SEHEMU YA 17
Ilipofika majira ya saa moja usiku, Cassian akampigia simu Evelyne na kumwambia kwamba siku hiyo walitakiwa kulala hotelini ili asubuhi wajiandae na harusi iliyokuwa imepangwa kufanyika siku hiyo.
Hilo halikuwa tatizo, kwa kuwa alimwamini sana Cassian na aliamini kwamba hakuwa akifahamu kitu chochote kile, akaondoka nyumbani na kuelekea katika Hoteli ya Twiga iliyokuwa Masaki na kukutana huko.
Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kukumbatiana kwa furaha, wakaenda bafuni kuoga, walipomaliza, wakatupana kitandani na kuanza kuvuana nguo.
Akilini mwa Evelyne aliyaona mapenzi mazito ya mwanaume huyo, aliamini kwamba kusingekuwa na mwanamke yeyote ambaye angemtoa katika ulimwengu wake.
Walipomaliza kufanya mapenzi, simu ya Cassian ikaanza kuita, alipoliona jina la Osman wala hakujiuliza, akaipokea simu ile na kuanza kuzungumza naye.
“Umekwishafika? Ndiyo...ni kesho...ooh! mchungaji ndiyo amefika! Umempeleka hoteli gani? Serena...safi sana...anataka kuniona...basi sawa nakuja...” alisema Cassian na kukata simu.
“Nani?”
“Osman! Anasema kwamba mchungaji Mark ameingia kutoka Ufaransa! Hivyo anataka nikamuone mara moja,” alisema Cassian.
“Sawa. Ila usichelewe kurudi mpenzi!”
“Usijali!” alisema Cassian, hakuishia hapo tu, akamvuta Evelyne na kumbusu mfululizo kisha kuondoka.
Msichana huyo akabaki na amani moyoni mwake, hakuamini kama kweli siku inayofuata ndiyo ilikuwa ya kufunga ndoa na kuwa mke halali wa mwanaume huyo.
Alikuwa na tamaa ya utajiri, alijitahidi kuficha siri ambayo hatimaye alijua ndiyo ilikuwa imedumu pasipo kugundulika mpaka hapo alipokuwa akitaka kufunga naye ndoa.
Hapohapo akampigia simu Mwajuma, akajisifia sana kwamba alikuwa mwanamke wa shoka aliyemkamata vilivyo Cassian na mwisho wa siku kutaka kufunga naye ndoa huku akiwa amemdanganya vya kutosha kuhusu kuzaa watoto.
“Shoga kesho ndiyo naanza safari! Nikitoka hapo, ni kuleta vituko, akiniacha kesi inakwenda mahakamani tunagawana utajiri,” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na furaha ya ajabu.
“Jamani shoga mpaka nakuonea wivu! Unakwenda kuuchukua ubilionea hivihivi!” alisema Mwajuma.
“We acha tu! Ndiyo tayari nishatajirika!” alisema Evelyne.