Nimeulizwa kuhusu kujuzu au kutokujuzu kwa Mwislamu kuuza chakula mkahawani (kwenye magenge) mchana wa mwezi wa Ramadhani, NANUKUU:-
“assalaam alaykum mm nauliza jee ina faa muislamu kuuza chakula mwezi waramadhani mchana hali ndo biashara yake hana nyengine”
JIBU
BISMILLAH
Haijuzu. Haram!
Sharia za Mwenyezi Mungu, khasa Sharia-mama ألأصول -si matawi الفروع- zinawahusu vile vile wasiokuwa Waislamu, isipokuwa wanatakiwa KWANZA wasilimu kisha watii sharia. Sharia-mama ni kama Tawhidi, Swaumu na Swala, hizi ni Sharia za msingi, nguzo za kufuatwa na wanaadamu wote, isipokuwa wanatakiwa wasilimu kwanza: wawe Waislamu kwanza.
Watu wa Peponi watawauliza makafiri, watu wa Motoni:
{ مَا سَلَكَكُمْ فِي سَقَرَ {42} قَالُوا لَمْ نَكُ مِنَ الْمُصَلِّينَ {43} وَلَمْ نَكُ نُطْعِمُ الْمِسْكِينَ {44} وَكُنَّا نَخُوضُ مَعَ الْخَائِضِينَ {45} وَكُنَّا نُكَذِّبُ بِيَوْمِ الدِّينِ {46}
“Ni kipi kilichokutokomezni kwenye kina cha Moto? Waseme: Hatukuwa miongoni mwa wenye kuswali. Wala hatukuwa tunawapa chakula masikini. Na tulikuwa tukizama pamoja na walio zama katiika maovu. Na tulikuwa tukikana Siku ya Kiyaa.” Al-Muddathir: 42-46.
Hivyo, hata wanaokana kuwepo Siku ya Kiyama; makafiri, wanatakiwa wawe miongoni mwa wenye kuswali, na wataadhibishwa kwa kutokuswali. Vivyo hivyo, kwa kutokufunga na kadhalika. Hakuna khilafu miongoni mwa wanazuoni kuyusu wasiokuwa Waislamu kuwajibika mbele ya sharia-mama. Kuna khilafu ndogo, tu, kuhusu kuwajibika au kutowaajibika mbele ya matawi ya sharia, kama kutia nia ya kufunga, kutawadha kwa swala, ect., ect. Ama sharia-mama hakuna khilafu.
Hivyo, haijuzu kumuuzia chakula mwislamu au asiyekuwa mwislamu, mchana wa Ramadani. Haramu. Ni kumsaidia kuasi.
Kudai kwamba kuuza chakuka ndiyo kazi yake, na hana kazi nyengine, ni madai ya kitoto, na hakumaanishi kuwa atakufa njaa iwapo hakuuza chakula mchana, kwa muda wa michana 30.
Na hakuzuwiwa kuuza usiku, au kuanzia magharibi hadi kabla ya alfajiri. Kwanini iwe kutokuuza chakula kwa muda wa masaa kama 12, kwa michana kama 30, katika mwaka mzima, kuwe kutamfilisisha au kumfanya awe masikini au akose ajira? Je, alipoanzisha biashara hiyo alikuwa akiwauzia wasiokuwa Waislamu tu, hadi adai, hii leo, kwamba kama hajauza mchana atapata shida? Haijuzu, haramu!
Baadhi ya wanazuoni wanasema hata kama ana mfanyakazi wa nyumbani, ambaye si Mwislamu, na ambaye masharti ya kazi yake ni pamoja na kumpa chakula cha mchana, basi bado hapaswi kumpa chakula mchana, katika Ramadhani. Ampe chakula chake magharibi pale wanapokula wao, na ampe vile vile cha mchana, kabla ya kuchomoza alfajiri- wanapokula daku wao, ili kama anataka kujiwekea chakula chake hicho hadi mchana unaofuatia, basi huo ni utashi wake mwenyewe, ajifnyie mwenyewe. Hatokufa njaa kwa kutokula mchana. Mbona waajiri wao hawafi wala hawaumwi.
Kwa kweli, watu wengi, ambao si Waislamu na hawafugi, bado wanaheshimu mchana wa Ramadhani na hawali mbele ya ndugu zao Waislamu. Ni baadhi ya wanaojiita Waislamu tu, ndio wenye ukorofio huo wa kudai kuwa anawauzia wasiokuwa Waislamu, kwa sababu kuuza chakula ndiyo kazi yake, hana kazi nyengine!
Hivyo, midhali hana sababu halali ya kutokufunga, na akawa mtu mzima wa kuwajibika binafsi, basi hapaswi kupewa chakula mchana wa Ramadhani mpaka magharibi.
Kwa ufupi, haifai kwa Mwislamu kuuza chakula kilichokwisha pikwa kwa walaji wa mchana, tena kwenye mkahawa wake. Wanaingia humu wauza vyakula magengeni, vile vile.
Usisaidie watu kuvunja sharia za Mwenyezi Mungu. Waache wavunje wenyewe! وتعاونوا على البر والتقوى ولا تعاونوا على ألإثم والعدوان
Naam, wagonjwa, wazee, wasafiri na kadhalika wanaweza kupewa chakula mchana wa Ramadhani, maana hawana ulazima wa kufunga Ramadhani, kwa muda wa kuwa na venye kuwaruhusu kula.
والله أعلم
وبالله التوفيق
السيد عبد القادر شريف آل الشيخ أبى بكر بن سالم
Imejbiwa na Sayyid Abdulqadir Shareef
NI RUHUSA KUNUKUU, kama ilivyo, pasi na kubadilisha au kuongeza chchote, na kuweka kwenye FB yako au kwenye WhatsApp na kwenye Makundi ya Mitandao ya Kijamii za Kiislamu, kwa lengo la kusambaza na kuelimisha Dini. Changia kusambaza Dini, ujipatie thawabu.
kcwajawema@gmail.com