Vipepeo weusi season 2: From Zurich with rules

Vipepeo weusi season 2: From Zurich with rules

VIPEPEO WEUSI



SEASON 2 - FROM ZURICH WITH RULES



EPISODE 19

Nikapiga hatua za haraka mpaka pale kwenye meza ya mapokezi.

Yule muhudumu alikuwa ananikodolea macho kama vile ameona jini.

"Can I help you sir?" Aliongea kwa wasiwasi huku anajitahidi kuficha wasiwasi alio nao.

"I need a room!" Nikajikuta nimeropoka tu.

Mpaka muda huu akili yangu ilikuwa kama vile haifanyi kazi. Nilikuwa sijui hata nifanye kitu gani hasa ukizingatia niko ugenini hapa kwenye nchi ya watu. Nilichokuwa nahisi ni sahihi kukifanya labda ni kujaribu kuwachanganya kama kuna watu wowote wale ambao walikuwa wananifuatilia wasiweze kutabiri 'next move' ambayo nitafanya. Kwa hiyo nilikuwa nafanya mambo hovyo hovyo tu.

"Excuse me?" Yule muhudumu akaniuliza kwa mshangao zaidi.

"Can I get a room please?" Nikamjibu kwa kujiamini kabisa.

"No…aaah no sir we dont have one!" Akajibu kwa kigugumizi huku anaangalia nyuma yangu kila baada ya kuongea neno moja.

Nilikuwa na hakika kabisa kwamba alikuwa anamuangalia yule jamaa aliyekaa kwenye sofa aliyevalia kofia ya pama na koti jeusi.
Bado akili yangu ilikuwa inajaribu kupiga hesabu kwa nini muhudumu huyu kila mara alikuwa anamuangalia yule mtu. Lakini nilihisi mambo mawili. Moja, inawezekana kwamba muhudumu huyu alikuwa anajua kwamba yule jamaa ndiye ambaye aliingia chumbani kwangu na kufanya upekuzi na kisha kufuta alama za vidole kwa windex. Au pili, labda jamaa huyu alikuwa amempa onyo fulani la vitisho muhudumu huyu labda ndio maana kila sentesi ambayo alikuwa anaongea alikuwa anageuka nyuma kuhakikisha kwamba haendi kinyume na matakwa ya yule mtu.

"What? What do you mean? How can you not have a room… I checked out like ten minutes ago!" Nikaongeakwa kukereka huku nimemkazia macho.

"It has already been taken by another customer… am sorry sir!" Akanijibu huku anajitahidi kulazimisha tabasamu lake la 'customer care'. Lakini japokuwa alikuwa anajitajidi sana kulazimisha tabasamu, wasiwasi wake usoni ulikuwa haufichiki.

"What? It has been taken? By who?"

"I am sorry sir but that is non of your business!" Safari hii alinijibu kwa kujiamini walau kidogo. Hata mwenyewe nilijishtukia kwa kuuliza swali la kijinga vile. Lakini bado hasira zangu ziliiuwa hazijapoa. Kuna mchezo hapa ulikuwa unafanyika na huyu muhudumu alikuwa anaujua.

"What the *** is going on here.!??"Nikamuuliza kwa hasira kwa kunong'ona huku nimemsogezea uso wangu kukaribia kabisa kugusana na uso wake.

"What do you mean sir?"

"Well lets see… for staters… who the hell is that guy you are looking at after every two seconds?"

Tulibakia tumekaziana macho kwa muda wa karibia nusu dakika hivi. Kwa namna fulani nilianza kuona ule wasiwasi ambao nilikuwa nauona awali usoni kwa huyu muhudumu ulianza kuondoka. Sasa hivi ghafla alikuwa na hali fulani hivi ya kujiamini. Hata kile kitendo cha kuangalia nyuma yangu alipo yule jamaa kwenye sofa kila baada sekunde kadhaa sasa hivi alikuwa hafanyi hivyo tena.
Alikuwa na uso fulani hivi wa kujiamini ambao kwa kiasi fulani ulianza kunifanya nianze kuogopa kuendelea kuongea naye hovyo hovyo.

Nikageuka kuangalia nyuma yangu pale kwenye masofa ya wateja kupumzika. Yule jamaa mwenye koti jeusi na kofia ya pama hakuwepo!!
Nikajikuta natabasamu mwenyewe… halikuwa tabasamu la furaha, bali tabasamu la woga na kuchanganyikiwa. Kuna jambo la ajabu sana hapa lilikuwa linaendelea. Iweje huyu muhudumu aanze kujiamini ghafla tu baada ya yule jamaa kuondoka? Alikuwa anamuogopa? Kwa nini amuogope?


