala la wenzake kuvamiwa wakiwa wanatekeleza kazi.

Akakimbia haswa. Ilimchukua kama dakika ishirini tu kufika eneo la tukio lakini ajabu bado alikuwa amekawia. Alikuta wadhalimu wameshatoweka na watu wake wapo hoi sana.

Harold alikuwa ametobolewa na risasi mbili, na kwa upande wa Gerrard yeye alikuwa amekula risasi si chini ya tano! Wote walikuwa hoi. Haikupita muda mrefu, Gerrard akafa ikiwa ni muda mfupi kabla ya gari la wagonjwa halijafika.

Mwili wa Gerrard ulichukuliwa kwa ajili ya mahifadhi, na Harold akawahishwa hospitali baada ya kupata huduma ya kwanza upesi.

Inspekta James alipekua makazi yale ya bwana Willy na kubaini matundu mengi ya risasi ukutani, mlangoni na madirisha ya kioo yakiwa yamevunjwavunjwa.

Maganda ya risasi yalikuwa yametapakaa karibia kila eneo, na pia damu baadhi ya maeneo na maeneo.

Alibaini pia makabati na madroo yalikuwa yamefunguliwa, kupekuliwa na kuachwa wazi. Akiwa amevalia glovu, alitazama kitu kimoja baada ya kingine.

Baada ya muda mfupi wakaja watu wa ‘Forensic’ - watu wanaohusika kukusanya vielelezo vya kipelelezi, wakaanza kupekua na kukusanya kila kilicho cha muhimu.

Kitu kikubwa ambao mabwana hao walikipata ilikuwa mabaki ya damu. Walitunza sampuli za damu na kuzipeleka maabara kwa ajili ya upembuzi zaidi.

Mpaka yafikia majira ya jioni, tayari inspekta James alikuwa amempoteza Willy na Gerrard ikiwa yeye hajapata kitu! Siku mbaya kiasi gani?

Alionana na mkuu wake na kumweleza kila jambo, na kwa kupitia hayo basi, ili atimize kazi yake vema, akaona kuna haja ya kuongezewa nguvu maradufu.

Alikuwa anahitaji watu kama watano kwa ajili ya kazi.

Kazi ambayo alikuwa anaiona yeye kichwani.

Habari zilitapakaa kwenye vyombo vya habari vyote; redioni, runingani na zaidi mitandaoni. Mosi, kifo cha mazingara cha bwana Willy, pili mauaji ya maafisa wa polisi wakiwa wanatekeleza kazi zao juu ya kesi ya bwana Willy.

Mambo yalikuwa yanawaka na kuunguza.

Taifa zima la Marekani lilikuwa limezama kwenye bumbuwazi kutokana na matukio haya ya kufululiza. Watu walikuwa wanataka hitma. Walikuwa wanataka nchi yao irudi kwenye amani iliyozoeleka hapo nyuma.

Swala hilo lilitafuna kichwa cha inspekta. Aliona mzigo huo wote upo mgongoni mwake.


**

Saa sita mchana …


“Wamemuua asitoe siri!” alisema Jack akitoa macho. Marshall alikuwa anatazama tarakilishi yake mezani kwa udadisi. Alikuwa yu mtandaoni.

“Ni ajabu, wamemuua akiwa kwenye kituo cha polisi!” Jack aliendelea kubweka. “Si bure kuna watu kila eneo. Ni kazi kwelikweli.”

Jack aliweka kituo akamtazama Marshall.

“Kwahiyo naongea mwenyewe hapa, sio?” akauliza akipandisha nyusi.

“Kuna cha maana ambacho umeongea sijasikia?” Marshall akauliza pasipo kumtazama Jack, bado alikuwa bize na tarakilishi yake.

“Marshall, usikiite usichoweza kupambana nacho!”

“Kipi hicho?”

“Unakijua wewe. Yani mimi kuongea kote huko we hujaona la maana?”

“Kabisa.”

“Marshall, nikinyamaza, utajuta.”

“Nitanenepa maana utakuwa umeniepusha na ujinga.”

“Aaanh!”

“Sikia, Jack. Nipo bize hauoni? Waweza kunipa muda wa kuhema tafadhali.”

Basi Jack akakwapua mfuko wa chocolate uliokuwepo pembeni, kwa hasira akaufungua na kuanza kumumunya. Baada ya muda kidogo, akafunggua tarakilishi yake na yeye akaanza kufanya mambo yake.

Lakini muda kidogo, tarakilishi ya Marshall ikaanza kukonyezakonyeza. Ilifanya vivyo kwa kama dakika kisha ikazima!

Marshall akaibamiza,

“What the f*ck!” akalalama. Akajaribu kuiwasha tena lakini isidumu ikafanya kama awali na kuzima tena.

Alishindwa cha kufanya. Alimtazama Jack, akamwona mwaname huyo akiwa yu bize na tarakilishi yake kana kwamba hakuwa anamwona wala kumsikia akilalama.

Akajaribu kuchomoa tarakilishi yake toka kwenye umeme na kulazimisha kuizima kisha akangoja kwa kama dakika tano, akaiwasha tena!

Alikuwa amekunja uso kwa hasira. Alikuwa anafanya mambo kwanguvu na kwa upesi.

Tarakilishi iliwaka, akashusha pumzi ndefu ya ahueni, pheeeeeeww!

Asifanye kitu, sekunde tano tu mbele, tarakilishi ikaanza kukonyeza, mara ikazima tena! Marshall akatukana akibamiza meza.

“Jack, nini shida na hii mashine?” akauliza.

Jack hakumjibu, badala yake akawa analiza mluzi. Hapa ndio Marshall akapata jambo kichwani -- atakuwa ni --

“Jack, wewe ndo umefanya hivyo, sio?” akapaza kuuliza. Jack akamtazama pasipo kumjibu kisha akarudisha macho yake kwenye kioo cha tarakilishi na kuendelea kuperuzi.

Mdomoni alikuwa analiza mluzi.

“Jack, si naongea na wewe?”

“Huoni nipo bize, ama?”

Marshall akashindwa kujizuia kutabasamu.

“Jack, niko serious!”

“Sawa sawa, mimi nimekuelewa. Endelea kuwa serious na kazi yako, na mimi niko serious na kazi yangu. Kwani kuna shida?”

“Najua ni wewe, nirekebishie basi ndugu yangu?”

Jack hakujali, akaendelea na kazi yake. Marshall akambembeleza mpaka alipoona anyanyuka na kumfuata akimlazimisha ampatie tarakilishi yake atumie.

Wakiwa wanazozana na kuvutana, Danielle akaingia.

“Habari njeeeema!” mwanamke huyo alipaza sauti akiwa amenyoosha mikono yake juu. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea bahasha rangi ya kaki.

Akiwa na furaha, akaiweka bahasha mezani, upesi Marshall akawahi kuifungua bahasha hiyo, ndani akakuta nakala za vibali.

“Kila kitu kipo tayari sasa!” alisema Danielle. “Kuanzia kesho tutaanza kazi!”

Marshall aliendelea kupekua kwa macho yake nakala moja baada ya nyingine. Kulikuwamo na nyaraka nne.

“Hadi na ya gazeti?” akauliza Marshall akitazama nyaraka. Alitabasamu kwa ukubwa kabisa kisha akampongeza Danielle kwa kazi aliyofanya.

“Lakini imekuwa ni upesi sana! Sikujua kama hili swala la gazeti lingechukua muda mfupi,” alisema Marshall.

Danielle akatabasamu.

“Hiyo haili muda. Haina vigezo vingi kama kibali cha kufungua taasisi ya kipelelezi. Vilevile ghushi ambazo ametengeneza Jack zimesaidia sana!”

Baada ya kufurahia mafanikio hayo, wakaanza kujadili kuhusu matukio yaliyotokea siku hiyo. Moja ya jambo kubwa kabisa ambalo walikubaliana ni juu ya usalama wa bibie Marietta.

Kama Willy ameweza kuuawa kwasababu ya kuficha maneno, Marietta atapona?

Basi usiku mzima wakajadili kuhusiana na jambo hilo, na kwa kushirikiana wakaandaa habari ndefu na ya kina ambayo ndiyo ilikuwa ya kwanza kabisa kwa ajili ya gazeti lao la kesho.

Gazeti lao hilo wakalipa jina la MWAMBA.

Kumaanisha mwamba waliokataa waashi, umegeuka kuwa …


**


Asubuhi ya saa tatu …


“Haya hapa majibu, mkuu,” alisema afisa akiwa anamkabidhi inspekta James bahasha. Yalikuwa ni majibu ya vinasaba ambavyo vimepatikana kwenye mabaki ya damu yaliyokusanywa kwenye eneo la tukio na wataalamu - forensic experts.

Alipotazama zaidi ndani ya bahasha akapata kuona picha za wanaume wawili.

Wanaume ambao ni watuhumiwa wa tukio la kuwavamia maafisa na hata kusababisha kifo.


**


*SEHEMU YA 10*


Baada ya kupata picha hizo, inspekta akafanya namna zikuzwe na kutandazwa mitaani kwa ajili ya msako wa watu hao wawili. Lakini katika namna ya ajabu kidogo, ilibainika kuwa watu hao ni maafisa wa USSS! - shirika linalohusika na ulinzi wa Raisi, makamu na watu wengine wakubwa na familia zao.

Kwenye majira ya mchana, bwana James akaenda hospitali kuonana na Harold apate kumjulia hali. Alipofika huko akapata kuongea machache na mwanaume huyo kabla ya simu yake kuita mfukoni.

Alipotazama, akaona ni Marietta!

Basi akasonga kidogo kando apate kuongea.

“Inspekta, naweza nikaonana na wewe?” sauti ya Marietta ilisema. Ilikuwa inatikisika ikiakisi woga. Kabla inspekta hajatia neno, Marietta akaongeza,

“Naogopa sana. Nahisi sipo salama!”

Inspekta akamuuliza,

“Upo wapi muda huu?”

“Kwangu!” Marietta akajibu.

“Unaweza fika kituoni?”

“Sawa.”

Inspekta alipokata simu, akafanya namna kurudi kituoni apate kuonana na Marietta. Aliagana na Harold akimuahidi kuja tena kesho kumjulia hali.

Basi baada ya muda mfupi akawa ameshawasili kituoni, na isichukue muda, Marietta akafika pia.

“Nipo hatarini inspekta!” alisema Marietta kwa hofu. Uso wake ulikuwa umejikunja, mikono yake ameifumbata.

Alifungua pochi yake akatoa gazeti na kuliweka mezani. Inspekta aliponyanyua gazeti hilo na kulitazama, akaona picha ya Marietta na habari iliyokuwa inasomeka juu,

“MLENGWA ANAYEFUATA!”

Alisoma jina la gazeti hilo, akaona ni MWAMBA. Basi akajipa muda kidogo kupitia gazeti hilo na habari yake.

Akasoma namna ambavyo mwandishi alivyohariri kutabiri kuwa Marietta ndiye mtu anayefuata kuuawa sababu zikiwa yeye kuwa karibu na polisi lakini pia kuandamwa na mambo kadhaa yanayotishia usalama wake hapa karibuni.

Inspekta alipomaliza kusoma habari hiyo, akaliweka gazeti hilo pembeni na kumtazama Marietta,

“Una kitu cha kuniambia, madam?” akauliza.

Marietta alikuwa akitetemeka, anatazama chini. Macho yake yalikuwa mekundu akiwa anaminya lips.

“Kwanini unajihisi upo hatarini? Ni muda wa kuongea madam, siwezi kukusaidia kama umefunga kinywa.”

Basi baada ya Marietta kufikiria kidogo, akasema amekuwa akipokea jumbe za vitisho na anahisi kuna mtu anamfuatilia.

“Unahisi mtu huyo ni yule ambaye alikunywesha hotelini?” inspekta akauliza.

