SEHEMU YA NANE
SEHEMU YA NANE
Lile kundi lilizidi kunighasi bila kunipa nafasi ya kunisikiliza. Mwanzoni walisema wanaufuata mwanga ili wanitambue vizuri lakini sasa waliupita ule mwanga na kukifuata kichochoro walichokijua wao. Kuna lugha zao waliambiana na sikuweza kuzikumbuka wala kuambulia chochote!!
Baada ya kukifikia kichochoro kile mara ghafla mimi na yule mzee mwenye kibalaghashia tukajikuta tumewekwa katikati. Harufu kali ya moshi wa bangi ilitawala eneo lile na palikuwa kimya.
“Toa kila kitu ulichonacho bazazi wewe!!!” aliamrisha bwana mmoja, nikashuhudia kisu kikubwa mkononi mwake!! Mzee mwenye kibalaghashia akatumbua macho, hakutarajia kama tukio linaweza kubadilika namna ile!! Yeye alitarajia labda nikishatambuliwa basi atapongezwa lakini mambo yaliharibika wale waliotuzunguka neno kifo cha Kindo lilikuwa la kawaida sana kwao.
Wote tukajikuta tunatetemeka, lakini kwangu ilikuwa nafuu zaidi kutekwa na wale watu ambao niliamini kuwa ni vibaka tu wa kawaida kuliko kuingia katika mikono ya wale watu wabaya ama serikali ambayo ilikuwa imehadaika na sasa ikinisaka kama muuaji na mbakaji!!
Niliangusha simu yangu wakaikwapua!! Nikajipekua na kutoka na kiasi cha pesa na hiki pia wakachukua. Wakatoa vitisho kadha wa kadha
Yule mzee alikuwa na kanzu tu hakuwa na kitu cha ziada, wakamweka kando!!
Si kwamba walimwachia la!!
Nilishangaa ghafla alikuwa hewani na mara akatua chini, alikuwa amepigwa ngwala ya ghafla, yule mpigaji akajikausha kana kwamba si yeye aliyetoka kufanya tukio lile lililoipasua kanzu ya yule mzee na kukirusha kibalaghashia chake kando!! Hawakumwambia lolote.
Wakanirudia mimi tena, hawakuwa na utani hata kidogo na nyuso zao zilijawa chuki tupu!!
Kujifanya wananizongazonga waweze kunitambua mimi ni nani hiyo ilikuwa hila tu hakuna lolote walilotaka zaidi ya kuniibia na hilo walikuwa wamefanikiwa!!
Ajabu ni kwamba kuna watu walilishuhudia tukio hili lakini hata kujihusisha kutusaidia hawakujisumbua, na ilikuwa heri hawakujihusisha nasi maana wangeweza kutokea ambao aidha wangeweza kunitambua ama wangeyafanya mambo kuwa magumu zaidi!!
Hakika jiji la Dar es salaam lilikuwa limeoza na maovu kama haya yalikuwa kama kitu cha kawaida mbele ya macho ya watu!!
“Kindo umemfahamia wapi we bwege?” mara aliniuliza yule bwana aliyezungumza kama kiongozi na wenzake kumsikiliza.
“Ni jamaa yangu tu….mimi ni mtu wa Iringa nd’o nilikuwa namuulizia jamani” nilijitetea. Mara bwana mmoja akadakia hoja.
“Na wewe ndo wahanga wa ridandansi ya Michigani ama?” aliniuliza, akili ikafyatuka hilo neno Michigani halikuwa geni hata kidogo masikioni mwangu.
“Hapana, ni ndugu tu jamani!!” niliendelea kujitetea.
Ile kusema neno Michigani basi kila mmoja akacheka kati ya wale vibaka. Bila shaka halikuwa neno geni kwao. Ajabu ni kwamba neno lile hata kwangu pia halikuwa geni kuna mahali niliwahi kuliona kisha nikalipuuzia na sasa nalisikia tena.
“Yaani kila mtu wa Iringa huwa anadanganya kuwa alikuwa Michigani amefukuzwa kazi aisee sijui huko Michigani nd’o kampuni pekee kubwa??….haya dakika moja potea hapa urudi Michigani kwenu huko!!! Moja mbili…..” aliamuru na hakuwa na utani, kabla hajafika tatu nikatimua mbio kali huku nyuma nikimsikia yule mzee mwenye kibalaghashia akilalamika kwa maumivu, bila shaka alikuwa akipokea kipigo kingine kwa kutembea bila pesa.
Sikusimama maana nilikuwa nimeponea katika tundu la sindano, nilikimbia bila kukoma hadi maeneo ya Tandale, nikachepuka na kona kadhaa kabla sijairuhusu akili yangu kufanya kazi tena.
Uzuri ni kwamba nilikuwa nimechukua tahadhari mapema sana, pesa zangu niliziweka katika mafungu mbalimbali kwenye nguo nilizokuwa nimevaa. Hivyo hata nilipowapa wale wakora zile pesa na simu bado nilibakiwa na fedha nyingine ambazo zilinitosha kufanya safari ya kurejea kule nilipofikia kwa kutumia usafiri wa pikipiki tena!!!
Badala ya kusikitikia suala la kukaribia kukamatwa nilitamani tufike upesi Kimara niweze kuwa huru na kisha kujipanga tena upya kujitafutia haki yangu bila uhai wa Kindo!!
Maeneo ya Tandale sokoni, kabla sijachukua pikipiki, kwa tahadhari kubwa nilifanikiwa kununua kofia nyingine, na pia nikavutika kununua fulana kubwa na suruali nyingine.
Ile kofia nikaivaa muda uleule na kisha kutoweka, nikiwa kama mzuka aliyefufuka kutoka katika wafu nisiamini kama na hatua ile nimepona pia.
Majira ya saa mbili nilikuwa chumbani!! Upesi nikachukua bahasha yangu ambayo nilikuwa nimeificha chini ya godoro, nikamwaga makaratasi yote chini na hapo nikaiona ile picha ambayo jengo lake dogo limeandikwa Michigan. Ni hapa nilipokuwa nikisumbua akili yangu kupatambua!!
Niliitazama kwa makini sana, na hapo nikaanza kuunganisha matukio, nikayakumbuka mazungumzo baina yangu na Anitha aliponambia kuwa Kindo ambaye anasadikika kuwa marehemu tayari alikuwa mwenyeji wa Iringa, kama hii haitoshi wale vibaka waliposikia kuwa mimi ni jamaa yake Kindo mara moja wakadakia kuwa na mimi ni wa Michigan!!
Huko Michigan ni wapi?
Na je panahusika nini ni mauaji ya Ezekiel ambaye kwa jina halisi ama vyovyote vile ni Alvin.
Kwa maana hiyo Kindo aliwahi kuwaambia vibaka hao kuwa yeye alikuwa muajiriwa huko Michigan? Baadaye akapewa ridandansi!!!
Hapa kuna tatizo lazima!! Kindo amekufa na siri kubwa sana!!
Nikatamani sana kuzungumza na Anitha usiku huo lakini tatizo sikuwa na simu tena wale mabazazi huenda walishaiuza kwa bei ya kutupa tayari!!
Nikatoka nje na kumkabili muhudumu aliyekuwa mapokezi, nilimkuta akiwa ametingwa katika kusikiliza muziki na ilinilazimu kumuita mara tatu hata akanisikia, nikamsihi aniazime simu yake kuna simu ya muhimu sana nahitaji kupiga!!!
Akalalamika kuwa simu yake huwa haibadilishwi kadi, nikamweleza kuwa sitabadili. Bado akalalamika mengi na klusema simu yake haina muda wa maongezi, nikatoa shilingi elfu tano mfukoni. Uzuri huduma ya vocha ilikuwa pale, hapo akakosa ujanja na kufikia hatua ya kuniazima!!
Nikatoweka na ile simu na kuelekea chumbani kwangu!!
Nikajisifu kwa uwezo wangu mkubwa wa kukariri. Nikaziandika namba za Anitha katika simu ile na kungojea simu ile iiite.
Ikaanza kuita na baada ya dakika kadhaa ikapokelewa!!
Kama mimi nilivyotegea upande wa pili uanze kuzungumza na upande wa pili nao ukangoja mimi nianze kuzungumza!!
Mtego!! Nikajiwazia huku nikiendelea kukaa kimya!!
“Halo!” hatimaye sauti kutoka upande wa pili ilinong’ona. Alikuwa Anitha!!
Hapo nikapata ujasiri wa kujitambulisha upesiupesi!!
Anitha akasikika akikurupuka kwa fujo kutoka alipokuwa na nikasikia vishindo na baada ya hapo aliniuliza kama nilikuwa salama!! Nikajibu kuwa nipo salama kabisa, akaniuliza tena na tena kama nina uhakika na usalama wangu nami nikasisitiza kuwa hakuna baya lolote upande wangu!!
“Kindo amekufa….” Aliniambia binti huyu kitu ambacho nilikuwa nakitambua tayari.
“Nini kivipi?” nilimuuliza kana kwamba hakuna nijualo!!
Alinielezea kuwa na yeye hajui lolote lakini katika mapito yake pale kuhakikisha kuwa anazungumza tena na Kindo alipewa taarifa hiyo.
“Mbona unaulizia mara mbilimbili juu ya usalama wangu lakini!!” nilimuuliza kutaka kujua.
ANITHA akachukua nafasi kusimulia!!
SAM naomba nikiri kuwa naipongeza nafsi yangu kwa kuendelea kukuamini kila kukicha. Sikuwahi kukatishwa tamaa na habari za kwenye magazeti. Kashfa na tuhuma zote ulizozushiwa hazikuwahi kuniteteresha kamwe! Baada ya kifo cha Kindo, nimeamini kuwa kuna watu wabaya wengi wamelizunguka tukio hili na hakika u katika wakati mgumu sana.
Sam najua hujipiganii peke yako na labda unaona haya kunieleza kuwa unao uchungu sana kuwa hujui mkeo alipo na usalama wa mtoto wako. Ni kweli ninao wivu kwa sababu nakupenda lakini amini haya ninayokuambia. Sam naumia sana ten asana, juu ya mama Eva na Eva mwenyewe. Mama Eva ni mwanamke mwenzangu, hana kosa alilowahi kunitendea zaidi tu ya kujikuta katika penzi lako.
Eva ni mtoto mdogo hajui lolote kuhusu hisia zangu kwako!! Hastahili kuchukiwa!! Na sijawahi kumchukia unalitambua hilo.
Sam kwa hali ya amani ilivyo juu yako, kwa jinsi watu wabaya wanavyoisaka roho yako.
Nipo radhi niambie unahitaji kitu gani kingine naweza kufanya kwa ajili yako wewe, Eva na mama Eva. Niambie chochote hata kama ni kigumu nami nitakujibu kuwa naweza ama kipo nje ya uwezp wangu!!!” alinieleza kwa hisia kali huku akizungumza kwa sauti ya chini, kila neno likawa na maana kwangu nami nikajibu.
“Anitha, kama nilivyosema awali kuwa hata nikikushukuru namna gani bado sitafikia kiwango unachostahili.
Anitha naomba niwe muwazi kuwa hakika baada ya usaliti alioufanya mzee Matata ambaye ni baba yako imani yangu kwa wanadamu imekuwa hafifu sana. Yaani namuogopa kila mtu!!
Laiti kama ningekuwa sina familia nisingeogopa lolote lakini Eva ndo ananiumiza zaidi huku mama yake akinipagawisha kabisa, sijui alipo huenda hata wamemuua naye tutasikia kama hivyo kwa Kindo!! Anitha nimeamua kitu kimoja, nimeamua kujikabidhi kwako Anitha. Kujikabidhi kwa asilimia zote mia moja.
Kama sitakuwa sahihi basi chozi la Eva na damu ya mama Eva iwe juu yangu kwa upumbavu wangu!! Kilio cha Eva na kinisulubu iwapo sitakuwa sahihi kukuamini wewe kama mtu wa mwisho pekee ninayeamini upo upande wangu!!
Sina lolote la kufanya ikiwa sura yangu haitakikani mtaani na sasa Tanzania nzima wanaijua sura na jina langu popote pale nitakamatwa tu! Anitha narudia tena na samahani kama nitakuwa nakukera, tambua kuwa mimi Sam sijaua mtu wala kulawiti!! Iwapo baba yako ama familia kwa ujumla zimekumezesha sumu na kuamua kunikamata mimi sasa nipo radhi, lakini nikiwekewa kitanzi shingoni, neno nitakalosema juu yako ni kwamba lawama za Eva na mama yake ziwe juu yangu lakini damu yangu na uhai nitakaoupoteza kwa hila na hujuma ya hali ya juu, vyote vitakuwa juu yako Anitha. Namkabidhi Mungu uaminifu huu wa mwisho mkubwa ninaoamua kuuleta kwako. Yeye pekee ndiye ajuaye ni kiasi gani nipo upande wa haki na sijui lolote kuhusu kuua. Na ni yeye huyuhuyu aliyeniambia kuwa kesho nikutane na wewe ana kwa ana!!” nilimaliza huku nikishindwa kuyazuia machozi yangu nilipomkumbuka mke wangu asiyejulikana mahali alipo na Eva anayesadikika kutunzwa na jeshi la polisi Tanzania.
Upande wa pili nilimsikia Anitha naye akililia kilio cha kwikwi, na hata alipozungumza alitoa kauli fupi tu.
“Na kilaaniwe kizazi changu chote milele na milele iwapo siku moja nitasimama na kutetea maovu…Sam tukutane kesho saa tatu usiku. Utaniambia muda huo nije wapi??” kisha akakata simu!!
Sikutaka kumpigia simu kwa sababu nilijua hataweza kuzungumza tena, maneno yangu huenda yamemuumiza moyoni ama yamemtia aibu kwa mpango aliokuwanao na sasa anajutia kwa machozi!!
Nikamtumia ujumbe mfupi. Nikamuelezea wapi nitakuwepo, sitakuwa na simu lakini nitafika kwa wakati!! Pia nikamsisitiza asitumie namba ile tena!!
Nikamaliza nikaifuta namba yake katika simu ile na kumrejeshea muhudumu, salio lililobaki mle lilimfanya atokwe na tabasamu, meno yake ya njano yakaonekana.
Sikurudi kulala, nikaondoka na kujipatia mkate na soda dukani, nikarejea chumbani kwangu kupooza njaa huku nikitafakari Michigani ni kitu gani na kwanini Kindo ahusike nayo na kisha Alvin.
Michigan Michigan!!!
Nililala nikiwaza hayo!!
SIKU iliyofuata kama ilivyoutaratibu wangu nilihama nyumba ile na kuhamia kwingine kabisa maeneo ya Ubungo. Baada ya kuwa nimepata supu ya maana nilijifungia ndani mara nilale mara niamke huku nikitafakari mambo mengi yasiyokuwa na ufumbuzi, kisha nikamtafakari Anitha na uamuzi wangu wa kukutana naye!!
Roho ilinidunda sana na kujiona kuwa najikabidhi kwa muuaji kirahisi, lakini ni kipi ningefanya iwapo hakuna anayeniamini na ushahidi wangu wenyewe ulikuwa utata mkubwa kuliko utata uliokuwepo. Picha na maandishi yaliyoandikwa na msichana ama mvulana asiyejua kuandika vizuri yangeisaidia nini mahakama zaidi ya kubambikiwa kesi nyingine ya kudanganya mahakama.
Eva na mama yake hawa ndio waliniumiza zaidi!!
Hawakuwa na kosa na huenda wangekuwa wameaminishwa kuwa mimi ni mtu mbaya, mwanangu Eva anaambiwa baba yako ni gaidi,.
Nikazichanga karata na kisha nikaitupa kete moja tu kubwa nay a mwisho kwa Anitha!! Kama ana mnapenzi ya kweli ama anatumiwa!!
Nikasinzia tena!!
Majira ya saa mbili nilitoka nyumbani na kwenda eneo la miadi ambalo nilimtumia Anitha katika ujumbe mfupi wa maneno.
Niliwahi maksudi ili niweze kusoma mchezo kama utakuwepo japo hiyo ilikuwa mbinu hafifu tu ya kujihami, kama wamejipanga tayari nisingeweza kuchomoka tena!!
Saa mbili na nusu kwa mujibu wa saa iliyokuwa katika mnara nilimuona Anitha akitembea kwa madaha kuelekea katika eneo nililomwelekeza.
Baada ya kutingwa na mawazo siku kadhaa sasa nilikumbuka kuwa kumbe Anitha ni msichana mrembo kiasi kile. Nalivalia vazi refu jeusi lililozichora nyonga zake vyema, vazi lile halikuishia kiunoni bali lilipanda hadi usawa wa kifua chake na kuzistiri embe sindano ndogo zilizong’ang’ania kukomalia pale kifuani na si mahali pengine, mgongo ulikuwa wazi lakini si wazi kiasi cha kuitwa uchi la! Ulifunikwa na nywele ndefu ambazo alijitambia kila leo!!
Macho yake yalizibwa na miwani yenye mahadhi ya kuvaliwa usiku, mkononi alibeba kipochi kilichofanana na miwani.
Hakika aliwaka!!!
Niliwahi kuwa naye katika mahusiano lakini sasa alipendeza zaidi!! Alichukua nafasi na kuagiza maji ya matunda!!
Akiwa anakunywa kinywaji kile hakuonyesha hofu yoyote machoni mwake.
Nikatazama juu mbinguni na kusema na Mungu!!
“Wajua kuwa sikuua, wajua kuwa mimi ni mja wako!! Nitazame baba huku ninapoelekea, kama ni sahihi nyanyua mguu wangu sasa lakini kama si sahihi baba nitegue nisiweze kuifikia meza ile” nilimaliza ile dua na kisha hatua moja hadi nyingine hadi nikaifikia ile meza.
Nilikuwa nimevaa zile nguo nilizonunua Tandale usiku uliopita!!
Anitha aligeuka na kunbitambua akasimama na kunikumbatia.
Marashi yake yakamfanya azidi kuwa mrembo, joto lake tulivu likanikumbusha mengi yaliyopita!!
Nikavuta kiti na kuketi mkabala naye sasa tukawa tunatazamana. Alipotoa miwani uso wake ulikuwa umechafuliwa na michirizi ya machozi.
Anitha alikuwa analia, na hapa akanyanyua mdomo na kuniambia jambo ambalo sikuwahi kuliwaza.
“Sam umekonda hivi jamanii!!”
Nikashangaa!! Akasema tena, “Yaani umepauka kabisa si wewe Sam. Pole sana.”
Alinibembeleza, nikajisikia vibaya badala ya kupata ahueni!!
Robo saa baadaye tukiwa tumeagiza vyakula, nilikuwa nikimuelezea juu ya Michigan na utata niliokutana nao nikiwa namtafuta Kindo.
“Kwa hiyo hukuniamini hata kidogo Sam ukaamua kwenda mwenyewe!! Ni lini utaamini kuwa Anitha yu upande wako.” Alilalamika, nikajifanya sikumsikia nikaendelea kumweleza mambo kadha wa kadha!! Yote haya nilimsimulia nikiwa sijaifungua bahasha mkononi mwangu!!
Ukafika wakati wa kuifungua bahasha, hapa akalazimika kuja kuketi katika ubavu wangu ili nimwelekeze kitu kimoja baada ya kingine ili atambue ni kitu gani namaanisha.
Picha moja baada ya nyingine, andishi moja baada ya nyingine…
MARA tukakatishwa na sauti ya mwanamke, “Heloow!!” tukadhani ni muhudumu wa ile sehemu tukapuuzia na kuendelea na mambo yetu!!
Niliponyanyua macho kwa mbali niliona kitu kama ninacho kifananisha na mzimu usiotakikana machoni kwangu!! Lakini wakati naendelea kuduwaa mara mbele yetu akaketi mwanamama akiwa anatabasamu. Tabasamu la kinafiki.
Nikamtambua upesi yeye na kisha nikapata jibu la yule niliyemfananisha alikuwa ni nani!!
Mbele yangu alikuwa ni mama yake Anitha na yule mzee aliyekuwa anakaribia kufika pale alikuwa ni mzee MATATA…..baba yake mzazi Anitha…….
Bahasha yangu mezani, najilazimisha kufumbua macho lakini hayafumbuki zaidi ili iwe ndoto!!
Nilikuwa maeneo ya Saveyi karibu na chuo kikuu cha Ardhi na mbele yangu alikuwapo mama Anitha na huyu anayemalizia hatua afike nilipokaa alikuwa ni mzee Matata.
Mapigo ya moyo badala ya kwenda kasi yakaanza kushuka kwa fujo!!
Jasho halikutoka lakini mwili ukawa wa baridi sana. Ganzi ikanishika.
NAKUFA!!!! Nikajiwazia…………..

JIFUNZE!!! DUNIA inapokugeuka mwamini Mungu pekee, yeye hadanganyi, yeye si mnafiki wala si msaliti!! Ukimwambia baba tenda miujiza anasikia palepale!! Sema naye kwa imani naye atatenda!!!