Date::11/25/2008
Pinda: Punde mtasikia ya Hoseah, Mwanyika
Na Yahya Charahani
Mwananchi
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, amesema kuwa hatima ya Mwanasheria Mkuu, Johnson Mwanyika na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Edward Hosea, itawekwa hadharani muda mfupi ujao baada ya vigogo hao kutajwa kwenye kashfa ya utoaji zabuni ya ufuaji wa umeme wa dharura kwa Kampuni ya Richmond.
Mbali na hatima ya vigogo hao kuwekwa bayana muda mfupi ujao, kashfa zingine mpya zilizo ndani ya sakata la Richmond zimegundulika na zitawekwa hadharani katika muda huo, Waziri Pinda aliwaambia wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari jana.
Kauli ya Pinda imekuja wiki moja baada ya Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo, kukana kuwa anashughulikia suala la vigogo hao waliotajwa kwenye ripoti ya Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza kashfa hiyo ya Richmond.
Akizungumza na wahariri jana ofisini kwake, Waziri Mkuu Pinda alisema yeye na timu yake wanakamilisha taratibu na kila kitu kitawekwa hadharani.
"Mimi ndiye msimamizi wa kile kikosi cha kazi kilichopewa jukumu na Bunge kushughulikia utekelezaji wa hili suala... napenda nilizungumzie wazi kuwa litafahamika ndani ya muda si mrefu," alisema Waziri Pinda.
"Nafahamu Watanzania wanayo shauku kubwa kujua nini kimejiri na kama wakuu hao walihusika au hawakuhusika, ndiyo maana kila kukicha serikali iko makini kushughulikia suala hilo na mengineyo yanayoleta utata.
"Jambo hili litamalizika ndani ya muda si mrefu. Mtapata matokeo, limechukua muda mrefu kwa kuwa suala lenyewe linahusu utumishi wa umma na hivyo halina budi kufuata taratibu.. na siyo wao peke yao, yapo mambo mengi ndani ya hili dudu linaloitwa Richmond mtayafahamu."
Alisema kuna mambo mengi sana wameyagundua ndani kashfa ya Richmond ambayo nayo yatawekwa wazi na hakuna kitu kitakachofichwa na hatua mwafaka zitachukuliwa.
Taarifa ya Kamati ya Bunge kuhusu kashfa ya Richmond ilisababisha Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa kujiuzulu na baadaye kufuatiwa na vigogo wengine.
Katika maazimio yake, Bunge lilitaka mwanasheria mkuu wa serikali na Wakili wa Serikali, Donald Chidowu, wawajibishwe na mamlaka ya juu ya nchi kwa "kuchangia kuiingiza nchi katika mkataba wa aibu."
Pia katika azimio jingine namba 9, Bunge liliazimia kuwa "mkurugenzi wa Takukuru awajibishwe kwa manufaa ya umma na maofisa wa Takukuru walioshiriki katika zoezi la uchunguzi na kuandaa taarifa ya Richmond Development Company LLC, iliyoficha ukweli, nao pia wawajibishwe kwa manufaa ya umma."
Katika utekelezaji wake, Waziri Pinda aliliambia Bunge kuwa, Hoseah ametakiwa ajieleze na mamlaka yake ya nidhamu, ambaye ni katibu mkuu kiongozi; na kwamba wasaidizi wake wametakiwa kutoa maelezo yao kwake.
Kuhusu Mwanyika, Waziri Pinda aliliambia Bunge kuwa kutokana na nafasi yake kikatiba, "mamlaka yake ya nidhamu ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, Mwanasheria Mkuu ambaye alikuwa miongoni mwa watendaji wakuu watatu waliokuwa wanaishauri serikali, suala lake la kuhusishwa katika mchakato mzima wa mkataba huo linashughulikiwa na ofisi ya rais, Ikulu."
Waziri Pinda alizungumzia mambo mengi katika kikao hicho na wahariri, likiwemo suala la magari ya kifahari.
"Hili suala la kusema yanayotumika ni ya kifahari... eti ya gharama kubwa, mimi napingana nalo kidogo nikizingatia kazi zinazofanywa na wahusika," alisema Pinda ambaye ametangaza kusimamisha semina na warsha zote isipokuwa zile tu zitakazopata kibali kutoka ofisi yake.
"Hivi jamani, mtumishi wa umma na hasa hawa wa ngazi za juu si wanatakiwa wafanye kazi za wananchi? Hii inahitaji comfort kidogo kwa hiyo kwangu gharama ya gari siyo suala, bali suala ni namna magari hayo yanavyotumika.
"Natambua magari hayo yanatumia gharama kubwa, lakini ni kwa manufaa ya umma, hata hivyo, hatua kadhaa zinachukuliwa sasa ili kupunguza matumizi mabaya ya magari hayo.
"Hebu jamani fikirieni eti inaitishwa semina halafu inafanyika Arusha sasa ile fleet ya magari yanayokwenda huko utasikitika ni fedha nyingi sana za walipakodi zinatumika ndiyo maana nimeamua kuzisimamisha semina kwa muda."
Alisema serikali yake haijaelemewa hata kidogo na kwamba inachokifanya sasa ni kurekebisha mifumo ili masuala yaende sawasawa na serikali iweze kutumikia wananchi.
Pinda aliyekuwa akizungumza akiwa mtulivu alishangazwa na namna watendaji katika serikali yake wanavyofanya kazi katika sekta mbalimbali na akasema uongozi mbovu wa baadhi yao ndiyo unaosababisha matatizo ya sasa.