Ndani ya Jiji la Dar es Salaam kuna mnyukano. Ni baina ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na mfanyabiashara Ghalib Said Mohammed (GSM). Wanagombea ardhi.
Makonda analalamika kuwa GSM anataka kumdhulumu mali yake. Wakili wa GSM, Alex Mgongolwa akatoa ushahidi wa umiliki wa ardhi yenye mgogoro. Kwamba ni mali halali ya mteja wake.
Nani mmiliki? Hilo jawabu litajulikana mbele ya sheria. Msingi wa makala hii ni kumtazama Makonda anayelalamika kuwa anadhulumiwa na mfanyabiashara aliyemwita tapeli. Hana nguvu!
Ikikupendeza, rudi nyuma miaka mitatu tu. Je, ungedhani yule Makonda, mkuu wa mkoa, angekuwa huyu anayesema yupo tayari kupigwa risasi lakini si kushuhudia mali yake ikichukuliwa?
Yule Makonda tishio, mpaka Serikali ya Marekani ikatoa taarifa ya kumpiga marufuku kukanyaga kwenye taifa hilo, kwa sababu waliyoitaja kwamba ni kudhulumu haki ya watu wengine kuishi, ndio huyu asiye na nguvu zozote?