“Hapana, lakini kuna mahusiano naye,” Marietta akajibu na sasa kwa wazi akafunguka kwamba, anahofia taarifa alizompatia mtu yule hotelini ndizo ambazo zinamuweka kwenye hatari ya kupoteza maisha.

“Habari gani hizo unadhani ulimpa mtu huyo kiasi cha kukuhatarisha?” akauliza inspekta. Alikuwa anamtazama Marietta machoni ingali mwanamke huyo akitazama chini.

“Inspekta, sijui wapi pa kuanzia. Ni mlolongo mrefu sana.”

“Usijali, nina muda wa kutosha.”

Basi Marietta kwa woga, akaelezea yale yote anayoyafahamu. Akaelezea tangu alivyokuwa anamjua bwana Ian na namna gani ambavyo alikuwa na mahusiano naye kwa siri.

Alieleza kila kitu, kila kitu. Sasa inspekta akapata picha kamili juu ya kinachoendelea. Kumbe bwana Willy yupo nyuma ya bwana Ian, na mabwana hao pamoja na jeshi lao ni washukiwa kuhusu kupotea kwa Raisi.

Sasa kwanini wanataka kumuua Marshall? Inspekta akajiuliza.

Alipofikiri kwa muda akakubaliana na akili yake kwamba huenda Marshall ana taarifa ambayo mabwana hawa hawataki ivuje.

Lakini pia kama haitoshi, Marshall ndiye yule aliyemnywesha Marietta kisha akatokomea na habari ambazo ndizo zimechapishwa kwenye gazeti/

Na kuhusu yale mabaki ya damu yaliyokutwa kwenye nyumba ya Jack Pyong, yalikuwa ni ya afisa wa usalama ambaye anahusika pia na genge lan. Walikuwa kwenye mapambano haya kwa muda.

Na wale watu wote ambao Marshall anadaiwa kuuawa, watakuwa ni washirika wa bwana Ian pia vilevile!

Alishangazwa sana na namna ambavyo habari hiyo ilivyozunguka. Kwa namna moja ama nyingine aliikuta akipata hamu sana ya kuonana na Marshall. Pengine ulimwengu sivyo vile anavyouona.

Lakini atampatia wapi?

Alitazama gazeti lile la MWAMBA akajikuta akipata wazo.

“Madam, ina maana unataka kuniambia haujui kabisa mahali ambapo mumeo atakuwapo?” inspekta akamuuliza Marietta.

“Sijui kabisa!” Marietta akaapa. “Laiti ningelikuwa najua, basi ningeshafanya jambo. Najutia sana kwa nilichokifanya kwakweli. Najiona mkosefu kabisa!”

“Na vipi kuhusu Ian?”

“Sijui kuhusu yeye, ila naamini atakuwa anajua. Naomba unisaidie inspekta nimwone mume wangu. Nataka nimwombe radhi kabla sijafa ama kufungwa kama ikitokea.”

Marietta akaanza kudondosha machozi.

“Tunawezaje kumpata Ian?” inspekta akauliza.

“Si rahisi kumpata,” Marietta akajibu, “hana makazi maalum, anapohitaji kuonana nami huwa anakuja ofisini kwangu ama nyumbani.”

“Vipi kuhusu mawasiliano yake?”

“Ana namba kadhaa na barua pepe moja ninayoifahamu. Labda inaweza kusaidia.”

Inspekta akachukua namba hizo na kuzinakili kwenye kijitabu chake.

“Inspekta,” Marietta akaita. Alimtazama inspekta machoni na kumwambia, “kuwa makini sana, hata humu ndani kuna watu wa Ian.”

Inspekta akamtazama Marietta kwa umakini.

“Kifo cha Willy ni ishara tosha kuwa humu kuna maajenti wasaliti,” alimalizia Marietta.

Hilo jambo likazama kwenye kichwa cha inspekta.


**

Jioni ya saa kumi na moja …


“Changamka, hatuna muda wa kukaa hapa!” alisema jamaa mmoja aliyevalia koti la ngozi. Mkono wa kuume alikuwa amebebelea bunduki ndogo na wa kushoto kuna begi dogo.

Alikuwa amesimama akimtazama mwenzake ambaye alikuwa anakusanyakusanya vitu kuvitia kwenye begi.

Mwenzake huyo alikuwa amevalia sweta, suruali ya kadeti na viatu vyeusi imara vya ngozi. Walikuwa wapo kwenye haraka sana.

Upesi walifungua mlango na kutoka ndani, wakaelekea kwenye gari na kujipaki kisha wakatimka.

Mabwana hawa walikuwa ndiyo wale waliokuwa wakitafutwa baada ya picha zao kutandazwa mitaani kama wahusika wa mauaji ya bwana Gerrard na kujeruhiwa kwa bwana Harold.

Walinyooka na gari lao moja kwa moja mpaka kwenye makazi fulani tulivu. Humo waliketi sebuleni na baada ya muda mfupi wakaonana na bwana Ian.

Walipoongea kidogo, Ian akatoa ishara ya kichwa, wanaume hao wakauawa kwa kumiminiwa risasi kisha wakawekwa kwenye mfuko na kuwekwa ndani ya gari kwa ajili ya kwenda kutupwa.

Lakini kulikuwa na jambo …
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 11 & 12*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Mabwana hawa walikuwa ndiyo wale waliokuwa wakitafutwa baada ya picha zao kutandazwa mitaani kama wahusika wa mauaji ya bwana Gerrard na kujeruhiwa kwa bwana Harold.

Walinyooka na gari lao moja kwa moja mpaka kwenye makazi fulani tulivu. Humo waliketi sebuleni na baada ya muda mfupi wakaonana na bwana Ian.

Walipoongea kidogo, Ian akatoa ishara ya kichwa, wanaume hao wakauawa kwa kumiminiwa risasi kisha wakawekwa kwenye mfuko na kuwekwa ndani ya gari kwa ajili ya kwenda kutupwa.

Lakini kulikuwa na jambo …

ENDELEA

Ingali wanaume hao wawili wanaenda kutupwa, kuna gari lilikuwa linawafuata kwa nyuma, tena kwa utaratibu na tahadhari.

Gari hilo lililokuwa linawafuata si kwamba lilianzia hapa, hapana, lilikuwapo tangu mabwana hawa wawili wanatoka zao kwenye yale makazi.

Basi lile gari lililobebelea maiti likaenda mpaka baharini na huko wakashuka watu wawili na kutupa miili hiyo. Pasipo kutambua wakapigwa picha za mnato ambazo ziliwavuta vema.

Wakarudi zao kwenye gari na kuhepa.

Bado wasiwe wanajua kama wanafuatwa.

Walilivuka gari lile lililokuwa linawafuatilia, wakaenda zao na safari yao. Kwa ushahidi zaidi, picha zingine zikapigwa mbele na nyuma ya gari hilo kukamata namba za usajili.

“Hizo namba zingine nimekutumia, umeziona?” alisema mwanaume kwenye simu. Alikuwa ni bwana Marshall akiwa amevalia glovu nyeusi mkononi na macho yake ameyafunika na miwani meusi ya jua.

“Ndio, nimezipata,” sauti ikamjibu kwenye simu.

“Basi zifanyie kazi na unipe majibu upesi!” akasema Marshall na kisha akakata simu.

Akawasha gari na kuhepa.

**

“Kila kitu kipo hapa,” alisema Marshall akiweka kamera mezani. Jack akaikwapua kamera na kutazama picha zilizomo. Kulikuwa na picha nyingi sana.

“Vema!” akabwatuka, “hizi tutazitumia kwenye gazeti.”

“Hapana, si zote,” Marshall akampa angalizo. “Kuna ambazo tutazitumia na kuna ambazo hatutazitumia mpaka pale tutakapokamilisha kazi yetu kwanza.”

“Picha zipi hizo?” akauliza Jack. Marshall akampokonya kamera na kumwonyesha zile picha za jengo ambapo bwana Ian anapatikana. “Hili eneo linatakiwa kuwa siri mpaka pale tutakapompata ama kuwa na uhakika wa kumpata Ian.”

Basi Jack akaziweka picha zote kwenye tarakilishi yake, alafu akamtumia Miss Danielle picha kadhaa kwa kutumia mtandao akiwa yu kwenye faragha kubwa.

Danielle alikuwa kule kwenye ofisi ipatikanayo jijini.

Punde aliona picha hizo na maelezo kadhaa. Akafurahishwa sana.

Akiwa anazitengenezea picha hizo maelezo, mara mtumishi wake aliingia na kumwambia ana ugeni. Kabla hajasema jambo akarusha macho yake kwenye tarakilishi kutazama mrejesho wa kamera alizozifunga.

Alikuwa anataka kumjua mgeni huyo ni nani.

Basi kwa kutazama, akamwona bwana James Peak. Bwana huyo akiwa amevalia suti alikuwa amekunja miguu yake nne akingoja.

“Anataka nini?” Danielle akajiuliza. Alifikiri kidogo kish akamtaka mtumishi wake amruhusu bwana huyo aingie ndani.

Alipoingia, akaketi na kusalimiana na miss Danielle. Mkononi mwake alikuwa amebebelea gazeti. Hapo Danielle akajua bwana huyo alikuwa amekuja kwasababu gani.

Inspekta aliweka gazeti mezani kisha akamtazama Danielle.

“Nadhani una kitu cha kuniambia kuhusu gazeti hili,” akasema bwana huyo, sasa akiwa anamtazama Danielle kwa macho ya mkazo.

“Inspekta, nilidhani nimemalizana na wewe,” akasema Danielle. Akapandisha nyusi moja na kupindisha shingo yake akimtazama inspekta, “Ile faini haikutosha?”

Bwana James akamtazama mwanamke huyo kwa sekunde kadhaa kabla hajashusha pumzi na kutia neno, “Miss Danielle, najua una mahusiano na Marshall. Najua kabisa kuwa mnawasiliana na huenda mnafanya vitu pamoja. Na--”

“Kwanini usinikamate?” akakejeli Danielle.

“Sikia, Danielle, mimi sipo hapa kukuhukumu ama kukutuhumu. Nipo hapa kutazamia kama kuna uwezo wa kufanya kazi kwa pamoja kwasababu ya taifa letu kwa ujumla. Waweza kufikiria kuhusu hilo?” alisema bwana James.

“Inspekta,” akaita Danielle. “Mimi nipo hapa kila uchwao. Nipo radhi kutoa msaada wowote ule kwa ajili ya taifa langu. Hilo halina shida.”

“Danielle, kwenye gazeti hili imeonyesha kuwa Marietta yupo kwenye hatari, na jambo hili limekuwa kweli. Kama inawezekana naomba niwe napata taarifa hizi, zitanisaidia sana.”

“Inspekta, nadhani nimeshakuambia hapo kabla. Sijui lolote unalozungumza.”

Basi inspekta baada ya kuona jitihada zake hazizai matunda, akanyakua gazeti na kusimama aende.

“Utakapobadilisha mawazo, karibu sana!” alisema vivyo kisha akaenda zake. Danielle akamsindikiza kwa macho mpaka alipotoka.

Akahamishia macho yake kwenye runnga ya kamera, akamtazama bwana huyo mpaka anaondoka kuacha jengo.


**

Usiku wa saa tatu …

“Ni mapema sana,” alisema Marshall akitazama mbele. Walikuwa wawili ndani ya gari, yeye pamoja na Danielle.

Watu hawa walikuwa wamevalia nguo nyeusi za kubana, kila mmoja amevalia kofia ya soksi kichwani. Mahali hapa ambapo wameweka kambi palikuwa pametulia sana.

Ni kiza.

“Hatuwezi jua yupo upande gani,” Marshall aliendelea kusema. “Ni vema tukajipa muda zaidi tukajua mienendo yake.”

Baada ya Marshall kusema vivyo akamtazama Danielle na kumuuliza, “Au unasemaje?”

