Hii ndiyo risala ya wapigakura wa Kyela kwa Mbunge wao
RISALA YA WAPIGAKURA WA KYELA KWA MBUNGE WA KYELA DK. HARRISON MWAKYEMBE JUMAPILI TAREHE 29 MACHI, 2009
Mheshimiwa Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, awali ya yote sisi wapigakura wa Wilaya ya Kyela tunakupa pole kwa msiba uliokupata hivi karibuni wa mama yetu mpenzi, Tukusuma Kibole Mwakyembe. Ninawaomba wapigakura wenzangu wote tuliopo uwanjani hapa tukae kimya kwa dakika moja kwa heshima na kumbukumbu ya marehemu. Ahsanteni.
Mheshimiwa Mbunge, naomba vilevile nikushukuru kwa kukubali mwaliko wetu (tuliokutumia rasmi jana jioni) wa kuyapokea maandamano haya yaliyoanzia Community Centre mpaka hapa Uwanja wa Mwakangale. Madhumuni ya maandamano haya ni kuelezea hisia zetu na kupata maelezo yako kuhusu maana na lengo la kampeni ya chuki ya magazeti yanayomilikiwa na Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz. Mbali na kuonyesha dhahiri nia ya kutaka kukuchafua tu kisiasa, magazeti hayo sasa yanadai Mbunge wetu uondolewe ubunge.
Mheshimiwa Mbunge, katika toleo la Machi 24 hadi 30 mwaka huu la gazeti la TAZAMA, moja ya magazeti lukuki anayomiliki Rostam, imeelezwa bayana kwamba utasimamishwa ubunge. Taarifa hii imetushitua sana wapigakura wa Kyela na kutufanya wengi tujiulize KULIKONI? Rostam Aziz, pamoja na kwamba ni fisadi asiyeguswa nchi hii, kapata wapi nguvu na mamlaka ya kumwondoa Mbunge aliyechaguliwa kwa asilimia 93 ya wapiga kura wa Kyela?
Kiu yetu kubwa ya kutaka kuujua ukweli, imezaa wazo la kuja hapa uwanjani leo hii ili utupe picha sahihi badala ya kutegemea maelezo ya juujuu ya magazeti ambayo tayari yamegubikwa na ushabiki.
Mheshimiwa Mbunge, wapigakura wa Kyela tulikusikiliza kwa makini sana ulipoongea na vyombo vya habari Dar es Salaam tarehe 17, mwezi huu. Tulielewa kuwa kampuni hiyo anayoiimba Rostam usiku kucha (ili kukulaumu mbunge wetu) haikuwa miongoni mwa makampuni yaliyojitokeza na kushiriki kwenye mchakato wa zabuni ya umeme wa dharura, na kwamba pamoja na uchanga wake kampuni hiyo ambayo imeanzishwa kushughulikia nishati ya upepo isingeweza kushiriki kwenye zabuni iliyolenga uzalishaji umeme kwa kutumia gesi asilia tuliyonayo. Sasa katika hali hiyo, mgongano wa kimaslahi ambao Rostam Aziz anauimba kila kukicha utokee wapi kama si porojo na uchochezi tu wa kisiasa?
Ikiwa sisi wapigakura wa Kyela (pamoja na uelewa wetu mdogo) tulikuelewa, ni nini kinamfanya Rostam Aziz asielewe? Ni nini kinamfanya kiongozi mwandamizi wa CCM, kama Rostam (ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM) ahangaike kiasi hicho kujaribu kumbomoa kiongozi mwenzake wa CCM, ambaye pia ni Mjumbe wa NEC? Mheshimiwa Mbunge sisi wapigakura wako tunakuomba leo utueleweshe, tujue: KULIKONI!
Mheshimiwa Mbunge, baadhi yetu tunaosoma sana magazeti tunaelewa kuwa Rostam Aziz hajaanza leo kukuchafua. Ameanza tangu Kamati Teule ya Bunge iwasilishe taarifa yake Bungeni mwezi Februari mwaka juzi, 2007 kupitia magazeti yake lukuki ya Mtanzania, Rai, Tazama, Tanzania Leo, Nyundo, Sauti ya Umma, Taifa Tanzania, the African n.k. Tangu muda huo, siku haipiti bila habari au maoni au makala moja au zaidi inayomshambulia Mbunge wa Kyela: mara kaiba maji ya DAWASCO, mara yeye na wenzake waliandika taarifa yao baada ya muda kupita; mara si mwanamtandao; mara anatumiwa na maadui wa Lowassa na Rostam na mambo mbalimbali ya kipuuzi ambayo yamekuja onekana baadaye kuwa uongo mtupu.
