Wanawake wa China na Afrika watafuta njia za kushirikiana na kutekeleza majukumu makubwa zaidi katika jamii

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG111367032306.jpg


Maonesho makubwa ya tatu ya Uchumi na Biashara kati ya China na Afrika yalifungwa mwishoni mwa mwezi uliopita katika mji wa Changsha, mkoani Hunan, hapa nchini China. Mbali na maonesho ya bidhaa mbalimbali, makongamano kadhaa pia yalifanyika likiwemo ‘Kongamano la Wanawake la China na Afrika’ lililoandaliwa na Shirikisho la Wanawake la China kwa kushirikiana na serikali ya mkoa wa Hunan.

Kwenye Kongamano hilo Mke wa Rais wa China Bibi Peng Liyuan ambaye ni mjumbe maalumu wa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) anayeshughulikia kuhimiza elimu kwa wanawake na watoto wa kike, alihutubia kwa njia ya video.

Kongamano hilo linalenga kuangalia namna wanawake wa China na Afrika wanavyoweza kutafuta njia za kushirikiana na kutekeleza majukumu makubwa zaidi katika jamii. Kwa maana hiyo kujumuishwa kwa mara ya kwanza kwa Kongamano hilo katika maonesho haya, kunathibitisha ile kauli kwamba China na Afrika ni jumuiya yenye mustakabali wa pamoja, na wanawake ni watu muhimu wa familia ya China na Afrika.

Halikadhalika kufanyika kwa maonesho ya kwanza ya Ubunifu na Ujasiriamali wa Wanawake kati ya China na Afrika, pia kumetoa taswira ya mafanikio mapya ya wanawake wa pande zote mbili katika uchumi na biashara, utamaduni na elimu, kupunguza umaskini, kufanya shughuli za hisani, na maeneo mengine ya ushirikiano.

Kwenye hotuba yake, Mama Peng Liyuan alisema, China na Afrika zote zinatilia maanani kuhimiza maendeleo ya wanawake. Kuhusu juhudi zinazofanywa na China ili kuwawezesha wanawake, alibainisha kuwa China siku zote imekuwa ikijitahidi kukamilisha mfumo wa sheria unaolinda haki za wanawake, kuinua kiwango cha elimu cha wanawake, kuwaunga mkono kujihusisha na ujasiriamali na uvumbuzi, na kukamilisha huduma kwa wanawake na watoto, ili kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya maendeleo ya wanawake katika pande zote.

Kongamano hili likiwa na azma ya kutafuta usawa wa kijinsia na haki sawa kwa wanawake, mkusanyiko kama huu ni mfano wa namna Afrika na China zinavyoendelea kusaidiana kufikia malengo yao. Kwa mujibu wa Ripoti ya Pengo la Kijinsia Duniani ‘Global Gender Gap 2023’ iliyotolewa na Baraza la Uchumi Duniani, China imeshika nafasi ya kwanza kati ya nchi 146 katika kuwapatia wanafunzi elimu ya juu kwa kupata alama 1.00 ambazo zinaonesha kutokuwepo kwa pengo la kijinsia.

Sambamba na juhudi za China, nchi za Afrika pia nazo ziko mstari wa mbele katika kuboresha mazingira ya kazi na maisha ya wanawake, na pia zimejitahidi kuwaondoa wanawake hawa kwenye umaskini, kuwahamasisha kushiriki kwenye usimamizi wa nchi na jamii, na juhudi hizo zinaonekana kuzaa matunda.

Kongamano hili lililofanyika chini ya kaulimbiu "kuunganisha nguvu za wanawake wa China na Afrika, na kukuza kwa pamoja maendeleo ya kina", limehudhuriwa na wake wa marais kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika akiwemo mke wa rais wa Zanzibar, Mama Mariam Mwinyi, ambapo miongoni mwa mambo kadhaa waliyojadili ni pamoja na kueleza imani yao ya kuwawezesha wanawake katika nyanja mbalimbali.

Mke wa Rais wa Burundi, Angeline Ndayishimiye Ndayubaha alisema kwenye kongamano hilo kwamba ni muhimu kuendeleza jumuiya yenye mustakabali wa pamoja kati ya China na Afrika. Kwani jumuiya hii inadhihirisha kwa kina umuhimu wa kushirikiana katika masuala mbalimbali yakiwemo matibabu na teknolojia, na kueleza kuwa wakati wa kipindi cha UVIKO-19, ushirikiano huu uliendelezwa na ukawa mkubwa katika maeneo haya.

China na Afrika ambazo zina nia na dhamira moja, siku zote zinasonga mbele bega kwa bega kwenye safari ya kuhimiza maendeleo ya wanawake. Hivi sasa ukienda katika sehemu mbalimbali za Afrika, utakuta wanawake kutoka China wakifanya kazi kikamilifu katika timu za matibabu, katika kazi za kulinda amani, kwenye maeneo ya ujenzi wa miundombinu, na katika programu za mafunzo ya kiufundi.

Hii ndio maana halisi ya kujenga Jumuiya yenye mustakabali wa pamoja kati ya China na Afrika iliyopewa msisitizo kwenye kongamano hilo.
 
Back
Top Bottom