Viganja Mashavuni Mwangu

Viganja Mashavuni Mwangu

Sehemu ya 112

Patricia hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuchukua teksi na kuanza kuondoka mahali hapo huku akionekana kuwa na furaha tele.

Wakati gari likiwa limeingia katika Barabara ya St. Louis IV, ghafla honi nyingi zikaanza kusikika, dereva alikuwa amejisahau kuzembe kabisa, hakuangalia vizuri taa zilizokuwa zikiwaka na hivyo kuingia katika barabara hiyo iliyokuwa ikiruhusu magari yaliyokuwa yakikimbia kuanzia kasi ya 100 mpaka 150. Ni mlio mmoja mkubwa ndiyo uliosikika mahali hapo.

“Puuuuuuuu!” Teksi ile ikagongwa, ikaruka angani, ikabingirika mara tano, watu wakashika vichwa, ilipotua chini, damu tu ndizo zilizokuwa zikionekana kwenye lami. Patricia akatulia kwenye kiti kama alivyokuwa huku akitokwa na damu mfululizo.

*** Hakukuwa na siku ambayo Walker alikuwa na hamu ya kuzungumza na Patricia kama siku hiyo. Wakati wakiwa kwenye mkutano kwa ajili ya kusaini mkataba huo ambao ungewafanya kuwa majaji katika Shindano la American Got Talent, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria msichana huyo mrembo.

Wakati mwingine alitamani asimame na kuondoka, aliona kila kitu kikiendelea taratibu sana, alitamani yeye ndiye angekuwa msimamizi wa mkutano huo mdogo ambao angeamua ni muda gani walitakiwa kuondoka humo ndani.

Muda ulizidi kwenda mbele, baada ya dakika kadhaa, akapokea notification ya CNN ambayo ilimwambia kwamba kulikuwa na ajali mbaya iliyokuwa imetokea katika Barabara ya St. Louis.

Hilo wala halikumtisha, kwake, lilionekana kuwa jambo la kawaida akaendelea kukaa kwenye kikao mpaka kilipokwisha ambapo kitu cha kwanza kabisa akachukua simu yake na kumpigia Patricia ambaye alimwambia atangulie hotelini.

Simu ikaanza kuita pasipo kupokelewa, hilo halikumtia hofu sana kwani alihisi kwamba msichana huyo alikuwa bafuni akioga hivyo kusubiri zaidi na baada ya dakika kadhaa kumpigia tena.

Majibu hayakubadilika, yaliendelea kuwa vilevile kwamba simu haikupokelewa.
Hilo likaanza kumtia hofu, akaanza kuhisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea huko alipokuwa.

Alichokifanya ni kupiga simu katika hoteli aliyomuwekea chumba kwa lengo la kusikia kama msichana huyo alikuwa amefika humo au la.
 
Mapacha walioungana (Mfano wa Walker na Walter).
Screenshot_20180824-200802.jpeg
 
Sehemu ya 113

“Hajafika,” sauti na msihana upande wa pili ilisikika.
“Hajafika?”
“Ndiyo!”
Hilo likamchanganya zaidi, likamfanya kuipiga simu ya msichana huyo zaidi lakini majibu yalikuwa yaleyale kwamba simu haikupokelewa kitu kilichomfanya kuwa na hofu kubwa.

Akamwambia Walter kile kilichokuwa kikiendelea, jinsi alivyokuwa na hofu kwamba inawezekana kulikuwa na jambo baya limemtokea mpenzi wake kwani kila alipokuwa akimpigia simu haikuwa ikipokelewa kitu ambacho hakikuwa kawaida kabisa.

“Sidhani kama kuna jambo baya limetokea. Au amelala hotelini baada ya kuchoka na safari,” alisema Walter manano ambayo aliamini kwamba yangemfariji ndugu yake huyo.
“Walter! Nahisi kuna tatizo!” alisema Walker.

“Hakuna tatizo! Usihofu braza, hakuna kitu chochote kile, niamini!” alisema Walter.
Japokuwa alifarijiwa vya kutosha lakini Walker hakufarijika, bado moyo wake ulimwambia kwamba kulikuwa na kitu cha hatari kilichokuwa kimetokea. Hakuacha kumpigia simu, kuna kipindi kila alipokuwa akipiga simu, haikuwa ikiita, ilionyesha kabisa ilikuwa imezima.

Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya. Wakati akiendelea kuwa katika hali ya mawazo huku akiwa hajui ni kitu kilimtokea Patricia mpaka kuamua kuzima simu, akasikia tena mlio kwenye simu yake kuonyesha kwamba kulikuwa na notification ilikuwa imeingia.

Haraka sana akaifungua, ilitoka katika akaunti ya CNN ambayo ilionyesha kwamba jina la mtu aliyekuwa amepata ajali hatimaye alijulikana kwa jina baada ya kupatikana kwa vitambulisho vyake kwenye gari.

“Ni Patricia...” alisema Walker huku akiwa ameshutuka.
Akahisi kama moyo wake ukipigwa ganzi, hakuamini kile alichokuwa amekiona, msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote, aliyemuona kuwa kila kitu katika maisha yake alikuwa amepata ajali mbaya ya gari.

Hakukukalika tena, machozi yanaanza kumtoka na kububujika mashavuni mwake, hakutaka kubaki mahali hapo, akamwambia Walter kwamba ni lazima waelekee hospitalini kwani Patricia alipata ajali mbaya ya gari.
 
Sehemu ya 114

Kazi ya Walter ilikuwa ni kumbembeleza ndugu yake huyo, alimuonea huruma, alikuwa akibubujikwa na machozi tu kitu kilichomfanya kuumia mno moyoni mwake kwani hakupenda kumuona Walker akiwa kwenye hali hiyo, ila kwa kuwa alimpenda sana Patricia, hakuwa na jinsi.

Wakaondoka mpaka katika Hospitali ya St. Monica iliyokuwa hapohapo New York. Walipofika, kama kawaida watu wakaanza kuwazunguka, kila mtu alitaka kusainiwa kitabu na nguo zake kwani kitendo cha kukutana na watu maarufu kama hao lilikuwa jambo moja adimu sana.

Wakatembea pasipo kuzungumza na mtu yeyote mpaka walipofika katika chumba walichoambiwa wasubiri. Muda wote huo Walker alikuwa akilia, moyo wake ulimuuma, hakuamini kama msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote alikuwa hoi hospitalini hapo.

Madaktari walikuwa bize wakihangaika na hali yake, walimtibu kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba msichana huyo anapata nafuu na kurudi katika hali yake ya kawaida. Muda ulizidi kwenda mpaka baada ya saa tatu ndipo mlango ukafunguliwa na kuchukuliwa kupelekwa katika ofisi ya daktari.

Huko, wakapewa taarifa ambazo hazikuwa nzuri, Patricia alikuwa ameumia vibaya mno, ubongo wake ulipata ufa huku uti wa mgongo ukiwa umevunjika mara moja hali iliyomaanisha kwamba hata kama angerudiwa na fahamu, angepooza mwili mzima.
“Unasemaje?” aliuliza Walker huku akimwangalia daktari.

“Hatoweza kusimama! Amepooza mwili mzima. Cha msingi tumuombe Mungu tu,” alisema daktari maneno yaliyomfanya Walker kulia mno.
 
Sehemu ya 115

Walter akaanza kumbembeleza ndugu yake aliyekuwa ameumia sana, alilia kama mtoto, hakubembelezeka wala kunyamaza, kitendo cha Patricia kupata matatizo hayo kilimfanya kuumia moyoni mwake na kujiona kwamba yeye ndiye alikuwa sababu kubwa ya msichana huyo kupata matatizo hayo kwani pasipo kumwambia kwamba aelekee nchini Marekani, asingepata ajali hiyo.

“Pole sana Walker! Huu si mwisho wa Patricia,” alisema Walter huku akimpigapiga ndugu yake huyo mgongoni kama njia ya kumfariji.

Daktari alinyamaza, mbali na taarifa hiyo pia alikuwa na taarifa nyingine kuhusu msichana huyo, taarifa ambayo aliamini ingekuwa mbaya zaidi, kila alipotaka kuwaambia, alinyamaza kwani kama kwa taarifa hiyo tu Walker alilia hivyo, ingekuwaje kama angempa taarifa nyingine ambayo aliamini ingemuumiza zaidi?

Hakutaka kunyamaza, ilikuwa ni lazima kumwambia ukweli juu ya kila kitu kilichokuwa kikiendelea.

Akawaambia kwamba mbali na tatizo hilo, pia kitendo cha ubongo wake kupata ufa uliufanya kutikisika na kupata tatizo jingine ambalo lingeonekana kuwa la hatari kama lilivyokuwa lile la kupooza.
“Kitu gani?” aliuliza Walter.

“Hatoweza kukumbuka kitu chochote kile. Kumbukumbu zake zimefutika, zimekuwa kama za mtoto aliyezaliwa leo. Yaani hatoweza kumfahamu mtu yeyote yule, hatowafahamu wazazi wake, hatowafahamu nyie, hatokumbuka kitu chochote kile, ila yote hayo yatatokea kama tu atarudiwa na fahamu,” alisema daktari maneno yaliyomfanya Walker kulia zaidi.

JE, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 116

Edmund alikuwa akitafutwa kila kona, watu waliangalia mitaani, kila mtu waliyekuwa wakimtia hofu kwamba alikuwa yeye walimchukua. Hawakujua mahali jamaa huyo alipokuwa, japokuwa matangazo yalibandikwa kila kona lakini bado mwanaume huyo hakuonekana.
Hilo likawapa wasiwasi watu wengi na kuhisi kwamba inawezekana mwanaume huyo akawa amepotea sehemu fulani na hivyo alitakiwa kutafutwa kwa nguvu zote. Walipambana, walimtafuta lakini matokeo yaliendelea kuwa yaleyale kwamba hakuonekana sehemu yoyote ile.
Baada ya kuona kuwa wasingefanikiwa, M16 wakaamua kuanza kumtafuta kupitia simu yake, waliamini kwamba huko alipokuwa ilikuwa ni lazima kuwasiliana na familia yake hivyo kufanya hivyo.
Walipomtafuta kwa kutumia simu yake, waliona kabisa kwamba jamaa alikuwa akiondoka kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Walimfuatilia kwa nguvu zote, waliona akiondoka Uingereza na kuingia Wales, hawakutaka kubaki nyuma, wakawasiliana na polisi wa huko na kuwaambia uwezekano wa kumkamata Edmund.
Wakati akiwa ameondoka katika sehemu ya kuchezea watoto, dakika tatu mbele polisi wakafika mahali hapo na kuanza kuangalia kila kona, waliamini kwamba alikuwa hapo lakini kitu cha ajabu kabisa hawakuweza kumuona.
Kifaa cha GPS ndicho kilichokuwa msaada kwao, wakaanza kuangalia ili kuona kama alikuwa mahali hapo amejificha au la, walipoangalia, wakaona kwamba alikuwa amekwishaondoka mahali hapo na kuanza kumfuatilia kwa kutumia kifaa hicho.
Hilo lilifanyika kwa nguvu kubwa, wakafanikiwa kuifikia nyumba ambayo alikuwepo, kifaa kile kiliwaonyeshea kwamba Edmund alikuwa ndani ya nyumba hiyo na hivyo kuanza kuelekea humo.
 
Sehemu ya 117

Walipoufungua mlango, Mzee Vonn akatoka, kitu cha kwanza wakamuweka chini ya ulinzi na kuingia ndani ambapo huko, pamoja na kumtafuta sana, wakamkosa kabisa.
“Yupo wapi?” aliuliza polisi mmoja.
“Sijui! GPS inaonyesha yupo humu. Mungu wangu! Kumbe ameacha simu na yeye kukimbia,” alisema polisi mmoja huku akishangaa.
Waliifuatilia simu hiyo kwa kipindi kirefu, waliamini kwamba wangempata lakini mwisho wa siku waliweza kuipata simu na Edmund hakuwepo mahali hapo. Walichanganyikiwa, wakatoka ndani, wakamtafuta hata kwa nje na sehemu nyingine lakini hawakufanikiwa kumpata.
**** Japokuwa Edmund alikaribishwa kwa upendo mkubwa ndani ya nyumba ya Bwana Vonn lakini moyo wake haukuwa na amani hata kidogo. Alimwangalia mzee huyo, alionekana kuwa na furaha mno kwa yeye kuwa hapo na hakuona dalili zozote za mzee huyo kumkamata au kumfanyia mchezo mchafu wowote ule.
Akapelekwa chumbani kwake na kutulia huko. Usingizi haukuja, alijaribu kulala lakini usingizi ulikataa kabisa kitu kilichomfanya kuwa na hofu kwamba inawezekana kungekuwa na kitu kibaya ambacho kingemtokea mahali hapo.
Akatulia chumbani, muda ulizidi kwenda, usingizi ukakata na kutulia kitandani. Macho yakeyalikuwa dirishani, alikuwa akiangalia nje kuona kama kungekuwa na mtu yeyote ambaye angefika nyumbani hapo.
Muda ulizidi kwenda, baada ya dakika kadhaa akasikia muungurumo wa gari kutoka nje, haraka sana akainuka na kuangalia nje, alichokiona ni gari kubwa lililoandikwa SWAT ubavuni, gari ambalo alifahamu kabisa kwamba lilikuwa ni la polisi waliokuwa na silaha nzito.
Hakutaka kujiuliza sababu ya watu hao kufika mahali hapo, akajua kwamba walifika hapo kwa kuwa walikuwa wakimtaka yeye, hivyo akasimama na kuanza kufikiria ni kwa jinsi gani angeweza kuondoka nyumbani hapo pasipo kuonekana.
“Ni lazima niondoke!” alijisemea.
Wakati hajajua hata kitu gani alitakiwa kufanya, akasikia mlango wa sebuleni ukifunguliwa, hakutaka kujiuliza, alijua dhahiri kwamba huyo alikuwa Vonn ambaye bila shaka ndiye aliyewaita polisi hao kwa kuwa yeye alikuwemo ndani ya nyumba hiyo.
 
Sehemu ya 118

Kwa haraka sana akachomoka chumbani, akaelekea jikoni, huko, akakuta mlango mwingine wa kutoka nje, hakutaka kujiuliza, akaufungua taratibu na kuangalia kama kulikuwa na mtu.
Polisi walionekana kufanya uzembe mmoja tu, ni kweli walifika nyumbani hapo, mtu wao alikuwa ndani lakini uzembe waliokuwa wameufanya ni kutokuizunguka nyumba ile. Kitendo cha kumpata Vonn pale mlangoni walikuwa na uhakika kwamba Edmund alikuwa ndani na hivyo kuingia.
Hakukuwa na mtu, waliangalia kila kona, kabatini, chini ya kitanda na sehemu nyingine lakini hawakufanikiwa kumuona mtu yeyote yule.
Wakati wao wakiangalia huku na kule, Edmund alikuwa mbali kabisa na nyumba hiyo, alikuwa akikimbia kwa mwendo wa kasi, kubaki ndani ya nyumba hiyo kulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake.
Alikimbia mpaka sehemu moja aliyokuta nyumba kubwa iliyokuwa imezungushiwa fensi kubwa huku kwa pembeni kukiwa na mti. Alichokifanya ni kuufuata mti na kuupanda na kutulia huko, sehemu ambayo aliamini kwamba ingekuwa salama mpaka asubuhi yake ambapo angeamua ni kitu gani angetakiwa kufanya.
Kwake, alijiona kutokuwa na rafiki, aliamini kwamba inawezekana Mark alimfanyia ujanja ili akamatwe na kuvuna kiasi cha pesa kilichokuwa kimewekwa au mjomba wake, Vonn aliingiwa na tamaa na hivyo kutaka kumkamatisha na kuvuna kiasi hicho cha pesa.
Hakutakiwa kumwamini mtu yeyote yule kwa kipindi hicho. Alihitajika kupambana na hali yake mpaka kuona kwamba anafanikiwa kuwakimbia polisi hao kwa maisha yake yote.
Macho yake hayakutoka kule ilipokuwa nyumba ya Bwana Vonn, alikuwa akiiangalia kwa kuyaweka majani pembeni. Akaona mzee huyo akichukuliwa na kupakizwa ndani ya gari kisha kuondoka mahali hapo huku polisi wengine wakibaki kuhakikisha kwamba hatoki kama tu alikuwa ndani amejificha.
 
Sehemu ya 119

Walker alitia huruma, moyo wake ulikuwa ukimfikiria mpenzi wake, Patricia, alimpenda, kwake, msichana huyo alikuwa kila kitu. Bado hakuamini taarifa za madaktari kwamba mpenzi wake asingeweza kukumbuka kitu chochote wala kusimama kama ilivyokuwa zamani, wakati mwingine alihisi kwamba alikuwa kwenye ndoto mbaya na ya kusisimua ambapo baada ya muda fulani angeshtuka na kujikuta akiwa kitandani.
Kama kulia, alilia sana lakini hakukuwa na kitu kilichobadilika. Siku ziliendelea kukatika, kila siku alikwenda hospitalini hapo akiwa na pacha wake, Walter. Alihitaji kumuona mpenzi wake kitu ambacho baada ya siku tatu kuukatika, madaktari wakawaruhusu kuwaona.
Macho yake yalipotua kwa msichana huyo aliyekuwa kitandani hoi, hakuamini, alimsogelea na kumwangalia vizuri, hakuonekana kama alikuwa mzima, alionekana kama mfu kitandani pale. Alilia zaidi, akamsogelea na kumkumbatia.
Alijiona kuwa kwenye wakati mgumu, alijihukumu kwamba yeye ndiye aliyesababisha hayo yote kwani bila yeye Patricia asingesafiri mpaka nchini Marekani na kupata ajali hiyo.
“Patty! Wake up and talk to me,” Patty! Amka na uzungumze nami) alisema Walker huku akiendelea kulia.
Siku hiyo ilikuwa kimya, siku ziliendelea kukatika huku kila siku wakifika mahali hapo. Kwenye magazeti, mitandao ya kijamii na sehemu nyingine kila kona walikuwa wakiwazungumzia watu wao. Kila mmoja alimuonea huruma Walker, kwa jinsi alivyokuwa na pacha wake walipaswa kupata fulana maisha yao yote lakini kitu cha ajabu kabisa kilichokuwa kikiendelea kilikuwa ni maumivu makali.
Baasa ya siku kumi na sita kupita ndipo Patricia akayafumbua macho yake na watu wa kwanza kabisa kuwaona walikuwa mapacha hao hata kabla ya wazazi wake. “Patricia! Hatimaye umeamka,” alisema Walker huku akitabsamu.
Msichana huyo alinyamaza, hakukumbuka kitu chochote kile, alikuwa akiwashangaa, hakujua watu hao walikuwa wakina nani na walihitaji nini kutoka kwake.
Wazazi wake waliokuwa na nyuso za furaha hasa baada ya kumuona akiwa amefumbua macho wakamsogelea na kumwangalia, hata nao pia, Patricia hakuwa akiwakumbuka, alibaki akiwashangaa tu.
 
Sehemu ya 120

“Nyie ni wakina nani? Nipo wapi hapa?” aliuliza Patricia huku akimwangalia kila mmoja.
Swali hilo glikawapa maumivu makali zaidi mioyoni mwao, hawakuamini walichokuwa wamekisikia kutoka kwa binti yao, alikuwa amepoteza kumbukumbu zake zote na kitandani pale hakuwa akikumbuka kitu chochote kile.
Patricia alipojaribu kunyanyuka kitandani pale, alishindwa kabisa, akahisi mwili wake ukiwa umekufa ganzi, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea kitu kilichompelekea kuwauliza watu wale waliokuwa mbele yake kwamba ni kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka kuwa hivyo.
Hakukuwa na mtu aliyemjibu kitu chochote kile, msichana huyo aliendelea kushangaa na hata wakati mwingine kulia. Daktari akaingia, alipomuona yupo katika hali hiyo, akawaomba watoke chumbani humo kwani mgonjwa alitakiwa kupumzika zaidi kitu ambacho hakikuwa tatizo lolote lile, wakatoka chumbani humo.
Nje, Walker akaanza kulia, aliumia mno moyoni mwake. Alibaki nje ya chumba kile akiuangalia mlango wa kuingia ndani. Alimwambia Mungu kwamba mtu aliyekuwa akimuhitaji kwa kipindi hicho alikuwa msichana wake tu, hakuhitaji pesa, hakuhitaji umaarufu, kwake, Patricia alionekana kuwa kila kitu.
Alimuomba Mungu afanye muujiza lakini hilo halikuwezekana, msichana Patricia akaendelea kuwa kitandani pale huku akiendelea kushangaa sababu za kutokusimama na hata watu wale waliokuwa chumbani mule, kilichokuwa kikiendelea, hakukielewa kabisa.
*** Naseku hakuwa na raha hata kidogo, kila alipokuwa akiwaangalia watoto wake alikuwa akilia tu. Walikuwa na umaarufu mkubwa, pesa nyingi lakini kitu cha ajabu kabisa maisha waliyokuwa wakipitia, yaliwapa maumivu makubwa mno.
Walter na Walker walikuwa watu wa huzuni tu, kila siku walikuwa wakipitia majanga mbalimba, kama walinusurika katika janga hili, kesho walikuwa wakitumbukia katika janga jingine kabisa. Hayo yalikuwa maisha yao, ni kama walikuwa wamezoea kumbe kwa jinsi walivyokuwa hawakutakiwa kabisa kupita katika maisha waliyokuwa wakipitia kila siku.
 
Back
Top Bottom