HADITHI: KIVULI CHEUSI
SEHEMU YA KUMI NA TISA
TULIPOISHIA....
Jafari Hiza akazungumza "Hiyo sumu ndiyo ile niliyokuambuia Vannesa" akamwangalia Vannesa kisha akagota kwenye uso uliomvimba Raymond kwa kulia "Huyu muuwaji ndiye huyu huyu aliyemuua mwanao Bertha na wote niliokupa taarifa juu ya vifo vyao. Huyu ndiye aliyewaua wamiliki wa apartment aliyofanyia mauaji ya shahidi namba moja aliyekuwa akimfahamu kule masaki kwa sumu hiyo hiyo" akawaeleza aina ya sumu ambayo aliitumia kwa kuichanganya katika chupa ya manukato. Habari hiyo haikumfanya Raymond kuacha kulia. Alilia kama mtoto.
Jafari Hiza akaeleza kuwa "hewa hiyo yenye sumu hudumu kwa dakika tano tu hewani, hivyo hakuna shaka kama tukiingia"
Wote wakaingia na kukuta miili ya watu kumi na moja ukiwemo wa bi Furahiya, Majura, walinzi sita na wafanyakazi watatu. Walikuwa wamefunikwa katika mifuko maalumu ya maiti.
******
ENDELEA...........
Wakati ambao walikuwa wakizungumza pale nje, ni wakati ambao Vannesa alimuona tena yule mtu aliyemuona kule hotelini kwa Raymond. Hakuwa amebadili shati lake jeupe, alifunga tai ya pink na suruali nyeusi juu akiwa amehifadhiwa na koti jeusi. Alipendeza sana.
Ila kwa Vannesa ikawa ni tatizo.
Akajiuliza kuhusu kumuona sehemu mbili zote zikiwa ni sehemu za ajabu. Alipatwa na wasiwasi sana juu ya Moses. Akaamua kumpigia simu baada ya kujitoa pembeni kidogo katika maongezi ya Raymond, mama koku na Jafari Hiza.
"Uko wapi Moses?.. Upanga.. Na mimi nipo hapa.. Hallo.. Hallo.."
Simu ikawa imekatwa na alipojaribu kupiga mara ya pili ikawa haipatikani. Akaamua kumtafuta mwenyewe.
Akawa haonekani.
Kulikuwa na umati mkubwa wa watu. Hivyo haikuwa rahisi kumuona.
Alirudi kwa Raymond kumuuliza kuhusu kufahamiana kwake na Moses. Aliamini fika kulikuwa na uhusiano fulani kati yao. Yeye hakuwa akijua kuwa Moses ndiye muhusika mkuu wa mauaji hayo, lakini kwanini Moses awe mtu kama anayeficha jambo kila anapomuona katika mazingira ya himaya ya Raymond? Raymond alikuwa tayari yupo ndani akilia juu ya maiti ya mke wake. Alimuacha kwa muda mpaka atakapopata nafasi nzuri ya kuzungumza.
Wakati ukafika, walikuwa wawili tu majira ya jioni ndani ya gari ya Raymond. Ilikuwa ni baada ya kutoka hospitali.
"Naomba nikuulize jambo Raymond"
Raymond akaitika kiunyonge "Sema chochote Vannesa"
"Unamfahamu mtu anayeitwa Moses?" Raymond akapiga breki ya ghafla na kutumbua macho juu ya uso wa Vannesa, akamuuliza kwa mshituko "Umemfahamu vipi Moses? Umemuona? Namtafuta sana, umemuona wapi huyo kijana tafadhali niambie nitampata vipi?"
Vannesa akaonesha tabasamu tu la kutoridhisha wala kuonesha kama alikuwa anafahamu chochote kuhusu Moses. Yeye mwenyewe akajisuta kuwa hakuwa akimfahamu Moses zaidi ya kumfahamu Moses wa kitandani, alimfahamu Moses wa chumbani, juu ya kitanda cha hoteli aliyekuwa akioga naye bafuni. Hakujua kazi ya moses wala hakuwahi kumuuliza. Hakujua nyumbani kwa Moses wala ndugu zake, ndio sababu hakujibu kitu mpaka Raymond alipozungumza kwa sauti iliyoonesha kukata tama "Moses ameshakufa siku nyingi" akawasha gari na kuanza safari ya kuondoka
"Amekufa!?"