“Nakuunga mkono,” akasema Danielle akitikisa kichwa. “Japo ana nia safi, hatujajua mdomo wake unaweza kupanuka kiasi gani.”

Basi baada ya mazungumzo hayo mafupi kumwongelea inspekta James, Marshall akafanya namna kuwasiliana na Jack Pyong. Mwanaume huyo wa kichina alikuwa nyumbani mbele ya tarakilishi zake nne ambazo ameziunga na mtandao lakini pia akiwa amedukua mfumo wa satelaiti.

Pembeni yake kulikuwa na kopo la bluu lenye kubebelea soda.

“Kuna kitu huko?” akauliza Marshall.

“Hapana,” akajibu Jack. “Bado ni kimya.”

Ukapita kama muda wa nusu saa. Kimya kwa Jack na pia kimya kwa wakina Marshall.

Ukimya huo usidumu zaidi, mara Marshall akaona gari jeupe aina ya van ikiwa inapita barabarani kwa mwendo wa stara. Alitilia mashaka gari hiyo. Alimshtua Danielle wote wakaitupia macho.

“Nadhani wameshawasili!” akasema Marshall.

“Jack ameshakupa taarifa?” Danielle akauliza. Alikuwa amesinzia kidogo wakati wakingoja.

“Hapana, watakuwa wametumia usafiri mwingine,” akasema Marshall akiendelea kutazama van ikienda.

Kama yalivyokuwa makisio yake, van ile ikaelekea mashariki mwao. Hapo wakashusha kofia zao na kuwa barakoa kisha Marshall akatia moto chombo na kusonga.

**

“Hakikisha haufanyi makosa!” alisema mwanaume ndani ya van akimwambia mwenziwe. Walikuwa watu watatu kwa idadi.

“Najua cha kufanya,” akasema mwanaume mwingine karibu na mlango. Alikuwa amebebelea bunduki mkononi. Bunduki ambayo tayari ameshaikoki kwa ajili ya tukio.

“Na nyie fanyeni kazi yenu,” akasema bwana huyo alafu akajiveka kinyago chenye uso wa mbuzi na ndevu zake kisha akajongea kuufuata ukuta na kuukwea.

Tih! Akashukia kwa ndani.

Kwa tahadhari akasonga na kufyatua risasi kuwalenga walinzi wawili waliokuwa wamesimama getini. Baada ya hapo akauendea mlango na kuushindilia risasi kabla hajaukita teke na kuzama ndani.

Sebule ilikuwa tupu. Alitazama kushoto na kulia; koridoni kwenda chumbani na kisha jikoni.


***


Marietta akiwa chumbani, akiwa amelowa kwa hofu kubwa, alisumbuka na simu yake. Kila alipopiga namba haikuwa inapatikana. Alikuwa anatetemeka kupita kiasi. Anavuja jasho na machozi pia.

Alitazama chumba chake aone wapi anaweza kujificha, kote akaona hapafai.

Hakuwa anajua cha kufanya, na kwa muda fulani akawa kama zuzu fulani!


***

*SEHEMU YA 12*


Akiwa amepigwa na butwaa ndipo akili ikamjia. Alikuwa na bunduki kabatani!

Basi upesi akaendea bunduki hiyo na kuijaza mkononi. Kwa mkono wake unaotetemeka akashika bunduki hiyo.

Alitazama kushoto na kulia. Dirishani na mlangoni akiwa anatarajia kumwona mtu. Alikuwa anahema kwanguvu, moyo unamkimbia.

**

Basi bwana yule ambaye amezama ndani, kabla hajafanya maamuzi ya maana ya aidha kwenda kufuata korido ama kwenda jikoni, akasikia sauti kadhaa za bunduki huko nje!

Alishtuka na upesi akainama kwa usalama kisha akawasiliana na wenzake aliowaacha kwenye van. Nini kinaendelea?

Aliuliza mara tatu pasipo majibu. Kidogo kabla hajakata tamaa akasikia, “Tupo under attack! Tunashambuliwa!”

Basi upesi akatoka ndani ya sebule na kujikuta nje, lakini kabla hajafanya jambo mkono wake uliobebelea bunduki ukatunguliwa na kumsababishia maumivu makali!

Upesi, akiwa anavuja damu, akasonga na kujibana kwenye nguzo. Lakini ubaya ni kwamba hakuwa anajua anayemshambulia yupo upande gani.
Alipokaa hapo, akatunguliwa tena risasi ya mguu, akadondoka akilalama kwa sauti kubwa. Mguu ulikuwa unamwaga damu haswa!

Alitazamia bunduki yake, akaiona ipo mbali. Asingeweza kujikokota kuifuata kwa maana alikuwa anasikia maumivu makali lakini pia ingekuwa ni hatari zaidi kwa usalama wake.

Basi akanyoosha mikono juu ishara ya ku - ‘surrender’. Akapaza sauti yake kuwa amefanya vivyo na basi asishambuliwe zaidi.

Punde akatokea mtu toka upande wake wa kushoto, mtu ambaye amejifunika uso wake kwa barakoa nyeusi.

Mtu huyo kwa mwonekano na hata kwa mwendowe alikuwa ni mwanamke. Mkono wake wa kuume ulikuwa umeshikilia bunduki ndogo iliyokuwa inatema moshi.

“Usiniue!” alisema bwana yule aliyewekwa chini ya ulinzi. “Usiniue, tafadhali!”

Maneno hayo yakafika kwenye ngoma za masikio ya Marietta. Mwanamke huyo bado akiwa ameendelea kushikilia bunduki yake kule chumbani, akajongea dirishani na kuangaza nini kinachoendelea huko nje.

Alirusha macho lakini hakubahatika kuona. Watu walikuwa mbele ya nyumba ingali dirisha likiwa pembeni.

Basi akatega sikio lake kuskiza.

Alijitahidi kuskiza kwa uwezo wake wote.

Punde akasikia maongezi machache.


**


“Tupo tunashambuliwa! … unasikia, unasikia? Tupo tunashambuliwa!” alisema mwanaume wa pili aliyekuwa ameketi pembezoni mwa dereva wa van. Mwanaume huyo alikuwa ameshikilia kifaa cha maongezi mdomoni mwake.

“Tunaomba backup, tunaomba backup!” aliendelea kuropoka na kutaja eneo lakini bado majibu hayakuwa yanasikika. Ni kama vile alikuwa anaongea na mfu.

“Vipi?” mwenzake akamuuliza. Uso wake ulikuwa umejawa na mashaka. Alikuwa amekanyagia mafuta kwanguvu gari likipepea kishada!

“Siwapati!” akajibu yule mwenye kifaa cha kuongea kisha akarudia tena kuita kwenye kifaa. Bado patupu!

Kidogo dereva akaona gari ikiwa imesimama mbele yao. Katika namna ya upesi sana, wakaanza kutupiwa risasi kiasi kwamba wakapoteza kabisa mwelekeo na kwenda kukita mti. Hapo ukawa mwisho wa safari yao!

Gari likatema moshi mwingi sana! Likakoroma na kukoma. Kioo kilikuwa kimesagika na shoo ya mbele ilikuwa imechakaa kabisa.

Wote waliokuwapo ndani wakawa hoi sana. Walikuwa hawajiwezi kwa kuvuja damu.

Mmoja, yule ambaye alikuwa anwasiliana kifaani, akatanua mkono wake na kufungua mlango wa gari apate kujitupia nje. Ndani ya gari alikuwa amebanwa, kujitupia chini kungempa ahueni.

Alikuwa amelowa damu karibia mwili mzima. Ni kheri hata alikuwa na nguvu ya kujikomboa. Mguu wake wa kushoto ulikuwa umejruhiwa sana.

Basi akajiangushia chini akiwa anahema kwanguvu na kuskizia maumivu yake. Alikuwa anaona kwa uhafifu.

Akiwa hapo, punde akaja mtu na kusimama kando yake. Mtu huyo alikuwa ni mwanaume aliyavalia barakoa nyeusi na mkono wake wa kuume umebebelea bunduki.

“Usiniue, tafadhali,” akalalama yule bwana chini. “Nihifadhie uhai wangu tafadhali.”

Uso wake ulikuwa unatia imani, ukijumlisha na maumivu aliyokuwa nayo nadhani unapata picha kamili. Alinyoosha mkono wake wa kuume kumwelekea mtesi wake akimwomba ambakizie uhai.

Mtesi pasipo kujali, akamnyooshea tundu la bunduki pasipo kutia neno.

Lakini wakati hilo linaendelea, yule bwana dereva aliyekuwa ndani ya van akarusha macho yake kuangaza.

Hakuwa amekufa lakini alikuwa amejeruhiwa vibaya sana. Kuanzia kiunoni mpaka kushuka chini hakukuwa kunafanya kazi, kumebanwa na kunavuja damu. Lilikuwa ni swala la muda tu kwa bwana huyu kufia hapa.

Ila ingali akiwa na nguvu na akiwa anaona kilichotokea, akanyanyua bunduki ndogo iliyokuwa pembeni yake na kisha akamwonyeshea yule mwanaume mwenye barakoa nyeusi apate kumlenga.

Lakini kabla hajatimiza haja yake hiyo, mara sauti ya risasi ikavuma - pah! Kufumba na kufumbua bwana huyo dereva akawa amekiwsha kufa. Risasi ilitoboa kichwa chake na kumlaza kwa amani pasipo shurba!

Mwanaume yule mwenye barakoa akasimamisha shingo yake kuangaza wapi amesikia risasi. Hakuwa yeye aliyefyatua!

Alipotazama vema akabaini kuna mwanaume tokea upande wa magharibi. Mwanaume huyo alikuwa amevalia koti refu rangi ya kahawia, suruali ya kumbana na viatu vya kupandia farasi.

Mkono wake wa kulia ulikuwa umebebelea bunduki.

Mwanaume huyo aliposonga mbele kidogo, ndipo akaonekana vema kuwa ni inspekta James! Basi upesi mwanaume yule aliyevalia barakoa akakimbilia gari lake na kulitia moto kuyoyoma akimwacha yule jamaa aliyekuwa amemwonyeshea bunduki palepale chini.


**


Usiku wa tano …

“Atakuwa amekutambua?” aliuliza Jack akiwa ametoa macho. Walikuwa sebuleni wote watatu, yaani huyo Jack, Marshall na Danielle.

“Hapana,” akajibu Marshall. “Hajanitambua kwani nilikuwa nimejifunika sura.”

“Una uhakika?” Jack akaongezea swali.

“Ndio,” Marshall akajibu na kuongezea, “sasa atanionaje na nilikuwa nimeficha sura?”

“Mbona mimi nakujua ukiwa umeficha sura?” Jack akauliza. Marshall akamtazama jamaa huyo pasipo kusema kitu kisha akamtazama Danielle na kumuuliza, “Vipi wewe? Kila kitu kilienda sawa?”

Miss Danielle akatikisa kichwa, “Yah! Kila kitu kilikuwa kwenye order!”

“Vema, nadhani sasa ni muda wa kuchapa ile habari yetu kuhusu wale maafisa waliokuwa wanatafutwa hatimaye wakauawa na kutupwa,” akashauri bwana Marshall.


**


Asubuhi ya saa tano na nusu …

Mezani mwa inspekta kulikuwa na gazeti la MWAMBA. Bwana huyo alikuwa ameshakunywa kikombe cha kwanza cha kahawa na sasa anacho cha pili.

Kichwa chake kilikuwa kimetingwa na mawazo sana kuhusu jana. Alikuwa ameweka tama akiwa yu mbali kifikra. Alikuwa anamuwaza yule mwanaume aliyemuona jana yake usiku akiwa amejiveka barakoa.

Alikuwa ni Marshall ama?

Kwanini alisita kumlenga wakati anakimbia? Kwa namna fulani alijiona mkosefu, lakini tena kwa namna nyingine akijipongeza kwamba huenda alichofanya kilikuwa ni sahihi kwani bwana huyo alifanya jitihada za kumwokoa Marietta.

