Siku za mwisho za Mpakanjia
Mwandishi Wetu
Kifo cha mfanyabiashara maarufu Mohamed Mpakanjia ambaye pia alikuwa mume wa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Marehemu Amina Chifupa, kimeibua majonzi makubwa kwa wengi wanaomfahamu huku wengine wakijaribu kuelezea siku za mwisho za mpendwa wao huyo.
Kwa mujibu wa baadhi ya wale waliokuwa wakimfahamu vya kutosha marehemu Mpakanjia, ni kwamba mwishoni mwa siku za uhai wake, alijtahidi kuzidisha ibada, huku akiswali sana pale katika Msikiti wa Masjid Noor, uliopo Sinza Palestina Jijini.
Akizungumza na Alasiri, mmoja wa waumini wanaoswali mara kwa mara katika msikiti huo wa Masjid Noor, amesema Mpakanjia alionekana kuzidisha ibada na kufanya mambo mengi mema.
Amesema muumini huyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Mohamed kuwa hata Ijumaa iliyopita, Mpakanjia aliswali naye kwenye safu moja pale Masjid Noor na kwamba alimshangaza zaidi kwani aliomba sana dua na kulala kwenye zulia.
"Kwakweli kati ya walioguswa sana na kifo chake, mimi ni mmojawapo kwa sababu nilikuwa naye kwenye safu moja wakati wa swala ya Ijumaa iliyopita," akasema muumini huyo.
Akieleza zaidi, akasema kuwa wakati mtoa mawaidha wa siku hiyo ya Ijumaa msikitini hapo ambaye ni Sheikh Hashim Rusaganya, Mpakanjia alionekana akisikiliza kwa umakini, kabla hajamaliza kuswali swala nyingi za sunna na hatimaye kuanza kujinyenyekeza mbele za Muumba, kisha akaomba sana dua.
"Nilimshuhudia mwenyewe jinsi alivyokuwa akiomba dua kwa Allah (Mwenyezi Mungu)... alinyoosha mikono yake, akawa kama anayefumba macho na kuomba sana," akasema.
"Baada ya hapo, alilala chali msikitini humo na kuendelea kuomba huku Sheikh Rusaganya akiendelea kutoa mawaidha... aliendelea kulala huku mikono ikiwa kifuani mwake hadi wakati wa swala ya Ijumaa ndipo akasimama na kuswali kama waumini wengine ," akaongeza.
Akasema baada ya swala, yeye alitoka msikitini hapo na kumuacha Mpakanjia akiendelea na maombi yake msikitini.
"Kwakweli nilishangaa jana kusikia kuwa amefariki... inasikitisha sana," akasema.
Aidha, taarifa nyingine zinaeleza kuwa siku chache kabla ya umauti, Mpakanjia alishirikiana na familia yake katika kutoa mchango mkubwa wa kufanikisha mashindano ya usomaji Qur-an yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Starlight Jijini ambapo washindi walitunukiwa vitita vikubwa vya pesa.
Mpakanjia alifariki jana saa 8:30 mchana katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo ambako alilazwa kuanzia saa 5:00 asubuhi, hiyo hiyo jana.
Inaelezwa kuwa awali, marehemu alikuwa akisumbuliwa na homa ya matumbo (typhoid).
Pia inadaiwa kuwa figo yake moja ilishindwa kufanya kazi na kusababisha umauti wake.
Aidha, kwa mujibu wa kaka wa marehemu, Abdul, mazishi yake (Mpakanjia) yalitarajiwa kufanyika leo mchana, pale kwenye makaburi ya Kisutu ambapo mamia ya watu wanatarajia kuhudhuria, akiwemo Mbunge wa Temeke Abbas Mtemvu na Mbunge wa Mbinga Magharibi, Kapten John Komba.
ALASIRI