Mshangao wa Raymond akawa ameupokea Vannesa mapigo ya moyo yakamuenda mbio na jasho likamtiririka kiasi cha kutoonekana umuhimu wa kiyoyozi. Akaropoka kwa nguvu licha ya kuwa alikuwa anawaza tu "Ina maana"
*****
Baada ya moses kushindwa kuingia katika hoteli ya Raymond, kuna nafsi ikamsukuma kuelekea nyumbani kwake, Raymond. Ilikuwa ni kama alivyotarajia. Umati mkubwa wa watu wakizungumza kila jambo.
Alichokisikia katika vingi walivyovizungumza ni kile alichokijua.
Jambo lile lile la watu wawili kufa kwa hali ya kushangaza. Lakini sasa hawakuwa wawili tena, waliongezeka watu tisa. Ikamshangaza sana lakini hakupenda kustaajabu sana kwakuwa alifahamu ulikuwa ni uzembe wa mtu yeyote ambaye angekuwa hafahamu kuhusu hila zake. Akajitenga na watu ambao walionekana si aina yake. Watu ambao walionekana ni waswahili na wafupi wa elimu.
Akatazama huku na huko, akavutiwa na kikundi kimoja. Kikundi hicho kilikuwa na watu wa rika lake. Watu walioonekana wenye elimu pamoja na jambo alilokuwa akilidadisi, alikuwa na hakika wao wangekuwa na majibu yake.
Akakisogelea taratibu akajiunga nao.
Ulikuwa ni wakati wa simanzi, hivyo hakuna ambaye alijali ongezeko la mtu kati ya kikundi chao kilichobeba watu sita kabla ya Moses.
"Raymond amepatikana"
Kijana aliyeukaribia uzee, akasema kwa upambe. Mwingine na mwingine wakaendelea kudakia bila kuwa na hakika na chochote. Alichokuwa akikitafuta akawa amekipata. Mmoja kati ya wale waliokaa kwenye kikao akaropoka
"Kwani nyinyi hamfahamu biashara haramu anazozifanya Raymond?" Akanyamaza kwanza. Aliwakagua kila mmoja bila kujali ugeni wa Moses kati kati yao. "Inawezekana amewadhulumu wenzake ndio maana wanamlipizia"
Mwingine akadakia kwa udaku "Unachosema kinawezekana" huyu aliyekuwa anaongea akainama kabisa "walianza kwa mtoto wake Bertha huko kijitonyama sasa wanaendeleza mauaji zaidi"
Kabla hajamaliza kuzungumza, yule ambaye Moses alimkuta akiongea akakohoa.
Moses akamtazama kama wengine walivyokuwa wamefanya. Akamkuta naye akimtazama. Yule kijana aliyetawaliwa na ufukara na shida aliyekonda kwa mawazo, akauliza "Sijuhi wewe ni nani mwenzetu?"
Alikuwa akimuuliza Moses. Moses akajichekelesha pale bila kujibu chochote. Alipoona wote wakimtazama, akapata la kuongea
"Mimi ni mgeni katika mtaa huu ila nimeshitushwa na habari za vifo vya watu hawa" aliwatazama watu wale na kuonyesha waliridhika na majibu yake.
Akamalizia "mnisamehe kama nimeingilia mkutano wenu"
Yule ambaye alikuwa kama kiongozi katikati yao, akamsimamisha Moses mara alipokuwa akigeuka na kutaka kuondoka "Hapana usiondoke" Moses akasimama na kurudi miongoni mwao "tusamehe bwana, unajua hizi habari ni nyeti sana hivyo nilishitushwa na sura yako kwa kuwa wewe ni mgeni katikati yetu"
"Hamna .."
Kabla Moses hajamaliza kuongea, akaiona gari ya Raymond. Akabaki akiwa ameduwaa kuitazama. Kwa nyuma ilikuwa inafuatwa na gari ya Jafari Hiza. Hakufahamu kama ndani yake alikuwepo pia Vannesa. Wote kati yao wakawa wanashangaa alichokuwa akikitazama Moses. Wakaliona gari ya Raymond. Kila mmoja alianza kuaga na mwisho Moses alijikuta amesimama peke yake.
Ni wakati huo alipomuona Vannesa akishuka na Jafari Hiza kutoka ndani ya gari ya jafari. Alipoendelea kutazama kwa muda wa dakika ishirini zaidi, aliyaona macho ya Vannesa yakimtazama.
Alishuhudia mshangao juu ya macho hayo ya Vannesa. Lakini alijizugisha pale na kujiingiza kati kati ya vikundi vya watu kumkimbia Vannesa.
Alipotazama kwa mbali akiwa ameuacha mtaa wa Raymond, alimuona Vannesa akihangaika kumtafuta.
Akacheka kwa kuuzika na kujisemea moyoni
"Hutaniona tena Vannesa"
Akatokomea anapopajua.
*****
ITAENDELEA...................!!!