Shaffih Dauda
Usajili ambao mimi umenishangaza ni wa mshambuliaji Paul Onuachu kutoka KRC Genk [Belgium] Southampton [England] sio mchezaji mwenye jina kubwa ndio maana uhamisho wake haujawa habari kubwa.
Onuachu alikuwa mfungaji mahiri tangu amejiunga na Genk, kuna wakati alikuwa na rekodi ya mchezaji wa Afrika mwenye magoli mengi kwenye Ligi kubwa za Ulaya.
Akiwa Genk amecheza Mechi 134, amefunga Magoli 85, na kushinda tuzo ya mfungaji bora wa msimu mara 1.
Hivi karibuni wakati nipo Belgium nilipata fursa ya kushuhudia game ya Genk vs Zulte Waregem, ukimwangalia uwanjani kwa mazingira yetu ya Tanzania hapewi nafasi hata kwenye timu ya Ligi Daraja la Nne.
Wakati mechi inaendelea Onuachu ndio alikuwa mjadala kwa baadhi ya watanzania waliokuwepo uwanjani wanashuhudia mchezo ule. Wengi wao walikuwa wanahoji kwa nini Onuachu anacheza wakati kukimbia hawezi wala kumpita hata mchezaji mmoja!
Mimi nikawa nawaambia naheshimu sana maamuzi ya kiufundi kwa maana ya benchi la ufundi lazima watakuwa wameona kitu kwa mchezaji huyo hawawezi kumchezesha tu kama hana kitu.
Wenzetu wana vipaumbele vyao kulingana na nafasi. Mfano golikipa, beki wa kati na mshambuliaji wanaangalia umbo sio kipaji pekeyake. Mtu mrefu kwenye maeneo hayo wao watamchukua halafu hivyo vitu vingine watamuongezea wenyewe.
Hatakiwi kuwa kama Messi awe na uwezo wa ku-control na kupasia ila faida ya umbo lake ndio wanaitaka kwa sababu unaweza kumfundisha mchezaji ku-control na kupasia lakini huwezi kumpa kimo.
Kwa sasa sehemu ya ushambuliaji ni kumalizia tu, mshambuliaji anatakiwa kujua ni eneo gani awepo kwa wakati ili apate nafasi ya kumalizia lakini pia anatakiwa awe anajua ni namna gani ataifanya timu yake ifike kwenye eneo la kushambulia
Kama mshambuliaji ana uwezo mzuri wa kumalizia hana haja ya kukimbia na mpira umbali wa mita 10 au 20, makocha wanachotaka timu ikishambulia mshambuliaji awe kwenye aneo ambalo akipewa mpira atafunga.
Kwetu bado tunafikiria mchezaji mwenye kufanya vitu vingi uwanjani ndio mchezaji mzuri. Ndio maana hivi karibuni Anthony wa Manchester United amekuwa akikosolewa kwamba, akiwa uwanjani utaona ana vipande vingi ambavyo vita-trend YouTube lakini hajaisaidia timu kwa lolote.