Nani watakaopewa jukumu la kumchunguza Mkapa? Polisi, TAKUKURU, au kamati maalum ya Wabunge wa CCM na wale wa kutoka upinzani? Je, wananchi tutakuwa na imani na watakaopewa jukumu hilo hasa ukitilia maanani mafisadi wote wa EPA waliokupua shilingi 288 bilioni toka BoT bado wanapeta mtaani na wala hakuna dalili ya wao kufunguliwa mashtaka?
Posted Date::4/26/2008
Serikali ya Rais Kikwete yawasha moto kumchunguza Rais Mstaafu Mkapa
Na Mwandishi wetu
Mwananchi
SERIKALI ya Rais Jakaya Kikwete imeamua kutofautiana na zile za marais waliomtangulia kwa kutamka uamuzi mzito ambao haukuwahi kufanyika tangu Tanzania ipate uhuru, kwa serikali yake kuamua kuchunguza kashfa ya Rais Mstaafu , Benjamin Mkapa.
Uamuzi huo umetoa mwelekeo mpya wa serikali ya Kikwete kwamba sasa ameamua kufumba macho na kuwatosa watu muhimu kwake wanaotuhumiwa kwa ufisadi bila ya kujali wana nyadhifa gani.
Kitendo cha kuachia ngazi mawaziri wanne katika kipindi cha miezi mitatu kutokana na kashfa za ufisadi na kuanza kumchunguza Mkapa kinaonyesha wazi kuwa sasa shikizo la wananchi na nchi wahisani kuhusu vitendo vya ufisadi limemfanya Kikwete abadili mwelekeo wa utendaji wake wa kazi.
Hata hivyo, mtihani mkubwa ulioko mbele yake ni namna atakavyoendesha uchunguzi dhidi ya Mkapa na endapo atabainika amehusika kutumia madaraka vibaya na kukiuka maadili ya uongozi akiwa Ikulu, je ataweza kumfikisha mahakamani?
Mtihani utakuwa mgumu kwa Kikwete kutokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuweka vipengele vinavyomlinda mno rais aliyepo madarakani au ambaye amestaafu.
Kwa mujibu wa katiba ibara ya 46 (3) wakati wote Rais atakapokuwa bado ameshika madaraka yake, haitaruhusiwa kufungua mahakamani shauri kuhusu jambo lolote alilotenda au alilokosa kulitenda yeye binafsi kama raia wa kawaida ama kabla au baada ya kushika madaraka ya urais, ila tu kama angalau siku 30 kabla shauri kufunguliwa mahakamani, rais atapewa au ametumiwa kwanza taarifa ya madai kwa maandishi kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge na taarifa hiyo ikiwa na maelezo kuhusu chanzo cha shauri hilo, kiini cha madai yenyewe, jina la mdai na anwani ya mahali anapoishi na anapaswa aliainishe jambo analodai.
"Isipokuwa kama ataacha kushika maradaka ya urais kutokana na masharti ya ibara ya 46 (A) (10), itakuwa ni marufuku kushitaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la kumdai mtu aliyekuwa anashika madaraka ya rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo alilofanya yeye kama rais wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya rais."
Hata hivyo, Bunge linaweza kumshitaki rais kama ametenda makosa ambayo yanavunja katiba au sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
Kwa mujibu wa katiba hiyo, kabla ya Bunge kumshitaki, taarifa ya maandishi iliyotiwa saini na kuungwa mkono na wabunge wasiopungua asilimia 20 ya wabunge wote itawasilishwa kwa Spika siku 30 kabla ya kikao ambapo hoja hiyo inakusudiwa kutolewa bungeni, ikifafanua makosa aliyotenda na ikipendekeza kuwa kamati maalum ya uchunguzi iundwe ili ichunguze mashtaka yaliyowasilishwa dhidi ya rais.
Iwapo uchunguzi wa serikali utabaini kuwa Mkapa anahusika katika kashfa ya kutumia vibaya ofisi ya umma alipokuwa madarakani, kuanzisha kampuni binafsi kinyume cha sheria ni wazi kwamba itabidi katiba ya nchi ifanyiwe marekebisho ili iwe rahisi kwa rais mstaafu kushtakiwa kwa makosa aliyoyafanya akiwa madarakani.
Hata hivyo, kama wabunge wakiamua kufuata taratibu hizo na kama serikali haitaweka vikwazo, Mkapa anaweza kushtakiwa na kuhukumiwa kutokana na matendo ambayo yatabainika kayafanya wakati akiwa rais na ambayo ni kinyume na maadili ya uongozi.
Uchunguzi uliofanywa unaonyesha kuwa tayari baadhi ya wabunge wamejipanga sawa kuhakikisha wanaendelea kutoa hoja binafsi za kuwabana vigogo wote waliohusika katika ufisadi.
Wachunguzi wa mambo ya kisiasa wanaona hatua hiyo ya Kikwete ni ya kijasiri na inapaswa kufanyika wakati huu ambao nchi imekumbwa na ufisadi wa kutisha.
Hata hivyo, baadhi ya watu wanaona kwamba hatua ya kumchunguza na kisha kumchukulia hatua Rais aliyeondoka madarakani ni nzuri lakini pia Rais aliyepo madarakani naye anapaswa kuwa msafi ili anayekuja asije kumwigiza naye katika matatizo.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wiki hii aliliambia Bunge mjini Dodoma kuwa serikali ina taarifa za tuhuma hizo, ambazo alisema zimeibuka kwa nguvu katika siku za hivi karibuni.
Kutokana na hali hiyo, alisema serikali inazichunguza ili kufahamu ukweli wa kilichotokea na kwamba ukipatikana ushahidi wa kutosha, hatua zitachukuliwa kwa maslahi ya taifa.
Kauli hiyo ya Pinda ambayo ni ya kwanza kutolewa na serikali tangu kuibuliwa kwa tuhuma hizo dhidi ya Mkapa na aliyekuwa Waziri wake wa Nishati na Madini, Daniel Yona, inafuatia maswali yaliyoulizwa na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni, Hamad Rashid Mohamed.
Katika swali lake la msingi, Hamad ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF), alisema Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ya Mwaka 1995, inamzuia mtumishi yeyote wa serikali kutumia ofisi ya umma (serikali) kufanya shughuli binafsi.
Sasa Mheshimiwa Waziri Mkuu, kuna taarifa kwamba, Mheshimiwa Rais Mstaafu Mkapa na kiongozi mwingine wa serikali ya awamu ya tatu, walitumia ofisi zao kuanzisha kampuni binafsi je, serikali inasema nini juu ya hilo? aliuliza.
Baada ya Pinda kujibu swali hilo, Hamad aliuliza swali la nyongeza akisema: "Kwa kuwa tuhuma dhidi ya watu hao, ni za muda mrefu, BRELA (Kitengo cha serikali cha Kusajili Makampuni), inalifahamu suala hilo na kuna watu wengine waliobainika kutenda kosa kama hilo walichukuliwa hatua. Kwa nini serikali imekuwa na kigugumizi kuwafikisha mahakamani watu hao?"
Waziri Mkuu alisisitiza kuwa kinachofanywa na serikali hivi sasa ni kuangalia iwapo kuna jinai katika tuhuma zinazowakabili watu hao na kwamba, itakapojiridhisha itachukua hatua zinazotahili kwa maslahi ya nchi.
Februari mwaka huu, mawaziri watatu akiwamo waziri mkuu, Edward Lowassa walijiuzulu kutokana na kukumbwa na kashfa ya mkataba wa kampuni kuzalisha umeme wa dharura ya Richmond na hivi karibuni, Waziri wa Miundombinu, Andrew Chenge amejiuzulu baada ya kutuhumiwa kuwa na dola za Marekani milioni moja ambazo zimewekwa katika Kisiwa cha Jersey ambazo zinahusishwa na ununuzi tata wa rada.