Makapuku Forum

Makapuku Forum

Muziki: Huhitaji Leseni Kuendesha, Funga Mkanda

Maisha yanakwenda kasi sana, kataa kubali maana sijauliza swali ujibu ndiyo au hapana. Ukweli unabaki kusimama muda wote na uongo hata ukisimama si muda mrefu utachutama kabisa na kwa aibu kubwa. Ninakusalimia wewe Kapuku ambaye unalifanya Jukwaa hili kuwa sehemu nzuri ya kuwepo, nipo kwa sababu wewe upo. Asante sana.

Nilikuwa najisomea gazeti na nilivutiwa na katuni, yeah, ninapenda kuangalia katuni na kuzisoma, huwa zinawasilisha ujumbe kwa maana kubwa sana. Sote tunajua kuendesha kiuhalali kunahitaji kwanza upitie mafunzo (namaanisha kuendesha barabarani), upate majaribio na kisha ndo unaruhusiwa kukata leseni, hapo utaitwa dereva kamili na una nafasi ya kutumia barabara pamoja na watumiaji wengine. Lakini si kila anayeendesha kaipitia hizo hatua, wengine unakuwa umekula mlo mbaya na unasikia leo ninaendesha na sifungi mkanda kama dereva mwingine na ninapoendeshea nakuwa peke yangu nguo ya ndani magotini

Muziki sasa, furahia muziki maana kesho ikimpendeza Manani ni furahiday


Asante Obe Ubarikiwe
 
The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 57
ILIPOISHIA:

Ni kama fahamu zake zilikuwa zimemrejea kwani alishtuka sana kuniona ndani ya chumba chake, akageuka huku na kule huku akijaribu kujitoa kwenye mikono yangu kwa hofu kubwa.
“Togoo! Umeingiaje humu?” aliniuliza kwa sauti ya juu, nikasikia mlango wa chumba cha pili ukifunguliwa kuashiria kwamba kuna mtu alikuwa amesikia na sasa anatoka.
SASA ENDELEA...

“Nimekwisha!” nilijisema huku nikigeuka huku na kule, sikumuona baba wala baba yale Rahma, Sadoki akanibadilikia na kunishika kwa nguvu ii nisipate nafasi ya kukimbia.
Akili za haraka, zilinituma kutumia nguvu zangu kujiokoa na kwa kuwa nilikuwa na ile kinga yangu ya hirizi mkononi, nilipiga mguu wa kushoto chini huku nikiwa nimevibana vidole gumba na vile vya mwisho. Hii ni mbinu niliyofundishwa ya kutaka kupotea kwenye macho ya watu, yaani unakuwepo sehemu hiyohiyo lakini huonekani.
Nilipofanya hivyo, nilishtukia nikiwa mwepesi kama upepo, Sadoki akabaki ameduwaa kwani japokuwa alikuwa amenishika, alishtukia nikiyeyuka mikononi mwake, giza nene likatanda chumba kizima.
Mara mlango ulianza kugongwa kwa nguvu, Sadoki akaenda kuufungua maana alikuwa amefunga kwa komeo kwa ndani, mama yake Sadoki akaingia mbiombio akiwa ameshika kibatari.
“Una nini Sadoki?”
“Mama! Nimemuona Togo kwa macho yangu, hata sijui ameingiaje humu ndani wakati milango ilikuwa imefungwa.”
“Togo huyu rafiki yako? Wewe utakuwa unaota, Togo ataingiaje humu wakati milango yote imefungwa? Halafu mbona watu wenyewe hawapo hapa kijijini na hakuna anayejua walikohamia?” mama yake Sadoki alisema huku akionesha kumshangaa mwanaye.
“Kweli mama, nimemuona kwa macho yangu!”
“Kwanza umemuonaje wakati hukuwa umewasha kibatari? Acha kutushtua wenzako kwa sababu ya ndoto zako,” alisema mama yake Sadoki huku akimulika huku na kule kwa kibatari. Japokuwa nilikuwa mlemle ndani, hakuna aliyeniona, mwanamke huyo akawa anamtuliza mwanaye na kumwambia kwa kuwa wanalindwa na Mungu hakuna jambo lolote baya linaloweza kuwapata.
