Juliana - Erick Shigongo

Juliana - Erick Shigongo

Asante sana shunie. Unanikumbusha shule kulikuwa na kaka mmoja hivi alikuwa bonge la handsome. Na wadada walikuwa wanampapatikia. Sasa hivi nilimuona namuona wa kawaida tu.na kuna mdada mwengine alikuwa Happy Happy. Mwendo Wa twiga mzurii sasa hivi ameokoka sio yule tena hata lipstick hapaki.maisha ni safari na mapito tu
 
SEHEMU YA 11...

“Nimemaanisha Halima! Siwezi kuja peke yangu, ukitaka nije na Juliana,” alisema Gideon kwani alijua ni kitu gani kingetokea huko.
“Hapana Gideon! Ninahitaji uje wewe tu!”
“Haliwezekani!”
“Gideon!”

“Nimesema haiwezekani!”
Gideon hakutaka kubaki mahali hapo, akaondoka zake na kumuacha msichana huyo akimwangalia tu. Halima aliumia moyoni mwake, alitamani kumsimamisha mwanaume huyo lakini halikuwezekana kabisa.
Alimpenda, hakutaka kumuacha hivyohivyo, hakutaka kukata tamaa, aliamini kwamba kama angeendelea kumuomba sana mwanaume huyo mwisho wa siku angemkubalia na hivyo kukutana faragha na kuzungumza.

Halima alijua kusumbua, alijua kupiga simu kiasi kwamba ikaonekana kuwa kero kwa Gideon hali iliyomfanya kukubali kuonana naye kwani kwa jinsi alivyokuwa akisumbua, alijua kabisa kuna siku Juliana angejua kile kilichokuwa kikiendelea.

“Aya nimekuja! Unahitaji nini?” aliuliza Gideon baada ya kuonana na msichana huyo.
“Gideon! Nimeshindwa kuvumilia. Ninakupenda mno. Nimekuwa nikitamani sana kuwa nawe, umenitesa sana moyoni mwake, sijiwezi, nimekuwa mtu mwenye mawazo sana juu yako, najua kwamba una mtu lakini sidhani kama Juliana anaweza kukuondoa moyoni mwangu,” alisema Halima huku akimwangalia Gideon aliyeonekana kushangaa.

Halima alikuwa msichana mrembo sana, tena zaidi ya Juliana. Gideon alishangaa, ilikuwaje msichana mrembo kama huyo amtongoze na wakati kulikuwa na wanaume wengi waliokuwa wakimfuata? “Unanichanganya Halima,” alisema Gideon.

“Gideon! Nakuchanganya!”
“Inakuwaje msichana mrembo kama wewe uniambie kwamba unanipenda? Kuna wanaume wengi wanakufuata na kukuhitaji, inakuwaje uje kwangu?” aliuliza Gideon.
“Kwa sababu nakupenda.”
“Lakini nina mtu!”
“Hata kama Gideon! Ninakupenda, ninakuhitaji, naomba uwe wangu,” alisema msichana huyo.

Gideon alibaki kimya, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria mpenzi wake, Juliana. Ni kweli Halima alikuwa mzuri wa sura, alipendeza na kuvutia machoni mwake lakini kumsaliti Juliana kwa ajili yake aliliona jambo gumu sana.
Alikumbuka jinsi alivyoteseka kwa ajili ya Juliana, zaidi ya miezi mitatu alijifanya mlokole akishinda na Biblia, iweje leo aje kumsaliti msichana huyo kiwepesi namna hiyo?

Je,nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 12...

“Haiwezekani!” alisema Gideon.
Huo ndiyo ulikuwa msimamo wake, hakutaka kabisa kuwa na Halima, moyoni mwake, hakukuwa na msichana aliyekuwa na nafasi kubwa kama Juliana.
Siku ziliendelea kwenda mbele, msichana huyo hakutulia, aliendelea kumsisitizia mwanaume huyo kwamba alikuwa akimpenda sana lakini Gideon hakuwa mwepesi kukubaliana naye. Moyoni mwake kulikuwa na msichana mmoja tu, Juliana ambaye kwake alikuwa kila kitu.

Juliana akaanza kuingiwa na hofu, kila alipokuwa akimwangalia mpenzi wake aliona kabisa kukiwa na utofauti, hakuwa na furaha kama kipindi cha nyuma, hakuwa amechangamka kama siku chache zilizopita.
Alimzoea sana, mabadiliko hayo yakamtia hofu na kuanza kumuuliza, kama mpenzi wake alitakiwa kujua kila kitu. Alipomuuliza, Gideon hakumwambia ukweli, alimwambia kwamba hakukuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, alikuwa kawaida kama zamani.

