Ile ndege "mpya" iliyokodiwa na ATC kutoka kampuni ya Wallis Trading ya Liberia aina ya Airbus 320 bado haijaanza safari zake, na kwa karibu miezi saba sasa imeishaligharibu shirika hilo zaidi ya shilingi Bilioni 2 za malipo ya kukodi na matengenezo mbalimbali ya kuifanya ndege hiyo ipendeze.
Habari za kuaminika toka ndani ya shirika hilo kongwe la ndege nchini zinasema kuwa hadi hivi sasa ndege hiyo ambayo ilipokewa kwa mbwembwe wiki chache zilizopita bado haijaanza safari zake na hata itakapoanza itaanza kwa deni kubwa ambalo itachukua muda mrefu sana kuweza kuona faida. Kwa mwezi huu tu unaoisha shirika hilo litalipa karibu shilingi milioni 700 kama malipo mbalimbali yanayohusiana na ndege hiyo.
Baadhi ya wajumbe wa bodi ya wakurugenzi ya ATCL wameanza kuonesha wasiwasi endapo habari za jinsi ndege hii inavyoshughulikiwa zitajulikana na vyombo vya habari. Hata hivyo hofu hizo zimechelewa kwani hadi hivi sasa inajulikana wazi kuwa mkataba mzima na jinsi ndege hii ilivyopatikana, kuingizwa na kusimamiwa na uongozi wa juu wa ATCL ni aibu kubwa kwa taifa.
Licha ya mkataba huo wa Wallis ambao unakodisha ndege hiyo kwa karibu dola milioni 30, shirika la ATCL liliingia mikataba mingine na kampuni ya Aeroman ya El Salvador ambayo ilipewa jukumu la kuitengeneza ndege hiyo ambayo ilikuwa na mapungufu mengi ambayo unaweza kuyaona kwenye eneo la "Pics and Documents" hapo juu. Mkataba huo ambao na wenyewe si chini ya shilingi milioni 400 nao unaliongezea deni shirika hilo.
Pamoja na kampuni ya Aeroman, ATCL imeingia mkataba mwingine na shirika la ndege la Mauritius ili kuwapatia mafunzo na mafundi wa kuisimamia ndege hiyo. Kinachoshangaza watu wengi ambao wamekuwa wakifuatilia suala hili ni jinsi gani shirika ambalo halina wataalamu na marubani wenye uzoefu wa kurusha ndege aina ya Airbus ambayo ni mojawapo ya ndege za kisasa na zinazotumika zaidi duniani hasa kutokana na kutumia kiasi kidogo cha mafuta kulinganisha na Boeing iliweza kuingia mkataba wa kuipata ndege hiyo bila kuandaa raslimali watu.
Habari mpya zinasema kuwa baada ya taarifa za ndege hii kucheleweshwa kuruka kutoka mapema leo kuna dalili kuwa safari za ndege hiyo zinaweza kuanza saa yoyote kuanzia sasa na si mwezi mmoja baadaye kama ilivyokuwa inatarajiwa.
KLH News inatoa wito wa serikali kufuatia ukodishaji wa ndege hiyo na kuangalia mapungufu yote yaliyotokea kabla (Mungu aepushie mbali) jambo baya halijatokea na ndipo watu wajifanye wanajali na wanataka kufuatilia.
Kabla ya kukodishwa na ATCL ndege hiyo ilikuwa inamilikiwa na shirika la ndege la Jamaica ambao walipoiachia ilikuwa na kila aina ya ubovu wa ndani ambao haulingani na umri wake. Hata hivyo haijulikani ni kwanini ilipoingia nchini ndege hiyo ilisemwa kuwa imekodishwa toka kampuni ya Wallis Trading ya Ufaransa wakati mkataba uliosainiwa ambao KLH imeuona unaonesha wazi kuwa kampuni hiyo ni ya Liberia (hata kama kampuni yake mama ni ya Ufaransa).