"Sir… i am going to ask you to leave!" Akaongeak kwa kujiamini zaidi nilipogeuka tena upande wake kumuangalia.

Nikajikuta tu nimeishiwa maneno ya kuongea. Nikabaki namuangalia tu huku naye amenikazia macho. Hapepesi wala kuangalia pembeni. Kuna kitu fulani moyoni kilikuwa kinaniambia kuwa huyu dada alikuwa ni zaidi ya muhudumu. Kuna kitu fulani hivi cha ziada alikuwa. Namna ambavyo alikuwa anajiamini, namna ambavyo alikuwa anaongea kwa mamlaka, namna ambavyo alikuwa ananikazia macho bila kupepesa… kuna hisia fulani nilianzakuipata, kwamba huyu dada alikuwa ni zaidi ya "receptionist".

"What is going on here?"

Wote wawili tuligutushwa kutoka kwenye kukaziana macho na sauti ya mtu pembeni yetu. Alikuwa ni jamaa fulani hivi.. mzungu mtu mzima wa makamo kama katikati ya miaka ya arobaini hivi. Alikuwa amevalia suti ya kibiashara nadhifu na miwani ya macho.

"Who are you?" Nikamuuliza kwa kiburi… bado nilikuwa na hasira kutokana na huu mchezo ambao nilikuwa nahisi ulikuwa unafanyika dhidi yangu hapa.

"I am the Manager!" Akanijibu kwa tabasamu huku ananipa mkono.

Nikajifanya kama vile ule mkono alionipa nilikuwa siuoni. Nikamtazama tu kwa hasira na kuanza kung'aka.

"Ok Mr. Manager… your employee here is dening to give me a room… is that how you do business.!"

"Is that true Erica?" Meneja akamuuliza muhudumu ambaye sasa nilijua kuwa anaitwa Erica. Alimuuliza kwa mshangao kidogo.

"No sir that is not true… all rooms have been taken and I was trying to explain that to Mr. Ray here but he doesn't seem to understand…"

"What…??" Yule muhudumu alikuwa anajitetea kwa boss wake lakini nilimkatisha kwa mshtuko wangu usoni na swali ambalo lilinitoka ghafla pasipo mimi mwenyewe kujua. "What".

"Sorry sir!" Akaniuliza kwa tabasamu la kufoji.

"What did you call me?" Nilimuuliza kwa mshangao mkubwa kama vile nimeona shetani mbele yangu. Nilikuwa siamini kile ambacho nilikuwa nafikiria kichwani mwangu. Ameniita 'Ray'??

"I said your name… aaah you did register here earlier that your name is Rwe…ye…ma…mu Charles! Right?" Alijifanya kulisoma jina langu kwa shida kama ambavyo wazungu wote wanavyopataga shida kulitamka.

Sikuwa naogopa yeye kulifahamu jina langu. Wala sikuwa naogopa yeye kulikumbuka jina langu kiusahihi licha ya ukweli kwamba ni ngumu mtu kukumbuka tu jina langu ukizingatia kwamba anahudumia mamia ya watu hapo mapokezi kila siku. Kilichokuwa kimeniogopesha ni yeye kuniita "Ray". Ningeelewa kama angeliniita "Rweye" labda ningesema amefupisha. Lakini sio 'Ray'. Ray ni 'nick name' ambayo wananiita watu wangu wa karibu na wale ambao nafahamiana nao vizuri. Huyu muhudumu ameijuaje?

Nikamuangalia tena. Alikuwa ananitazama kwa jicho fulani hivi la kifedhuli. Nina hakika kabisa na yeye alikuwa amejishtukia kwamba amefanya makosa makubwa kuniita 'Ray'. Amenifanya ning'amue kwamba kuna kitu cha ziada alikuwa anakijua na alikuwa ni zaidi ya 'receptionist'.

"Sorry sir we can…………"

Nilimsikia kwa mbali sana yule meneja akiwa anaongea. Tayari nilikuwa nimeshageuka na kuanza kuondoka nikikaribia mlango wa kutoka nje. "Who is she? And what does she want?" Nilijiuliza maswali mwenyewe baada ya kutoka nje ya hotel.

Kwa muda wa kama dakika nzima nilisimama tu kando ya barabara nisijue nifanye nini hasa. Nilijikuta ghafla tu naogopa hata kwenda kukaa kwenye hoteli nyingine. Nilianza tena kujilaumu huu uamuzi wangu wa kuja Zurich. Ugeni nilio nao ulikuwa unanifanya nisijue hata nielekee wapi au nifanye nini ambacho kitakuwa sahihi.
"Mr. Ray", nilijikuta kama naisikia tena sauti ya yule muhudumu akitamka jina ambalo wananiita watu wanaonifahamu kwa uzuri na watu wangu wa karibu. Amelijuaje huyu muhudumu. Nikakumbuka tena namna ambavyo alikuwa anajiamini. Nikakumbuka tena namna ambavyo aliniangalia kwa jicho la kifedhuli baada ya kujishtukia kuwa "ameropoka" jina langu ambalo hapaswi kulijua.
Moyo ulinilipuka.

