Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola amewataka wachezaji wake kuepuka mipira ya adhabu karibu na goli lao na kutopaki basi wakati watakapowakabili watani zao wa jadi Manchester United kwenye Uwanja wa Old Trafford leo Jumapili.
Guardiola amewaonya wachezaji wake kuacha kutengeneza mazingira ya mipira ya adhabu katika mchezo huo muhimu zaidi kwao.
Kocha huyo Mhispania, anahofia Man United inaweza kupata mabao kupitia mipira ya adhabu endapo Man City haitakuwa makini.
Man United ina wachezaji wengi warefu kulinganisha na Man City. Romelu Lukaku, Nemanja Matic, Chris Smalling na Zlatan Ibrahimovic ni wachezaji warefu ambao watakuwa tishio kwa Man City.
Kiungo wa pembeni aliyerudishwa kucheza beki wa kushoto Ashley Young amepata umaarufu kwa mashuti ya mpira wa adhabu.
Inakadiriwa kuwa watu zaidi ya bilioni moja watakuwa wakitazama pambano la Manchester United dhidi ya Manchester City.
Kiungo wa Manchester United, Paul Pogba ataukosa mchezo huo akitumikia adhabu yake ya kufungiwa mechi tatu baada kuonyeshwa kadi nyekundu katika pambano lililopita dhidi ya Arsenal baada ya kumkanyaga mlinzi wa kulia, Hector Bellerin na pia atazikosa mechi dhidi ya Bournemouth na West Brom.
Wengine watatu watakaokosa mechi hiyo ni mabeki watatu, John Stones na Benjamin Mendy wa Manchester City na Eric Baily wa Manchester United wote hawa ni majeruhi.