Viganja Mashavuni Mwangu

Viganja Mashavuni Mwangu

SEHEMU YA 08

Siku hazikuwasubiri, ziliendelea kukatika kama kawaida. Baada ya kubaki wiki moja, maandalizi yakachachamaa, Evelyne hakutulia, kichwa chake kilifikiria mali, kwa jinsi alivyokuwa na presha aliona kama watu aliowaweka kwenye kamati walikuwa wakimchelewesha.

“Mwajuma! Wamesemaje?” aliuliza Evelyne.
“Kila kitu kipo tayari! Hoteli imekwishaandaliwa huko Comoro! Fungate tu ndiyo inasubiriwa,” alijibu msichana huyo baada ya kumpigia simu.
“Nashukuru sana shosti!”

“Halafu kuna kitu umesahau! Hivi umewaalika wale madaktari ambao walikusaidia kuficha siri?” aliuliza Mwajuma.

“Mungu wangu! Nilikuwa nimesahau! Ngoja niandike meseji halafu niwatumie wote kwa pamoja,” alisema Evelyne na kuanza kuandika ujumbe huo.

Aliandika harakaharaka, akakumbuka kwamba alitakiwa pia kumpigia Cassian na kumpa taarifa kwamba tayari hoteli ilikuwa imeandaliwa kwa ajili yao.

Mara baada ya kuandika ujumbe huo wa kuwashukuru madaktari kwa mchezo walioufanya, na kwa sababu jina la Cassian lilimkaa sana kichwani, kwenye kutuma, akamtumia na Cassian, anakuja kushtuka baada ya ujumbe huo kwenda huko.

“Mungu wangu! Nimemtumia na Cassian pia!” alisema Evelyne, hapohapo kwa kuchanganyikiwa, akadondosha simu. Mapigo ya moyo yakaanza kumdunda kwa nguvu.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 09

Cassian hakuwa na furaha kabisa, moyo wake ulikuwa na mawazo tele. Kila wakati alikuwa akimfikiria mpenzi wake, Evelyne, alionekana kuwa mwanamke shupavu, mwenye uvumilivu ambaye alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini si kumpoteza.

Alijiona kuwa na bahati kubwa, hakuwa na mawazo kwamba kitu alichokuwa akikihitaji msichana huyo kilikuwa mali zake na si mapenzi kama alivyokuwa amefikiria.

Akampigia simu rafiki yake aliyeitwa Osman na kumwambia kwamba alitaka kuzungumza naye, alihitaji kuwa bestman wake katika harusi hiyo iliyokuwa imebakiza siku moja kabla ya kufungwa katika boti moja ya kifahari aliyokuwa akiimiliki.

Kwa kuwa lilikuwa jambo muhimu, hakutaka kuzungumza naye kwenye simu, alichokitaka ni kuonana naye na kumwambia kwamba walitakiwa kuonana Serena Hotel kwa ajili ya kuzungumza suala hilo muhimu.

“Serena ni mbali sana. Kwa nini tusionane hapa Manyema?” aliuliza Osman kwenye simu. Alichokuwa akikiangalia zaidi kilikuwa ni foleni kubwa ya magari.
“Ipo wapi?”

“Hapa Kinondoni! Makaburini Mkwajuni!” alijibu Osman maneno yaliyomfanya Cassian kushtuka.
“Yaani nije kuonana na wewe Kinondoni?”
“Ndiyo! Njoo bwana!”

“Poa. Ila ninahitaji ulinzi, nisije kudandiwa na wahuni,” alisema Cassian, hilo halikuwa tatizo, kila kitu kiliandaliwa.
Cassian akatoka ofisini kwake, alijua kwamba alikuwa akienda katika mitaa ya Kiswahili hivyo hakutaka kwenda na gari lake la kifahari la Jaguar bali akachukua gari la mfanyakazi wake, Opa na kwenda nayo huko.

Hakutaka kugundulika, alijua kwamba kama angefika mahali hapo na gari la kifahari kila mtu angelitolea macho na kuangalia kuona ni mtu gani angeteremka katika gari hilo.

Njiani, kichwa chake hakikutulia, bado alimfikiria Evelyne, alimuona kuwa mwanamke shupavu, mwenye moyo wa chuma ambaye alijitolea maisha yake kwa asilimia mia moja kuishi naye japokuwa hakuwa na uwezo wa kumpa mimba.

Hakuchukua dakika nyingi akafika mahali hapo. Akapaki gari lake na kuteremka. Kwa kuwa lilikuwa gari la kawaida, hakukuwa na mtu aliyelitolea macho.
 
SEHEMU YA 10

Hakutaka kugundulika, hivyo akachukua miwani yake ya jua na kuvaa kisha kuanza kupiga hatua kwenye sehemu ya kulia chakula ambayo ilikuwa maarufu Kinondoni nzima kwa kupika ugali mzuri na nyama ya kuchoma.

“Karibu bwana. Umebadilika! Hiyo miwani kama komando,” alisema Osman, ndiyo ilikuwa kawaida yake, kila walipokuwa wakikutana, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumtania kutokana na muonekano wowote aliokuwa nao.

Wakakaa na kuagiza chakula. Macho ya Cassian hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, hakuonekana kujiamini, swali lililokuwa kichwani mwake ni nini kingetokea mahali hapo kama tu watu wangegundua kwamba alikuwa yeye.

Wakati akiangalia macho yake huku na kule, yakatua usoni mwa msichana mmoja, mrefu kidogo, msichana aliyekuwa na sura nzuri, kifua kidogo huku uso wake tu ukiwa na tabasamu la asili.

Cassian akabaki kimya, akamwangalia msichana huyo kwa muda. Aliuona uzuri wake lakini tatizo kubwa alilokuwa nalo ni umasikini uliokuwa ukimwandama.
Alibalia khanga moja iliyoonekana kuchoka, kwa ndani alikuwa na gauni lake refu na blauzi ya rangi nyekundu.

Japokuwa alionekana kuwa masikini kwa muonekano wake tu lakini msichana huyo alikuwa mchangamfu mno, aliongea na wateja kana kwamba alikuwa akimjua kila mtu.

“Mbona unamwangalia sana Naseku?” aliuliza Osman mara baada ya kumuona rafiki yake akimwangalia sana msichana huyo.

“Naseku! Ndiye nani?”
“Si huyo msichana unayemwangalia. Ngoja nimuite aje kutuhudumia,” alisema Osman na hapohapo kumuita msichana huyo.

Bila hiyana, huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana Naseku akaanza kupiga hatua kuelekea kule walipokuwa wanaume hao. Macho yake Cassian hayakutoka kwa msichana huyo, alikuwa akimwangalia mpaka alipofika mahali pale.

Mapigo yake ya moyo yalikuwa juu, alisahau kwa muda kwamba nyumbani alimuacha msichana ambaye kila siku alimwambia kwamba alikuwa akimpenda kuliko wanawake wote katika dunia hii.

“Naseku! Kutana na mshikaji wangu huyu,” alisema Osman huku akimtambulisha Cassian kama rafiki yake. Cassian alipovua miwani na kumwangalia vizuri msichana huyo, Naseku akashtuka.
 
SEHEMU YA 11

“Umeshtuka sana kumuona Cassian hapa kwenu. Ndiye huyo unayemuona! Hebu msikilize kwanza,” alisema Osman.
Cassian alibaki kimya kwa muda, alikuwa akimwangalia msichana huyo kwa mshangao. Hakuamini kama angekutana na msichana aliyekuwa mrembo kama alivyokuwa.

Umbo lake maridadi, sauti yake na sura yake ya kitoto vilimfanya kuishiwa nguvu na kumsifu Mungu kwamba alikuwa akijua sana kuumba.
“Unaitwa Naseku?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Bila shaka Mmasai?”
“Ndiyo!”

“Nimefurahi kukufahamu! Una chakula gani?”
“Ugali na nyama choma!”
“Huna baga au pizza?” aliuliza Cassian na wote kuanza kucheka kwani walijua kwamba alikuwa akitania.

“Tuna sandwich!” alijibu Naseku kwa utani, vicheko vikazidi.
“Naomba ugali na nyama choma.”
“Sawa.”

Wakati anaondoka, mwanaume huyo alibaki akimwangalia kwa nyuma. Naseku alikuwa mrefu mwenye umbo maridhawa lililomfanya Cassian kuchanganyikiwa.
“Kaka una mke!” alisema Osman.

“Mke au mchumba! Unataka kunibania nini?” aliuliza Cassian na wote kucheka mpaka kugongeana mikono.

Naseku hakuchukua muda, akapeleka chakula mezani pale na wanaume hao kuanza kula. Kila mmoja alikuwa na furaha, walikuwa wakizungumza mambo mengi kiasi kwamba hakukuwa na mtu aliyechoka.

Muda wote huo Cassian hakumwambia Osman kilichokuwa kimemfanya kupigia simu na kukutana, alitaka wamalize kula na ndipo wazungumze.

Wakati wakiendelea kula, mara simu ya Cassian ikatoa mlio uliomaanisha kwamba kulikuwa na ujumbe mfupi uliokuwa umeingia kwenye simu. Haraka sana akaingiza mkono mfukoni na kuitoa simu hiyo.

Macho yake yakatua katika kioo cha simu hiyo na kuliona jina la Evelyne. Moyo wake ukapiga paa kwani kwa jinsi alivyokuwa akimpenda, kila alipokuwa akiona ujumbe wake moyo wake ulifarijika mno, hivyo akaufungua ujumbe huo na kuanza kuusoma.

Haukuwa ujumbe mrefu sana, aliposoma mstari kwa mstari, alijikuta akibadilika, hakuamini kama ujumbe ule ulikuwa umetoka kwa msichana aliyekuwa akimpenda.

Ulikuwa ni ujumbe uliobeba maumivu mazito, hakuamini kile alichokiona, akashusha pumzi nzito kiasi kwamba mpaka Osman akashangaa.

“Vipi?”
“Osman! Osman! Osman!” alijikuta akiliita jina hilo bila kuzungumza lolote.
 
SEHEMU YA 12

“Kuna nini?”
“Evelyne! Evelyne!” alisema Cassian huku akimpa simu rafiki yake huyo na kuanza kuusoma ujumbe huo ambao uliandikwa ‘Dokta! Nashukuru sana kwa kunifichia siri ya kutokushika mimba.

Mume wangu hajui lolote, anahisi tatizo ni lake. Naomba uje kuhudhuria harusi yangu wiki ijayo. Nitakupa taarifa zaidi’
“Mungu wangu!” alijikuta akisema Osman huku akiiweka mezani simu hiyo.

Cassian alishindwa kuvumilia, machozi yakaanza kumtoka. Moyo wake ulisikia maumivu makali ambayo hakuwa ameyategemea hapo kabla.

Kila siku alijua kwamba yeye ndiye alikuwa na tatizo la kutokumpa mimba mwanamke lakini kwa meseji ile ilionyesha kabisa kwamba hakuwa na tatizo lolote lile.

Lawama zake za kwanza zilikwenda kwa madaktari ambao aliwaamini na kuwaambia wampime, wao ndiyo waliomwambia kwamba mpenzi wake hakuwa na tatizo lolote lile bali aliyekuwa na tatizo alikuwa yeye.

“Cassian! Unatakiwa kutulia, yaani usifanye maamuzi yoyote mabaya,” alisema Osman huku akionekana kumfariji sana rafiki yake huyo.

“Osman! Yaani huyu malaya ananifanyia hivi? Yaani ananifanya nijione sina uwezo wowote wa kumpa mwanamke mimba! Yaani ananifanyia hivi mimi!” alisema Cassian huku akilia kwa uchungu mkubwa.

Hakuweza kuvumilia, akainuka na kuelekea ndani ya gari. Osman akasimama na kumfuata kulekule.

Kila mtu aliyekuwa ndani ya mgahawa ule alibaki akiwashangaa, si wao tu bali hata msichana Naseku naye alikuwa akishangaa na hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mpaka Cassian kuinuka na kuelekea ndani ya gari lake huku akionekana kuwa tofauti.

Kazi ilikuwa kwa Osman, alikuwa akimpoza rafiki yake huyo ambaye alionekana kuumia kupita kawaida.

Alijua kwamba kwa hali moja au nyingine ilikuwa ni lazima kufanya jambo kama tu angekwenda nyumbani akiwa katika hali hiyo. Alikaa naye ndani ya gari na kumpoza sana na mwisho wa siku mwanaume huyo kurudi katika hali ya kawaida.

“Nifanye nini?” aliuliza Cassian.
“Kitu cha kwanza kabisa hutakiwi kuonyesha hali yoyote ya kuupata huu ujumbe!” alisema Osman.
“Sawa.”
 
Huyu Jamaa ni mwandishi mzuri sana huyu nilisoma kazi zake kama vile HEKAHEKa,
Humo ndani utakutana na Jaccob Matata akimtumia kama shujaa katika mikasa yake.
Kuna ile ZAMU YAKO KUFA.
Ahsante Shunie kwa kuileta hii, sijawahi kuisoma hii.
 
Mm namkubali sana huyu mkaka ni fan wake
Huyu Jamaa ni mwandishi mzuri sana huyu nilisoma kazi zake kama vile HEKAHEKa,
Humo ndani utakutana na Jaccob Matata akimtumia kama shujaa katika mikasa yake.
Kuna ile ZAMU YAKO KUFA.
Ahsante Shunie kwa kuileta hii, sijawahi kuisoma hii.
 
ndo maana unashinda mitandaoni kumbe ni mtunzi wa riwaya...hongera kwa kujiajiri, hapo hela za mabwana zinaishia kwenye bundle tu🙂
 
Sawa kaka akee shunie
Kabisa anafanya kazi nzuri sana huyu.
Pia kuna yule Richard Mwambe wa Kamanda Amata.
Tuko pamoja hapa kwa sisi wapenzi wa haya mavitu hizi ndio kona zetu.
Pamoja sana.
 
Dah Mungu akubariki tu nimekosa cha kukujibu
ndo maana unashinda mitandaoni kumbe ni mtunzi wa riwaya...hongera kwa kujiajiri, hapo hela za mabwana zinaishia kwenye bundle tu🙂
 
Back
Top Bottom