SEHEMU YA 23
Cassian aliamshwa na alamu ya simu yake, haraka sana akashtuka kutoka usingizini, mwili wake ulikuwa umechoka kwani usiku uliopita alichelewa kulala kutokana na kwenda baa kunywa huku akiwa na rafiki yake, Osman.
Akaanza kuangalia huku na kule, hakuwa sawa, akayapeleka macho yake katika saa yake ya ukutani ambayo ilimuonyesha kwamba tayari ilikuwa ni saa 12:00.
Akapeleka mkono wake pembeni kwa lengo la kumgusa mpenzi wake, Evelyne, alikuwa amesahau kile kilichotokea usiku uliopita, alipomkosa, kumbukumbu zake zikamjia kwamba aliachana na msichana huyo.
Hapo ndipo mawazo juu ya Evelyne yalipoanza kurudi kichwani mwake. Alijiona shujaa, alifanya kitu ambacho kwa wanaume wengine wasingeweza kufanya, alipoteza muda wake, alilia kwa kuwa aliumia sana lakini baadaye, kila kitu kilichokuwa kimetokea hakikuwa kama kile alichokuwa amekifikiria.
Wakati akiwaza hayo, picha ya msichana mmoja ikaja kichwani mwake, hakuwa msichana mwingine zaidi na Naseku. Alimkumbuka binti huyo wa kimasai, jinsi alivyokuwa mrembo, umbo matata ambalo lilitosha kumfanya mwanaume yeyote duniani kuwa kwenye mhemko mkubwa.
Akatoa tabasamu, kwa jinsi alivyokuwa, alihisi kabisa kwamba msichana huyo alistahili kuwa mke wake, alikuwa msichana masikini, aliyetafuta maisha kwa kuwa mhudumu katika mgahawa uliokuwa Kinondoni, hakutaka kujali kwa kuwa alikuwa na pesa, aliamini kwamba angeweza kumbadilisha na kuwa na muonekano mzuri kama ilivyokuwa kwa Kim Kardashian.
Hakuwa amezoeana naye, ila aliamini kwamba kama angemtumia rafiki yake, Osman ingekuwa rahisi kuonana na msichana huyo kisha kuzungumza naye. Hapohapo pasipo kuchelewa akaichukua simu yake na kumpigia rafiki yake huyo.
“Vipi mzee mzima?” ilisikika sauti ya Osman kwenye simu.
“Poa tu! Una nafasi leo?” aliuliza Cassian.
“Yeah! Hasa kwa mtu kama wewe ukiuliza hivyo! Kuna ishu?” aliuliza Osman.
“Ndiyo! Nataka unipeleke kwa yule msichana!”
“Msichana gani?”
“Naseku!”
“Duh! Mpaka jina lake umelikariri! Wewe noma!”
“Hahaha! Itawezekana?”
“Haina shida!”