Baada ya kufikiria kwa karibia dakika tatu hivu hatimaye nikakata shauri. Sikujua ni kwa nini lakini kuna sehemu moja tu kwa sasa hapa Zurich ambako moyo wangu ulikuwa na amani kwenda.
Nikasimamisha taxi na kukwea ndani.

"Hardstrasse!" Nikamuambia dereva taxi mara tu baada ya kukwea ndani.

Nilikuwa natamani kungekuwa na chaguo lingine la mahala kwa kwenda ambako moyo wangu ungekuwa unasikia amani, lakini hapakuwepo. Japokuwa kwenye lile jengo ninalokwenda sikujua hasa undani wale ni upi zaidi ya nyaraka zinazoonyesha kwamba ni langu kutokakwa marehemu mzee wangu, lakini walau moyo wangu ulikuwa unasikia amani kwenda.

Kama dakika kumi na tano baadae tayari nilikuwa nimeshuka kwenye taxi na nilikuwa mbele ya mlango wa jengo.
Namna ambavyo nilikuwa nakokota mabegi yangu usiku huu kuingia kwenye jengo ambalo limetelekezwa muda mrefu nilikuwa naonekana kama kichaa au chokoraa. Ati mimi Rweyemamu Charles, mume na baba wa mtoto… mjasiriamali, na 'kichwa' wa kutegemewa huko nyumbani Tanzania, kama kungekuwa na mtu ananiangalia sasa hivi nikiingia kwenye hili jengo pasina shaka yoyote angeamini kuwa ni chokoraa natafuta 'kambi' ya kulala usiku huu. Nijakuta natabasamu peke yangu na kukumbuka watu wote ambao nilikuwa nikiwaona wakilala kwenye mitaro au nje ya 'fremu' za maduka usiku Dar es Salaam, ni nadra sana kuwafikiria mara mbili baadaya kuwaona… mara nyingi tunadharau tu, "chokoraa hawa" kumbe yawezekana kabisa wako wenye mambo mazito ambayo yamejificha nyuma ya pazia kama leo hii 'chokoraa Ray' na hii hali yangu ninayopitia.

Niliingia kwenye jengo na moja kwa moja nikaelekea kwenye kile chumba ambacho siku ya kwanza nilijikuta nimeamka ndani yake na baadae kutazama ule ujumbe wa video wa mzee Charles.
Chumba kilikuwa vile vile kama ambavyo nilikiona mara ya mwisho nilivyokuwa hapa. Nikasimama huku nimejishika mikono kiukoni nikatazama huku na huko pale chumbani kujaribu kuangalia namna gani ambavyo nitalala humu ndani. Lakini kila ambavyo nilikuwa nikifikiria kulala ndivyo ambavyo usingizi ulikuwa unanikimbia.

Kichwani wazo moja tu lilikuwa linanitesa… Erica, yule muhudumu wa pate Hotelini ni nani? Amenifahamu vipi? Na kwa nini alikuwa anaongea kwa wasiwasi sana kipindi yule mtu aliyevaa kofia ya pama na koti jeusi lakini mara tu baada ya yule mtu kuondoka alibadilika ghafla na kuwa na hali ya kujiamini kwa hali ya juu? Yule mtu mwenye kofia na koti jeusi ni nani? Vipi wale vijana wawili wa kizungu? Nao ni akina nani? Kwa nini nao walikuwa wananifuatilia?
Hii ndio sababu ambayo ilinifanya hata niogope kwenda kukaa kwenye hoteli nyingine… kwa kiasi fulani nilianza kuwa 'paranoid'. Nilikuwa na mashaka na kila mtu ambaye alikuwa mbele yangu… kila mtu nilimuhisi kwa namna moja au nyingine alikuwa ananiwinda mimi. Kwa hakika nilikuwa nahitaji kutuliza akili ili niweze kung'amua kile ambacho kilikuwa kinaendelea na kubwa zaidi nijue hicho ninachopaswa kujua na kurudi nyumbani Tanzania.

Siku ambayo nilipanda ndege kuja huku Zurich kwa hakika sikudhani kama kutakuja kuwa na vitendawili namna hii na endapo kama ningelijua basi kamwe nisingethubutu kufunga safari ya kuja huku. Kipindi nakuja niliamini labda nitafika tu na kukabidhiwa kama ni nyaraka au taarifa zote ambazo napaswa kuzipata hapa mara moja na kisha kurejea nyumbani. Lakini tofauti na mategemeo sasa nimegeuka kama swala kwenye msitu uliojaa simba na chui. Kila jani ambalo litatikisika nahisi ni mimi nawindwa kukamatwa.


Nikakitazama kile chumba kwa dakika kadhaa… usingizi haukuwepo kabisa.
Nikavuta moja ya begi langu na kulifungua na kisha kutoa lundo la zile nyaraka ambazo nilizipata hapa na nyingine nilizopewa na Hudini.

Nikapekua karatasi kwa karatasi… hakuna chochote kile ambacho nilikielewa zaidi ya mfululizo wa anuani kadhaa, namba za akaunti za benki na baadhi ya majina ya watu. Na kilichofanya kazi ya kuelewa nyaraka hizi kuwa ngumu ni namna ambavyo zilikuwa 'reducted'. Sehemu kubwa za maandishi zilikuwa zimefutwa kwa kuzibwa na wino mweusi. Nilipekua mpaka kuifikia tena ile picha ya mgahawa wa kichina. Nikaiangalia tena na tena kisha nikaendelea kutazama nyaraka zilizokuwa zinafuata baada ya picha hii. Kuna hisia fulani hivi ilikuwa inanijia nilikuwa nimeanza kujihisi kama kuna kitu mimeanza kukielewa hasa hasa nyaraka zilizofuata chini baada ya picha hii ya mgahawa wa kichina. Zilikuwa na uhusiano fulani hivi au mfanano wa baadhi ya vitu.

Nikaanza kupekua haraka haraka nione ni nyaraka ngapi zilikuwa na huu mfanano. Nilipekua haraka haraka mpaka kufikia nyaraka ambayo macho yangu yalipotua juu yake ilinifanya nihisi moyo unalipuka kiasi kwamba kama ulikuwa unataka kuchomoka kifuani. Ilikuwa ni nyaraka ambayo juu kabisa upande wa kulia ilikuwa na picha ya 'passport'. Japokuwa ilikuwa kwenye rangi ya 'black and white' lakini macho yangu yaliona sawia kabisa ile picha na kuing'amua. Ilikuwa ni passport ya Erica, yule binti wa mapokezi pale hotelini. Chini ya picha hii kulikuwa na maandishi yalisomeka;

IVANKA WYCLIFFE
AFFOLTERNSTRASSE 44
CITYPORT
POSTFACH 8131
8050
ZURICH

Chini ya anuania hii kulikuwa na maandishi mengine lakini yote yalikuwa yamefutwa kwa wino mweusi.

Jambo ambalo lilinishitua zaidi ni kwamba anuani hii inafanana kabisa na ile anuani ambayo niliikuta kwenye bahasha ambayo nilipewa na mzee wangu ambayo niliifungua siku ile usiku nyumbani kwangu na kuwa chanzo cha mpaka mimi kusafiri kuja huku… tofauti yake ilikuwa ni moja tu… jina la kwanza la mwenye anuani. Anuani ile kutoka kwenye bahasha niliyoifungua nyumbani iliandikwa;


HUDINI
AFFOLTERNSTRASSE 44
CITYPORT
POSTFACH 8131
8050
ZURICH
SWITZERLAND.

Sikutaka kupoteza muda zaidi… nikaanza kupekua nyaraka za chini yake ili nione kama kuna mfanano zaidi na kama nitaweza kuanza kung'amua kitendawili ambacho kilikuwa kinanizunguka tangu nifike hapa Zurich.
Lakini nikiwa naanza kupekua tu nikasikia kama mlango wa kule nje wa kuingilia ndani ya jengo umefunguliwa. Niliweza kusikia kwa usawia kabisa kutokana na ukimya mkubwa ambao ulikuwa kwenye jengo hili.

Nikainuka haraka haraka na kutoka ndaji ya chumba. Nikatembea mpaka kufika kwenye korido ambayo inaelekea nje. Ghafla tu hapa koridoni nikakutana ana kwa ana na 'jinamizi'. Ilikuwa ni kama vile nilikuwa usingizini nimeota shetani na hatimaye kuamka na kumkuta amesimama pembeni mwa kitanda.
Mbele yangu alikuwa amesimama Erica, yule binti wa mapokezi pale Hotelini. Mkononi ameshika bastola. Nilijikuta nainua mikono juu kabla hajasema chochote kile. Uso wake haukuonyesha mzaha hata kidogo, alikuwa anajiamini na aliniangalia moja kwa moja usoni bila kupepesa macho.

"Give it to me!"

Akaongea kwa sauti ya upole lakini iliyojaa mamlaka na kujiamini.

