2009-04-19 21:35:40
Na Restuta James
Mbunge wa Kishapu (CCM), Fred Mpendazoe, ametoa changamoto kwa wazee wa Chama Cha Mapinduzi kukishinikiza chama hicho kiwafukuze wanachama wake wanaotuhumiwa kuhusika katika kashfa mbalimbali za ufisadi badala ya kuwakebehi wanaoongoza mapambano hayo kwa kuwaita wanatafuta umaarufu wa kisiasa na umaarufu wa mtu binafsi.
Mpendazoe aliyasema hayo jijini Dar es Salaam, alipozungumza na gazeti hili na kutoa maoni yake juu ya tamko la wazee hao, vita dhidi ya ufisadi na rushwa.
Bila kuwataja, alisema wanachama wa CCM wanaotuhumiwa kuhusika katika kashfa mbalimbali za ufisadi ni sawa na misumari ndani ya chama na hivyo wazee wanapaswa kukishinikiza chama kiwaondoe kwenye nyadhifa walizonazo.
Nilitegemea wazee wetu katika kumuunga mkono Mwenyekiti wetu wa chama, Rais Jakaya Kikwete, katika vita dhidi ya ufisadi wangetoa tamko kwamba chama kiwaondoe kwenye nyadhifa wale wote wanaokichafua kwa kuthibitika kuhusika na ufisadi mbalimbali, kwani kuwaacha na nyadhifa wanakuwa ni sawa na mzigo wa misumari kwa chama, alisema.
Alisema sio sahihi kuwaita wanaopambana na rushwa kuwa wanatafuta umaarufu wa kisiasa au umaarufu binafsi ilihali vitendo hivyo vinaongeza ufa kati ya walionacho na wasionacho.
Alitoa mfano kwamba ubadhirifu uliofanywa na watu wachace kupitia kampuni za Meremeta, Richmond na nyinginezo unakadiriwa kufikia Sh. trilioni 1.25, ambazo kama zingetumiwa kwa manufaa ya taifa zingeweza kujenga barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 500 au madarasa 7, 500.
Sio sahihi wazee hawa kuona watu wanaopambana na ufisadi wanatafuta umaarufu ilani ya CCM na katiba ya nchi yetu vinatamka bayana kabisa kwamba kila mwananchi anapaswa kushiriki katika ulinzi wa rasilimali za taifa letu, tunapaswa kuwaunga mkono wale wote wenye nia ya dhati ya kulinda mali za taifa kwa manufaa ya Watanzania wote, alisema.
Kuhusu Jumuiya za CCM kutangaza kumuunga mkono Rais Kikwete na kuwataka wanaotaka kugombea urais mwaka ujao wahame CCM, alisema nia hiyo si sahihi kutangazwa sasa kwa sababu kufanya hivyo ni kuwanyima wananchi haki ya kumchagua mgombea watakayempenda.
Alisema suala la nani awe mgombea urais lipo mikononi mwa wanachama baada ya mgombea kutangaza nia yake ya kutaka kuwa Rais wa nchi hivyo, kufanya maandamano sasa ya kumuunga mkono mgombea fulani ni sawa na kuwashinikiza wanachama wa chama hicho wakubaliane na matakwa ya viongozi wao.
Yanayoanza kutokea ni dalili za mizengwe, nawakumbusha wanachama wenzangu wasubiri muda ufike na wazingatie taratibu za kumpata mgombea na wakumbuke pia kuwa kila mwanachama mwenye sifa anayohaki ya kupiga na kupigiwa kura alisema.
Amewataka wanachama wenzake kuacha chokochoko zisizo na msingi na badala yake wapambane na changamoto nzito zinazolikabili taifa kwa sasa.
Mpendazoe amelipongeza Bunge, Rais Kikwete na Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Reginald Mengi kwa kuongoza vita dhidi ya ufisadi na kuwataka wasikate tamaa.
Kadhalika, amewapongeza wabunge wa CCM wanaopambana na ufisadi akiwemo Anne Kilango Malecela, Same mashariki (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe, Kyela (CCM), Lucas Selelii, Nzega (CCM) na Aloyce Kimaro, Vunjo (CCM).
Mapema wiki iliyopita Wenyeviti wastaafu wa mikoa wa (CCM) wakiongozwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa mkoa wa Dodoma, Pancras Ndejembi, walionya watu wasitumie vita ya ufisadi kama mtaji wa kisiasa na kujipatia umaarufu.
* SOURCE: Nipashe