Alishusha pumzi ndefu, akakumbuka sauti ya Marietta jana yake wakati anaongea naye baada ya tukio.

“Alikuwa ni mwanamke,” sauti ya Marietta ilinena masikioni mwa inspekta. “Nilisikia sauti yake. Ni yeye ndiye alimweka mwanaume huyo chini ya ulinzi kabla hajatokomea akiwa ameondoka na silaha ya adui, ndipo watu wako wakamshika!”

Mwanamke huyo ni nani? Inspekta akajiuliza. Akanywa fundo moja la kahawa kisha akaendelea kutafakari kile alichoambiwa na Marietta.

Je, mwanamke huyo ni Danielle? Akili yake ilijituma kung’amua.


**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 13*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Alishusha pumzi ndefu, akakumbuka sauti ya Marietta jana yake wakati anaongea naye baada ya tukio.

“Alikuwa ni mwanamke,” sauti ya Marietta ilinena masikioni mwa inspekta. “Nilisikia sauti yake. Ni yeye ndiye alimweka mwanaume huyo chini ya ulinzi kabla hajatokomea akiwa ameondoka na silaha ya adui, ndipo watu wako wakamshika!”

Mwanamke huyo ni nani? Inspekta akajiuliza. Akanywa fundo moja la kahawa kisha akaendelea kutafakari kile alichoambiwa na Marietta.

Je, mwanamke huyo ni Danielle? Akili yake ilijituma kung’amua.

ENDELEA

Aliendelea kujiuliza mwishowe akachukua gazeti lililokuwapo mezani kwake na kuliperuzi. Gazeti la MWAMBA.

Alipomaliza kulipitia, baadae akaenda kuonana na Marietta kumjulia hali. Mwanamke huyo alikuwa yupo chini ya ulinzi mkali wa polisi kwasababu za usalama wake.

Alikuwa ameketi sebuleni kwake akiwa anakunywa mvinyo. Glasi ndefu ilikuwa imejaa kinywaji ilikuwa karibu yake kama ilivyokuwa kwa mawazo kichwani mwake.

Alikuwa anamuwazia sana mumewe. Alikuwa anajutia. Hakuwa analala usiku kwa kutingwa.

“Unaendeleaje hivi sasa?” inspekta alimuuliza na kuongezea, “nimwite dokta?”

“Hamna haja hiyo,” Marietta akasema akitikisa kichwa. “Nipo sawa tu.”

Sauti ya Marietta ilikuwa inakoroma kana kwamba ametoka kulala. Uso wake ulikuwa umenywea. Macho yamelegea. Nywele zake zilikuwa zimetibuka. Na japo alikuwa anakunywa mvinyo, lips zake zilikuwa kavu.

“Unaonekana haupo sawa lakini,” alisema imspekta akimtazama Marietta kana kwamba daktari anayemkagua mgonjwa.

Marietta akaguna kwa sauti ya puani. Akanywa zake mvinyo kwa muda kisha ndiyo akarudi kwenye maongezi na inspekta.

“Bwana James, siwezi kuwa sawa hata ukiniitia madaktari wote nchini,” alisema Marietta alafu akamgeuzia macho yake mazito bwana James. “Shida yangu ni kumwona mume wangu tu. Nadhani nikimwona yeye hali yangu itakuwa sawa.”

Bwana James akashusha pumzi.

“Madam, unajua taifa zima linamtafuta bwana huyo. Laiti ungelikuwa na taarifa yoyote kumhusu, ingetusaidia wapi pa kuanzia.”

Kukawa kimya kidogo.

“Vipi? Haujui hata baadhi ya maeneo tunapoweza kumpata?”

“Bwana James, si rahisi kama unavyodhani.”

“Kwanini unasema hivyo?”

“Unadhani kama ingekuwa rahisi si angeshapatikana? Donge nono lililoahidiwa, mtu mkubwa kama yule anayefahamika dunia nzima, mpaka leo hii hamna hata ujumbe!”

Marietta aliposema hivyo akachuruza chozi. Akanywa tena kinywaji chake kumpooza.

“Lakini naamini bwana Ian anajua!” akasema aking’ata meno. “Najua ni mtu mwenye mtandao, mtu mwenye kujuana na watu wengi, anashindwaje kujua hili?”

Marietta alisema akikunja sura. Ni kama vile alikuwa anatafuna mwarobaini. Haikupita muda akaanza kumimina machozi kupita kiasi na kubanwa na kwikwi za kilio.

Ilimpasa bwana James ashughulike na kumbembeleza.

Alipotulia, akamweleza bwana James nia yake ya kutaka kuonana na mtoto wa mumewe. Pengine akimwona atampatia faraja.

“Nakuomba sana, mtafute popote alipo. Nataka kumwona tu, nimshike, nimkumbatie. Tafadhali!”

Bwana James akamuahidi kufanyia kazi jambo lake. Ampatie kama juma moja tu atakuwa amekwishalifanikisha hilo.

“Nitafurahi sana.”

“Usijali, lakini hakikisha afya yako inaimarika,” akasema inspekta kabla ya kwendaze.


**

Saa nne usiku …

Kulikuwa ni kiza na tulivu kwenye eneo hili. Kwa kushoto kwako kulikuwa na gari ambalo limeegeshwa kwa utulivu mkubwa, yani halingurumi wala halijawashwa taa.

Gari hilo kwa ndani lilikuwa limekaliwa na watu wawili wa kazi. Mwanaume na mwanamke, Marshall na Danielle!

Danielle alikuwa anakata kucha zake za mkononi ingali Marshall akiwa anatazama upande wao wa magharibi. Kama kawaida wawapo kwenye tukio, walikuwa wamevalia nguo za kazi, nguo nyeusi na kofia za soksi ambazo huwa barakoa wakizivuta kwa chini.

Ni kama vile walikuwa wanangoja kitu. Masikioni mwao walikuwa wamefungia vifaa vya usikivu na mawasiliano.

“Leo ndiyo siku,” akasema Marshall akiwa anatafuna bubblegum. “Endapo tukimpata Ian, kazi yetu itakuwa rahisi kupita kiasi.”

“Kwanini unawaza vivyo?” Danielle akauliza akiendelea na zoezi lake. Ni kama vile hakuwa anaskiza na kujali, ila ilikuwa ni kinyume.

“Ian ndiyo kitovu wa yote haya,” akasema Marshall. “Tukimpata yeye na --” akatazama mkono wake wa kuume, alikuwa ameshikilia chupa ya Sodium thiopental, “-- na akatueleza kila tunachotaka, hatimaye nitakuwa huru kwa kila mtu kujua ukweli.”

Kukawa kimya kidogo. Marshall akamtazama Danielle na kumuuliza, “Ama unasemaje?”

Danielle akapandisha mabega juu, “Sijui, Marshall. Lakini naamini tukimpata bwana Ian tutajua tuelekee njia ipi baada ya hapa.”

Danielle akajitengenezea vema kwenye kiti na kuweka kikatio cha kucha pembeni.

“Itabidi tuwe makini sana,” akasema akitazama jengo upande wao wa magharibi. “Endapo tukitoka salama kwenye lile jengo basi tutakuwa tumeshinda.”

“Na ni lazima tushinde!” Marshall akatia neno kisha akageuza shingo kumtazama Danielle. "Si kila kitu kipo tayari?" Akauliza

"Ndio," Danielle akajibu. "Kila kitu kipo kama tulivyopanga."

"Basi vema. Tutafuata mpango wetu vivyo hivyo."

Baada ya hapo, Marshall akabinya kifaa chake cha mawasiliano sikioni na kuuliza, "bado?"

"Bado. Ngoja kidogo!" Sauti ya Jack ikamjibu sikioni.

"Jack, muda unazidi kwenda!"

"Najua. Lakini bado target haijakaa sawa. Endapo mkienda mtapata ugumu."

"Kwahiyo tungoje mpaka saa ngapi?"

"Ngoja kama nusu saa."

"Yote hiyo!"

"Nadhani katika muda huo n'takuwa n'shajua cha kufanya!"

"Na je huo muda ukipita?"

"Hauwezi kupita!"

Basi ikabidi Marshall na Danielle waendelee kusubiri taarifa toka kwa Jack Pyong ambaye alikuwa ana 'trace' location ya destination yao.

Wakangoja hapo kwa hilo nusu saa Marshall akiwa anaskiza muziki na Danielle akiwa anaendelea na zoezi lake la kukata kucha, sasa za miguuni.

Kule upande wa nyumbani Jack akaendelea kukodolea tarakilishi yake kama ataona kitu. Alifanya zoezi hilo dakika zikienda na kwenda.

Alikuwa anapiga mihayo na kujinyoosha kila baada ya muda. Alikuwa amechoka. Alirembua macho yake mekundu akijitutumua kutazama.

Mwishowe akapitiwa na usingizi, akajilazia kando. Hata muda ulipowasili bwana huyu akawa hajui wala hajitambui, lakini mpaka muda huo unawasili, bado target haikuwa inaonekana kwenye tarakilishi!

Bwana Marshall alifanya jitihada za kuwasiliana na Jack pasipo mafanikio! Aliita na kuita lakini Jack alikuwa amekwapuliwa na usingizi kupita kiasi, alikuwa ameachama akichuruza mate.

Basi likapita lisaa limoja kabisa. Ikaongezeka na nusu saa pia kukiwa kimya. Bwana Jack alipokuja kuzinduka, ilikuwa ni tayari masaa mawili kamili.

Alijifuta mate mashavuni kisha akakodoza macho yake mekundu. Alikuwa haamini alichofanya! Alijilaumu akifanya jitihada za kuwasiliana na wenzake.

Alitazama saa yake ya mkononi. Ni saa saba na dakika kumi ma mbili usiku!

"Marshall!" Jack akaita. "Marshall, unanikopi? Marshall, unakopi?"

Kimya.

"Danielle!" Akaita. "Danielle, unakopi?" Napo kimya. Akitazama kwenye tarakilishi, bado target haikuwa inaonekana. Akajawa na hofu.

Alitega sikio lake kwa umakini asikie kinachoendelea, lakini napo kulikuwa ni kimya asipate cha maana. Usingizi wote ulimkata akijihisi amewaangusha wenzake. Alijihisi mkosefu.

Na ubaya akiwa hana cha kufanya.

Alipofikiri kidogo ndipo wazo likamjia, atazame gps ya gari la wenzake apate kubaini wao upande upi wa dunia. Alipofanya vivyo, punde napo akabaini hata gps haikuwa inaonekana kwenye tarakilishi!

Inawezekanaje? Akastaajabu.

Akafanya kila kitu lakini napo haikusaidia. Hakuna taarifa aliyokuwa anaipata kwenye tarakilishi yake wala kwa simu. Basi akaona hamna namna, akaenda chumbani na kukwapua nguo zake za kazi, akajiveka na kukwapua bunduki ndogo.

Akaipakia bunduki hiyo risasi za kutosha kisha upesi akaenda kujipaki kwenye gari na kuhepa kuelekea kule ambako wenzake walielekea.
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 14*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Alipofikiri kidogo ndipo wazo likamjia, atazame gps ya gari la wenzake apate kubaini wao upande upi wa dunia. Alipofanya vivyo, punde napo akabaini hata gps haikuwa inaonekana kwenye tarakilishi!

Inawezekanaje? Akastaajabu.

Akafanya kila kitu lakini napo haikusaidia. Hakuna taarifa aliyokuwa anaipata kwenye tarakilishi yake wala kwa simu. Basi akaona hamna namna, akaenda chumbani na kukwapua nguo zake za kazi, akajiveka na kukwapua bunduki ndogo.

Akaipakia bunduki hiyo risasi za kutosha kisha upesi akaenda kujipaki kwenye gari na kuhepa kuelekea kule ambako wenzake walielekea.