"Give you what?" Nikaongea huku sauti inakwama kwama kama nina kigugumizi. Sikumbuki kama nimewahi kunyooshewa bastola tangu nizaliwe. Licha ya misukosuko yote niliyopitia lakini hii ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kwa mdomo wa bastola kuwekwa mbele ya uso wangu.

"I said give it me"

Akaongea tena kwa ufupi tu.

"I don't understand... give you what?"

"I am going to ask you one last time… give me the keys!"

Akaongea kwa hasira na 'kuikoki' bastola kwa kidole gumba.

"What key are you……??"

"BAAAAAAAAANNNGG..!!"

Sikujua ni nini kilitokea lakini nilijikuta nimedondoka chini kwa kishindo kama gunia la mchele. Siku zote nilikuwa nikidhani kwamba ukipigwa risasi kuna maumivu makali unapitia… lakini sijui kama ilikuwa ni mshtuko nilioupata au nini, lakini sikusikia maumivu… kitu pekee ambacho nilikihisi ni baridi kali sana tumboni, kama vile napepewa na kipupwe… mwili ulikuwa unashindwa hata kusogea… nikiwa nimelala pale pale chini nikapeleka mkono mpaka pale tumboni nilipokuwa nahisi baridi kali… palikuwa pamelowa chapa chapa. Nikajipapasa tumbo kwa mkono na kisha kuinua mkono mpaka usoni nione. Kiganja cha mkono chote kilikuwa kimelowa damu. Kitu cha mwisho nilichokiona ilikuwa ni Erica akiniruka pale chini nilipodondoka na kuingia kule chumbani nilikoacha nyaraka. Mwili ukaniishia nguvu na macho yakafunga.




Itaendelea…


The Bold
To Infinity and Beyond
 
Kichwa katika ubora wako! tunasubiri mkuu
 
tapatalk_1519472923336.jpeg


VIPEPEO WEUSI



SEASON 2 - FROM ZURICH WITH RULES




EPISODE 20



"…jasho tunalovuja, damu inayomwagika na maumivu yote ambayo tunapitia, ili kumfanya mtu mmoja tu awe na furaha, mtu mmoja ambaye ameufanya moyo wako kuwa dhaifu na kuanguka kwenye mapenzi… kuna muda unajiuliza kama huwa anawaza, kama huwa anakaa chini na kutafakari na kushukuru kwa kafara zote ambazo umezifanya juu yake. Siku zote ambazo haukulala ili tu upate fedha za kutosha kununua gauni lake la ndoto, maumivu yote ambayo umeyavumilia kupambana na adui zake kumuweka salama, namna uhai wako uliuweka rehani ili kufanikisha maisha yenu ya ndoto, damu iliyomwagika kutetea furaha yenu. Je, huwa anakaa na kutafakari na kusikia fahari juu yako? Ubaya nikwamba kafara zote hizi unazifanya pasipo yeye kufahamu, siri ambazo nyingi utakufa nazo moyoni mwako, na siku tu ambayo utakufa siku chache baadae ataanguka tena kwenye mapenzi na mtu mwingine. Je, tukiwa kwenye maisha hayo mengine baada ya kifo, kisha tukatazama chini na kuwaona tuwapendao ambao tulitoa kafara maisha yetu kwa ajili yao, tukiwaona wakiwa na furaha mapenzini na mtu mwingine… ni nini ambacho roho zetu zitasikia? Uchungu wa kuhisi tumesalitiwa au furaha kwa kuwa tuwapendao wanaishi maisha ya furaha huku nyuma tulikowaacha?

Labda maisha hayahitaji kutafakari sana na kujiuliza… muheshimu Mungu, mpende mkeo na tetea nchi yako. Labda tunapaswa kuishi kwa kanuni hii bila kujiuliza sana italeta matokeo gani.. tunapswa kuishi tu huku tukinuia kuacha alama kubwa duniani ambayo itatufanya tusikie fahari siku tukiwa kwenye maisha mengine baada ya kifo na kutazama nyuma duniani…"



*****


Tulikuwa nyumbani kwa Luke yule jamaa ambaye alikuwa na yule chokoraa ambao walinikuta kwenye lile jumba mtaa wa Hardstrasse nilipopigwa risasi.
Luke alikuwa anakaa mtaa wa Sahilstrasse hapa hapa Zurich.

Tayari nilikuwa nimemaliza kumsilimulia kila kitu ambacho kimenitokea mpaka kupelekea kupigwa ile risasi tumboni na wao kunikuta pale. Swali moja ambalo bado alikuwa hajanijibu ni kwa namna gani walinikuta pale? Ni nini ambacho wao kiliwapelekea kufika kwenye lile jumba?


"…nahisi ni muhimu twende hospitali.!" Nilimueleza huku najiangakia tumboni kwenye kidonda kibichi ambako nilikuwa nimepigwa risasi.

Kwa namna ambavyo hapa kwake kulivyo nilikuwa na mashaka kama ndio nyumbani kwake halisi au ni sehemu tu ambayo alikuwa anaitumia kwa dharura. Ilikuwa ni aina ya chumba ambacho wazungu wanaita 'studio apartment'. Yaani ni chumba kimoja kikubwa sana ambacho sehemu ya kulala, sebule na jiko vyote viko pamoja ndani ya chumba hiki hiki. Lakini sio sababu ambayo ilinipa wasi wasi kama luke alikuwa anaishi hapa au la… ni mazingira ya chumba hiki ndiyo ambayo yalikuwa ynanipa wasiwasi. Hakikuwa na runinga humu ndani, vyombo pale jikoni vilikuwa vimekaa katika namna ambayo ilionyesha wazi kabisa kwamba huwa havitumiwi mara kwa mara. Pia hata kitanda nacho kilionyesha kuwa kimetandikwa nadhifu vivyo kilivyo siku nyingi kidogo.


"Ukienda hospitali alafu unawapa maelezo gani?" Luke alinijibu huku anaendelea kuchemsha kitu fulani pale jikoni.

"Nitajificha hapa mpaka lini… pia hili ni tukio la kihalifu nimefanyiwa. Polisi wanapaswa kujua!" Nikamjibu.

"Na polisi wakishajua utawaeleza ulikuwa unafanya nini pale kwenye lile jumba ulipopigwa risasi?" Luke akanijibu tena bila kugeuka akiendelea kuchemsha kitu pale jikoni.


Kwa kiasi fulani alichokuwa anaongea kilikuwa kinaingia akilini.


Nilifikiria mara mbili mbili. Je, niko tayari kuwaeleza polisi nimekuja hapa Zurich kufanya nini? Niko tayari kuwaeleza matukio yote ambayo yametokea mpaka kufikia hatua hiyo ya kupigwa risasi? Na je nikiwaeleza haitavuruga kile ambacho nimekuja kukifanya hapa Zurich?

Nikahisi ili niweze kufikia lengo ambalo limenileta hapa Zurich ni vyema nikafuata ushauri wa Luke, nisiende polisi wala kuwahusisha kwenye suala hili.

"Kwa hiyo tunafanyaje baada ya hapa?" Nikamuuliza Luke.

"Hatua ya kwanza nadhani ni kwenda pale hotelini na kupata taarifa juu huyo binti muhudumu Erica ambaye unasema amekupiga risasi!"

Luke alinijubu huku anakuja kukaa kwenye sofa karibu yangu na pale ambako nilikuwa nimejilaza. Alanikabidhi kikombe chenye kitu ambacho alikuwa anachemsha…

"Kunywa hii!"

"Ni nini?"

"Chong Ko! Chai fulani ya majani ya kichina… inasaidia kwa ajili ya kudhibiti maumivu na msongo!"

Nilipokea likombe na kuanza kuchwa chai hiyo yenye harufu kama miti shamba na uchungu wa wastani kama kahawa.

"Nitahitaji kupiga simu.… sijui una simu humu?" Nilimuuliza huku nikiangaza angaza pale chumbani.

"Unampigia nani?" Luke aliniuliza kwa mshangao.

"Relax! Sihitaji kuwapigia polisi… nataka kupiga simu nyumbani Tanzania!"

"Ile simu ya mezani hauwezi kupiga nje ya nchi… tumia hii simu yangu!" Luke aliongea na kurusha simu kwenye sofa ambalo nilikuwa nimejilaza na kuanzankusimama.

"Unanipa simu yako hii vipi nikihitaji kikupigia ukiwa umeenda huko hotelini?"

"Sitachukua muda mrefu… ndani ya nusu saa tu nitakuwa nimerudi.!" Luke aliongea huku anajifunga skafu ya kujikinga na baridi na kuanza kuondoka.

"Ok.!" Nikamjibu kwa kifupi tu.

Alipotoka tu nje ya mlango nikaanza kujiuliza tena na tena. Luke ana maslahi gani haswa kwenye suala hili mpaka amelivalia njuga hivi? Japokuwa amekuwa akinieleza kwa fumbo kwamba "kuna deni anayaka kuwalipa Hudini" lakini bado nilikuwa nahisi kuna jambo la zaidi. Kuna kitu kimejificha nyuma ya hili.
Kila ambavyo nilikuwa nikiwaza ni kwa namna gani Luke na yule Jimmy chokoraa walinikuta pale kwenye lile jengo nilikuwa sipati jawabu.

"Kuna kitu gani ambacho kimejificha?"

Nikajiukiza peke yangu kimoyo moyo.

Nikainamisha tena shingo kuangalia kidonda cha risasi pale tumboni. Nilikuwa nasikia maumivu kwa mbali sasa hivi. Labda na hii chai tiba niliyopewa na Luke ilikuwa imesaidia.
Nikajikaza kiume na kujiinua kutoka pale kwenye sofa na kuanza kutembea kwa kuchechemea mpaka kwenye dirisha la hiki chumba.

Nje kilikuwa kumepambazuka na ilikuwa asubuhi murua kabisa isiyo na mawingu. Jua lilikuwa linaangaza vyema nje. Chumba hiki cha Luke kilikuwa kwenye ghorofa ya tatu ya jengo hili tulilomo. Kwa hiyo hapa dirishani ambako nilikuwa nachungulia nilikuwa naweza kuona vyema kabisa huko nje mitaani.

Nilijikuta nawaonea wivu watu waliokuwa wanapita pita kule chini barabarani kuwahi makazini na kwenye mihangaiko yao.
Nilijikuta nasikia wivu na kutamani maisha yale… maisha rahisi tu, ambayo hayana siri za kufichua, hayana watu wa kuwatafuta na wala hayana jumuiya ya siri ya kupambana nayo. Ni kwa namna gani maisha hayo yanapendeza. Kuamka tu asubuhi kwenda kwenye mihangaiko na kurejea kwa familia yako.

"Wengine hatukupata fursa ya kuchagua maisha… tumezaliwa kwenye maisha tuliyonayo!"

Niliongea mwenyewe kwa sauti ya taratibu huku bado nikitazama nje dirishani. Hii ndio ilikuwa imani yangu siku zote. Kuna baadhi yetu hapa duniani tangu kuzaliwa hatujapata fursa ya kuchagua maisha tunayoyataka. Tumejikuta tumezaliwa tu na tuna maisha ambayo tuko nayo. Usiri, hatari, migogoro na mapambano. Sikuchagua kuzaliwa na kuwa mtoto wa Charles Bernard Kajuna.
Lakini upande mwingine wa akili yangu ulinikosoa, kwa sababu ilikuwa ni chaguo langu kuja hapa Zurich, hakuna mtu ambaye alinilazimisha. Ni kiu yangu ya kutaka kujua, ni 'curiosity' yangu imenileta hapa.

"Wengine hatukupata fursa ya kuchagua maisha… tumezaliwa kwenye maisha tuliyonayo!"

Nikarudia tena ile kauli huku nikiitazama simu ambayo Luke alinipa kiganjani mwangu.

Nikajiukiza kama nina ujasiri wa kupiga simu ambayo nilikuwa nataka kupiga. Kama nitaweza hata kuongea.

Lakini sikuwa na jinsi. Nilijihisi kama niko msituni nimepotea. Nilijihisi kama niko mtupu nafsini mwangu. Nilijihisi kama nimepoteza ramani kabisa. Kuna mtu mmoja tu ambaye anaweza kunifanya akili yangu ikae sawa sawa na kujihisi nina kila kitu juu ya uso wa dunia.

Nikabofya namba kwenye simu.

Nikaweka simu sikioni.


"Hello.!"

Moyo wangu ulipasuka niliposikia sauti upande wa pili wa simu. Kwa jinsi ambavyo nafsini mwangu nilikuwa mtupu na jinsi ambavyo nafsi ilikuwa imepotea… sauti hii ya upande wa pili ilipenya mpaka kwenye nafsi yangu kama vile kisu cha moto kinavyopenya kwenye siagi.


"Hello.!" Nikajibu.


Japokuwa sikuwa namuona lakini niliweza kuhisi mshituko wake. Hakujua kwamba ilikuwa ni simu yangu na alishituka kusikia sauti yangu.


"Ray.!" Aliongea kwa sauti ya kinyonge kabisa kama vile anataka kuanza kulia.


"Cheupe.!" Nilimuita huku nikijikaza na kutabasamu.

Nilihisi pia tabasamu lake upande wa pili. Kwa miezi kadhaa ambayo tumekuwa na migogoro na Cheupe hata majina yetu ya utani tangu utoto tulikuwa hatuyatamki wala kuitana.

"Uko wapi Ray.!" Cheupe alijikuta anashindwa aseme nini na kuniuliza swali ambalo alikuwa na jawabu lake.

"Bado niko Zurich… mwanangu ajambo?"

"Ajambo! We miss you please come back..!"

Kwa jinsi ambavyo aliongea niliweza kuhisi majuto kwenye sauti yake. Nilihisi kabisa kwa namna fulani labda anajutia ni kwa namna gaji mgogoro wetu ulianza kutokana na ajira yake.

"Nitarudi mama… kuna masuala namalizia!" Nikamjibu.


"Hapana Ray! Nataka kesho upande ndege na kurudi…!" Cheupe aliongea kwa kumaanisha.

"Siwezi kuondoka haraka namna hiyo kwa sababu…." Nilijishtukia na kushindwa kumaliza sentensi.

"Kwa sababu gani Ray?" Cheupe aliuliza kwa shauku.

"No its nothing! Kuna masuala tu namalizia..!" Nikijaribu kudanganya.

"Hapana Ray! Kwa sababu gani? Nieleze ukweli!!"

Wakati mwingine ndio ubaya wa mtu kukufahamu kana kwamba kiganja cha mkono wake. Cheupe alikuwa ananifahamu kama mimi mwenyewe ninavyojifahamu. Tayari alihisi kuna changamoto nilikuwa nayo.

"Nimepata ajali… nina majeraha! Sidhani kama nitaruhusiwa kusafiri.!" Nikaongea kwa upole.

"Majereha? Ajali? Nini kimetokea Ray?" Cheupe aliongea kwa taharuki.

"Usijali mama… nitakuwa sawa!"

"Hapana niambie ni nini kimetokea!"

"Ah… mh! Nimepigwa risasi tumboni lakini…."

Sikumalizia hata sentensi yangu nilimsikia Cheupe anaanza kulia.

"Ray! Please come back! You are losing yourself honey… please come back.!" Cheupe aliongea kati kati ya kilio.

Kwa mara nyingine tena ni kama kisu cha moto kilipitisha nafsini mwangu. Hakuna kitu ambacho kilikuwa kinanipasua nafsikama kumsikia mkewangu akilia. Tena akilia kwa kosa ambalo sikupaswa kukifanya. Lakini pia aliongea kitu ambacho nilikuwa nakihisi muda wote. I was loosibg myself. Mimejitumbukiza kwenye masuala mazito ambayo sasa yakikuwa yananigharimu. Nilijisikia uchungu. Nilisikia hasira. Nilijihisi kujichukia ghafla.

"I am so sorry..!" Nilishindwa kusema chochote zaidi. Niliongea kwa kwikwi nikijizuia kulia.

"Please come back!" Cheupe aliongea huku bado akiwa na sauti ya kilio.


Kabla sijajibu chochote ghafla nilisikia mlango unagongwa. Ulikuwa unagongwa kitemi isivyo kawaida. Mara moja nafsi yangi ikatambua kuna jambo haliko sawa.

"Honey! Naomba nikupigie tena baadae kidogo.." niliongea haraka haraka kwa sauti ya chini.

"What is happening Ray!" Cheupe aliongea kwa taharuki zaidi.

"will call you back honey!" Niliongea kwa sauti ya chini zaidi.

"Please take care of yourself… please cone back!"

Nilishindwa hata kujibu. Mlango ulikuwa unagongwa kwa nguvu sana na kitemi.

"Nakupenda mkewangu…!"

Sikusubri jibu. Nikakata simu na kusogea katikati ya chumba kusikiliza kwa makin.


"NGO NGO NGO NGO.!!"

Mlango uligongwa kwa nguvu zaidi.

Ugongaji huu wa mlango ulinifanya nishikwe na hofu ya ghafla. Haukuwa ugongaji wa heri.

"Who is this?" Nikauliza kwa sauti ya juu.

"It's the police! Open the door!"

Sauti upande wa pili wa mlango iliongea kwa nguvu.

Nilihisi kama vile nijirushe na kupiga mbizi sakafuni na kupotea. POLISI.!
Wameshitukia kilichotokea? Nimekuja kukamatwa au kuna nini la hatari zaidi?

Sikujua kama nikafungue mlango au niruke dirishani nikimbie? Lakini nitakimbiaje na hiki kidonda tumboni?

Nikiganda kama sanamu kijasho chembamba kikinitoka ghafla.



Itaendelea….



Muhimu: Ushauri ambao mmekuwa mkinipa kwa muda mrefu hatimaye nimeufanyia kazi. Ndani ya wiki mbili zijazo nitatoa kitabu changu cha kwanza kabisa cha simulizi ya Vipepeo Weusi. Kama ambavyo mmekuwa mkiniunga mkono kwenye nyuzi hizi kwa miaka mitatu sasa naomba pia sapoti yenu katika hatua hii mpya ambayo naichukua. Kwa pamoja tupambane kurejesha utamaduni wa watu kujisomea na tuinue kizazi kipya chenye maarifa.

Naomba baraka zenu ili project hii iwe na mafanikio na hatimaye nitoe vitabu vingi zaidi na zaidi.

Asanteni sana.


Habibu B. Anga "The Bold"
To Infinity and Beyond
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom