Informer
JF-Expert Member
- Jul 29, 2006
- 1,582
- 6,627
- Adai kuna mpango wa kumuua mumewe kwa sumu, uchawi
MWANDISHI WETU | Kulikoni | Sep 21, 2012
MCHUMBA wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Mandeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, Josephine Mushumbusi, ametoa madai mazito kwa vyombo vya dola akidai kuwapo kwa mpango wa kumdhuru mumewe.
Josephine amekataa kuingia undani wa madai hayo, pamoja na kukiri kuyaweka katika mtandao kupitia ukurasa wake wa Facebook, kwa maelezo kuwa yuko nje ya nchi kwa sasa.
Madai hayo yanataja baadhi ya watu wazito ndani ya serikali, ambao wanadaiwa kuwa katika mpango huo, lakini baadhi ya wanaotajwa kutokuwapo kiunganishi na tuhuma husika.
Katika madai yake, mama huyo machachari, ameandika kwamba kumekuwa na vikao vya watu ndani ya serikali vyenye lengo la kutaka kummaliza Dk. Slaa, kwa njia yoyote ile.
Wanaamini kwamba Slaa ndiye mzizi katika Chadema na anaweza kuiangusha CCM 2015. wameona mazingira ya kuchakachua 2015 ni magumu sana, anaeleza.
Anaendelea kwa kudai kwamba njia pekee ambayo imebakia ni kuwaondoa wagombea ambao ni tishio na wenye ushawishi wa kuhamishia wanasiasa wengine walio CCM kwenda Chadema.
Katika madai yake hayo, Josephine amewataja watu ambao wamekuwa wakitajwa mara kwa mara wakihusishwa na matukio ya utesaji kukiwa na jina moja jipya. Majina tunayahifadhi kwa sasa.
Kama hadithi ama sinema, madai hayo yanawataja watu mbalimbali walioathiriwa na matukio yanayoituhumu serikali kuhusika.
Katika hali ya kutatanisha, Josephine anahusisha madai ya kuwapo hata ushirikina ambao utatumika kumdhuru Dk. Slaa.
Kwenye kikao chao cha kidhalimu, mmoja wao akapendekeza matumizi ya ama uchawi au sumu inayoua taratibu. Huyu aliyependekeza anahofia kuwa njia yoyote itakayofanana na nyingine italeta kelele na dunia nzima itagundua. Anajaribu kuwashawishi wenziwe waachane na hiyo, isipokuwa watumie njia hizi mbili mbadala; sumu au uchawi, anaeleza Josephine na kuendelea;
Jamaa wanamiliki wachawi wengi sana na wachawi hawa wako makundi mawili. Kundi la kwanza ni lile linalotumika kulinda viongozi na huwa linafanya kazi kila wiki mara moja. Kundi hilo liko kwenye payroll ya serikali.
Anaendelea: Kundi la pili ni lile la wachawi waliotaka kumuua .... (anataja jina la kiongozi) kipindi fulani. Kundi hili liko katika mazungumzo na ... (anataja kiongozi) kwa ajili hiyo.
Imeelezwa na mama huyo kwamba mkakati huo unapangwa kutekelezwa baada ya Dk. Slaa kurejea kutoka nje ya nchi.
Katika madai yake hayo, Josephine anataja hadi namba za gari ambalo linaelezwa kutumika katika mkakati huo unaofanana na sinema ya Kinigeria.
Mbali ya Dk. Slaa, mama huyo anadai kwamba kuna mpango wa kuwadhuru wabunge ambao wanaamini hawahongeki kifedha.
Hata hivyo, viongozi mbalimbali wa serikali na watu mbalimbali, wameelezea tuhuma hizo kama njia ya kumchota akili Dk. Slaa ili kumuondoa katika hoja za msingi na hata kumtisha asirejee nchini na hazina ukweli wowote.
Hizi tuhuma zinachanganya sana maana inaonekana baadhi ya wanaotajwa ni wale wale wanaotajwa katika tuhuma nyingine na hii inaonesha kwamba ni madai ya kupikwa na watu wenye nia ya kutaka kummchezea akili Dk. Slaa na pengine kumfanya asiaminike katika jamii, anaeleza kiongozi mmoja mstaafu serikalini.
Habari zimethibitisha kwamba vyombo vya dola vimeanza kufuatilia kwa karibu taarifa hizo na huenda ikatolewa taarifa rasmi hivi karibuni, pamoja na kutokuwapo kiongozi aliyekuwa tayari kuzungumzia tuhuma hizo.