Kagoda ni hatari
• Mtikisiko utazidi wa Lowassa, Karamagi, Msabaha
na Salehe Mohamed
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
KITENDAWILI cha kufikishwa mahakamani ama kutajwa majina ya watuhumiwa wa wizi wa fedha katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) kupitia Kampuni ya Kagoda kimeendelea kuwa kigumu baada ya kuelezwa kuwa kunaweza kusababisha kuyumba kwa utawala wa nchi, siasa na uchumi.
Habari za kuaminika ambazo Tanzania Daima Jumapili, imezipata zinadai kuwa umiliki wa kampuni hiyo hadi hivi sasa imegubikwa na utata kutokana na serikali pamoja na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kushindwa kuweka bayana majina ya wamiliki, licha ya kuwapo kwa kelele za wananchi wakitaka watuhumiwa watajwe na kufikishwa mahakamani.
Habari hizo zinaeleza kuwa ni vigumu zaidi kwa vigogo hao wa Kagoda kupandishwa kizimbani, kwani hiyo itakuwa ni hatari na mtikisiko mkubwa zaidi kutokea hapa nchini kuliko hata ule uliotokea katika sakata la Richmond ambalo lilisababisha aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri wawili kuachia ngazi kwa kuhusishwa na kashfa hiyo.
Mtikisiko huo ulimfanya Rais Jakaya Kikwete, kuvunja baraza la mawaziri na kuunda jingine huku akiwaacha mawaziri kadhaa ambao wanadaiwa kuhusika kwa namna moja au nyingine katika vitendo vya kifisadi, ikiwemo kutoa baraka juu ya uchotaji wa fedha hizo.
"Kuna mkakati wa hali ya juu kuhakikisha vigogo wa Kagoda hawafikishwi mahakamani na siku wakipandishwa, basi kuna kila dalili nchi kutikisika na watu wenye heshima zao kuumbuka," kilisema chanzo hicho cha habari.
Miongoni mwa waasisi wa wizi wa EPA, kupitia Kampuni ya Kagoda ni mwanasiasa mkongwe aliyewahi kupata nyadhifa mbalimbali katika vipindi vyote vya utawala wa nchi hii tangu ipate uhuru wake.
Mwanasiasa huyo ambaye alitarajiwa kuwa mfano wa kuigwa kutokana na kuishi na kufanya kazi muda mrefu na hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, hivi sasa ameonekana ndiye kinara wa kuvunja maadili.
Kampuni ya Kagoda inadaiwa kujichotea sh bilioni 40 katika kipindi cha mwezi mmoja tangu iliposajiliwa mwaka 2005 na inadaiwa kuwa uanzishwaji wake ulitokana na mawazo ya vigogo kadhaa wa kisiasa waliopo madarakani na wengine wamemaliza muda wao.
Uchotaji fedha huo mara ya kwanza ulihusishwa na matumizi ya usalama baada ya aliyekuwa Waziri wa Fedha, Zakhia Meghji, kuthibitisha taarifa hizo wakati akitoa ufafanuzi kwa wanasiasa machachari waliokuwa wakizihusisha fedha hizo na vitendo vya kifisadi.
Kitendo cha Meghji kushindwa kujieleza vizuri ndani ya Bunge, kilionyeshwa wazi kwamba kuna kasoro, hali iliyosababisha baadhi ya wabunge kuomba itafutwe kampuni ya kufanya ukaguzi wa hesabu dhidi ya tukio hilo (BoT).
Meghji, hakuweza kuendelea kuibeba kauli yake hiyo kwani baadaye alinukuliwa kuwa alipewa taarifa zisizo na ukweli na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) marehemu Daud Ballali.
Kuhusika kwa vigogo wa siasa katika wizi huo ndiko kunakowafanya wahahe usiku na mchana ili kuhakikisha hakuna nyaraka zinazowahusisha moja kwa moja na umiliki wa kampuni hiyo, sambamba na kufanya kila wawezalo kuhakikisha hawapandi kizimbani.
Mazingira ya uchotaji wa fedha hizo yalifanyika wakati taifa likiwa katika mchakato wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, ndiyo maana baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakikituhumu chama kimoja kikubwa cha siasa kuhusika katika kashfa hiyo, licha ya viongozi wake kukataa kuhusika na wizi huo.
Kagoda, iliweza kujichotea kiasi kikubwa hicho cha fedha katika muda wa mwezi mmoja tangu imesajiliwa, jambo ambalo limezua maswali mengi yasiyo na majibu miongoni mwa Watanzania na kuhoji imekuwaje kampuni ngeni kuaminiwa na kupatiwa kiasi kikubwa cha fedha bila kufanyiwa uhakiki wa kina na watendaji wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambao ndio waliokuwa na dhamana ya kutoa fedha hizo.
Pamoja na kampuni hiyo kuchota kiasi kikubwa cha fedha lakini hadi hivi sasa wamiliki wake hawajulikani na hawajafikishwa mahakamani, licha ya wamiliki wa kampuni nyingine zilizoiba fedha za EPA kufikishwa mahakamani, hali inayoibua maswali mengi kwa jamii.
Mmoja wa kigogo ambaye kampuni yake ilihusishwa na wizi wa EPA, hivi karibuni aliumwa ghafla na kuchanganyikiwa, baada ya kupewa taarifa kuwa yeye ni mmoja wa watu watakaoburuzwa mahakamani, licha ya kulipa fedha alizoiba.
