Zitto Kabwe awanasa CCM katika nyavu zao
:: Atumia ndoano ya PPRA kuwachota wenye msigano CCM
:: Ahoji upya wa mashine za IPTL, uzee wa mashine za Dowans
:: Maslahi ya makundi yazidi kujidhihirisha, kila mtu na lake
Na Innocent Munyuku
KABWE Zitto, yule mwanasiasa kijana machachari wa kambi ya upinzani, aliyeijeruhi CCM na kuiacha kwenye wodi ya wagonjwa mahututi wa kisiasa mwaka 2007, sasa anakaribia kufanya hivyo, lakini safari hii akipitia mlango wa mitambo ya kufua umeme ya Dowans.
Na kwa bahati mbaya, kama ilivyokuwa kwa John Samwel Malecela aliyeshindwa kuzuia jaribio la kumtoa bungeni kipindi kile, sasa mpira upo mikononi mwa kundi la wanasiasa wa CCM wanaojiita machachari ambao inaelekea wako tayari kugawana mbao za boti lao; tendo ambalo matokeo yake ni boti kuzama.
Na kama vile Zitto anajua udhaifu wa makundi ya CCM, safari hii anatumia hoja nzito inayogusa mustakabali wa taifa zima na matokeo ya aina yoyote ile, yatamuibua Zitto kama shujaa.
Hoja iliyopo mbele yetu, ni ununuzi wa mitambo ya kufua umeme ya Dowans ambao unaungwa mkono na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma huku ukipingwa na Kamati ya Madini na Nishati chini ya uenyekiti wa William Shellukindo na msaidizi wake, Dk. Harrison Mwakyembe. Viongozi wa kamati hii wote ni wanachama wa CCM.
Maamuzi au tuseme dalili za kamati hiyo chini ya Zitto ya kutaka kubariki ombi la TANESCO kununua mitambo ya Dowands, na kauli za makundi kadhaa zilizofuatia msimamo huo, ni ishara tosha kwamba Rais Jakaya Kikwete anahitaji kutumia juhudi za ziada, kuchungulia ndani ya chama chake na kuupata ukweli kuliko kuusubiri ukweli huo nje kwani hadi ukweli huo unatoka, yeye ndiye atakuwa majeruhi wa kwanza.
Wakati hoja ya ununuzi wa mitamboya Dowans ilipowasilishwa mbele ya Kamati ya Nishati, wajumbe wa kamati hiyo walipinga na sababu kubwa ikiwa kwamba Sheria ya Manunuzi ya mwaka 2004, inaizuia Serikali kununua vitu chakavu. Wajumbe hao walisema kwa sababu mitambo ya Dowans si mipya, kwa hiyo ni chakavu.
Hata hivyo, wajumbe wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, wanaituhumu Kamati ya Nishati ambayo tangu Bunge hili linaanza imekuwa chini ya Mwenyekiti Shellukindo na Makamu wake Dk. Mwakyembe kwamba kamati hiyo imekuwa championi wa kuishauri Serikali kununua mitambo chakavu ya IPTL.
"Ni ajabu kabisa. Soma Hansard zote zinazozungumzia nishati, kamati hii ya Shellukindo imekuwa ikiishauri Serikali kununua mitambo ya IPTL. Wanashauri hivyo wakijua kwamba ipo sheria inayozuia ununuzi wa vitu vikuu kuu. Lakini linapofika suala la Dowans, hii mitambo iliyofanya kazi hapa mwaka mmoja imekuwa chakavu, lakini ya IPTL, ni mipya, alisema mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo na kuongeza:
Mitambo ya IPTL imeingizwa nchini hapa mwaka 1990. Na hata kama mitambo hiyo wakati inaingizwa ingekuwa na umri wa mwaka mmoja, basi sasa ingekuwa na umri wa miaka 20 tangu ilipotengenezwa.
Wachunguzi kadhaa wa mambo ya siasa hapa nchini waliozungumzia na Rai, wamesema mazingira ya mitambo ya Dowans, hayana tofauti na mazingira ya mitambo ya IPTL.
