Joe Biden ameshinda uchaguzi wa rais wa Marekani dhidi ya Donald Trump, vituo vya televisheni vimetangaza -- ushindi ambao umehitimishwa na mgombea huyo wa Democratic kushinda maeneo yote yenye ushindani yaliyochukuliwa na Republican mwaka 2016.
Vituo vya televisheni vya CNN, NBC News na CBS News vimetangaza kuwa mbio hizo zimeisha kwa Biden kuibuka kidedea baada ya kukadiria ushindi katika jimbo ambalo lilitarajiwa kuamua mshindi la Pennsylvania.
Biden, mwenye miaka 77, ni mgombea mwenye umri mkubwa kuwahi kuchaguliwa kuingia ikulu ya Marekani, maarufu kwa jina la White House.
Trump, 74, ametoa malalamiko yasiyo na ushahidi dhidi ya wizi mkubwa wa kura, na timu yake ya kampeni imefungua kesi katika majimbo kadhaa.
Ushindi wa Biden umemaliza utawala wa Trump uliotingisha siasa, kuistua dunia na kuiacha Marekani ikiwa imegawanyika zaidi kuliko wakati mwingine wowote.
Vituo hivyo vya televisheni vilimpa ushindi Biden muda mfupi kabla ya saa 5:30 asubuhi baada ya uongozi wa mgombea huyo wa Democratic katika kura za jimbo la Pennsylvania kuwa wa tofauti kubwa isiyoweza kufikika na hivyo kuwa juu katika majimbo yanayoamua mshindi wa uchaguzi wa rais.
Trump hakusema lolote kuhusu tangazo la mshindi, lakini wakati Biden akiongoza wakati wa kuhesabu kura, rais huyo kutoka Republican alitoa tuhuma zisizo na ushahidi za kuwepo na wizi wa kura na kudai kuwa alishinda uchaguzi.
Mapema leo, wakati akielekea katika uwanja wa golf Virginia, alirudia kuandika katika akaunti yake ya Twitter akisema: "Nimeshinda uchaguzi kwa kiasi kikubwa!"
Hata hivyo, matokeo sasa yanamfanya Trump ambaye ana miaka 74 kuwa rais wa kwanza kuongoza kwa muhula mmoja tangu George H. W. Bush aliposhindwa kutetea nafasi yake miaka ya tisini.
Biden, ambaye kura milioni 74 zimeweka rekodi, alikuwa pamoja na mgombea mwenza wake, Kamala Harris, katika mji wa kwao wa Wilmington, Delaware.
Credit: Mwananchi