SEHEMU YA 77
Baada ya dakika kadhaa, mapacha hao wakateremka huku wakiwa na ulinzi mkubwa, kama kawaida yao wakaanza kuwapungia watu mikono huku wakipiga hatua kuelekea ndani.
“Can you sign an autograph on my book, pleaseee?” (unaweza kusaini kwenye kitabu changu?) aliuliza msichana mmoja kwa sauti ya upole kabisa, japokuwa kulikuwa na ulinzi mkubwa, yeye alifanikiwa kupenya, na walinzi walipotaka kumtoa, Walke akawazuia.
“Mine or his?” (yangu au yake?) aliuliza Walker.
“Both of you,” (nyie wote)
“Okay.” (sawa)
Hilo halikuwa tatizo, wakafanya kama msichana huyo alivyotaka na kisha kupiga naye picha na kuanza kuelekea ndani ya hospitali hiyo. Bwana Cassian na mkewe, Naseku walikuwa na furaha kupita ajabu, hawakuamini kama watoto wao walikuwa wakikubalika kiasi hicho japokuwa walionekana kuwa na matatizo.
Wakati watu wakiwa bize, haraka sana Edmund akateremka kutoka kwenye gari lake na moja kwa moja kuanza kusogea kule gari lililokuwa limewabeba mapacha wale lilipokuwa huku mkononi akiwa na mtungi wa gesi.
Alipofika, akaangalia ndani, akamuona dereva akiwa anavuta sigara, akaanza kulisogelea gari zaidi, alipolifikia, akakigonga kioo, dereva akafungua.
“Unajua kwamba unavunja sheria?” aliuliza Edmund huku akimwangalia dereva.
“Sheria gani?”
Akamuonyeshea bango dogo lililoandikwa kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa akiruhusiwa kuvuta sigara katika eneo la watu wengi likiwemo hospitali kama hiyo.
Haraka sana dereva akaizima sigara yake kwani kwa jinsi Edmund alivyoonekana, jinsi alivyokuwa amevaa sare za bandia za kipolisi, aliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa polisi.
“Samahani sana.”
“Hebu teremka, nenda nyumba ya gari nikukute huko. Nataka nipekue, unaweza kuwa na bangi au madawa ya kulevya humu,” alisema Edmund, kwa kuwa alikuwa amefanya kosa, haraka sana dereva akafungua mlango na kwenda nyuma, Edmund akaingia ndani, akachukua sumu ile na kuanza kuipulizia katika sehemu ya kiyoyozi, aliipulizia kwa wingi huku kiyoyozi hicho kikiwa kimezimwa, alipomaliza, akafunga mlango.