Kuanguka kwa CCM - Unabii Utatimia!

Kuanguka kwa CCM - Unabii Utatimia!

Kuanguka kwa CCM – Unabii Utatimia?

Iko siku ambapo Watanzania wataamka na watakuta kwamba Chama cha Mapinduzi hakishiki tena hatamu za uongozi wa nchi, na badala yake Ikulu na Bunge vimechukuliwa na chama kingine. Siku hiyo ambayo haina jina, itakuwa ni siku ambapo Chama cha Mapinduzi kitaanguka kwa kishindo kikuu na sauti ya kuanguka kwake itasikika kila kona ya Tanzania, na mwangwi wa kuporomoka kwake kurindima katika bara letu la Afrika na mabaki ya mtetemo wa kuvunjikavunjika kwake kusimuliwa kama hadithi za Alfu Leyla wa Uleyla kwa vizazi vijavyo vya Watanzania. Kuanguka kwa Chama cha Mapinduzi kutakuwa ni mwanzo wa msemo, na bila ya shaka kutatungiwa methali.

Siku hiyo ni siku ambayo kina Malecela, Msuya, Kingunge, Kikwete,Lowassa,Makamba,Karume na magwiji wengine wa Chama hicho waombee wasijeiona. Kwani itakuwa ni siku ya huzuni kwa watawala na furaha kwa watawaliwa! Itakuwa ni siku ambapo "nyota ya jaha" itaangazia Taifa letu na nuru ya "jua la haki" itachomoza na miale yake kumulika kila kona ya Taifa letu. Hiyo ni siku ambapo kama mwali atolewaye nje, kila mtu atatamani kuiona isipokuwa wale ambao huyo mwali ni ishara ya wao kukosa mke na wengine kupata!

Bila ya shaka unajiuliza iweje nianze kwa kusema maneno hayo. Nilikuwa natafakari maneno ya Mwalimu aliyoyatoa mwanzoni mwa miaka ya 90 mara baada ya vyama vingi kuruhusiwa tena nchini. Baada ya Mwalimu Nyerere kutoa maneno makali ya "Ikulu inanuka Rushwa" watu wengi walianza kujiuliza mapenzi ya Mwalimu kwa chama alichokiasisi na kama anaweza kujitoa kwenye chama hicho. Alipoulizwa kuhusu kujiondoa CCM, mwalimu alijibu "CCM siyo Mama yangu". Maneno hayo ya Mwalimu yamebakia mawazoni mwangu (na bila shaka ya wengine pia) kama unabii na kama wosia. Hii leo kuna baadhi ya viongozi wa Chama tawala ambao wanasisitiza maneno ya Mwalimu ya "Bila CCM madhubuti Tanzania Itayumba" na kusahau kabisa maneno hayo ya onyo kali kuwa hata kama mtu ana mapenzi kiasi gani na CCM, iko siku anaweza kukiacha na kujitahidi kukivunja! Ni rahisi kukiacha CCM kuliko kumuacha Mama mzazi!

Siku hiyo ambapo Chama hiki maarufu kitakapojikuta kiko katika kambi ya upinzani ndipo viongozi wake na mashabiki wake watakapotambua kuwa "CCM siyo Mama" na Tanzania itaendelea na inaweza kuwepo bila CCM kuwa madarakani! Hiyo siku iso jina, iko, yaja, na yafanya hima kufika! Kwanini basi CCM itakuja kuanguka kwa mshindo mkuu namna hiyo?