Japokuwa mama yake Sadoki aliamini kwamba mwanaye alikuwa ndotoni, mwenyewe aliendelea kushikilia msimamo wake na alipoona mama yake hamuamini, aliamua kunyamaza lakini mara kwa mara alikuwa akigeuka huku na kule, akionesha kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake.
“Haya sogea huku tusali,” alisema mama yake Sadoki, akamshika mwanaye mikono, wote wakafumba macho. Kabla hata hawajaanza kusali, nilishtukia nikivutwa kwa nguvu kuelekea nje, kutazama vizuri kumbe walikuwa ni baba na baba yake Rahma, tukadondokea kwenye majani pembeni ya nyumba ya akina Sadoki, wote wakiwa wanahema kwa nguvu.
“Mpumbavu sana wewe,” alisema baba huku akinizabua kibao kwa nguvu, nikashangaa kwa nini ananipiga kwa sababu sikuwa nimefanya kosa lolote.
“Kwa nini hukumgeuza kinyumenyume kama wewe?” alisema baba kwa ukali, ni hapo ndipo nilipolitambua kosa langu. Wakati nikitoka na Sadoki, mimi ndiye niliyetanguliza mgongo lakini yeye alikuwa ameelekea nilipo mimi kwa sababu nilikuwa nimemshika mikono nikimvuta, hakutanguliza mgongo.
“Lakini hukuniambia hivyo baba,” nilisema huku nikiugulia maumivu makali ya kibao cha baba. Muda huo tayari walishaanza kusali, wakawa wanakemea na kutaja jina la Mungu kwa nguvu.
Ukweli ambao wengi hawaujui, ambao hata mimi mwenyewe nilikuwa siujui, hakuna sumu mbaya kwa jamii ya watu wa nguvu za giza, kama mtu anayesali na kumuamini Mungu kwa moyo wake wote, bila kujali ni wa dini gani.
Hapa nazungumzia wale watu ambao kweli wanafuatisha amri za Mungu, yaani kama ni Mkristo, awe anafuatisha yale yote aliyoagizwa na dini yake na kama ni Muislam vivyo hivyo.
Watu wa namna hii, huwa hawagusiki kabisa maana hata pale baba aliniambia kama wasingetumia nguvu za ziada kuingia na kunivuta kwa nguvu, maombi ya Sadoki na mama yake yangenidhuru vibaya sana na hata wao hawajui nini kingenipata.
Ila kitu ambacho nilikuja kujifunza baadaye, ambacho ningependa watu wengine wajue, kinga waliyonayo watu wanaomuamini Mungu, haiwahusu wale wanaosali kinafiki, kwamba ukifika kwenye nyumba za ibada unajifanya wewe ni mwema sana lakini kumbe ni mwizi, mwongo, mwasherati au unashinda kwa waganga wa kienyeji.
Ilibidi tuondoke haraka pale nyumbani kwa akina Sadoki kwa sababu sasa palikuwa hapakaliki tena kutokana na maombi yaliyokuwa yanaendelea ndani, njia nzima baba akawa ananilaumu kwa uzembe nilioufanya. Kwa bahati nzuri baba Rahma alinitetea kwamba ni kwa sababu sikuwa najua.
Kiukweli lawama za baba zilikuwa ni uonevu wa hali ya juu, maelezo aliyokuwa ananipa, alikuwa ananielekeza vitu nusunusu, sasa kwa mfano hapo kwa akina Sadoki, mimi ningejuaje kama natakiwa kumgeuza Sadoki pia atoke kinyumenyume huku nikiwa nimemshikilia bila kupewa maelekezo?
“Sisi tunakusaidia wewe mwenyewe kwa sababu ya upumbavu ulioufanya, kwani sisi ndiyo tulikutuma uende kwenye msiba ambao wewe mwenyewe ndiye uliyeusababisha? Utajuana mwenyewe na Mkuu, we fanya masihara utaona mwisho wake,” alisema baba.
