Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Mwigulu Nchemba leo akiwa Dodoma amekutana na Waandishi wa Habari kutolea ufafanuzi ishu ambayo imekua gumzo nchini kuhusu masuala ya tozo kwenye miamala ya simu na benki ambapo amesema “Tumesikia maoni ya Wananchi wengine walisema tupo kimya, tulikuwa kimya tukisikiliza maoni ya Wananchi, tumekutana na Watalaamu wa Kodi tumepata maoni yao maoni yamelenga maeneo mbalimbali ila kubwa ni tozo za miamala ukituma na ukitumiwa na kwenye inatozwa, tumepokea na tunayafanyia kazi na tutatoa majibu ya utekelezaji wake siku sio nyingi”
“Kuweni watulivu wakati tunashughulikia hoja hiyo, tumeona wengine wakizungusha risiti zenye viwango vya tozo wakionesha pesa iliyokusanywa kwenye Benki, tutakutana na Taasisi za Fedha tuone kuhusu hilo, Nchi hii ni yetu wala Mtu usihofie kutoa maoni, hatuna sababu ya kugombana kwenye hoja zenye mantiki”
“Nimesikia malalamiko kuhusu kodi ya upangishaji wa majengo, hii sio sheria mpya ila utekelezaji wake umeanza mwaka huu, wengine wanasema kwanini Mpangaji apewe kazi ya TRA ya kukusanya apeleke fedha TRA, hii sio kodi ya Mpangaji, anayepaswa kulipa kodi ya kupangisha ni Mwenye nyumba na kuhusu Mpangaji anageukaje kuwa mkusanya kodi tumeipokea na tunaifanyia kazi, ni kweli inaweza kumgombanisha na Mwenye nyumba wake na kumpotezea muda”
“Sisi wote ni Watanzania hakuna aliye Mtanzania na nusu, twendeni kwenye misingi ya haki, hivi kama Mtu mwenye kima cha chini anatozwa kodi halafu kuna anayemiliki majengo anapangisha pesa karibu Tsh. Mil 60 halafu tusimtoze kodi kisa mazoea tu, wengine wanasema ‘Huyu Waziri huyu kasoma wapi huyu!?, Phd gani huyu anatoza tozo kwenye majengo ya kupangisha!?’, mnaona ni sawa tumtoze Mtu wa kima cha chini cha Milioni tatu kwa mwaka halafu anayepata Mil 60 tusimtoze?, nyie mnaona ni sawa?”