Kwanza Richmond ambayo ndiyo iliiuzia mitambo Dowans iligubikwa na sintofahamu ambayo ilihusishwa na rushwa. Lakini mitambo ya IPTL iligubikwa na tuhuma za rushwa na Katibu Mkuu mmoja aliiambia Mahakama kwamba mmoja wa wawekezaji alitaka kumuhonga. Pili, Dowans ina kesi mahakamani na Serikali. Lakini wote tunajua jinsi Serikali ilivyoshtakiana na IPTL na kwa muda mrefu mambo yake yako mahakamani. Lakini kama ni suala la mitambo chakavu, ya IPTL ni chakavu na imetumika zaidi ya miaka 20 wakati ya Dowans ni chakavu imetumika kwa miaka mitatu. Kwa hiyo mambo yote haya tuyapime katika mizani ya uzalendo kabla ya kufanya maamuzi au kusema chochote, alisema mmoja wa wataalamu wa manunuzi kutoka serikalini.
Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na kupishana kwa kauli kati ya Zitto kwa upande mmoja na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Dk. Harrison Mwakyembe pamoja na Mbunge wa Bumbuli, William Shellukindo kwa upande wa pili.
Zitto kwa upande wake ameshikilia msimamo wa kuunga mkono kusudio la Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) la kutaka kununua mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura yenye uwezo wa kutoa megawati 100 inayomilikiwa na Kampuni ya Dowans.
Hata hivyo, Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema) amejikuta akisigana na Dk. Mwakyembe ambaye ni Mbunge wa Kyela (CCM) anayeungana mkono na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, William Shellukindo. Mwakyembe ndiye alikuwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza suala la Richmond. Hata hivyo, Kamati hiyo haikusema chochote juu ya kununua au kutonunua mitambo ya Dowans.
Siku chache zilizopita, Shellukindo aliweka msimamo wake hadharani kwamba dhamira ya TANESCO haikubaliki kwake.
Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa na Rai umebaini kuwa kusigana kwa Zitto na Dk. Mwakyembe kunatokana na ukweli kwamba Zitto anafahamu maslahi ya baadhi ya makundi ya wabunge wa CCM.
Hivi karibuni Zitto aliongea na mwandishi wa gazeti hili akisema kuwa suala hili ni jaribio kubwa si kwake bali kwa kamati yake nzima.
Hili ni jaribio la kiuongozi ambalo kamati yangu inakabiliwa nalo. Kuna kipindi kiongozi anachukua maaamuzi yanayowaudhi watu unaowaheshimu ili kuokoa taifa.
Kamati itapeleka maoni yake kwa Spika kwani kanuni zinanibana kusema kuhusu maamuzi ya kamati. Ila ni kweli tumeomba kukutana na Kamati ya Nishati na Madini na ninaamini tutakubaliana, alisema Zitto.
Kauli hiyo ya Zitto inatafsiriwa na wachambuzi kuwa ni kukataa kuingia katika mtego wa kisiasa. Kwa mara kadhaa Zitto amekuwa akisema kuwa malumbano yanayoendelea hivi sasa ndani ya CCM si ya ujenzi wa taifa bali ni ya maslahi binafsi yenye mwelekeo wa uchaguzi wa mwaka 2015.
Sisi ndiyo tulianzisha hoja ya ufisadi. Lakini wenzetu ndani ya CCM wakaidaka na kuifanya hoja yao. Kwa bahati mbaya, wao hawapingi ufisadi bali wanapigana wao kwa wao kutaka kutafuta nafasi ya kuwa karibu na rais. Ndiyo maana mimi hunisikii nikitaja watu majina. Naogopa kuwa sehemu ya historia ya siasa chafu, alisema Zitto katika mahojiano maalumu na gazeti hili matoleo kadhaa yaliyopita.
Hoja ya ununuzi wa Dowans, imekuja baada ya TANESCO kuwasilisha ripoti yake kwenye Kamati ya Bunge ikieleza matatizo makubwa inayokabiliwa nayo.
Katika mkutano huo, kamati ilijadili ripoti hiyo iliyowasilishwa na Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Dk. Idrisa Rashid aliyewaeleza wajumbe kuwa mipango yote iliyopo haiwezi kuziba pengo la umeme kabla ya mwaka 2010 kwa sababu mipango yote mikubwa ya umeme huhitaji si chini ya miaka miwili.
Alisema njia pekee inayoweza kulinusuru taifa hili ni kununua mitambo ya dharura ya umeme inayoweza kukamilika katika kipindi cha miezi sita.
Hoja yake hiyo ilikuja baada ya Kampuni ya Barrick, kujitoa katika udhamini wa mradi wa umeme wa Mtwara wa megawati 300 unaojulikana kama umeme wa Artumas. Barrick ilikuwa itoe dola za Marekani milioni 400 wakati TANESCO ilikuwa itoe dola milioni 500.
Katika mradi huo, kazi ya Tanesco ilikuwa kutengeneza njia ya umeme hadi Kibaha kwa gharama ya dola za Marekani milioni 500 wakati Barrick na artumas kwa pamoja walikuwa na kazi ya kuzalisha umeme yaani generation kwa gharama ya dola milioni 400.
Kutokana na upungufu huo, kamati hiyo ya Zitto ilishauri TANESCO kuchukua hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na kufufua miradi kadhaa ya umeme ukiwamo ule wa upepo wa Singida wenye uwezo wa kutoa megawati 50 na umeme wa Kinyerezi wenye uwezo wa kutoa megawati 240.
Zipo dhana kwamba makundi yanayopingana ndani ya CCM mengine yanataka nchi iwe katika giza hasa katika kipindi hiki cha kuelekea katika uchaguzi ili wapate nafasi ya kumzomea Rais Kikwete. Na ili kuipa hoja yao nguvu, wanashikiria msimamo kuwa kununua mitambo ya Dowans ni sawa na kushiriki ufisadi.
Hali hii ndiyo imemshtua Waziri wa Nishati na Madini, William Ngereja na kusema kuwa kununua mitambo ya Dowans si ufisadi na kwamba Serikali imejifunza mengi katika mgogoro wa Richmond.
Tayari kuna taarifa pia kuwa kusigana kwa wabunge hao machachari ndani ya Bunge kunaashiria uwazi wa maslahi kwa makundi fulani katika mchakato mzima wa ununuzi wa Dowans.
Dk. Mwakyembe anapozungumzia suala hilo anasema anashangazwa na msimamo wa kamati ya Zitto kuhusu mitambo ya Dowans wakati jukumu la kuizungumzia si lake.
Kwa mujibu wa Dk. Mwakyembe, kazi kubwa ya kamati ya Zitto ni kuangalia hesabu na wala si sera kama kanuni za Bunge zinavyosema. Anasema uamuzi uliofanywa na Kamati ya Madini na Nishati kuhusu kutonunua mitambo ya Dowans hauwezi kutenguliwa na kamati nyingine ya Bunge.
Zitto analijua hilo na ndiyo maana anasema kuwa hakuna hoja yoyote iliyowahi kupitishwa na bunge iliyozuia kununua mitambo hiyo.
Hata hivyo, hoja ya Dk. Mwakyembe inakinzana na hoja aliyoitoa Katibu wa Bunge, Dk. Kashilillah aliyesema kuwa si sehemu ya kazi za Bunge au kamati zake, kuiambia Serikali jinsi ya kufanya manunuzi bali kazi ya Bunge ni kushauri tu.
Hofu ya Zitto ni kwamba taifa lisije kuingia katika giza kutokana na kukosekana kwa umeme. Na ndio maana kamati yake ikamwomba kibali Spika wa Bunge ili aruhusu kuitisha kikao cha kamati hizo mbili ambacho Katibu wa Bunge alisema hakiwezi kuitishwa kwa sababu hakuna kamati ya bunge yenye mamlaka hayo.
Katika kikao hicho, Zitto akapendekeza wakutanishwe pia na wawakilishi wa Serikali, Tanesco yenyewe na Mamlaka ya Usimamizi wa Manunuzi ya Umma (PPRA).
Zipo taarifa kutoka Tanesco kwamba kwa kila Sh 100 inayopata shirika hilo kwa siku, Sh 84 hulipwa kampuni zinazoiuzia umeme na umeme unaonunuliwa ni asilimia 45 tu ya umeme wote unaozalishwa. Kwa sasa taifa linakabiliwa na upungufu wa megawati za umeme zaidi ya 100.
Desemba mwaka jana, Kamati ya Nishati na Madini inayoongozwa na Shellukindo ilipinga ununuzi wa mitambo hiyo huku Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja akitaka inunuliwe.
Waziri Ngeleja alisema utetezi wake kutaka kununuliwa kwa Dowans unatokana na ukweli kwamba mpango huo hauna chembe za ufisadi.
Wakati akitoa msimamo wake huo, Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ilishashauri kuwa Serikali isinunue mitambo hiyo kwa vile imeshatumika lakini pia ikasema kufanya hivyo ni kinyume cha sheria ya manunuzi ya umma.
Ngeleja aliwakumbusha wananchi wanaodhani kuwa kuna ufisadi katika mchakato huo kukumbuka mlolongo wa suala la Richmond na kwamba Serikali ya sasa haijalala.
Kununuliwa kwa mitambo hiyo kunatokana na shinikizo la ukuaji wa uchumi ambao kwa sasa mahitaji yake ya umeme yanaongekeza kwa asilimia kati ya 10 hadi 15 kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2008 hadi 2012. Ongezeko hilo limo katika taarifa ya utafiti uliofanywa na Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Umeme.
Thamani ya mitambo ya Dowans kwa sasa ni kati ya dola za Marekani 58 hadi 60 milioni na kama ikiwa mipya thamani yake ni dola za Marekani milioni 120.
Suala la ununuzi wa mitambo hiyo limekuwa tata kutokana na historia ya utata wa mkataba wa Kampuni ya Richmond Development Company LLC katika ufuaji umeme wa dharura ambao baada ya Kamati Teule ya Bunge kutoa ripoti yake baadhi ya watendaji wakuu Serikali walilazimika kujiuzulu.
Dowans ililetwa nchini mwaka 2006 baada ya Richmond kushindwa kutekeleza jukumu lake la kuleta mitambo ya kufua umeme wa dharura na ilisaini mkataba wa miaka miwili.
Hata hivyo, Serikali ilivunja mkataba na Dowans Julai mwaka jana, kwa maelezo kwamba wakati wa kuipa mkataba, taratibu za PPRA zilikiukwa.
Serikali ilidai kuwa wakati wa kuipa Dowans mkataba, kuna mambo hayakuwekwa sawa ikidai utata wa uhalali wa usajili wa Kampuni ya Richmond na hivyo kuutangaza mkataba wake kuwa batili, hali iliyobatilisha hata mkataba wa Dowans.
Dowans iliamua kukimbilia katika Mahakama ya Biashara ya Kimataifa iliyopo jijini Paris nchini Ufaransa na mitambo hiyo inashikiliwa na Tanesco ili wakishinda kesi mitambo ifidie hasara. Lakini kwa sasa shirika hilo la umeme limedhamiria kuinunua.
Pamoja na hayo yote, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, iliridhika kwamba hapajakuwapo na Azimio la Bunge la kuzuia mitambo kununuliwa lakini ikakubaliana kuwa ili pawepo na uelewano bungeni, ikutane kwanza na kamati ya nishati.
Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo alisema kuwa gharama za kutafuta mitambo mipya ni kubwa sana kwa bei na kwa muda wa zaidi ya miaka miwili na akashauri kutenganisha mitazamo ya kisiasa kwenye maamuzi ya kiuchumi.
source: RAI