Tayari tulishakaribia pale kwenye uwanja wa shule ya msingi niliyosoma ambapo ndipo tulipofikia.
“Sasa mzee mwenzangu, tukiendelea kufanya mambo kwa hasira, kweli tutampoteza huyu kijana, hapa kinachotakiwa ni kuhakikisha tunamaliza kwanza suala la Mkuu na Togo na kama unavyoona huku ndiyo tayari tumeshakwama na muda unayoyoma,” alisema baba yake Rahma.
Mwanzo nilikuwa nalichukulia suala hilo kama jepesi lakini kwa jinsi mazungumzo hayo yalivyokuwa, niligundua kwamba kweli nipo kwenye hatari kubwa kwa sababu ya makosa niliyokuwa nimeyafanya bila kujua.
“Hivi si kuna yule mtu aliyepoteza maisha kwenye ile ajali ya bodaboda aliyoisababisha huyu mwendawazimu?” baba aliuliza. Baba yake Rahma akamjibu kwa kutingisha kichwa, nikiwa na shauku kubwa ya kutaka kusikia baba atasema nini.
“Taarifa zinaonesha kwamba amezikwa jioni ya leo, ila sijui amezikwa wapi, kama tukifanikiwa kujua, tunaweza kumtumia kama mbadala wa Sadoki ili tulimalize hili tatizo la huyu mwendawazimu,” alisema baba huku akiendelea kunishutumu.
Sikuelewa anamaanisha nini na hata kama tungelijua kaburi lake tungefanya nini.
“Twendeni Mlandizi, tutajua hukohuko tukifika, si unalikumbuka eneo la ajali?” baba aliniuliza, nikatingisha kichwa kwa sababu ilikuwa ni palepale kwenye nyumba iliyokuwa na msiba ndipo hiyo ajali nyingine ilipotokea. Yaani baba alivyokuwa akizungumza, utafikiri kutoka Chunya mpaka Mlandizi ni karibu sana.
Kukukumbusha tu, hapa aliyekuwa anazungumziwa aliyekuwa ni yule dereva wa bodaboda ambaye wakati nikiwa nakimbia kuokoa maisha yangu baada ya wale wazee kunishtukia pale kwenye msiba, nilimgonga wakati nikivuta barabara, yeye akiwa kwenye bodaboda iliyokuwa kwenye kasi kubwa. Pale alipodondoka hakuweza hata kuomba maji, alipoteza maisha palepale na sikuwa najua mpaka nilipokuja kuambiwa na akina baba ambao hata sijui wao walijuaje.
Basi tulienda mpaka pale chini ya ule mti, tukakuta kuna watu wengine wengi wakiwa wanafanya mambo ambayo hata sikuyaelewa lakini yalionesha kuhusiana na nguvu za giza.
Tukakaa na kuweka duara kama tulivyofanya kule Kunduchi wakati tukitaka kuondoka, nikaambiwa nifumbe macho na nisifumbue mpaka nitakapoambiwa, lakini baba akanisisitiza kwamba natakiwa kuwa nalifikiria eneo lile ajali ilipotokea.
Kweli nilifanya hivyo, wao wakafanya tena mambo yao kama kule Kunduchi na muda mfupi baadaye, upepo mkali ulianza kuvuma, sikuelewa tena kilichoendelea mpaka nilipokuja kuzinduliwa na baba aliyekuwa akinitingisha kwa nguvu.
Yaani kilichokuwa kinatokea, inakuwa kama nimepitiwa na usingizi mzito wa ghafla, kisha nikizinduliwa najikuta nipo kwenye mazingira mengine tofauti kabisa. Nilishtukia nikiwa nimelala pembeni ya barabara ya lami, baba aliponiamsha, nikawa nashangaashangaa, nikageuka huku na kule kama ninayejaribu kuvuta kumbukumbu.
Sikuyaamini macho yangu kugundua kwamba tulikuwa Mlandizi, tena jirani kabisa na pale ile ajali ilipotokea. Nilipotazama upande wa pili wa barabara, niliwaona watu wengi wakiwa wamekaa na kuuzunguka moto, pale kwenye ile nyumba iliyokuwa na msiba wa kwanza wa yule mtoto, moyo ukashtuka sana nikikumbuka kilichotokea.