Ndugu zangu, punda mnyama wa kazi kuna mahali anafikia kikomo! Na akifikia kikomo, punda hendi hata kwa mijeredi mia. Mtu unaweza kumtwisha punda mizigo, lakini akifikia kikomo chake hata umfanye nini punda hanyanyui mguu. Kuna baadhi ya viongozi ambao wanadhani kuwa Watanzania wataendelea kuinama na kukubali kutwishwa mizigo ya kila namna kana kwamba hawasikii maumivu! Ni hawa viongozi ambao huendelea kutuingiza katika mikataba mibovu, wanaendelea kuvumilia ufujaji wa mali ya umma katika maofisi yao, wanaendelea kupuuzia rushwa hadi imezoeleka na kuonekana kama kawaida. Viongozi hawa wanaimba wimbo na pambio ya uongozi bora wakitumbuiza kwa kasida za maneno ya kizalendo. Mawazoni mwao wanaishi wakifikiri kwamba Watanzania wataendelea kuvumilia. Kama punda iko siku hugoma, iko siku Watanzania nao watasema "Sasa inatosha"!

Siku moja ambayo ipo, Watanzania watajiuliza iweje viongozi wetu wanunue rada Bilioni 40 wakati hospitali yetu ya kijiji yenye kugharibu shilingi milioni moja haina hata bomba la maji! Hiyo siku Watanzania watajiuliza iweje ili kupata elimu nzuri ni lazima wapeleke watoto wao kwenye shule binafsi wakati shule za serikali zilizokuwa zikisifika huko nyuma zikibakia historia? Hawa wana na mabinti wa Tanzania wataamka siku moja na kusema "Imetosha".

Chama cha Mapinduzi kitaunguka pia kwa sababu hatimaye Watanzania wataelewa ya kwamba kuendelea kukaa kwa chama hicho madarakani ni kujitakia kutokuendelea na kurudi nyuma kwa maisha yao. Wataelewa kuwa CCM haina lengo hata chembe la kutimiza na zaidi ya kutimiza ahadi zake ambazo imekuwa ikizitoa tangu uhuru. Itadhihirika kuwa CCM iko madarakani ili kuendelea kujikita katika kutawala huku wakifanya mambo machache ya manufaa kwa wananchi huku viongozi wao na watu wachache waliobarikiwa na chama hicho wakiishi katika paradiso ya Bongo.

CCM itaunguka kwa sababu hata kipofu akigonga ukuta anauzunguka! Kutokuona siyo kikwazo cha kujua kukwama. Chama cha Mapinduzi kimekuwa kikifanya mambo kana kwamba Watanzania wote ni vipofu na viziwi. Miaka nenda rudi tumewapa imani kuwa labda watabadilika. Wanavutia kwa maneno matamu na nyimbo za shangwe, wanafurahisha kwa rangi nzuri za mavazi yao, na mvuto wa kupepea kwa vibendera vyao vya kijani! Lakini wamekuwa kama makaburi yaliyopakwa chokaa, lakini ndani yake ni mifupa mitupu! Siku hiyo watanzania watakuwa kama kipofu aliyeona mwezi. Watagundua kuwa CCM siyo jua bali ni mwezi mchanga na mwanga ambao watu wamekuwa wakiusifia si mwangaza wa jua, bali mmuliko wa mbalamwezi. Watagundua kuwa wanachotaka kimulike maisha yao na kuanzia maisha ya watoto wao ni chama na viongozi wenye nuru ya jua, ambao mwangaza wao hautegemei kuakisiwa na kitu kingine bali unatoka ndani yao wenyewe! Wataamua kuachana na Chama ambacho miaka nenda rudi kimekuwa kikijificha kati yao mwangaza wa jua na hivyo kuwapa kivuli cha "kupatwa jua". Watu wamekuwa wakiogopa kuwa huo mwezi ukiondoka kati yao na jua, dunia itafikia mwisho! Kumbe zote hizo ni porojo. Mwezi huzija jua, lakini hatimaye hupisha!

Chama hicho kitaanguka si kwa sababu hakina watu wenye sura nzuri, na watanashati kwani wamejaa tele, siyo kwa sababu hakina watu waliosoma na kubobea katika nyanja mbalimbali kwani wapo bwelele, bali kwa sababu wale waliodhaminiwa uongozi katika chama hicho na kwa kupitia chama hicho nchi yetu, ni viongozi wasio na maoni, waliolala hadharani, wenye kutetea maslahi ya matumbo yao na ya wanawe, wakihangaika kutwa kucha kufikiri ni jinsi gani watamegeana fedha za walipa kodi. Kwa kutumia vipaji vyao na elimu yao baadhi ya viongozi wa vyama hivyo wamebuni miradi hewa ya kugereshea umma huku fedha nyingi za miradi hiyo zikiishia vibindoni mwao. Watanzania hatimaye watatambua kuwa wakati wa kuangalia onesho la mazingaombwe umepita, na watataka kitu halisi! CCM haiwezi kubadilika, imelewa ugimbi wa madaraka na kuvimbiwa na mlo wa uchu! Ndiyo! Watanzania watagundua ya kuwa kuwa na CCM au kutokuwa nayo yote ni sawa! Hawana cha kupoteza tena. Kama miaka yote hiyo CCM imeshindwa kuboresha elimu yetu, sekta ya afya na maji, matatizo ya nishati n.k itakuwaje waweze kufanya hivyo miaka arobaini ijayo wakati kizazi kinachoingia madarakani sasa ni cha wana na wajukuu wa viongozi wa chama hicho!? Watanzania watasema "CCM Asante, lakini Kwaheri"!

Watakishukuru chama hicho kwa kutujengea misingi ya udugu, umoja na mshikamano. Watakishukuru chama hicho kwa kutulindia utaifa wetu na kuhakikisha kuwa tunabakia kuwa huru kisiasa. Watakishukuru Chama hicho kwa kutujengea utambulisho wetu wa "watanzania" na kutufutia hisia ya ukabila na udini. Ndiyo, watakishukuru chama hicho kwa yale machache mazuri ambayo kimefanya kwa muda mrefu, barabara chache za lami, shule, mahospitali, n.k Ndiyo, Watanzania watasema "asante"!!

Lakini wana hao na mabinti hao wa Kitanzania pia watasema "Kwaheri"! Watakiambia chama hicho kwaheri kwa kushindwa kujenga misingi mizuri ya utawala wa kidemokrasia! Watakiaga chama hicho kwa mamia baada ya kugundua kuwa hakina lengo la dhati la kuwashughulikia wala rushwa wakubwa na viongozi wabadhirifu! Watakiaga chama hicho baada ya kuona kuwa Mikakati yake mingi yenye majina ya ajabu ni sehemu ya mazingaombwe hayo! Wataangalia maisha ya viongozi hao na watoto wao na kuona kuwa wenzao wananeemeka wakati wao wanaganga njaa! Ndiyo! Watakiaga chama hicho kwa sababu, hatimaye watagundua ya kuwa njia pekee ya kukifundisha somo la utawala ni kuwaweka nje ya madaraka na kuwanyima nafasi nyingine ya kura na kula! Ndiyo, CCM itaanguka! Watatambua ya kuwa CCM ni chama cha kisiasa na siyo mama yao mzazi! Watakiaga na kushukuru kwa onesho lao la mazingaombwe, lakini wakati umefika wa kuingia kazini!

Ni matumaini yangu kuwa maandamano ya wapinzani yanayofanyika jijini Dar hayatakuwa ni ishara tu ya kuchukizwa na matendo ya serikali ya CCM na ufisadi uliokithiri. Ni matumaini yangu kuwa viongozi wa vyama vya upinzani watadhamiria kushirikiana siyo katika kupiga kelele kwa kutumia vipaza sauti hapo Jangwani bali ushirikiano wa kweli utakaofanya waziunganishe nguvu zao na kuunda chama kipya cha siasa chenye itikadi inayoakisi matamanio na matarajio ya Watanzania wengi, na chenye viongozi ambao kwao utumishi wa Taifa lao ndio kitu kinachowasukuma!

Endapo wapinzani wataishia kuwa waandamanaji, na wapiga kelele lakini wakishindwa kuungana na kutuonesha kuwa wako makini na mafanikio ya nchi yetu, basi CCM itaendelea kupeta kila kukija uchaguzi! Wapinzani wasililie huruma ya CCM ili wabadilishe Katiba au kuwajengea mazingira mazuri ya kushindana nao! Wapinzani wachukua hatima yao mikononi mwao wao wenyewe! Wawaambie Watanzania kuwa lengo lao mwaka 2010 ni kulichukua Bunge la Tanzania kwani limeendelea kuwa kicheko na dhihaka katika utawala wetu wa Demokrasia! Bunge lenye kutoa azimio la kulaani filamu ya mapanki kabla hawajaiona, na likakaa kimya kwenye mikataba ya madini na nishati bila kutoa azimio la kulaani mikataba hiyo, wabunge wa bunge hilo waondolewe kwa kura! Bunge ambalo linatumia siku 60 kuzungumzia maneno ya watu wawili na kushindwa kutumia siku moja kuzungumzia suala la rada, Richmond, IPTL, ATC n.k hilo ni bunge uchwara!! Bunge lenye spika anayeangalia matumizi ya maneno "kukaza" na "kutia" badala ya kuangalia matumizi ya shilingi Bilioni 80 ya vitu tusivyovihitaji Bunge hilo ni karibu ya Bunge la serikali ya nchi ya Wagagagigikoko! Kama kweli wanataka kuwapa Watanzania matumaini viongozi wote wa upinzani ifikapo 2010 wagombee Ubunge wakiwa wamuengana na kuhamasisha Watanzania wawachague wanachama wao! Kama Watanzania watataka Kikwete apewe nafasi nyingine hilo lao, lakini Bunge lisiende CCM!

Wapinzani wakiweza kunyakuwa wingi katika Bunge la Muungano, basi mwanzo wa CCM kuporomoka utakuwa umefika! Wakiweza kuwashawishi Watanzania baada ya wao kuungana kuwa wanamaanisha wanachosema basi CCM itaanza kutikisika! Watakapochaguliwa Wabunge na wakaanza kusimamia na kupitisha sheria ambazo zina manufaa kwa wananchi watamlazimisha Rais azikubali au atumie uwezo wake wa turufu. Na akifanya hivyo kwenye miswada fulani mara kadhaa avunje Bunge na uchaguzi mpya utafanyika! Huo utakuwa ni mwisho wa Kikwete, huo utakuwa ni mwisho wa CCM!

Je wapinzani wako tayari kusimama na kuchukua nafasi yao ambayo historia imewatengenezea? Je wako tayari kuitwa majina na kujipanga mstari kuongoza Taifa letu? Je, ndani ya vyama hivyo wapo kweli viongozi ambao Tanzania inaweza kuwaangalia na kuwategemea kuwavusha kutoka katika jangwa la utawala wa CCM.

Kuna maneno ya Maandiko Matakatifu yanayosema "Mlivyouzunguka mlima huu vyatosha, geukeni upande wa kaskazini." (Kumb. 2:3). Ndugu zangu Watanzania, tulivyouzunguka mlima wa CCM sasa imetosha! Tulivyouimbia kwa kuuzoea na kuusifia utawala mbovu wa chama hicho sasa inatosha! Tulivyozoea mazingaombwe na mikataba iliyodumaza uchumi wetu sasa inatosha! Ndiyo CCM inaweza kuwa na watu wachache waadilifu, wamwogopao Mungu, na waipendao nchi yao! Ndiyo inawezekana kuna wale wanaojaribu kuibadilisha toka ndani ili ikidhi mahitaji ya Taifa letu, hata hivyo kuombea watu hawa wapo, inatosha! CCM imefanya mambo mengi mazuri kwa Taifa lakini yakipimwa na yale mabaya kwenye mizani ya Mama Haki, mambo mabaya yanazidi kwa uzito na wingi wake yale mazuri! Kuombea kuwa miaka mitano ijayo mambo yatabadilika inatosha! Tugeuke upande tofauti! Labda tutafika iliko NCHI YA AHADI!

Kwani kuanguka kwa chama hicho kupo, kunakuja, na kunafanya hima kutufikia. CCM siyo mama yetu! Unabii huo utatimia!!!

( nitasahihisha kesho)
Hii ni ndoto ambayo itakuja kuotwa na vitukuu vyako, ambapo karne ya 50 huko.
CCM MBELE DAIMA
NYUMA MWIKO
 
Maneno yako Mzee Mwanakijiji ni mazito; nimetafuta jina la kukubatiza sijalipata.

Naamini mambo manne ni muhimu ili huu utabiri wako utimie.

Kwanza, watu wapigike sana kimaisha na waweze kuhusisha kikamilifu madhira wanayoyapata na utawala wa CCM. Pili, wananchi walio wengi watakapogundua kuwa CCM ni gari lililokwisha kufa na halikarabatiki hata aje dereva awaye yule, awe Mwinyi, Mkapa, Kikwete, na yeyote yule hii gari haiendi. Tatu, wananchi walio wengi waamini kwamba wana uwezo wa kuitoa CCM madarakani kwa kutumia kura zao. Nne, wananchi wakiangalia pembeni waone chama na viongozi mbadala cha kuwapa hizo kura zao. Yaani, waione gari mpya na dereva aliye mwerevu wa kuiendesha.

Mimi nafikiri wananchi walio wengi tayari wameshapigika sana na maisha na kwamba matumaini waliyopewa na Kikwete yameshayeyuka. Ila sidhani kwamba wananchi walio wengi wameweza kuoanisha sawasawa katika kupigika huko kimaisha na utawala wa CCM. Naamini pia kuwa wananchi walio wengi pia bado wanafikiri kwamba tatizo la CCM ni dereva na sio gari. Yaani, wanafikiri ukibadilisha dereva hamna neno. Hadi pale watakapoelewa kuwa CCM ni gari lililokwisha kufa, halikarabatiki hata aje fundi na dereva wa namna gani hawezi! Naamini kuwa wananchi sasa wanaamini kwamba wanaweza kubadilisha uongozi kwa kura zao. Vinginevyo, upinzani usingepata hao wabunmge wachache waliowapata.

Kuhusu vyama na viongozi mbadala (gari jipya na dereva mwerevu)-Japokuwa mwanga umeanza kupenyeza, nafikiri hapa ndio bado kuna kazi kidogo. Tatizo moja kubwa sana lililopo ni kukosekean kwa umoja wa vyama vya siasa. Watanzania wanapenda sana umoja. Kwa hivyo kwa hili la kuwa kila chama kinajiona bora kuliko chama kingine na kijiendeshea mambo yake chenyewe, ni kikwazo kikubwa kwa vyama vya upinzani kupenyeza katika nyoyo za watanzania. Ndio maana makala yako Mzee Mwanakijiji imenikuna hasa ulipogusia muungano wa vyama vya siasa. Nakwambie siku vyama vya upinzani vikiungana, utakuwa ndio mwanzo wa mwisho wa CCM. Lakini nisisitize hapa kuwa sio muungano, bali muungano miongoni mwa vyama vilivyo makini kwani tunajua kuna vyama vingine ni matawi ya haohao CCM.

Mimi ninashawishika sasa kuliko kipindi kingine chochote juu ya nguvu ya ushawishi tulio nayo katika forum hii. Kwa hivyo, nawaombeni ndugu zangu tuanze rasmi kuwapa shinikizo viongozi wa vyama vya siasa wa upinzani waanze mazungumzo ya kuunganisha vyama vyao. Kwa kuanzia ningeomba tuanze na vyama hivi: CHADEMA, CUF, NCCR, TLP na UDP. Ninaamini vyama hivi vikiungana, itakuwa ni nguvu kubwa na itakuwa ndio mwisho wa shutuma za udini na ukabila zinazotusumbua CHADEMA na CUF.

Tunaweza kuanza kwa kuandika barua ambayo wale tunao amini katika muungano tutaisaini. Barua hiyo iwe ni barua rasmi kutoka kwa watanzania wanaoishi nje na iende kwa viongozi wakuu wote wa vyama vya siasa vya upinzani.

Naomba kuwasilisha
That was then, now ?
P
Cc. Kitila Mkumbo
 
Maneno yako Mzee Mwanakijiji ni mazito; nimetafuta jina la kukubatiza sijalipata.

Naamini mambo manne ni muhimu ili huu utabiri wako utimie.

Kwanza, watu wapigike sana kimaisha na waweze kuhusisha kikamilifu madhira wanayoyapata na utawala wa CCM. Pili, wananchi walio wengi watakapogundua kuwa CCM ni gari lililokwisha kufa na halikarabatiki hata aje dereva awaye yule, awe Mwinyi, Mkapa, Kikwete, na yeyote yule hii gari haiendi. Tatu, wananchi walio wengi waamini kwamba wana uwezo wa kuitoa CCM madarakani kwa kutumia kura zao. Nne, wananchi wakiangalia pembeni waone chama na viongozi mbadala cha kuwapa hizo kura zao. Yaani, waione gari mpya na dereva aliye mwerevu wa kuiendesha.

Mimi nafikiri wananchi walio wengi tayari wameshapigika sana na maisha na kwamba matumaini waliyopewa na Kikwete yameshayeyuka. Ila sidhani kwamba wananchi walio wengi wameweza kuoanisha sawasawa katika kupigika huko kimaisha na utawala wa CCM. Naamini pia kuwa wananchi walio wengi pia bado wanafikiri kwamba tatizo la CCM ni dereva na sio gari. Yaani, wanafikiri ukibadilisha dereva hamna neno. Hadi pale watakapoelewa kuwa CCM ni gari lililokwisha kufa, halikarabatiki hata aje fundi na dereva wa namna gani hawezi! Naamini kuwa wananchi sasa wanaamini kwamba wanaweza kubadilisha uongozi kwa kura zao. Vinginevyo, upinzani usingepata hao wabunmge wachache waliowapata.

Kuhusu vyama na viongozi mbadala (gari jipya na dereva mwerevu)-Japokuwa mwanga umeanza kupenyeza, nafikiri hapa ndio bado kuna kazi kidogo. Tatizo moja kubwa sana lililopo ni kukosekean kwa umoja wa vyama vya siasa. Watanzania wanapenda sana umoja. Kwa hivyo kwa hili la kuwa kila chama kinajiona bora kuliko chama kingine na kijiendeshea mambo yake chenyewe, ni kikwazo kikubwa kwa vyama vya upinzani kupenyeza katika nyoyo za watanzania. Ndio maana makala yako Mzee Mwanakijiji imenikuna hasa ulipogusia muungano wa vyama vya siasa. Nakwambie siku vyama vya upinzani vikiungana, utakuwa ndio mwanzo wa mwisho wa CCM. Lakini nisisitize hapa kuwa sio muungano, bali muungano miongoni mwa vyama vilivyo makini kwani tunajua kuna vyama vingine ni matawi ya haohao CCM.

Mimi ninashawishika sasa kuliko kipindi kingine chochote juu ya nguvu ya ushawishi tulio nayo katika forum hii. Kwa hivyo, nawaombeni ndugu zangu tuanze rasmi kuwapa shinikizo viongozi wa vyama vya siasa wa upinzani waanze mazungumzo ya kuunganisha vyama vyao. Kwa kuanzia ningeomba tuanze na vyama hivi: CHADEMA, CUF, NCCR, TLP na UDP. Ninaamini vyama hivi vikiungana, itakuwa ni nguvu kubwa na itakuwa ndio mwisho wa shutuma za udini na ukabila zinazotusumbua CHADEMA na CUF.

Tunaweza kuanza kwa kuandika barua ambayo wale tunao amini katika muungano tutaisaini. Barua hiyo iwe ni barua rasmi kutoka kwa watanzania wanaoishi nje na iende kwa viongozi wakuu wote wa vyama vya siasa vya upinzani.

Naomba kuwasilisha
Kumbukumbu
 
Back
Top Bottom