kutokana na ugumu wa ajira kwenye zama hizi watu wengi wanaona kujiajiri au kuwa mjasiriamali ndio njia mbadala ya kuyakomboa maisha yao. Hivyo kumekuwa na wimbi kubwa la watu kuondoka kwenye kazi na kwenda kujiajiri au kuanzisha biashara zao. Ni kitu kizuri sana kwa sababu angalau watu wanaweza kuwa na mamlaka na maisha yao na wanaeza wakaajiri na wengine pia. Ila kwa upande wa pili sio wote wanaokwenda njia hiyo wanafanikiwa kufikia malengo waliyojiwekea. Wengi sana wanashindwa na kujikuta wako kwenye mazingira magumu kuliko hata yale waliyokuwa nayo kwenye ajira.
Leo tutazungumzia mambo unayotakiwa kuyajua au kuyafanya kabla hujaacha kazi na kuingia kwenye ujasiriamali au biashara. Sisemi mambo haya ili kukukatisha tamaa na uendelee kuwa mtumwa, ila nayasema ili kukupatia mwanga wa kule unakokwenda ili usije kushangazwa na mambo haya baadae. Mambo hayo ni kama ifuatavyo;
1. Kujiajiri au ujasiriamali ni kugumu.
Kama unafikiri kujiajiri au kuingia kwenye ujasiriamali ndio nJia rahisi kwako kufanikiwa ni vyema ukabadili mawazo yako mara moja kabla hujaingia na ukashindwa vibaya. Zaidi ya nusu ya biashara zinazoanzishwa zinakufa ndani ya mwaka mmoja baada ya kuanzisha. Na hata zile zinazoendelea kudumu zinakuwa na hali ngumu sana na hazitengenezi faida kubwa. Hizi ni takwimu ambazo zinasikitisha sana ila ndio ukweli wenyewe.
Kujiajiri ni kugumu, ujasiriamali ni mgumu na biashara ni ngumu. Jua kabisa unaingia kwenye njia ambayo uwezekano wa kushundwa ni mkubwa hivyo mipango na kufanya kazi kwa bidii na maarifa ni muhimu sana
2. Utafanya kazi kuliko ulivyokuwa umeajiriwa.
Unafikiri ukishajiajiri wewe ndio bosi mwenyewe unakaa nyuma ya meza kubwa yenye kiti cha kuzunguka huku ukiongea na simu au wageni na wateja waliokutembelea ofisini. Ndoto za mchana hizo. Unaweza kukaa kwenye kiti cha kuzunguka na meza kubwa ila utafanya kazi zaidi ya unavyofanya kwenye ajira. Unaweza kujikuta unafanya kazi masaa kumi na mbili ofisini na ukirudi nyumbani unaendelea tena na kazi kwa zaidi ya masaa mawili. Mwanzo wa biashara au ujasiriamali kuna misingi mingi unayotakiwa kuijenga na ni wewe pekee utakaefanya hivyo.
3. Utavaa kofia nyingi kwa wakati mmoja.
Kwenye ajira yako una jukumu moja tu au machache yaliyoelezwa. Labda unafanya kazi kwenye idara ya masoko, au idara ya uzalishaji au idara ya huduma kwa wateja na kadhalika. Unapojiajiri utajikuta unafanya kazi za kila idara katika biashara yako. Kuna wakati utavaa kofia ya kiongozi, wakati mwingine masoko, wakati mwingine huduma kwa wateja na kadhalika. Kuwa tayari kubadilika kutokana na hitaji la biashara yako kwa wakati husika.
4. Usichome madaraja.
Kuna dhana moja iliyokuwa ikitumika sana kipindi cha nyuma ambapo mtu alikuwa akiondoa uwezekano wowote wa kurudi nyuma. Kwa mfano kama wewe unataka kuacha kazi na kwenda kujiajiri basi unagombana na waajiri wako kiasi kwamba huwezi kurudi tena kwenye ulimwengu wa ajira, hii inakusababisha uhakikishe unafanya kila mbinu kufanikiwa kwani huna kimbilio jingine. Dhana hii ilifanya kazi sana zamani ila kwa sasa usijaribu kuitumia. Ondoka kwa amani na kama ikiwezekana mwambie muajiri wako unakwenda kufanya nini, mwajiri wako tayari ana mtandao mkubwa hivyo anaweza kukusaidia kupata wateja wa biadhaa au huduma uayokwenda kutoa. Nguvu ya mtandao ni kubwa sana kwenye ulimwengu wa sasa wa biashara na ujasiriamali.