ENDELEA

“Kila kitu kipo sawa!” alisema mwanaume mmoja akimtazama bwana Ian. Mwanaume huyo alikuwa amevalia overall ‘dark blue’ mkononi mwake akiwa ameshikilia spana na vifaa vingine. “Sasa hawaweza kuonekana na yeyote yule.”

“Uhakika?” Ian akauliza. Alitoa macho akitikisa kichwa.

“Ndio, uhakika,” akajibu mwanaume ndani ya overall na punde basi akaenda zake akimwacha Ian na wanaume wawili, wanaume ambao walikuwa wamebebelea bunduki ndogo mikononi mwao wakiwa wamevalia nguo nyeusi.

Bado kulikuwa ni kiza lakini ukimya haukuwa mkubwa tena kama mwanzoni.

Basi bwana Ian na watu wake wawili wakaelekea ofisini ambapo bwana Ian aliketi na kucheka sana. Alikuwa ana furaha isiyo na kifani kwani alikuwa amewatia kimyani watu waliokuwa wanampa presha kwa muda wote huo.

Watu waliokuwa wanamkosesha usingizi wala amani moyoni mwake. Alikuwa anajihisi yupo huru sasa.

Kweli duniani ni kuzidiana. Unapowazia hatua ya kwanza, mwingine anawazia ya pili tokea hapo ulipoishia. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wakina Marshall.

Ni kosa moja tu laweza gharimu meli kuzama. Waliwaza nini kutoa habari ile ya watu kutupa miili alafu wahusika wasichukue hatua zaidi kujilinda?

Basi Marshall na Danielle wakiwa wamefungwa mikono na miguu yao walitupiwa kwenye chumba chenye kiza wakingoja hatma yao, na si nyingine bali kuuawa na kwenda kutupwa.

Kitu pekee kilichofanya zoezi lao lisifanyike kwa upesi ni kukagua usalama wa kufanya hilo waliloadhimia, lakini pia kwa bwana Ian kufikiria afanye namna gani ya kuwamaliza watu wake katika namna ambayo itamsafisha na kumwacha salama kabisa.

Hilo lilikuwa ni jambo kubwa.

Apate kusafisha mikono yake.

Aliwaza kama anaweza kufanya lile jaribio la kwanza kabisa lakini akaona kuna kaugumu ama kaukakasi fulani. Mambo hayakuwa mepesi katika hilo.

Basi akiwa anavuta sigara akaendelea kuwaza. Lilikuwa ni swala la kauli tu ili jambo lolote lifanyike kwa wakina Marshall waliotiwa ndani ya chumba. Lakini kauli hiyo ilikuwa ngumu, nzito.

**

Alikuwa anahofia. Moyo wake ulikuwa unakita kwanguvu na kwa kasi. Haya mambo hayakuwa katika nyanja yake kabisa!

Yake yalikuwa ni kuketi kwenye kiti na kubofya vitufe vya tarakilishi ama kupapasa ‘sensor’ kuhamisha mshale kwenye kioo.

Jack alishusha pumzi ndefu kisha akazima gari yake na kutulia kwa muda. Kichwa kilikuwa kinamgonga, kwa hofu. Tumbo lilikuwa linanguruma na kwa muda mmoja alikuwa anahisi kubanwa na haja ndogo na kubwa!

Kajasho kalikuwa kanamchuruza.

“Tulia Jack. Tulia, kila kitu kitakuwa poa,” alisema na nafsi yake huku akipigapiga kifua . Alipiga moyo konde. Alitoa kinyago cha uso wa binadamu alafu akajivika, akawa amebadilika kabisa. Alikuwa ni mtu mwingine usimtambue kama ni Jack!

Akatoka kwenye gari na kuanza safari ya kwenda kwenye eneo la tukio. Uwanja wa kifo.

Kuna haja gani ya kuwa hai kama wenzangu watakuwa wamekufa? Alisema na nafsi yake. Kama wamekufa, basi tufe wote. Siwezi kukaa pasipo kufanya jambo. Roho yangu itanisuta, itanihukumu.

Kitu pekee ambacho alitakiwa kukifanya hapa ni kukumbuka angalau robo ya mafunzo aliyowahi kuyapitia kama ajenti wa CIA.

Ingawa yeye hakuwa mtu wa kupambana kwenye uwanja wa vita, alikuwa amepitia kwenye mafunzo ya lazima mwanzoni kabisa wa course. Mafunzo ambayo kila muhusika wa CIA anayapitia pasipo kujali atakuwa kwenye kitengo gani.

Mafunzo kwa ajili ya usalama binafsi.

Akajongea zaidi akiwa amelenga kuukuta ukuta, kuupanda na kuzama ndani kisha amuweke chini ya ulinzi mtu mmoja na kukwapua nguoze kama watakuwa na sare.

Baada ya kufanya vivyo afanye namna ya kujua wapi walipo wenzake.

Lakini kabla adhma yake haijatekelezeka, akahisi gari linakuja kwa nyuma yake. Lilikuwa ni gari la doria ambalo lilikuwa linafanya safari za kuhakikisha usalama. Ndani yake walikuwapo wanaume wawili, wote wakiwa wameketi kwenye viti vya mbele.

Basi kabla jamaa hao hawajatambua kitu, Jack akafanikiwa kujificha mahali na kurusha macho kuangaza.

Jamaa hao wakiwa kwenye gari lao linalotembea kwa mwendo wa chini, wakatambua uwapo wa gari wasilolijua pembezoni kidogo mwa barabara, umbali wa kama kilomita mbili na nusu tokea jengo lao lilipo.

Walitilia shaka gari hilo, na kwakuwa walikuwa kwenye doria ya kuhakikisha kuna usalama, mmoja akashuka akafanye ukaguzi.

Aliwasha kurunzi yake na kuangazia gari kuanzia kwa dereva mpaka kwenye viti vya nyuma. Hakuona mtu. Akapima joto la gari kwa kuweka mkono wake kwenye uvungu wa gari, akabaini uvuguvugu.

Gari lilikuwa limetoka kuzimwa muda si mrefu!

Akamtaarifu mwenzake kwa kupitia vifaa vyao vya mawasiliano ili aje kujumuika naye kufanya ukaguzi.

“Kuna alama za viatu zikielekea jengoni. Njoo upesi, huyu mtu atakuwa hajafika mbali!”

Mwenzake akaungana naye upesi wakaanza kufanya doria, wakirusha macho na kurunzi huku na kule.

Walipotembea kwa kama robo kilomita, wakasikia amri toka nyuma yao. Amri kwenye sauti nzito.

“Tulia vivyo hivyo! Weka silaha chini, nyosha mikono juu!”

Hawakuwa na budi kutimiza amri. Walidondosha silaha zao mara moja alafu wakaanika mikono yao wakiwa wamejawa na hofu nyusoni.

Wakasikia mtu akisonga karibu yao, kidogo mtu huyo akasimama mbele na kuokota zile bunduki zilizotupiwa chini kwa hali ya tahadhari. Alikuwa ni Jack Pyong!

Akamwamuru mmoja amfunge mwenzake mikono na miguu kwa kutumia shati na mkanda, alipofanya vivyo, akamjongea huyo aliyefungwa na kumkita na kitako cha bunduki chini ya kisogo, akazirai!

Jack akajipongeza kwa kufanya zoezi hilo vema. Hakutarajia kama angekumbuka namna ya kutenda. Alipoona ni vema, akamgeukia pia na yule wa pili na yeye akamfanya vivyo hivyo.

Hakuona sasa haja ya kuwafunga ingali wameshapoteza ufahamu. Alichofanya ni kuwatekeleza hapo, kuendea gari lao, kuliwasha na kulitumia kwenda jengoni.

Sasa akawa amebadilisha mipango yake.

**

Honi ya gari ililia mara moja, jamaa mmoja aliyeshiba mwili akatchungulia nje. Alipoona ni gari analolitambua, akatoa amri na gari hilo likazama ndani pasipo kukaguliwa.

Lilienda kujiegesha mbali kidogo na geti, na Jack hakujivuta, akashuka upesi kwenda zake ndani. Ni kama vile alikuwa anajua huenda akatiliwa shaka.

Ni punde tu baada ya kutoka kwenye gari, akaja mwanaume aliyebebelea bunduki kutazama chombo hicho. Alikuwa ni pande la baba akiwa amebanwa na tshirt nyeupe.

Akatazama asione mtu.

Naye akaelekea ndani.

Alipotembea kwa kama hatua kumi na tano, akahisi chuma kichwani mwake, ikafuatiwa na amri ya kumtaka atulie. Alikuwa ni Jack aliyemweka chini ya ulinzi. Na kwakuwa tayari tundu la risasi lilikuwa kichwani, hakuwa na namna zaidi ya kuwa mpole.

Lakini mabwana hawa wangetambua kwamba silaha ya Jack haikuwa hata imekokiwa, wangejiona wajinga wa kutupwa kuhofia kitu ambacho kisingewapa madhara.

**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 15*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Naye akaelekea ndani.
Alipotembea kwa kama hatua kumi na tano, akahisi chuma kichwani mwake, ikafuatiwa na amri ya kumtaka atulie. Alikuwa ni Jack aliyemweka chini ya ulinzi. Na kwakuwa tayari tundu la risasi lilikuwa kichwani, hakuwa na namna zaidi ya kuwa mpole.

Lakini mabwana hawa wangetambua kwamba silaha ya Jack haikuwa hata imekokiwa, wangejiona wajinga wa kutupwa kuhofia kitu ambacho kisingewapa madhara.
ENDELEA
Basi Jack akamtaka bwana huyo amweleze walipo wenzake. Kidogo kwa kiburi bwana huyo akagoma. Alisema hajui hicho anachoulizwa. Ni kigeni kwake.
Jack akafikiria cha kufanya, kama angemuua jamaa huyo kwa bunduki mlio ungeamsha taharuki. Akaamua kumbinya mwanaume huyo korodani kwanguvu huku akimtaka aseme anachotaka.
Bwana huyo akashindwa kuhimili maumivu, akaropoka, basi Jack akamkita kichwa na kumziraisha alafu akamvutia mahali alipopaona ni salama. Akakusanya na silaha ya adui na kwenda zake.
Alishajua wenzake walipo, sasa akasonga kuelekea huko.
Alitembea akitazama chini, akapishana na wanaume watatu ambao hawakumjali sana, akazidi kwenda. Watu walikuwa wengi humo ndani, ilikuwa ni ngumu kumjua nani ni mhusika na nani sio, hata sare hawakuwa nazo.
Jack akasonga na alipokaribia mahali ambapo ndipo ameambiwa wenzake wapo, akawaona wanaume wawili waliobebelea bunduki wakiwa wamesimama hapo.
Wanaume hao walikuwa ni wanaume waliojaza misuli mwilini. Vichwa havina nywele. Mikononi wamebebelea bunduki, si ndogo kama yake.
Akafikiria cha kufanya, punde akaona ajitoe mhanga.