“Mbona umeshtuka,” baba aliniuliza.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
 
The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 58
ILIPOISHIA:
Sikuyaamini macho yangu kugundua kwamba tulikuwa Mlandizi, tena jirani kabisa na pale ile ajali ilipotokea. Nilipotazama upande wa pili wa barabara, niliwaona watu wengi wakiwa wamekaa na kuuzunguka moto, pale kwenye ile nyumba iliyokuwa na msiba wa kwanza wa yule mtoto, moyo ukashtuka sana nikikumbuka kilichotokea.
“Mbona umeshtuka,” baba aliniuliza.
SASA ENDELEA...

Sikumjibu zaidi ya kumuonesha kidole kwenye ile nyumba ambapo bado watu walikuwa wakiendelea kuota moto huku wakipiga stori za hapa na pale msibani. Baba wala hakuhangaika hata kugeuka, akanitaka kuelekeza akili zangu kwenye jambo lililotupeleka pale kwani muda ulikuwa umetutupa mkono.
Ilionesha baba alikuwa anaelewa kila kitu kilichokuwa kikiendelea, nikawa najiuliza ameyajuaje yote hayo? Kiukweli sikupata jibu, baba Rahma naye wala hakujishughulisha na chochote na wale watu kama baba.
“Onesha aliangukia wapi? Unatupotezea muda,” alisema baba, nikawa najaribu kuvuta kumbukumbu, nikawa natembea pembeni ya barabara kuelekea pale yule dereva wa bodaboda alipodondokea, wakawa wananifuata kwa nyuma.
“Nadhani ni hapa.”
“Unadhani? Kwani huna uhakika?”
“Nilipomgonga aliyumbayumba kwa mita kadhaa, akaja kudondokea hapa, sina uhakika kwa sababu mimi nilikuwa nimesimama kule mbali.
“Hebu nenda ulipokuwa umesimama,” alisema baba. Ilionesha hakuwa akitaka majibu ya kubahatisha, nikageuka na kutazama tena kule msibani. Bado moyo wangu ulikuwa na hofu, nikiamini wale wazee wanaweza kuwa miongoni mwa watu waliokesha pale msibani halafu nikayazua mengine tena.
Nilirudi kwa hofu mpaka pale nilipokatiza barabara nikiwa spidi kali kama kiberenge, nikasimama na kuwageukia akina baba. Niliweza kupata ramani halisi, nikatembea harakaharaka kuelekea mpaka pale nilipokuwa nimewaacha.
“Ni hapa,” nilisema huku nikioneshea kidole katikati ya barabara. Ni kweli nilipatia kwa sababu bado palikuwa na alama za damu na vioo vya ile bodaboda, baba akainama pale katikati ya lami kisha akawa ni kama anaokota vitu fulani hivi.
Baada ya hapo alikuja upande wa pili tulipokuwa tumesimama, akawa anatazama chini kisha akainua uso na kunitazama:
“Walipomtoa pale katikati ya barabara walimlaza hapa,” alisema huku akionesha, ni kweli pale pembeni napo palikuwa na alama za damu nyingi zilizokaukia, kwa kutumia mikono miwili, alizoa udongo uliokaukia damu, kisha akapiga magoti na kuuinua juu, akazungumza maneno fulani kama anayenuiza jambo kisha akausogeza ule udongo puani kwake, akaunusa kisha akapiga chafya mfululizo.
Hakusema chochote baada ya hapo zaidi ya kuinuka na kuanza kutembea kwa haraka kuelekea upande wa kusini, kama anayetafuta kitu, baba yake Rahma alinipa ishara kwamba tumfuate, akawa anatembea kwa kasi huku akiongea maneno ambayo sikuwa nayaelewa.
Alivuka barabara, na sisi tukawa tunamfuata, akawa anazidi kuongeza kasi kiasi kwamba nililazimika kuwa nakimbia ili kwenda nao sawa. Bahati nzuri ni kwamba tulikuwa tukielekea upande tofauti kabisa na kule kulikokuwa na msiba.
Ilifika mahali akachepuka na kuingia vichakani, safari hii akaanza kutimua mbio, sote tukawa tunakimbia kumfuata. Japokuwa ilikuwa ni usiku, tulikimbia vichakani kwa muda mrefu sana, baadaye tukatokezea kwenye makaburi mengi, baba akawa anazunguka huku na kule na mwisho aliishia kwenye kaburi moja lililoonesha kuwa jipya.
“Amezikwa hapa,” alisema baba huku akigeuka huku na kule, nikawa natetemeka kwa hofu, sikujua nini kinachoenda kutokea.
“Simama kwa kule,” alisema baba huku akinielekeza kusimama upande uliokuwa na msalaba ambapo kimsingi ndiyo kichwani. Nilifanya hivyo, baba yake Rahma akasimama upande wa miguuni na baba akasimama katikati, juu ya kaburi.
Baada ya kusimama hapo, aligeuka huku na kule kama anayetafuta kitu kisha akashuka kutoka pale juu ya kaburi na kunifuata, akawa ananiongelea sikioni.
“Huyu amezikwa leo, katika sheria za jamii yetu, anaruhusiwa kutolewa kafara kwa hiyo tutamchukua huyu badala ya Sadoki, kule tutarudi siku nyingine kwa sababu kuna mambo hayakwenda sawa kwa sababu yako, sasa ukifanya ujinga tena na hapa, hakuna wa kumlaumu,” alisema baba.
Hofu ikazidi kuongezeka kwenye moyo wangu. Kama nilivyoeleza, hakuna sehemu niliyokuwa naiogopa kama makaburini, nikawa nahisi kama mwili na akili vinatengana. Kibaya zaidi ilikuwa ni usiku na nimeshawahi kusikia kwamba makaburini nyakati za usiku kunakuwa na mambo mengi sana ya ajabu, sikuelewa baba anavyosema tunamchukua yule dereva bodaboda aliyefariki kwenye ajali, alimaanisha nini.
Ninavyojua mimi, huwezi kufukua kaburi na kutoa maiti kwa sababu kwanza siyo kazi nyepesi lakini pia, lazima watu watakuona ukiwa unalifukua kwa sababu makaburi mengi huwa yanakuwa na ulinzi, na kama si hivyo, mizimu mibaya iliyopo makaburini lazima itakudhuru tu. Sikuelewa malengo ya baba ni nini lakini kama mwenyewe alivyokuwa anasisitiza kwamba lengo ni kunisaidia mimi, ilibidi nitulie kuona mwisho wake.
Baada ya kuzungumza na mimi, alimfuata baba yake Rahma, wakawa wanajadiliana jambo pale, wakazungumza kwa zaidi ya dakika mbili kwa sauti ya chini kiasi kwamba sikuwa nikisikia walichokuwa wanakisema.
Baada ya hapo, baba yake Rahma alinifuata na kuniambia natakiwa kuvua nguo zote na kukaa juu ya kaburi kwa sababu kazi iliyokuwa inaenda kufanyika, si ya kitoto. Nilishtuka, yaani nivue nguo halafu nikae juu ya kaburi? Mapigo ya moyo yakaanza kunienda mbio tena.
Ni kama baba yake Rahma alinielewa jinsi nilivyokuwa na hofu, akaniambia sitakiwi kuwa na hofu yoyote kwa sababu kwenye jamii yao, kukaa bila nguo ni kitu cha kawaida kabisa, isitoshe wao ni baba zangu ambao wananijua tangu nikiwa mtoto mchanga, kwa hiyo lazima nifanye walichoniambia.
Ilibidi nikubaliane naye maana baba alikuwa akisisitiza kwamba muda unakwenda. Nikasogea pembeni na kuvua nguo zote, nikajiziba sehemu ya mbele kwa mikono yangu na kupanda kwenye tuta la lile kaburi, nikawa natetemeka mno.
Baada ya kukaa juu ya tuta la kaburi, nikiwa nimeupa msalaba mgongo kama nilivyoelekezwa, baba na baba Rahma, mmoja akiwa amesimama upande wa kichwani na mwingine upande wa miguuni, walianza kuimba nyimbo za kutisha kwa kupokezana, akiimba baba, baba yake Rahma anaitikia, wakaendelea hivyo kwa dakika kadhaa kisha wakaanza kulizunguka lile kaburi, kutoka kulia kwenda kushoto.
Walifanya hivyo kwa dakika kadhaa, baadaye baba akaniambia nisimame. Nilifanya hivyo huku nikijiziba kwa soni, akanielekeza kuelekea upande ule wa kichwani niliokuwa nimesimama awali, kisha akaniambia niwe makini kutazama anachokifanya.
Milio ya bundi na ndege wengine wa usiku, iliendelea kusikika na kufanya hali iwe ya kutisha mno pale makaburini. Baba alionesha kwa ishara kwamba natakiwa kupiga makofi na kupiga mguu wangu wa kushoto chini kwa nguvu, na vyote vifanyike kwa wakati mmoja.
Alinihesabia kwa alama za vidole kisha akaniruhusu, nikapiga makofi kwa nguvu na wakati huohuo nikapiga kishindo cha nguvu. Alinionesha kwa ishara kwamba natakiwa kufanya hivyo mara tatu, nikarudia mara ya pili, kisha nikafanya kwa mara ya tatu.
Kilichotokea baada ya kufanya hivyo kwa mara ya tatu, kilinifanya nihisi kama mwili wangu unakufa ganzi kwa hofu, sijawahi kushikwa na hofu kama niliyoipata siku hiyo na kama baba asingeniwahi, huenda ningedondoka kama mzigo chini maana mwili wote uliisha nguvu.
Japokuwa ilikuwa ni usiku, tena nikiwa sina nguo na kulikuwa na baridi kali, nilihisi kijasho chembamba kikinitoka, ama kweli duniani kuna mambo na ukishangaa ya Musa, utayaona ya Firauni.
Je, nini kilitokea? Usikose next issue.
 
The Graves of The Innocents (Makaburi ya Wasio na Hatia)- 59
ILIPOISHIA:
Kilichotokea baada ya kufanya hivyo kwa mara ya tatu, kilinifanya nihisi kama mwili wangu unakufa ganzi kwa hofu, sijawahi kushikwa na hofu kama niliyoipata siku hiyo na kama baba asingeniwahi, huenda ningedondoka kama mzigo chini maana mwili wote uliisha nguvu.
Japokuwa ilikuwa ni usiku, tena nikiwa sina nguo na kulikuwa na baridi kali, nilihisi kijasho chembamba kikinitoka, ama kweli duniani kuna mambo na ukishangaa ya Musa, utayaona ya Firauni.
SASA ENDELEA...

Kitendo cha kufuata maelekezo yale tu, mara kaburi lilifunuka lote, yaani ule udongo wote uliokuwa umetumika kulifukia, ukapotea kiasi kwamba kila kitu kilichokuwa ndani ya kaburi kilikuwa kikionekana.
“Ingia tukasaidiane kumtoa kwenye jeneza,” alisema baba, nikajikuta nguvu za kuendelea kusimama zimeniisha maana miguu ilikuwa ikitetemeka kuliko kawaida, nikakaa kwenye kaburi lililokuwa pembeni, uso wote ukiwa umelowa kwa machozi.
Ni hapo ndipo nilipoelewa kwa nini baba alikuwa akiniambia kwamba bado sijakomaa kiakili na sitakiwi kuingizwa kwenye hayo mambo.
“Inuka acha kuleta mambo ya kijinga hapa, upumbavu wako ndiyo uliotufikisha hapa,” alisema baba kwa ukali, nikajikakamua na kusimama huku nikiwa bado natetemeka. Alichokifanya baba baada ya kuona kama nasuasua, alinisukumia ndani ya lile kaburi, nikaporomoka na kwenda kujibamiza kwenye jeneza.
Nilijikuta nikipiga kelele kwa sauti kubwa huku nikitafuta sehemu ya kutokea, kwa kuwa ilikuwa ni ndani ya shimo kelele zangu hata hazikufika mbali, zikawa zinajirudia na kusababishwa mwangwi. Tayari baba naye alishaingia mle kaburini, akaninyamazisha kwa ukali kama kawaida yake.
“Wewe ndiyo unatakiwa uifanye hii kazi, mimi nakusaidia tu,” alisema huku akihangaika kulifungua jeneza lililokuwa na ule mwili.
Nisingependa sana kueleza kuhusu kipengele hiki kwa sababu hata mwenyewe nikikumbuka huwa naogopa sana, lakini kwa kifupi, nilisaidiana na baba kuutoa ule mwili kwenye jeneza, sanda yote ikiwa imelowa damu hasa maeneo ya kichwani inakoonesha marehemu aliumia sana kwenye ile ajali.
Tukautoa na kuulaza pembeni ya kaburi huku lile jeneza baba akilirudishia kama lilivyokuwa mwanzo. Huku nikitetemeka kuliko kawaida, baba aliniamuru tena kufanya kama nilivyofanya mwanzo, nikafanya mara ya kwanza, ya pili, kisha nikafanya mara ya tatu.
Cha ajabu kaburi lilijifukia vilevile na kurudi kama lilivyokuwa mwanzo, tofauti yake ni kwamba kidogo lilikuwa limetitia. Ni hapo ndipo nilipoamini kauli niliyokuwa nikiisikia kwa muda mrefu, kwamba ukiona kaburi jipya limetitia sana, kuna uwezekano mkubwa kwamba kilichozikwa ndani siyo mtu au kama ni maiti, basi imechukuliwa na wachawi.
Baada ya zoezi hilo kukamilika, baba aliniamuru niibebe ile maiti huku baba yake Rahma akinitoa hofu kwamba mtu akishakufa hana madhara yoyote, hawezi kunidhuru kwa namna yoyote, nikajikakamua na kuiweka begani, tukaanza kuondoka makaburini hapo huku ikichuruzika vitu ambavyo hata bila kutazama nilijua ni damu.
Unajua baadaye nilikuja kujifunza kitu kingine, kwamba watu wanaofariki katika mazingira ya kishirikina, unaweza kutambua maiti zao kwa haraka kama na wewe una uelewa kuhusu mambo hayo, kwa sababu kwanza imezoeleka kwamba mtu akifa mwili wake hupoa na kuwa wa baridi sana lakini kama amekufa kwa mipango ya watu, mwili huendelea kuwa na joto kwa muda mrefu.
Pia maiti za namna hii zinakuwa na kawaida ya kutoka damu. Inafahamika kwamba mtu akifa, moyo unakuwa umeacha kusukuma damu kwa hiyo hata mzunguko mzima wa damu nao unasimama lakini kwa watu waliochukuliwa kabla ya muda wao, japo kwa nje anaonekana amekufa, bado mzunguko wa damu unakuwa unaendelea japo kwa kasi ndogo sana na ndiyo maana, utakuta maiti inatoka damu puani, mdomoni, masikioni au kama ni ya ajali kama hiyo, majeraha yanakuwa yanaendelea kuchuruzika damu.
Tulitoka huku nikijikaza kiume na ule mwili begani kwa sababu ulikuwa mzito sana lakini kwa kuwa na mimi kidogo nilikuwa na ubavu, niliweza kuhimili uzito huo mpaka kwenye mti mkubwa uliokuwa pembeni ya makaburi hayo, kama kawaida, maandalizi ya safari yakaanza kufanyika ambapo baba aliniambia niulaze ule mwili chini.
Mchakato ulifanyika na kama kawaida, muda mfupi baadaye, akili ilinitoka, nilipokuja kuzinduka, tulikuwa tayari kwenye lile eneo letu tunalokutania, watu wengi wakiwa wamezunguka na kutengeneza duara kama kawaida huku nyimbo za ajabuajabu zikiendelea kuimbwa na kuifanya hali iwe ya kutisha sana.
“Mkuu akikusogelea, inabidi uinamishe kichwa chako chini na kuweka mikono hivi maana umefanya makosa,” baba aliniambia kwa sauti ya chini, akinielekeza nini cha kufanya. Kwa mbali nikawa namuona Mkuu akija huku kama kawaida yake, vishindo vyake vikisikika eneo lote hilo.
