Askari wa Tanzania wengi - ingawa sio wote- hawana adabu, wanapenda kutumia uaskari wao kuonea watu.
Hizi habari zinanikumbusha mbali sana.
Kuna siku tulikuwa tumekaa maskani Upanga, muda wa jioni vijana wanakutana maskani. Mara paap, tukawa tumeaona askari kibao wanakuja kutoka mbali, wako doria kundi zaidi ya ishirini, wamebeba bunduki na marungu.
Basi nikawaambia madogo tuliokuwa tumekaa nao maskani, kama hamjiamini, ondokeni kabisa, wale wanakuja kutaka kututingisha hapa.
Basi kuna madogo wakaondoka, wengine tuliojiamini tukabaki.
Wakaja wakafika maskani, sisi kama kumi, wao zaidi ya ishirini. Mmoja akatuuliza "Haroo, mnafanya nini hapa?".
Basi hawakujua wanaongea na watu wa aina gani, jamaa mmoja wa maskani akamjibu "Afande hivyo ndivyo ulivyofundishwa kusalimia watu?". Ikabidi yule askari astuke kwanza. Alitegemea watu wataogopa, hakutegemea kujibiwa vile.
Sasa akaja askari mmoja, nafikiri ndiye alikuwa mkubwa wao yule, akaanza kuuliza watu, mmoja mmoja, "Wewe unakaa wapi?" Mtu anamwambia hapo, "Wewe unakaa wapi?" Mtu anamwambia hapo. Wakamfikia jamaa mmoja.Wakamuuliza "Wewe unakaa wapi?" Akajibu kwa Baba Ben.
Askari akauliza, "Kwa Baba Ben? Baba Ben gani?" Jamaa akajibu "Kwa Ben huyo huyo wa Jamhuri ya Muungano, kwani wewe unamjua Ben gani mwingine Tanzania?" (Hapo kipindi cha urais wa Ben Mkapa).
Yule Polisi akawa kastuka, kama hajaamini hivi, sasa kumbe kuna wenzake huwa walikuwa wanaenda kulinda kwa Mkapa, wakawa wamemjua yule kijana wa kwa Mkapa. Ikawa kama wanamwambia yule mkubwa wao kwamba huyu tunamjua anakaa kwa Mkapa, tunamuona tukienda kulinda pale.
Basi hapo hapo nikaona wale polisi wanabadilika mara moja, wanasema unajua wazee ni suala la kufahamiana tu, tulikuwa tunajuana tu, hamna tatizo, hamna tatizo tulikuwa tunatambuana tu.
Kuanzia siku hiyo mpaka kituoni kwao kile kijiwe walikiwekea alama ya X kisiguswe, wakasema hapa kuna watoto wa Mkapa huwa wanakaa.
Nikasema hapa ingekuwa wamewakuta watu wasio na majina wangewasumbua sana.