BARD AI
JF-Expert Member
- Jul 24, 2018
- 3,379
- 8,124
Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo amesema kupanda kwa Bei ya Data hakukuwa na utaratibu mzuri na pia huduma imekuwa mbovu kwa gharama kubwa zaidi, jambo ambalo linaua ndoto za wabunifu wengi wanaotumia Mtandao.
Melo amesema hayo wakati akijibu utetezi wa Bei Mpya za Vifurushi uliotolewa na Emmanuel Manase, Mkurugenzi wa Mambo ya Kisekta kutoka TCRA aliyesema Bei za Vifurushi vya Data ni ndogo na stahimilivu na zimetokana na maboresho ya huduma.
==========
TCRA yatetea bei vifurushi vya data, Melo apinga
Mkurugenzi wa Mambo ya Kisekta kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Emmanuel Manase amesema bei za vifurushi vya data zimeongezeka baada ya mamlaka hiyo kuingilia kati huduma zinazotolewa na kampuni za simu ili kuboresha huduma hizo kwa gharama ndogo ambayo ni stahimilivu.
Manase ameyasema hayo leo Alhamisi Agosti 24, 2022 jijini Dar es Salaam wakati majadiliano yaliyofanyika wakati wa Tuzo za Vijana Wanaochipukia za mwaka 2022.
Amesema kati ya mwaka 2019 na 2020, bei ya vifurushi vya data zilikuwa chini na mitandao ya simu ilikuwa na ushindani mkali katika kuuza vifurushi hivyo.
Hata hivyo, amesema TCRA iliamua kuingilia kati baada ya kuona huduma zinakuwa mbovu kama vile kasi ndogo ya mtandao na vifurushi kwisha mapema.
"Baada ya kuona hivyo, tuliwaita watoa huduma tunazungumza nao, wakatuambia wanauza bei ndogo lakini hawapati faida, kwa hiyo hata uendeshaji wao unakuwa mgumu. Tukasema kwanini tusiwe na huduma ya uhakika kwa bei ambayo haitaumiza upande wowote ili huduma ziwe bora wakati wote," amesema Manase.
Amesisitiza Tanzania ni moja ya nchi barani Afrika ambazo vifurushi vya data vinauzwa bei rahisi.
Hata hivyo, kauli hiyo imepingwa vikali na Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo ambaye amesisitiza sasa huduma ni mbovu zaidi na kwa gharama kubwa zaidi.
"Naomba kupingana na mkurugenzi hapa, niseme tu kwamba kupanda kwa data hakukuwa nanutaratibu, yaani sasa huduma ni mbovu kwa gharama kubwa zaidi.”
“Kwa hiyo, naomba mkakae na kuliangalia tena jambo hili. Kwanza kunaua ndoto za wabunifu wengi wanaotumia mtandao," amesema Melo.
Mwananchi