Kwa karibu masaa sita ka nzi kalikuwa kametulia kwenye ukumbi makao makuu ya Tanesco ambapo Mkurugenzi wa Shirika hilo Dr. Idris Rashid alikuwa aje kuzungumza na waandishi hususan suala kununua majenereta ya kufulia umeme ambayo yanamilikiwa na kampuni yenye utata wa umiliki wake na yenye kuhusishwa na kampuni ya kifisadi ya Richmond, Dowans.
Hata hivyo, muda si mrefu uliopita mtumishi wa Tanesco aliingia ukumbini na kuwaambia waandishi waliokuwa wanasubiri kwa muda mrefu kuwa Bw. Idris hatozungumzia nao na kuwaomba radhi.
Hata hivyo, vyanzo vyetu vyenye uwezo wa kupenya kuta na madari vinadokeza kuwa suala la Dowans limefikia mahali pagumu ambapo sasa Tanesco wako tayari kuachana na wazo hili ili kutafuta vyanzo vingine vya umeme wa dharura na ya kuwa wametilia maanani "kelele" za wadau mbalimbali. Hili linakuja baada ya sauti za Spika wa Bunge la Muungano Mhe. Samuel Sitta na Mbunge wa Kyela Mhe. Harrison Mwakyembe kupaza sauti zao kupinga mpango huo. Ujumbe ambao umepokelewa toka kwa watunga sheria hao ni kuwa yeyote atakayenunua majenereta ya Dowans ajiandae kuwajibika Dodoma kama walivyowajibishwa wengine!
Tishio hilo ambalo limepokelewa kwa hisia ya kunyong'onyea limetuma ujumbe ulio wazi kuwa endapo serikali itatekeleza au kutoa baraka kwa Tanesco kufanya kitu ambacho wanajua hawapaswi kufanya basi patakuwa hapakaliki. Hadi hivi sasa kundi kubwa la wabunge waliosimama upande wa ripoti ya Kamati Teule kuhusu Richmond, limeshajipanga tayari kuanzisha "kasheshe" jingine ambalo linaweza kabisa kuitikisa serikali.
Hata hivyo, Dr. Idris inaonekana bado amekuwa na 'kichwa ngumu' hasa baada ya serikali na kamati za Bunge zote kuiachia uamuzi wa mwisho kuhusu suala la mitambo. Hata hivyo, kuna imani kuwa alichofanyiwa Dr. Idris ni kupewa kisu ashike, tatizo ni kuwa amepewa upande wa makali huku mpingi ukiwa umeshikwa na wengine ambao wako tayari kuuvuta.
Kutokana na hili, kuna kila dalili Dr. Idris anaweza kutangaza kujiuzulu wadhifa huo kitu ambacho alijaribu kukifanya muda si mrefu uliopita kuhusiana na suala la kampuni ya saruji ya huko Tanga. "Hayuko tayari kujitundika mwenyewe kitanzini kwa kamba yake mwenyewe!" amedokeza mmoja wa watu wanaojua suala hilo.
Sasa hivi kinachosubiriwa ni muda tu kuona Dr. Idris atafanya nini huku akijua kuwa tayari anahusishwa na kashfa ya rada suala ambalo nalo hajalitolea maelezo yoyote. Hadi hivi sasa uchunguzi wetu unaonesha kuwa asilimia 90 ya uamuzi uliofikiwa hadi sasa ni kutoendelea na suala la Dowans.
Hata hivyo upande mwingine bado unadokeza kuwa endapo serikali haitanunua mitambo ya Dowans na hivyo kuwasababishia hasara "wawekezaji" hao ambao walikuwa na uhakika kuwa serikali itanunua mitambo hiyo basi Watanzania "watakiona" kwani upungufu mkubwa wa umeme ambao tulidokeza unakuja mwezi wa nne, utaifanya serikali iipigie magoti Dowans na hata kununua majenereta yale yale katika bei ya juu!!
"Watanzania hawawezi kuvumilia kukaa gizani muda mrefu hasa huku mjini, kwa hiyo usishangae hao hao wanaopinga sasa wakaja baadaye kutaka serikali inunue mitambo hiyo aidha kutoka kwa dowans au kwa mtu atakayekuw ameinunua" alisema mdokezaji huyo.
Uwezekano wa kutokea yote mawili ni mkubwa zaidi. Hata hivyo, kama dhamira ya kuwalipa Dowans kwa gharama yoyote itatekelezwa basi kuna dalili Dr. Idris na timu yake watacheza bahati nasibu na kuendelea na mradi huo wakijua kuwa huko Bungeni tayari wana kura za kutosha kuzuia mapigo ya kina "mwakyembe".