Mzindakaya alipuliwa bungeni
na Mwandishi Wetu, Dodoma
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
WABUNGE wawili wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameeleza kusikitishwa kwao na tabia ya baadhi ya wabunge wenzao kuwashambulia wenzao wanaotoa maoni yao kuhusu viongozi wakuu serikalini na wale waliostaafu.
Mtu wa kwanza kueleza dukuduku lake hilo alikuwa ni Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shellukindo ambaye katika mchango wake alioutoa juzi jioni wakati anajadili hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopitishwa jana jioni, alisema kuwa anaamini michango inayotolewa na wabunge hailengi mtu bali inazingatia umuhimu wa hoja.
Mbunge huyo ambaye ni mke wa mwanasiasa mkongwe na Mbunge wa Bumbuli, William Shellukindo (CCM) alisema wabunge wamekuwa wakichangia mijadala mbalimbali bungeni, lengo likiwa ni kuhakikisha Watanzania wanasaidiwa kupiga hatua za maendeleo na si vinginevyo.
"Lengo na nia (ya kutoa hoja hizo) ni moja tu kuhakikisha Mtanzania anatoka hatua moja kwenda nyingine," alisema Shellukindo kauli ambayo ilionekana waziwazi kukosoa hoja zilizotolewa na Mbunge wa Kwela, Chrisant Mzindakaya (CCM) au Mbunge wa Kyela, Harrison Mwakyembe (CCM).
Aliwataka watu wanaodhani kuwa yanayosemwa bungeni na baadhi ya wabunge yanamlenga mtu fulani kuachana na fikra hizo kwani hilo si lengo la kauli hizo.
Mbunge huyo alikwenda mbali zaidi kwa kuwalaumu baadhi ya wabunge na viongozi kwa kusema kuwa wameshindwa kufikiri na kuwa wabunifu, na ndiyo maana mambo mengi yanakwama.
"Hata hapa bungeni watu hawafikiri, wanasubiri mtu aseme halafu wao wanadakia hoja," alisema Shellukindo pasipo kufafanua.
Muda mfupi baadaye, Mbunge wa Vunjo, Aloyce Kimaro (CCM) ambaye ndiye aliyekuwa wa kwanza kumnyoshea kidole Rais mstaafu Benjamin Mkapa wakati wa mkutano uliopita wa Bunge, alisimama na kusisitiza hoja hiyo ya Shellukindo.
Akizungumza huku akinukuu, vifungu kadhaa katika ahadi za wanachama na viongozi wa CCM, Kimaro alisema anaamini kila mbunge anayo haki ya kutoa maoni yake kuhusu mambo anayoyatetea pamoja na yale anayotumwa na wapiga kura wake.
Miongoni mwa ahadi alizonukuu Kimaro, ambaye hoja yake hiyo dhidi ya Mkapa imezua maneno ya kumpinga ndani ya vikao vya CCM na miongoni mwa wabunge wenzake wa CCM, ni zile zisemazo; Nitaitumikia nchi yangu kwa nguvu na moyo wangu wote, Rushwa ni adui wa haki, sitatoa wala sitapokea rushwa, Cheo ni dhamana, sitatumia cheo changu au cha mtu mwingine kwa manufaa yangu binafsi na ile isemayo Nitasema kweli daima fitina kwangu mwiko.
Alisema mbunge au mwananchi yeyote anapotoa maoni yake, hapaswi kushambuliwa kwa sababu anafanya hivyo akilindwa na katiba, sheria na kanuni zilizopo.
"Kwa hiyo hapa bungeni ni ukweli, fitina ni mwiko, tukisimamia hilo maisha bora yatapatikana
hakutakuwa na kutafutana
CCM si mali ya mtu, ni ya wanachama," alisema Kimaro.
Alisema kuwa kila mtu anapaswa kula jasho lake mwenyewe, lakini inashangaza kuwa siku hizi vitendo vya rushwa, wizi na ubadhirifu wa fedha za serikali, vimegeuka kuwa wimbo wa taifa.
"Kila Mtanzania na kiongozi lazima akemee mambo haya. Rais na Waziri Mkuu wanakemea, lazima tuwaunge mkono kama tusipowaunga mkono, nani mwingine atawaunga?" alihoji mbunge huyo.
Kimaro aliwataka watu wanaosikiliza tuhuma zinazotolewa kutoona kuwa zinalenga kumchafua mtu kwani hata ilipoelezwa awali kuwa fedha za EPA zimeibwa, watu hawakuamini hadi rais alipotangaza kuwa ni kweli sh bilioni 133 za EPA zilikuwa zimeporwa.
Alisema yeye amejitolea kumuunga mkono rais katika suala hilo na kamwe hatorudi nyuma.
"Wapo watu hapa wanasema, wana sauti zao kubwa wengine wanapayuka
waache wapayuke, kama microphone zitapasuka Spika ataweka nyingine...Wenye kusema taratibu nao waendelee kusema na sauti zao zichome kama mwiba...Wengine wanasema sungura ni mdogo, jamani Tanzania ni ndovu mkubwa tuna kila kitu humu, lakini wanakula wachache, Tanzania ni nchi nzuri," alisema.
Katika kauli yake, Mzindakaya aliwanyooshea kidole wabunge wanaomtuhumu Mkapa na kusema kiongozi huyo mstaafu amefanya mambo mengi kwao, ikiwamo na kufanikisha ujenzi wa jengo la kisasa la Bunge.
Aidha, aliishangaa serikali kwa kuendelea kukaa kimya wakati kiongozi huyo akituhumiwa na kuchafuliwa na watu pamoja na vyombo vya habari.