“Hapana! Hebu niambie mpenzi wangu. Kuna nini?” aliuliza Juliana huku akimwangalia Gideon.
“Hakuna kitu!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo mpenzi! Naomba uniamini,” alisema Gideon, hapohapo akamsogelea Juliana na kumkumbatia, akampiga mabusu mfululizo kwenye paji la uso wake na mdomo.

Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, Gideon hakutaka kabisa kumsogelea Halima, kila alipokuwa akimuona alikuwa akimkwepa. Msichana huyo hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kuchukua simu yake na kuanza kuwasiliana na mwanaume huyo huko.

Bado Gideon hakutaka kuelewa, hakuwa tayari kuona akitembea na msichana mwingine zaidi ya Juliana. Halima alijitahidi, alipambana kwa nguvu zote kulichukua penzi la Gideon lakini ikashindikana kabisa, hivyo alichokifanya ni kuanza kumtumia picha mbalimbali.

Zilianza picha za kawaida ila kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele msichana huyo akabadilisha picha zake na kumtumia picha za nusu utupu mpaka zile za utupu kabisa. Gideona aliziona, akachukia mno moyoni mwake kwani alijua madhara ya kuwa na picha zile katika simu yake. Hapohapo akampigia Halima.

“Ndiyo unafanya nini?” aliuliza Gideon huku akionekana kuwa na hasira sana.
“Kwani nimefanyaje mpenzi?

” Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 13...

“Nani mpenzi wako? Hivi unaona mimi ni mjinga mpaka kunitumia mapicha yako. Wewe mwanamke nielewe. Usinitumie tena picha zako,” alisema Gideon kwa hasira. “Nitashindwa kujizuia. Ukikata simu, nakutumia tena!” alisema Halima na kukata simu.
Gideon alifikiri ulikuwa utani, msichana huyo hakukoma, akamtumia tena na tena kitu kilichomfanya kuwa na hasira kupita kawaida.

Hofu yake kubwa ilikuwa ni mpenzi wake, Juliana, alijua kwamba endapo msichana huyo angeendelea na tabia yake ya kumtumia picha hizo kila siku basi kuna siku ingetokea balaa endapo tu msichana huyo angeziona.
Hakutaka hilo litokee kwani kwenye kitu ambacho hakutaka kabisa kuona kikipotea mikononi mwake kilikuwa ni mpenzi wake, Juliana, msichana mpole, mnyenyekevu na aliyekuwa na mapenzi ya dhati kutoka moyoni mwake.

Kazi kubwa ya Gideon ilikuwa ni kuzifuta picha za msichana huyo. Alizituma nyingi tena huku zikimuonyesha akiwa kama alivyozaliwa na nyingine zikiwa ni video ambazo zilimuonyesha akicheza mtupu na wakati mwingine akifanya matendo yasiyoandikika hadithini.

Gideon alichukia lakini hakuwa na jinsi, moyo wake ulishikwa na ghadhabu kiasi kwamba akaamua kuiblock namba ya msichana huyo ili asiweze kupokea ujumbe wowote kutoka kwake.
“Gideon! Nahisi kuna kitu kinaendelea, hebu niambie kuna nini,” alisema msichana Juliana huku akimwangalia mpenzi wake.

“Hakuna kitu!” “Umekuwa ukiniambia hivyo mara nyingi na kila ninapokuangalia nagundua kwamba kuna kitu, naomba uniambie, kuna nini mpenzi wangu!” alisema Juliana.
Majibu yake hayakubadilika, hakutaka kumwambia kuhusu msichana Halima kwa kuamini kwamba wawili hao wangeweza kugombana. Siku zikaendelea kukatika huku ugomvi baina yake na Halima ukiendelea kila siku.

“Ngoja nifanye kitu,” aliwaza Gideon, alipata njia ya kumzuia msichana huyo asimfanyie mchezo ule tena.
Akamfuata rafiki yake aliyeitwa Fred na kumwambia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Fred hakuamini, alimjua Halima, alikuwa msichana mrembo aliyekuwa akitongozwa na wanaume wengi na kuwakatalia, hakuamini kama msichana huyo angeweza kufanya vitu vya kipumbavu kama hivyo.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 14...

“Kwa Halima! Hapana Gideon! Labda useme wakina Stella lakini si Halima huyu,” alisema Fred huku akimwangalia Gideon.
“Niamini! Huyu msichana mchafu sana. Alinitumia mapicha yake mengi sana ya utupu utupu,” alisema Gideon.
“Kwanza hebu nizione.”
“Uone nini?”
“Hizo picha. Nataka nione akiwa mtupu anafananaje!” alisema Fred huku akionekana kuwa na mshawasha wa kuona picha hizo.

