CIIE ni jukwaa bora kwa nchi za Afrika zilizojiunga na BRI kuingia kwenye soko la China

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG111463250973.jpg


Kutoka mpunga chotara hadi nyasi za juncao, kutoka maeneo ya kielelezo ya kilimo hadi vijiji vya kielelezo vya kuondokana na umaskini... katika miaka ya hivi karibuni, China na Afrika zimeendelea kuimarisha ushirikiano wa kilimo kutokana na msukumo wa mifumo mbalimbali kama vile Pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja (BRI) na Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika FOCAC.

Kilimo ni nguzo ya uchumi wa nchi nyingi za Afrika, na mauzo ya nje ya mazao ya kilimo yamekuwa chanzo kikuu cha mapato ya fedha za kigeni kwa nchi za Afrika. Katika Maonyesho ya 6 ya Kimataifa ya Uagizaji Bidhaa ya China (CIIE) yanayofanyika mjini Shanghai, matunda na mazao ya kilimo ya Afrika yamependwa sana na watu. Nchi nyingi zaidi za Afrika zilizojiunga na BRI zinatumia Maonyesho hayo kama jukwaa bora la kuingia na kunufaika na soko kubwa la China.

Kama mshiriki muhimu na mnufaika mkubwa wa BRI, mwaka 2018 Kenya ilileta parachichi zilizogandishwa kwenye awamu ya kwanza ya Maonyesho CIIE, ili kujitayarisha kuingia katika soko la China. Mwaka jana parachichi mbichi za Kenya ziliingia rasmi nchini China kupitia "njia ya kijani" kwa bidhaa za kilimo za Afrika, na baada ya kuonyeshwa tena kwenye CIIE, parachichi za Kenya zimepata umaarufu mkubwa katika soko la China. Hivi leo, asilimia 30 ya parachichi mbichi za Kenya zinasafirishwa China. Kwa mujibu wa makadirio ya idara ya kilimo ya Kenya, biashara hii itaongeza mapato ya wakulima wa Kenya kwa 30% hadi 50% kila mwaka.

"Safari ya CIIE" ya parachichi za Kenya ni mfano wa jinsi nchi za Afrika zinavyonufaika na soko la China. Hivi sasa bidhaa 16 za kilimo kutoka nchi 11 za Afrika zimepata fursa ya kusafirishwa China, nchi 21 za Afrika zinafurahia kutolipa ushuru kwa asilimia 98 ya bidhaa zinazosafirishwa kwenda China, na China imekuwa nchi ya pili kwa mauzo ya nje ya bidhaa za kilimo za Afrika. Mwezi wa Agosti mwaka huu, wakati wa mkutano wa 15 wa viongozi wa BRICS, Rais Xi Jinping wa China alipendekeza hatua tatu za kuunga mkono mfungamano na ujenzi wa kisasa wa Afrika, moja ikiwa ni “China kuchangia mpango wa kilimo cha kisasa wa Afrika”, jambo ambalo litakuwa tija muhimu ya kuinua hadhi na umuhimu wa nchi za Afrika katika mnyororo wa viwanda duniani.

Inachostahiki kutajwa ni kuwa katika miaka ya hivi karibuni, vitendo vya kujilinda kibiashara vya nchi za magharibi zikiongozwa na Marekani, vimedhoofisha mchakato wa utandawazi duniani. Hali hii imezifanya nchi za Afrika zenye uwezo mdogo wa kibiashara kimataifa hasa nchi zenye maendeleo duni zaidi barani Afrika, kupata taabu kuingia kwenye masoko ya kimataifa. Katika mazingira haya, China imeandaa maonyesho ya kwanza ya kitaifa duniani yanayoangazia kuagiza bidhaa kutoka nje yaani CIIE. Imezikaribisha nchi zenye maendeleo duni kushiriki katika maonyesho hayo tangu awamu ya kwanza, na kutoa sera mbalimbali za unafuu ili kusaidia bidhaa zao kuingia katika soko la China. Kitendo hicho ni tofauti na hali ya "kutowapenda maskini na kuwapenda matajiri" inayozoeleka katika soko la kimataifa, na kimeonyesha kikamilifu kanuni kuu za “uwazi, ushirikishwaji na manufaa ya pande zote” zinazotetewa na China katika kukuza ujenzi wa pamoja wa BRI.

Hali halisi ni kuwa si CIIE tu, bali pia majukwaa kama vile Maonesho ya Uchumi na Biashara ya China na Afrika na Tamasha la Bidhaa Bora la Afrika yaliyofanyika miaka ya hivi karibuni ni madirisha ambayo China inaandaa kama fursa kwa bidhaa za Afrika kujitangaza. Wachina husema "kwa sababu niliwahi kunyeshewa na mvua, hivyo niko tayari kushikilia mwavuli kwa wengine." China imeendelea kutoka nchi maskini ya kilimo hadi nchi ya pili kiuchumi duniani, na inafahamu zaidi umuhimu wa uchumi wa dunia ulio wazi kwa maendeleo ya nchi. Inaaminika kuwa kadiri soko la China linavyoendelea kufunguliwa nje kwa kiwango cha juu, bidhaa zaidi za nchi za Afrika zinazojenga BRI kwa pamoja zitaingia kwenye soko la China kupitia majukwaa haya, na kupata umaarufu mkubwa miongoni mwa watu wa China.
 
Back
Top Bottom