Ukomo wa ndoa na aina zake katika sheria za Tanzania
Lusungu Hemed
Leo hii tuendelee kutazama ukomo wa ndoa na aina za ndoa kwa sheria za Tanzania. Kwanza kabisa, nianze kwa kusema kuwa muungano wa kindoa kati ya mwanamume na mwanamke lazima uwe na kusudio la kudumu maishani.
Tunaposema kwamba muungano wa mwanamke na mwanamume lazima ukusudiwe kuwa wa kudumu kwa muda wa maisha yao, nina maana ya kawaida kabisa ambayo ni kusudio la kutotengana au kuachana.
Sheria inatahadharisha uwezekano wa kuwa na muungano wa muda mfupi tu wa wanandoa. Sehemu fulani za jamii na dunia miongoni mwa jamii ya ‘Khoja Shia Ithna – Asheri' wanatambua kitu kinachoitwa ‘mutaa' au ndoa ya muda fulani unaopangwa.
Sheria ya Tanzania haitambui ndoa ya muda mfupi ambayo inatamkwa rasmi wakati wa kufunga ndoa hiyo. Sheria hiyo ya Ndoa ya mwaka 1971 inasema kwamba ndoa itadumu hadi pale litakapotokea tukio fulani linaloweza kuivunja.
Kufa kwa mume au mke ni mfano mmoja wapo wa tukio ambalo linakomesha kuwepo kwa ndoa. Mume au mke anaweza pia kuyumkinika kuwa amekufa iwapo ametoweka bila kujulikana au kusikia aliko kwa muda mrefu, miaka saba au zaidi na mahakama ikatamka.
Vile vile ndoa itabaki kuwa hivyo mpaka mahakama itoe amri ya kuibatilisha au kwa kutoa amri ya talaka. Kwa mujibu wa Sheria ya Ndoa ya Tanzania kuna aina mbili za ndoa.
Aina hizo ni zile ndoa za mke mmoja au zinazokusudiwa ziwe za mke mmoja na ndoa mitala, yaani zile zinazoweza kuwa za wake wengi.
Zipo pia taratibu tatu za kujenga ndoa, yaani kimila, kidini na kiserikali. Ndoa ya mke mmoja ni muungano wa mwanamume mmoja na mwanamke mmoja tu bila mwingine yeyote.
Muungano ambao unamwezesha mume kuoa mke mwingine au wake wengine, wakati ndoa ya mwanzo ingalipo, huitwa ndoa ya mitala.
Hapa Tanzania ndoa inaweza kugeuzwa. Ndoa inaweza kugeuzwa kutoka kwenye ndoa ya mke mmoja na kuwa ndoa inayoweza kuwa ya mitala.
Vile vile ndoa inaweza kugeuzwa kutoka ndoa inayoweza kuwa ya mitala na kuwa ya mke mmoja. Lakini wakati mabadiliko hayo yanapofanyika itakuwa ni lazima kuzingatia mila, desturi na imani ya wahusika.
Ndoa inaweza kugeuzwa kwa tamko rasmi litakalotolewa na mume pamoja na mkewe kwamba kila mmoja wao kwa hiari yao wenyewe wamekubaliana juu ya mabadiliko hayo.
Pia kwa kuzingatia namna ilivyofungwa, yaani mila, desturi na imani ya wahusika. Tamko hilo lazima litolewe mbele ya jaji, hakimu mkazi au hakimu wa wilaya.
Ni lazima pia tamko hilo lithibitishwe kwa maandishi yatakayosainiwa na mume na mke. Tamko hilo pia itabidi lisainiwe na shahidi ambaye tamko hilo lilitolewa mbele yake.
Ndoa ya Wakristo wawili inayofungwa kanisani kwa mujibu wa dini yao, haiwezi kugeuzwa kutoka ndoa ya mke mmoja na kuwa ndoa ya mitala.
Ndoa hiyo itabaki kuwa ya mke mmoja kwa wakati wote wafunga ndoa hao wanapoendelea kuwa Wakristo. Masharti ya sheria inayoruhusu kugeuzwa ndoa hayahusishi ndoa yoyote ya Kikristo.
Hata kama ndoa ya Kikristo ilitanguliwa au kufuatiwa na ndoa iliyofungwa kiserikali au kwa namna yoyote nyingine, taratibu za kugeuza ndoa hazitaihusu ndoa hiyo.
Iwapo ndoa yake ingalipo, basi mwanamke haruhusiwi kufunga ndoa nyingine. Ni dhahiri kwamba mwanamke akifiwa na mumewe ataruhusiwa kufunga ndoa nyingine.
Kadhalika mwanamke ataruhusiwa kufunga ndoa nyingine baada ya amri ya kubatilisha ndoa yake ya awali au baada ya amri ya talaka.
Tukutane juma lijalo!