Baba na baba Rahma walimsogelea na kuinamisha vichwa vyao kwa utii, akawa anawagusa na mkia wa mnyama ambaye simjui, aliokuwa ameushika, harakaharaka wakaondoka na kwenda kukaa kule walikokuwa wamekaa wale watu wengine.
Mkuu akanisogelea mpaka pale nilipokuwa nimepiga magoti huku uso wake akiwa ameukunja, nilipomtazama mara moja sikurudia tena kumtazama kwa sababu alikuwa anatisha sana. Nilizoea kumtazama akiwa hajakasirika lakini siku hiyo alikuwa kama mnyama mkali wa porini kwa jinsi alivyokuwa anatisha, midomo ikimchezacheza kwa hasira.
Ilibidi niinamishe kichwa kama baba alivyonifundisha, mikono nikaiweka kifuani kwa unyenyekevu, aliendelea kunitazama bila kusema chochote kwa sekunde kadhaa kisha nikasikia akinipigapiga na ule mkia.
“Sirudie masiku mengine,” alisema Mkuu kwa Kiswahili kibovu huku akiendelea kunipigapiga, kidogo kamoyo kalitulia ila nilichojifunza ni kwamba kumbe nilikuwa nimefanya kosa kubwa sana na pengine bila kufanya kile tulichokifanya kwa msaada wa baba na baba yake Rahma, huenda huo ndiyo ungekuwa mwisho wangu.
Kumbe ndiyo maana ni rahisi sana kusikia wachawi wamekufa ghafla vifo vya kutatanisha, wakati mwingine inakuwa ni kukosea masharti kama kilichotaka kunitokea mimi na adhabu inayomfaa mtu anayekiuka masharti, ni kuuawa na kuliwa nyama, kama siyo yeye basi mtu wake wa karibu.
Baada ya kupitisha msamaha kwangu, niliinua uso wangu, mkuu akaugeukia ule mzigo niliokuwa nao ambapo kwa kutumia kisu kikali alikata ile sanda kisha akanigeukia na kutingisha kichwa, akainua ule mkia wake juu na watu wote wakapaza sauti zao kutamka maneno ambayo hata sikuwa nayaelewa.
Basi kilichoendelea hapo ni utaratibu wa kawaida, watu wakala na kucheza ngoma huku mara kwa mara Mkuu akinikata jicho kama anayenichunga kuhakikisha siharibu kitu kingine.
“Amefurahishwa na kazi uliyoifanya, amesema anataka kukuongeza nguvu maana japikuwa umefanya makosa, lakini kupitia makosa hayo umeweza kuonesha ushujaa ambao wengine huwa wanashindwa, mshukuru sana baba yako,” baba Rahma aliniambia kwa sauti ya chini, nikageuka kumtazama Mkuu, macho yake na yangu yakagongana, nikamuona akiachia tabasamu hafifu.
“Akikupa nafasi ya kuchagua akuongezee uwezo gani utachagua nini?”
“Nataka niwe na uwezo wa kupata hela kirahisi, nataka kuwa tajiri.”
“Tajiri? Utajiri wa kichawi ni mbaya sana, jaribu uone mwenyewe, bora hata uombe kitu kingine chochote,” alisema baba yake Rahma lakini maneno yake wala hayakuwa yakiniingia akilini. Kiukweli na mimi nilikuwa natamani kuwa tajiri kwa sababu tangu nizaliwe, maisha yetu yalikuwa ya kimaskini kule kijijini na umuhimu hasa wa kuwa tajiri, niliuona baada ya kufika mjini.
Vijana wadogo tu kama mimi, wengine hata nawazidi lakini wanaendesha magari ya kifahari barabarani, kwa nini na mimi nisionje kidogo hata kama ni mbaya? Wakati akiendelea kunipa nasaha zake, Mkuu alinipa ishara kwamba nimfuate, harakaharaka nikainuka na kumuacha baba yake Rahma akiendelea kuongea.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom