Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Mpwapwa, George Chiteto amefariki dunia muda mfupi baada ya kutoa mahubiri katika ibada ya mazishi ya mke wa Askofu mwenzake, Hilda Lugendo iliyofanyika wilayani Muheza mkoani Tanga.
Akizungumza kwa simu na Mwananchi, Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Maimbo Mndolwa aliyeongoza misa hiyo katika Kanisa la Kristo Mfalme Muheza, amesema wamepewa taarifa kutoka hospitali kuwa Askofu Chiteto alipatwa na mshtuko wa moyo.
“Madaktari wametuarifu kuna kitu kinaitwa cardiac arrest. Alikuwa na shida ya pressure (shinikizo la moyo) na kisukari,”
“Yeye alikuwa mhubiri na kwa kweli mahubiri yake yaliwavuta watu na neno lake la mwisho ni mlango umeandaliwa twendeni, basi anakwenda kukaa na Mungu akamwita,” amesema Askofu Mndolwa.
Akifafanua jinsi kifo cha askofu huyo kilivyotokea, msemaji wa kanisa hilo, Maiko Luoga amesema, Askofu Chiteto alihubiri katika misa hiyo na kumaliza, kisha alipokaa aliishiwa nguvu na kukimbizwa katika hospitali teule ya Muheza.