“Nilizifuta!”
“Gideon! Unapata picha za utupu za Halima unazifuta! Daah! Sasa huo si ndiyo ushahidi wenyewe! Halafu picha za Halima kweli unazifuta kaka, tena unaniambia mimi bila kunificha! Haki ya Mungu ningekuwa Syria, ningevivisha mabomu nije kujilipua mbele yako, hutakiwi kuishi kabisa, Mungu kakupa pumzi za kuishi, wewe unazitumia kufuta picha za utupu za Halima! Haupo siriazi kabisa,” alisema Fred huku akimwangalia Gideon kwa macho yaliyoonyesha mshangao mkubwa.

Gideon hakutaka kujali, alichokuwa akihitaji ni kusaidiwa na kijana huyo tu, alimwambia dhahiri kwamba walitaka kufanya mchezo ambao ungemfanya msichana huyo kutokutuma picha tena au kumsumbua na jambo zuri ambalo lilitakiwa kufanywa ni kumfuata na kumwambia kuhusu picha hizo za utupu.

Kwa Fred wala hakukuwa na tatizo, akakubaliana na Gideon kwamba kitu hicho kingefanyika kwa haraka sana na hivyo baada ya kuachana, jioni ya siku hiyo akamtafuta msichana huyo na kumuomba kuonana naye kwa ajili ya kuzungumza.
“Uzungumze na mimi?” aliuliza Halima, kama kawaida yake akabinua kidogo midomo.

“Ndiyo!”
“Hapana! Nipo bize sana,” alisema huku akichukua mkoba wake na kuanza kuondoka.
“Sawa. Tutakutana kwenye Mtandao wa Global Publishers kwa ajili ya kuzioa picha zako za utupu,” alisema Fred, hakutaka kubaki mahali hapo, huyo akaanza kuondoka zake.

Halima akashtuka, hakuamini kile alichokisikia, alihisi kwamba alisikia vibaya alichokuwa ameambiwa na mwanaume huyo, akahisi damu yake ikianza kuzunguka kwa kasi mwilini mwake, mapigo ya moyo yakaanza kudunda kwa nguvu, hakutaka kubaki mahali hapo, kwa kasi akaanza kumfuata Fred.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 15...

Kwa kuwa naye alijua kwamba msichana huyo alikuwa akimfuata, akaongeza mwendo, japokuwa Halima alikuwa akiita ili asimame lakini hakusimama, aliendelea kutembea kwa mwendo wa haraka.
Moyo wake ukawa na hofu kubwa, aliufahamu mtandao wa Global Publishers, aliamini kwamba kama picha zake zingetolewa katika mtandao huo, mwisho wa siku zingemaliziwa katika magazeti kitu ambacho kingemfanya kupata aibu ya mwaka ambayo hakuwahi kuipata maishani mwake.

Hakukuwa na picha za utupu alizowahi kupiga zaidi ya zile ambazo alijipiga na kumtumia Gideon, moyo wake ukaanza kujuta, kitendo chake cha kuonyesha mapenzi kwa mwanaume huyo kwa kuamini kwamba angependwa kukaonekana kuanza kumtia aibu ambayo hakuwahi kuifikiria kabla.
“Naomba unisubiri wewe kaka,” alisema Halima huku akikimbia kumfuata Fred.

Fred akasimama, msichana huyo akamsogelea, alikuwa akihema kwa nguvu, alichoka kukimbia, tayari macho yake yalibadilika, yakawa mekundu kwani tayari machozi yalianza kukusanyika machoni mwake. Alimwangalia mwanaume huyo huku akionekana kutia huruma sana, kwa sababu alikuwa amedharauliwa, naye akamuonyeshea dharau msichana huyo kwa kumwangalia juu mpaka chini, halafu akamsonya.

“Naomba uifiche aibu hii!” alisema Halima.
“Eti msichana mzuri unatuma picha kwenda kwa mwanaume, hata aibu huoni. Sasa dawa yako moja tu, picha zako nawapa watu wa magazeti ya udaku ili ukome, tutafanya kama tulivyofanya kwa msichana Salma,” alisema Fred, yote ilikuwa ni kumtisha msichana huyo, hakukuwa na kitu kilichotokea, ila aliamua kulitumia jina la Salma kwa kuamini kwamba msichana huyo angeamini kwamba kulikuwa na mtu ambaye naye alifanyiwa mchezo kama huo.

“Naomba unihurumie kaka yangu!”
“Nikuhurumie wewe! Wewe nguchiro, wewe kibweka! Naanzaje kwa mfano?” aliuliza Fred kwa nyodo na kuanza kuondoka.

Halima aliendelea kulia, alichanganyikiwa, alichokuwa akikiona mbele yake ni aibu nzito ambayo hakujua angeificha wapi sura yake. Huo haukuwa muda wa kumlaumu Gideon kwa kile alichokuwa amekifanya bali alitakiwa kupambana kuhakikisha kwamba picha zake hazitolewi kwenye mitandao ya kijamii na magazetini.

Je, nini kitaendelea?
 
JULIANA-03....

Moyo wa Juliana ukachoma, akahisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake, hakutegemea kusikia maneno kama hayo yakitoka mdomoni mwa mume wake. Alimkumbuka, alihitaji faraja, alijua kwamba alikuwa akipitia katika kipindi kigumu, alitakiwa kubembelezwa, alitakiwa kufarijiwa na kutiwa moyo sana lakini kwa mume wake huyo, hilo lilionekana kuwa kama ndoto. Angeanzaje kumkumbatia?
“Unalala sebuleni au chumbani?” aliuliza Gideon.

“Popote utakapolala! Siwezi kulala peke yangu tena! Gideon mume wangu! Kumbuka tulivyokuwa, kumbuka ulivyoahidi mbele ya kanisa, shida na raha, ugonjwa na afya! Umesahau yote hayo mume wangu?’ aliuliza Juliana huku akimwangalia Gideon.

“Clock is ticking…” (muda unakwenda tu)
“Gideon! Pleasee..” (tafadhali, Gideon..)
Gideon akasimama, kwake, maneno yote aliyokuwa akiambiwa na mkewe hayakuonekana kuwa na maana kabisa, hayakumuingia hata kidogo moyoni mwake. Alimchukia Juliana, hakumpenda, alikuwa radhi kulala na mbwa lakini si kulala na mtu kama Juliana.

Alibadilika, hakuwa mzuri, hakuwa na mvuto, kila alipomwangalia, alionekana kuwa kama kituko. Bosi yeye, milionea, eti alale na mtu kama Juliana! Ili iweje? Thamani ya mwanamke huyo ilipotea moyoni mwake, mapenzi yakapotea, chuki ikaingia moyoni mwake.

Kila alipomwangalia, alitamani kumuua, alitamani kumchukua na kwenda kumtelekeza mahali fulani lakini si kuendelea kukaa ndani ya nyumba yake, yaani kila alipokuwa akiamka, amkute chumbani humo. Alimchukia kupita kawaida.

“Kuna siku nitamuua tu! Nitakuja kumuwekea sumu kwenye maji,” alisema Gideon huku akipiga hatua kuelekea chumbani, hakuyajali machozi ya Juliana, jinsi alivyokuwa akilia, kwake alimuona kama muigizaji wa Bongo Muvi ambaye alikuwa kwenye filamu kali ya majonzi.
Huo ndiyo ulikuwa msimamo wake, alimchukua mkewe, yuleyule mwanamke ambaye kipindi cha nyuma alimwambia kwamba alimpenda kwa moyo wote, alimpenda hata zaidi ya alivyokuwa akiwapenda wazazi wake.

Kansa ikabadilisha kila kitu, ikayaondoa mapenzi aliyokuwa nayo na kupandikiza chuki moyoni mwake. Hakukuwa na jingine alilokuwa akilifikiria zaidi ya kumuua mwanamke huyo ambaye bado alikuwa akiteseka kila siku.

Unajua nini kiliendelea?
Pamoja sana shunie
 
SEHEMU YA 16...

Hakutaka kujiuliza kama mwanaume huyo kweli alikuwa na picha zake au la, jibu alilokuwa nalo ni kwamba alikuwa nazo kwani kama hakuwa nazo, alijuaje kama alipiga picha za utupu na kumtumia mwanaume? Hakutaka kuona akiadhirika na watu kugundua kile kilichokuwa kimetokea.

Akawafikiria wazazi wake, akawafikiria marafiki zake na ndugu zake, endapo picha zake zingeanza kusambaa na kuzipata, nini kingetokea? Jamii ingemchukuliaje kama tu wangegundua kwamba yeye ndiye aliyepiga picha zile za utupu? Je, chuo kingeweza kumvumilia kuwa naye kama mwanafunzi wao, kitendo cha picha hizo kuwa hewani kilimaanisha ndiyo ungekuwa mwisho wa kusoma chuoni hapo.

“Naomba usitume picha hizo, nitakupa chochote utakachotaka,” alisema Halima huku akimwangalia Fred, macho yake tu yalionyesha kumaanisha alichokuwa akikisema.
“Hahaha! Mimi nataka vingi sana! Huwezi kunipa vyote,” alisema Fred huku akimwangalia msichana huyo.

“Niamini! Nitakupa kitu chochote utakachotaka!” alisema Halima huku akiomba hasa.
“Sawa. Nahitaji milioni mia moja. Ukizipata, njoo nazo kesho,” alisema Fred huku akimwangalia msichana huyo.
“Jamani wewe kaka!”

“Sasa mbona sikuelewi! Unaniambia utanipa chochote, nimekwambia mkwanja unaanza kulialia,” alisema Fred.
“Naomba uniambie kingine. Nakuomba!”
“Basi tukutane pale Jumanj hotel tuzungumze kidogo manake kuna waandishi washanipigia simu wanataka kuzinunua picha zako,” alisema Fred, kichwa chake kilikuwa makini sana kwenye kutengeneza mikwara ya harakaharaka.

“Sawa kaka yangu! Nitakuja!”
Wakakubaliana ni muda gani walitakiwa kuonana mahali hapo. Halima alijua kile ambacho kingekwenda kutokea huko, lawama zake nyingi zilikuwa kwa Gideon ambaye hakuonekana kujali na aliamua kufanya hivyo kwa ajili ya kumkomoa tu.

Hakutaka kuwasiliana na Gideon, alitaka kumaliza tatizo lililokuwa mbele yake kwanza kwani kama angemwambia mwanaume huyo, alikuwa na uwezo wa kuwatumia picha hizo wanaume wengine kitu ambacho kingekuwa kibaya zaidi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 17...

Kwa Fred, moyo wake ulikuwa na furaha tele, muda wote alikuwa akicheka kwa furaha. Kwa kipindi kirefu alimtamani msichana huyo, alimvutia lakini hakujua angempata vipi lakini leo, alikuwa na uhakika wa kuwa na msichana huyo chumbani.
Hakutaka kuvumilia, akampigia simu Gideon na kumshukuru sana kwani kwa tekniki aliyokuwa ameitumia hatimaye alikuwa akienda kukamilisha jambo ambalo hakuwahi kulifikiria maishani mwake.

“Kaka kwanza nashukuru sana. Mtoto kajaa! Nakutana naye baadaye! Hii ndiyo dawa yao hawa wanaowatumia wanaume picha za hasarahasara. Nashukuru sana mkombozi kwa kuniunganisha na mtoto Halima, kama kawa mtoto mwingine akileta shobo za kukutumia picha za utupu, nisakizie mimi mzee wa kumalizia, wewe ziasisti kama Ozil vile,” alituma ujumbe wa maneno kwenda kwa Gideon.

Wakati Fred akituma ujumbe huo uliokwenda katika simu ya Gideon, hakujua kwamba mwanaume huyo alikuwa akioga na ujumbe huo ulipoingia, mtu aliyekuwa karibu na simu yake alikuwa Juliana.

Haraka sana baada ya kuona ujumbe umeingia katika simu ya mpenzi wake, hakutaka kuchelewa, akaichukua simu hiyo, akatoa password na kisha kuufungua ujumbe huo.
Kwanza mtumaji hakuwa na hofu naye, alimfahamu, alikuwa rafiki wa mpenzi wake lakini ujumbe ambao uliandikwa katika simu hiyo ndiyo uliomtia hofu.

Akahisi mwili wake ukitetemeka kwa hasira, hakuamini alichokuwa akikiona. Machozi yakaanza kumlenga, hasira kali ilimkamata, alimfahamu Halima, alikuwa msichana mrembo na hakuamini kama msichana huyo aliwahi kumtumia picha za utupu mpenzi wake.

Kwa kuwa Gideon alikuwa ameanza kuoga, akaenda sehemu ya picha, akazitafuta picha hizo, akazikosa, hakutaka kusubiri, alikuwa akifanya mambo hayo harakaharaka huku akitetemeka, akaenda WhatsApp na kulitafuta jina la msichana huyo, alipoliona, akaona ikiwa imeblokiwa. Hakutaka kuridhika, aliamini kulikuwa na kitu.

Akatoa block kisha kumtumia ujumbe mfupi uliosomeka ‘Simu yangu noma, njoo huku 0256780953’ kisha akamtumia na kuzifuta meseji hizo. Akatulia kusikiliza ujumbe kutoka kwa msichana huyo katika laini yake nyingine, alihitaji kujua ukweli juu ya msichana huyo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom