Viganja Mashavuni Mwangu

Viganja Mashavuni Mwangu

SEHEMU YA 69

“Kitu gani?”
“Kuna mwanaume ninampenda. Tena zaidi ya ninavyokupenda wewe. Kama utataka tuendelee kuishi pamoja, sawa, ila tukubaliane kwamba kama mwanaume huyo akija tena maishani mwangu, naomba tu tuachane kwa amani,” alisema Catherine huku akimwangalia Edmun.

Edmund akakaa kimya kwa muda, akamwangalia Catherine, maneno aliyozungumza msichana huyo yalikuwa ni yenye kuumiza mno, hakuamini mtu kama Catherine angemwambia maneno hayo kwamba wawe wapenzi wa muda na kama mwanaume aliyekuwa akimpenda angerudi maishani mwake basi huyo ndiyo ungekuwa mwisho wao.

Hilo halikumuingia akilini hata kidogo lakini aliamini kwamba kama angemkatalia Catherine basi huo ndiyo ungekuwa mwisho wao hivyo alichokifanya ni kumkubalia ili aone huyo mwanaume alikuwa nani ambaye alitaka kulikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo.

“Haina shida!”
“Una uhakika umekubali kutoka moyoni?”
“Ndiyo mpenzi!”
“Kabisa?”
“Kabisa.”

Catherine akamkumbatia mwanaume huyo, machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka kwani hakuamini kama Edmund angekubaliana naye katika hilo.

Siku zikaendelea kukatika, moyo wa mwanaume huyo ulimkereketa, alitamani sana kumfahamu mwanaume huyo, alikuwa wapi, aliishi wapi na alikuwa akifanya ni kipindi hicho.

Alijaribu kumdadisi sana Catherine ili amwambie kuhusu mwanaume huyo lakini Catherine alikuwa mgumu kufanya hivyo, alichoambulia ni kujua jina lake tu kwamba aliitwa Walter.

“Jina tu linatosha,” alisema Edmund huku akionekana kuwa na hasira kali mno.
Edmund hakujiskia raha hata kidogo, kila alipokuwa akikaa, jina la Walter ndilo lililokuwa likimjia kichwani mwake. Akatokea kumchukia mwanaume huyo hata kabla hajamtia machoni mwake, alijua kwamba huyo ndiye alikuwa mtu pekee ambaye angelikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo mrembo.

Hakuwa tayari kuona hilo likitokea, hakuwa tayari kuona akimkosa Catherine kwa kuwa kulikuwa na mwanaume aliyeitwa Walter katika dunia hii.

Hakuwahi kufikiria kama mwanaume huyo alikuwa Mtanzania, alichohisi ni kwamba alikuwa Muingereza hivyo kuanza kufuatilia chini kwa chini huku wakati mwingine akiuliza kama kulikuwa na mwanaume aliyekuwa na jina hilo.
 
SEHEMU YA 70

Baada ya miezi minne kupita huku akiendelea kuwa katika penzi na Catherine ndipo akapewa taarifa kwamba mpenzi wake huyo alikuwa amepata ajali ya gari baada ya kugongwa na hivyo kukimbizwa katika Hospitali ya Queen Elizabeth.

Alichanganyikiwa, kama kichaa akaondoka nyumbani kwao na kuelekea katika hospitali hiyo. Alipofika, akauzuiliwa kwa kuwa msichana huyo alikuwa katika chumba cha upasuaji akipewa matibabu.

“Ilikuwaje?” aliuliza Edmund huku macho yake yakiwa mekundu mno na machozi kumtiririka mashavuni mwake.
“Alipata ajali ya gari!”
“Aligongwa au?”

“Alikuwa ndani ya gari lake, likagongwa na mgongaji kukimbia,” alijibu kijana aliyeishuhudia ajali hiyo ambaye ndiye alishughulika na watu wengine kumkimbiza msichana huyo katika hospitali hiyo.

Moyo wake ukachoma sana lakini hakuwa na jinsi. Siku hiyo hakuweza kumuona msichana huyo na hata wazazi wa msichana huyo walipofika, walimsifu Edmund kwa moyo wake kujitolea kuwa mtu wa kwanza kufika hospitalini hapo.

Siku iliyofuata ndipo wakaruhusiwa kumuona msichana huyo. Alikuwa ameumia vibaya kichwani mwake huku akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani na kwa maelezo ya madaktari waliwaambia kwamba fuvu la kichwa chake lilikuwa limepata ufa ambapo kwa kitaalamu lilijulikana kama skull fracture.

“Atapona?” aliuliza Bwana Gordon.
“Ndiyo! Kwa kawaida fuvu la kichwa likipata ufa, maumivu huwa kwa siku saba mpaka kumi, baada ya hapo mgonjwa atakuwa kwenye hali ya kawaida na ili fuvu lirudi katika hali ya kawaida, itamchukua miezi zaidi ya ishirini na nne, ila akiwa chini ya uangaliazi,” alisema Dk. Wayne.

Hizo zilikuwa ni kama siku za mateso kwa msichana huyo, alikuwa kimya kitandani na hata baada ya kuyafumbua macho yake hakuweza kuzungumza lolote lile, alikuwa kimya huku akiwaangalia watu waliokuwa katika chumba chake.
 
SEHEMU YA 71

Siku ziliendelea kukatika, msichana huyo aliendelea kupatiwa matibabu hospitalini pale na baada ya siku tatu, Walter na Walker wakafika hospitalini hapo.

Siku hiyo ilikuwa kizaazaa, kila mtu aliyekuwa akiwaona, alitaka kupiga nao picha, walikuwa maarufu, watu waliokuwa na vipaji ambavyo havikuwa vya kawaida kabisa.

Kwa kuwa muda wa kuona wagonjwa ulikuwa umefika, wakaruhusiwa kwenda moja kwa moja katika chumba kile. Edmund aliwaona lakini hakuwajua, alikuwa bize na masomo na hakuweza kufuatilia mambo ya habari au yale yaliyokuwa yakiendelea katika mitandao ya kijamii.

Aliwashangaa wanaume hao lakini wazazi wa Catherine walikuwa wakiwakumbuka vizuri, walikuwa marafiki wa binti yake.

Kidogo Walter alipomuona Catherine kitandani pale moyo wake ukafurahi, wakamsogelea na kisha kumshika mkono.
Edmund alikuwa kimya akifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Catherine aliposhikwa mkono, akayafumbua macho yake, tabasamu pana likamjia usoni mwake.

“Walter! Atlast you have come to see me,” (Walter! Hatimaye umekuja kuniona) alisema msichana huyo huku tabasamu pana likiendelea kuonekana usoni mwake.

Edmund aliposikia jina la Walter tu, akashtuka, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini kama mmoja wa mapacha wale walioungana alikuwa Walter ambaye Catherine alisema wangeachana kama tu mwanaume huyo angerudi maishani mwake.

JE, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 72

Kupatikana kwa Walter kulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa uhusiano wake na msichana Catherine aliyekuwa kitandani. Moyo wa Edmund uliuma na kuchoma sana, kila alipokuwa akimwangalia mwanaume huyo ambaye aliungana na pacha mwenzake kulimaanisha kuwa huo ndiyo ungekuwa mwisho, yaani alitakiwa kusahau kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Hakutaka kukubali, kwa wakati huo alikuwa tayari kupoteza kila kitu isipokuwa kumpoteza Catherine ambaye kila alipokuwa akimwangalia, kila siku uzuri wake uliongezeka maradufu.
Japokuwa alikuwa kitandani lakini kitendo cha kumuona Walter akiwa amefika mahali hapo, Catherine akaonekana kuwa na furaha mno, furaha ambayo Edmund mwenyewe alikiri moyoni kwamba hakuwahi kumuona msichana huyo akiwa kwenye furaha kama siku hiyo.
“Nilikukumbuka sana,” alisema Catherine huku akimwangalia Walter machoni.
“Nilikukumbuka pia. Sikutaka nione ukiendelea kuwa kwenye matatizo halafu mimi nipo. Nitahakikisha nakulinda maisha yangu yote,” alisema Walter.
Wazazi wa pande zote tatu walibaki wakiwaangalia watu hao, kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele ndivyo ambavyo Edmund alivyozidi kuumia. Hakukuwa na mtu aliyefahamu kile walichokuwa wameongea zaidi ya wao wawili tu.
Alivumilia tu kukaa na hata alipokuwa akitambulishwa, alijibaraguza kwa kuonekana kuwa na tabasamu pana na wakati moyo wake ulikuwa ukiwaka moto kwa wivu.
Hakutaka kubaki mahali hapo, akaondoka na kurudi nyumbani. Ndani ya gari, alikuwa akilia kama mtoto, hakuamini kilichokuwa kikiendelea. Uwepo wa Walter ulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha yake.
Alipofika nyumbani, akajifungia chumbani na kuanza kulia. Alipenda mpaka kufikia hatua ya mwisho kabisa, hatua ambayo aliona ikivuka hapo angekuwa kichaa, mapenzi yaliuendesha moyo wake, yalimsumbua kupita kawaida na ndiyo maana alipogundua kwamba mwanaume aliyekuwa amemuona alikuwa Walter, alihisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake.
“I must kill him,” (ni lazima nimuue)
Huo ndiyo ulikuwa uamuzi alioufikia kipindi hicho, hakutaka kuona akimkosa Catherine kwa sababu ya Walter, alitamani kuendelea kulilinda penzi lake lakini si kuona likipotea na kuchukuliwa na mtu mwingine.
 
SEHEMU YA 73

Alichokifanya ni kuanza kufikiria ni watu gani ambao angewatumia kwa ajili ya kumuua Walter. Ilikuwa ni lazima afe kwani aliamini kwamba kama asingemuua basi ingekuwa ngumu sana kwake kuendelea na msichana huyo.
Wazo ambalo lilimjia kichwani lilikuwa ni kuwamaliza kwa kuwekea sumu ndani ya gari alilokuwa akilitumia. Alijua kwamba ilikuwa ni lazima kwa mwanaume huyo kufika hospitalini hapo mara kwa mara hivyo kama angeweka sumu, wakati wanaingia ndani ya gari, kuwashwa na kiyoyozi kuwashwa basi sumu ienee ndani ya gari na mwanaume huyo kufa.
“Yeah! I can use Hydrogen Selenide to kill him through air condition,” (Yeah! Naweza kutumia Hydrogen Selenide kumuua ndani ya gari lake)
Huo ndiyo ulikuwa mpango wake, hakutaka kujua ni watu wangapi angewaua mara baada ya kuweka sumu hiyo katika gari hilo, kitu alichokuwa akihitaji ni kuona anammaliza mwanaume aliyetokea kuumiza moyo wake.
Kuipata sumu hiyo kali halikuwa jambo jepesi, kulikuwa na ugumu sana na ilihitaji kupata barua maalumu kutoka serikali ambayo ingeeleza sababu ya yeye kuihitaji sumu hiyo ili kama kutaonekana hakukuwa na msingi wowote wa kupewa, basi asipewe na kama angepewa wakati wa kutumia ilikuwa ni lazima mtu wa serikalini awepo mahali husika.
Aliuona ugumu huo hali iliyomfanya kuwasiliana na rafiki yake, Thomson ambaye baba yake alikuwa daktari mkuu katika Hospitali ya The Royal London, alihitaji Thomson afanye kila linalowezekana mpaka baba yake ampe sumu hiyo ya gesi na kwenda kuitumia kumuua Walter.
“I will talk to him,” (nitazungumza naye)
“I just need your help Thom,” (ninahitaji msaada wako Thom) alisema Edmund huku akionekana kweli kuhitaji msaada.
“I will give you a hand,” (nitakusaidia)
Wakakubaliana na kuondoka mahali hapo. Thomson hakutaka kwenda kumuomba baba yake sumu hiyo kwani aliamini kuwa ni lazima amkatalie, alichokifanya ni kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anaiiba sumu hiyo hospitalini kwa kuchukua mtungi mdogo na kuondoka nayo.
 
SEHEMU YA 74

Hilo ndilo alilolifanya, siku iliyofuata akaenda katika hospitali aliyokuwa akifanya kazi baba yake kwa lengo la kumsaidia kumbe upande mwingine alikuwa na jambo jingine kabisa alilotaka kulifanya.
Alipofika huko, akasalimiana na baba yake na muda wa kuondoka, akaanza kwenda maabara ambapo aliamini kwamba ni lazima gesi hiyo ingekuwa mahali huko.
Hakuonekana kuwa na hofu, hata madaktari waliokuwa wakimuona akielekea katika maabara ile hawakuwa na hofu naye kwani hiyo haikuwa mara ya kwanza kwenda huko, alikuwa akifika mara kwa mara na kuingia katika maabara hiyo.
Alisalimiana na watu mbalimbali mpaka alipoufikia mlango na kuingia ndani. Humo akakukatana na watu zaidi ya thelathini ambao walikuwa wakisomea uuguzi na walikuwa humo kwa ajili ya kuonyeshwa vitu mbalimbali kwa vitendo.
Naye akajifanya kuungana nao, macho yake hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, alipoiona mitungi ya gesi na mingine midogo kama fire extinguisher zile zinazokaa kwenye pikipiki, akaona kwamba hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake.
Wanafunzi wale walichukua dakika arobaini, walipomaliza wakaondoka na haraka sana Thomson kwenda kule kulipokuwa na mitungi ile. Kabla ya kuichukua, akaanza kuisoma ili kuipata gesi ya Hydrogen Selenide.
“Haipo!” alisema mara baada ya kuangalia sana.
“Nitrogen trioxide, Nitrosyl chloride, sasa nichukue ipi kama Hydrogen Selenide haipo?” alijiuliza, lakini hata kabla hajajijibu, akaichukua Nitrosyl chloride na kuuingiza ule mtungi mdogo ndani ya begi lake na kuondoka ndani ya maabara ile.
Akamfuata Thomson na kumkabidhi, akamwambia jinsi ambavyo ilitakiwa kutumika. Alimpa maelekezo kwamba ni lazima achukua mpira, aitoboe na haraka sana aingize mpira katika tundu la gesi ile kisha kuanza kuichukua kwa kuiweka katika kiyoyozi cha gari na kukaa humo, kiyoyozi kama kingewashwa, basi gesi hiyo ingetoka na kummaliza audui yake ndani ya gari.
“Nashukuru sana!” alisema Walter na kumpa Thomson zawadi ya paundi elfu mbili ambazo ni zaidi ya milioni nne kama shukrani kwa kile alichomfanyia.
 
Back
Top Bottom