Lengo kuu la Rostam Aziz linajulikana kwa Watanzania wote, hata sisi wananchi wa kawaida tu: kuwasafisha wale wote waliohusishwa na kashfa ya Richmond na kuwabeza na kuwazomea wale wote waliokuwa wajumbe wa Kamati Teule ya Bunge.
Tunazo taarifa za uhakika za mafisadi kukutana mara kwa mara kupanga njia za kuwamaliza kisiasa na hata kuwaua wanasiasa jasiri wanaotetea maslahi ya Taifa, ukiwemo Mbunge wetu. Vyombo husika vya dola visilifanyie mzaha suala hili. Ni hatari kwa mstakabali wa Taifa letu!
Tumeona kwa masikitiko makubwa kuwa Rostam akiguswa kidogo tu, kama ambavyo Mbunge wetu ulivyomgusa tarehe 17 mwezi huu, viongozi waandamizi wa CCM wanajitokeza mara moja kuingilia kati. Bahati nzuri Mbunge wetu hukufungua tena mdomo, lakini Rostam Aziz kwa kutumia magazeti yake hayo ya udaku, ameendelea na kampeni yake hiyo chafu bila wasiwasi na bila kukemewa.
Sisi wapigakura wa Kyela tunajiuliza na tunataka kujua: Je hii ni sera ya CCM? Je, Rostam anaendesha mchezo huu mchafu tena kwa muda mrefu dhidi ya viongozi wenzake kwa Baraka za Chama? Kama si hivyo, mbona Chama cha Mapinduzi hakikemei mchezo huo mchafu wa Rostam?
Mheshimiwa Mbunge, leo wapigakura wa Kyela tunamtumia Rostam Aziz ujumbe ufuatao: Pamoja na mbinu zake za kifisadi, hawezi kumwondoa mbunge wetu madarakani! Vilevile Bwana Rostam atambue kuwa Dk. Mwakyembe alichaguliwa na asilimia 93 ya wapigakura wa Kyela na atake asitake katika uchaguzi mkuu mwakani wana-Kyela tunasema: RAIS NI JAKAYA MRISHO KIKWETE na MBUNGE NI HARRISON GEORGE MWAKYEMBE!
Tunamtahadharisha Rostam Aziz kuwa kama huko nyuma alizoea kuwaangusha watu kwa kutumia vijigazeti vyake hivyo vya kigaidi, safari hii amekwaa kisiki cha mpingo!
Tunaomba vilevile tutume ujumbe wa pili kwa CCM. Wana-Kyela tunaipenda sana CCM, chama cha Baba wa Taifa ambaye daima tutampenda na kumuenzi! Ili CCM ipate ushindi wa uhakika na wa kishindo mwakani, lazima iandae mazingira mazuri kwa ushindi huo: iwaondoe katika safu ya uongozi watu wote wenye tuhuma za ufisadi. Kwa mfano, tunaelezwa na vyombo vya habari vinavyoaminika kuwa Rostam Aziz ana tuhuma ya kuchota fedha za EPA zaidi ya shilingi bilioni 40 kupitia kampuni yake ya KAGODA, lakini bado ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM!
Hivi, CCM bila Rostam Aziz na mafisadi wenzake, haiwezekani? Mheshimiwa Mbunge, kwa hayo machache tunaomba tusikie sauti yako na sisi tutakuwa mabalozi kwa wenzetu wengine ambao hawakuelezwa na hawajafika hapa.
Kyela Oyee!!! Mwakyembe Oyee!!! Rostam Aziz na Mafisadi Wenzake ziiiii!!!
Imesomwa na Gabriel Mwakalinga, Katibu wa Kamati ya Maadalizi ya Maandamano ya Amani ya Wapigakura wa Kyela, tarehe 29 Machi, 2009.