Ofisi ya Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika, imetangaza kufuta rasmi uamuzi wa kumsimamisha kazi Katibu wa chama hicho Mkoa wa Morogoro, Barnabas Okola, na kuagiza arejee kwenye majukumu yake mara moja.
Uamuzi huo umetolewa kupitia barua rasmi iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Sheria na Haki za Binadamu wa CHADEMA, Gaston Shundo, kwa niaba ya Katibu Mkuu, baada ya kupitia rufaa iliyowasilishwa na Okola kupinga hatua iliyochukuliwa dhidi yake na uongozi wa CHADEMA Kanda ya Kati.
Kwa mujibu wa barua hiyo, Ofisi ya Katibu Mkuu ilipokea barua ya rufaa ya Okola ya Julai 15, 2026, na kumpa nafasi mlalamikiwa—ambaye ni Katibu wa Kanda ya Kati—kuwasilisha maelezo yake ya kujitetee, ambapo aliwasilisha maelezo hayo Julai 19, 2026.
Baada ya kupitia maelezo ya pande zote mbili, Ofisi ya Katibu Mkuu ilijiridhisha kuwa Okola hakupewa haki ya msingi ya kusikilizwa kabla ya kuchukuliwa kwa hatua ya kusimamishwa uongozi, jambo linalokiuka misingi ya haki.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa uamuzi wa Kanda ya Kati wa tarehe 9 Julai, 2026 umefutwa rasmi, na kueleza kuwa kama Kanda bado ina malalamiko dhidi ya Okola, inapaswa kufuata utaratibu wa kikatiba unaoelekezwa katika kanuni ya 6.5.5 ikisomwa pamoja na kanuni ya 6.5.6 za Chama hicho.
Itakumbukwa kuwa Julai 9, 2026, Katibu wa CHADEMA Kanda ya Kati, Ashura Mashaka Masoud, alimsimamisha kazi Okola kwa tuhuma za kukiuka kanuni za maadili ya viongozi baada ya kuitisha mkutano na waandishi wa habari na kutoa shutuma za ubadhirifu wa fedha dhidi ya Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho (Bara), John Heche.
#SasaLive #CHADEMA #JohnMnyika #BarnabasOkola #SiasaTanzania