**

Ndani kulikuwa kimya na kiza. Marshall na Danielle hawakuwa na matumaini ya kutoka ndani ya chumba walichofungiwa kwani walikuwa chini ya ulinzi mkali na hata mikono na miguu imefungwa.
Ulikuwa ni mwisho ambao hawakuutarajia. Ilikuwa ni ajabu namna mambo yalivyogeuka.
Wakiwa wameegemea ukuta, Marshall alifikirisha akili yake lakini haikuwa na namna yoyote. Ndani kulikuwa ni kiza, ngumu kutambua hata ufa ukutani.
Sauti pekee waliyokuwa wanaisikia ilikuwa ni ile ya walinzi waliokuwa wamesimama mlangoni. Walinzi hao walikuwa wanateta na kucheka.
Marshall alishusha pumzi ndefu kisha akajaribu tena kuchomoa mikono yake kwenye nyira. Haikuwa inawezekana. Mikono ilikuwa imebanwa haswa.
Vidole vyake vilikuwa vimeminywa kiasi kwamba ilikuwa ni ngumu hata kutekenya kamba ya miguuni.
Alimwita Danielle akamuuliza kuhusu hali yake, mwanamke huyo akamwambia yu sawa. Akamuuliza kuhusu kamba yake ya mkononi. Vipi hata vidole vilikuwa vinasonga?
"Hapana!" Danielle akanong'ona. "Nahisi pia vimekufa ganzi!" akaongezea. "Sivihisi hata ninapovyisogeza."
Kabla Marshall hajatia tena neno, mara wakasikia sauti huko nje.
"Mkuu anawahitaji upesi!"
Sauti hiyo haikuwa ngeni kwao. Upesi waliitambua ni ya Jack Pyong!
"Mkuu?" Sauti ikauliza. "Mkuu gani unayemwongelea wewe?"
Marshall na Danielle wakatega sikio kwa umakini kuskiza.
"Mkuu ametuagiza tukae hapa mpaka atakaokuja yeye mwenyewe!" Mmoja akasema na kisha mwingine akatia neno upesi. "Wewe ni wa bloku gani? Mbona ni mgeni machoni?"
"Mimi?" Sauti ya Jack ikauliza. Akajiumauma kujibu. Hapo Marshall akatambua shughuli itaharibika muda si mrefu kama hatochukua hatua.
Endapo Jack ataendelea kuulizwa maswali atadhalilika na hatimaye kukamatwa ama kuuawa kabisa.
Basi upesi Marshall akakita mlango kwa miguu yake mizito kwa dhumuni la kuhamisha attention ya walinzi. Baada ya kubonda mlango kwa punde, walinzi wakajiuliza ni nini kinaendelea, kidogo mmoja akafungua kutazama.
Kilichomtokea kilichukua muda mfupi sana. Mlango ulikitwa kwanguvu kumbamiza mlinzi kichwa, Jack naye upesi akachomoa bunduki na kuwaonyeshea walinzi akiwaamuru waweke silaha zao chini kabla hajawamaliza.
Kwa usalama akawataka waingie mule chumbani kabla hajaonekana.
Lakini akiwa anazama humo, mabwana wawili wakawa wamemwona na wakapata shaka. Upesi mabwana hao wakatoa taarifa juu ya mashaka yao huku wakijongea kwenye eneo la tukio.
Walikuwa wamebebelea 'Sub-machine gun'.
Walipofika kwenye eneo la tukio, kwa tahadhari, wakapaza sauti ya kutaka waliomo ndani watoke. Walikuwa wanahofia kuingia ndani kichwakichwa ingawa mlango ulikuwa wazi kwa kiasi.
Jack alilazimika kuacha mlango huo vivyo kwaajili ya mwanga. Endapo angeufunga, hata walengwa wake asingewaona.
Humo ndani Jack akawatumikisha mateka wake kuwafungua kamba Marshall na Danielle. Marshall akafunguliwa kuwa huru lakini kabla Danielle hajamalizika, wale wanaume waliokuwa wamebebelea bunduki mlangoni wakaufungua mlango kwa teke na kunyooshea midomo ya bunduki ndani!
Alah!
Kabla hawajafanya jambo, Marshall ambaye alikuwa ameshabebelea bunduki ya mateka akawafyatulia risasi za kutosha na kuwalaza chini wafu!
Baada ya hapo akawamiminia risasi na wale walinzi mateka!
"Marshall kwanini umefanya hivyo?" Jack akaduwaa akiwatazama wale walinzi ambao washakuwa wafu. "Hakukuwa na haja ya kuwaua!"
"Jack!" Marshall akaita na kusema, "Ni aidha uue ama uuawe!"
Kisha akanyanyuka na kumtaka kila mtu abebelee bunduki kwani ana mpango.
"Inabidi tutimize lengo, nawatakie kheri kila mtu atoke akiwa hai!" Ilikuwa kauli yake ya mwisho kabla hajatoka ndani ya chumba.

**

King'ora kilikuwa kinalia kwenye jengo lote! Na mara kadhaa milio ya risasi ilikuwa inasikika huku na kule.
Bwana Ian akiwa amesimama na amekunja sura, aliingiza mkono wake mfukoni akatoa pakti ya sigara. Alichomoa sigara mbili akazitia moto na kuzivuta kwa pamoja.
Habari hii haikuwa nzuri kabisa! Mikono yake ilikuwa inatetemeka ingawa alikuwa ameweka bunduki mezani na mlangoni kuna walinzi.
Alikuwa anahofia, na kwa kiasi akajiona amefanya upumbavu kutowamaliza wakina Marshall pale alipopata nafasi. Alitukana mipango yote aliyokuwa ameainisha, aliiona yote ni batili kwa sasa.
Alimaliza sigara zake. Bado risasi zilikuwa zinaita huko nje.
Alishindwa kuvumilia zaidi akawafuata walinzi waliokuwapo mlangoni na kuwataka wamwongoze atoroke jengoni hapo.
"Mkuu, si salama kabisa," akasema mlinzi mmoja. "Hatujui adui yupo upande gani, bila shaka wamejigawa, itakuwa ni hatari!"
"Hata kukaa hapa ni hatari pia," akasema bwana Ian. Akawahimiza walinzi wake wafanye namna apate kuondoka hapo kabla mambo hayajaharibika zaidi.
"Sawa, mkuu, ngoja tuwasiliane na wengine kwa ajili ya backup!"
Basi kungoja hilo, bwana Ian akazama ndani na kuwasha sigara nyingine. Akaifyonza sigara hiyo kwanguvu kiasi cha kuimaliza ndani ya dakika moja tu!
Akawasha nyingine na kuiweka mdomoni, kabla hajaimaliza, akasikia mlio wa risasi karibu kabisa na yeye! Ilikuwa ni mlangoni kabisa kama masikio yake hayakukosea.
Upesi akadaka bunduki yake na kunyooshea mlangoni. Akasikia tena sauti ya risasi mara tatu! Akahofia zaidi. Akaita walinzi wake pasipo majibu.
Akiwa ametoa macho, akakakamaza mkono wake wenye silaha.
Punde mlango ukafunguka asione mtu. Akaita, kimya. Hajakaa sawa, mwili ukatupiwa mlangoni. Kwa woga akaufyatulia mwili huo risasi, kumbe ulikuwa ni mtego tu, alipokuja kutambua mwili huo ulikuwa ni wa mlinzi wake akawa tayari amekawia!
Marshall alitokeza na kumbangua risasi mbili za mabega, bwana huyo akadondosha silaha yake na kulegea kwa maumivu.
Basi Marshall na wenzake wakatokea na kumweka bwana huyo chini ya ulinzi. Na kwa kumtumia mateka wao kama chambo wakafanikiwa kutoka ndani ya jengo wakiwa salama.
Wakajipaki ndani ya gari na kutimka.

**

Saa sita mchana ...

"Nilipaswa kukuua wewe mbuzi!" Aling'aka Ian akiwa ameng'ata meno. Bwana huyo alikuwa amefungiwa kwenye kiti jasho linamchuruza.
Mikono yake haikuwa inafanya kazi sababu ya majeraha mabegani. Majeraha ambayo hayakuwa yamepata tiba tangu alipojeruhiwa usiku uliopita.
Mbele yake alikuwa amesimama Marshall na Danielle, Jack alikuwa amejitenga kwa kusimama nyuma kabisa.
Nguo za Ian zilikuwa zimelowana na kunuka damu.
"Ningekuchinja kwa mkono wangu mpuuzi wewe kisha nikakutupie mtoni uliwe na mamba!" Aliendelea kusema bwana Ian. Uso wake ulikuwa unaonyesha maumivu, mara kadhaa alikuwa anang'ata meno na kuachia.
"Najilaumu sana ku - spare pumzi yako! Lakini najua hautafika popote pale. Utakufa tu mshenzi wewe. Utaishi kama mbwa maisha yako yote!"
Marshall akatabasamu.
"Pole sana, Ian. Ulizoea kuwafanyia vivyo wenzako, leo imekuwa wewe! Niliapa sitakufa mpaka wewe ufe kwanza na ahadi yangu itatimia." Marshall alivyosema hivyo akanyoosha mkono wake, Danielle akampatia chupa ya 'truth serum' pamoja na bomba la sindano.
Marshall akanyonya dawa hiyo kuijaza sindanoni.
"Ninachotaka ni taarifa chache tu kisha mimi na wewe tutaachana kwa amani," akasema Marshall akimfuata bwana Ian.

