666-nyayo za kuzimü

666-nyayo za kuzimü

666-NYAYO ZA KUZIMU--28-

Lile jitu baada ya kuwafunga vitanzi wakina Mrisho alianza kuwaburuza kama nyama!! Halikujali kitu chochote juu yao na wala sura yake haikuonyesha hata chembe ya kulifikiria hilo.Walipowadia kwenye mti mmoja wa mkuyu,waliwatundika wale watu,wakaungana na shingo zingine zilizoonja kamba nyekundu, utofauti wao na wale waliotangulia ni kwamba wao walinyongwa bila mioyo yao iliyochukuliwa na yule mdada mithili ya Paka aliekua na mahitaji nayo,walibaki na mashimo tu yaliyokua yanamimina damu!!!
Ile Mioyo iliingizwa kinywani mwa yule dada na moja kwa moja ilianza kutafunwa mithili ya keki huku lile jibaba likishuhudia,baada ya kumaliza lile tendo ghafla walibadilika na kuchukua sura za waliowauwa!! Lile jibaba liligeuka na kua Tabwe huku yule mdada akiichukua sura ya Mrisho!! Taratibu huku wakiwa wameshikilia mifuko isiyojulikana ilitokea wapi walianza safari ya kuelekea kule wanakijiji walipo!! Hapakukalika tena!! Hatari ilizidi kuchukua nafasi!!
* * * * * * *
Baada ya muda mrefu kupita bila ujio wa wakina Mrisho mzee Patili na wanakijiji wengine walianza kupata hofu,akili zao zilianza kuruhusu mawazo mabaya kupenya na mioyo yao ilianza kupokea taarifa za simanzi,wanakijiji waliokua hawajapakwa dawa walikua na hofu mara mbili kwani wao walijiona si salama ulikilinganisha na wenzao,walitamani wakina Mrisho waje haraka ili nao miili ipate kunawiriwa na dawa ambayo waliiamini kwa asilimia zote itakua kinga madhubuti kwao dhidi ya hali endelevu,walisali mioyoni,waliomba sana mungu wao apate kutanakabali sala zao.
Muda si muda Mrisho na Tabwe feki waliingia,wanakijiji waliokwisha kata tamaa walilipuka kwa furaha na kuwalaki kwa upendo ulioonyesha matumani,masikini ya mungu hawakufahamu kwamba wale siyo,mzee Patili aliupokea mfuko aliopewa na haraka akawaambia wale waliokua bado hawajapakwa wajipange mstari,wakapanga,akaanza kuwapakaa kama ilivyokua mwanzoni ila sasa hivi alihusika kwenye kuwapaka wote yani wanaume na wanawake wakiwa wamepanga mstari mmoja tu,kutoka na dawa waliyopakwa wanakijiji wengine Tabwe na Mrisho walishindwa kustahimili,walisogea pembeni mbali na wanakijiji wengine,kujitenga kwao kulimpa kidogo maswali mwalimu Baraka alieamua kuwafuata kwa lengo la kuwapongeza kwa ujasiri wao,alipowakaribia aliwapa mkono wa kheri uliopokelewa na Mrisho ambaye ni yule mdada mwenye roho ya paka,kha!! Alishtuka mno mwalimu Baraka!! Mkono wa Mrisho ulikua wa baridi mno mithili ya barafu,hali hiyo ilimpelekea autoe mkono wake haraka na kuuliza...
"we Mrisho mbona mkono wako wa baridi hivi???"
"kawaida tu,si unajua tulikua tunakimbia ili tuwahi!!"
alijibu Mrisho,mwalimu Baraka hakuridhika na lile jibu hivyo akauliza tena
"sasa kama mlikua mnakimbia mbona mlichelewa??"
swali hilo lilifanya kidogo Mrisho akwame,alimuangalia mwenzie Tabwe aliewahi akajibu,
"tatizo kule kwa yule mzee ndo' kulituchelewesha,madawa yaliku mengi mno!!"
"ah-ahaa! Ila poa haina tatizo,hongereni bwana kwa ujasiri wenu mliouonyesha! Bella alikua ana wasiwasi kweli..teh! Teh!"
mwalimu Baraka alimtania Tabwe kuhusu mchumba wake Bella,cha ajabu uso wa Tabwe ulimdhihirishia mwalimu Baraka ya kua halikua hajui kiongeleachwo,
"Bella?? Ndio nani??"
aliuliza Tabwe swali lililozidi kumshangaza mwalimu Baraka!!
Moyo wa mwalimu ulisita,alipata hofu,hakutaka kukaa tena pale,taratibu aliaga na akajiondoa lile huku maswali kichwani yakizidi kupapaliwa na kuchipukia.
Lile jibaba lilimuangalia mwenzie alie ndani ya sura ya Mrisho kisha akamuuliza..
"unadhani atakua amegundua chochote??"
"sidhani,ila kama ukiniuliza ni moyo wa nani ninaoutaka kwa sasa,dhahiri nitakujibu ni wake!"
"ile dawa waliyopakwa nayo itaanza kufanya kazi muda gani? Mbona kama inachelewa??"
"tuliza munkari,ipe kama nusu saa,utaona majibu yake nadhani unafahamu huwa sibahatishi"
alijigamba bimdada,
"nafahamu hilo,ila ile dawa waliyoipakaa ni kali mno! Nadhani uliona jinsi tulivyokua tunapata shida alipokuwepo yule mbaba"
"ni kweli,ila siwezi kuondoka mpaka nione ikifanya kazi!"
"sawa."
maongezi yakakomea hapo.
Hayawi hayawi yakawa!! Dawa waliopakwa watu wa awamu ya pili ilianza kufanya kazi bara-bara!! Miili yao ilianza kuwasha hatari!! Na kila walipojikuna ngozi ilitoka na kuruhusu damu iruke kama bomba!! Makelele ya kuomba msaada yaliteka ile sehemu!! Muwasho wa ajabu usiovumilika uliwafanya wawe machizi kwa kuranda huku na kule wakipiga makelele kwa nguvu!!!! Mzee Patili alishikwa na butwaa!! Wanakijiji walitawaliwa na taharuki!! Walipotizama wakina Mrisho wako wapi,HAWAKUWAONA!! Mungu wangu!! Wale waliokua wanawashwa wakaanza kukauka na kuwa magofu meupe kama chumvi!!


