Nimekuwa nikosoma na kufuatilia sehemu kubwa ya taarifa kuhusiana na kinachoitwa "kauli ya Zitto" kuhusiana na sakata la mitambo ya Dowans.
Tatizo nililoliona na ambalo wajumbe wengi wa kamati ya bunge ya hesabu za mashirika ya umma ambayo Zitto ni Mwenyekiti wake wanaliona. Tatizo lenyewe ni lile la taarifa za kwamba kamati imebariki/inashinikiza/inataka mitambo ya Dowans inunuliwe. Wajumbe wote akiwamo Zitto hawajasema LAZIMA mitambo ya Dowans inunuliwe.
Kabla ya kueleza maelezo ya wajumbe wengi wa kamati niliobahatika kuzungumza nao, niweke wazi kwamba Zitto ni Mwenyekiti (anayeongoza vikao) na kuwa Mwenyekiti (si Mwenyekiti Mtendaji) maana yake ni kufanya kazi kwa vikao na kauli zako zinazingatia vikao. Kama hivyo ndivyo tujadili KAMATI.
KAMATI ya POAC (Kamati ya Zitto) imefanya vikao vyake na katika kikao kimoja wapo walikutana na Tanesco katika kupitia hesabu za shirika hilo na kuangalia matatizo yao ya kifedha. Kama kawaida Tanesco ya Dk Rashid ikapenyeza kwa umakini mkubwa matatizo yake ya kifedha na tatizo la ongezeko la mahitaji ya umeme huku kukiwa na upungufu wa uzalishaji baada ya Dowans kutimuliwa na kadhalika.
Maelezo ya Tanesco yakawagusa wajumbe wa POAC na wakaona ni vyema wakapata maoni ya wenzao wa Kamati ya Nishati na Madini (ya kina Mwakyembe) na kwamba wakaweka wazi katika maazimio yao kwamba kuna umuhimu kwa Tanesco kusaidiwa na serikali katika kununua mitambo mipya hata ikibidi kununua ya Dowans kwa sharti la kuzingatia sheria. Ikiwamo sheria ya manunuzi ya 2004. Kwa makini kabisa kamati imesema, "haijabariki ununuzi wa mitambo ya Dowans" na kwamba kamati ya POAC wala ya Nishati na Madini hazina mamlaka ya kuidhinisha wala kuzuia manunuzi ya Tanesco.
Maelezo ya POAC hayajatofautiana na yale ya Kamati ya Nishati na Madini kwamba hata wao hawana mamlaka ya kuzuia manunuzi. Tofauti ya kamati hizi mbili ni kwamba ile ya POAC ilitaka kukaa pamoja na wenzao wa Nishati na Madini kujadiliana jinsi ya kuisaidia Tanesco kiushauri na ili wapate maelezo ya kuridhisha kuweza kuishauri serikali na ili kuzuia kutokea kwa matatizo yaliyotokea wakati wa Richmond. Suala la kununua au kutonunua ama kutaifisha mitambo ya Dowans lingekuja kujulikana baada ya kukaa pamoja.
Kuna matatizo makubwa matatu ambayo yamesababisha hali hii kufikia hatua ya kuanza kushambuliana na hata kuanza kuibuka kwa tuhuma dhidi ya wabunge husika akiwamo Zitto ambaye imefikia hata kutuhumiwa kuhongwa.
1. Tatizo la kwanza ambalo kwa kiasi kikubwa limesababishwa na Zitto mwenyewe kujiamini kupita kiasi na kuwaamini waandishi wa habari kupita kiasi. Amezungumza nao na kwa bahati mbaya sana (kwa kujua ama kutojua) waandishi hao wamepotosha kabisa kauli ya Kamati (si ya Zitto) kwa kusema kwamba kamati imebariki/inataka Dowans inunuliwe. Kamati haikusema hivyo.
2. Tatizo lingine ni lile la kauli kwamba kamati ya Nishati na Madini haijawasikiliza Tanesco, nalo limetokana na tafsiri ya baadhi ya waandishi. Maelezo ya wajumbe wa Kamati na Nishati na Madini ni kwamba wamewasikiliza Tanesco kupitia kwa Waziri wa Nishati na Madini, ambaye alifika katika kikao cha Desemba 14, 2008. Kawaida waziri akiona amezidiwa ndipo huwaita wataalamu wake (Tanesco) kujieleza. Ngeleja alipomaliza kuwasilisha mbele ya uongozi wa Tanesco na Tanesco kutoka nje kuwaacha wabunge wajadili, Ngeleja angeweza kuomba Tanesco warudi wamsaidie, lakini aliridhika na kukubali. Waandishi wakaandika kwamba Kamati imeikatalia Wizara kununua mitambo. Kamati ya Nishati haijakanusha kama ambavyo kamati ya Zitto haijakanusha, kwa sababu ambazo naomba nizianike kwamba wanasiasa ni waoga sana kubishana na vyombo vya habari. Kimsingi hakuna kamati iliyokataa wala kubariki ununuzi wa mitambo ya Dowans.
3. Tatizo kubwa ambalo sasa limeguswa kiaina na baadhi ya wahusika akiwamo Zitto na Dk. Mwakyembe ni tatizo la kisiasa. Zitto amenukuliwa akisema kuna siasa za makundi, Mwakyembe akasema anaona kama operesheni sangara inaendelea. Hilo ni tatizo kubwa kwa kuwa linaweza kubadili mjadala kutoka katika hoja za msingi na kuanza kwa SIASA. Kubadilika kwa hoja kutoka tatizo na kwenda kuwa SIASA.
4. Lakini pamoja na kuwa hoja si ya kisiasa, msingi wake unaweza kuwa wa kisiasa zaidi na kwamba Zitto kama mwanasiasa angepaswa kuangalia pia upande wa hatima yake kisiasa zaidi badala ya kutaka kuwa MAKINI kutenda HAKI kwa kutaka kusikiliza pande zote husika. Hilo linahitaji mjadala pekee kwa kuwa Zitto amekuwa na hulka ya kusikiliza hata wale ambao watu hawapendi kuwasikiliza. Hiyo ni hulka nzuri lakini ni HATARI SANA.
Kwa maoni yangu:
Suala la Dowans asili yake ni hoja tete ya Richmond ambayo ilisababisha kuenguliwa kwa aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri Nazir Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha (ambaye yuko kimya sana). Kuanguka kwa Waziri Mkuu ni hatua nzito katika historia ya nchi hii na kulisababisha kuvunjika kwa Baraza zima la mawaziri. Zitto alilumbana na Spika kuhusu hilo na Rais Kikwete alithibitisha maneno ya Zitto kwa kutangaza kuvunjika kwa Baraza la Mawaziri.
Tukio hilo lilirudisha imani ya umma kwa vyombo vyote vya dola ambavyo walikwisha kupoteza imani navyo na kuona kwamba sasa kumbe hakuna aliye juu ya sheria. Bunge, wabunge, serikali zilipata heshima ndani na nje ya nchi. Sakata la Richmond likawa mtaji mkubwa wa kisiasa kwa wanasiasa ndani ya Bunge na hata kwa Rais. Wapinzani nao waliona kama ushindi kwao. Nchi ilichangamka na masuala mengine kama EPA na kesi za kina Mramba yakafuatia mkondo.
Sasa hivi, yeyote ambaye anathubutu kutaka kubadili HADHI ya Bunge kwa kuhalalisha kwa mlango wa nyuma maovu yaliyotokana na Richmond, atakuwa anairudisha nchi nyuma (si wanasiasa).
Jambo la msingi ni kuzingatia mambo yote ya msingi, ikiwa ni pamoja na kuangalia kwamba Dowans tunawadai bilioni 23, Dowans wametushitaki lakini pia ni kweli kwamba tuna tatizo la UMEME sasa? na Je, ni dharura? Tumejua lini tatizo? Nani awajibike kwa hili? Je, Sheria inasemaje ikiwa mtu amedanganya wakati wa manunuzi? munaendelea kufanya naye biashara? Je, hakuna mitambo mengine hata kwa bei ya ziada kidogo? Tusiponunua Dowans watapeleka wapi mitambo yao? wakinunua wafanyabiashara wengine (hao hao) watamuuzia nani umeme ikiwa tutakuwa na mitambo mipya?
TUZINGATIE: Rostam anamiliki 35% ya Vodacom, Dk. Rashid alikuwa Mkurugenzi wa Vodacom, Ngeleja alikuwa mtumishi wa Vodacom.