Kigogo huyo ambaye anasifika kwa kufadhili mambo mbalimbali ya kijamii, alichanganyikiwa zaidi pale alipotaka kwenda kutibiwa nchi jirani na kukataliwa kusafiri na watu wa usalama, kwa kile kilichodaiwa ni maandalizi ya kumburuza mahakamani.
Kukataliwa huko kulimfanya awajie juu baadhi ya watendaji na kuwatishia kuanika namna wizi ulivyofanyika na watu waliohusika, bila kuangalia vyeo vyao na nafasi waliyonayo katika jamii, iwapo serikali itadhamiria kumpandisha kizimbani.
Tishio hilo lilimsaidia, kwani aliruhusiwa kwenda nchi jirani kupatiwa matibabu huku akilenga kutorejea hapa nchini kwa hofu ya kuburuzwa kortini, alirejea hapa nchini baada ya kuhakikishiwa kuwa si mmoja wa watu watakaopandishwa mahakamani kama alivyosikia awali.
Kigogo huyo inadaiwa hakuhusika katika wizi huo wa EPA, lakini alijikuta akihusishwa baada ya kununua kampuni iliyoshiriki kuchota fedha za EPA kutoka kwa rafiki yake wa karibu na mwanasiasa ambaye aliogopa kuendesha kampuni hiyo kwa kisingizio cha kuonekana ana mali nyingi ndani na nje ya chama.
Alipokuja kutambua kauziwa kampuni iliyoshiriki wizi wa EPA, alimfuata rafiki yake ambaye hakumpa ushirikiano unaotakiwa, jambo lililosababisha wawili hao kutokuelewana mpaka hivi sasa.
"Wafanyabiashara hawa uhusiano wao mpaka hivi sasa si mzuri, yule aliuza kampuni haonekani kujali tatizo linalomkabili rafiki yake aliyemuuzia kampuni," kilisema chanzo chetu cha habari.
Kagoda imeendelea kuwa gumzo hapa nchini, kiasi cha kumfanya Mwenyekiti wa Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI), Reginald Mengi, kutamka waziwazi kwamba mafisadi wote waliohusika lazima wafikishwe mahakamani bila kujali walikuwa wana miliki kampuni gani, wana nyadhifa gani serikalini au kwenye chama tawala.
Mengi, mmoja wa wafanyabiashara wanaoheshimika nchini, alisema litakuwa jambo la ajabu kama wamiliki wa kampuni ya Kagoda hawatatajwa majina ili wajulikane na kufikishwa mbele ya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili.
Wakati Mengi, akitoa kauli hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Dk. Edward Hoseh, kwa nyakati tofauti amenukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwakamata mafisadi hao mara moja kunaweza kuyumbisha uchumi wa taifa.
Hatua ya kiongozi huyo aliyepewa jukumu zito la kuhakikisha anaokoa haki za Watanzania, inaonyesha wazi kwamba uchumi wa taifa hili unashikiliwa na watu fulani ambao hawapaswi kuguswa.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba, katika mkutano wake na waandishi wa habari mwannzoni mwa wiki iliyopita alisisitiza kuwa fedha za EPA zinahusika na uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 uliokipa ushindi Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Alisema inawezekana fedha zote hazikwenda katika uchaguzi kutokana na waliopewa jukumu la kuiba fedha hizo kuzitumia kwa mambo yao, lakini ukweli unabaki pale pale kuwa wizi huo uliratibiwa na viongozi wa CCM.
"Inawezekana CCM hawakupelekewa fedha zote lakini ukweli unabaki pale pale kuwa mazingira yanaonyesha wazi ziliibwa kipindi cha uchaguzi na zilitumika kuwapa ushindi CCM," alisema Lipumba.
Wakati Lipumba akisema hayo, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), amesema atahakikisha watuhumiwa wa Kagoda wanafikishwa mahakamani hata kama wataendelea kulindwa na serikali.
Alisema wamiliki wa Kagoda wanapaswa wafikishwe kortini, kwani wamechota kiasi kikubwa cha fedha ukilinganisha na kampuni nyingine.
Sakata la EPA linatokana na makampuni 22 kukwapua sh bilioni 133, kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), jambo lililomfanya Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa aliyekuwa Gavana wa BoT, Daud Ballali na kuunda tume iliyoongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Johnson Mwanyika, kuchunguza wizi huo baada ya ripoti ya Kampuni ya Ernst & Young kuthibitisha kuwapo kwa wizi.
Timu hiyo ilifanya kazi yake na kukabidhi ripoti kwa rais, ambaye alitoa muda kwa baadhi ya kampuni kurejesha kiasi hicho kabla ya Novemba mosi na kuahidi kuwa kampuni itakayoshindwa kufanya hivyo itaburuzwa kortini.
Rais Kikwete, aliitekeleza ahadi hiyo kwa kumkabidhi Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Elieza Feleshi, majalada ya kampuni zilizokwapua fedha za EPA.
DPP hadi sasa ameshawafikisha katika Mahakama ya Kisutu, watuhumiwa 20 wa wizi huo huku 18 kati ya hao wakipata dhamana ambazo zilikuwa na masharti magumu.
Washitakiwa waliofanikiwa kutoka kwa dhamana ni pamoja na Jeetu Patel, Amit Nandy, Ketan Chohan, Vinodbhai Patel, Bahati Mahenge, Davies Mwakale, Eddah Mwakale, Japhet Lema, Ajay Somani, Jay Somani na Johnson Lukaza.
Wengine ni Mwengesi Lukaza, Godfrey Mosha, Davis Kamungu, Ester Komu na kada maarufu na mweka hazina wa CCM, Shaaban Maranda.