JE NINI KITAENDELEA? USIKOSE SEHEMU YA 29 IJAYO
 
Unarusha story vpande zake fup sana ama uko mbele inaboa,wasiwasi ntachana nayo saa sita natakiwa niwe nimelala asee,acha uswahili
 
666-NYAYO ZA KUZIMU--29

Wale waliokua wanawashwa wakaanza kukauka na kua magofu meupe kama chumvi!!!

Kilio kilichobeba uchungu na uoga kilipata kutoka vizuri toka kwenye midomo ya wakina mama na watoto,vilevile mioyo ya wakinababa ilikita kwa nguvu na macho yao yalitoka kwa kutoamini,ulikua ni kama mchezo wa kuigiza,sehemu ile yote ilitawaliwa na magofu
ishirini na mawili yote yakitokana na ile dawa ya awamu ya pili! Wanakijiji walipungua kwa kiasi kikubwa,watoto wengi walipoteza wazazi,wanawake wengi walipoteza waume zao,na hata vile watu wengi walipoteza watu wao wa karibu,simanzi iliyoje!!!
Mzee Patili alichanganyikiwa kabisa,hakujua cha kufanya japokua mzee Otongo alikua anajitahidi mno kumtuliza,alijiona yeye ndie muuaji na hata baadhi ya wanakijiji walianza kufikiria hivyo,walifikiria ya kwamba vile vifo ni dhahiri vimesababishwa na mzee Patili ilihali wengi wao bado walikua kwenye tahamaki ya njia panda hasa baada ya wale walioleta dawa kupotea kiajabu machoni mwao!!
Mama Kadogo aliutumia ule mwanya kuita rai na kuteka hamsha za wanakijiji,kwa kujiamini alisimama mbele yao na kusema
"Jamani..jamani!! Naomba tusikilizane! (ukimya ukatawala lakini bado vikwikwi na vimafua vya vilio vilikua vinachukua nafasi)....katika vita hii tunayopambana nayo kufa kwa mtu au watu isiwe kitu cha kutushangaza,mtu yeyote kwa muda wowote anaweza akafa kwenye mapambano haya hilo inabidi liwe kichwani,naomba tusiruhusu roho za simanzi ziweke kiza kwenye njia yetu bali roho ya ushupavu na ya kusonga mbele,ni hakika tumezidiwa akili na hili jeshi la 666 katika huu mchezo,waliutumia ipasavyo ule mwanya tuliowapa wa kuwatuma wale vijana,nadhani hilo halina maswali...tumeona kwa macho yetu walivyopotea kiajabu na kuudhihirishia uma ya kwamba wao sio wale tuliowategemea!"
haraka Mwalimu Baraka alidakia
"hakika mama,hakika!! Wale hawakua wakina Mrisho kama tulivyodhani,mie mwenyewe naweza nikasema hivyo kwa ushahidi wangu mdogo nilioushuhudia,walikua ni watu wa baridi mno! Na hata baadhi ya maswali niliyowauliza walishindwa kabisa kujibu,kusema ukweli nilipata hofu lakini sikuwa na uhakika asilimia mia hivyo nikaamua nijitoe lile eneo kimyakimya!"
maneno hayo ya mwalimu Baraka yaliamsha minong'ono miongoni mwa watu,mama Kadogo aliwatuliza na kisha akaendelea kunena..
"ni matumaini yangu dawa tulizopaka zina msaada kwetu,bado ninaamini hivyo japokua hili tukio la wakina Mrisho linaweza kuwatia mashaka mioyoni,hapo ndipo tunapoweza kurudia kauli yangu ya mwanzoni ya kwamba walituzidi akili,nahisi kuna kitu walichokifanya hawa jeshi ambacho bado hatujakifumbua...."
(kabla hajamalizia mzee Rama kwa jazba alidakia)
"sasa tufanye nini?? Hamuoni ya kwamba tunaendelea tu kufa!! Au nyie bado hamjatosheka???"
kauli ya mzee Rama ilizua tena minong'ono na malumbano,baadhi ya wanakijiji walionekana kumuunga mkono na baadhi yao walionekana kumpinga,makundi mawili yakazaliwa miongoni mwao!! Ni dhahiri imani zao haba zilianza kuwachonyota,mzee Patili taratibu alisimama na kuelekea pale alipo mama Kadogo kisha akawaomba utulivu kwa muda ili apate kunena,wale waliokua bado na imani nae walifunga midomo yao na kumpa masikio lakini wale ambao imani zao zilitiwa doa hawakujali hilo,waliendelea kururuma tu,mzee Patili akatoa tamko..
"kama imani yako haiko nami tena,sitofanya jitihada zozote kuiinua maana umeamua hivyo,kama nilikua nanyi tokea ujana nikiwahudumia na bado imani zenu zina madoa kuhusu mimi,hakuna chochote ninachoweza fanya kwenu kwa sasa.Ninaelekea upande wa kulia nilipotokea,kama bado una imani nami waweza nifuata,kama huna imani nami waweza kubaki.."
sura ya mzee Patili ilionekana si yenye furaha,alikua anawaza jambo na dhahiri alionekana ameumia,alishika njia ya kuelekea nyumbani kwake na kundi la watu huku nyuma lilimfuata akiwemo Julina mwenye mtoto aliebeba matumaini yao,bila hata kuonyesha aibu usoni mzee Rama nae na wenzake walioonyesha kutia shaka juu ya mzee Patili nao walikuwemo ndani ya msafara wakiivuta miguu yao kumfuata,hawakufanya hivyo kwa kupenda bali iliwabidi kwani mtoto ambaye ndie ngao ya matumaini alikua upande ule hivyo hawakua na jinsi,mzee Rama bado alikua na gubu jeusi lililokua linamkereketa,hakupendezewa kabisa na ile hali ya uongozi wa mzee patili,wivu ulimkua unamsumbua kwa kiasi kikubwa,alitaka yeye ndie awe anasikilizwa na yeye ndie awe anatoa amri,wivu ulimshika mishipa yake ya damu,akili yake ilimtuma amuibe yule mtoto wa Julina,alifahamu fika ya kua akimmiliki yule mtoto jamii nzima itamsikiliza yeye kwani ndie atakaekua ameshikilia matumaini yote ya wanakijiji,atafanyaje sasa?? Alijiuliza kichwani mwake,baada ya kupata jibu haraka alimvuta mwenzie pembeni na kumwambia..
"unataka kufa na wewe,ama??"
swali hilo lilimshangaza alieulizwa,kiuoga nae akajibu..
"hapana!!"
"sasa nisikilize nitakayokuambia..."
JE ANATAKA KUMUAMBIA NINI?
UADUI WA MZEE RAMA MWISHO WAKE NI NINI??


USIKOSE SEHEMU 30 IJAYO
 
Ama kweli hasidi hana sababu na sikio la kufa halina dawa. MziziMkavu asante sana.
 
Last edited by a moderator:
Mzizi hayuko kama Mentor............... tehe tehe!! Mentor mpaka keshooooooooo!!
 
666-NYAYO ZA KUZIMU--30-

"unataka kufa na wewe ama??"
swali hilo lilimshangaza alieulizwa,kiuoga nae akajibu
"hapana!"
"sasa nisikilize nitakayokuambia.."
"enhe.."
"najua wewe ni mwenzangu na ninakuamini hautoniangusha,hivi we unadhani haya yote yanayojiri ni sababu ya nani??"
"mh...kusema ukweli mie sijui!"
"we unahisi ni nani??"
"mmmh....labda ni hawa wageni au...."
"ah-ah! Hawa wageni waliruhusiwa na nani??"
".......mzee Patili!"
"unavyodhani ni nani sasa hivi anatuua??"
"si lile jeshi la 666 walilotuambia!!"
"..kwani wale ndio waliowapakaa nyie dawa??"
"hapana! Ni mzee Patili!"

"majibu yote yapo wazi kama unavyoona,huyu mzee ndio kikwazo kwetu,na hivi ninavyokuambia ni kwamba lengo lake si kukabili jeshi la 666 kama anavyotudanganya bali anataka amtumie yule mtoto kwa malengo yake binafsi,yani kujinyanyua na kufanikisha hamu yake ya uongozi!! Hivyo basi ili atudhoofishe na asafishe njia yake anatupunguza idadi kama unavyoona...!!"


haikuishia hapo tu,kukaa kwake nyuma ya ule msafara alikutumia kama ngazi ya kuigeuza mioyo ya wanakijiji,alipenyeza uongo kwa walio karibu na kufanikiwa kuiteka mioyo yao yenye imani haba,na alitamani zaidi.


Baada ya muda msafara wa wanakijiji uliwasili kwa mzee Patili,walishangazwa na hali waliyoikuta ikiwemo mzee Patili mwenyewe,mlango haukuwepo sehemu yake na mwanga wa mwezi uliokuwepo uliruhusu kuonekana unga fulani wa manjano chini mzee Patili aliougundua kwamba ni dawa ile aliyoiagiza,alama za miburuzo zilizokuwepo chini ziliwatia mashaka hivyo

wakasogeza koroboi na kuanza kuzifuatilia mpaka pale zilipowafikisha kwenye miili ya wakina Mrisho iliyokua imetundikwa!

Macho yaliwatoka kwa kushuhudia zile maiti zilizokua zinaning'inia na mashimo vifuani,machozi na simanzi havikuzuilika kuwa miongoni mwao,miili ile ilishushwa na kumpa ruhusa mzee Patili kuikagua kisha akatoa neno..
"watu waliotumwa ni wazi walivamiwa! Nadhani mazingira husika yanaeleza hivyo,dawa niliyoiagiza tumekuta imemwagika,mlango umevunjwa,vilevile wamenyongwa! Hiki ni kielelezo tosha ya kua dawa iliyoletwa kule haikua sahihi.."
alivuta pumzi kidogo kisha akaendelea

"miili ya wakina Mrisho japokua imenyongwa kama ile mingine lakini kuna utofauti juu yao,utofauti huu unatudhihirishia ya kwamba kuna kiumbe kingine ambacho ni hatari kwetu kimeongezeka,na ndio hasa kinachohusika na hii mioyo iliyobebwa! Inatubidi tuongeze kinga yetu!"


mzee Patili akanyamaza kidogo,ila taratibu mzee Otongo alimkaribia na kuanza kumnong'oneza kitu hali iliyohamsha vimaongezi vya chinichini hasa kutoka kwa mzee Rama aliekua anapigilia misumari maelezo yake ya uongo aliyoyaingiza ndani ya vichwa vya watu huku akihakikisha mzee Patili hagundui hilo.


Baada ya mzee Patili na Otongo kujadili waligundua cha kufanya japokua ilikua vigumu kuwaeleza watu,kazi ngumu ilibidi ifanyike na pia ilihitaji watu jasiri watakaojitolea kuifanikisha,baada ya kujiulizauliza sana mzee Patili aliamua apasue jipu,

"tunahitaji dawa kwa ajili ya kuongeza kinga yetu madhubuti,kama nilivyowaambia hapo kabla ya kwamba ni lazima kinga yetu iendane na mazingira husika,sijamaanisha ya kuwa tuliyonayo haifai,hapana,ila inabidi tuiongeze nguvu..."
alishindwa kuendelea,mzee Otongo ikabidi aendeleze alipoishia..
"tunahitaji Mdigidigi!!"
"Mdigidigi!!!"
wanakijiji walihamaki,

"ndio Mdigidigi!!...na kama tunavyojua haipatikani hapa karibu......."

"ndio! Ni mpaka mtoni!!"
"haswaa!..Mpaka mtoni!...inabidi tuwe na ule mti ili tuweze tengeneza dawa,tatizo ni kwamba tutaipataje?"
Otongo aliuliza,
mama Kurwa akatoa maoni yake
"inabidi watu wafuate kama ni hivyo!!"

kauli hiyo ilizua mjadala mzito,hakuna mtu alieonekana yu tayari kufanya hicho kitu kwani waliona ni kama kujiingiza kwenye mdomo wa kifo wenyewe,kila mtu alitaka kuilinda roho yake.


Katika hali ya kushangaza mzee Patili alinyamazisha watu na kuwataarifu ya kwamba ataenda yeye mwenyewe,taarifa hiyo badala ya kunyamazisha mjadala iliuzua zaidi,uamuzi wa mzee Patili kwenda kutafuta ule mti ilipokelewa na mawazo tofauti,asilimia nyingi ya watu walionekana kutoafikiana nalo huku wengine wakiliunga mkono....wakati taharuki bado ikichukua nafasi sauti ya mzee Rama tokea nyuma kabisa ilipata kusikika ikisema..

"mimi nitaenda huko mtoni!...mimi nimejitolea kwenda!! Nitumeni!"

hakuna mtu alietegemea kuisikia hiyo kauli tena toka kwenye kinywa cha mzee Rama,miguno na maswali ya chinichini ilizuka lakini hivyo vyote havikubadilisha uamuzi wake,alijisogeza mbele kabisa ya umati huku akimtizama mzee Patili,kisha akarudia kauli yake..

"nitume mimi!!"
Je KiPI KIMO KICHWANI MWA MZEE RAMA? Kwanini anataka kazi wengne wanayoiogopa?


USIKOSE SEHEMU YA 31 IJAYO!
 
Aaah!! jamani mbona imekatikia patamu natamani nimuone Mzee rama mpaka mwisho maana ni muoga kama CCM!! tehe teh!! Ndugu Mzizi Mkavu!! twasubiri kwa hamu!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom