BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,769
- 288,283
Wakaguzi kuimaliza Kagoda mahakamani
Mwandishi Wetu Aprili 22, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
- Ni wale waliosema ni wizi mtupu
- DPP asema yote yana mwisho
Akizungumza na Raia Mwema katika mahojiano maalumu, jana Jumanne, Feleshi alisema, hakuna marefu yasiyo na mwisho, na kwamba suala hilo litapatiwa ufumbuzi utakaozingatia matakwa ya kisheria ikiwa ni pamoja na sheria ya ushahidi.
Feleshi alikwepa kuzungumzia ni lini wahusika watafikishwa mahakamani, akiegemea zaidi kwenye maadili ya taaluma yake, lakini alisisitiza kwamba wapelelezi wanakamilisha kujibu maswali yote muhimu kuhusiana na kesi hiyo.
Kila kesi inaamuliwa kwa vigezo vyake na viwango vyake vya maelezo na ushahidi unaojitegemea. Tunasubiri wakamilishe upelelezi na sisi tufanye kazi yetu. Mimi ni mwendesha mashitaka. Lazima tujiridhishe kabla ya kufanya maamuzi, alisema.
Alipoulizwa kuhusu maelezo ya wazi kutoka kwa wakaguzi na mashahidi yanayoonyesha kuwapo kwa jinai kutokana na nyaraka nyingi kughushiwa, Feleshi alisema ni lazima sheria ya ushahidi itumike ili nyaraka na maelezo ya wakaguzi na ripoti zao ziweze kutumika kama ushahidi mahakamani.
Ni lazima tufuate taratibu za sheria ya ushahidi. Ripoti za wakaguzi haziwezi kutumika hadi taratibu zifuatwe na hapo ndipo zitaweza kuwasilishwa mahakamani kama ushahidi, alisema Feleshi, huku akikwepa kuingia undani wa hatua waliyofikia.
Akizungumzia kuhusiana na ushahidi wa kimataifa, Feleshi alisema mambo yote hufanyika kwa kuzingatia sheria na mikataba ya kimataifa inayohusiana na masuala ya ushirikiano katika upelelezi na uendeshaji mashitaka.
Kila nchi ina mamlaka inayosimamia usajili wa kampuni na hivyo kampuni zilizotajwa kuhusiana na EPA ni lazima zitolewe maelezo kutoka mamlaka husika. Wao ndio waseme kwa maandishi kwamba kampuni X haipo, kampuni Y imefilisika, kampuni Z ni ya fulani, alisema DPP.
Kumekuwa na hoja kutoka kwa wanasiasa, vyombo vya habari na hata wananchi wa kawaida pamoja na watu waliokwisha kushitakiwa kuhusiana na kutofikishwa mahakamani kwa wahusika wa kampuni ya Kagoda, ambayo pekee inatajwa kuchukua sehemu kubwa ya fedha zilizoibwa katika akaunti ya EPA.
Kampuni ya Kagoda ambayo hadi sasa wamiliki na uhalali wake ni mambo yenye utata mkubwa, inatajwa kutumia nyaraka za kughushi katika kupata kiasi cha Dola za Marekani 30,732,658.82 (takriban Sh bilioni 40) kutoka BoT kwa kutumia mbinu chafu.
Mbinu hizo ni pamoja na kughushi nyaraka mbalimbali na kutumia kivuli cha siasa katika kupitisha nyaraka husika bila kufanyika kwa uhakiki wa kina wa uhalali wa nyaraka hizo, kazi iliyofanyika kwa kasi iliyowashangaza hata wakaguzi wazalendo na wale wa kimataifa waliopitia hesabu za BoT.
Mfano wa dhahiri uliotolewa tokea mwanzo ni ule wa wahusika wa Kagoda kughushi nyaraka za kampuni 12 za kigeni kuweza kujichotea kiasi cha Sh Bilioni 40,ikiwa ni pamoja na nyaraka zilizopitishwa na maofisa wa BoT bila kufanyiwa uhakiki.
Walioanza kuwasha moto wa wizi huo walikuwa ni wakaguzi wa kimataifa wa kampuni ya Deloitte & Touche, ambao walitimuliwa na serikali baada ya kutoelewana katika ukaguzi wa akaunti hiyo ambayo sasa inazidi kuchanganya wengi.
Deloitte & Touche, ambayo ilipewa kazi ya kukagua akaunti za BoT, ilikumbana na utata mkubwa katika akaunti ya EPA namba 99915091 01, na hivyo kuwa kiashirio cha kwanza cha utata mkubwa katika akaunti hiyo.
Maelezo yaliyoibua utata huo yanaonyesha kwamba aliyekuwa Gavana wa BoT, Marehemu Dk Daudi Ballali, alianza kujulishwa mapema kuhusiana na wizi huo akipewa mfano wa dhahiri jinsi Kagoda Agriculture Limited ilivyoghushi nyaraka.
Mfano uliotolewa kudhihirisha uhalifu huo ni jinsi ambavyo mikataba ya ununuzi wa madeni kwa kampuni 12 ilivyosainiwa katika kipindi kifupi cha kati ya Septemba 10, 2005 na Novemba 5, 2005, kipindi ambacho kilielezwa kuwa ni vigumu kwa wahusika kutembelea nchi mbalimbali duniani kutiliana saini.
Aidha, imefahamika kwamba nyaraka zote zilisainiwa na wakili mmoja tu Bhyidinka Michael Sanze, wa Malegesi Law Chambers ya Dar es Salaam, na kati ya hizo mikataba minne ilisainiwa Oktoba 18, 2005 na mitano ilisainiwa siku moja baadaye Oktoba 19, 2005, jambo ambalo lilitia shaka jinsi wawakilishi wa kampuni hizo za kigeni walivyoweza kusafiri kwa wakati mmoja wakitofautiana kwa saa chache, jambo ambalo lilishindwa kuthibitishwa kwa kutumia kumbukumbu za uhamiaji.
Sanze anatajwa kama shahidi muhimu ambaye maelezo yake kwa wachunguzi wa Tanzania yanawataja wanasiasa na watendaji muhimu wa serikali ambao hata hivyo hawatajwi katika kesi zilizokwisha kufikishwa mahakamani.
Katika nyaraka hizo, mikataba miwili iliyosainiwa Oktoba 18, 2005 kuhusiana na kampuni mbili za Ujerumani, Lindeteves J Export BV na Hoechst ikionyesha kwamba kulikuwa na deni la Euro 1,164,402.76 badala ya fedha za Ujerumani (Deutsche Marks.)
Wachunguzi na wakaguzi wameshitushwa na kasi ya ajabu ya jinsi marekebisho makosa hayo yalivyofanyika kwa kipindi kifupi baada ya BoT kuifahamisha Kagoda Agriculture Limited huku barua ya kutaka marekebisho yafanyike ikiwa na maelekezo ya kuidhinisha malipo ya Sh 8,196,673,600.53 kwenda kwenye akaunti ya Kagoda. Kampuni hiyo iliwasilisha mkataba uliorekebishwa siku mbili tu baada ya kujulishwa.
Pamoja na kubainika kuwa mikataba na nyaraka zote hazikuwa na nembo ya kampuni husika, nyaraka zote zilisainiwa katika ukurasa mmoja pekee wa mwisho tofauti na nyaraka za kisheria zinavyopasa kusainiwa katika kurasa zote.
Uchunguzi wa kina umebaini kufanana kwa mihuri ya kampuni zote zilizopitishwa ikiwa inalandana kabisa na muhuri wa kampuni za Kitanzania, tofauti ikiwa ni majina na anuani ya kampuni husika.
Mfano uliotolewa ni wa kampuni za Kitaliano za Fiat Veicoli Industriali na Adriano Gardella S.P.A pamoja na kampuni ya Kimarekani ya Valmet ambazo zote zimeonekana kuwa na mihuri na lugha zilizofanana katika nyaraka zote.
Utata mwingine uliodhihirika kughushi ni katika mkataba wa kampuni ya Valmet ya Marekani uliohusu Dola za Marekani 2,398,439.96 kusainiwa na Patrick Kevin, aliyetajwa kuwa Mhasibu wa kampuni hiyo, jambo ambalo limeelezwa kwamba ingekuwa vigumu kwa mhasibu kuachiwa kufanya kazi hiyo.
Utata mwingine uliobainika ni katika mkataba wa kampuni ya Daimler Benz AG ambao ulionyesha kusainiwa na Mkurugenzi aliyetajwa kwa jina la Christopher Williams, huku sahihi yake ikisomeka W Christopher.
Uchunguzi wa ziada ulithibitisha kwamba baadhi ya kampuni zilikwishakufa wakati mikataba hiyo ikisainiwa na kampuni za Kitanzania, jambo ambalo linaendelea kuthibitisha wizi mkubwa wa kutumia maandishi uliofanywa katika akaunti ya EPA.
Mifano hai ni kampuni za Hoechst AG iliyobadilika na kuwa Aventis mwaka 1999, Daimler Benz AG iliyobadilika na kuwa Daimler Chrysler AG mwaka 1998 na Fiat Veicoli Industriali iliyobadilishwa na kuwa Industrial Vehicle Corporation (IVECO) tokea Januar1 1, 1975.
Kampuni nyingine zilizobadilika ni Mirrlees Blackstone kuwa MAN B&W Diesel Limited mwaka 2002/03 na Valmet iliyobadilishwa na kuwa Metso Paper kuanzia Mei 10, 2000. Utata huo uliwafanya wachunguzi na wakaguzi kujiuliza ilikuwaje kampuni zote hizo kuingia mikataba mwaka 2005 kwa kutumia majina ya zamani.
Pamoja na kuingiwa kwa mikataba hiyo na kampuni zilizokwisha badilishwa majina na umiliki wake, kampuni za sasa zenye uhusiano na kampuni zilizoingia mkataba zimekanusha kufahamu watu waliotajwa kuziwakilisha katika mikataba hiyo.
Kagoda ambayo imekithiri katika uhalifu wa kughushi ilisajiliwa Septemba 29, 2005, na kujichotea Sh bilioni 40 katika kipindi cha mwezi mmoja tu, jambo ambalo limewashangaza wengi kuona kampuni ngeni isiyofahamika inawezaje kuaminiwa kiasi kikubwa cha fedha bila kuhakikiwa.
Inafahamika kwamba kati ya shilingi bilioni 90 zilizoibwa katika akaunti ya EPA, sehemu kubwa ilichukuliwa na kampuni ya Kagoda Agricultural Limited ambayo hadi sasa wahusika wake hawajaguswa pamoja na kujitokeza kwa vigogo wawili kurejesha fedha zilizoibwa na kampuni hiyo.
Vyanzo vya uhakika vinaeleza kwamba sehemu kubwa ya Shilingi bilioni 90 zilizothibitika kuchukuliwa kihalifu zilichukuliwa na makundi mawili tu, kundi la kwanza likiwa chini ya Jeetu Patel na lingine likiwa chini ya usimamizi wa vigogo wawili waliotumia kampuni ya Kagoda. Jeetu Patel amekwisha kufikishwa mahakamani.
Imefahamika kwamba kwa sasa kuna hekaheka kubwa za kutaka kuzuia kushitakiwa kwa wahusika wa Kagoda, lakini vyanzo vya ndani ya serikali vimeeleza kwamba kwa sasa serikali haitabiriki na lolote linaweza kutokea wakati wowote, na kauli ya Feleshi inaashiria kuendelea kwa kazi ya kuwashughulikia.
Kumekuwa na utata kuhusiana na ilipo na umiliki wa Kagoda Agricultural Limited na hakuna anayeweza kubainisha hasa zilipo ofisi na wahusika wa kampuni hiyo tata.
Kumbukumbu za Wakala wa Usajili Kampuni na Uandikishaji Leseni (BRELA) zinaonyesha kwamba ofisi za Kagoda zipo Kipawa Industrial Area Plot namba 87, Temeke, Dar es Salaam lakini eneo hilo lina makampuni tofauti jirani lakini namba iliyotajwa haionekani na badala yake eneo lenye ofisi na kampuni viwanja vyenye namba kuanzia 76, 77, 86 na 88 katika eneo hilo la viwanda.
Katika ukaguzi wake wa awali wa mkaguzi wa nje Samuel Sithole kutoka kampuni ya Kimataifa ya Deloitte & Touche yenye makao yake Afrika Kusini alionya kuhusu matendo ya kihalifu ndani ya Kagoda kabla ya kuandikiwa barua na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji kwamba fedha hizo zilienda katika mambo "nyeti" ya kiusalama.
Hata hivyo siku nne baada ya kuandika barua hiyo, Meghji alifuta barua hiyo akielezea kupotoshwa na aliyekua Gavana, Dk. Daudi Ballali, uamuzi ambao ulimgharimu kwa kiasi kikubwa mwanamama huyo makini ambaye alijikuta akiachwa nje ya Baraza la Mawaziri, pamoja na kuwa miongoni mwa mawaziri wachache waadilifu.
Wakati Rais Jakaya Kikwete akisema serikali yake haitomuingilia DPP, watuhumiwa wengi waliokamatwa na kufikishwa mahakamani walikuwa wamejiaminisha kuwa wamekwishapona na sasa waliobaki "hawalali" kuhofia kushitukizwa na kupandishwa kizimbani.