SEHEMU YA 61
Uwezo wake ulikuwa mkubwa mno, kila alipokuwa, maisha yake yalikuwa ni kuimba tu.
Kanisani alikuwa gumzo, japokuwa alikuwa na miaka saba lakini kila mmoja alipenda kusikia namna alivyokuwa akiimba, aliwafurahisha watu wengi kiasi kwamba kanisani hapo akawa muimbaji kiongozi, kwenye kila ibada ya kusifu na kuabudu, alikuwa akichaguliwa yeye.
Wakati Walter akiwa muimbaji, Walker hakuwa na uwezo wowote wa kuimba, yeye alikuwa mchoraji, alikuwa na uwezo mkubwa wa kuchora kiasi kwamba mpaka watu wengine walikuwa wakishangaa.
Walter alikuwa mzungumzaji, alipenda sana kuongea, alikuwa na uwezo wa kuongea maneno mengi kwa wakati mmoja lakini Walker alikuwa mkimya, hakuwa mzungumzaji, mpole ambaye muda wote alionekana kuwa siriazi kupita kawaida.
“Who do you want to be?” (unataka kuwa nani?) aliuliza Cassian huku akiwaangalia watoto wake.
“A Pop star like Michael Jackson,” (niwe staa wa Pop kama Michael Jackson) alijibu Walter harakaharaka.
“What about you?” (vipi kuhusu wewe?) aliuliza Cassian huku akimwangalia Walker.
“I want to be a greatest picture artist ever in the world,” (nataka kuwa mchoraji bora kuliko wote waliowahi kutokea katika dunia hii) alisema Walker huku akimwangalia baba yake.
Waliishi katika ndoto, kila siku ilikuwa ni lazima kufanya mazoezi kwa kile walichokuwa wakitaka kuwa. Bado vipaji walivyokuwa navyo viliwashangaza watu wengi, hawakuamini kama kungekuwa na watoto waliokuwa na uwezo mkubwa kwa vile walivyokuwa nacho kama wao.
Kwenye mashindano mbalimbali shuleni, walipewa zawadi nyingi, waandishi wa habari waliposikia kuhusu wao, wakaanza kuwatafuta kwa lengo la kuzungumza nao na kuandika mengi kuhusu watoto hao.
Kuwapata halikuwa jambo jepesi, kila walipokwenda shuleni hapo, walikataliwa kuonana nao kwani ulinzi wao ulikuwa mkubwa kutokanma na heshima kubwa aliyokuwanayo baba yao.
Waandishi hao hawakukoma, kila kona walipokuwa waliendelea kusikia sifa za watoto hao, walikuwa wakiwashangaza kila mtu aliyekuwa akisikia kuhusu wao, juu ya vipaji vikubwa walivyokuwa navyo.