Slaa aapa kufa na Kagoda
2008-11-22 10:52:04
Na Waandishi Wetu
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, amesema atatoboa siri ya majina ya wamiliki wa kampuni ya Kagoda Agriculture Limited, katika ziara ya operesheni Sangara inayotarajiwa kuendelea hivi karibuni kama wahusika wakuu hawatafikishwa mahakamani.
Kagoda ni miongoni mwa kampuni zilizotajwa kuhusika katika ufisadi wa fedha za Akaunti ya Malipo ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambapo msemaji wa Wizara ya Katiba na Mambo ya Sheria, Omega Ngolle, alisema kamwe Mkurugenzi wa Mashitaka ya Jinai (DPP), Elieza Feleshi, hawezi kutaja majina ya wamiliki hao, licha ya kukagua mafaili ya watuhumiwa wa EPA.
Badala yake, Ngolle alisema jukumu la kutaja majina hayo linaweza kufanywa na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela).
Hata hivyo, taarifa kutoka Brela ambazo zilichapishwa kwenye gazeti hili jana, zilieleza kuwa timu iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza wizi wa EPA ndani ya BoT chini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika, ndiyo inayojua majina ya wamiliki wa kampuni hiyo.
Umiliki wa kampuni hiyo inayodaiwa kuchota asilimia 45 ya Sh. bilioni 90 zilizoibwa na kampuni 13 kati ya 22 ambayo yaliiba jumla ya Sh bilioni 133 ndani ya EPA, umezidi kuzua utata na maswali mengi kwa jamii.
Brela ilisema Kamati ya Mwanyika ndiyo inashikilia jalada hilo kwa sasa na yale ya makampuni mengine 21 yanayotuhumiwa kuchota fedha za EPA.
Akizungumza na Nipashe kwa njia ya simu jana, Dk. Slaa ambaye pia ni Mbunge wa Karatu (Chadema), alidai kuwa inashangaza kuona mamlaka zinazohusika, 'zinatupiana mpira' kuhusu umiliki wa Kagoda na suala zima la EPA, licha ya ukweli wake kujulikana wazi.
Kwa mujibu wa Dk Slaa anayeaminika kuwa ndiye mtu wa kwanza kuibua sakata la ufisadi wa EPA na BoT kwa ujumla, wamiliki wa kampuni hiyo wanaojulikana, aliwataja kwa majina (tunayahifadhi).
Hawa wamiliki wa Kagoda wanajulikana, lakini hata kama wanatoa visingizio, basi wangewakamata watu wawili na kuwafikisha mahakamani, huko ndipo siri za wamiliki wengine zingejulikana,`` alisema.
Dk. Slaa alisema sakata la ufisadi uliofanywa na Kagoda haliwezi \'kufumbiwa macho` kwa kuwa linahusu na kuathiri maisha ya wananchi.
Alidai kuwa miongoni mwa matukio yanayotia shaka ni kampuni hiyo kufanikiwa kuchota kiasi cha Sh bilioni 40, ikiwa ni ndani ya wiki nane tu tangu ipate usajili.
Alidai kuwa tukio hilo lilifanyika mwaka 2005, ikiwa ni muda mfupi kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani, hali inayozua hoja ya kutaka kujua mahali zilipoelekezwa fedha hizo.
Nacho Chama cha Wananchi (CUF), kimemtaka Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) kuacha ``kigugumizi`` juu ya Kagoda na badala yake awafikishe mahakamani watuhumiwa wa Kampuni ya Kagoda kwa kuwa wamiliki wake wanafahamika.
Akizungumza na Nipashe jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema kampuni hiyo ndiyo ya kwanza kugundulika kuchota fedha za EPA.
Alisema inashangaza kuona kuwa licha ya kampuni hiyo kuwa ya kwanza kugundulika kuiba fedha hizo mpaka sasa wahusika hawajafikishwa mahakamani.
Alisema wakaguzi wa ndani wa BoT walibainisha kuwa Kagoda ilichota zaidi ya Sh. bilioni 40.
Lazima hawa watu wajulikane na washtakiwe, hata kama wamerejesha fedha, lazima washtakiwe maana walighushi nyaraka na kama mtu amerejesha fedha zitumike kama kidhibiti kuwa kweli aliiba,� alisema Lipumba.
Alimshauri DPP kuwafikisha mahakamani haraka ili kujibu maswali ya wananchi ambayo wamekuwa wakijiuliza kuhusu nani hasa wamiliki wa kampuni hiyo.
Inawezekana kuna watu waliwekwa mbele tu, lakini waliokula fedha wengine, lakini hao vigogo ni rahisi kupatikana watafutwe wakasimame mahakamani kama wenzao,`` alisema.
Naye Mwenyekiti wa chama cha PPT Maendeleo, Peter Mziray, alisema watu wanashauku ya kuwaona vigogo wa Kagoda kwa kuwa ndiyo ya kwanza kushutumiwa katika wizi huo.
Alisema kama kuna watu walibambikizwa, lakini fedha zikaliwa na watu wengine ni vyema DPP akawasaka watu hao na kuwaunganisha na washtakiwa wengine.
Kagoda sio mzimu ni watu na lazima wajulikane hata kama kule Brela hawapo, ile akaunti iliyotumika lazima kuna picha ya waliokuwa wakiitumia,� alisema.
Katika hatua nyingine, mshtakiwa Rajabu Maranda, anayekabiliwa na kesi ya wizi wa fedha za EPA ameachiwa kwa dhamana baada ya kutoa hati ya mali yenye thamani ya Sh. milioni 450.
Maranda alidhaminiwa mbele ya Hakimu Mkazi, Hadija Msongo, wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana.
Mshitakiwa huyo anakuwa wa 18 kuwa nje kwa dhamana kati ya 20 ambao walifikishwa mahakamani hapo kwa siku tofauti kuanzia Novemba 5, mwaka huu.
Mshitakiwa huyo alipata dhamana baada ya kukaa gerezani kwa muda wa wiki mbili akikabiliwa na kesi nne tofauti za kuibia BoT.
Hata hivyo, kabla ya mshitakiwa kuachiwa kwa dhamana, mahakama hiyo iliahirisha kusoma maelezo ya awali baada ya upande wa utetezi kuomba muda wa kupitia maelezo hayo ambayo yalichelewa kuwafikia.
Mahakama ilikubaliana na ombi hilo na ikapanga Desemba 5 mwaka huu kuwa ndiyo siku ya itasikilizwa maelezo ya awali.
Aidha, mshitakiwa mwenzake katika kesi hiyo Farijala Hussein alishindwa kutimiza masharti ya dhamana na hivyo alirudishwa gerezani hadi atakapotimiza masharti.
Katika kesi hiyo, Maranda na Farijala wanadaiwa kuiba Sh. 1,864,949,294.05 baada ya kudanganya kuwa kampuni ya Kiloloma Brothers ya Tanzania imehamishiwa deni na Kampuni ya B.C Cars Export Ltd ya Mumbai.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Desemba 5, mwaka huu watakaposomewa maelezo ya awali.
Maranda ambaye ni Kada wa CCM Mkoa wa Kigoma akisubiri kusikilizwa kwa maelezo ya awali ya kesi yake katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana, aliyashambulia magazeti ya kampuni ya The Guardian Ltd kuwa yanamwandama .
Magazeti hayo yamekuwa yakifuatilia kwa karibu suala la EPA tangu liibuliwe mwaka jana hadi kesi zilipofunguliwa mahakamani.
Wakati huo huo, kesi ya wizi inayowakabiliwa Jayantkumar maarufu kama Jeetu Patel, Amit Nandy na Ketan Chohan iliahirishwa jana mbele ya Hakimu Mkazi, Richard Kabate wa mahakama hiyo.
Katika kesi hiyo, washitakiwa wanadaiwa kughushi na kujipatia Sh. 3,323,974,942.30, baada ya kudanganya kuwa Navy Cut Tobacco (T) Ltd imehamishiwa deni na kampuni ya Matsushita Electric Trading ya Japan.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Januari 18, mwakani itakapotajwa tena.
Imeandaliwa na Mashaka Mgeta, Joseph Mwendapole na Hellen Mwango.
SOURCE: Nipashe