***
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 16 & 17*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
"Pole sana, Ian. Ulizoea kuwafanyia vivyo wenzako, leo imekuwa wewe! Niliapa sitakufa mpaka wewe ufe kwanza na ahadi yangu itatimia." Marshall alivyosema hivyo akanyoosha mkono wake, Danielle akampatia chupa ya 'truth serum' pamoja na bomba la sindano.
Marshall akanyonya dawa hiyo kuijaza sindanoni.
"Ninachotaka ni taarifa chache tu kisha mimi na wewe tutaachana kwa amani," akasema Marshall akimfuata bwana Ian.
ENDELEA
Basi Marshall akamdunga sindano bwana Ian na kukaa kidogo kabla ya bwana huyo hajaanza kulewa na kupoteza uwezo wake wa kuficha mambo, akaanza kubwabwaja kama mtu asiye na akili.
Kila alichoulizwa akawa anamiminika pasipo kusita. Hapo ndipo Marshall akajifunza na kuhakikisha yale yote ambayo bwana Ian alikuwa anatuhumiwa nayo.
Mosi, bwana Ian akaeleza tangu Raisi alipokuwa anaumwa muda mfupi kabla hajapotea. Kumbe walikuwa wametia madawa kwenye kahawa ya Raisi kwa dhumuni la kumdhoofisha hali!
Akiwa pamoja na wenzake toka vitengo mbalimbali, bwana Ian akafanikiwa kuingia kwenye mawasiliano na Raisi wa UAE (United Arab Emirates) kwa ajili ya kumshinikiza Raisi wa Marekani akubali kutia saini kwenye makubaliano ya mfumuko-bei wa mafuta duniani.
Kwa kufanikisha hilo, wakateka familia ya siri ya Raisi na kuiweka chini ya angalizo na wakamtumia ujumbe Raisi kuwa ahudhurie kikao kitakachofanyika Ujerumani, kinyume na mipango yake.
Huko Ujerumani atapata kuona familia yake kuikagua usalama lakini pia atakuwa ni kura kubwa yenye uzito juu ya mwelekeo wa biashara ya mafuta na mabadiliko ya tabia nchi kwa mbali.
Kufanikisha kazi kubwa kama hiyo bwana Ian alikuwa na kikosi cha maajenti na maafisa wa vitengo mbalimbali. Ambao watumishi hao aliwapata kwa kuwalaghai na pesa ingali wengine akiwa anawatumikisha kwanguvu kutokana na kushikilia rekodi zao chafu.
Rekodi ambazo hawakuwa wanataka zijulikane.
"Ilibidi ni-fake kifo changu ili nipotee kabisa kwenye macho na akili ya watu. Nikachoma nyumba yangu na kuhamishia makazi yangu nchini Ujerumani kumaliza kazi huko," alisema bwana Ian akiwa anarembua. Mwili wake ulikuwa ni mhaba wa nguvu.
"Na vipi kuhusu Marietta?" Akauliza Marshall. "Alikuwa anajua yote hayo?"
"Hapana!" Akafoka bwana Ian kisha akaangua kicheko. "Utamwambiaje mwanamke siri kubwa kama hiyo? In fact, Marietta alikuwa ameshapitwa na wakati. Nilichokitaka alikuwa ameshanitimizia.
Na ilikuwa rahisi kabisa maana alikuwa anaendeshwa na chuki dhidi ya mumewe."
Kukatisha maongezi marefu, Marshall akamuuliza bwana Ian juu ya wapi alipo Raisi, nani anahusika na kumtokomeza asionekane mpaka siku hiyo.
Kabla ya kujibu, Ian akacheka kwanza na kufinya macho yake. Alitazama paa kwa macho yake ya kilevi alafu akajikuta akitikisa kichwa.
"Hapo ndipo story nzuri ilipoishia," akasema kwa kufinya uso wake. "Kila kitu kilikuwa poa kabisa. Kila kitu kilikuwa kwenye mipango lakini ghafla hali ikabadilika!"
"Unamaanisha nini kusema hivyo?" Marshall akadadisi.
"Haikuwa kama tulivyotaraji," Ian akabwatuka. "Nakumbuka mpaka Raisi anaenda kukwea ndege aende mahali tulipokuwa tunataka sisi, kila kitu kilikuwa sawa. Sawa na shwari.
Robo saa tu kabla mambo hayajajikwea vema, nikapokea simu kavu toka kwa ajenti Sam Kent. Sauti yake ilikuwa inakoroma na akisikika kwa chini kabisa.
Nakumbuka nilikuwa karibu na eneo la bunge la Ujerumani, barabarani ambapo magari yakipita, ikanibidi nisogee kando nipate kusikia vema.
Kitendo tu cha kufanya vivyo, nikawa tayari nipo nyuma ya muda. Alishakufa!"
Bwana Ian akaweka kituo kwanza akikoroma. Ni kama vile alikuwa akikumbuka kitu fulani cha thamani.
"Kidogo ndipo nikajifunza kwamba Raisi alikuwa amepotea, ndege yake imeanguka na hakuna aliyebahatika kuona hata mabaki ya mwili wake. Ajabu na kweli!
Tangu hapo hatujui mahali alipo ilhali tumefanya msako wa kila eneo tulilohisi huenda akawapo ama kujificha."
Marshall akashusha pumzi ndefu, akakuna pua yake na kuuliza, "kama mlikuwa amhusiki na kupotea kwa Raisi, kwanini mlikuwa mnaniwinda mniue?"
Ian akaguna kwa cheko, alafu akatabasamu na kutikisa kichwa taratibu kwa mbali. "Marshall, kilichotufanya sisi tukuwinde wewe ni sababu tatu. Mosi, ulihatarisha usalama wetu kwa kulivalia njuga hili jambo.
Ni wazi kama ungeendelea kuchimba zaidi ungetutia hatiani. Hatia ya kumteka ama kumpoteza Raisi, kitu ambacho hatukuwa tumekifanya.
Pili, kupata chochote kile ambacho umekifukua. Pengine kingetusaidia kujua wapi Raisi alipo maana nasi tulikuwa tunamsaka.
Tatu, ni kukutumia kama chambo cha kupotezea mwelekeo wa watu na jamii ya kiitelijensia. Endapo watu wangeamini kama wewe ndiye umehusika na kumpoteza Raisi basi sisi tungekuwa salama zaidi."
"Na vipi kuhusu pesa?" Akauliza Marshall. "Umewezaje kuongoza yote haya mpaka leo hii ingali makubaliano yako na Raisi wa UAE hayakuwa yametimia? Pesa ulitolea wapi?"
Bwana Ian akacheka na kusema, "Marshall, katika ulimwengu huu mtaji wako wa kwanza ni akili. Akili timamu. Bwana Khalifa aliamini ni sisi ndiyo ambao tumempoteza Raisi wa Marekani. Kwake hilo ni bado jema.
Na kwa kupata pesa zaidi za kutimiza maadhimio yetu, nikaingia naye makubaliano ya dola bilioni kadhaa ili nimpatie Raisi. Amekuwa akinilipa kidogo kidogo mpaka atakapotimiza pesa kamili ndani ya mwaka.
Kwa pesa hizo zikanitosha kabisa kufungua miradi kadha wa kadha lakini pia kuwekeza kwenye biashara ya mafuta."
Bwana Khalifa ni Raisi wa UAE.
Marshall akameza aliyoambiwa. Akageuza shingo yake kumtazama Jack na kisha Danielle kabla ya kurejesha uso wake kwa bwana Ian.
"Kwanini ulimuua O'neil? Na yeye alikuwa anahusika kwa chochote kile? - ama alikuwa ni hatari kwenu?"
Wamkumbuka bwana O'neil? Mwanaume aliyemkabidhi Marshall ujumbe wa Raisi kabla hajapotea? Ujumbe uliosomeka 'Nipo shidani'.
"O'neil?" Bwana Ian akauliza kana kwamba hakusikia.
"Ndio, bwana O'neil. Rafiki yake na--"
"Najua!" Akadakia bwana Ian. "Namjua bwana huyo na hata ujumbe alioupokea toka kwa Raisi. Ni mimi ndiye nilimletea."
"Alikutwa akiwa ameteswa na kuuawa akatupiwa msituni!"
"Ndio. Nilisikia hilo, linatia huruma sana kwani alikuwa ni mtu mwema na mtaratibu, lakini sikuhusika kumuua! Wala sikutoa agizo hilo.
Nimemwaga damu nyingi pengine, ila hiyo siyo kazi ya mikono yangu!"
Jambo hilo likampatia shaka bwana Marshall kwani hata Miss Danielle aliripoti kufanyiwa majaribio kadhaa ya kummaliza pasipo mafanikio na watu ambao hakuwafahamu.
Kama bwana Ian hakuwa anahusika nayo, ni nani mwingine?
Basi baada ya Marshall kumuuliza bwana Ian kila alichokuwa anataka, akampa nafasi pia na Miss Danielle na kisha mwishoni kabisa bwana Jack Pyong.
Maelezo yote hayo ya bwana Ian yalikiwa yanarekodiwa na pia video inachukuliwa. Kamera zilikuwa zipo nyuma ya wakina Marshall kiasi kwamba sura zao hazikwa zinaonekana, bali sauti tu kusikika.
Basi wakamwacha hapo bwana Ian na kwenda zao kupumzika.

**

"Ni nini unawaza?" Danielle alimuuliza Marshall kisha mwanamke huyo akanyonya juisi yake ndani ya glasi.
Marshall akashusha pumzi ndefu. "Kuna kitu kinanitatiza hapa," alisema akiwa anatazama kifikra.
"Najua, Marshall. Ila pumzisha kichwa sasa. Nikupatie juisi?"
"Ni ya kitu gani?"
"Zabibu."
"Umeitengeneza muda gani?"
"Aah muda si mrefu sana. Kweli ulikuwa umechoka, hukuniskia?"
"Hapana, sikuskia kabisa. Bila shaka hujatumia blender."
"Yah! Nimetumia ujuzi wangu tu lakini nimegongesha sana vyombo."
Marshall akatabasamu. "Ningependa kuonja."
Danielle akamletea juisi akawa anainywa pamoja naye.
"Unaonaje tukajipa likizo kidogo?" Danielle akauliza. "Naona kila tunapokaribia kikomo, dahari yaongezeka. Hatujui safari yetu hii itatupeleka mpaka wapi."
Marshall akatabasamu tena.
"Niambie wewe unafikiria nini?" Akauliza.

**

*SEHEMU YA 17*

"Unajua mimi napenda sana maeneo ya ufukweni," akasema Danielle kisha akatabasamu na kunywa juisi yake. "Ninapokuwa huko akili yangu hutulia kabisa. Upepo ule hufukuza matatizo yangu kichwani.
Na mwonekano wa bahari unanisahaulisha damu, mateso na vilio ninavyokumbana navyo nikiwa kazini."
Marshall akamtazama Danielle kwa undani kidogo. Kuna kitu alikuwa anawaza.
"Vipi Marshall?" Danielle akauliza. "Ni nini hiko unawaza? Haujapenda wazo langu?"
"Hapana," Marshall akajibu akitazama chini. Akatazama glasi yake ya juisi na kisha akayapeleka macho yake kwa Danielle.
"Ulikuwa astonishing sana usiku uliopita," Marshall alisema kwa sauti yenye kina. Macho yake yalikuwa yanamtazama Danielle kwa ndani. "Ilikuwa ni kama muujiza. Kila ulichofanya na kugusa kiligeuka kuwa dhahabu."
Danielle akacheka. Akanywa juisi yake lakini punde tena akacheka.
"Nini kimekufurahisha hivyo?" Marshall akauliza akiwa amekunja ndita na kutabasamu kwa wakati mmoja.
"Marshall, sikuwa najua kama una vituko kama Jack."
"Vituko?"
"Hujaona ulivyokuwa unaongea. Laiti ungejiona, ungecheka!"
"Kwanini? Nipo serious!"
"Sidhani. Hamna cha ajabu nilichokifanya Marshall. Nadhani ninahitaji muda wa kujifunza sana kutoka kwako."
"Mimi?"
"Ndio, wewe! Napenda sana maana wajua kufikiria kwa upesi nini cha kufanya. Nadhani ni talanta yako hiyo mbali na mafunzo."
Marshall akanyamaza akimtazama Danielle. Macho yake yalionekana makubwa kuliko awali.
"Marshall, kwanini unanitazama hivyo? Wataka kunimeza au?"
"Hapana, natafakari sana ya jana na yaliyopita. Pengine kweli tunahitaji mapumziko kidogo." Akasema Marshall kisha akagida juisi yake yote kukausha glasi akisimama.
"Itabidi unifundishe namna unavyoweza kuwaza mambo makubwa kwa njia nyepesi!" Marshall akaweka glasi mezani kisha akatabasamu na kwenda zake akiaga anaenda kulala kwani kichwa ni kizito.
"Ahsante sana kwa juisi. Tamu haswa!"
Alipokunja kona ya korido, akamkuta Jack hapo. Kumbe bwana huyo alikuwa amesimama hapo muda wote Danielle na Marshall wakiwa wanateta.
Jack alitabasamu tabasamu pana akikunja na kutikisa ngumi, "safi sana!" Akanong'ona. "Nakuaminia jembe langu! Hivyohivyo mpaka kieleweke."
Marshall akamtazama bwana huyo kwa macho ya mapuuzo. "Ndicho unachowaza kichwani mwako?" Marshall akauliza.
"Sh!-sh!-sh!" Jack akamsihi aongee kwa sauti ya chini. "Sio mpaka tusikike sasa na wewe!"
"Jack, hauna kazi ya kufanya?" Marshall akauliza.
"Ninazo," Jack akajibu. "Sasa ningeendaje pale kufanya kazi, si ningeharibu maongezi yenu. We mwenyewe umeona mood mliyokuwa nayo pale!"
Marshall akapuuzia na kuchukua zake hatua kuelekea chumbani.
"Nakukubali sana mwanangu!" Jack akabwatuka akitabasamu. Marshall asimjali tena akazama zake ndani ya chumba na kufunga mlango.
Usiku huo Jack akakesha kwenye tarakilishi yake akipembua na kuchambua mambo.
Kesho kwenye majira ya saa nane mchana, Danielle akapiga simu kumwambia Marshall kwamba Miss Marietta amesafiri. Amepata taarifa kuwa mwanamke huyo ameondoka zake nchini.
"Unajua wapi ameelekea?" Akauliza Marshall.
"Sijajua," akajibu Danielle. "Lakini nadhani ni Morocco."
"Kwanini wadhani huko?"
"Ndipo alipoenda wakati uliopita. Sina uhakika lakini."
Baada ya maongezi hayo machache, simu ikakata.
Marshall akakaa kwenye kiti akiwaza, simu mkononi. Alipomtazama Jack Pyong akamwona mwanaume huyo akiwa anakodolea tarakilishi. Yu bize haswa.
"Jack," Marshall akaita na kuuliza "kuna kitu umepata?"
Jack akiwa ametabasamu hakuwa anasikia. Aliendelea na kazi yake ya kukodolea tarakilishi na kubofya.
"We Jack!" Marshall akapaza sauti. Mara hii Jack akamsikia.
"Vipi umepata kitu?"
"Hamna!" Jack akajibu kisha upesi akaendelea kubofya akiwa anatabasamu.
"Mbona umefurahi hivyo ndugu, kipi kimekufurahisha?"
"Nachat na Kelly!" Jack akajibu pasipo kumtazama Marshall.
"Kelly?"
"Ndio, Kelly!"
"Yule mwanamke wa New Zealand tuliyekutana naye Hong Kong?"
"Yah!"
Marshall akaamka upesi na kumsogelea Jack. Mwanaume huyo alikuwa kwenye mtandao wa Facebook akiteta na mwanamke Kelly.
"Sikia, Marshall, mimi nimekuachia Danielle. Huyu Kelly atakuwa wangu sasa."
"Yuko wapi?" Marshall akauliza.
"Chuoni," Jack akajibu. "Kwani sikukuambia anasoma Harvard?"
"Sikumbuki," akasema Marshall akisoma jumbe kwenye kioo.
"Anataka kuonana na mimi leo usiku."
"Umekuwa ukichat naye kwa muda gani sasa?"
"Si muda mrefu sana. Wiki iliyopita!"
"Kwahiyo utaenda kuonana naye?" Marshall akauliza akimtazama Jack.
"Ndio. Nitakula naye dinner," Jack akasema akitabasamu. Alikuwa amefurahi mno.
Lakini Marshall alikuwa anatamani kupitia zaidi jumbe za Jack na Kelly.
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 18 & 19*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
"Sikumbuki," akasema Marshall akisoma jumbe kwenye kioo.
"Anataka kuonana na mimi leo usiku."
"Umekuwa ukichat naye kwa muda gani sasa?"
"Si muda mrefu sana. Wiki iliyopita!"
"Kwahiyo utaenda kuonana naye?" Marshall akauliza akimtazama Jack.
"Ndio. Nitakula naye dinner," Jack akasema akitabasamu. Alikuwa amefurahi mno.
Lakini Marshall alikuwa anatamani kupitia zaidi jumbe za Jack na Kelly.
ENDELEA
Ikiwa ni usiku, mandhari haya yakawa yamenawiri kwa mwanga toka kwenye kwenye taa zilizonakshiwa kwa urembo. Taa hizo zilikuwa za rangi mbalimbali mathalani bluu, nyekundu na manjano.
Mahali palikuwa panavutia haswa. Viti na meza vilikuwa vichache vikipeana nafasi ya faragha. Kwa mbali wimbo ulikuwa unapiga, wimbo wa mahadhi ya 'country' akiwa anaimba mwanamke maarufu wa miondoko hiyo, kwa jina Dolly Parton.
Jack aling'aza macho yake, hakuwa amefika hapo muda, ndani ya muda mfupi mhudumu ambaye amevalia sare nadhifu alifika na kumwonyesha tabasamu pana.
"Naweza kukusaidia?"
"Oh! Ndio, tafadhali waweza niletea sharubati ya matufaha tafadhali?"
"Bila shaka!"
Mhudumu akaenda zake na baada ya punde akaleta glasi kubwa iliyojaa sharubati ya baridi. Jack akashukuru na kisha mhudumu akaenda zake baada ya kuonyesha tabasamu.
Jack akakaa hapo kwa kama robo saa mbele ndipo Kelly akaonekana. Alifurahi sana kumwona. Alimkarimu mwanamke huyo kwa furaha kisha mhudumu akaja na mwanamke huyo kuagiza kinywaji laini pia.
"Ni muda mrefu sasa!" Alisema Kelly. "Unaendeleaje lakini?"
"Niko poa," Jack akajibu akipandisha mabega. "Maisha yamekuwa yakitutenganisha, si unajua?"
"Ni kweli!"
Kukawa kimya kidogo. Kelly akanywa mafundo mawili kisha akamtazama Jack aliyekuwa anatazama glasi yake. "Jack, nimesikitishwa sana na kile ulichonambia. Pole, ndiyo maisha."
Jack akatabasamu kiuongo.
"Yah! Ni kweli. Lakini sijutii sana."
"Kweli? Ni kazi gani sasa unafanya kuingiza kipato?"
"Aahm, sifanyi kazi yoyote kwa sasa."
"Kabisa? Sasa unaishije?"
Jack akatabasamu. Sasa hivi tabasamu lake lilikuwa la kweli.
"Usijali, utajua kadiri muda unavyosonga."
"Ni vibaya kujua saaa hivi?"
"Hapana, ila si muda muafaka."
Kelly akanywa juisi yake na kunyamaza.
"Nadhani sijakukwaza," Jack akasema kwa tahadhari.
"Hapana! Haujanikwaza!" Kelly akajibu kisha akatabasamu kana kwamba ameshangazwa na swali hilo.
"Unajua mimi si mzoefu sana wa wanawake!"
"Kivipi? Umekuwa kwenye uchumba kwa muda mrefu, ama ulin'danganya?"
"Hapana. Ni kweli kabisa. Mimi na vio tulidumu kwa muda mahusianoni lakini namna ambavyo mahusiano yetu yalivyoishia inanifanya niamini hiko nilichokisema. Mimi si mzoefu wa wanawake."
"Kumaanisha nini Jack?" Akauliza Kelly. Sauti yake ilikuwa laini na nyororo. Alimtazama Jack machoni kwa sura iliyoguswa kihisia.
"Nilifanya kila jambo lililopo ndani ya uwezo wangu kumfurahisha Vio lakini vyote hivyo havikutosha. Bado alikuwa na mwanaume mwingine. Sijui ni namna gani alikuwa anataka. Sikujua anahitaji nini!"
"Usihuzunike Jack. Kila kitu hutokea kwa sababu, naamini hivyo."
Kukawa kimya kidogo. Ni Jack alikuwa amatafakari jambo kichwani. Kelly alimtazama mwanaume huyo na kumuuliza kwa sauti ya chini, "nini Jack?"
Kwa kumtazama tu ungebaini Jack alikuwa ameguswa kihisia. Uso wake ulibadilika, macho yake yakapooza.
"It's ok, Jack," Kelly akasema akimshika Jack bega. "Huna haja ya kunung'unika vivyo kila uchwao. Acha lililopita liende."
Jack akanywa juisi mafundo manne makubwa kukausha glasi yake. Angalau moyo wake ukawa umetulia sasa. Akavuta hewa ndefu kwa pua yake na kuishusha.
"Samahani, Jack. Sikujua kama tutafikia huku!" Kelly akaomba radhi.
"Usijali," Jack akasema na punde akatazama kumtafuta mhudumu. "Unakula nini?" Akamuuliza Kelly. Muda si mrefu mhudumu akaja wakaagiza chakula na kula huku wakiendelea kupiga soga.
Walifurahi sana.
Lakini ghafla furaha yao ilifikia kikomo pale Kelly alipomuulizia bwana Marshall. Jack hakupenda hilo jambo. Aliona kama bado mwanamke huyo ametwaliwa na Marshall kichwani.
Kitu hicho kilijidhirihisha tangu Kelly alipoonana na Marshall huko Hongkong. Kipindi hiko halikuwa jambo kubwa kwa Jack Pyong lakini sasa hivi lilikuwa linamuumiza.
Kwa kiasi tayari alikuwa ameshamuingiza mwanamke huyo kwenye korido ya moyo wake.
"Sikudhamiria kukuudhi, Jack!" Alijitetea Kelly. "Sikutaraji kama ningekukwaza. Nisamehe."
"Usijali. Ni ujinga wangu, nilipaswa kujizuia."
"Nilitaka tu kufahamu hali yake. Naamini utakuwa unajua yupo wapi."
Jack akanyamaza kimya asitie neno. Badala yake akaendelea kutafuna. Basi Kelly kuona hivyo, akaona aachane na hiyo mada.
Wakala na kama baada ya nusu saa wakaongozana kutoka eneo hilo. Jack alilipia 'bill' na pia akamkarimu Kelly atumie usafiri wake kumpeleka huko anakokaa.
Pasi na tatizo, Kelly akajumuika na Jack kwenye safari iliyogharimu masaa mawili mpaka kufikia kikomo. Mbele ya nyumba kubwa ghorofa, Jack akasimamisha gari lake na kumtazama Kelly.
"Nadhani tumefika!"
"Yah! Nashukuru sana Jacky. Nashukuru sana Jack, umekuwa mkarimu sana kwangu."
"Usijali. Ni kawaida tu japo naumia sana kukuacha uende."
"Kweli?"
"Yah. Nilishajisahau kwa muda mchache niliokuwa na wewe. Nilidhani ni jambo la kudumu!"
Kidogo wakatazamana. Kelly akacheka kwa haya.
"Ulikuwa unasemaje, Jack?" Akauliza kwa sauti ya puani. Kope za macho yake zilikuwa zimelegea.
"Sina usemi. Inabidi niamini kila lenye mwanzo lina mwisho wake."
Kelly akatabasamu. Akamshika Jack mkono akiwa anamtazama mwanaume huyo. Kidogo Jack akapoteza akili.
"Nimefurahi sana kuwa na wewe. Umeniondoa upweke wangu wa siku nzima!"
"Kwani ulikuwa mpweke?"
"Ndio," Kelly akajibu akikuna kichwa chake kwa kucha ya kidole cha kati. "Nadhani nimezoea sasa japo kuna muda inazidi. Nimekuwa nikiishi peke yangu tangu nilipokanyaga Marekani!"
"Ndiyo maana hata lafudhi yako bado haijabadilika!" Jack akatania, wakacheka. "Sasa naweza kuja kukuondolea upweke kwa leo?" Jack akauliza. Alijitahidi macho yake yamtazame Kelly.
Kelly akatabasamu.
"Bwana, mbona itakuwa mapema sana Jack?" Akauliza kwa sauti ya puani. Uso wake ulisaliti maneno yake.
***

Mlango ulifunguka akaingia Kelly.
"Utaniwia radhi, sebule yangu ipo hovyo sana!"
Punde naye Jack akazama ndani. Macho yake yalipekua sebule kwa upesi. Ilikuwa ni sebule yenye samani za kawaida na kwa chini kulikuwa makaratasi kadhaa hususani ya biskuti na chokoleti.
Runinga ndogo ukutani. Picha kadhaa za Kelly ukutani na kati ya picha hizo kuna mojawapo ilikuwa ni ya bendera ya New Zealand. Sofa mbili za ngozi na zulia rangi ya kahawia.
Jack akatulia hapo sebuleni na Kelly akaingia ndani. Kelly aliporejea, wakakaa pamoja kwa kama lisaa hivi kabla watu hawa hawajajikuta wakianza kutomasana, kushikana na kujitupia kitandani.
Walifanya lile tendo na kuishia kulala fofofo. Katikati ya usingizi, simu ya Jack ikaita sana. Alikuwa ni Marshall anampigia.
Bwana huyo akiwa ameketi na Danielle alikuwa amejawa na mashaka juu ya Jack, rafiki yake. Hakuwa amesema kama atalala huko bali atarejea.
Simu iliita mara nne, mara Kelly akaamka na kuitazama. Akaona ni jina la Marshall! Ubaya simu hiyo ilikuwa inaonyesha pia na namba ya mpigaji.
Basi upesi Kelly akanakili namba ya Marshall kwenye simu yake kisha akaendelea kulala.
"Yani huyu fala hapokei!" Marshall akalalama. Alitupia simu yake chini akiwa na uso wa tafakuri.
"Pengine atakuwa amelala huko. Usihofu sana," Danielle akasema akimshika Marshall bega.
"Dani," Marshall akaita na kuuliza, "unajua password ya tarakilishi?"
"Ipi? Ile anayotumia Jack?"
"Yah! Nilijaribu kuifungua lakini sikufanikiwa."
"Naijua."
"Naomba unifungulie."
Danielle akamfungulia Marshall tarakilishi na upesi bwana huyo akazama kwenye jumbe kati ya Jack na Kelly.

HUKO ATAONA NINI?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom